Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • wt sura 3 kur. 23-31
  • Lishike kwa Mkazo Neno la Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Lishike kwa Mkazo Neno la Mungu
  • Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wasaidie Wengine Waithamini
  • Usomaji Wetu wa Biblia
  • Kusudi Letu
  • Kunufaika kwa Usomaji wa Biblia Kila Siku
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Usomaji wa Biblia—Wenye Kufaidi na Wenye Kupendeza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Biblia—Kitabu Kinachofaa Kusomwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Jitahidi Uwe Msomaji Mzuri
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
Pata Habari Zaidi
Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
wt sura 3 kur. 23-31

Sura Ya Tatu

Lishike kwa Mkazo Neno la Mungu

1. (a) Waisraeli wa kale waliuonaje ukweli wa neno la Mungu? (b) Kwa nini hilo linatupendeza?

“NANYI nyote mnajua mioyoni mwenu, na rohoni mwenu, ya kuwa halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena BWANA, Mungu wenu, katika habari zenu; yote yametimia kwenu.” (Yoshua 23:14-16) Hivyo ndivyo Yoshua alivyowaambia wazee wa Israeli baada ya kuingia katika Nchi ya Ahadi. Naam, ahadi za Yehova zilitimia. Simulizi hilo—na Biblia nzima—lilihifadhiwa kwa ajili yetu ili “tupate kuwa na tumaini.”—Waroma 15:4.

2. (a) Biblia ‘imepuliziwa na Mungu’ katika maana gani? (b) Kujua kwamba Biblia imepuliziwa na Mungu kunatupatia daraka gani?

2 Yehova ndiye Mtungaji wa Biblia ingawa aliwatumia wanadamu 40 hivi kuiandika. Je, hilo lamaanisha kwamba aliwaelekeza kuandika kila jambo lililo katika Biblia? Ndiyo. Alitumia roho yake takatifu ambayo ni nguvu yake ya utendaji. Mtume Paulo alisema kweli aliposema hivi: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu . . . ili mtu wa Mungu apate kuwa hodari, aliyeandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.” Watu wote wanaoamini jambo hilo huitii Biblia na kufuata mafundisho yake maishani mwao.—2 Timotheo 3:16, 17; 1 Wathesalonike 2:13.

Wasaidie Wengine Waithamini

3. Ni njia gani iliyo bora kabisa ya kuwasaidia watu wengi wasioamini kwamba Biblia ni Neno la Mungu?

3 Watu wengi tunaozungumza nao hawaamini kwamba Biblia ni Neno la Mungu. Tunawezaje kuwasaidia? Mara nyingi njia bora ya kuwasaidia watu hao ni kufungua Biblia na kuwaonyesha yaliyomo. ‘Neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili na linaweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo.’ (Waebrania 4:12) “Neno la Mungu” liko hai wala si hadithi tu! Ahadi za Biblia hutimia kikamili. Ujumbe wa Biblia una nguvu za kuuchochea kabisa moyo wa mtu kuliko jambo lolote tunaloweza kusema.

4. Ni kweli zipi za Biblia zimebadili maoni ya watu fulani kuihusu, na kwa nini?

4 Watu wengi wameamua kujifunza Biblia kwa undani baada ya kuona jina la Mungu ndani yake. Wengine waliamua kujifunza Biblia walipoonyeshwa inavyosema kuhusu kusudi la uhai, kwa nini Mungu ameruhusu uovu, maana ya matukio ya sasa, au tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani. Katika nchi ambazo watu wamesumbuliwa na roho waovu kwa sababu ya mazoea ya kidini, wengi wamevutiwa na maelezo ya Biblia kuhusu chanzo cha tatizo hilo na jinsi ya kupata kitulizo. Kwa nini watu wanyofu wanavutiwa na maelezo hayo? Kwa sababu ni Biblia tu ndiyo inayosema ukweli kuhusu mambo hayo muhimu sana.—Zaburi 119:130.

5. (a) Ni sababu zipi ambazo huenda zinawafanya watu wasiiamini Biblia? (b) Tunaweza kuwasaidiaje watu hao?

5 Lakini vipi watu wakituambia kwamba hawaiamini Biblia? Je, mazungumzo yetu yaishie hapo? Tutasababu nao ikiwa wako tayari kufanya hivyo. Labda wanaiona Biblia kuwa kitabu cha Jumuiya ya Wakristo. Huenda watu wengi wanaikataa Biblia kwa sababu ya unafiki wa Jumuiya ya Wakristo na jinsi ambavyo imejiingiza katika siasa na zoea lake la kuomba-omba pesa. Huenda ikafaa kuwauliza iwapo wanaikataa Biblia kwa sababu hizo. Labda wanaweza kupendezwa wakijua kwamba Biblia inashutumu mazoea ya kilimwengu ya Jumuiya ya Wakristo, na kwamba kuna tofauti kati ya Jumuiya ya Wakristo na Wakristo wa kweli.—Mika 3:11, 12; Mathayo 15:7-9; Yakobo 4:4.

6. (a) Ni jambo gani linalokuthibitishia wewe kwamba Biblia ni Neno la Mungu? (b) Ni hoja gani nyingine tunazoweza kutumia kuwasaidia watu waone kwamba kwa kweli Biblia ni Neno la Mungu?

6 Wengine wanaweza kupendezwa wanapoonyeshwa waziwazi mambo yanayothibitisha kwamba Biblia imepuliziwa na Mungu. Ni jambo gani linalokuthibitishia wewe kwamba Biblia ni Neno la Yehova Mungu? Je, ni maelezo ya Biblia kuhusu chanzo chake? Au ni kwa sababu ina unabii mwingi sana kuhusu mambo ya wakati ujao, unabii ambao ulitoka kwa mwenye uwezo unaozidi wa wanadamu? (2 Petro 1:20, 21) Je, ni kwa sababu vitabu vyote vya Biblia vinapatana vizuri sana vijapoandikwa na watu 40 walioishi katika muda unaozidi miaka 1,600? Au ni kwa sababu Biblia ni sahihi kisayansi tofauti na vitabu vingine vya kale? Au je, ni unyofu wa waandishi wake? Au ni kwa sababu imehifadhiwa licha ya jitihada kubwa za kuiharibu? Unaweza kuwasaidia wengine kwa kutumia jambo lolote ambalo limekuvutia.a

Usomaji Wetu wa Biblia

7, 8. (a) Tunapaswa kufanya nini na Biblia? (b) Tunahitaji nini mbali na kusoma Biblia kibinafsi? (c) Wewe binafsi umepataje kuelewa makusudi ya Yehova?

7 Mbali na kuwasaidia wengine waiamini Biblia, tunapaswa kuisoma kwa ukawaida. Je, unafanya hivyo? Biblia ni kitabu muhimu sana kuliko vitabu vinginevyo vyote vilivyowahi kuandikwa. Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba inatosha tu kujisomea Biblia tukiwa peke yetu. Maandiko yanatuonya tusijitenge. Tusifikiri kwamba tunaweza kuelewa kila jambo kwa kujifanyia utafiti wetu wenyewe. Ni lazima tujifunze kibinafsi na kuhudhuria mikutano ya watu wa Mungu kwa ukawaida ili tuwe Wakristo wenye usawaziko.—Mithali 18:1; Waebrania 10:24, 25.

8 Biblia inatuambia juu ya afisa mmoja Mwethiopia ambaye alikuwa anasoma unabii wa Isaya. Malaika alimwelekeza mweneza-evanjeli Mkristo anayeitwa Filipo amwulize mtu huyo hivi: “Je, wewe kwa hakika wajua unayosoma?” Kwa unyenyekevu, Mwethiopia huyo akajibu: “Kwa kweli, ningewezaje kufanya hivyo, isipokuwa mtu fulani angeniongoza?” Alimsihi Filipo amfafanulie Maandiko hayo. Filipo hakuwa msomaji wa Biblia mwenye kujitegemea, aliyetoa tu maoni yake kuhusu Maandiko. Alishirikiana sana na tengenezo la Mungu linaloonekana. Ndiyo sababu aliweza kumsaidia Mwethiopia huyo kufaidika na mafundisho ambayo Yehova alitoa kupitia tengenezo hilo. (Matendo 6:5, 6; 8:5, 26-35) Hali moja leo, hakuna mtu anayeweza kueleza kwa usahihi makusudi ya Yehova bila msaada. Sote tunahitaji msaada ambao Yehova anatoa kwa upendo kupitia tengenezo lake linaloonekana.

9. Sote tunaweza kufaidika na mpango gani wa kusoma Biblia?

9 Tengenezo la Yehova linatupatia vichapo vyenye habari bora sana za Kimaandiko ili kutusaidia kuielewa Biblia. Isitoshe, tumepangiwa ratiba ya kusoma Biblia kwa ukawaida katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inayofanywa katika makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni. Unaweza kupata faida kubwa sana kwa kujichunguzia Maandiko Matakatifu. (Zaburi 1:1-3; 19:7, 8) Jitahidi sana kuisoma Biblia kwa ukawaida. Hata ingawa huenda usifahamu kikamili kila jambo, utafaidika sana ukijua mambo yaliyo katika Biblia kwa ujumla. Kwa mfano, ukisoma kurasa nne au tano tu kwa siku, unaweza kuimaliza Biblia nzima kwa muda wa mwaka mmoja hivi.

