Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 12/8 kur. 16-18
  • Pigano la Biblia ya Kifaransa la Kuokoka

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Pigano la Biblia ya Kifaransa la Kuokoka
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Pigano Laanza kwa Bidii
  • Kutetea Biblia Kwahamasishwa
  • Pigano Lenye Hatari
  • Rudisho la Shambulio
  • Pigano la Kukata Maneno
  • Lefèvre d’Étaples​—Alitaka Watu wa Kawaida Waelewe Neno la Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2016
  • Matatizo ya Kutafsiri Biblia ya Kiitaliano
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Walijaribu Kuwazuia Watu Wasilipate Neno la Mungu
    Amkeni!—2011
  • Olivétan—“Mtafsiri Mnyenyekevu” wa Biblia ya Kifaransa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 12/8 kur. 16-18

Pigano la Biblia ya Kifaransa la Kuokoka

NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA UFARANSA

WATU zaidi ya milioni mia moja ulimwenguni huongea Kifaransa. Hata kama wewe si mmoja wao, kusoma juu ya pigano la Biblia ya Kifaransa la kuokoka kwavutia sana, kwa kadiri fulani, kwa sababu ya uhusiano wake na uhuru wa kidini. Kwa karne kadhaa Biblia za Kifaransa zimeharibiwa kwa ukatili na adui na marafiki wasio waaminifu. Wajapopatwa na mambo hayo yasiyopendeza, watafsiri na wachapishaji walihatarisha maisha zao ili kushinda pigano hilo.

Katika karne ya 12, tafsiri za sehemu za Biblia zilipatikana katika lugha kadhaa za wenyeji, kutia na Kifaransa. Vikundi vya wale walioonwa kuwa wazushi na Kanisa Katoliki vilitia moyo watu wazitumie. Lakini ni hadi karne ya 19 tu ndipo Biblia ilipoanza kugawanywa sana katika Kifaransa. Kupita huku kwa muda mrefu wa karne kadhaa hudhihirisha majaribu yenye hatari ambayo Biblia ya Kifaransa ilipatwa nayo ili kuokoka.

Mojawapo ya vitabu vya kwanza vya Kifaransa kilikuwa kamusi ya Biblia iliyochapishwa karibu mwaka wa 900 W.K. Ilikuwa imekusudiwa kusaidia wasomaji kuelewa Biblia katika Kilatini, lugha iliyotumiwa na Kanisa Katoliki. Lakini kufikia wakati huo watu wa kawaida, ambao walitumia lahaja kadhaa hawakuwa wakisema Kilatini. Hivyo walinyimwa njia ya kulifikia Neno la Mungu. Uwezo wa kulifikia ulibaki ukiwa pendeleo la pekee kwa makasisi waliokuwa wamejifunza Kilatini, ambao wangeweza kukisoma.

Katika 842 W.K., nyaraka ya kwanza ya taifa katika Kifaransa ilipatikana kirasmi. Huo ulikuwa utambuzi wa kimya kwamba watu walio wengi hawakuwa wakisema Kilatini tena. Mashairi ya kidini katika lugha ya wenyeji yalianza kutokea katika Ufaransa wapata mwaka wa 880 W.K. Hata hivyo, tafsiri za Biblia hazikutokea kwa karne mbili nyingine. Miongoni mwa tafsiri za mapema zaidi zilikuwa za Kifaransa cha watu wa Normani za sehemu za Biblia, zilizotokezwa mwanzoni mwa karne ya 12.

Pigano Laanza kwa Bidii

Jitihada iliyotegemezwa ya kwanza ya kufanya Maandiko Matakatifu yapatikane kwa watu wa Ufaransa katika njia ambayo wangeweza kuyasoma ilitokana na Peter Waldo, mfanya-biashara wa karne ya 12 kutoka Lyons, katikati mwa Ufaransa. Waldo aliagiza tafsiri ya sehemu za Biblia katika lugha ya Provençal, lahaja inayosemwa kusini-mashariki mwa Ufaransa. Katika mwaka wa 1179, kwenye Baraza la Tatu la Lateran, aliagiza tafsiri yake ya sehemu ya Biblia itolewe kwa Papa Alexander wa Tatu.

Baadaye, kanisa lililaumu Waldo na wafuasi wake likiwaita wazushi, na watawa wa kiume wakachoma tafsiri alizokuwa ameagiza. Kuanzia hapo na kuendelea, kanisa lilikinza kila jitihada ya kufanya Neno la Mungu lipatikane mikononi mwa watu wa kawaida.

Kanisa lilidhihirisha hila yake mwaka wa 1211 kwa kuchoma Biblia katika jiji la Metz, mashariki ya Ufaransa. Mwaka wa 1229 Baraza la Toulouse lilikataza kabisa watu wa kawaida kutumia Biblia za lugha za wenyeji katika lugha yoyote ile. Hilo lilifuatwa mwaka wa 1234 na Baraza la Tarragona, Hispania, ambalo lilikataza mtu kuwa na Biblia katika yoyote ya lugha za Kiroma (lugha zilizotokana na Kilatini), hata na makasisi.

Ujapokuwa upinzani huo wenye ukatili, tafsiri kamili ya Biblia ya kwanza ya lugha ya Kifaransa ilitokea nusu ya pili ya karne ya 13. Ikiwa imetafsiriwa bila majina kujulikana, Biblia hii iligawanywa kwa uchache tu. Kufikia wakati huo Biblia haikupatikana kwa watu wa kawaida katika njia yoyote ile. Nakala zilifanywa kwa mikono. Bei ya juu na kutopatikana kwa wingi kulizuia watu kuwa na Biblia kabisa ila tu makabaila na makasisi.

Kutetea Biblia Kwahamasishwa

Kukiwa na ubuni wa matbaa za uchapaji na chapa zenye kusonga zilizobuniwa na Johannes Gutenberg wapata mwaka wa 1450, Ufaransa iliathiriwa vikali na badiliko kubwa la uchapaji katika Ulaya. Majiji matatu ya Ufaransa—Paris, Lyons, na Rouen—yakawa vitovu vya maana vya uchapaji, mategemezo katika kutetea Biblia.a

Hadi kufikia hatua hii ya kushindana, tafsiri za Biblia ya Kifaransa zilikuwa zimetegemea Vulgate ya Kilatini. Maandishi ya Kilatini yalikuwa yametiwa doa na makosa mengi sana baada ya miaka elfu moja ya unakili wa kurudia, lakini kanisa liliambatana na Vulgate. Hata hivyo, Mkatoliki Mfaransa Jacques Lefèvre d’Étaples aliamua kufanya Biblia ipatikane kwa watu. Mwaka wa 1530 alitafsiri Vulgate kwa Kifaransa, akirekebisha baadhi ya makosa yake kwa kurejezea hati za Kiebrania na Kigiriki ambazo zilikuwa zimepatikana karibuni. Pia aliondoa ufafanuzi wa kimafundisho wenye kutatanisha ambao kanisa lilikuwa limeuingiza katika maandishi hayo.

Upesi tafsiri ya Lefèvre ikashambuliwa. Ilibidi tafsiri fulani zichapwe nje ya Ufaransa. Hizo ziliwekwa kwenye orodha ya vitabu vilivyopigwa marufuku na kanisa. Kwa wakati fulani ilimbidi Lefèvre atafute kimbilio katika Strasbourg, lililokuwa jiji la kifalme lenye kujitegemea mashariki ya Ufaransa. Hata hivyo, tafsiri yake ilifanikiwa.

Tafsiri ya kwanza ya Kifaransa ya Biblia iliyotegemea maandishi ya lugha ya awali ilichapwa mwaka wa 1535. Mtafsiri alikuwa Mprotestanti Mfaransa Pierre-Robert Olivétan, binamu ya Mwanamapinduzi wa kidini John Calvin. Kwa sababu ya upinzani wa kanisa, haingeweza kuchapwa Ufaransa, kwa hiyo tafsiri hii ikachapwa Neuchâtel, Uswisi, jumuiya mpya ya Protestanti. Tafsiri ya Biblia ya Kifaransa ya Olivétan ilitumika kuwa kiwango kwa mabadiliko ya baadaye mengi na tafsiri za Biblia katika lugha nyingine.

Pigano Lenye Hatari

Katika Ufaransa baadhi ya wachapaji jasiri kama Étienne Dolet katika mwaka wa 1546, walichomwa mtini kwa sababu ya kuchapa Biblia. Baraza la Trent, katika mwaka wa 1546, lilihakikisha “uasilia” wa Vulgate, yajapokuwa makosa yake, na tangu wakati huo na kuendelea kanisa lilichukua msimamo uliozidi kuimarika dhidi ya tafsiri za lugha ya wenyeji. Mwaka wa 1612 Baraza la Kuhukumu Wazushi la Hispania lilianzisha kampeni kali ya kukomesha Biblia za lugha ya wenyeji.

Nyakati nyingine mnyanyaso uliongoza kwenye uvumbuzi mnyoofu. “Msokoto wa nywele,” au “fundo la nywele,” Biblia zilikuwa zikitokezwa, ambazo zilikuwa na udogo wa kutosha kufichwa katika fundo la nywele za mwanamke. Na mwaka wa 1754, madondoo ya Maandiko ya Kiebrania na Kigiriki yalichapwa katika kitabu kilichokuwa na kipimo cha sentimeta tatu kwa tano tu.

