Sura 23
Tengenezo la Mungu Linaloonekana
1. Biblia inasema nini juu ya tengenezo la Mungu lisiloonekana?
NI KWA SABABU gani tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu ana tengenezo linaloonekana? Sababu moja ni kwamba yeye ana tengenezo lisiloonekana. Yehova aliumba makerubi, maserafi na malaika wengine wengi wafanye mapenzi yake katika mbingu. (Mwanzo 3:24; Isaya 6:2, 3; Zaburi 103:20) Yesu Kristo ndiye Malaika Mkuu juu ya wote hao. (1 Wathesalonike 4:16; Yuda 9; Ufunuo 12:7) Biblia inawasimulia malaika kuwa wametengenezwa kuwa “viti vya enzi au maubwana au serikali nyingi au mamlaka nyingi.” (Wakolosai 1:16; Waefeso 1:21, NW) Wote hao wanatumikia kwa kufuata amri ya Yehova, wakifanya kazi ambayo amewapa kwa umoja.—Danieli 7:9, 10; Ayubu 1:6; 2:1.
2. Namna Mungu alivyoumba ulimwengu wetu unaoonekana inaonyeshaje kwamba anazingatia sana tengenezo?
2 Vilevile tunapata kuujua umaana ambao Mungu anaweka juu ya tengenezo tunapovifikiria vitu vinavyoonekana alivyoviumba. Kwa mfano, kuna maelfu ya mabilioni ya nyota katika ulimwengu mzima yaliyopangwa katika makundi makubwa sana yanayoitwa magalaksi. Magalaksi hayo yanasafiri katika anga kwa utaratibu mzuri, hata nyota moja moja na sayari zilizo katika magalaksi hayo. Kwa mfano, dunia-sayari yetu inasafiri kila mwaka kuzunguka jua, ambalo ndilo nyota yetu ya karibu zaidi. Na inafanya hivyo muda wa siku 365, saa 5, dakika 48 na sekunde 45.51 barabara. Ndiyo, ulimwengu mzima wa vitu vinavyoonekana umefanyiwa mipango yenye utaratibu bora sana!
3. Tengenezo zuri kati ya viumbe vya Mungu visivyoonekana na katika ulimwengu wa vitu vinavyoonekana linatufundisha nini?
3 Je! tengenezo hilo la ajabu kati ya viumbe vya Mungu visivyoonekana na katika ulimwengu wake wa vitu vinavyoonekana linatufundisha jambo fulani? Ndiyo, linatufundisha kwamba Yehova ni Mungu mwenye kupanga mambo kitengenezo (kwa utaratibu mzuri). Basi, bila shaka Mungu wa namna hiyo hangewaacha wanadamu wanaompenda kweli kweli duniani wasiwe na mwongozo na tengenezo.
TENGENEZO LA MUNGU LINALOONEKANA—LA ZAMANI NA LA SASA
4, 5. Tunajuaje kwamba Mungu aliongoza watu wake kwa njia ya kitengenezo siku za Abrahamu na za taifa la Israeli?
4 Biblia inaonyesha kwamba nyakati zote Yehova ameongoza watumishi wake kwa njia ya kitengenezo. Kwa mfano, watu wenye imani kama vile Abrahamu waliongoza jamaa zao na watumishi wao katika kumwabudu Yehova. Yehova alimjulisha Abrahamu mapenzi yake kwa kusema naye. (Mwanzo 12:1) Naye Mungu akamwagiza awapitishie wengine taarifa hiyo, akisema: “Kwa maana nimemjua [Abrahamu] ya kwamba atawaamuru wanawe, na nyumba yake baada yake waishike njia ya [Yehova].” (Mwanzo 18:19) Hapo palikuwapo mpango wenye utaratibu wa kuwa na kikundi cha watu ili wamwabudu Yehova sawasawa.
5 Baadaye, Waisraeli walipoongezeka wakawa mamilioni, Yehova hakuruhusu kila mtu aabudu katika njia yake mwenyewe, tofauti na mpango wo wote wa kitengenezo. Hapana, Waisraeli walifanyizwa kuwa taifa la waabudu waliopangwa kitengenezo. Taifa hilo la Israeli liliitwa “kundi la Yehova.” (Hesabu 20:4; 1 Mambo ya Nyakati 28:8, NW) Kama ungalikuwa mwabudu wa kweli wa Yehova wakati huo, ungalilazimika kuwa sehemu ya kundi hilo la waabudu, wala hungalijitenga nalo.—Zaburi 147:19, 20.
6. (a) Mungu alionyeshaje kwamba kibali yake ilikuwa juu ya wafuasi wa Kristo? (b) Kuna ushuhuda gani wa kuonyesha kwamba Wakristo walipangwa kitengenezo kwa ajili ya ibada?
6 Katika karne ya kwanza hali ilikuwaje? Biblia inaonyesha kwamba kibali ya Yehova ilikuwa juu ya wafuasi wa Yesu Kristo Mwanaye. Yehova alimwaga roho takatifu yake juu yao. Ili kuonyesha kwamba sasa yeye alikuwa akitumia tengenezo hilo la Kikristo badala ya taifa la Israeli, aliwapa Wakristo fulani wa kwanza uwezo wa kuponesha wagonjwa, kufufua wafu na kufanya miujiza mingine. Huwezi kusoma Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo bila kuvutwa sana na uhakika wa kwamba Wakristo walipangwa kitengenezo ili watoe ibada. Kwa kweli, waliamriwa wakutane pamoja kwa kusudi hilo. (Waebrania 10:24, 25) Basi kama wewe ungalikuwa mwabudu wa kweli wa Yehova katika karne ya kwanza, ungalilazimika kuwa sehemu ya tengenezo lake la Kikristo.
7. Tunajuaje kwamba Yehova hakutumia zaidi ya tengenezo moja katika kipindi cho chote?
7 Je! Yehova amepata kutumia zaidi ya tengenezo moja wakati wa kipindi cho chote? Katika siku za Noa ni Noa peke yake na wale waliokuwa pamoja naye ndani ya safina waliolindwa na Mungu wakaiokoka gharika. (1 Petro 3:20) Vilevile, katika karne ya kwanza hakukuwako matengenezo ya Kikristo mawili au zaidi. Mungu alishughulika na tengenezo lile moja tu. Kulikuwako “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja” tu. (Waefeso 4:5) Vilevile katika wakati wetu Yesu Kristo alitabiri kwamba kungekuwako chanzo kimoja tu cha mafundisho ya kiroho kwa ajili ya watu wa Mungu.
8. Yesu alionyeshaje kwamba kungekuwako tengenezo moja tu la Mungu lenye kuonekana duniani katika wakati wetu?
8 Alipokuwa akisimulia kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme, Yesu alisema: “Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote.” (Mathayo 24:45-47) Aliporudi katika mamlaka ya Ufalme mwaka wa 1914, je! Kristo alikuta jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ikitoa “chakula” au taarifa ya kiroho? Ndiyo, alikuta “mtumwa” huyo ambaye ndiyo jamii ya waliobaki duniani wa “ndugu” zake 144,000. (Ufunuo 12:10; 14:1, 3) Na tangu mwaka wa 1914 mamilioni ya watu wamekikubali “chakula” wanachotoa, nao wameanza kuizoea dini ya kweli pamoja nao. Tengenezo hilo la watumishi wa Mungu linajulikana kuwa Mashahidi wa Yehova.
9. (a) Ni kwa sababu gani watumishi wa Mungu wana jina Mashahidi wa Yehova? (b) Ni kwa sababu gani wanaita mahali pao pa ibada Majumba ya Ufalme?
9 Mashahidi wa Yehova wanamtegemea Mungu na Neno lake ili wapate kuelekezwa katika yote wanayofanya. Jina lao lenyewe Mashahidi wa Yehova linaonyesha kwamba utendaji wao mkuu ni kutoa ushuhuda juu ya jina na ufalme wa Yehova Mungu, kama alivyofanya Kristo. (Yohana 17:6; Ufunuo 1:5) Vilevile, mahali ambapo wanakutania kwa ibada wanapaita Jumba la Ufalme kwa sababu ufalme wa Mungu kupitia Masihi au Kristo, ndicho kichwa kikuu cha mazungumzo ya Biblia nzima. Kwa kuwa ni wazi kwamba Ukristo ule wa karne ya kwanza ulikuwa na kibali ya Mungu, Mashahidi wa Yehova wanafuatisha tenge-nezo lao kulingana na kielelezo hicho. Ebu tuangalie kifupi tengenezo hilo la Kikristo la kwanza kisha tuyaone mambo yanayofanana na ya tengenezo la Mungu linaloonekana leo.
KIELELEZO CHA KARNE YA KWANZA
10. Nyingine kati ya sehemu zilizokuwa katika tengenezo la Kikristo la karne ya kwanza ni sehemu gani?
10 Po pote walipokuwapo Wakristo katika karne ya kwanza, walikusanyika pamoja katika vikundi ili waabudu. Makundi hayo yalikutana kikawaida kwa ushirika na kwa funzo. (Waebrania 10:24, 25) Utendaji wao mkuu ulikuwa ni kuhubiri na kufundisha juu ya ufalme wa Mungu, kama Kristo alivyofanya. (Mathayo 4:17; 28:19, 20) Kama mshiriki wa kundi hilo alifuata njia mbaya ya maisha, aliondolewa katika kundi hilo.—1 Wakorintho 5:9-13; 2 Yohana 10, 11.
11, 12. (a) Ni nini kinachohakikisha kwamba makundi ya kwanza ya Kikristo yalipokea mwongozo na mwelekezo kutoka kwa mitume na “wanaume wazee” katika Yerusalemu? (b) Maana yake nini kusema mwelekezo “wa kitheokrasi”? (c) Matokeo ya kukubali mwelekezo huo yalikuwa nini kwa makundi?
11 Je! makundi hayo ya Kikristo katika karne ya kwanza yalikuwa yasiyotegemeana, kila kundi likijifanyia maamuzi yalo lenyewe? Hapana, Biblia inaonyesha kwamba yaliungana katika ile imani moja ya Kikristo. Makundi yote yalipokea mwongozo na mwelekezo kutoka chanzo kile kile kimoja. Hivyo, kulipotokea mabishano juu ya suala la tohara, makundi au watu mmoja mmoja hawakujiamulia wenyewe la kufanya. Hapana, badala yake, mtume Paulo, Barnaba na wengine waliagizwa “wapande kwenda Yerusalemu kwa mitume na wazee kwa habari ya swali hilo.” Wanaume hao waliokomaa, wakisaidiwa na Neno la Mungu na ‘roho yake takatifu,’ walipofanya uamuzi wao, walituma wanaume waaminifu wakayapashe makundi habari.—Matendo 15:2, 27-29.
12 Makundi yalipata matokeo gani yalipopokea mwongozo na mwelekezo huo uliotolewa na Mungu, au wa kitheokrasi? Biblia inasema: “Basi [mtume Paulo na wenzake] walipoendelea kusafiri katika miji walikuwa wakiwapelekea wale waliokuwa huko washike maamuzi yaliyokuwa yameamuliwa na mitume na wanaume wazee waliokuwa katika Yerusalemu. Kwa hiyo, makundi yakaendelea kuthibitika kweli kweli katika imani na kuongezeka katika hesabu siku kwa siku.” (Matendo 16:4, 5, NW) Ndiyo, makundi yote yalifuata mambo ambayo baraza ya wanaume wazee katika Yerusalemu ilikuwa imeamua, nayo yakazidi kuwa na nguvu katika imani.
MWELEKEZO WA KITHEOKRASI LEO
13. (a) Tengenezo la Mungu linaloonekana linapokea mwongozo leo kutoka mahali gani duniani na kupitia baraza gani ya wanaume? (b) Baraza inayoongoza ina uhusiano gani na yule “mtumwa mwaminifu mwenye akili”?
13 Tengenezo la Mungu linaloonekana leo linapokea vilevile mwongozo na mwelekezo wa kitheokrasi. Katika makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York, kuna baraza inayoongoza ya wanaume wazee Wakristo kutoka sehemu mbalimbali za dunia wanaotoa uangalizi unaohitajiwa wa shughuli za ulimwenguni pote za watu wa Mungu. Walio katika hiyo baraza inayoongoza ni washiriki wa “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” Baraza hiyo inatumika kuwa msemaji wa huyo “mtumwa mwaminifu.”
14. Baraza inayoongoza ya watu wa Mungu inategemea nini wakati wa kufanya maamuzi?
14 Kama wale mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu, wanaume wa hiyo baraza inayoongoza wana miaka mingi ya ujuzi katika utumishi wa Mungu. Lakini wao hawategemei hekima ya kibinadamu katika kufanya maamuzi. Hapana, wanaongozwa kitheokrasi, kisha wanaufuata mfano ule wa ile baraza inayoongoza ya kwanza iliyokuwako Yerusalemu, ambayo maamuzi yake yalitegemea Neno la Mungu na kuamuliwa kwa mwelekezo wa roho takatifu.—Matendo 15:13-17, 28, 29.
KUELEKEZA TENGENEZO LA ULIMWENGUNI POTE
15. Sababu gani maneno ya Yesu katika Mathayo 24:14 yanaonyesha kwamba Mungu angekuwa na tengenezo kubwa duniani wakati wa mwisho?
15 Yesu Kristo alidokeza ukubwa wa tengenezo ambalo Mungu angekuwa nalo duniani wakati huu wa mwisho aliposema: “Na habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14, NW) Ebu ifikirie kazi kubwa inayohitajiwa kufanywa ili kuyaambia maelfu ya mamilioni ya watu wa dunia juu ya ufalme wa Mungu uliosimamishwa. Je! tengenezo la Kikristo la kisasa, linalotegemea baraza inayoongoza lipate mwongozo na mwelekezo, lina vifaa vya kufanyia kazi hiyo kubwa?
16. (a) Ni kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wamejenga matbaa nyingi kubwa? (b) Ni nini kinachopigwa chapa katika matbaa hizo?
16 Sasa Mashahidi wa Yehova wanauhubiri ujumbe wa Ufalme katika nchi na visiwa vya bahari zaidi ya 200 katika dunia yote. Ili kuwasaidia wahubiri wa Ufalme zaidi ya 2,300,000 (katika mwaka wa 1981) watimize kazi hiyo, matbaa (viwanda vya kupigia chapa) kubwa zimejengwa katika nchi nyingi. Humo ndimo Biblia na vitabu vya kusaidia watu kujifunza Biblia vinamochapishwa kwa idadi; kubwa sana. Kila siku, kwa wastani, magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zaidi ya milioni moja yanachapishwa na kusafirishwa kutoka matbaa hizi.
17. (a) Ni kwa sababu gani vitabu hivi vya kusaidia watu kujifunza Biblia vinatayarishwa? (b) Unakaribishwa ufanye nini?
17 Vitabu vyote hivyo vya kusaidia watu kujifunza Biblia vinatayarishwa ili kusaidia watu wapate maendeleo katika maarifa ya kujua makusudi matukufu ya Yehova. Kwa kweli, maneno “Unaotangaza Ufalme wa Yehova” ni sehemu ya jina la gazeti Mnara wa Mlinzi. Unakaribishwa ushiriki kugawa gazeti hilo la Kibiblia na kuwaeleza wengine zile kweli za Biblia zilizomo. Kwa mfano, je! kuna mtu fulani unayeweza kushiriki naye taarifa ya maana sana ambayo umejifunza katika kitabu hiki, Unaweza Kuishi Kanada Milele Katika Paradiso Duniani?
18. (a) Tengenezo la Mungu leo ni tengenezo la aina gani? (b) Kwa sababu gani watu wa Mungu wanahitaji kipa-moyo kingi sasa?
18 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, tengenezo la Mungu leo ni tengenezo la wahubiri wa Ufalme waliojiweka wakf na kubatizwa. Na limewekwa ili kusaidia washiriki wake wote waushiriki utendaji huo wa kuhubiri. Watu hao wanahitaji kipa-moyo kikubwa sana na kutiwa nguvu nyingi za kiroho, kwa kuwa Shetani na wale anaoweza kuwavuta wamfuate wanaupinga ujumbe wa Ufalme. Wapinzani hao waliagiza Yesu auawe kwa sababu ya kuuhubiri, nayo Biblia inaonya kwamba wafuasi wake wangeteswa pia.—Yohana 15:19, 20; 2 Timotheo 3:12.
19. (a) Ni akina nani wanaotolewa sasa ili wasaidie watu wa Mungu na kuwatia nguvu? (b) Kundi linalindwaje lisipatwe na mavutano mabaya ambayo yangeweza kulichafua?
19 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza ndivyo na leo “wanaume wazee” wanavyowekwa wasaidie kila kundi na kulitia nguvu. Wanaweza kukusaidia wewe pia kwa kukupa shauri la Biblia ili ushindane na matatizo mbalimbali. Wazee hao wanalilinda vilevile “lile kundi la Mungu.” Hivyo, mshiriki wa kundi anapofuata njia mbaya ya maisha na kukataa kubadilika, “wanaume wazee” hao wanahakikisha kwamba mtu huyo ameondoshwa nje, au ametengwa na ushirika, katika kundi hilo. Kwa njia hiyo, kundi safi lenye afya ya kiroho linadumishwa.—Tito 1:5; 1 Petro 5:1-3, NW; Isaya 32:1, 2; 1 Wakorintho 5:13.
20. (a) Ni nani katika karne ya kwanza waliotumwa na baraza inayoongoza ya Yerusalemu, na kwa sababu gani? (b) Ni nani wanaotumwa leo na baraza inayoongoza?
20 Vilevile, kama vile baraza inayoongoza katika Yerusalemu ilivyotuma wajumbe wa pekee, Paulo na Sila, wakatoe maagizo na kutoa kipa-moyo kwa watu wa Mungu, ndivyo na baraza inayoongoza ya leo inavyofanya katika wakati huu wa mwisho. (Matendo 15:24-27, 30-32) Karibu mara mbili kila mwaka mhudumu mwenye ujuzi, anayeitwa mwangalizi wa mzunguko, anaagizwa atumie juma moja akiwa na kila kundi katika mzunguko wake.
21. Mwangalizi wa mzunguko anasaidiaje makundi ya watu wa Mungu?
21 Kuna makundi ya Mashahidi wa Yehova zaidi ya 43,000 katika ulimwengu wote, na hayo yamegawanywa katika mizunguko yenye karibu makundi 20 kila mzunguko. Anapotembelea makundi yaliyo katika mzunguko wake, mwangalizi wa mzunguko anawajenga mashahidi wa Ufalme kwa kwenda pamoja nao katika utendaji wao wa kuhubiri na kufundisha. Zaidi ya kuwachochea katika njia hiyo, anatoa mawazo ya kuwasaidia wafanye huduma yao kuwa bora.—Matendo 20:20, 21.
22. (a) Ni mpango gani zaidi wa kuwatia nguvu watu wa Mungu unaofanywa mara mbili kila mwaka? (b) Ni mwaliko gani unaotolewa kwako?
22 Kipa-moyo na kitia-nguvu zaidi vinatolewa, kwa kuwa kwa ujumla makundi yaliyo katika kila mzunguko yanakutana pamoja mara mbili kwa mwaka, kwenye kusanyiko la mzunguko la siku mbili. Penye vipindi hivyo huenda kukawa na hesabu ya kuanzia wahudhuriaji 200 au 300 mpaka 2,000 au zaidi ya hao. Unakaribishwa uhudhurie kusanyiko lile litakalofuata katika eneo lenu. Tuna hakika kwamba utaliona kusanyiko hilo kuwa lenye kuburudisha kiroho na lenye kukufaidi binafsi.
23. (a) Ni mikusanyiko gani mingine inayofanywa mara moja kila mwaka? (b) Ukubwa wa mmoja wa mikusanyiko hiyo ulikuwaje?
23 Halafu, mara moja kila mwaka, mkusanyiko mkubwa zaidi unaoitwa kusanyiko la wilaya huenda ukafanywa kwa siku kadha. Sababu gani usijitahidi sana uhudhurie na kujionea mwenyewe namna kusanyiko kama hilo linavyoweza kuwa zuri na lenye kufaidi kiroho? Miaka fulani, badala ya makusanyiko ya wilaya, kumekuwako mikusanyiko mikubwa zaidi ya kitaifa au ya kimataifa. Kusanyiko kubwa zaidi lililopata kufanywa mahali pamoja ni lile lililokuwa katika wanja mbili za Mji wa New York, yaani, Yankee Stadium na Polo Grounds kwa siku nane katika mwaka wa 1958. Pindi hiyo watu 253,922 walihudhuria hotuba ya watu wote yenye kusema “Ufalme wa Mungu Unatawala—Je! Mwisho wa Ulimwengu U Karibu?” Tangu wakati huo hakuna mahali ambapo pameonekana kuwa pakubwa vya kutosha watu wengi hivyo, kwa hiyo mipango imefanywa ili miji mingi mikubwa itumiwe kwa mikusanyiko mikubwa.
MIKUTANO KATIKA MAKUNDI
24. Ni mikutano gani mitano ya kila juma inayofanywa na makundi ya watu wa Mungu?
24 Baraza inayoongoza ya Mashahidi wa Yehova inafanya mpango vilevile kuwe na programu yenye upatani mmoja ya maagizo ya Biblia inayofanywa katika makundi yote ya watu wa Yehova. Kila kundi lina mikutano mitano kila juma. Hiyo ni Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, Mkutano wa Utumishi, Mkutano wa Watu Wote, funzo la Mnara wa Mlinzi na funzo la kitabu la kundi. Kwa vile huenda ikawa bado hujapata habari juu ya mikutano hiyo, tutaieleza kifupi.
25, 26. Kusudi la Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi ni nini?
25 Kusudi la Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ni kusaidia wanafunzi wawe wenye matokeo zaidi katika kusema na wengine juu ya ufalme wa Mungu. Mara kwa mara, wale waliojiandikisha katika shule wanatoa hotuba fupi juu ya habari za Biblia wakihutubia kikundi kizima. Ndipo mzee mwenye ujuzi anapotoa mashauri ya kufanya maendeleo.
26 Kwa kawaida jioni iyo hiyo Mkutano wa Utumishi vilevile unafanywa. Muhtasari wa mkutano huo unachapwa katika Huduma ya Ufalme Yetu, kichapo cha kila mwezi chenye kurasa mbili au zaidi kinachotungwa na baraza inayoongoza. Wakati wa mkutano huo mashauri yenye kufaa na maonyesho juu ya njia zenye matokeo za kuzungumza na wengine juu ya ujumbe wa Ufalme yanatolewa. Kwa namna iyo hiyo, Kristo aliwatia moyo wafuasi wake na akawapa maagizo juu ya namna ya kutimiza huduma yao.—Yohana 21:15-17; Mathayo 10:5-14.
27, 28. Mkutano wa Watu Wote, funzo la Mnara wa Mlinzi na funzo la kitabu la kundi ni mikutano ya aina gani?
27 Vilevile Mkutano wa Watu Wote na wa funzo la Mnara wa Mlinzi inafanywa kwa kawaida Jumapili. Jitihada za pekee zinafanywa kuwakaribisha watu wapya wanaopendezwa waje kwenye Mkutano wa Watu Wote, ambao ni hotuba ya Biblia inayotolewa na mhudumu anayestahili. Funzo la Mnara wa Mlinzi ni mazungumzo ya maulizo na majibu ya makala ya Biblia iliyo katika toleo la karibuni la gazeti Mnara wa Mlinzi.
28 Ijapokuwa kundi zima huenda likakutana kwenye Jumba la Ufalme ili kuhudhuria mikutano iliyotangulia kutajwa, vikundi vidogo-vidogo vinakusanyika katika nyumba za faragha ili viwe na funzo la kitabu la kundi kila juma. Kitabu cha kusaidia kujifunza Biblia, kama hiki unachosoma, kinatumiwa kuwa msingi wa mazungumzo hayo ya Biblia, nayo yanaweza kuendelea kwa muda wa saa moja.
29. (a) Ni ukumbusho gani ambao Wakristo wa kweli wanaadhimisha kila mwaka? (b) Ni nani kwa kufaa wanaoshiriki kula mkate na kunywa divai?
29 Kuongeza kwenye mikutano hiyo ya kawaida, Mashahidi wa Yehova wanafanya mkutano wa pekee kila mwaka katika siku ambayo Yesu alikufa. Alipokuwa akifanya kwa mara ya kwanza mpango wa kuwa na ukumbusho huo wa kifo chake, Yesu alisema: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19, 20, NW) Wakati wa sherehe hiyo isiyo na mambo mengi Yesu alitumia divai na mkate usiotiwa chachu kuwa mifano ya uhai ambao alikuwa akikaribia kutolea wanadamu. Hivyo penye chakula hicho cha kila mwaka cha Ukumbusho mabaki walio duniani wa wale wafuasi 144,000 wa Kristo waliopakwa mafuta wanaonyesha wazi tumaini lao la kimbingu kwa kushiriki kula mkate na kunywa divai.
30. (a) Ni nani wengine ambao kwa kufaa wanahudhuria Ukumbusho, na mataraja yao ni nini? (b) Watu hao wanasimuliwa na Yesu kuwa namna gani?
30 Mamilioni wengine wanaohudhuria Ukumbusho katika Majumba ya Ufalme katika dunia yote wanafurahi kuwa watazamaji. Wao vilevile wanakumbushwa juu ya mambo ambayo Yehova Mungu na Yesu Kristo walifanya ili wao waweze kukombolewa katika dhambi na kifo. Lakini badala ya kutazamia uzima wa kimbingu, wanalifurahia taraja la kuishi milele katika paradiso duniani. Wako kama Yohana Mbatizaji aliyejisema kuwa “rafiki yake bwana arusi” badala ya kujisema kuwa sehemu ya bibi-arusi aliye na washiriki 144,000. (Yohana 3:29) Mamilioni hayo ya watu ni sehemu ya “kondoo wengine” ambao Yesu alitaja. Wao si washiriki wa lile “kundi dogo.” Walakini, kama Yesu alivyosema, wao wanatumikia kwa umoja wakiungana na lile “kundi dogo,” hivi kwamba wote ‘wanakuwa kundi moja.’—Yohana 10:16; Luka 12:32.
KUMTUMIKIA MUNGU PAMOJA NA TENGENEZO LAKE
31. Kuna ushuhuda gani wa kuonyesha kwamba Mungu hakubali wale wanaoendelea kuwa sehemu ya dini ya uongo na huku vilevile wakijaribu kuwa sehemu ya tengenezo lake?
31 Lo! ni wazi kama nini kwamba, katika nyakati za zamani, Yehova Mungu ana tengenezo linaloonekana leo! Yeye analitumia ili kuzoeza watu kwa ajili ya uzima katika mfumo (taratibu) wake mpya wenye uadilifu. Walakini, hatuwezi kuwa sehemu ya tengenezo la Mungu na wakati uo huo tuwe sehemu ya dini ya uongo. Neno la Mungu linasema: “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? . . . Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini?” Hivyo Mungu anaamuru hivi: “Tokeni kati yao, mkatengwe nao.”—2 Wakorintho 6:14-17.
32. (a) Ikiwa ‘tutatoka kati yao,’ ni lazima tufanye nini? (b) Ni baraka gani tutakayopokea tukichukua hatua iliyo hakika ya kumtumikia Mungu pamoja na tengenezo lake la kitheokrasi linaloonekana?
32 Maana yake nini ‘kutoka kati yao’? Bila shaka, hatungeweza kuwa tukitii amri hiyo kwa kuendelea kuwa sehemu ya tengenezo jingine la kidini au kuliunga mkono, badala ya lile ambayo Yehova Mungu anatumia. Basi ikiwa wo wote kati yetu bado ni wa tengenezo tofauti la kidini, ni lazima tutoe taarifa ya kuwaeleza kwamba sasa tumeliacha. Tukitoka sasa kati ya hao wanaozoea dini ya uongo na kuchukua hatua ya hakika tumtumikie Mungu pamoja na tengenezo lake la kitheokrasi linaloonekana, tutakuwa kati ya wale ambao Mungu anasema hivi juu yao: “Nitakaa [kati] yao, na kati yao nitatembea, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.”—2 Wakorintho 6:16..
[Picha katika ukurasa wa 192]
Wakati wa Gharika, je! Mungu alikuwa na zaidi ya tengenezo moja?
[Picha katika ukurasa wa 196]
MAKAO MAKUU YA MASHAHIDI WA YEHOVA ULIMWENGUNI
AFISI ZA UTEKELEZAJI
Mifumo ya Kompyuta
MATBAA YA BROOKLYN
Mashine za Chapa Aina ya Rotari
Ujalidi wa Vitabu
Idara ya Kusafirisha Vitabu
[Picha katika ukurasa wa 197]
BAADHI YA MATBAA NYINGINE NYINGI ZA MASHAHIDI WA YEHOVA
Brazili
Uingereza
Afrika Kusini
Wallkill, New York
Kanada
[Picha katika ukurasa wa 198]
Baadhi ya watu 253,922 waliohudhuria mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova katika New York
Polo Grounds
Yankee Stadium
[Picha katika ukurasa wa 201]
Programu ya maagizo ya Biblia inafurahiwa kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova