Kuandika Barua
BARUA zimeboresha maisha na tabia za mamilioni ya watu. Awali vitabu vingi vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo vilikuwa barua. Leo, tunaweza kuandika barua ili kuwajenga waamini wapya, kuwasiliana na marafiki, kuwatia moyo akina ndugu na dada ambao wamepata mapendeleo ya kipekee, kuwaimarisha wale wanaokabili magumu, na kupeleka habari zinazohitajiwa kushughulikia utendaji wa kutaniko.—1 The. 1:1-7; 5:27; 2 Pet. 3:1, 2.
Pia kuandika barua ni njia muhimu ya kutoa ushahidi. Katika maeneo mengine, watu wanaishi katika majengo yanayolindwa sana au majengo ya hoteli ambayo si rahisi kufikia. Wengine hawapatikani sana nyumbani, na tunawakosa tunapohubiri nyumba kwa nyumba. Wengine wanaishi sehemu zilizojitenga.
Nyakati fulani ugonjwa, hali mbaya ya hewa, au amri ya kutotoka nje zinaweza kutulazimu kubaki nyumbani. Je, labda unaweza kumwandikia barua mtu wa ukoo au mtu mwingine uliyeongea naye kivivi-hivi na kumtolea ushahidi zaidi? Je, mmojawapo wa wanafunzi wako wa Biblia amehama? Huenda barua yako ikamchochea aendelee kupendezwa na mambo ya kiroho. Au labda unaweza kuandikia watu ambao karibuni wamefunga ndoa, wamepata mtoto, au wamefiwa na wapendwa wao, habari zinazofaa za Kimaandiko.
Kutoa Ushahidi kwa Barua
Unapoandika barua ili kumtolea ushahidi mtu ambaye hujapata kukutana naye, kwanza jitambulishe. Unaweza kueleza kwamba unashiriki kazi ya kujitolea inayofanywa ulimwenguni pote. Kama inafaa, taja kwamba wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Umjulishe kwa nini unamwandikia barua badala ya kumtembelea binafsi. Andika kana kwamba unaongea naye uso kwa uso. Na pia kwa kufuata mwelekezo wa ‘kujithibitisha wenyewe kuwa wenye hadhari kama nyoka na bado kuwa wasio na hatia kama njiwa,’ fikiria kwa uzito kadiri unavyopaswa kujitambulisha.—Mt. 10:16.
Taja katika barua hiyo jambo ambalo ungalimwambia kama ungalimtembelea. Unaweza kutumia utangulizi mmoja unaopatikana katika kitabu Kutoa Sababu au utangulizi mmoja wa Kimaandiko unaopatikana katika toleo la karibuni la Huduma Yetu ya Ufalme. Unaweza kuuliza swali na kumtia moyo alifikirie. Wahubiri wengine hueleza tu kwamba tuna programu ya kujibu maswali ya Biblia bila malipo kisha wanataja baadhi ya sura za kimojawapo cha vichapo vyetu vya mafunzo. Barua ya mfano inayoonyesha jinsi ya kutoa ushahidi iko kwenye ukurasa wa 73. Inaweza kukuonyesha mambo fulani ya kuandika, lakini ni vizuri kuandika juu ya mambo tofauti-tofauti. Ama sivyo, baada ya muda watu wataanza kupokea barua ileile mara nyingi.
Watu wengine hawapendi kusoma barua ndefu iliyoandikwa na mtu ambaye hawamjui. Basi inaweza kuwa jambo la hekima kuandika barua fupi ili isimchoshe yule unayemwandikia. Ingefaa kutia ndani mwaliko uliochapwa wa kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Unaweza kutia ndani trakti, broshua, au Mnara wa Mlinzi au Amkeni! na ueleze kwamba anaweza kupokea vichapo hivyo kwa ukawaida ikiwa anataka. Au unaweza kumwomba umtembelee nyumbani kwake ili uzungumze naye zaidi juu ya habari uliyoandika.
Tahadhari Kuhusu Kutumia Fomu
Tazama ile barua ya mfano. Ona mambo yafuatayo: (1) Inaonekana nadhifu, si shaghalabaghala. (2) Hata bahasha ikipotea, mtu aliyepokea barua hiyo bado ana jina na anwani ya mwenye kuituma. (3) Kusudi la barua hii limetajwa kwa njia rahisi na ya moja kwa moja katika fungu la kwanza. (4) Kila jambo kuu linatajwa katika fungu tofauti. (5) Tukifikiria kusudi la hiyo barua, hiyo si barua ya kivivi-hivi tu wala si rasmi sana.
Katika barua rasmi zaidi, kama zile ambazo mwandishi wa kutaniko hutumia ofisi ya tawi, jina la kutaniko linapasa kuonyeshwa, hali kadhalika jina la mwandishi, anwani yake, na tarehe. Jina na anwani ya mtu au shirika ambalo linatumiwa barua hiyo zinapaswa kuonyeshwa pia. Kisha salamu zinazofaa hufuata. Kumalizia barua, katika lugha mbalimbali maneno kama “Ni mimi wako mwaminifu” au “Ni mimi” huandikwa juu ya jina lako. Andika jina lako kwa mwandiko wako mwenyewe.
Katika barua yoyote, zingatia mwendelezo mzuri wa maneno, sarufi, vituo na, bila shaka, unadhifu. Hizo zitafanya barua yako iheshimiwe pamoja na ujumbe wake.
Kwenye bahasha, sikuzote andika anwani unayotaka atumie kukujibu—labda anwani yako mwenyewe ya posta. Ukihisi kwamba si hekima kuandika anwani yako unapowatolea ushahidi kwa barua watu usiowajua, uwaombe wazee kama wanaweza kukubali utumie anwani ya Jumba la Ufalme. Anwani ya Watch Tower Society isitumiwe kamwe, kwa sababu inaweza kudhaniwa kwa makosa kwamba ni ofisi ya Sosaiti iliandika barua yako na hali hiyo inaweza kusababisha mvurugo. Anwani ya mwandikaji isipoonyeshwa ilhali kichapo kimetiwa ndani, hiyo pia inaweza kufanya ionekane kwa makosa kwamba ni Sosaiti iliyoiandika.
Hakikisha kwamba umeweka stampu za kutosha, hasa kama umetia ndani kichapo fulani. Kama stampu haitoshi, yule uliyemtumia barua hiyo anaweza kutozwa pesa fulani, na hiyo inaweza kumfanya asisikilize ujumbe wetu. Kumbuka kwamba katika nchi nyingi, broshua au magazeti yanapotiwa ndani ya barua, ada ya posta hupanda kuliko barua tupu.
Hali ya Barua
Baada ya kumaliza kuandika barua, uisome na kuchanganua yaliyomo. Inasikikaje? Je, ni ya kirafiki na ina maneno ya busara? Tunaposhughulika na wengine, sisi hujaribu kuonyesha upendo na fadhili pamoja na sifa nyinginezo. (Gal. 5:22, 23) Ukigundua kidogo mambo yasiyofaa, rekebisha maneno yake.
Barua inaweza kufika sehemu ambazo wewe huwezi. Hiyo pekee inafanya iwe chombo muhimu katika huduma. Kwa kuwa barua zako zinakuwakilisha pamoja na itikadi zako, fikiria maneno yake, unadhifu wake, na jinsi inavyosikika. Inaweza kuanzisha, kuimarisha, au kumtia moyo mtu atembee kwenye barabara ya uhai.