10. (a) Unasoma Biblia wakati gani? (b) Ni nani wengine wanaopaswa kushiriki usomaji wa Biblia, na kwa nini ni muhimu kuisoma kwa ukawaida?

10 Unaweza kuisoma Biblia wakati gani? Utafaidika sana ukitenga hata dakika 10 au 15 kila siku. Ikiwa haiwezekani, panga ratiba ya kusoma Biblia kwa ukawaida kila juma, na ufuate ratiba hiyo. Wale ambao wamefunga ndoa wanaweza kuwasomea wenzi wao Biblia kwa sauti. Iwapo mna watoto wanaoweza kusoma, wanaweza kuwa na zamu za kuisoma Biblia kwa sauti. Usomaji wa Biblia unapasa kuwa zoea la kila siku, kama kula chakula. Kama ujuavyo, afya ya mtu inaweza kudhoofika asipokula chakula cha kutosha. Ndivyo ilivyo na afya yetu ya kiroho. Tutaishi milele ikiwa tu tutapata kwa ukawaida “kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.”—Mathayo 4:4.

Kusudi Letu

11. Tunapaswa kusoma Biblia tukiwa na kusudi gani?

11 Tunapaswa kusoma Biblia tukiwa na kusudi gani? Kusudi letu halipasi kuwa kumaliza tu sehemu fulani. Kusudi letu linapasa kuwa kumjua Mungu vizuri zaidi ili tuweze kumpenda zaidi na kumwabudu kwa njia anayokubali. (Yohana 5:39-42) Tunapaswa kuwa na mwelekeo kama wa mwandishi wa Biblia aliyesema: “Ee BWANA, unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako.”—Zaburi 25:4.

12. (a) Kwa nini kupata “ujuzi sahihi” ni muhimu, na huenda mtu akahitaji kutia jitihada gani ili kupata ujuzi huo anaposoma Biblia? (b) Ni hoja gani nne tunazoweza kutumia kuchanganua kwa manufaa Maandiko tunayosoma? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 30.) (c) Tumia njia hizo unapojibu maswali yaliyo kwenye fungu hili. Soma maandiko yaliyotajwa bila kunukuliwa.

12 Tunapofundishwa na Yehova, tunapaswa kuwa na hamu ya kupata “ujuzi sahihi.” Bila ujuzi sahihi hatuwezi kamwe kutumia Neno la Mungu ifaavyo maishani mwetu au kuwafundisha wengine kwa usahihi. (Wakolosai 3:10; 2 Timotheo 2:15) Ili kupata ujuzi sahihi, tunahitaji kuisoma kwa makini, na kusoma tena na tena sehemu zisizoeleweka kwa urahisi ili tuelewe maana yake. Tutafaidika pia tukitafakari na kufikiria njia mbalimbali tunazoweza kutumia habari tunayosoma. Hoja nne tunazoweza kutumia zimeonyeshwa kwenye ukurasa wa 30. Unaweza kuchanganua kwa manufaa Maandiko mengi kwa kutumia baadhi ya hoja hizo. Utaona jinsi unavyoweza kufanya hivyo unapojibu maswali yaliyo kwenye kurasa zifuatazo.

(1) Mara nyingi, Maandiko unayosoma yanaweza kukufundisha jambo fulani kumhusu Yehova. Kwa mfano, Zaburi 139:13, 14, inatuonyesha jinsi Mungu anavyowajali sana watoto ambao hawajazaliwa: “Uliniunga tumboni mwa mama yangu. Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu na nafsi yangu yajua sana.” Uumbaji wa Yehova ni wa ajabu sana! Mungu ametuumba kwa njia inayoonyesha kwamba anatupenda sana.

Kulingana na Yohana 14:9, 10, tunaposoma jinsi Yesu alivyoshughulika na wengine, ni kana kwamba tunaona jinsi ambavyo Yehova mwenyewe angetenda. Hivyo basi, masimulizi ya Luka 5:12, 13 na Luka 7:11-15 yanatufunza nini kumhusu Yehova?

(2) Fikiria jinsi yale unayosoma yanavyohusiana na habari kuu ya Biblia: kutetewa kwa haki ya Yehova ya kutawala na kutakaswa kwa jina lake kupitia Ufalme wa Yesu Kristo, Mbegu aliyeahidiwa.

Ezekieli na Danieli walikaziaje habari kuu ya Biblia? (Ezekieli 38:21-23; Danieli 2:44; 4:17; 7:9-14)

Biblia inaonyeshaje waziwazi kwamba Yesu ndiye Mbegu aliyeahidiwa? (Wagalatia 3:16)

Kitabu cha Ufunuo kinasimuliaje upeo mtukufu wa habari kuu ya Ufalme? (Ufunuo 11:15; 12:7-10; 17:16-18; 19:11-16; 20:1-3; 21:1-5)

(3) Jiulize jinsi unavyoweza kutumia habari unayosoma. Kwa mfano, kuanzia kitabu cha Kutoka hadi Kumbukumbu la Torati tunasoma kuhusu ukosefu wa adili na uasi wa Waisraeli. Twajifunza kwamba matendo na mielekeo hiyo ilikuwa na matokeo mabaya. Hilo linatuhimiza tumfurahishe Yehova kwa kutoiga mfano mbaya wa Waisraeli. “Mambo hayo yaliendelea kuwapata kuwa vielelezo, nayo yaliandikwa kuwa onyo kwetu sisi ambao juu yetu miisho ya mifumo ya mambo imewasili.”—1 Wakorintho 10:11.

Kisa cha Kaini kumwua Abeli kinatufundisha nini? (Mwanzo 4:3-12; Waebrania 11:4; 1 Yohana 3:10-15; 4:20, 21)

Je, shauri la Biblia kwa Wakristo wenye tumaini la kwenda mbinguni linawafaa wale wanaotumaini kuishi milele duniani? (Hesabu 15:16; Yohana 10:16)

Hata ingawa tuna sifa nzuri katika kutaniko la Kikristo, kwa nini tunapaswa kufikiria jinsi tunavyoweza kutumia kikamili shauri la Biblia ambalo tayari tunajua? (2 Wakorintho 13:5; 1 Wathesalonike 4:1)

(4) Fikiria jinsi unavyoweza kutumia habari unayosoma kuwasaidia wengine. Watu wote wanahangaikia afya yao, kwa hiyo tunaweza kuwasomea miujiza ya Yesu ambayo inaonyesha mambo atakayofanya duniani kote akiwa Mfalme mwenye nguvu wa Ufalme wa Mungu: “Umati mkubwa ukamkaribia yeye, ukiwa pamoja na watu waliokuwa vilema, walioharibika viungo, walio vipofu, mabubu, na wengi wa hali tofauti, . . . naye akawaponya.”—Mathayo 15:30.

Unaweza kutumia kisa cha kufufuliwa kwa binti ya Yairo kuwasaidia watu gani? (Luka 8:41, 42, 49-56)

13. Matokeo yatakuwa nini tukiendelea kusoma na kujifunza Biblia kwa msaada wa tengenezo la Yehova?

13 Usomaji wa Biblia unakuwa wenye kujenga sana tunapotilia maanani mambo manne yaliyotajwa hapo juu. Kwa kweli, kusoma Biblia kunahitaji jitihada. Lakini kunaweza kutufaidi maisha yetu yote, kwa sababu kadiri tunavyosoma Maandiko ndivyo tutakavyoimarika kiroho. Tukisoma Biblia kwa ukawaida, tutamkaribia zaidi Baba yetu mwenye upendo, Yehova, na ndugu zetu Wakristo. Kutatusaidia kutii shauri la “kushika kwa mkazo neno la uhai.”—Wafilipi 2:16.

[Maelezo ya Chini]

a Ili kujua kwa nini tunapaswa kujifunza Biblia, ona broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Mazungumzo ya Kurudia

• Kwa nini Biblia iliandikwa na kuhifadhiwa hadi leo?

• Tunaweza kuwasaidiaje wengine waithamini Biblia?

• Kwa nini kusoma Biblia kibinafsi kwa ukawaida kunafaidi? Ni hoja gani nne tunazoweza kutumia kuchanganua kwa manufaa habari tunayosoma?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 30]

UNAPOSOMA MAANDIKO FULANI YA BIBLIA, FIKIRIA

Yale ambayo habari hiyo inakufundisha kumhusu Yehova

Jinsi yanavyohusiana na habari kuu ya Biblia

Jinsi unavyoweza kutumia habari hiyo maishani mwako

Jinsi unavyoweza kutumia habari hiyo kuwasaidia wengine

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki