‘Ukurasa Mmoja Waweza Kupenya Giza Kama Nyota’
TAFSIRI nyingi za Maandiko Matakatifu zapatikana karibu ulimwenguni pote leo. Lakini vita juu ya Biblia mara nyingi imekuwa jambo la kufa na kupona.
Katika kitabu Fifteenth Century Bibles, Wendell Prime aliandika hivi: “Miaka thelathini baada ya kuvumbuliwa kwa matbaa za uchapishaji, Baraza la Kuwahukumu Wazushi lilifanikiwa sana nchini Hispania. Kati ya watu 342,000 walioadhibiwa na baraza hilo katika nchi hiyo watu 32,000 walichomwa moto wakiwa hai. Ni Biblia iliyosababisha wawe wafia-imani kwa kuchomwa. Baraza hilo lenye kuangamiza sana lilikuwa lenye ukatili sana vilevile nchini Italia, upande wa kaskazini na pia kusini. Maaskofu wakuu, wakisaidiwa na Baraza la Kuwahukumu Wazushi walikuwa moto ulao Biblia na wasomaji wazo pia. Nero alifanya baadhi ya Wakristo wawe nuru katika ulimwengu kwa kuwawasha moto wakiwa wamefungwa magunia, kupakwa lami, akiwatumia kuwa mishumaa ya kuwasha tamasha zake zenye ukatili. Lakini barabara za majiji ya Ulaya ziliwaka kwa mioto ya kuchoma Biblia. Biblia hazikuwa kama wasomaji ambao wangenyimwa vitu fulani, kuvuliwa mavazi, kuteswa, kukatakatwa na kutengwa na jamii. Hata ukurasa unaookoka waweza kupenya giza hili tititi kama nyota.” (Italiki ni zetu.)
Jambo ambalo mtungaji wa vitabu Prime afafanua hapo kwa kweli lilitendeka katika kisa cha ukurasa wa Biblia ambao umetokezwa hapa. Huo ni ule ukurasa wa maandishi ya mwisho yanayotambulisha mtafsiri. Safu mbili zenye kuambaana kwenye sehemu ya juu ni mistari ya mwisho ya Apokalipsi, au kitabu cha Ufunuo.
Kuhusu kitabu hiki, The Cambridge History of the Bible chataarifu hivi: “Tafsiri ya Biblia ya Kikatalonia ya Bonifacio Ferrer ilichapishwa katika Valencia, 1478; nakala zote zilizopatikana ziliharibiwa na Baraza la Kuhukumu Wazushi kabla ya 1500, lakini ukurasa mmoja uliokoka na unapatikana katika maktaba ya Hispanic Society of America.” (Italiki ni zetu.)
Wendell Prime alisema pia hivi: “Kwa habari ya makasisi waliohofu kabisa, hakukuwa na njia nzuri ya kushughulikia Biblia ila kuzichoma tu. Mioto hiyo mitakatifu ingetukia mara nyingi sana na kwa uangavu zaidi kama tu Biblia nyingi zaidi zingepatikana zichomwe. Katika sehemu nyingi hakukuwa mioto ya kuchoma Biblia kwa sababu wenye mamlaka walikuwa na bidii sana hivi kwamba hakukuwa na Biblia za kuchomwa.” Zijapokuwa jitihada hizo nyingi za kuangamiza Biblia zilizokusudiwa kutumiwa na watu wa kawaida, nakala nyingi ziliokoka. Prime aliongeza hivi: “Biblia zilihifadhiwa kwa kubebwa na watu walioenda uhamishoni, au kwa kufichwa kama mawe na vyuma vya thamani katika nyakati za taabu na za hatari.”
Nabii wa Mungu Isaya aliandika hivi: “Mwili ni majani . . . . Majani yakauka, ua lanyauka; bali neno la Mungu wetu litasimama milele.” (Isaya 40:6, 8) Kwa karne nyingi zilizopita, watu wengi wapendao Biblia na watafsiri wengi wenye moyo mkuu wamejihatarisha sana na kupatwa na taabu sana kwa sababu ya Neno la Mungu. Lakini, jitihada za binadamu pekee hazingaliweza kamwe kufanya iokoke. Twamshukuru Mtungaji wa Biblia, Yehova, kwa sababu ya kuokoka kwayo.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 7]
Kwa hisani ya The Hispanic Society of America, New York