Yehova—Yeye Ni Nani?
AKIFYEKA msitu katika Kambodia ili apate njia ya kupitia, Henri Mouhot, mvumbuzi Mfaransa wa karne ya 19, alifikia handaki pana la maji lililozunguka hekalu. Lilikuwa ile nguzo ya ukumbusho ya kidini iliyo kubwa zaidi duniani, iitwayo Angkor Wat. Kwa kulitupia jicho Mouhot angeweza kuona kwamba jengo hilo lililofunikwa kwa kuvumwani lilikuwa limetengenezwa kwa mikono ya mwanadamu. “Lilisimamishwa na mjenzi wa kale mwenye stadi kama za Michelangelo,” akaandika, “ni kubwa zaidi kuliko mabaki yoyote ya jengo lililobuniwa na Ugiriki au Roma.” Ijapokuwa kwa karne kadhaa lilikuwa limeachwa na kupuuzwa, yeye hakuwa na shaka kwamba kulikuwa na mbuni wa jengo hilo tata.
Kwa kupendeza, kitabu chenye hekima kilichoandikwa karne kadhaa zilizopita kilitumia kusababu hukohuko kikieleza hivi: “Bila shaka, kila nyumba imejengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyejenga vitu vyote ni Mungu.” (Waebrania 3:4) Lakini huenda wengine wakasema, ‘Namna za utendaji wa asili ni tofauti na zile za kutengenezwa na watu.’ Hata hivyo, si wanasayansi wote ambao hukubaliana na kipingamizi hicho.
Baada ya kukubali kwamba “mifumo ya kibiokemia si vyombo visivyo na uhai,” Michael Behe, profesa-mshiriki wa biokemia kwenye Chuo Kikuu cha Lehigh, Pennsylvania, Marekani, auliza hivi: “Je, mifumo ya biokemia yenye kutenda kazi yaweza kubuniwa kwa kutumia akili?” Aendelea kuonyesha kwamba wanasayansi sasa wanabuni mabadiliko ya msingi katika viumbehai vinavyoishi kupitia njia kama vile kupanga na kuanzisha tabia za urithi. Naam, vitu vyote vilivyo na uhai na visivyo na uhai vyaweza “kujengwa”! Kwa kuchunguza chembe zilizo hai ambazo ni ndogo sana, Behe aliona mifumo yenye kustaajabisha iliyo migumu kufahamika, inayofanyizwa na tanzu zinazotegemeana ili kufanya kazi. Umalizio wake ni nini? “Matokeo ya jitihada nyingi za kuchunguza chembe—kuchunguza uhai kwa kiwango cha molekuli—ni kilio kikubwa kilicho kikali kisemacho ‘ubuni!’”
Basi, je, ni nani yule Mbuni aliyeibuni mifumo yote hii iliyo migumu kufahamika?
Mbuni Huyo Ni Nani?
Jibu lapatikana katika kile kitabu cha kale chenye hekima kilichonukuliwa mwanzoni—Biblia. Katika maneno yake ya kufungua, Biblia hujibu kwa njia sahili ajabu na waziwazi lile swali juu ya yule aliyebuni vitu vyote: “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi.”—Mwanzo 1:1.
Hata hivyo, katika kujitofautisha mwenyewe na wengine wasemwao kuwa Mungu, Muumba hujitambulisha mwenyewe kwa jina la pekee: “Mungu BWANA [“Yehova,” “NW”] anena, yeye aliyeziumba mbingu, . . . , yeye aliyeitandaza nchi na mazao yake; yeye awapaye pumzi watu walio juu yake.” (Isaya 42:5, 8, italiki ni zetu.) Yehova ndilo jina la Mungu aliyeubuni ulimwengu na kuwaumba wanaume na wanawake duniani. Lakini Yehova ni nani? Yeye ni Mungu wa aina gani? Na kwa nini wewe umsikilize?
Umaana wa Jina Lake
Kwanza kabisa, jina la Muumba, Yehova, lamaanisha nini? Jina la Mungu limeandikwa katika herufi nne za Kiebrania (יהוה) nalo lapatikana karibu mara 7,000 katika sehemu ya Kiebrania ya Biblia. Jina hili lafikiriwa kuwa namna ya kutendesha ya kitenzi cha Kiebrania ha·wahʹ (“kuwa”) na hivyo humaanisha “Yeye Husababisha Iwe.” Yaani, Yehova hujifanya kwa hekima awe chochote atakacho kuwa ili atimize makusudi yake. Yeye huwa Muumba, Hakimu, Mwokozi, Mwendelezaji wa uhai, na kadhalika, ili atimize makusudi yake. Isitoshe, kitenzi cha Kiebrania huchukua namna ya sarufi inayoonyesha tendo lililo katika hatua ya kutimizwa. Hilo laonyesha kwamba Yehova bado ajifanya kuwa mtimizaji wa ahadi zake. Naam, yeye ni Mungu aliye hai!
Sifa Kuu za Yehova
Biblia yamwonyesha Muumba na mtimizaji huyu wa makusudi yake kuwa mtu mwenye kuvutia sana. Yehova mwenyewe alifunua sifa zake tofauti-tofauti na kusema: “BWANA [“Yehova,” NW], BWANA [“Yehova,” NW], Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema [“fadhili-upendo,” NW] na kweli; mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi.” (Kutoka 34:6, 7) Yehova afafanuliwa kuwa Mungu wa fadhili-upendo. Neno la Kiebrania linalotumiwa hapa, pia laweza kutafsiriwa kuwa “upendo wenye uaminifu-mshikamanifu.” Katika kutimiza kusudi lake la milele, Yehova aendelea kwa uaminifu-mshikamanifu kuonyesha viumbe wake upendo. Je, hungethamini upendo huo?
Yehova si mwepesi wa hasira na si wa polepole kusamehe makosa yetu. Inatia moyo kuwa karibu na mtu ambaye si mwenye kutafuta-tafuta makosa bali aliye tayari kutusamehe. Lakini hiyo haimaanishi kwamba Yehova hukubali makosa. Yeye alitangaza hivi: “Mimi, BWANA [“Yehova,” NW], naipenda hukumu ya haki, nauchukia wivi na uovu.” (Isaya 61:8) Akiwa Mungu wa haki, yeye havumilii milele watenda-dhambi wenye kujasiria ambao huendelea na uovu wao. Hivyo, twaweza kuwa na uhakika kwamba katika wakati wake ufaao, Yehova atarekebisha ukosefu wa haki ulio katika ulimwengu wenye kutuzunguka.
Kudumisha usawaziko mkamilifu kati ya sifa ya upendo na ya haki kwahitaji hekima. Yehova husawazisha sifa hizi mbili katika njia ya ajabu anaposhughulika nasi. (Waroma 11:33-36) Bila shaka, hekima yake yaweza kuonwa kila mahali. Ajabu za maumbile zashuhudia hilo.—Zaburi 104:24; Mithali 3:19.
Hata hivyo, kuwa na hekima hakutoshi. Ili kutimiza kikamili kile afikiriacho, ni lazima Muumba pia awe na nguvu kamili. Biblia humwonyesha kuwa Mungu wa aina hiyo: “Inueni macho yenu juu, mkaone; ni nani aliyeziumba hizi; aletaye nje jeshi lao kwa hesabu . . . kwa ukuu wa uweza wake, . . . hapana moja isiyokuwapo mahali pake.” (Isaya 40:26) Kwa kweli, Yehova anaweza kutumia “ukuu wa uweza” kutimiza mapenzi yake. Je, sifa hizo hazikufanyi uvutiwe na Yehova?
Manufaa za Kumjua Yehova
Yehova “hakuiumba [dunia] ukiwa” bali “aliiumba ili ikaliwe” na binadamu ambao wana uhusiano wenye maana pamoja naye. (Isaya 45:18; Mwanzo 1:28) Yeye huwajali viumbe wake wa kidunia. Aliwapa wanadamu mwanzo mkamilifu katika makao yaliyo ya kibustani, paradiso. Binadamu, kwa upande wao, wanaiharibu, wakikosa kumfurahisha Yehova. Hata hivyo, kulingana na vile jina lake huonyesha, Yehova atatimiza kusudi lake la awali kwa wanadamu na dunia hii. (Zaburi 115:16; Ufunuo 11:18) Atarudisha Paradiso duniani kwa wale walio tayari kumtii wakiwa watoto wake.—Mithali 8:17; Mathayo 5:5.
Kitabu cha mwisho cha Biblia hufafanua ubora wa maisha unaoweza kufurahia katika Paradiso hiyo: “Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:3, 4) Hayo ndiyo maisha halisi ambayo Yehova anataka ufurahie. Yeye ni Baba mkarimu kama nini! Je, uko tayari kujifunza mengi zaidi kumhusu na yale unayotakwa kufanya ili uishi katika Paradiso?
Isipokuwa imeonyeshwa vingine, manukuu ya Maandiko ya Kiebrania ni kutoka katika Union Version ya Kiswahili chapa ya 1994, na manukuu ya Maandiko ya Kigiriki ni kutoka katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Mahali ambapo herufi NW zinafuata nukuu, zaonyesha kwamba tafsiri inatoka katika New World Translation of the Holy Scriptures—With References ya Kiingereza.