Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 6/15 kur. 21-22
  • Biblia—Kitabu Kinachopasa Kusomwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Biblia—Kitabu Kinachopasa Kusomwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Sababu Gani Kuisoma kwa Ukawaida?
  • Tunatiwa Moyo Kuisoma
  • Biblia—Kitabu Kinachofaa Kusomwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Kunufaika kwa Usomaji wa Biblia Kila Siku
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Usomaji wa Biblia—Wenye Kufaidi na Wenye Kupendeza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Jitahidi Uwe Msomaji Mzuri
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 6/15 kur. 21-22

Biblia​—Kitabu Kinachopasa Kusomwa

BIBLIA ndicho kitabu kilichoenezwa mahali pengi zaidi ya kitabu kingine cho chote katika historia yote. Ndicho kitabu chenye kutafsiriwa zaidi, ndicho kitabu ambacho maneno yacho yanatajwa-tajwa zaidi, na ndicho kitabu cha zamani zaidi. Ndiyo, pia ndicho kitabu ambacho kimepingwa vikali zaidi lakini bado kikaendelea kuwapo. Hata hivyo, jambo la kusikitisha ni kwamba haielekei kuwa Biblia ndicho kitabu kinachosomwa na watu wengi zaidi ulimwenguni.

Hata hivyo Biblia inapasa kusomwa. Fikiria mambo fulani yanayoihusu.

Kwa Sababu Gani Kuisoma kwa Ukawaida?

Neno letu la Kiswahili “Biblia” limetokana na neno la Kigiriki bi·bliʹa, maana yake “vitabu vidogo.” Hilo linatukumbusha kwamba Biblia imefanyizwa na hesabu fulani ya vitabu​—ingawa vingine ni “vidogo” sana! Hivyo viliandikwa katika kipindi cha miaka zaidi ya elfu moja. Ingawa viliandikwa na wanadamu, vina roho ya Chanzo cha juu zaidi. Hata leo, mamilioni ya watu wanakubali kwamba ‘kila andiko ni lenye pumzi ya Mungu na linafaa.’ (2 Timotheo 3:16) Ndiyo, “vitabu vidogo” hivyo vimejawa na mawazo ya Yehova Mungu mwenyewe. (Isaya 55:9) Si ajabu vimeendelea kuwapo muda mrefu sana!

Zoea la kusoma Maandiko kwa ukawaida limekuwa lenye faida katika nyakati zilizopita. Wafalme wa Israeli walipaswa kufanya nakala za kibinafsi zilizoandikwa za Torati, ambayo sasa ni sehemu ya maana ya Biblia. Walipaswa kuisoma kila siku, hicho kikiwa ni kikumbusho cha daima watumikie kwa unyenyekevu na kufuata sana amri za Mungu. (Kumbukumbu la Torati 17:18-20) Kwa uhakika, sisi tunaweza kujipatia faida kama hizo kwa kusoma Biblia kwa ukawaida.

Nalo ni jambo la maana kama nini kuuangalia unabii wa Biblia! Kwa sababu nabii Danieli alikuwa na funzo la kibinafsi la Maandiko, aliweza kufahamu kwamba unabii wa maana katika kitabu cha Yeremia ulikuwa karibu kutimizwa.​—Danieli 9:1, 2; Yeremia 29:10.

Yohana Mbatizaji alipokuwa akihubiri, ‘watu walikuwa wakingoja’ Masihi atokee. (Luka 3:15) Hilo linadokeza kwamba wengi kati yao walifahamu sana unabii mbalimbali kuhusu Kristo uliokuwa umeandikwa katika Maandiko. Hilo ni jambo la kupendeza sana, kwa kuwa vitabu havikupatikana kwa urahisi siku hizo. Nakala za vitabu vya Biblia zilipasa kufanywa kwa mkono kwa uangalifu mwingi sana. Kwa hiyo watu walivifahamuje sana?

Mara nyingi ilikuwa ni kwa usomaji wa hadharani. Mwanafunzi Yakobo alitamka hivi: “Tangu zamani za kale Musa anao watu wahubirio mambo yake; katika kila mji husomwa kila sabato katika masinagogi.”​—Matendo 15:21.

Leo ni jambo jepesi watu mmoja mmoja kuwa na nakala ya kibinafsi ya Biblia, na angaa vingine vya vile “vitabu vidogo” vinapatikana katika lugha za asilimia 97 ya watu wa ulimwengu. Hivyo inasikitisha kwamba watu wengi hawapendezwi sana na kujua Biblia inawaambia nini.

Tunatiwa Moyo Kuisoma

Mashahidi wa Yehova wameifanya iwe sehemu kubwa ya kazi yao kutia watu moyo wasome Biblia kwa ukawaida. Kwenye kimoja cha viwanda vyao vya uchapaji katika makao makuu ya ulimwengu katika Brooklyn, New York, yameandikwa maneno ya herufi zenye rangi nzito yanayosema “SOMA NENO LA MUNGU BIBLIA TAKATIFU KILA SIKU” (kwa Kiingereza).

Katika yale makundi zaidi ya 46,000 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote, kuna Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kila juma. Usomaji wa hadharani wa kisehemu kilichochaguliwa cha Biblia kila juma ni sehemu ya mtaala huo. Wote wanaohudhuria wana mgawo wa kila juma wa kusoma sura chache za Biblia katika faragha ya nyumba yao wenyewe, na wale wanaofuata orodha hiyo mwishowe wanasoma Biblia nzima.

Hayo yanafanywa kupatana na Kiongozi cha Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ambacho ni kimoja cha vitabu vya mafundisho vinavyotumiwa katika mtaala huo. Kinasema hivi: “Orodha yako ya kipekee imepaswa itie wakati wa kuisoma Biblia peke yake. Kuna faida kubwa katika kuisoma mwanzo mpaka mwisho. . . . Walakini, mradi wako katika kusoma haupaswi kamwe uwe kumaliza habari tu, bali kupata kujua ilivyo kwa kusudi la kukumbuka. Chukua wakati utafakari juu ya yale ambayo inasema.”​—Ukurasa 21.

Mashahidi wa Yehova wanajisikia kwamba Wakristo wa kisasa wanapaswa kuwa watu wenye maarifa ya Biblia. Kwa kufikiria hilo, wameendeleza namna ya karne ya 20 ya kusoma Biblia hadharani. Wametia vingi vya vile “vitabu vidogo” vya Biblia katika kanda za kaseti. Hivyo wale wanaojisikia kwamba hawawezi kuwa na wakati wa kuketi na kusoma kwa vipindi virefu wanaweza sasa kusikiliza habari za vitabu vya Biblia zilizotiwa katika kanda huku wakiendelea na kazi nyumbani, wakiendesha magari, au wakifanya mambo kadha mengine. Bila shaka, kanda zenyewe ni msaada mzuri pia wakati tunapoketi ili kusoma Biblia. Ni jambo la kupendeza kusikiliza usomaji wa Maandiko huku ukifuata kwa kutazama nakala yako mwenyewe ya Biblia.

Kwa vyo vyote, jifaidi mwenyewe kwa ukamili kutokana na mwongozo wa kiroho unaoandaliwa katika vichapo vya Ukristo wa kweli vinavyoandaliwa na Mungu kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 24:45-47) Lakini pia mbona usilifanye liwe zoea lako kusoma Biblia kila siku. Faida zitakuwa kubwa, kama ilivyosemwa katika amri aliyopewa zamani za kale Yoshua kiongozi wa Kiisraeli: “Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana.”​—Yoshua 1:8.

[Picha katika ukurasa wa 22]

Kwa miaka mingi, ishara kwenye kiwanda cha uchapaji cha Sosaiti yetu huko 117 Adams Street, Brooklyn, New York, imehimiza wapitaji wasome Maandiko Matakatifu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki