Biblia—Kitabu Kinachofaa Kusomwa
NI RAHISI kuishiwa maneno ya sifa mtu anapoongea juu ya Biblia. Ndicho kitabu kilichogawanywa zaidi katika historia yote, kikishinda vingine kwa mbali sana. Biblia ndicho kitabu cha kale zaidi, chenye kutafsiriwa zaidi, chenye kunukuliwa zaidi, chenye uvutano zaidi, na chenye kustahiwa zaidi ya vyote. Labda pia ndicho kitabu chenye kubishaniwa zaidi ya vyote. Na kwa hakika ndicho kitabu ambacho kimeokoka zaidi marufuku, uchomaji, na upinzani wenye jeuri. Lakini inasikitisha kwamba kuna sifa moja ambayo haiwezi kutumiwa tena juu ya Biblia. Haielekei kuwa kitabu chenye kusomwa zaidi ulimwenguni.
Ingawa watu waweza kuwa na Biblia mahali fulani katika nyumba, watu wengi huhisi kwamba wana shughuli nyingi mno wasiweze kuchukua wakati hasa wa kuisoma. Zamani watu wengi walipenda kusoma wakati wa kupumzika. Hata hivyo, siku hizi watu walio wengi wanapendelea kutumia wakati wao wa ziada kutazama televisheni au kufanya kitu kingine. Wale ambao bado husoma kidogo kwa kawaida hupendelea kusoma kitu kisichohitaji bidii na kilicho rahisi. Kusoma Biblia huhitaji kukazia akili, na siku hizi watu walio wengi hawakazi akili sana kwenye mambo wanayosoma.
Lakini, Biblia haikuokoka ili tu ibaki kwenye rafu zetu za vitabu. Kuna sababu nzuri zinazofanya ifae kusomwa. Ebu fikiria mambo fulani kuihusu.
Si Ajabu Kwamba Ilivumilia!
Neno “Biblia” latokana na neno la Kigiriki bi·bliʹa, linalomaanisha “vitabu vidogo.” Jambo hilo latukumbusha kwamba Biblia imefanyizwa na vitabu kadhaa—vingine vikiwa si vidogo sana! Viliandikwa kwa muda unaozidi miaka elfu moja mia sita. Ingawa waandikaji walikuwa wanaume, walipuliziwa na Chanzo cha juu zaidi. Mwandikaji mmoja wa Biblia alisema hivi: ‘Unabii haukuletwa po pote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa kwa roho takatifu.’ (2 Petro 1:21) Jinsi unabii wa Kimaandiko ulivyo kweli ndivyo ilivyo na sehemu nyingine za Biblia. “Vitabu [hivyo] vidogo” vyenye kupuliziwa kimungu vimejaa mawazo ya juu sana ya Yehova Mungu. (Isaya 55:9) Si ajabu kwamba Biblia imevumiliwa kwa muda mrefu hivyo!
Kwa watumishi wa Mungu, nyakati zote Biblia imekuwa kitabu chenye umaana zaidi ya vitabu vyote. Wao wakubaliana na mtume Paulo, yeye mwenyewe akiwa mmoja wa waandikaji wa Biblia. Alisema hivi: “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho.” (2 Timotheo 3:16) Kwa kupatana na maneno hayo, Biblia ndio msingi wa imani ya Mashahidi wa Yehova leo. Inaamua mafundisho yao na kuongoza mwenendo wao. Wao hupendekeza kwa moyo wote kwamba kila mtu asome sehemu fulani ya Neno la Mungu kila siku na kuyatafakari kwa uthamini yaliyomo.—Zaburi 1:1-3.
Mazoea ya Kusoma Biblia
Mazoea ya kusoma Maandiko yamenufaisha katika nyakati zilizopita. Wafalme Waisraeli waliamriwa waandike kwa mkono nakala zao wenyewe za Sheria—ambayo sasa ni sehemu muhimu ya Biblia—na kuisoma kila siku ikiwa kikumbusha cha mapenzi ya Mungu kwao. (Kumbukumbu la Torati 17:18-20) Wafalme wengi walianguka kwa sababu ya kukosa kufanya hivyo.