Rudisho la Shambulio

Ingawa hivyo, baada ya muda fulani, badiliko kubwa lilitokea. Baada ya Biblia kushinda karne nyingi za mashambulio makali, mapigo ya kukata maneno yalitolewa kwa upendeleo wake. Mawazo mapya na uhuru wa ibada, uliopewa Wafaransa baada ya Mapinduzi ya Ufaransa, yalithibitika kuwa mapigo ya kukata maneno dhidi ya upinzani wa kanisa. Hivyo, mwaka wa 1803 Agano Jipya la Kiprotestanti lilichapwa Ufaransa, lilikuwa la kwanza katika miaka 125!

Pia msaada ulitoka katika sosaiti za Biblia. Katika mwaka wa 1792 French Bible Society ilifanyizwa London, Uingereza, “kupata, kadiri iwezekanavyo, Biblia za Kifaransa kwa Wafaransa ambao hawana hazina hii ya kimungu katika lugha inayoeleweka kwao.” Sosaiti nyingine za Biblia zilijiunga na pambano hilo. Mradi wao wa kutokeza na kugawanya Biblia katika Kifaransa ulifurahia mafanikio.

Pigano la Kukata Maneno

Kanisa Katoliki lilikinza badiliko lolote katika mbinu zake, lakini lilikuwa linashindwa. Katika karne yote ya 19, mapapa walitoa mfululizo wa maagizo yakipinga kikatili Biblia za lugha ya wenyeji. Kufikia mwisho-mwisho wa 1897, Papa Leo wa 13 alisisitiza tena kwamba “tafsiri zote za Vitabu Vitakatifu zilizofanyizwa na mwandikaji yeyote yule asiye Mkatoliki na kwa lugha yoyote ya kawaida zimekatazwa, hasa zile zilizochapishwa na sosaiti za Biblia, ambazo zimelaumiwa na Papa wa Roma mara kadhaa.”

Hata hivyo, kwa sababu ya kupatikana kwa Biblia za Protestanti zisizo ghali zilizochapishwa na sosaiti za Biblia, Kanisa Katoliki liliruhusu wasomi Wakatoliki watafsiri Biblia katika Kifaransa. Tafsiri ya Augustin Crampon, iliyochapishwa kwanza katika mabuku saba (1894-1904) kisha katika buku moja (1904), ilikuwa tafsiri ya kwanza ya Kifaransa ya Katoliki iliyotegemea maandishi ya awali. Vyenye kufaa kuangaliwa ni vielezi-chini vingi vya kiusomi na uhakika wa kwamba Crampon alitumia sana Jéhovah, namna ya Kifaransa ya jina la Mungu.

Ikibadili mawazo, Vatikani, katika waraka wake wa kipapa Divino Afllante Spiritu, wa 1943, hatimaye iliweka mwongozo wa kutafsiri Biblia katika lugha za wenyeji. Tafsiri nyingi za Kikatoliki zimechapishwa tangu wakati huo, kutia na Jerusalem Bible yenye kujulikana sana, iliyochapishwa kwanza katika Kifaransa na baadaye ikatafsiriwa katika lugha nyinginezo kadhaa, kutia na Kiingereza.

Biblia moja ambayo imesaidia watu wenye kusema Kifaransa ulimwenguni pote ni toleo la Kifaransa la New World Translation of the Holy Scriptures. Iliyochapishwa kwanza katika namna yake ikiwa kamili mwaka wa 1974, na kufanyiwa marekebisho 1995. Katika lugha nyingi ambazo kufikia sasa imechapishwa, New World Translation hutoa sifa kwa Mtungaji wa Biblia kwa kurudisha jina lake, Yehova, katika Maandiko ya Kiebrania na, panapolifaa, katika Maandiko ya Kigiriki. Hadi sasa, zaidi ya nakala milioni tano za toleo la Kifaransa zimechapwa. Pasipo shaka, Biblia imeshinda pambano lake la kuokoka katika Kifaransa.

[Maelezo ya Chini]

a Uchapaji wa Kifaransa ulikuwa wenye mafanikio sana hivi kwamba wakati Baraza la Kuhukumu Wazushi la Hispania lilipoagiza kukusanywa kwa habari za Biblia za kigeni katika mwaka wa 1552, baraza la mahakimu la Seville liliripoti kwamba asilimia 90 hivi ya zile zilizotwaliwa zilikuwa zimechapishwa Ufaransa!

[Picha katika ukurasa wa 16]

Biblia ya Lefèvre d’Étaple ya 1530

[Picha katika ukurasa wa 16]

Biblia ya Olivétan ya 1535

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kielelezo adimu cha “Biblia ya Karne ya 13”

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 17]

Biblia: Bibliothèque Nationale de France

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki