Je, Una Roho Isiyoweza Kufa?
JE, KUNA maisha baada ya kifo? Swali hilo limewatatanisha wanadamu kwa miaka mingi sana. Watu wa kila jamii wamefikiria mno swali hilo miaka nenda miaka rudi, nao wamebuni imani mbalimbali.
Kotekote ulimwenguni kutia ndani eneo la Pasifiki huko Polinesia, Melanesia, na Mikronesia, watu wengi huamini kwamba “roho” huendelea kuishi baada ya mtu kufa. Je, kweli mtu ana kitu fulani kinachotoka mwilini na kuendelea kuishi baada ya mwili kufa? Roho iliyo katika mtu aliye hai ni nini? Roho hiyo huenda wapi tunapokufa? Neno la Mungu lililopuliziwa, Biblia, hutoa majibu ya kweli na yenye kuridhisha kwa maswali hayo.
Roho Ni Nini?
Katika Biblia, maneno yanayotafsiriwa “roho” humaanisha “pumzi.” Lakini hilo halimaanishi kupumua tu. Kwa mfano, mwandishi wa Biblia Yakobo asema hivi: “Mwili bila roho umekufa.” (Yakobo 2:26) Kwa hiyo, roho hufanya mwili uwe hai.
Kani hiyo ya uhai haiwezi kuwa pumzi tu, au hewa, inayoingia mapafuni. Kwa nini? Kwa sababu mtu anapokoma kupumua, chembe za mwili huendelea kuwa hai kwa muda mfupi—kichapo The World Book Encyclopedia chasema “kwa muda wa dakika kadhaa.” Ndiyo sababu jitihada za kumhuisha mtu zinaweza kufaulu. Na ndiyo sababu viungo vya mwili vinaweza kupachikwa mwilini mwa mtu mwingine. Lakini mara tu kani hiyo ya uhai inapotoka kwenye chembe za mwili, jitihada zote za kuhuisha ni za bure. Wakati huo pumzi haiwezi kwa vyovyote kuhuisha hata chembe moja. Kwa hiyo, roho ni kani ya uhai isiyoonekana—cheche ya uhai—inayoendeleza uhai katika chembe. Kani hiyo ya uhai huendelezwa kwa kupumua.—Ayubu 34:14, 15.
Je, ni wanadamu tu walio na roho hiyo? Biblia hutusaidia kupata jibu sahihi kwa swali hilo. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Ni nani ajuaye kama roho ya binadamu huenda juu, na kama roho ya mnyama huenda chini?” (Mhubiri 3:21) Kwa hiyo, Biblia inasema kwamba wanyama na wanadamu wana roho. Inawezekanaje?
Roho, au kani ya uhai inaweza kulinganishwa na umeme unaoingia katika mashine au kifaa cha umeme. Vifaa mbalimbali vinavyotumia nguvu za umeme vinaweza kutenda kazi tofauti-tofauti. Kwa mfano, jiko la umeme ni chombo kinachopasha moto, kompyuta inaweza kutayarisha habari na kupiga hesabu, nayo televisheni inaweza kuonyesha picha na kutoa sauti. Lakini, umeme huo hauwi kamwe na umbo na sifa za kifaa kinachotumia nguvu za umeme. Umeme huo haubadiliki, hubaki ukiwa nguvu. Vivyo hivyo, kani ya uhai haichukui sifa zozote za kiumbe aliye hai. Kani hiyo haina utu wala haiwezi kufikiri. Wanadamu na wanyama “wanayo pumzi moja.” (Mhubiri 3:19) Kwa hiyo, mtu anapokufa roho yake haiendelei kuishi kwingineko ikiwa kiumbe wa roho.
Basi wafu wako katika hali gani? Na roho huenda wapi mtu anapokufa?
“Nawe Mavumbini Utarudi”
Mtu wa kwanza, Adamu, alipoasi kimakusudi amri ya Mungu, Yehova alimwambia hivi: “Kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” (Mwanzo 3:19) Adamu alikuwa wapi kabla hajaumbwa na Yehova kwa mavumbi? Hakuwa popote! Hakuwapo. Kwa hiyo Yehova Mungu alipomwambia Adamu kwamba ‘angeirudia ardhi,’ alimaanisha kwamba Adamu angekufa. Adamu hangeenda kuishi kwenye makao ya roho. Wakati wa kifo angepoteza uhai na kurudia hali ya kutokuwapo. Alihukumiwa kifo—kutokuwa na uhai—wala si kuhamishwa kwa makao mengine.—Waroma 6:23.
Vipi wengine waliokufa? Hali ya wafu inaelezwa waziwazi kwenye Mhubiri 9:5, 10, tunaposoma hivi: “Wafu hawajui kitu . . . Hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima ndani ya kaburi.” (Zaire Swahili Bible) Hivyo basi, kifo ni hali ya kutokuwapo. Mtunga-zaburi aliandika kwamba mtu anapokufa, “pumzi yake hutoka, huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.”—Zaburi 146:4.
Kwa wazi, wafu hawana fahamu, hawatendi. Hawajui jambo lolote. Hawawezi kukuona, kukusikia, wala kuongea nawe. Hawawezi kukusaidia wala kukudhuru. Bila shaka hupaswi kuhofu wafu. Lakini roho ‘humtokaje’ mtu anapokufa?
Roho ‘Humrudia Mungu’
Biblia yasema kwamba mtu anapokufa, ‘roho humrudia Mungu aliyeitoa.’ (Mhubiri 12:7) Je, hilo lamaanisha kwamba kitu fulani cha roho husafiri kihalisi angani hadi kwa Mungu? La hasha! Neno ‘rudia’ halirejezei kusafiri kihalisi kutoka sehemu moja hadi nyingine kila mara linapotumiwa katika Biblia. Kwa mfano, Waisraeli wasio waaminifu waliambiwa hivi: “Nirudieni mimi, nami nitawarudia ninyi, asema BWANA wa majeshi.” (Malaki 3:7) Waisraeli wangeweza ‘kumrudia’ Yehova kwa kuacha kabisa mwenendo mbaya na kuishi tena kupatana na njia ya Mungu ya uadilifu. Na Yehova angeweza ‘kuwarudia’ Waisraeli kwa kuwakubali tena watu wake. Katika visa vyote viwili ‘kurudia’ kulihusisha mtazamo, wala si kusafiri kihalisi kutoka sehemu moja hadi nyingine.
Vivyo hivyo, roho ‘inapomrudia’ Mungu wakati wa kifo, haisafiri kihalisi kutoka duniani hadi mbinguni. Kumbuka kwamba roho ni kani ya uhai. Mara tu roho hiyo inapomtoka mtu, ni Mungu peke yake anayeweza kuirudisha. Kwa hiyo, roho ‘humrudia Mungu’ katika maana ya kwamba tumaini lolote la mtu huyo la kuishi wakati ujao sasa humtegemea Mungu tu.
Kwa mfano, fikiria kile ambacho Maandiko yanasema kuhusu kifo cha Yesu. Mwandishi wa kitabu cha Luka aeleza hivi: “Yesu akaita kwa sauti kubwa na kusema: ‘Baba, ndani ya mikono yako naikabidhi roho yangu.’ Alipokuwa amesema hilo, akaisha.” (Luka 23:46) Roho ya Yesu ilipokuwa ikimtoka, yeye hakuwa akisafiri kihalisi kwenda mbinguni. Yesu alifufuliwa kutoka kwa wafu baada ya siku ya tatu. Naye alipaa mbinguni baada tu ya siku 40. (Matendo 1:3, 9) Hata hivyo, wakati wa kifo chake, Yesu aliacha roho yake mikononi mwa Baba yake, akiwa na uhakika kabisa kwamba Yehova angeweza kumfufua.
Naam, ni Mungu tu anayeweza kumfufua mtu. (Zaburi 104:30) Hilo ni tumaini zuri kama nini!
Tumaini Hakika
Biblia yasema: “Saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake [Yesu] na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Naam, Yesu Kristo aliahidi kwamba wote walio katika kumbukumbu la Yehova watafufuliwa, au wataishi tena. Badala ya matangazo ya kuhuzunisha ya vifo, kutakuwapo ripoti za shangwe za wale waliofufuliwa. Itafurahisha kama nini kuwakaribisha wapendwa kutoka kaburini!
Je, ungependa kujua mengi kuhusu jinsi unavyoweza kunufaishwa na tumaini hili linaloahidiwa na Mungu? Twakualika uandike ukitumia mojawapo ya anwani zilizoorodheshwa hapa chini na kuomba nakala ya broshua Roho za Wafu—Je! Zaweza Kukusaidia au Kukuumiza? Je! Ziko Kweli?
Isipokuwa imeonyeshwa vingine, manukuu ya Maandiko ya Kiebrania ni kutoka katika Union Version ya Kiswahili chapa ya 1994, na manukuu ya Maandiko ya Kigiriki ni kutoka katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.