Jua Jinsi Unavyopaswa Kujibu
MASWALI fulani ni kama miamba ya barafu. Sehemu kubwa zaidi imefichika chini ya maji. Sehemu iliyofichika huwa muhimu kuliko swali lenyewe.
Hata kama anayeuliza swali anataka sana kujibiwa, kujua jinsi unavyopaswa kumjibu kunatia ndani kufahamu kadiri utakavyojibu na jinsi utakavyojibu. (Yn. 16:12) Katika hali fulani, kama Yesu alivyoonyesha mitume wake, mtu anaweza kutaka habari ambayo hastahili kujua au ambayo kwa kweli haimfaidi.—Mdo. 1:6, 7.
Maandiko yanatushauri hivi: “Acheni tamko lenu liwe na upendezi sikuzote, lenye kukolezwa chumvi, ili kujua jinsi mpaswavyo kumpa jibu kila mmoja.” (Kol. 4:6) Kwa hiyo, kabla ya kujibu, tunahitaji kufikiria yale tutakayosema na jinsi tutakavyoyasema.
Fahamu Maoni ya Anayeuliza Swali
Masadukayo walijaribu kumnasa Yesu walipomwuliza swali la ufufuo wa mwanamke fulani aliyeolewa mara nyingi. Lakini, Yesu alijua kwamba kwa hakika wao hawaamini ufufuo. Basi alipowajibu, alizingatia maoni yao yenye makosa yaliyochochea swali hilo. Yesu alisababu nao kwa ustadi akitumia simulizi wanalofahamu katika Maandiko, akawaonyesha jambo ambalo hawakupata kamwe kulifikiria awali—uthibitisho wa wazi kwamba kwa kweli Mungu atafufua wafu. Jibu lake liliwashangaza sana wapinzani wake hivi kwamba wakaogopa kumwuliza maswali mengine zaidi.—Luka 20:27-40.
Ili ujue jinsi unavyopaswa kujibu, ni lazima pia ufahamu maoni na mahangaiko ya wale wanaokuuliza maswali. Kwa mfano, mwanafunzi wa darasa lenu au mfanyakazi mwenzako anaweza kukuuliza mbona husherehekei Krismasi. Kwa nini anauliza? Je, kweli anataka kujua sababu, au anauliza tu ili ajue kama unaruhusiwa kujifurahisha? Ili ujue, unaweza kumwuliza kwa nini ameuliza swali hilo. Kisha ujibu kulingana na hali. Kuhusu sherehe hiyo, pia unaweza kutumia fursa hiyo kuonyesha jinsi kufuata mwongozo wa Biblia kunavyotulinda dhidi ya mambo fulani ambayo yamefadhaisha watu na kuwatweza.
Tuseme umealikwa uhutubie kikundi cha wanafunzi juu ya Mashahidi wa Yehova. Baada ya hotuba yako, huenda wakauliza maswali. Maswali yakionekana kuwa manyofu na ya waziwazi, ni bora kutoa majibu rahisi na ya moja kwa moja. Ikiwa wanauliza maswali kuhusu jinsi watu wanavyosema vibaya juu yetu, inaweza kuwa bora kuzungumzia kwanza kwa ufupi mambo yanayoweza kuathiri maoni ya wengi juu ya masuala kama hayo na sababu inayofanya Mashahidi wa Yehova watumie Biblia kuwa kanuni yao. Mara nyingi, kuna faida ya kuyaona maswali hayo kama masuala yanayowahangaisha badala ya kuyaona kuwa vipingamizi—hata kama huenda yamezushwa kwa njia hiyo. Basi, jibu lako linakupa fursa ya kuwaelewesha wasikilizaji, kuwapa habari sahihi, na kuonyesha Maandiko yanayounga mkono imani yetu.
Utamjibuje mwajiri ambaye hataki kukupa ruhusa ya kuhudhuria kusanyiko? Kwanza, jiweke katika hali yake. Je, anaweza kukubali ukijitolea kufanya kazi ya ziada wakati mwingine? Je, anaweza kubadili maoni ukimweleza kwamba maagizo tunayopewa katika makusanyiko hutusaidia kuwa wafanyakazi wanyofu na wenye kutumainiwa? Ukionyesha kwamba unafikiria hali zake, labda atakubali ombi lako kwa sababu anaona hilo ni jambo muhimu maishani mwako. Lakini namna gani kama anataka ufanye jambo lisilo la haki? Onyesha msimamo wako kwa kukataa katakata na kumwonyesha jinsi Maandiko yanavyosema kuhusu jambo hilo. Lakini je, haingekuwa afadhali zaidi kusababu naye kwanza kwamba mtu aliye tayari kusema uongo kwa niaba yake pia anaweza kumdanganya au kumwibia?
