Tazamio Moja la Pekee!
“Kila mtu aliye hai na hudhihirisha imani katika mimi hatakufa hata kidogo kabisa.”—YOHANA 11:26.
1. Mamilioni ya watu ambao sasa wamekufa watafufuliwa waje kuishi katika mazingira ya namna gani?
WAKATI mamilioni ya watu watainuliwa katika ufufuo, hawatarudishwa kwenye uhai juu ya dunia tupu. (Matendo 24:15) Wataamka wakiwa katika mazingira mazuri yenye kusitawi na watakuta makao ya kuishi ndani, mavazi na chakula kingi vimetayarishwa kwa ajili yao. Nani watakaofanya matayarisho haya yote? Kwa wazi, watu watakuwa wakiishi katika ulimwengu mpya kabla ya ufufuo wa kidunia kuanza. Lakini, hao ni nani?
2-4. Tazamio gani la pekee langojea wale wanaoishi katika “siku za mwisho”?
2 Utimizo wa unabii wa Biblia unaonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo.a (2 Timotheo 3:1) Karibuni sana sasa, Yehova Mungu ataingilia mambo ya wanadamu na kufuta kabisa uovu kutoka katika dunia. (Zaburi 37:10, 11; Mezali 2:21, 22) Wakati huo, jambo gani litawafikia wale ambao kwa uaminifu humtumikia Mungu?
3 Yehova hataharibu waadilifu na waovu pamoja. (Zaburi 145:20) Hajafanya jambo kama hilo kamwe, na hatafanya hivyo wakati atakapoisafisha dunia na ubaya wote. (Linganisha Mwanzo 18:22, 23, 26.) Kwa kweli, kitabu cha mwisho cha Biblia husimulia juu ya “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha,” wakitoka katika “dhiki kubwa.” (Ufunuo 7:9-14) Ndiyo, mkutano mkubwa utaiokoka dhiki kubwa ambayo itaukomesha ulimwengu mwovu wa sasa, nao wataingia katika ulimwengu mpya wa Mungu. Humo, wanadamu wenye kutii wanaweza kufaidika kikamili na maandalizi ya ajabu ya Mungu ya kuweka wanadamu huru kutoka dhambi na kifo. (Ufunuo 22:1, 2) Hivyo, “umati mkubwa” hautaona kifo kamwe. Tazamio la pekee kama nini!
4 Je! tunaweza kutia imani katika tumaini hili la ajabu? Bila shaka! Yesu Kristo mwenyewe alionyesha kwamba kungekuwa na wakati ambapo watu wataishi bila kufa kamwe. Kabla tu ya kumfufua rafiki yake Lazaro, Yesu alimwambia Martha: “Kila mtu aliye hai na hudhihirisha imani katika mimi hatakufa hata kidogo kabisa.”—Yohana 11:26.
Wewe Pia Unaweza Kuishi Milele
5, 6. Ikiwa unataka kuishi milele katika Paradiso duniani, unapaswa kufanya nini?
5 Je! watamani kuishi milele katika Paradiso duniani? Je! unatamani kuona wapendwa wako tena? Basi, unapaswa kuyatwaa maarifa sahihi ya mapenzi na makusudi ya Mungu. Katika sala kwa Mungu, Yesu alisema: “Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.
6 Ni mapenzi ya Mungu kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:3, 4) Sasa ndio wakati wa kujifunza namna wewe, pamoja na mamilioni ya wengine ambao tayari wanafanya mapenzi ya Mungu, mnaweza kuishi milele katika Paradiso duniani. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia ujifunze zaidi kuhusu Mungu na matakwa yake. Kwa nini usikutane nao kwenye Jumba la Ufalme karibu na mahali unapokaa au kuandika kwa kutumia anwani ya karibu zaidi inayoorodheshwa kwenye ukurasa ufuatao?
[Maelezo ya Chini]
a Tazama Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kurusa 98-107, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 31]
“Umati mkubwa” hauhitaji kamwe kuonja kifo