Pendezwa Kibinafsi na Wengine
“Mkiangalia, si upendezi wa kibinafsi juu ya mambo yenu wenyewe tu, bali pia upendezi wa kibinafsi juu ya yale ya wengine.”—WAFILIPI 2:4, NW.
1, 2. Ni nini baadhi ya sababu za kupendezwa kibinafsi na wengine?
SISI tuna sababu nzuri za kupendezwa kibinafsi na wengine. Mathalani, twapaswa kupendezwa na wanadamu wenzetu kwa sababu twatofautiana mtu na mwingine. Vifaa vilivyofanyiza chembe za urithi-tabia katika mwili wetu vina ramani iliyochorwa jinsi umbo letu la urithi-tabia lingekuwa. Ramani hiyo yatofautiana sana mtu na mtu hivi kwamba mashirika yenye kupeleleza uhalifu yameongezea “alama za vidole” kwenye mbinu zao mbalimbali za kuwatambua wahusika.
2 Kuna sababu nyingine ambazo hufanya sisi tutofautiane na tuwe wenye kupendeza tukiwa watu mmoja mmoja. Kuanzia wakati wa kuchukuliwa mimba, sisi hupasishwa kupatwa na uvutano wa mazingira yetu. Kuna ushuhuda mwingi wa kwamba vitoto visivyozaliwa huitikia mambo yenye kutendeka nje ya tumbo la uzazi. Halafu, tukiisha kuingia ulimwenguni tukiwa wapumuaji wenye kujitegemea, au nafsi, mielekeo na njia za wazazi wetu hutuathiri. Tuwapo tukikua, huenda ikawa ni sisi tulio mtoto wa pekee au huenda wengine wakajiunga nasi kuwa ndugu na dada zetu na sisi tushiriki kuwatunza. Kuwa na ushirika huo au kutokuwa nao kuna matokeo fulani juu ya ukuzi wetu. Pia mambo tusomayo, tufundishwayo shuleni, na tutazamayo katika televisheni hutia uvutano pia katika mawazo na vitendo vyetu.
3. Kupatana na Wafilipi 2:4, twapaswa kuwa na upendezi gani hasa katika wengine?
3 Kwa hiyo, basi, utofautiano wetu huendeleza upendezi fulani katika mtu na mwingine. Lakini sababu ya kupendezwa na wengine ambayo mtume Paulo alikuwa akifikiria ni ya hali ya juu zaidi. Hivyo, yeye alihimiza Wakristo wenzake wawe ‘wakiangalia, si upendezi wa kibinafsi juu ya mambo yao wenyewe tu, bali pia upendezi wa kibinafsi juu ya yale ya wengine pia.’ (Wafilipi 2:4, NW] Badala ya kutafuta faida yetu wenyewe, yatupasa hasa tupendezwe kiroho na wengine. Basi, ni nini baadhi ya njia ambazo sisi twapendezwa na wengine kibinafsi hivyo?
Upendezi wa Kiroho na Tofauti za Kiutu
4. Kulingana na Waefeso 4:22-24, ni mabadiliko gani huongezea kupendezwa kwetu kiroho na wengine?
4 Kupendezwa kwetu kiroho na wengine huongezeka tutumiapo kibinafsi maarifa ya ukweli wa Kimaandiko na kujifunza kujipatanisha na kigezo chenye kulingana na kielelezo cha Yesu Kristo. (1 Petro 2:21) Sisi Wakristo wa kweli, ‘twavua utu wa kale wenye kufanana na namna ya mwenendo wetu wa zamani’ na badala ya huo twajitahidi kuwa na “utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.” (Waefeso 4:22-24, NW] Hivyo, badala ya mielekeo ya ubinafsi sisi twaonyesha hangaikio lenye fadhili na la kufikiria hali za wengine.—Isaya 65:25.
5. Kwa nini kuna nyutu tofauti-tofauti katika kundi la Kikristo, hiyo ikichochea swali gani?
5 Ingawa mabadiliko ya kiutu yamekuwa makubwa miongoni mwa watu wa Yehova, maelekeo yenye dhambi yangali yamebakia. Hata Paulo alikiri hivi: “Nitakapo kufanya lifaalo, lililo baya lipo pamoja nami.” (Warumi 7:21, NW) Bila shaka, kuna tabia nyingine za kurithi na za kujipatia wenyewe, nazo ndizo hututambulisha. Watu fulani wana silika ya kuvutiwa upesi na mambo ya usanifu mwingi, hali wengine hawaamui ubora wa mambo kabla ya kuyachanganua-changanua kindani. Ijapokuwa watu fulani ni wanyamavu na wenye kujikalia peke yao, wengine ni wenye kuchangamana sana na watu na hujitokeza kwenda kufanya urafiki. Basi, je! muungamano wa kundi la Kikristo utadumishwaje katikati ya tofauti hizo za kiutu?
6. Twapaswa kuwa na maoni gani juu ya tofauti za kiutu, nawe ungetoaje kielezi cha jambo hili?
6 Ikiwa tutaonyesha kupendezwa kiroho na wengine na kuhifadhi muungamano wa Kikristo, ni lazima tuyaone mambo kama yalivyo hasa na kuwa wenye uelewevu. Kwa kuwa Mungu hatokezi takwa la kwamba sisi tuwe na ukamilifu, wala sisi hatupaswi kuudai kwa washirika wetu Wakristo. Zaidi ya hilo, Yehova hatarajii watumishi wake wote wafanane kabisa. Katika kundi la Kikristo, sisi sote tuna mahali patufaapo na twaweza kutumia uwezo wetu mbalimbali tuliopewa na Mungu kwa kurithi ili tuendeleze kazi yake. (1 Wakorintho 12:12-26) Tukiendelea na shughuli nyingi za jasho tukiwa chini ya mwelekezo wa Kichwa cha kundi, Yesu Kristo, hatutakuwa na wakati wa kutazamana kwa njia ya uchambuzi. (1 Wakorintho 4:1-4) Kama vile fundi ajuavyo, kila chombo kimeundwa kwa umbo la kufanya kazi fulani. Je! nyundo yaweza kutoboa lile tundu laini sana ambalo keekee (drili) hutoboa? Je! randa ambayo hutumiwa kufanyiza umbo zuri la ubao yaweza kupigilia skrubu ndani yao? Sivyo, kwa maana kila chombo kina utumizi ukifaacho.
7. Tushirikipo utumishi wa Ufalme pamoja, ni jambo gani ambalo twapaswa kuliweka kwanza kabisa akilini?
7 Ni ya kweli kama nini maneno ya ule wimbo wa Ufalme “Utumishi Wenye Furaha”! Huo huhimiza hivi: “Kwa furaha tutumikie Mungu, kwa vipawa hata ujuzi wetu.” Ni kweli, huenda tusiwe tuna uwezo wa kutokeza. Hata hivyo, jambo la kwanza kabisa ambalo twaweka akilini ni ile kazi tuliyogawiwa tukiwa Mashahidi wa Yehova nasi twajitoa kuifanya kwa moyo wote. Kama vile wimbo huo uongezeavyo: “Hata kazi ndogo yahakikisha moyo kamili, pendo, twaonyesha.”—Mwimbieni Yehova Sifa, wimbo 130.
Waone Wengine Kuwa Bora
8. Muungamano huendelezwaje kwa kutumia aliyosema Paulo kwenye Wafilipi 2:1-3?
8 Muungamano huendelezwa pia kwa kuwaona wengine kuwa bora kuliko wewe mwenyewe. Paulo aliandika hivi: “Ikiwa, basi, kuna kitia-moyo chochote katika Kristo, ikiwa kuna uliwazo wowote wa upendo, ikiwa kuna ushirikiano wowote wa roho, ikiwa kuna shauku nyororo na huruma zozote, fanyeni shangwe yangu iwe kamili katika jambo la kwamba nyinyi ni wa akili ile ile na mna upendo ule ule, mkiunganishwa pamoja katika nafsi, mkishika lile wazo moja akilini.” Angalia kwamba mtume aongezea hivi: “Mkiwa hamfanyi jambo lolote kwa ushindani wala kwa kujivuna, bali kwa udhalili wa akili mkiona kwamba wengine ni bora kuliko nyinyi.”—Wafilipi 2:1-3, NW.
9. Yamaanisha nini kuwa mwenye ushindani na majivuno, na twaweza kuepukaje vitabia hivi?
9 Kwa kutofikiria wengine kuwa bora, mtu mwenye ushindani huonyesha “elekeo la kinyume lenye kushikiliwa sana na lenye kuchosha sana la kuwa na magomvi na mabishano.” (Webster’s New Collegiate Dictionary) Huenda kitabia hiki kikajidhihirisha katika majadiliano kuhusu maneno.” (1 Timotheo 6:4, NW) Kwa uhakika, jambo la kuhangaikiwa zaidi ni kuangalia ni roho ya namna gani yenye kusababisha maneno na mawazo yaliyo katika maneno hayo. Kwa hiyo epuka kuwa mkwamiliaji wa maneno fulani yaliyotumiwa kwa mdomo au katika maandishi. Na namna gani ukitokezewa maoni tofauti kuhusu imani fulani? Ukiwa na uaminifu mshikamanifu ambatana na habari za Kimaandiko zenye kuandaliwa kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 24:45-47) Ingawaje, hivyo ndivyo tulivyojifunza ukweli hapo kwanza. Kutambua hivyo hutusaidia kuepuka kuwa wenye majivuno, yaani, kujihisi tukiwa watu wa maana kupita kiasi.
Sitawisha Kupendezwa Kibinafsi na Wengine
10. Ni utumizi gani wa Wafilipi 2:4 wapasa kufanywa katika kundi?
10 Kumbuka kwamba Paulo alituhimiza ‘tuangalie, si upendezi wa kibinafsi juu ya mambo yetu wenyewe tu, bali pia upendezi wa kibinafsi juu ya yale ya wengine.’ (Wafilipi 2:4, NW) Hii yamaanisha nini? Sawa na vile kuwa na macho yenye wepesi wa kung’amua hali ya mazingira yetu kwaweza kutusaidia katika huduma ya shambani, ndivyo kupendezwa na hali njema ya wengine katika kundi kutatutolea fursa ya kuimarisha sana kifungo cha upendo ambacho hutuunganisha. Hasa wazee wana daraka la kuwaonyesha waamini wenzao hangaikio, kwa maana mithali moja yataarifu hivi: “Fanya bidii kuijua hali ya makundi yako.” (Mithali 27:23) Bila shaka, sisi sote twaweza na twapaswa kuwa na uangalifu wa kuona mahitaji ya waamini wenzetu.—1 Petro 2:17.
11. Kwa nini twahitaji kuwa na uangalifu wenye makini tuongeapo na ndugu na dada zetu wa kiroho?
11 Njia nyingine ya kuendeleza muungamano na kukuza kupendezwa na wengine ni kuchukua wakati wa kuwasiliana vema pamoja na ndugu na dada zako wa kiroho. Pata kujua wanafikiria nini. Jambo hili laweza kufanywa uzurupo makao yao, kabla na baada ya mikutano kwenye Jumba la Ufalme, na katikati ya vipindi vya makusanyiko yetu. Nawe sikiliza kwa uangalifu wanenapo. Huenda hii ikamaanisha kwamba tutasikia habari za magumu wayakabiliyo, lakini hata ikiwa hivyo huenda tukaweza kuwasaidia kubeba mizigo yao na hivyo tutimize sheria ya Kristo. (Wagalatia 6:2) Hata hivyo, jambo fulani zaidi ya kuongea na ndugu zetu litalinda salama muungamano wa kundi. Nini hilo?
Dhihirisha Hisia-Mwenzi
12. Kwa nini yatupasa tudhihirishe hisia-mwenzi?
12 Hisia-mwenzi pia huendeleza muungamano wa Kikristo. Huku mibano ya maisha ikiongezeka, sisi sote twahitaji kudhihirisha sifa hii. Tusikazanie sana jambo ambalo twafikiria akilini hivi kwamba tushindwe kufikiria hisia za wengine. Kwa kielelezo: Wakati ule ule ambapo mshiriki mmoja wa programu alipokuwa akiwasili kwa ajili ya Mkutano wa Utumishi, mzee mmoja alinena naye haraka-haraka kuhusu jambo fulani la kutangazwa. Mzee huyo akashangaa na kuaibika wakati mshirika yule alipomtazama, akatabasamu, na kusema: “Kwanza, Ndugu, habari ya jioni!” Jambo lile la kutangazwa lilizungumzwa walipokwisha kupeana salamu za kirafiki na baada ya ndugu yule kustareheshwa mawazo. Lo, mzee huyo alijifunza somo lililoje! Usiwe mwenye haraka mno, hivyo ukipuuza hisani ambazo hufanya uhusiano wako na wengine ufurahishe.
13. Hisia-mwenzi husukuma wazee kufanya nini katika kushughulika pamoja na washirika wao Wakristo?
13 Hisia-mwenzi husukuma wazee waonyeshe huruma na vitabia vingine vizuri. Nyakati fulani, ni lazima wanaume hawa wawe wanana, “kama vile [mama] mlezi awatunzavyo watoto wake mwenyewe.” (1 Wathesalonike 2:7) Kusaidia watu fulani mmoja mmoja hutaka saburi nyingi na tegemezo lenye upendo. Wale ambao ‘wameacha upendo wao wa kwanza’ huenda wakahitaji kuchochewa kwenye utendaji mkubwa zaidi na huenda wakahitaji msaada ili wathamini uharaka wa nyakati zetu. (Ufunuo 2:4; 2 Timotheo 4:2; Waebrania 6:11, 12) Kama Paulo, wazee wana “shauku nyororo” kwa washirika Wakristo, wakiwapa mawaidha na kuwaliwaza ‘kwa kusudi la kwamba wao wapaswa kuendelea kutembea kwa njia yenye kustahiki Mungu.’—1 Wathesalonike 2:8, 11, 12.
14. Paulo alionyesha ushuhuda gani wa kwamba yeye alikuwa na hisia-mwenzi?
14 Paulo aliachia wazee kielelezo kizuri cha jinsi ya kuonyesha hangaiko kwa hali njema ya ndugu na dada za kiroho. Aliandika hivi: “Zaidi ya mambo yale ya aina ya kinje-nje, kuna kile ambacho chaingia kasi juu yangu siku baada ya siku, ule wasiwasi kwa ajili ya makundi yote.” Kwa sababu Paulo alikuwa na hangaiko hilo, angeweza kuuliza hivi: “Ni nani aliye dhaifu, nami je! si dhaifu? Ni nani aliyekwazwa, nami je! sikuchukizwa sana?” Ikiwa wewe ni mzee, je! una hisia-mwenzi ya jinsi hiyo?—2 Wakorintho 11:28, 29, NW.
Kumpata Ndugu Yako
15. Magumu mazito yatokeapo kati ya akina ndugu, ni shauri gani la Yesu kwenye Mathayo 18:15 lapasa kufuatwa, na shabaha yapasa kuwa nini?
15 Kuonyesha hisia-mwenzi huendeleza muungamano miongoni mwa watumishi wa Yehova. Hata hivyo, huenda tofauti za kiutu zikatokea katika pindi chache. Iwapo mambo ya hali nzito yahusika, Wakristo wapaswa wafuate shauri la Yesu lililoandikwa kwenye Mathayo 18:15-17. Angalia hatua ya kwanza. Ni kuongea na ndugu yako kwa faragha ili ‘ukafunue kosa lake.’ Shabaha yako yapasa kuwa nini? Naam, ni ‘kumpata ndugu yako’! Yesu alisema hivi: “Ikiwa yeye anakusikiliza wewe, umempata ndugu yako.” Jambo la kufurahisha ni kwamba, kwa kawaida kuongea faraghani hutosha kurudisha mahusiano yenye amani kati yako na mwabudu mwenzako wa Yehova.
16. Ni jambo gani lapasa kufanywa ukiona kwamba ndugu yako ana kitu fulani dhidi yako?
16 Ukiona kwamba ndugu yako ana kitu dhidi yako, fuata shauri la Yesu ‘upatane kwanza na ndugu yako.’ (Mathayo 5:24) Ongeeni juu ya tatizo hilo kwa njia ya utulivu na fadhili, kila mmoja akijaribu kuelewa maoni ya mwenzake. Kwa njia hii, kwa kawaida jambo hilo laweza kutatuliwa na amani ya kundi yaweza kudumishwa.
Kuwapata Wasioamini
17, 18. Paulo aliwapa shauri gani wake Wakristo wenye kuishi katika nyumba zilizogawanyika kidini?
17 Moja ya hali zilizo ngumu zaidi ya kutumilia kanuni za Kimaandiko ni ndani ya nyumba iliyogawanyika kidini. Wakristo wengi hufanya kazi ya jasho kwa uaminifu huku wakikabiliana na hali zenye kuwavuruga mawazo na wakiwa na magumu yenye kusababishwa na ukosefu wa muungamano wa kiroho katika ndoa yao. Wao waweza kusaidiwaje?
18 Kwa sababu ya kupendezwa kibinafsi na wengine, wazee huterema kuwaandalia msaada wa kiroho wale wanaoishi katika nyumba zilizogawanyika kidini. Mathalani, huenda uangalifu ukaelekezwa kwenye shauri la Petro kuhusu mwenendo wa wake Wakristo katika hali hii. Yeye awaambia wajitiishe kwa waume zao, hata ikiwa hawa ni wasioamini na ‘hawatii lile neno.’ Kwa nini wawe katika ujitiisho? “Ili kwamba . . . wapate kuvutwa [au, kupatwa] bila hata neno moja kupitia mwenendo wa wake zao.” (1 Petro 3:1; Kingdom Interlinear) Lakini kutumia shauri hili kuna matokeo gani?
19. Toa kielelezo cha kuonyesha manufaa ya kufuata 1 Petro 3:1.
19 Mwanamke mmoja ambaye jina lake ni Vera akiri kwamba alipopata kuwa Mkristo hapo mwanzoni, yeye aliambia-ambia mume wake kuhusu ukweli wa Biblia, na mume wake akachoshwa kabisa na jambo hilo. Mwanamke huyo aongezea kwamba, “kwa kufuata ushauri wa Kimaandiko uliopokewa kutoka kwa mzee, niliamua kwamba ilikuwa afadhali kuwa mwenye busara na kungojea fursa zenye kupendeleka zijitokeze zenyewe.” Kwa msingi, Vera alifuata 1 Petro 3:1, ingawa kwa kadiri fulani alichukua hatua ya kwanza kuchochea mume wake, Barry, wazungumze kanuni za Biblia. Baadaye mume huyo alieleza hivi: “Muda wa miaka ile, niliona kwamba Amkeni! [jarida lililo andamani la Mnara wa Mlinzi] lilitapakaa hapa na pale nyumbani katika sehemu zisizo za kawaida. Lilikuwa na habari zenye kutumika vizuri na nyakati fulani lilisema mambo kabla hayajatokea katika [vyombo vya] habari.” Tokeo ni kwamba, baada ya miaka 20 ya kutoungamana, Barry na Vera wana furaha wakiwa wameungamana katika utumishi wa Yehova.
20. Ni msaada gani ambao wazee waweza kuwapa waume Wakristo katika nyumba zilizogawanyika kidini?
20 Mume mwamini hukabili magumu makubwa ikiwa mke wake hupinga Ukristo wa kweli na huvuta watoto wao wawe dhidi yake. Kwa kupendezwa kibinafsi na mwanamume wa jinsi hiyo, wazee waweza kuvuta uangalifu kwenye kanuni za Biblia zenye kusaidia. Mathalani, yaweza kuonyeshwa wazi kwamba mke wake ajapokuwa mwenye upinzani, yeye mume ndiye kichwa cha jamaa na apaswa kuwapa watoto wake maagizo ya Kimaandiko. (Waefeso 6:4) Aweza kuhimizwa akae pamoja na mke wake “kulingana na maarifa,” akionyesha upendezi katika mambo ambayo afanya na kumsaidia kazi za nyumbani na kutunza watoto. (1 Petro 3:7, NW) Juu ya yote, mume na baba mwamini apaswa atiwe moyo kuweka njia za mawasiliano zikiwa wazi ili ajue kilichomo katika moyo wa kila mshiriki wa jamaa yake. Wazee waweza pia kumtia moyo ajaribu kusaidia mke wake kwa maneno ‘yaliyokolezwa munyu,’ akimtolea ukweli wa Kimaandiko kwa busara katika pindi zifaazo.—Wakolosai 4:6.
21. Mke asiyeamini angeweza kusaidiwaje awe na upendezi katika ukweli?
21 Nyakati fulani kuonyesha upendezi katika watu wa ukoo wa Wakristo katika nyumba zilizogawanyika kidini huamsha itikio kwenye ujumbe wa Ufalme. Kwa kutoa kielezi: Mwanamume mmoja Mkristo alivunjika moyo kwa sababu mke wake alikuwa amempinga vikali kwa miaka kadhaa. Mzee mmoja alijitolea kuwatembelea na kusaidia kwa mazungumzo ya Biblia. Alipowasili kwenye kao lile, mzee alisalimu mke yule kwa njia ya kufurahisha na kuuliza hivi: “Ungependa kuketi katika mazungumzo yetu?” Mwaliko huo wa kirafiki ulivutia mwanamke huyo hata akaterema kujiunga katika mazungumzo yale. Muda si muda alikubali ukweli na kuanza kuhubiria wengine.
22. Kwa nini kupendezwa kibinafsi katika mtu na mwenzake?
22 Basi, sisi Mashahidi wa Yehova acheni “tufanye mambo yote kwa ajili ya zile habari njema.” (1 Wakorintho 9:23, NW) Kwa kweli, “tukiwa bado na wakati, tuwatendee watu wote mema, na hasa ndugu wa imani yetu.” (Wagalatia 6:10, HNWW) Na tupendezwe kibinafsi na mtu na mwenzake ili kwamba upendo usitawi sana katika udugu wetu wa ulimwenguni pote.
Wewe Ungejibuje?
◻ Kwa nini, hasa, twapaswa kupendezwa na wengine?
◻ Twaweza kukuzaje upendezi wa kibinafsi katika waamini wenzetu?
◻ Wazee waweza kuonyeshaje hisia-mwenzi?
◻ Ni nini chaweza kutokana na kupendezwa kwetu kibinafsi na wasio waamini?
[Picha katika ukurasa wa 16, 17]
Kama vile kila chombo kimeundwa kwa umbo la kufanya kazi fulani, ndivyo wote katika kundi la Kikristo wawezavyo kutumia uwezo wao mbalimbali waliopewa na Mungu ili wasogeze mbele kazi ya Mungu
Ili kuendeleza muungamano wa Kikristo, pendezwa kibinafsi na wengine
[Picha katika ukurasa wa 18]
Paulo aliachia wazee kielelezo kizuri cha jinsi ya kuwaonyesha waamini wenzao hangaiko lenye upendo