Kwa upande mwingine, labda wewe ni mwanafunzi ambaye hataki kushiriki katika utendaji fulani usio wa kimaandiko shuleni. Kumbuka kwamba labda mwalimu ana maoni tofauti na yako, na ana wajibu wa kudumisha nidhamu darasani. Mambo unayokabili ni (1) kufikiria hangaiko lake, (2) kueleza msimamo wako kwa heshima, na (3) kusimama imara kwa jambo unalojua litampendeza Yehova. Ili ufanikiwe zaidi, kuna mengi yanayohitajika kuliko kusema tu mambo unayoamini. (Mit. 15:28) Ikiwa wewe ni kijana, inaelekea babako na mamako watakusaidia kutayarisha mambo ya kusema.
Nyakati nyingine huenda ukalazimika kukanusha mashtaka yanayotolewa na mtu fulani mwenye mamlaka. Afisa fulani wa polisi, wa serikali, au hakimu anaweza kutaka ujibu mashtaka yanayohusu kutii sheria fulani, msimamo wako wa Kikristo wa kutokuwamo, au kushiriki katika sherehe fulani za kizalendo. Utajibuje? Biblia inashauri hivi, “kwa tabia-pole na staha yenye kina kirefu.” (1 Pet. 3:15) Pia, jiulize ni kwa nini masuala hayo yanahangaisha, na ukubali kwa staha hangaiko hilo. Kisha ufanye nini? Mtume Paulo alitaja haki zilizoandaliwa na sheria ya Waroma, wewe pia unaweza kutaja haki zinazoandaliwa na sheria zinazohusu kesi yako. (Mdo. 22:25-29) Labda afisa huyo anaweza kuelewa ukimwambia mambo yanayohusu msimamo uliochukuliwa na Wakristo wa mapema na pia msimamo unaochukuliwa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Au unaweza kutaja jinsi kutii mamlaka ya Mungu kunavyowachochea watu watii sana sheria zinazofaa za wanadamu. (Rom. 13:1-14) Katika hali kama hizo, anaweza kukubali sababu zako za Kimaandiko zinazofanya uchukue msimamo huo.
Anayeuliza Maswali Anaonaje Maandiko?
Unapofikiria jinsi ya kujibu, pia unaweza kufikiria anayeuliza maswali anaonaje Maandiko Matakatifu. Yesu alifanya hivyo alipokuwa akijibu swali la Masadukayo juu ya ufufuo. Kwa kuwa alijua kwamba wao wanakubali tu maandishi ya Musa, Yesu alisababu nao juu ya simulizi fulani la vitabu vya Torati, akianza na maneno haya: “Lakini kwamba wafu wafufuliwa hata Musa alifunua.” (Luka 20:37) Wewe pia unaweza kuona faida ya kunukuu sehemu za Biblia ambazo yule unayeongea naye anakubali na anafahamu.
Lakini namna gani kama yule unayeongea naye haamini Biblia? Ona jinsi mtume Paulo alivyofanya alipotoa hotuba kule Areopago, kama ilivyoandikwa katika Matendo 17:22-31. Aliwaeleza kweli za Kimaandiko bila kunukuu Biblia moja kwa moja. Unaweza kufanya hivyo ikiwa inawezekana. Katika maeneo mengine huenda ikahitajika kuzungumza na mtu mara kadhaa kabla ya kunukuu Biblia moja kwa moja. Unapoelekeza kwenye Biblia, inaweza kuwa jambo la hekima kuonyesha kwanza sababu zinazofanya istahili kuzingatiwa, badala ya kukazia tu kishupavu kwamba ni Neno la Mungu. Lakini, kusudia kutoa ushahidi wa wazi juu ya kusudi la Mungu, na baadaye, kumwacha yule unayeongea naye ajionee mwenyewe mambo yanayosemwa na Biblia. Biblia inagusa moyo kuliko jambo lolote ambalo sisi wenyewe huenda tukasema.—Ebr. 4:12.
Usemi Wako na ‘Upendeze Sikuzote’
Yehova ni mwenye neema, na kwa kufaa watumishi wake wanaambiwa wawe na usemi ‘unaopendeza sikuzote, uliokolezwa chumvi’! (Kol. 4:6; Kut. 34:6) Hiyo inamaanisha kwamba tunapaswa kusema kwa fadhili, hata kama inaonekana haistahili. Usemi wetu unapaswa kuwa mzuri, si mbaya wala usio na busara.
Watu wengi wana mikazo sana, na wanatukanwa kila siku. Tunapowatembelea watu kama hao, huenda wakaongea kwa ukali. Tuwajibuje? Biblia inasema: “Jawabu la upole hugeuza hasira.” Jibu kama hilo linaweza kumtuliza mtu ambaye anapinga. (Mit. 15:1; 25:15) Tabia na sauti yenye fadhili zinaweza kuwavutia sana watu ambao wanapatwa na magumu kila siku hata waweze kusikiliza habari njema tunazowapelekea.
Hatuna haja ya kubishana na watu ambao hawaiheshimu kweli. Badala yake, tamaa yetu ni kutumia Maandiko kusababu na watu ambao watakubali. Hata tukabili hali ipi, tukumbuke kwamba tunapaswa kujibu kwa fadhili na kwa usadikisho kwamba ahadi za Mungu zenye thamani zinategemeka.—1 The. 1:5.
Maamuzi ya Kibinafsi na Masuala Yanayohusu Dhamiri
Mwanafunzi wa Biblia au mwamini mwenzako anapouliza afanyeje katika hali fulani hususa, utamjibuje? Huenda unajua jambo ambalo wewe binafsi ungefanya. Lakini ni lazima kila mtu abebe daraka la maamuzi yake mwenyewe maishani. (Gal. 6:5) Mtume Paulo alieleza kwamba aliwatia moyo watu aliowahubiria ‘watii kwa njia ya imani.’ (Rom. 16:26) Huo ni mfano mzuri tunaopaswa kuiga. Mtu ambaye anafanya maamuzi ili hasa kumpendeza mwalimu wake wa Biblia au kumpendeza mtu mwingine anatumikia wanadamu na haishi kwa imani. (Gal. 1:10) Basi, huenda haifai kumjibu kwa njia rahisi na ya moja kwa moja yule anayeuliza swali.
Basi, unawezaje kujibu kwa njia inayopatana na miongozo ya Biblia? Unaweza kuonyesha kanuni na mifano inayofaa iliyoko katika Biblia. Katika hali nyinginezo, unaweza kumwonyesha jinsi ya kufanya utafiti ili yeye mwenyewe apate kanuni hizo na mifano hiyo. Hata unaweza kuzungumzia kanuni hizo na faida ya mifano hiyo bila kuihusisha na suala mnalozungumzia. Mwulize kama anaona jambo lolote katika kanuni hizo na mifano hiyo linaloweza kumsaidia kufanya uamuzi wenye hekima. Akizingatia kanuni hizo na mifano hiyo, umtie moyo afikirie uamuzi ambao ungemfurahisha Yehova. Kwa njia hiyo unamsaidia ‘kuzoeza nguvu zake za ufahamu kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa pia.’—Ebr. 5:14.
Kutoa Maelezo Katika Mikutano ya Kutaniko
Mara nyingi mikutano ya kutaniko la Kikristo huandaa fursa za kutangaza imani yetu mbele ya watu. Njia mojawapo ya kufanya hivyo ni kutoa maelezo kwa kujibu maswali. Tutoeje maelezo? Tukiwa na tamaa ya kumbariki Yehova, au kusema mema juu yake. Ndivyo alivyofanya mtunga-zaburi Daudi alipokuwa katika “makusanyiko.” (Zab. 26:12) Pia tutoe maelezo kwa njia inayowatia moyo waamini wenzetu, tukiwachochea “kwenye upendo na kazi zilizo bora,” kama mtume Paulo alivyohimiza. (Ebr. 10:23-25) Kujifunza mapema masomo hayo kunaweza kutusaidia kutimiza jambo hilo.
Unapoombwa kutoa maelezo, toa maelezo rahisi, ya wazi, na mafupi. Usizungumzie fungu lote; zungumzia jambo moja tu. Ukitoa sehemu tu ya jibu, wengine pia watapata fursa ya kutoa maelezo ya ziada. Ni jambo lenye faida hasa kutaja maandiko ambayo yameonyeshwa katika habari hiyo. Unapofanya hivyo, jaribu kukazia sehemu ya andiko hilo inayohusu jambo linalozungumziwa. Jifunze kutoa maelezo yako mwenyewe badala ya kusoma fungu moja kwa moja. Usifadhaike kama maelezo yako hayatokei vizuri sana. Kila mmoja anayetoa maelezo hupatwa na hali hiyo mara kwa mara.
Ni wazi kwamba kujua jinsi tunavyopaswa kujibu kunatia ndani mambo mengi kuliko kujua jibu lenyewe. Ufahamu unahitajika. Na inaridhisha kama nini kujibu kutoka moyoni na kugusa mioyo ya wengine!—Mit. 15:23.