Utajibuje?
1. Kwa nini tunapaswa kufuata mfano wa Yesu tunapoulizwa swali?
1 Hadi leo hii, watu wanastaajabishwa na jinsi Yesu alivyojibu maswali kwa ustadi. Tunapoulizwa maswali mbalimbali katika huduma yetu, tunafanya vema kumwiga Yesu tunapoyajibu.—1 Pet. 2:21.
2. Ni nini kinachoweza kutusaidia kujibu swali vizuri?
2 Sikiliza Kabla ya Kujibu: Yesu alizingatia maoni ya yule aliyeuliza swali. Nyakati nyingine itakubidi uulize maswali ili uelewe mtu anataka kujua nini. Kwa mfano, mtu anayeuliza, “Je, unamwamini Yesu?” huenda anataka kujua kwa nini husherehekei Krismasi. Ukitambua sababu hasa inayomfanya mtu aulize swali fulani, unaweza kutoa hoja zako kwa njia bora.—Luka 10:25-37.
3. Tuna vifaa gani vinavyoweza kutusaidia kupata majibu yenye kusadikisha katika Biblia?
3 Tumia Biblia Unapojibu: Kwa kawaida ni vizuri kutumia Biblia unapojibu swali ambalo umeulizwa. (2 Tim. 3:16, 17; Ebr. 4:12) Wengi wameweza kujibu maswali kwa usahihi kwa kutumia kitabu Kutoa Sababu au “Vichwa vya Mazungumzo ya Biblia” katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Hata kama yule anayeuliza swali haamini Biblia, huenda ukaweza kumweleza kwa busara yale ambayo Maandiko yanafundisha. Mtie moyo afikirie kwa uzito maoni yenye hekima ya Biblia ambayo yamethibitika kuwa sahihi. Ukimwiga Yesu unapotoa jibu, majibu yako yatakuwa “kama matunda ya mtofaa ya dhahabu kwenye chombo cha fedha kilichopambwa,” yaani, yenye heshima, yenye kupendeza, na yenye manufaa.—Met. 25:11.
4. Ni katika hali gani ambazo haifai kujaribu kujibu kila swali?
4 Je, Tujibu Kila Swali? Usipojua jibu la swali fulani, usione haya kusema: “Sijui, lakini ninaweza kufanya utafiti kuhusu swali lako, na kurudi ili nikuonyeshe jibu nililopata.” Mwenye nyumba anapoona unyenyekevu wako na kwamba unamjali, huenda akataka urudi. Ukitambua kwamba wale wanaouliza swali ni wapinzani ambao wanataka kubishana, basi mwige Yesu kwa kukatiza mazungumzo kwa heshima. (Luka 20:1-8) Vilevile, iwapo mtu asiyependezwa na kweli anajaribu kukuingiza katika mabishano, katiza mazungumzo kwa upole na utumie wakati wako kuwatafuta watu wenye moyo mweupe.—Mt. 7:6.
5. Yesu aliweka mfano gani kuhusiana na kujibu maswali?
5 Yesu alijua kwamba alihitaji kumtegemea Yehova ili afanikiwe kutimiza utume wake wa ‘kutoa ushahidi juu ya ile kweli,’ na vilevile kujibu maswali ya watu ambao kwa kweli walitaka kupata majibu. (Yoh. 18:37) Tuna pendeleo kubwa sana la kumwiga Yesu kwa kujibu maswali ya wale ‘walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele’!—Mdo. 13:48.