Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 6/15 kur. 8-11
  • Vita vya Kuendelea Kuwapo kwa Biblia ya Kihispania

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Vita vya Kuendelea Kuwapo kwa Biblia ya Kihispania
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kufanyizwa kwa Biblia ya Kihispania
  • Kuhuishwa kwa Muda Mfupi
  • Biblia ya Kihispania Yaendelea kwa Siri
  • Ruhusa Yatolewa
  • Ushindi Wahakikishwa
  • Kutangaza Neno la Mungu Katika Hispania ya Enzi za Kati
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Pambano la Casiodoro de Reina kwa Ajili ya Biblia ya Kihispania
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Kutolewa kwa Toleo Lililorekebishwa la Kihispania la Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
    Habari Zaidi
  • Jinsi Biblia Ilivyotufikia
    Amkeni!—2007
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 6/15 kur. 8-11

Vita vya Kuendelea Kuwapo kwa Biblia ya Kihispania

SIKU moja ya Oktoba 1559, Wahispania Wakatoliki wapatao 200,000 walikusanyika katika jiji la kaskazini la Valladolid. Jambo lililowavutia lilikuwa ni kutekelezwa kwa hukumu ya kifo, ambapo “wahanga wawili walichomwa wakiwa hai, kumi wakanyongwa.” Wao walikuwa “wazushi wa kidini.”

Mfalme mchanga mwenye kupendwa na wengi Philip 2 mwenyewe aliongoza tukio hilo. Wakati mtu aliyehukumiwa alipoomba msamaha, mfalme alisema kwa hasira: “Ikiwa mwana wangu angekuwa mtu mbaya jinsi ulivyo, mimi mwenyewe ningebeba kuni za moto kumchoma.” Uhalifu wa mhanga huyo maskini ulikuwa nini? Yeye alikuwa tu anasoma Biblia.

Wakati huo huo, shirika la Baraza la Kikatoliki la Kuhukumu Wazushi wa Kidini lilikuwa na kazi nyingi katika jiji la Andalusian la Seville. Huko, kikundi cha watawa wa kiume kwenye makao ya watawa ya San Isidro del Campo, kilikuwa tu ndio kimepokea ugavi wa kisiri wa Biblia katika Kihispania. Je! washtaki wangewasaliti? Wengine waliotambua kuwa wamo katika hatari ya kuuawa walitoroka nchi hiyo. Lakini 40 kati ya wale waliobaki hawakufanikiwa hivyo na walichomwa kwenye mti, kati yao akiwepo yule mtu aliyeingiza nchini Biblia hizo. Hispania ya karne ya kumi na sita ilikuwa mahali pa hatari kwa wasomaji wa Biblia—wachache waliepa kuhukumiwa na Baraza la Kuwahukumu Wazushi wa Kidini.

Kati ya hao wachache alikuweko aliyekuwa mtawa wa kiume, Casiodoro de Reina (y. 1520-94). Alitorokea London, lakini hata huko hakuweza kupata usalama. Baraza la Kuwahukumu Wazushi wa Kidini lilitoa zawadi kwa yeyote atakayemshika, na balozi wa Hispania kwa mahakama ya Uingereza alifanya njama ya kumshawishi arudi eneo lenye kudhibitiwa na Hispania kwa njia yoyote ile. Kwa muda mfupi, mashtaka ya uwongo ya uzi-nzi na kulalana pamoja na wanaume kulimlazimisha aondoke Uingereza.

Akiwa na pesa kidogo na familia ya kutegemeza iliyozidi kuongezeka, kwanza alipata kimbilio katika Frankfurt. Baadaye, maombi yake ya kupata ulinzi akiwa mkimbizi wa kidini yalimwongoza hadi Ufaransa, Uholanzi, na hatimaye Uswisi. Na bado wakati huo wote, alikuwa mwenye shughuli nyingi. ‘Isipokuwa wakati nilipokuwa mgonjwa au nikisafiri, . . . sikuacha kazi yangu,’ yeye akaeleza. Alitumia miaka mingi akitafsiri Biblia katika Kihispania. Kuchapishwa kwa nakala 2,600 za Biblia ya Reina kulianza hatimaye katika 1568 katika Uswisi na kukamilishwa katika 1569. Jambo moja lenye kutokeza la tafsiri ya Reina ni kwamba alitumia Iehoua (Jehová) badala ya Seńor (Bwana) kwa Tetragramatoni, zile herufi nne za Kiebrania za jina la kibinafsi la Mungu.

Kufanyizwa kwa Biblia ya Kihispania

Kwa njia yenye kutofautiana, wakati ambapo kwa sababu ya ubuni wa matbaa za kuchapa, Biblia zilikuwa zimesambazwa sana Ulaya, katika Hispania zilikuwa nadra sana. Haikuwa hivyo sikuzote. Kwa karne nyingi Biblia ndicho kilikuwa kitabu kilichosambazwa sana katika Hispania. Nakala zilizoandikwa kwa mkono zilipatikana katika Kilatini na, kwa karne kadhaa, hata katika lugha ya Kigotha. Mwanahistoria mmoja alieleza kwamba wakati wa Muhula wa Kati, “Biblia—ikiwa chanzo cha kitia-moyo na mamlaka, ikiwa ndiyo kanuni ya imani na mwenendo—ilikuwa maarufu zaidi katika Hispania kuliko katika Ujerumani au Uingereza.” Vitabu vyenye historia ndefu za Biblia, Zaburi, kamusi, hadithi za maadili, na vitabu vinginevyo vikawa ndivyo vyenye kuuzwa zaidi wakati huo.

Wanakili stadi walifanyiza hati nzuri za Biblia kwa jitihada nyingi. Ingawa ilichukua waandishi 20 mwaka mzima kutokeza hati moja tu iliyo bora sana, Biblia nyingi za Kilatini na maelfu ya mafafanuzi ya Biblia ya Kilatini yalikuwa yakisambazwa katika Hispania kufikia karne ya 15.

Zaidi ya hiyo, lugha ya Kihispania ilipoanza kukua, kukawa kupendezwa na kuwa na Biblia katika lugha ya kwao. Mapema kufikia karne ya 12, Biblia ilitafsiriwa katika Kirumi, au Kihispania cha mapema, lugha iliyosemwa na watu wa kawaida.

Kuhuishwa kwa Muda Mfupi

Lakini kuhuishwa huko hakukuendelea kwa muda mrefu. Wawaldenisi, Waloladi, na Wahusaiti walipoanza kutetea imani zao kwa kutumia Maandiko, itikio lilikuwa la haraka na la jeuri. Wenye mamlaka Wakatoliki walitilia shaka kusoma Biblia, na utafsiri uliokuwa umeanza kukua katika lugha za kawaida ulishutumiwa kabisa.

Baraza la Kikatoliki la Toulouse (Ufaransa), lililokutana katika 1229, lilitangaza: “Sisi tunakataza kwamba mtu yeyote wa kawaida asiwe na vitabu vya Agano la Kale au Agano Jipya likiwa limetafsiriwa katika lugha ya kawaida. Iwapo mtu mcha Mungu ataka, yeye aweza kupata vitabu vya nyimbo na sala . . . lakini kwa vyovyote asiwe na vitabu vilivyotajwa juu vikiwa vimetafsiriwa katika Kirumi.” Miaka minne baadaye, James wa 1 wa Aragon (mfalme wa sehemu kubwa ya peninsula) aliwapa siku nane tu wale wote waliokuwa na Biblia katika lugha za kawaida ili wazikabidhi askofu wa huko azichome. Kukosa kufanya hivyo, iwe ni kiongozi wa kanisa au mtu wa kawaida, kungemfanya mtu huyo ashukiwe kuwa mzushi.

Yajapokuwa makatazo hayo—ambayo hayakufuatiliwa sana nyakati zote—baadhi ya Wahispania wangeweza kujivunia kuwa na Biblia ya Kirumi wakati wa sehemu ya mwisho ya Muhula wa Kati. Hilo lilifikia mwisho wa ghafula wakati Baraza la Kuwahukumu Wazushi wa Kidini la Hispania lilipoanzishwa chini ya Malkia Isabella na Mfalme Ferdinand katika 1478. Katika 1492, kwenye jiji la Salamanca pekee, nakala 20 za Biblia zenye thamani sana zilizoandikwa kwa mkono zilichomwa. Hati-mkono za kibiblia za Kirumi zilizopata kuokoka ni zile tu zilizowekwa kwenye maktaba za kibinafsi za mfalme au watu wachache matajiri wenye nguvu wasioweza kushukiwa.

Kwa miaka mia mbili iliyofuata, Biblia pekee ya Kikatoliki yenye kukubalika iliyochapishiwa Hispania—isipokuwa Biblia ya Kilatini Vulgate—ilikuwa Complutensian Polyglott, Biblia ya kwanza iliyotafsiriwa katika lugha nyingi, iliyodhaminiwa na Kardinali Cisneros. Kwa kweli kilikuwa kitabu chenye ustadi, kisichokusudiwa kwa watu wa kawaida. Ni nakala 600 tu zilizofanyizwa, na ni wachache ambao wangeweza kuielewa kwa sababu ilikuwa na maandiko ya Biblia katika Kiebrania, Kiaramu, Kigiriki, na Kilatini—si katika Kihispania. Zaidi ya hiyo, bei yacho ilikuwa ya juu sana. Iligharimu vipande vitatu vya dhahabu (inayolingana na mshahara wa miezi sita kwa mfanyakazi wa kawaida).

Biblia ya Kihispania Yaendelea kwa Siri

Mapema mwa karne ya 16, Mhispania aliyekuwa kama Tyndale aitwaye Francisco de Enzinas alitokea. Akiwa mwana wa Mhispania mwenye mashamba mengi, alianza kutafsiri Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kihispania akiwa bado mwanafunzi mchanga. Baadaye alichapisha tafsiri yake katika Uholanzi, na katika 1544 alijaribu kwa ujasiri kupata ruhusa ya mfalme ya kuisambaza katika Hispania. Maliki wa Hispania, Charles 1, alikuwa katika Brussels wakati huo, na Enzinas alitumia nafasi hiyo kuomba kibali cha kifalme kwa mradi wake.

Mazungumzo yasiyo ya kawaida kati ya watu hao wawili yameripotiwa kama ifuatavyo: “Hiki ni kitabu cha aina gani?” maliki akauliza. Enzinas akajibu: “Hii ni sehemu ya Maandiko Matakatifu inayoitwa Agano Jipya.” “Ni nani aliye mbuni wa kitabu hiki?” akaulizwa. “Ni roho takatifu,” akajibu.

Maliki alitoa idhini ya uchapishaji lakini chini ya sharti moja—kwamba lazima pia padri wake mwenye kumuungamisha dhambi na kumshauri, mtawa mmoja wa kiume Mhispania, atoe idhini yake. Mambo hayakuendea Enzinas vizuri, na idhini hiyo haikupatikana, na upesi akajipata amefungwa gerezani na Baraza la Kuwahukumu Wazushi wa Kidini. Baada ya miaka miwili aliweza kutoroka.

Miaka michache baadaye, chapa iliyosahihishwa ya tafsiri hiyo ilichapishwa katika Venice, Italia, na ilikuwa chapa hiyo ya Maandiko ambayo Julían Hernández alibeba kisirisiri hadi Seville, Hispania. Lakini alikamatwa, na baada ya miaka miwili ya kuteswa na kufungwa, aliuawa pamoja na wanafunzi wenzake wa Biblia.a

Kwenye Baraza la Trent (1545-63), Kanisa Katoliki lilikariri shutumu layo la tafsiri za Biblia katika lugha za kawaida. Lilichapisha fahirisi ya vitabu vilivyokatazwa, iliyotia ndani tafsiri zote za Biblia zilizokuwa zimefanyizwa bila idhini ya kanisa. Kihalisi hilo lilimaanisha kwamba Biblia zote za kilugha za Hispania zilipigwa marufuku na kwamba kuwa tu na moja kungeongoza kwenye waranti ya mtu kuuawa.

Miaka michache baada ya kuchapishwa kwa tafsiri ya Reina, Cipriano de Valera, aliyekuwa mtawa wa kiume pia aliyeokoka ghadhabu ya Baraza la Kuwahukumu Wazushi wa Kidini katika Seville, aliisahihisha. Tafsiri hiyo ilichapishwa katika Amsterdam katika 1602 W.K., na nakala fulani zikapelekwa Hispania. Katika tafsiri zayo za kwanza zilizosahihishwa, Biblia ya Reina-Valera ndiyo tafsiri inayotumika zaidi miongoni mwa Waprotestanti wenye kuzungumza Kihispania.

Ruhusa Yatolewa

Hatimaye, katika 1782 mahakama ya Baraza la Kuwahukumu Wazushi wa Kidini liliagiza kwamba Biblia ingeweza kuchapishwa mradi ingetia ndani maelezo ya historia na mafundisho ya kanuni. Katika 1790 askofu Mkatoliki wa Segovia, Felipe Scio de San Miguel, akitumia Biblia ya Kilatini iitwayo Vulgate, alitafsiri Biblia katika Kihispania. Kwa kusikitisha, iligharimu sana—reale 1,300, bei ya juu sana wakati huo—na maneno hayakuwa dhahiri sana, hivi kwamba mwanahistoria Mhispania aliieleza kuwa “ya kusikitisha sana.”

Miaka kadhaa baadaye, mfalme Mhispania Fernando 7 aliamuru askofu wa Astorga, Félix Torres Amat, afanye tafsiri iliyosahihishwa, ikitegemea Biblia ya Kilatini ya Vulgate. Tafsiri hiyo ilimalizwa katika 1823 na ikapata ugawaji mkubwa zaidi ya tafsiri ya Scio. Hata hivyo, kwa vile haikutegemea Kiebrania na Kigiriki cha awali, ilikuwa na vizuizi vya kawaida vya tafsiri ya tafsiri.

Yajapokuwa maendeleo hayo, kanisa na watawala wa nchi bado hawakusadikishwa kwamba Maandiko yapaswa kusomwa na watu wa kawaida. Wakati George Barrow, mwakilishi wa Sosaiti ya Biblia ya Uingereza na Nchi za Kigeni alipoomba ruhusa ya kuchapisha Biblia katika Hispania miaka ya 1830, aliambiwa na waziri wa serikali Mendizabal: “Bwana wangu, si Biblia tunayotaka, tunataka bunduki na baruti, ili kuwamaliza waasi, na zaidi ya yote, tunataka pesa, ili tuwalipe askari-jeshi.” Borrow alitafsiri Gospeli ya Luka katika lugha ya Wajipsi wa Hispania, na katika 1837 alifungwa kwa sababu ya kazi yake!

Hatimaye, uvutano huo haungeweza kuzuiwa tena. Katika 1944 kanisa la Hispania lilichapisha tafsiri yalo ya kwanza ya Maandiko Matakatifu ikitegemea lugha za awali—miaka ipatayo 375 baada ya tafsiri ya Casiodoro de Reina. Hiyo ilikuwa tafsiri ya wanachuo Wakatoliki Nácar na Colunga. Hiyo ilifuatwa na tafsiri ya Bover na Cantera katika 1947. Tangu wakati huo kumekuwako tafsiri nyingi sana za Biblia ya Kihispania.

Ushindi Wahakikishwa

Ingawa ilibidi Biblia ya Kihispania ipiganie kuokoka kwayo kwa karne nyingi, vita hivyo vilifanikiwa hatimaye. Dhabihu kubwa za watafsiri wajasiri kama Reina hazikuwa za bure. Ni watu wangapi leo wanaonunua Biblia hukumbuka wakati ambapo kuwa na Biblia kulikatazwa?

Leo, Biblia ndicho kitabu kinachonunuliwa zaidi katika Hispania na katika nchi zinazosema Kihispania, na tafsiri nyingi zinapatikana. Zilizotiwa ndani miongoni mwa hizo ni Versión Moderna (Tafsiri ya Kisasa, 1893), ambayo hutumia jina la Mungu, Jehová mara nyingi; Chapa ya Biblia ya Pauline (1964), inayotumia jina Yavé katika Maandiko ya Kiebrania; Nueva Biblia Española (Biblia Mpya ya Kihispania, 1975) ambayo kwa kusikitisha haitumii wala Jehová wala Yavé; na Traduccíon del Nuevo Mundo (New World Translation, 1967), iliyochapishwa na Watch Tower Society, ambayo hutumia Jehová.

Mashahidi wa Yehova huzuru kila juma makao ya mamilioni ya watu wanaozungumza Kihispania ili kuwasaidia wathamini thamani ya Biblia Takatifu—kitabu kinachostahili mtu kufa kwa ajili yacho, kitabu kinachostahili mtu kuishi kulingana nacho. Kwa kweli, hadithi ya vita vya kuendelea kuwapo kwa Biblia ya Kihispania ni ithibati moja ya ziada kwamba “neno la Mungu wetu litasimama milele.”—Isaya 40:8.

[Maelezo ya Chini]

a Wakati huo hakuna kitabu chochote ambacho kingeweza kuingizwa nchini bila leseni ya pekee, na hakuna mtunza vitabu yeyote ambaye angeweza kufungua safirisho lolote la vitabu bila idhini rasmi ya Mamlaka Takatifu (Baraza la Kuwahukumu Wazushi wa Kidini).

[Picha katika ukurasa wa 10]

Biblia ya Lugha Nyingi iitwayo Complutensian Polyglott imechapishwa tena na hivyo yaweza kuchunguzwa wakati wowote.

(Ona ukurasa wa 8.)

[Hisani]

Courtesy of the Biblioteca Nacional, Madrid, Spain

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki