Sitawisha Ustadi wa Kufundisha
UNA mradi gani ukiwa mwalimu? Ikiwa umekuwa mhubiri wa Ufalme hivi karibuni, bila shaka unatamani kujifunza kuongoza funzo la Biblia la nyumbani kwa sababu Yesu aliwaagiza wafuasi wake wafanye wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Ikiwa tayari una ujuzi wa kuongoza mafunzo, labda mradi wako ni kufikia mioyo zaidi. Ikiwa wewe ni mzazi, bila shaka ungependa kuwafundisha watoto wako ili kuwachochea waweke maisha yao wakfu kwa Mungu. (3 Yoh. 4) Ikiwa wewe ni mzee au unajitahidi kufikia kuwa mzee, labda unataka kuwa msemaji anayeweza kufanya wasikilizaji wamthamini Yehova zaidi pamoja na njia zake. Unaweza kuifikiaje miradi hiyo?
Jifunze kutokana na Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo. (Luka 6:40) Yesu alipokuwa akizungumza na umati kando ya mlima au na watu wachache wakitembea barabarani, maneno yake na njia yake ya kusema ilivutia sana. Yesu alichochea akili na mioyo ya wasikilizaji, na alionyesha jinsi maneno yake yanavyotumika kwa njia waliyoelewa. Je, wewe pia unaweza kufanya hivyo?
Mtegemee Yehova
Uhusiano wa karibu uliokuwapo kati ya Yesu na Baba yake wa mbinguni, na pia baraka za roho ya Mungu ziliboresha uwezo wake wa kufundisha. Je, wewe humwomba Yehova kwa bidii ili uweze kuongoza vizuri funzo la Biblia la nyumbani? Ikiwa wewe ni mzazi, je, wewe husali kwa ukawaida upate mwongozo wa Mungu wa jinsi ya kufundisha watoto wako? Je, wewe hutoa sala zinazotoka moyoni unapotayarisha kutoa hotuba au kuongoza mikutano? Kumtegemea Yehova kwa njia hiyo kutakusaidia kuwa mwalimu bora zaidi.
Kutegemea Neno la Yehova, Biblia, kunaonyesha unamtegemea Yeye. Yesu alimwambia Baba yake hivi katika sala aliyotoa jioni ya mwisho ya maisha yake akiwa binadamu mkamilifu: “Nimewapa wao neno lako.” (Yn. 17:14) Ingawa Yesu alikuwa na ujuzi sana, hakusema mambo yake tu. Sikuzote alisema mambo aliyofundishwa na Baba yake, akituwekea mfano wa kuiga. (Yn. 12:49, 50) Neno la Mungu lililohifadhiwa katika Biblia lina uwezo wa kubadilisha matendo, mawazo ya ndani, na hisia za watu. (Ebr. 4:12) Unapozidi kupata ujuzi wa Neno la Mungu na kujifunza kuutumia vizuri katika huduma yako, utakuwa unasitawisha uwezo wa kufundisha unaovutia watu kwa Mungu.—2 Tim. 3:16, 17.
Mheshimu Yehova
Kuwa mwalimu kwa kumwiga Kristo si kuwa na uwezo tu wa kutoa hotuba zenye kupendeza. Ni kweli kwamba watu walistaajabia ‘maneno ya Yesu yenye uvutio mwingi.’ (Luka 4:22) Lakini Yesu alikuwa na mradi gani alipokuwa akiongea vizuri? Kumheshimu Yehova, wala si kujitukuza. (Yn. 7:16-18) Naye aliwahimiza hivi wafuasi wake: “Acheni nuru yenu ing’ae mbele ya watu, ili wapate kuona kazi zenu bora na kumpa utukufu Baba yenu aliye katika mbingu.” (Mt. 5:16) Tufuate shauri hilo tunapofundisha. Tunapaswa kuwa na lengo la kuepuka jambo lolote ambalo linaweza kufanya tukose mradi huo. Basi, tunapopanga jambo tutakalosema au jinsi tutakavyolisema, inafaa tujiulize, ‘Je, litafanya watu wamthamini Yehova zaidi, au litanitukuza?’
Kwa mfano, tunapofundisha tunaweza kutumia vizuri vielelezo na mifano ya mambo halisi yaliyotokea. Lakini, mfano mrefu mno unapotolewa au jambo fulani lililoonwa linaposimuliwa kupita kiasi, tunaweza kupoteza somo muhimu la mfano huo. Vivyo hivyo, kusimulia tu hadithi za kutumbuiza hufanya tupoteze kusudi la huduma yetu. Kwa kweli, kufanya hivyo ni kujitukuza badala ya kutimiza mradi halisi wa elimu ya kitheokrasi.
‘Pambanua Mambo’
Kwa kweli ili mtu awe mwanafunzi, ni lazima aelewe vizuri mambo anayofundishwa. Ni lazima aisikie kweli na aone jinsi inavyotofautiana na mafundisho mengineyo. Kupambanua mambo kunasaidia kutimiza lengo hilo.
Yehova alirudia-rudia kuwahimiza watu wake ‘wapambanue’ kati ya yaliyo safi na yaliyo najisi. (Law. 10:9-11) Alisema kwamba wale ambao wangetumikia katika hekalu lake kuu la kiroho wangefundisha watu “kupambanua vitu vilivyo vitakatifu na visivyo vitakatifu.” (Eze. 44:23, Biblia Habari Njema) Kitabu cha Mithali kinaonyesha tofauti nyingi zilizoko kati ya uadilifu na uovu, kati ya hekima na ujinga. Hata mambo ambayo hayatofautiani sana yanaweza kupambanuliwa. Mtume Paulo alionyesha tofauti iliyoko kati ya mtu mwadilifu na mtu mzuri, kama inavyoonyeshwa katika Waroma 5:7. Katika kitabu cha Waebrania, alionyesha ubora wa utumishi wa Kristo akiwa kuhani wa cheo cha juu kuliko utumishi wa Aroni. Mwalimu mmoja wa karne ya 17, John Amos Comenius, aliandika hivi: “Kufundisha kunamaanisha tu kuonyesha tofauti zilizoko kati ya vitu kwa habari ya matumizi, maumbo, na chanzo. . . . Basi mtu anayefafanua vizuri tofauti hizo hufundisha vizuri.”
Tuseme unafundisha mtu juu ya Ufalme wa Mungu. Ikiwa hajui Ufalme ni nini, unaweza kumwonyesha jinsi maneno ya Biblia kuhusu Ufalme yanavyotofautiana na wazo la kwamba Ufalme ni hali tu iliyo moyoni mwa mtu. Au unaweza kumwonyesha jinsi Ufalme unavyotofautiana na serikali za wanadamu. Lakini unaweza kuzungumza mambo ya ndani zaidi na watu wanaojua kweli hizo za msingi. Unaweza kuwaonyesha jinsi Ufalme wa Kimesiya unavyotofautiana na utawala wa Yehova mwenyewe juu ya ulimwengu wote mzima, unaotajwa katika Zaburi 103:19. Pia unaweza kuonyesha jinsi Ufalme wa Kimesiya unavyotofautiana na ‘ufalme wa Mwana wa upendo wa Mungu,’ unaotajwa katika Wakolosai 1:13, au jinsi unavyotofautiana na “uhudumiaji,” unaotajwa katika Waefeso 1:10. Kuonyesha tofauti zilizoko kati ya mambo hayo kunaweza kufanya wasikilizaji waelewe vizuri fundisho hili muhimu la Biblia.
Yesu alitumia sana mbinu hii ya kufundisha. Alionyesha tofauti iliyoko kati ya jinsi wengi walivyoelewa Sheria ya Musa na kusudi halisi la Sheria. (Mt. 5:21-48) Alionyesha tofauti iliyoko kati ya ujitoaji wa kweli wa kimungu na unafiki wa Mafarisayo. (Mt. 6:1-18) Alionyesha tofauti iliyoko kati ya roho ya wale ‘wanaopiga ubwana’ juu ya wengine na roho ya kujidhabihu ambayo wafuasi wake wangeonyesha. (Mt. 20:25-28) Pindi nyingine, katika Mathayo 21:28-32, Yesu aliwaomba wasikilizaji wake waone wenyewe tofauti iliyoko kati ya kujiona kuwa mwadilifu na toba ya kweli. Hiyo inatufikisha kwenye sehemu nyingine muhimu ya ufundishaji mzuri.
Watie Moyo Wasikilizaji Wafikiri
Kwenye Mathayo 21:28, tunasoma kwamba Yesu aliuliza swali kwanza kabla ya kutoa ulinganifu: “Nyinyi mwafikiri nini?” Mwalimu stadi hasimulii tu mambo wala kujibu maswali. Badala yake, anawatia moyo wasikilizaji wakuze uwezo wa kufikiri. (Mit. 3:21; Rom. 12:1) Njia moja ya kufanya hivyo ni kuuliza maswali. Kama inavyoonyeshwa katika Mathayo 17:25, Yesu aliuliza: “Wewe wafikiri nini, Simoni? Ni kutoka kwa nani wafalme wa dunia hupokea ushuru wa forodhani au kodi ya kichwa? Ni kutoka kwa wana wao au ni kutoka kwa wageni?” Maswali ya Yesu yanayofanya mtu afikiri yalimsaidia Petro afikie uamuzi mzuri juu ya kulipa kodi ya hekalu. Vivyo hivyo, alipokuwa akimjibu mtu aliyeuliza, “Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?” Yesu alionyesha tofauti iliyoko kati ya matendo ya kuhani na Mlawi na tendo la Msamaria mmoja. Kisha akauliza: “Ni nani kati ya watatu hawa aonekana kwako kuwa alijifanya mwenyewe jirani kwa mtu aliyeanguka miongoni mwa wapokonyaji?” (Luka 10:29-36) Na hapa pia, badala ya kufikiri kwa niaba ya msikilizaji wake, Yesu alimwomba ajibu swali lake mwenyewe.—Luka 7:41-43.
Jaribu Kufikia Moyo
Walimu wanaoelewa maana ya Neno la Mungu hutambua kwamba ibada ya kweli si kukariri tu mambo fulani na kufuata sheria fulani. Inategemea uhusiano mzuri na Yehova na kuthamini njia zake. Ibada hiyo inahusu moyo. (Kum. 10:12, 13; Luka 10:25-27) Katika Maandiko, mara nyingi neno “moyo” hurejelea utu wote wa ndani wa mtu, kutia ndani mambo kama tamaa, upendo, hisia, na makusudio yake.
Yesu alijua kwamba Mungu huona moyo wa mtu lakini wanadamu hutazama sura ya nje. (1 Sam. 16:7) Utumishi wetu kwa Mungu unapaswa kuchochewa na upendo wetu kwake, wala si kuchochewa na jitihada za kuvutia wanadamu wenzetu. (Mt. 6:5-8) Kwa upande mwingine, Mafarisayo walifanya mambo mengi kwa kujionyesha. Walisisitiza sana kufuata mambo madogo-madogo ya Sheria na kutii sheria walizotunga wenyewe. Lakini maisha yao hayakudhihirisha sifa ambazo zingeonyesha kwamba wanamfuata Mungu ambaye walidai kumwabudu. (Mt. 9:13; Luka 11:42) Yesu alifundisha kwamba ingawa ni muhimu kutii matakwa ya Mungu, thamani ya utii huo hutegemea yaliyo moyoni. (Mt. 15:7-9; Mk. 7:20-23; Yn. 3:36) Ufundishaji wetu utafanikiwa sana tukiiga mfano wa Yesu. Ni muhimu tuwasaidie watu wajifunze matakwa ya Mungu. Lakini vilevile ni muhimu wamjue Yehova na kumpenda akiwa mtu halisi ili mwenendo wao uonyeshe jinsi wanavyothamini kuwa na uhusiano wenye kukubalika pamoja naye.
Bila shaka, watu wanahitaji kuchunguza yaliyo moyoni mwao ili wafaidike na ufundishaji huo. Yesu aliwatia moyo watu wachunguze nia zao na hisia zao. Alipokuwa akisahihisha maoni yenye kosa, aliwauliza wasikilizaji ni kwa nini walifikiri, kusema au kufanya mambo fulani. Lakini, bila kuwaacha hivyo, Yesu angefuatisha swali lake na jambo, mfano, au tendo ambalo lilifanya waone mambo ifaavyo. (Mk. 2:8; 4:40; 8:17; Luka 6:41, 46) Sisi vilevile tunaweza kuwasaidia wasikilizaji kwa kudokeza wajiulize maswali kama: ‘Kwa nini navutiwa na jambo hili? Kwa nini ninatenda hivi katika hali hii?’ Kisha watie moyo waone mambo kwa maoni ya Yehova.
Onyesha Jinsi Habari Inavyotumika
Mwalimu mzuri anajua kwamba ‘hekima ni bora.’ (Mit. 4:7) Hekima ni uwezo wa kutumia maarifa vizuri ili kusuluhisha matatizo, kuepuka hatari, kufikia miradi, na kusaidia wengine. Ni daraka la mwalimu kuwasaidia wanafunzi kufanya hivyo lakini si kuwafanyia maamuzi. Mnapozungumzia kanuni za Biblia, msaidie mwanafunzi kusababu. Unaweza kutaja hali fulani katika maisha ya kila siku kisha umwulize mwanafunzi jinsi kanuni ya Biblia ambayo mmetoka tu kujifunza inavyoweza kumsaidia iwapo angekabili hali iyo hiyo.—Ebr. 5:14.
Katika hotuba aliyotoa siku ya Pentekoste 33 W.K., mtume Petro aliandaa mfano wa jinsi ya kutumia habari kwa njia inayogusa maisha ya watu. (Mdo. 2:14-36) Baada ya kuzungumzia mafungu matatu ya Maandiko ambayo umati ulidai kuamini, Petro alionyesha jinsi Maandiko hayo yalivyohusiana na matukio ambayo wote walikuwa wameshuhudia. Basi, umati ukaona kwamba kuna uhitaji wa kufuata waliyosikia. Je, watu huitikia hivyo unapowafundisha? Je, unafanya zaidi kuliko kusimulia tu habari na kuwasaidia watu waelewe sababu za mambo? Je, unawatia moyo wafikirie jinsi mambo wanayojifunza yanavyopasa kubadili maisha yao? Huenda wasipaze sauti wakisema, “Tufanye nini?” kama ule umati ulivyofanya wakati wa Pentekoste, lakini ukitumia maandiko vizuri, wao watachochewa kuchukua hatua inayofaa.—Mdo. 2:37.
Enyi wazazi, mnaposoma Biblia pamoja na watoto wenu, hiyo ni nafasi nzuri sana ya kuwazoeza kufikiria njia za kutumia kanuni za Biblia maishani. (Efe. 6:4) Kwa mfano unaweza kuchagua maandiko machache ya usomaji wa Biblia ambayo yameratibiwa juma hilo, uzungumzie maana yake, kisha uulize maswali kama haya: ‘Kanuni hii inatupatia mwongozo gani? Tunaweza kutumiaje maandiko haya katika huduma? Yanafunua nini kuhusu jinsi Yehova anavyofanya mambo, na hilo linajengaje uthamini wetu kwake?’ Tia moyo familia waeleze mambo hayo wakati wa mazungumzo ya mambo makuu ya Biblia katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Inaelekea watatoa maelezo ya maandiko wanayokumbuka.
Weka Mfano Mzuri
Mtu hafundishi kwa maneno tu, bali pia kwa matendo. Matendo yako yanaonyesha mfano wa jinsi ya kutumia mambo unayosema. Watoto hujifunza hivyo. Wanapoiga wazazi wao, wanaonyesha wanataka kuwa kama wazazi wao. Wanataka kujua inakuwaje wanapofanya mambo ambayo wazazi wao hufanya. Hali kadhalika, wale unaowafundisha ‘wanapokuiga, kama vile wewe ulivyo mwigaji wa Kristo,’ wao huanza kupata baraka za kutembea katika njia za Yehova. (1 Kor. 11:1) Wao hujionea jinsi Mungu anavyowatendea.
Hicho ni kikumbusha kizito cha umuhimu wa kuweka mfano mzuri. “Kuwa watu wa namna [ya] matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu” kunasaidia sana wale tunaofundisha waweze kuona mfano wa jinsi ya kutumia kanuni za Biblia. (2 Pet. 3:11) Kama unamtia moyo mwanafunzi wa Biblia asome Neno la Mungu kwa ukawaida, wewe mwenyewe uwe na bidii ya kulisoma. Ukitaka watoto wako wajifunze kutii kanuni za Biblia, hakikisha kwamba matendo yako mwenyewe yanapatana na mapenzi ya Mungu. Kama unatia kutaniko moyo liwe na bidii katika huduma, hakikisha kwamba wewe mwenyewe unashiriki kikamili. Ukitenda kupatana na mafundisho yako, unaweza kuchochea wengine zaidi.—Rom. 2:21-23.
Ukiwa na kusudi la kuboresha ufundishaji wako, jiulize: ‘Ninapofundisha, je, ninafundisha kwa njia inayorekebisha mitazamo, usemi, au matendo ya wasikilizaji? Ili kufanya mambo yawe wazi, je mimi hutofautisha wazo moja au tendo fulani kutokana na jingine? Mimi huwasaidiaje wanafunzi wangu, watoto wangu, au wasikilizaji kwenye mkutano wakumbuke ninayosema? Je, ninawaonyesha wasikilizaji kwa njia iliyo wazi jinsi ya kutumia mambo wanayojifunza? Je, wanaweza kuona mambo hayo katika mfano ninaoweka? Je, wanatambua jinsi itikio lao kwa jambo linalozungumziwa linavyoweza kuathiri uhusiano wao pamoja na Yehova?’ (Mit. 9:10) Endelea kufikiria mambo hayo unapojitahidi kusitawisha uwezo wa kufundisha. “Daima kaza uangalifu kwako mwenyewe na kwa kufundisha kwako. Kaa katika mambo haya, kwa maana kwa kufanya hivi utajiokoa wewe mwenyewe na wale wakusikilizao pia.”—1 Tim. 4:16.