Umuhimu wa kujifunza Maandiko unaonyeshwa na hali ya nabii mkongwe Danieli. Kwa sababu ya funzo lake la binafsi la sehemu za Biblia zilizokuwako wakati wake, Danieli, akiwa uhamishoni katika Babiloni, aliweza ‘kufahamu kwa kuvisoma vitabu’ kwamba unabii wa maana ulioandikwa na Yeremia ulikuwa unakaribia sana kutimizwa.—Danieli 9:2.
Katika wakati wa kuzaliwa kwa Yesu, Simeoni aliyekuwa “mtu mwenye haki, mcha Mungu” alikuwa akitazamia kwa uhakika kuona yule ambaye angekuwa Kristo, au Mesiya. Simeoni alikuwa ameahidiwa kwamba hangekufa kabla ya kumwona Kristo. Jinsi alivyorejezea unabii wa Isaya alipombeba kitoto Yesu mikononi mwake yaonyesha kwamba Simeoni alikuwa akisoma kwa uangalifu sana vitabu vya Biblia vilivyokuwa vimeandikwa tayari katika siku zake.—Luka 2:25-32; Isaya 42:6.
Yohana Mbatizaji alipokuwa akibatiza, ‘watu walikuwa wakingoja’ Mesiya. Jambo hilo laonyesha nini? Laonyesha kwamba watu wengi miongoni mwa Wayahudi walifahamu unabii mbalimbali wa Kimesiya ulioandikwa katika Maandiko. (Luka 3:15) Jambo hilo lapendeza kwa sababu vitabu havikupatikana kwa urahisi siku hizo. Nakala za vitabu vya Biblia zilihitaji jitihada nyingi katika kuziandika kwa mkono kwa uangalifu mwingi, na kwa hiyo zilikuwa ghali na ngumu kupatikana. Watu walipata kufahamuje yaliyomo ndani ya vitabu hivyo?
Sanasana, kupitia usomaji wa peupe. Kwa kielelezo, Musa aliamuru kwamba katika pindi fulani zilizowekwa, Sheria yote iliyotolewa na Mungu ilikuwa isomwe kwa Waisraeli waliokusanyika. (Kumbukumbu la Torati 31:10-13) Kufikia karne ya kwanza W.K., kusoma vitabu vya Biblia peupe kulikuwa kumeenea sana. Mwanafunzi Yakobo alitaja hivi: “Tangu zamani za kale Musa anao watu wahubirio mambo yake; katika kila mji husomwa kila sabato katika masinagogi.”—Matendo 15:21.
Leo, ni rahisi kuwa na nakala ya binafsi ya Biblia. Angalau baadhi ya hivyo “vitabu vidogo” vinapatikana katika lugha asilimia 98 ya watu wa ulimwengu. Hivyo, inasikitisha kwamba wengi hawapendi kujifunza yale ambayo Biblia inawaambia. Huu waweza kuwa muhula wa kisayansi, lakini Neno la Mungu, Biblia, hasa ndilo “lafaa kwa mafundisho.” Hiyo hutoa mashauri mazuri juu ya adili, mahusiano ya kibinadamu, na mambo mengine mengi. Isitoshe, Biblia hutoa tumaini la pekee la hakika la wakati ujao wenye amani.
Uisome kwa Ukawaida
Kwa hiyo Mashahidi wa Yehova wameifanya iwe sehemu kubwa ya kazi yao kuwatia watu moyo waisome Biblia kwa ukawaida. Kwa maandishi ya herufi kubwa kwenye jengo la kiwanda katika makao makuu yao ya ulimwengu huko Brooklyn, New York, kuna himizo hili: “SOMA NENO LA MUNGU BIBLIA TAKATIFU KILA SIKU.” Mamilioni ya wapita-njia wameona maneno hayo, na twatumaini kwamba watu wengi wameyatii.
Katika makutaniko yanayozidi 73,000 ya Mashahidi wa Yehova kotekote ulimwenguni, vipindi vya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi hufanywa kila juma. Sehemu ya mtaala huo ni usomaji wa peupe wa sehemu iliyoteuliwa kutoka kwa Biblia. Wahudhuriaji wote pia wana mgawo wa kusoma sura chache za Biblia kila juma kwa faragha wakiwa nyumbani kwao. Wale ambao hudumu kufuata ratiba hiyo hatimaye humaliza kusoma Biblia nzima.
Mpango huo unapatana na mojapo vitabu vya mafunzo kinachotumiwa katika shule hiyo. Kitabu Kiongozi cha Shule ya Huduma ya Kitheokrasi chasema hivi: “Orodha yako ya kipekee imepaswa itie wakati wa kuisoma Biblia peke yake. Kuna faida kubwa katika kuisoma mwanzo mpaka mwisho. . . . Walakini, mradi wako katika kusoma haupaswi kamwe uwe kumaliza habari tu, bali kupata kujua ilivyo kwa kusudi la kukumbuka. Chukua wakati utafakari juu ya yale ambayo inasema.”
Vichapo vingine vilivyotokezwa na Mashahidi wa Yehova vilevile hutia moyo usomaji wa Biblia. Kwa kielelezo, katika gazeti jenzi la jarida hili, Amkeni!, kulikuwa na kitia-moyo hiki kwa ajili ya vijana: “Je! umepata kuisoma Biblia yote? Ndiyo, Biblia ni kitabu kikubwa, lakini kwa nini usigawanye usomaji wayo katika vipande vidogo vidogo? . . . Waberoya ‘waliokuwa waungwana waliyachunguza Maandiko kila siku.’ (Matendo 17:11) Ukifuata ratiba ya usomaji wa kila siku wa dakika 15 tu . . . ungeweza kukamilisha usomaji wa Biblia kwa mwaka mmoja.” Naam, Mashahidi wa Yehova wahisi kwamba Wakristo wa kisasa wapaswa wafahamu vizuri Maandiko, kama ilivyokuwa na watumishi wa Mungu katika nyakati za kale.
Wakikumbuka hayo Mashahidi wameendeleza namna ya kisasa ya usomaji wa Biblia peupe. Wametengeneza kaseti za usomaji zinazotia ndani Biblia nzima katika lugha kadhaa. Kwa watu wengi jambo hilo limewasaidia sana kushinda baadhi ya vizuizi vya usomaji wa Biblia. Wengine husikiliza kaseti hizo wanapofanya kazi nyumbani, wakiendesha magari yao, au wakifanya vitu vinginevyo mbalimbali. Kuketi na kusikiliza kwa ukimya usomaji wa sehemu fulani ya Biblia huku ukifuatia usomaji huo kwa nakala yako mwenyewe kwafurahisha sana.
Kama bado hujaanza kusoma Biblia kila siku, mbona usiwe na zoea la kuisoma kila siku? Jambo hilo halipasi kuchukua muda mrefu kila siku, lakini kutakuwa na manufaa makubwa kwa sababu kutumia Maandiko kutakufanya wewe utende kwa hekima na kufurahia maisha yenye kuthawabisha kiroho. Pia utakuwa ukitenda kwa kupatana na agizo hili lililotolewa zamani za kale kwa kiongozi wa Waisraeli Yoshua: “Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana.”—Yoshua 1:8.
Kurasa za Biblia zafunua kusudi la Yehova lenye upendo kwa wanadamu watiifu. Ujuzi sahihi wa Neno lake lililopuliziwa hutokeza furaha ya kweli na tumaini la kupata uhai wa milele katika Paradiso katika ulimwengu mpya ulio mzuri ajabu wenye baraka za milele. (Luka 23:43; 2 Petro 3:13) Na utwae fursa yako ya kusoma na kujifunza Biblia na kufikia maisha hayo mazuri ajabu.