Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • wt sura 14 kur. 128-135
  • Yehova Analiongozaje Tengenezo Lake?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Analiongozaje Tengenezo Lake?
  • Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kutambua Tengenezo Linaloonekana
  • Tengenezo Linaloongozwa na Mungu
  • Tengenezo la Mungu Linaloonekana
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Kaa Salama Ukiwa Sehemu ya Tengenezo la Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Uwe Mshikamanifu kwa Kristo na kwa Mtumwa Wake Mwaminifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • “Wakumbukeni Wale Wanaoongoza Kati Yenu”
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
Pata Habari Zaidi
Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
wt sura 14 kur. 128-135

Sura ya Kumi na Nne

Yehova Analiongozaje Tengenezo Lake?

1. Biblia inasema nini kuhusu tengenezo la Yehova, na kwa nini jambo hilo ni muhimu kwetu?

JE, MUNGU ana tengenezo? Maandiko matakatifu yanatuambia kwamba analo. Katika Neno lake, anatueleza kuhusu sehemu ya kimbingu ya tengenezo lake lenye kustaajabisha. (Ezekieli 1:1, 4-14; Danieli 7:9, 10, 13, 14) Ingawa tengenezo hilo halionekani, linawaathiri sana waabudu wa kweli leo. (2 Wafalme 6:15-17) Pia kuna sehemu inayoonekana ya tengenezo la Yehova hapa duniani. Biblia hutueleza kuhusu tengenezo hilo na jinsi Yehova anavyoliongoza.

Kutambua Tengenezo Linaloonekana

2. Mungu alianzisha kutaniko gani jipya?

2 Taifa la Israeli lilikuwa kutaniko la Mungu kwa miaka 1,545. (Matendo 7:38) Lakini Waisraeli walikosa kutii sheria za Mungu na wakamkataa Mwanaye. Kwa hiyo Yehova alilikataa kutaniko hilo na akalitupilia mbali kabisa. Yesu aliwaambia Wayahudi hivi: “Tazameni! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 23:38) Kisha Mungu akaanzisha kutaniko jipya, na akafanya agano jipya nalo. Kutaniko hilo lilikuwa na watu 144,000 waliochaguliwa na Mungu ili waungane na Mwanaye mbinguni.—Ufunuo 14:1-4.

3. Ni nini kilichotukia Pentekoste mwaka wa 33 W.K. kilichoonyesha waziwazi kwamba Mungu alikuwa akitumia kutaniko jipya kuanzia wakati huo?

3 Washiriki wa kwanza wa kutaniko hilo jipya walitiwa mafuta kwa roho takatifu ya Yehova wakati wa Pentekoste, mwaka wa 33 W.K. Twasoma hivi kuhusu tukio hilo lenye kustaajabisha: “Basi siku ya msherehekeo wa Pentekoste ilipokuwa ikiendelea walikuwa wote pamoja mahali palepale, na kwa ghafula kukatokea kutoka mbinguni kelele sawa na ile ya pepezi yenye nguvu inayovuma kwa kasi, nayo ikajaza nyumba yote ambayo katika hiyo walikuwa wameketi. Na ndimi kama kwamba za moto zikawa zenye kuonekana kwao, nazo zikagawanywa huku na huku, na mmoja ukaketi juu ya kila mmoja wao, nao wote wakawa wenye kujazwa roho takatifu.” (Matendo 2:1-4) Kwa hiyo, roho ya Mungu ilionyesha waziwazi kwamba Mungu angetumia kutaniko hilo kutimiza kusudi lake chini ya mwongozo wa Yesu Kristo akiwa mbinguni.

4. Ni nani leo walio tengenezo la Yehova linaloonekana?

4 Leo, ni mabaki tu ya wale 144,000 ndio walioko duniani. Lakini kupatana na unabii wa Biblia, mamilioni ya washiriki wa “umati mkubwa” wa “kondoo wengine,” wamejiunga na mabaki watiwa mafuta. Yesu, yule Mchungaji Mwema, ameunganisha hao kondoo wengine na mabaki katika kundi moja akiwa Mchungaji wao mmoja. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:11, 16) Makundi yote mawili yanakuwa kutaniko moja lenye umoja, tengenezo la Yehova linaloonekana.

Tengenezo Linaloongozwa na Mungu

5. Ni nani anayeliongoza tengenezo la Mungu, naye analiongozaje?

5 Usemi wa Kimaandiko “kutaniko la Mungu aliye hai” unaonyesha waziwazi ni nani anayeliongoza. Tengenezo hilo linatawaliwa na Mungu. Yehova huwaongoza watu wake kupitia Neno lake takatifu, Biblia, na pia kupitia Yesu, ambaye Alimweka rasmi kuwa Kichwa asiyeonekana wa kutaniko.—1 Timotheo 3:14, 15; Waefeso 1:22, 23; 2 Timotheo 3:16, 17.

6. (a) Ni matukio gani yanayothibitisha kwamba kutaniko lilielekezwa kutoka mbinguni katika karne ya kwanza? (b) Twajuaje kwamba Yesu angali Kichwa cha kutaniko?

6 Mwongozo huo ulionekana wazi wakati wa Pentekoste. (Matendo 2:14-18, 32, 33) Ulionekana pia malaika wa Yehova alipoelekeza kazi ya kuhubiri habari njema katika Afrika, Yesu alipotoa maagizo kuhusiana na kugeuzwa kwa Sauli wa Tarso, na wakati Petro alipoanza kuwahubiria watu wa Mataifa. (Matendo 8:26, 27; 9:3-7; 10:9-16, 19-22) Hata hivyo, baada ya muda, sauti hazikusikika tena kutoka mbinguni, malaika hawakuja duniani tena, na hakukuwa tena na zawadi za kufanya miujiza kwa uwezo wa roho. Lakini Yesu aliahidi hivi: “Tazameni! mimi nipo pamoja nanyi siku zote hadi umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:20; 1 Wakorintho 13:8) Leo, Mashahidi wa Yehova wanafuata mwongozo wa Yesu. La sivyo, hawangeweza kamwe kutangaza ujumbe wa Ufalme wanapokabili upinzani mkali.

7. (a) “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ni nani, na kwa nini? (b) “Mtumwa” huyo alikabidhiwa kazi gani?

7 Muda mfupi kabla ya kufa, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba Yeye akiwa Bwana-Mkubwa angemkabidhi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” daraka la pekee. “Mtumwa” huyo angekuwapo Bwana alipokuwa akipaa mbinguni na bado angekuwa akifanya kazi kwa bidii Kristo arudipo bila kuonekana akiwa na mamlaka ya Ufalme. Bila shaka mtu mmoja hawezi kutimiza maneno hayo, bali kutaniko la Kristo la watiwa mafuta linaweza kufanya hivyo. Baada ya kulinunua kwa damu yake, Yesu aliliita “mtumwa” wake. Aliwaamuru washiriki wa kutaniko hilo wafanye wanafunzi na kuwalisha hatua kwa hatua, kwa kuwapa “chakula chao [cha kiroho] kwa wakati ufaao.”—Mathayo 24:45-47; 28:19; Isaya 43:10; Luka 12:42; 1 Petro 4:10.

8. (a) Jamii ya mtumwa ina daraka gani sasa? (b) Kwa nini ni muhimu kutii maagizo ambayo Mungu anatoa kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu?

8 Ushuhuda unaonyesha kwamba jamii ya mtumwa ilikabidhiwa kazi zaidi mwaka wa 1919, kwa sababu Bwana-Mkubwa aliporudi bila kuonekana mnamo mwaka wa 1914, aliwakuta wakifanya kazi yake kwa uaminifu. Tangu mwaka huo habari za Ufalme zimekuwa zikihubiriwa ulimwenguni pote, na umati mkubwa wa waabudu wa Yehova unakusanywa ili uweze kuokoka dhiki kubwa. (Mathayo 24:14, 21, 22; Ufunuo 7:9, 10) Jamii ya mtumwa inawapa wao pia chakula cha kiroho wanachohitaji. Tunapaswa kukubali na kufuata maagizo ambayo Yehova anatoa kupitia jamii hiyo ikiwa twataka kumpendeza.

9, 10. (a) Ni nani waliojibu maswali kuhusu mafundisho na kuelekeza kazi ya kuhubiri habari njema katika karne ya kwanza? (b) Ni nani wanaoelekeza utendaji wa watu wa Yehova leo?

9 Nyakati nyingine maswali huzuka kuhusu mafundisho na jinsi ya kufanya mambo. Basi tufanyeje? Andiko la Matendo sura ya 15 linatuambia jinsi swali kuhusu watu wa Mataifa waliogeuzwa imani lilivyotatuliwa. Swali hilo lilipelekwa kwa mitume na wanaume wazee huko Yerusalemu, ambao walitumikia wakiwa baraza linaloongoza. Wanaume hao hawakuwa wakamilifu, lakini Mungu aliwatumia. Walichunguza maandiko yaliyozungumzia jambo hilo na vilevile ushuhuda wa utendaji wa roho ya Mungu katika kuwakubali watu wa Mataifa. Kisha wakafanya uamuzi. Mungu alibariki mpango huo. (Matendo 15:1-29; 16:4, 5) Baraza linaloongoza liliwatuma watu kuendeleza kazi ya kuhubiri habari za Ufalme.

10 Leo, washiriki wa Baraza Linaloongoza la tengenezo la Yehova linaloonekana ni ndugu waliotiwa mafuta kwa roho kutoka nchi mbalimbali na liko katika makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova. Baraza Linaloongoza likiwa chini ya ukichwa wa Yesu Kristo linaendeleza ibada safi katika kila nchi kwa kuelekeza kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova katika makumi ya maelfu ya makutaniko yao. Washiriki wa Baraza Linaloongoza wana maoni kama ya mtume Paulo ambaye aliwaandikia Wakristo wenzake hivi: “Si kwamba sisi ndio mabwana-wakubwa juu ya imani yenu, bali sisi ni wafanyakazi wenzi kwa shangwe yenu, kwa maana ni kwa imani yenu kwamba nyinyi mnasimama.”—2 Wakorintho 1:24.

11. (a) Wazee na watumishi wa huduma wanawekwaje rasmi? (b) Kwa nini tunapaswa kushirikiana kwa ukaribu na wale waliowekwa rasmi?

11 Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote hutegemea Baraza Linaloongoza liteue ndugu wanaostahili ambao wanapewa mamlaka ya kuwaweka rasmi wazee na watumishi wa huduma ambao wanatunza makutaniko. Biblia inataja matakwa ya wale wanaowekwa rasmi na inasema wazi kwamba wanaume hao hukosea kwa sababu si wakamilifu. Wazee wanaowapendekeza wengine na wale ambao wanawaweka rasmi wana daraka zito mbele za Mungu. (1 Timotheo 3:1-10, 12, 13; Tito 1:5-9) Kwa hiyo, wanasali ili roho ya Mungu iwasaidie na wanatafuta mwongozo katika Neno lake takatifu. (Matendo 6:2-4, 6; 14:23) Na tuonyeshe kwamba tunawathamini wale ambao ni “zawadi zikiwa wanadamu,” ambao wanatusaidia kufikia “umoja katika imani.”—Waefeso 4:8, 11-16.

12. Yehova anawatumiaje wanawake katika tengenezo lake?

12 Maandiko yanasema kwamba wanaume ndio wanaopaswa kuwa waangalizi kutanikoni. Jambo hilo haliwashushii wanawake heshima, kwa sababu baadhi yao ni warithi wa Ufalme wa kimbingu, na wanatimiza sehemu kubwa ya kazi ya kuhubiri. (Zaburi 68:11) Wanawake wanachangia pia sifa nzuri ya kutaniko kwa kutimiza madaraka yao ya kifamilia kwa uaminifu. (Tito 2:3-5) Lakini wanaume waliowekwa rasmi ndio wanaofundisha kutanikoni.—1 Timotheo 2:12, 13.

13. (a) Biblia inawahimiza wazee wawe na maoni gani kuhusu wadhifa wao? (b) Sote tunaweza kushiriki katika pendeleo gani?

13 Mtu aliye na cheo cha juu ulimwenguni anaonwa kuwa mtu wa maana sana, lakini sheria inayofuatwa katika tengenezo la Mungu ni: “Yeye ajiendeshaye mwenyewe kama aliye mdogo zaidi miongoni mwenu nyote ndiye aliye mkubwa.” (Luka 9:46-48; 22:24-26) Maandiko yanawashauri wazee wawe waangalifu wasipige ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, lakini wawe vielelezo kwa kundi. (1 Petro 5:2, 3) Mashahidi wote wa Yehova, waume kwa wake, wana pendeleo la kumwakilisha Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu, kutangaza jina lake kwa unyenyekevu na kuwaambia watu wote kuhusu Ufalme wake.

14. Ukitumia maandiko yaliyotajwa, zungumzia maswali yaliyoorodheshwa mwishoni mwa fungu.

14 Inafaa tujiulize hivi: ‘Je, kweli ninaelewa na kuthamini jinsi Yehova anavyoliongoza tengenezo lake linaloonekana? Je, mtazamo wangu, usemi, na matendo yangu yanaonyesha hivyo?’ Kila mmoja wetu anaweza kujichunguza kwa kutafakari mambo yafuatayo.

Ikiwa ninajitiisha kabisa kwa Kristo akiwa Kichwa cha kutaniko, basi nitafanya nini kulingana na maandiko yafuatayo? (Mathayo 24:14; 28:19, 20; Yohana 13:34, 35)

Ninapokubali kwa uthamini maandalizi ya kiroho yanayotolewa na jamii ya mtumwa na Baraza lake Linaloongoza, ninamheshimu nani? (Luka 10:16)

Kila mtu kutanikoni, hasa wazee wanapaswa kuwatendeaje wengine? (Waroma 12:10)

15. (a) Mtazamo wetu kuelekea tengenezo la Yehova linaloonekana unaonyesha nini? (b) Tunawezaje kumthibitisha Ibilisi kuwa mwongo na kuufurahisha moyo wa Yehova?

15 Yehova anatuongoza leo kupitia tengenezo lake linaloonekana ambalo linaongozwa na Kristo. Mtazamo wetu kuelekea mpango huo unaonyesha jinsi tunavyohisi kuhusu suala la enzi kuu ya ulimwengu. (Waebrania 13:17) Shetani anadai kwamba tunataka tu kujifaidi. Lakini tukitumikia kwa njia yoyote ile na kuepuka kujitukuza, tunamthibitisha Ibilisi kuwa mwongo. Tukiwapenda na kuwaheshimu wale wanaotuongoza na ‘kutowastaajabia watu mashuhuri kwa ajili ya manufaa yetu wenyewe,’ tunamfurahisha Yehova. (Yuda 16; Waebrania 13:7) Tunapokuwa waaminifu kwa tengenezo la Yehova, tunaonyesha kwamba Yehova ni Mungu wetu na kwamba tunamwabudu kwa umoja.—1 Wakorintho 15:58.

Mazungumzo ya Kurudia

• Tengenezo la Yehova linaloonekana leo ni nini? Na kusudi lake ni nini?

• Ni nani aliyewekwa rasmi kuwa Kichwa cha kutaniko, naye anatuelekeza kwa upendo kupitia mipango gani inayoonekana?

• Tunapaswa kuwa na maoni gani yanayofaa kuelekea wale walio katika tengenezo la Yehova?

[Picha katika ukurasa wa 133]

Yehova anatuongoza kupitia tengenezo lake linaloonekana ambalo linaongozwa na Kristo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki