Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • be funzo 30 uku. 186-uku. 189 fu. 4
  • Kupendezwa na Wengine

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kupendezwa na Wengine
  • Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Habari Zinazolingana
  • Kuonyesha Kupendezwa Kibinafsi na Wengine
    Huduma Yetu ya Ufalme—1991
  • Pendezwa Kibinafsi na Wengine
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Jinsi ya Kuboresha Stadi za Mazungumzo
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Jitahidi Kugusa Moyo
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
Pata Habari Zaidi
Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
be funzo 30 uku. 186-uku. 189 fu. 4

SOMO LA 30

Kupendezwa na Wengine

Unahitaji kufanya nini?

Unahitaji kuonyesha kwamba unajali maoni na hali za watu wengine.

Kwa Nini Ni Muhimu?

Hiyo ni mojawapo ya njia za kuiga upendo wa Yehova, na inaweza kutusaidia kugusa moyo wa mtu.

MBALI na kuwafundisha watu kweli za Biblia, kuna mambo tunayohitaji kufanya. Ni lazima tuvutie mioyo yao. Mojawapo ya njia za kuvutia mioyo ya watu ni kupendezwa sana nao. Tunaweza kuonyesha upendezi huo kwa njia kadhaa.

Fikiria Maoni ya Wasikilizaji. Mtume Paulo alifikiria malezi na maoni ya wasikilizaji. Alieleza hivi: “Kwa Wayahudi nilipata kuwa kama Myahudi, ili niweze kuwapata Wayahudi; kwa wale walio chini ya sheria nilipata kuwa kama aliye chini ya sheria, ingawa mimi mwenyewe siko chini ya sheria, ili niweze kuwapata wale walio chini ya sheria. Kwa wale wasio na sheria nilipata kuwa kama aliye bila sheria, ijapokuwa mimi siko bila sheria kuelekea Mungu bali niko chini ya sheria kuelekea Kristo, ili niweze kuwapata wale wasio na sheria. Kwa walio dhaifu nilipata kuwa dhaifu, ili niweze kuwapata walio dhaifu. Nimekuwa mambo yote kwa watu wa namna zote, ili nipate kwa vyovyote kuokoa wengine. Lakini nafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili nipate kuwa mshiriki wayo pamoja na wengine.” (1 Kor. 9:20-23) Tunawezaje ‘kuwa mambo yote kwa watu wa namna zote’ leo?

Ukiwatazama wengine hata kwa muda mfupi tu kabla ya kuongea nao, unaweza kuona dalili za mapendezi yao na hali zao. Je, unaweza kutambua kazi zao? dini zao? na hali za familia yao? Kulingana na hali unazoona, je, unaweza kufanya mahubiri yako yawavutie zaidi?

Ili mahubiri yako yavutie, unahitaji kufikiria mapema jinsi utakavyowafikia watu katika eneo lenu. Katika maeneo mengine, unahitaji kuwafikiria pia watu ambao wametoka nchi za kigeni. Ikiwa watu kama hao wanaishi katika eneo lenu, je, umepata njia bora ya kuwahubiria? Kwa kuwa mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli,” basi kusudi lako liwe kutangaza ujumbe wa Ufalme kwa njia inayowavutia watu wote unaokutana nao.—1 Tim. 2:4.

Sikiliza kwa Makini. Ingawa Yehova ana uwezo wa kujua mambo yote anayotaka kujua, yeye huwasikiliza wengine. Nabii Mikaya alipokea njozi fulani, na katika njozi hiyo Yehova aliwaomba malaika watoe maoni juu ya njia ya kushughulikia jambo fulani. Kisha Mungu akaruhusu mmojawapo wa hao malaika afuate maoni aliyotoa. (1 Fal. 22:19-22) Abrahamu alipohangaika kuhusu hukumu ya Sodoma, Yehova alimsikiliza kwa fadhili. (Mwa. 18:23-33) Tunawezaje kuiga mfano wa Yehova wa kusikiliza tunapokuwa katika huduma?

Waruhusu wengine watoe maoni. Uliza swali linalofaa, kisha utue kwa muda unaowatosha kujibu. Sikiliza vizuri. Kuwafikiria kwa njia hiyo kutawafanya wazungumze kwa uhuru zaidi. Kama majibu yao yanadokeza jambo fulani linalowapendeza, basi endelea kuuliza maswali kwa njia ya busara. Jaribu kuwafahamu zaidi bila kufanya mazungumzo yawe kama mahoji. Wapongeze sana kwa sababu ya maoni yao. Hata kama hukubaliani nao, uwe mwenye fadhili unapozungumzia maoni yao.—Kol. 4:6.

Lakini tujihadhari ili kupendezwa kwetu na watu wengine kusivuke mpaka. Kuwajali watu wengine si kuingilia mambo yao ya kibinafsi. (1 Pet. 4:15) Tunahitaji kutahadhari ili mtu wa jinsia tofauti asielewe vibaya upendezi wenye fadhili tunaomwonyesha. Tunahitaji kutumia utambuzi kwa sababu kile kinachoonwa kuwa upendezi unaofaa hutofautiana katika kila nchi, na hata kwa kila mtu.—Luka 6:31.

Kufanya matayarisho kunaweza kukusaidia kuwa msikilizaji mzuri. Ujumbe wetu ukiwa wazi akilini mwetu, tunakuwa watulivu na tunaweza kuwasikiliza wengine kwa njia ya kawaida. Hiyo inafanya wastarehe na kuwa huru zaidi kuzungumza nasi.

Ni tendo la heshima kuwasikiliza wengine. (Rom. 12:10) Inathibitisha kwamba tunathamini maoni yao na hisia zao. Wanaweza kutusikiliza kwa makini zaidi tukiwaonyesha heshima. Ndiyo sababu Neno la Mungu linatushauri tuwe ‘wepesi sana juu ya kusikia, wa polepole juu ya kusema.’—Yak. 1:19.

Wasaidie Wengine Wafanye Maendeleo. Ikiwa tunawajali wengine, tutaendelea kuwafikiria wale wanaopendezwa na kuwatembelea tena ili kuwafundisha kweli za Biblia zinazotimiza mahitaji yao. Unapofikiria ziara inayofuata, kumbuka mambo uliyopata kujua juu yao katika ziara za awali. Tayarisha habari zinazohusu hali zao. Kazia jinsi wanavyoweza kutumia habari hiyo maishani, ukiwasaidia kuona jinsi wanavyoweza kufaidika na mambo wanayojifunza.—Isa. 48:17.

Ikiwa yule unayezungumza naye anakuambia jambo fulani au tatizo fulani ambalo linamtatiza, hiyo ni nafasi nzuri ya kumhubiria habari njema. Iga mfano wa Yesu ambaye nyakati zote alikuwa tayari kufariji wale waliosononeka. (Mk. 6:31-34) Usitoe suluhisho la haraka-haraka wala usitoe mashauri ya kijuu-juu tu. Mtu huyo anaweza kufikiri hupendezwi naye. Badala yake mwonyeshe huruma. (1 Pet. 3:8) Kisha fanya utafiti katika vichapo vyetu vinavyotegemea Biblia, na umpe habari zenye kumjenga za kumsaidia kukabili hali hiyo. Bila shaka, hutafunua siri zake ikiwa unamjali kwa upendo, ila tu kuwe na sababu nzuri za kuzifunua.—Mit. 25:9.

Tupendezwe hasa na wanafunzi wetu wa Biblia. Fikiria kupitia sala mahitaji ya kila mwanafunzi, na utayarishe funzo ukikumbuka mahitaji hayo. Jiulize, ‘Yeye anahitaji kufanya nini ili aendelee kufanya maendeleo ya kiroho?’ Kwa upendo, msaidie mwanafunzi kufahamu mambo ambayo Biblia na vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” vinasema juu ya jambo hilo. (Mt. 24:45) Nyakati nyingine haitoshi tu kumweleza jambo. Inaweza kufaa kumwonyesha mwanafunzi jinsi ya kutumia kanuni fulani ya Biblia, hata kufanya jambo fulani pamoja naye linaloonyesha jinsi ya kutumia kanuni hiyo.—Yn. 13:1-15.

Unahitaji usawaziko na busara unapowasaidia wengine wafuate kanuni za Yehova maishani mwao. Watu wana malezi tofauti-tofauti na uwezo mbalimbali, na maendeleo yao hutofautiana. Basi, uwe na usawaziko kuhusu maendeleo yao. (Flp. 4:5) Usiwalazimishe kubadili maisha zao. Acha Neno la Mungu na roho yake iwachochee. Yehova anapenda watu wamtumikie kwa hiari, si kwa kulazimishwa. (Zab. 110:3) Epuka kuwapa maoni yako mwenyewe kuhusu maamuzi ambayo wanapaswa kujifanyia, na hata kama wanakuuliza, uwe mwangalifu usiwafanyie maamuzi.—Gal. 6:5.

Toa Msaada Unaofaa. Ingawa Yesu alijali sana hali ya kiroho ya wasikilizaji wake, pia alitambua mahitaji yao mengine. (Mt. 15:32) Hata kama sisi si matajiri, tunaweza kuwasaidia kwa njia nyinginezo nyingi.

Kupendezwa na wengine kunafanya tuwajali. Kwa mfano, kama hali ya hewa inamsumbua mtu unayezungumza naye, nendeni mahali panapofaa zaidi, au panga uendeleze mazungumzo wakati mwingine. Ukimtembelea mtu wakati usiofaa, mwambie utarudi baadaye. Kama jirani au mtu mwingine anayependezwa ni mgonjwa au amelazwa hospitalini, onyesha unamjali kwa kumpelekea kadi au barua fupi au umtembelee. Ikifaa, unaweza pia kumpelekea chakula chepesi au kumtendea fadhili nyinginezo.

Wanafunzi wa Biblia wanapozidi kufanya maendeleo, wanaweza kuwa na upweke fulani kwa sababu sasa hawatumii wakati mwingi na rafiki zao wa zamani kama walivyozoea kufanya. Uwe rafiki yao. Zungumza nao baada ya funzo la Biblia na nyakati nyinginezo. Watie moyo kuwa na mashirika mazuri. (Mit. 13:20) Wasaidie kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Keti nao mikutanoni, na uwasaidie kushughulikia watoto wao ili wote waweze kufaidika kabisa na mikutano.

Pendezwa na Watu Kutoka Moyoni. Kupendezwa na watu ni sifa ya moyoni wala si ustadi ambao mtu anajifunza. Kadiri tunavyopendezwa na wengine huonekana katika njia nyingi. Jinsi tunavyosikiliza na pia jambo tunalosema huonyesha kwamba tunapendezwa na wengine. Upendezi huo huonyeshwa na fadhili na jinsi tunavyowajali wengine. Hata wakati hatusemi au kutenda jambo fulani, mtazamo wetu na ishara za uso huonyesha kama tunapendezwa. Ikiwa kwa kweli tunawajali wengine, kwa wazi watatambua tunawajali.

Sababu muhimu zaidi ya kupendezwa sana na wengine ni kwamba tunaiga upendo na rehema ya Baba yetu wa mbinguni. Hiyo inawasaidia wale wanaotusikiliza wawe na uhusiano wa karibu na Yehova na kufanya wapendezwe na ujumbe ambao ametupa tutangaze. Basi, unapohubiri habari njema, jaribu kufikiria ‘si masilahi ya kibinafsi ya mambo yako mwenyewe tu, bali pia masilahi ya kibinafsi yale ya wengine.’—Flp. 2:4.

JINSI YA KUPENDEZWA KIKWELI NA WENGINE

  • Sikiliza mtu mwingine anapozungumza. Mshukuru kwa kueleza maoni yake na hisia zake. Uliza maswali ili umwelewe vizuri.

  • Baada ya kuzungumza na mtu huyo, mfikirie. Mtembelee upesi baadaye.

  • Mfundishe kweli za Biblia ambazo zinatimiza mahitaji yake.

  • Msaidie kwa njia mbalimbali. Fikiria mahitaji yake ya wakati huu na ya baadaye.

MAZOEZI: (1) Kabla ya mkutano wa kutaniko, pendezwa na mtu fulani ambaye amehudhuria. Usimsalimu tu. Jaribu kumfahamu vizuri. Onyesha unamjali. Uwe na mazoea ya kufanya hivyo. (2) Ukiwa katika utumishi wa shambani, pendezwa na mtu unayekutana naye. Usimhubirie tu. Jaribu kumjua vizuri. Jaribu kufanya mambo unayosema na kutenda yafaane na hali unazojua kumhusu. Endelea kutafuta nafasi za kufanya hivyo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki