Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 6/1 kur. 29-30
  • Pambano la Casiodoro de Reina kwa Ajili ya Biblia ya Kihispania

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Pambano la Casiodoro de Reina kwa Ajili ya Biblia ya Kihispania
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jina la Kimungu Katika Tafsiri za Kihispania
  • Vita vya Kuendelea Kuwapo kwa Biblia ya Kihispania
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Kutangaza Neno la Mungu Katika Hispania ya Enzi za Kati
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Jinsi Biblia Ilivyotufikia
    Amkeni!—2007
  • The Bible—A Book of Fact and Prophecy
    Huduma ya Ufalme—2009
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 6/1 kur. 29-30

Pambano la Casiodoro de Reina kwa Ajili ya Biblia ya Kihispania

HISPANIA ya karne ya 16 ilikuwa sehemu hatari kusoma Biblia. Kanisa Katoliki lilikuwa limeamuru Baraza la Kuhukumu Wazushi liangamize wonyesho wowote wa kupinga dini yenye imani ya kidesturi. Lakini kulikuwa na kijana mmoja kusini mwa Hispania ambaye hakusoma tu Maandiko bali pia alinadhiria kuyatafsiri katika lugha yake ili kila Mhispania aweze kuyasoma. Aliitwa Casiodoro de Reina.

Upendezi wa Reina katika Biblia uliamshwa wakati wa ile miaka aliyokuwa katika makao ya watawa ya San Isidro del Campo, kwenye viunga vya Seville, Hispania. Katika miaka ya 1550, watawa walio wengi katika makao hayo ya watawa yasiyo ya kawaida walitumia saa nyingi zaidi wakiyasoma Maandiko kuliko kutimiza wajibu wao wa kikanisa. Nao ujumbe wa Biblia ulibadili kufikiri kwao. Walikataa fundisho la Katoliki kuhusiana na matumizi ya mifano na itikadi katika pagatori. Bila kuepukika, maoni yao yakaja kujulikana katika eneo hilo, nao wakiogopa kukamatwa na Baraza la Kuhukumu Wazushi la Kihispania, wakaamua kutorokea ng’ambo. Reina alikuwa mmoja wa wale 12 waliofaulu kutorokea Geneva, Uswisi.

Baada ya kuponea chupuchupu, alifunga safari toka jiji moja la Ulaya hadi jingine, kwa njia fulani akifaulu kuwahepa waliotafuta kumnyanyasa. Katika 1562 wenye kuhukumu wazushi waliofadhaishwa walichoma mfano wake katika Seville, lakini hata tisho hilo la ukatili halikumfanya Reina aache kazi yake ya kutafsiri Maandiko. Licha ya kwamba wanyanyasi walikuwa wameahidi zawadi kwa yeyote ambaye angemkamata na akaishi kwa hofu sikuzote, aliendelea bila kukoma kuishughulikia tafsiri yake ya Kihispania. “Isipokuwa wakati nilipokuwa mgonjwa au nilipokuwa nikisafiri, . . . kalamu haikutoka mikononi mwangu,” yeye alieleza.

Baada ya miaka kumi Reina akaimaliza hiyo kazi. Katika 1569 tafsiri yake ya Biblia nzima ilichapishwa katika Basel, Uswisi. Kazi hiyo yenye kutokeza sana ilikuwa ndiyo tafsiri kamili ya kwanza ya Kihispania kutoka kwa lugha za awali. Kwa karne nyingi Biblia za Kilatini zilikuwapo, lakini Kilatini kilikuwa lugha ya watu wa tabaka la juu. Reina aliamini kwamba Biblia ilipaswa kueleweka na kila mtu, naye alihatarisha maisha yake ili kuutimiza mradi huo.

Katika utangulizi wa tafsiri yake, alieleza sababu zake. “Kuzuia Maandiko Matakatifu yasiwepo katika lugha ya kawaida huleta suto kuu kwa Mungu na madhara kwa hali-njema ya watu. Kuzuia huko kwa wazi ni kazi ya Shetani na wale awaongozao. . . . Tukitambua kuwa Mungu aliwapa watu wake Neno lake, akikusudia lieleweke na kutumiwa na wote, mtu yeyote ambaye angelizuia katika lugha yoyote hawezi kuwa na nia nzuri.”

Taarifa hiyo ilikuwa yenye ujasiri, hasa kwa kuwa ilitolewa miaka 18 tu baada ya Orodha ya vitabu vilivyokatazwa ya Baraza la Kuhukumu Wazushi la Hispania kukataza moja kwa moja kuisoma Biblia “katika [Kihispania] au katika lugha nyingine yoyote ya huko.” Ni wazi kwamba Reina hakuruhusu hofu ya mwanadamu izuie upendo wake kwa ajili ya kweli.

Zaidi ya kuwa na tamaa kubwa ya kuifanya Biblia ipatikane kwa watu wote wanaojua Kihispania, Reina vilevile alitaka kutokeza tafsiri iliyo sahihi kabisa iwezekanavyo. Katika utangulizi wake, alieleza kwa kina faida za kutafsiri moja kwa moja kutoka kwa lugha za awali. Reina alieleza kwamba makosa kadhaa yalikuwa yameingia katika maandiko ya Kilatini ya Vulgate. Mojawapo makosa makubwa sana ni kuondolewa kwa jina la kimungu.

Jina la Kimungu Katika Tafsiri za Kihispania

Reina alitambua kuwa jina la Mungu, Yehova, lazima liwepo katika tafsiri yoyote nzuri ya Biblia, kama lilivyo katika maandiko ya awali. Alikataa kufuata ile desturi ya kutumia majina ya cheo kama vile “Mungu” au “Bwana” badala ya jina la kimungu. Katika dibaji ya tafsiri yake, alieleza sababu zake waziwazi kama ilivyo kawaida yake.

“Tumelihifadhi hilo jina (Iehoua), kwa kuwa tulikuwa na sababu zilizo nzito zaidi. Kwanza, kwa sababu kila lipatikanapo katika tafsiri yetu, lapatikana vilevile katika maandiko ya Kiebrania, na twaona kwamba hatungeweza kuliacha au kulibadili bila kukosa uaminifu na kuvunja sheria ya Mungu, iamuruyo kwamba chochote kisiondolewe au kuongezwa. . . . Ile desturi [ya kuliacha hilo jina], iliyoanzishwa na Ibilisi, ilitokana na marabi wenye ushirikina ambao, ingawa wadai wanalistahi, kwa hakika wamelificha jina Lake takatifu, wakifanya watu wa Mungu wasahau jina ambalo alitaka atofautishwe kwalo kutoka kwa . . . miungu mingine.”

Tamaa ya Reina ya kulitukuza jina la Mungu istahiliyo pongezi imekuwa na matokeo makubwa sana. Hadi siku yetu, tafsiri nyingi za Kihispania—za Kikatoliki na Kiprotestanti—zimefuata kielelezo hicho, kwa kutumia jina la kimungu kotekote. Kimsingi, kwa sababu ya Reina, wasomaji wa karibu tafsiri yoyote ya Kihispania ya Biblia waweza kutambua kwa urahisi kwamba Mungu ana jina la kibinafsi linalomtofautisha na miungu mingine yote.

Jambo la kutokeza ni ule uhakika wa kwamba jina la Yehova katika Kiebrania laonekana wazi katika ukurasa wa kichwa wa Biblia ya Reina. Reina alitoa uhai wake kwa ajili ya kazi muhimu ya kulihifadhi Neno la Mungu, akifanya lipatikane katika lugha ambayo mamilioni wangeweza kuisoma.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki