Tengenezo la Yehova Lenye Kusonga Mbele
“Njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.”—Mit. 4:18.
1. Tengenezo la Mungu la kwanza lilikuwa tengenezo gani?
ZAMANI sana kabla hajaumba mbingu na dunia, Yehova Mungu aliunda tengenezo lenye nguvu sana. Lilikuwa tengenezo la kimbinguni lililofanyizwa kwa viumbe ambao wana namna ya uhai ambao ni tofauti kabisa na mambo tunayojua sana. Miili yao inaonyesha utukufu wa Muumba wao kwa kuwa katika namna yake. Neno lake linatuambia hivi: “Mungu ni Roho.” (Yohana 4: 24) Na kwa habari ya viumbe hawa wa kimbinguni linasema kwamba yeye hufanya “malaika zake kuwa pepo [roho, NW].” (Zab. 104: 4) Wakiwa kama yeye, wanaweza kuishi alipo.
2. Sababu gani hatuwaoni viumbe wa kiroho, nasi twajuaje kwamba wako?
2 Wakiwa roho, viumbe hawa wa mbinguni wanafanyizwa kwa namna ya kitu ambacho ni tofauti kabisa na vitu tujuavyo vilivyoko katika ulimwengu wote wa vitu vyenye mwili. Kwa sababu hiyo hawaonekani kwa macho yetu. Hakuna namna yo yote ya nguvu zenye kutoa nuru au joto katika ulimwengu wote ambazo tunaweza kufahamu kwa milango yetu ya maarifa inayoweza kutufunulia kuwapo kwao. Wao hawana asili ya mambo ya kimwili ambayo yangetuwezesha tuwajue. Wao ni wa namna ya juu sana ya uhai tusiojua hata kidogo. Ijapokuwa hatuwezi kuona viumbe hawa wa kiroho, tunajua kwamba wako kwa sababu wamepashana habari na wanadamu mara kwa mara. Muumba wao hutuambia habari zao na juu ya kupashana habari huku, katika Neno lake lililoandikwa.
3. Viumbe hawa wa kiroho walionaje dunia ilipoumbwa?
3 Akisema na Ayubu juu ya kuumbwa kwa dunia, Yehova Mungu anafunua namna hawa viumbe wake wa kiroho walivyofurahi alipoiumba dunia mwanzoni: “Ulikuwa wapi nilipoiweka misingi ya nchi? . . . Hapo nyota za asubuhi zilipoimba pamoja, na wana wote wa Mungu walipopiga kelele kwa furaha? ” (Ayubu 38:4, 7) Viumbe hawa wa kiroho wenye utukufu walioumbwa katika asubuhi ya kuumba walikuwa kama nyota za asubuhi. Wao ndio waliokuwa vitu vya kwanza vyenye uhai vilivyoumbwa na Mungu. Walipoona kwamba Muumba wao alikuwa akijitayarisha kuumba viumbe wengine wenye uhai, walifurahi sana.
4, 5. (a) Wanadamu wamewezaje kuwaona viumbe hawa wa kiroho? (b) Eleza namna tunavyoweza kujua kwamba kuna tengenezo la kimbinguni na kazi za makerubi ni kazi gani.
4 Kwa kuwavika miili na kwa njia ya njozi, Mungu aliwawezesha wanaume waaminifu wa nyakati zilizopita wawaone viumbe hawa wa kiroho na kuandika waliyoyaona. Danieli na Yohana walikuwa wanaume kama hao. Akiwa chini ya uongozi wa Mungu Danieli aliona makutano ya viumbe wa kiroho walioumbwa na Yehova. Aliwaona wakiwa wamekusanyika kuzunguka Muumba wao wakiwa tayari kumtumikia. Kwa kuwa Yehova ni Mungu wa utaratibu, bila shaka lazima awafanye hawa viumbe wa kimbinguni kuwa tengenezo. Angewafanya kuwa tengenezo lenye nguvu lililojitoa katika kufanya mapenzi yake. Danieli anatuambia yale aliyoona: “Maelfu elfu wakamtumikia, na elfu kumi mara elfu kumi wakasimama mbele zake.” (Dan. 7:10) Njozi inayofanana na hiyo ya jeshi la kimbinguni iliandikwa na Yohana, mtume wa Yesu Kristo. “Nikaona [, na] nikasikia sauti ya malaika wengi pande zote za kile kiti cha enzi, na za wale wenye uhai, na za wale wazee, na hesabu yao ilikuwa elfu kumi mara elfu kumi na elfu mara elfu.” (Ufu. 5:11) Kwa njozi hizi tunaona kwamba viumbe wa kiroho wa Mungu wanafanyizwa kuwa tengenezo la kimbinguni.
5 Katika njozi zote mbili, viumbe hawa wa kiroho wanaonekana wakikusanyika kukizunguka kiti cha enzi cha Muumba, Yehova. Hii inaonyesha kwamba wao ni watumishi wa Mungu waliotengezwa, nao wako tayari kumtumikia. Wengine wanamtumikia, ikionyesha kwamba wana migawo ya kazi waliyogawiwa kwa utaratibu. Neno la Mungu latujulisha kwamba amewaweka viumbe hawa katika vyeo mbalimbali vyenye madaraka. Wengine ni makerubi ambao huambatana kipekee na kiti chake cha enzi. Wao wanategemeza utukufu na ukuu wake po pote wanapogawiwa kufanya kazi. Wanatajwa kwa mara ya kwanza katika Biblia katika Mwanzo 3:24, pasemapo kwamba makerubi waliwekwa mlangoni wa kuingia katika bustani ya Edeni waitegemeze enzi kuu ya Yehova kwa kuwazuia wanadamu waasi wasirudi katika bustani hiyo.
6. (a) Maserafi ni akina nani? (b) Jeshi la mfano la kimalaika ni lenye ukubwa kadiri gani?
6 Kundi jingine la viumbe wa kiroho linaitwa maserafi. Wana kazi ya kuondoa uchafu katika tengenezo la Yehova na kutangaza utukufu wake. Wanatajwa katika njozi aliyopewa nabii Isaya akaiandika katika Isaya 6:1-3. Maelfu wengi wa hawa viumbe wa kiroho wanatumiwa kama wajumbe na katika utumishi mwingine. Viumbe hawa wengi wa kimbinguni wanatajwa katika kitabu cha Ufunuo kuwa sehemu ya jeshi kubwa litakalotumiwa na Mungu kuharibu adui zake katika vita inayokuja ya Har–Magedoni. Ikiwa jeshi la malaika ndilo linalofananishwa katika Ufunuo 9:16, hesabu yao inaonyeshwa kuwa elfu ishirini (20) mara elfu kumi, ambayo ni milioni 200. Hilo ni tengenezo kubwa kweli kweli.
TENGENEZO LA KIMBINGUNI LASONGA MBELE
7, 8. (a) Eleza namna tengenezo la Mungu la kimbinguni lilivyosonga mbele. (b) Toa mfano wa namna walivyosonga mbele.
7 Kutoka mwanzo wake tengenezo la kimbinguni la Mungu limeendelea kusonga mbele. Limeendelea kupata ufahamu mwingi zaidi wa makusudi ya Yehova na katika kupata mapendeleo makubwa zaidi ya utumishi. Ijapokuwa viumbe hawa wengi wa kimbinguni waliomo ni wakamilifu, Mungu hakuwajulisha yote yanayoweza kujulikana, wakati wa kuumbwa kwao, sawasawa kama vile hakuwajulisha mwanamume na mwanamke wa kwanza. Sikuzote kuna mengi zaidi wanayoweza kujifunza.
8 Kama vile Mungu alivyoendelea kufanya matukio yajulikane duniani, malaika waliendelea kufahamu zaidi makusudi yake. Kwa mfano, hawakujua Mzao aliyeahidiwa katika Mwanzo 3: 15 angekuwa nani wakati ahadi hiyo ilipofanywa. Wao hawakujua Huyu Aliyeahidiwa angekuwa nani mpaka zikapita karne nyingi. Petro anaonyesha hili na kuandika hivi: “[Manabii] wakafunuliwa ya kuwa si kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili yenu walihudumu katika mambo hayo, ambayo sasa yamehubiriwa kwenu na wale waliowahubiri ninyi Injili kwa [roho takatifu i]liyotumwa kutoka mbinguni. Mambo hayo malaika wanatamani kuyachungulia.” (1 Pet. 1:12) Kujifunza kwao Mzao aliyeahidiwa angekuwa nani kulikuwa hatua ya kusonga mbele katika kupata maarifa.
9. Roho walioasi wakoje ‘’shimoni,” “katika vifungo vya giza”?
9 Wale viumbe wa kiroho walioanguka kutoka katika tengenezo la kimbinguni la Mungu katika siku za Nuhu wakawa mashetani waliacha kusonga mbele pamoja nalo. Wao hawana nuru ya ufahamu walio nao viumbe washikamanifu wa kiroho. Wao wamekuwa katika giza kwa habari ya kweli ambazo amefunulia tengenezo lake la kimbinguni tangu siku hizo. Hata inawezekana kwamba wamerudi nyuma kwa habari ya kweli ambazo walijua wakati mmoja. Biblia inasema kwamba wamo “shimoni,” “katika vifungo vya giza.” (2 Pet. 2: 4) Wao hawana taraja lo lote la kutoka humo “shimoni.” Wanapoendelea kuwa katika giza, tengenezo la Mungu la kimbinguni laendelea kusonga mbele.
TENGENEZO LA KIDUNIA
10. Mungu alianzisha nini alipoumba wanadamu?
10 Kupitia kwa wanadamu wawili wa kwanza Mungu alisimamisha tengenezo la kidunia ambalo alikusudia lienee duniani pote katika wakati wake kama vile watu walivyoendelea kuongezeka. Lingemwabudu na kutumikia faida Zake, kama vile lilivyofanya tengenezo lake la kimbinguni. Uasi wa wanadamu hawa wawili wa kwanza, pamoja na ule wa idadi kubwa ya uzao wao, haukuzuia makusudi ya Mungu.
11. (a) Tengenezo la Mungu la kidunia limewakilishwaje? (b) Eleza namna lilivyosonga mbele katika siku za Nuhu na kile kilichohitajiwa kwa wale waliokuwamo ndani yake.
11 Katika zamani zote zilizopita tengenezo la Yehova la kidunia limewakilishwa na wanaume na wanawake waaminifu walioshikamana sana naye. Po pote walipoishi, waliwakilisha tengenezo lake la kidunia. Nyakati nyingine jamii hii ya waabudu washikamanifu ilikuwa na hesabu ndogo sana, kama vile mtu mmoja mpaka watu wanane, kama ilivyokuwa katika siku za Habili, Henoko na Nuhu. Ijapokuwa lilikuwa na watu wanane tu ndani yake baada ya gharika ya siku za Nuhu, lilikuwa tengenezo lenye kusonga mbele. Liliendelea kusonga mbele katika kufahamu makusudi ya Yehova lilipojulishwa juu ya Gharika na juu ya kuhifadhiwa kwa uhai wa kibinadamu na wa wanyama. Walioshirikiana nao walipewa kazi tofauti na ile waliyokuwa wakifanya hapo mbele. Walipewa mgawo wa kazi ya kujenga safina ili uhai wao wenyewe na wa wanyama ambao wangeingiza katika safina upate kuhifadhiwa. Kila mshiriki wa tengenezo hilo alisonga mbele pamoja nalo katika namna hii mpya ya kazi. Hakuna aliyeudhika kwa sababu ya badiliko hili la kazi akakataa kuifanya. Tengenezo hilo hata lilijulishwa kimbele wakati ambapo gharika ingeanza na muda ambao mvua ingenyesha. Iliwalazimu washiriki wote wanane wakae karibu na tengenezo hilo ili wahifadhiwe hai pamoja nalo katika safina.
12. Tengenezo la Mungu la kidunia lilikuwaje katika siku za Musa, nalo lilisonga mbele namna gani?
12 Baadaye, Yehova alipofanya agano na watu wa Israeli aliokomboa kutokana na utumwa wa Misri, tengenezo lake la kidunia likawa taifa. Yeye akawa Mfalme wake. Lilipokuwa jangwani, liliendelea kusonga mbele katika kupata maarifa kama vile Yehova alivyoendelea kulipa maagizo kupitia kwa Musa. Mabadiliko yalipofanywa katika njia ambayo Yehova angeabudiwa nayo, lilisonga mbele kwa kufuata mabadiliko hayo. Kujengwa kwa hema, kuwekwa kwa jamaa ya makuhani na kuanzishwa kwa dhabihu za wanyama yalikuwa mabadiliko katika njia yao ya ibada tofauti na ilivyokuwa katika Misri. Baadaye mabadiliko mengine yalifanywa Yerusalemu ulipochaguliwa kuwa mahali ambapo madhabahu ya Mungu yangewekwa na hata baadaye hekalu la Sulemani lilipojengwa mahali hapo.
13. Wayahudi walilazimika kufanya mabadiliko gani magumu katika karne ya kwanza ili waendelee kusonga mbele na tenegenzo la Mungu?
13 Katika karne ya kwanza Yohana Mbatizaji alileta ujumbe mpya, kwamba ufalme wa mbinguni ulikuwa umekaribia. Hii ilitangaza mwanzo wa kitu ambacho kingefanya kuwe na badiliko kubwa katika tengenezo la kidunia la Mungu. Yesu Kristo aliweka msingi wake kwa huduma yake pamoja na dhabihu yake ya ukombozi. Kusonga mbele kutoka kwa taratibu ya mambo ya Kiyahudi chini ya Torati ya Musa kuingia katika taratibu mpya ya mambo chini ya agano jipya lilikuwa badiliko ambalo Wayahudi wengi walikataa kufanya. Kwa hiyo waliachwa nyuma na tengenezo la Mungu lenye kusonga mbele lilipokuwa likiingia katika wakati wa Kikristo.
14, 15. (a) Pentekoste ilimaanisha nini kwa tengenezo la Mungu? (b) Tengenezo lilisonga mbele kwenye mambo gani mapya, na sana sana ni badiliko gani lililokuwa gumu kwa Wayahudi kufanya?
14 Katika Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. tenegenzo la Mungu la kidunia lilionyeshwa kuwa la Kikristo lililotengwa kabisa na taratibu ya kale ya mambo ya Kiyahudi. Lilikuwa limeacha nyuma taratibu ya mambo chini ya Torati ya Musa. Dhabihu ya Kristo ilikuwa imemaliza mpango huo wa kale kwa kutimiza makusudi ya Torati. Katika muda wa karne zilizotangulia ilikuwa ikiwaongoza Waisraeli kwa Kristo, kama vile Paulo, mtume wa Kristo, alivyosema: “Hiyo torati imekuwa kiongozi kutuleta kwa Kristo, ili tuhesabiwe haki kwa imani. Lakini iwapo imani imekuja, hatupo tena chini ya kiongozi.” (Gal. 3:24, 25) Tengenezo hilo lilikuwa limesonga mbele kuingia katika kitu kipya ambacho Yehova alikuwa amelitayarishia.
15 Wale wanafunzi wa Yesu Kristo 120 waliokuwa wamekusanyika katika chumba cha orofa katika Sikukuu ya Pentekoste walisonga mbele siku hiyo pamoja na tengenezo la Yehova kuingia katika mpango mpya wa mambo wenye matumaini mapya na mpango mpya wa kufunika dhambi. Kwa kuchukua pendeleo walilopewa sasa la kuwa tengenezo la Kikristo lenye wahudumu wanaotangaza makusudi ya Mungu na kufundisha kweli zake, kama alivyofanya Kristo, walisonga mbele kwenye mapendeleo makubwa zaidi ya utumishi. Kwa kuhubiri kwa bidii elfu nyingi za watu waliingia katika tengenezo la Mungu la kidunia. Kama vile Ukristo ulivyohubiriwa na kuenea kutoka Palestina mpaka nchi nyingine, idadi ya watu wasio Wayahudi iliyoanza kushirikiana na tengenezo hili iliongezeka sana sana. Walikubali kwa shauku sana kweli mpya ambazo Yehova alikuwa amefunua kupitia kwalo. Sasa watu ambao hawakuwa sehemu ya tengenezo la Mungu lilipokuwa chini ya Torati ya Musa walikuwa wakipokewa chini ya mpango wa Kikristo. Ili wawapokee Wakristo Wayahudi walitakiwa wafanye mabadiliko makubwa sana katika kufikiri kwao. Chini ya agano la Torati ya Musa Wayahudi walijitenga kabisa na Mataifa, hata hawakuwa wakila pamoja nao.—Matendo 10:28.
16. Upendo wa Wakristo kwa Mungu ulijaribiwaje? Toa mfano.
16 Yehova alipoendelea kufunua kweli mpya na njia mpya za kufanya mambo kupitia kwa mitume, wale waliokuwa katika tengenezo walijaribiwa. Je! walimpenda Yehova vya kutosha kuwa na nia ya kufanya mabadiliko yaliyokuwa ya lazima katika kufikiri kwao ili waweze kukubali ufahamu huu mpya? Wengine hawakumpenda hivyo na kwa hiyo walianguka wakatoka katika tengenezo. Wale waliompenda Mungu kweli kweli walibadili kufikiri kwao wakafanya maendeleo. Kutahiriwa lilikuwa jambo lililowajaribu Wakristo wengine Wayahudi, likawafanya wavuruge Wakristo katika Antiokia. Mkutano wa baraza yenye kuongoza katika Yerusalemu ulimaliza jambo hilo kwa kutangaza kwamba kutahiriwa halikuwa takwa la Kikristo. Hili lilikuwa badiliko la maana la maoni ya Wakristo Wayahudi waliokuwa wamefundishwa chini ya taratibu ya mambo ya kale ya Kiyahudi waone kutahiriwa kuwa jambo la maana sana. Badiliko hilo lilionyesha kwamba tengenezo la Mungu lilikuwa likisonga mbele. Wale waliopenda kufanya badiliko hili katika kufikiri kwao walisonga mbele katika ufahamu mpya.—Matendo 15:1, 2, 28, 29.
TENGENEZO LA YEHOVA LEO
17. (a) Sababu gani tengenezo la Mungu leo halishiriki daraka lo lote katika makosa yanayofanywa na serikali za ulimwengu? (b) Mengine ya matunda yake mema ni matunda gani?
17 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, ndivyo ilivyo katika karne hii ya 20, Yehova ana tengenezo la kidunia. Linaweza kujulikana kwa matunda yake. Tofauti na yalivyo matengenezo mengi ya kidini ambayo ni sehemu ya ulimwengu ulio na uadui na Mungu na yanayodai kuwa tengenezo lake, halikufanya urafiki na serikali za kisiasa za ulimwengu huu. Kwa kutii maneno ya Yesu, limejitenga na ulimwengu. Kwa kufanya hivyo limeweza kuzaa matunda mema kwa sifa ya jina la Yehova. Linafanya hivyo kwa njia mbalimbali. Linasaidia watu wengi wautumaini ufalme wa Mungu. Linawasaidia wageuze maisha yao yawe mema kwa kuyafanya yapatane na kanuni za haki za Neno la Mungu. Linawapa maagizo juu ya huduma ya Kikristo, na kutia wote moyo wafuate mfano wa Yesu wa kutangaza habari njema za ufalme wa Mungu. Linafurahi kuchukua jina la Yehova Mungu, kama vile tengenezo lake lilivyokuwa katika siku za Musa.
18. Eleza namna Mithali 4:18 linavyolifaa tengenezo la Mungu?
18 Baada ya kupita miaka katika karne hii ya 20, tengenezo la Yehova limesonga mbele katika kupata maarifa na ufahamu wa Maandiko pamoja na wajibu wake mbele za Mungu. Kama ilivyokuwa kwa habari ya tengenezo la Mungu katika nyakati zilizopita, ndivyo ilivyo leo, linatimiza maneno yaliyoandikwa katika Mithali 4: 18: “Njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.” Linazidi kuendelea katika kupata nuru zaidi. Wale waliokuwa nalo katika mwanzo wa karne hii na ambao bado wako nalo leo wameona kuendelea huku.
19, 20. Taja mifano inayoonyesha namna tengenezo la Mungu limekuwa likisonga mbele katika nyakati za kisasa?
19 Tukitazama nyuma katika miaka ambayo imepita, tunaweza kuona waziwazi namna tengenezo la Mungu katika nyakati za kisasa limepata kusonga mbele katika kufahamu. Kwa mfano, lilijifunza kwamba kuwapo kwa mara ya pili kwa Kristo kungekuwa katika roho, wala si katika mwili kama wanavyoamini wengi wa wale wanaodai kuwa Wakristo. Angetawala kutoka mbinguni. Huu ulikuwa ufunuo wa maana sana kwa watu wa Mungu waliokuwa wakingojea kuja kwake kwa mara ya pili kwa hamu kubwa sana karibu na mwisho wa karne ya 19. Ukweli wa kwamba mwaka 1914 ulionyesha mwisho wa “nyakati za mataifa” zilizoanza katika mwaka wa 607 K.W.K., na mwanzo wa “siku za mwisho” kwa mataifa na kwa hiyo mwanzo wa kuwapo kwake, ulikuwa ufahamu mpya ambao watu wa Mungu wangeweza kufurahia. Walakini, iliwapasa wabadili kufikiri kwao juu ya maoni waliyokuwa nayo hapo kwanza. Kuzidi kusonga mbele kuliwafahamisha kwamba wote wawili Yehova na adui yake Shetani, wana tengenezo lisiloonekana. Tengenezo la Yehova la kimbinguni linafananishwa na mwanamke anayeitwa “Yerusalemu wa juu.” (Gal. 4: 26) Shetani pia ana tengenezo la kimbinguni na la kidunia, lakini yote mawili yanapinga haki. Leo mambo hayo ni maarifa ya msingi tu kwa watu wa Mungu, lakini miaka fulani iliyopita yalikuwa mawazo mapya yaliyowahitaji wabadili maoni yao ambayo wengine waliona ugumu wa kufanya mabadiliko hayo.
20 Ulikuwa mwaka wa 1938 ambapo Mnara wa Mlinzi ulipochapa makala (tungo) juu ya tengenezo iliyoonyesha kwamba tengenezo la Mungu lapaswa kuwa la kitheokrasi. Linapaswa kuongozwa na Mungu kupitia kwa “mtumwa mwaminifu na mwenye akili,” mabaki yaliyoungana ya warithi wake wa ufalme. (Mt. 24:45-47) Mpaka wakati huo makundi ya watu wake yalikuwa yamefanyizwa katika njia ya kidemokrasi, makundi yakiwachagua wale waliokuwa na mamlaka juu yao. ‘Wazee waliochaguliwa’ waliotokana na mpango huu walifanya kuwe na kutoridhika na kukosa umoja kwa kuwa wengi wao walikuwa wakijitukuza na kuwa na kiburi. Walidharau yaliyosemwa na Yesu: “Ye yote atakayejikweza, atadhiliwa.” (Mt. 23: 12) Kwa kurudishwa kwa mpango wa kitheokrasi katika mwaka 1938 kama ulivyokuwa katika tengenezo la Kikristo katika karne ya kwanza, maafisa waliochaguliwa katika makundi walishushwa kutoka vyeo vyao vyenye utukufu. Mpango huu wa uchaguzi ulipoacha kutumiwa katika makundi, tengenezo lilianza kupata amani, upatano, umoja na matokeo zaidi.
21. Wengine walifanya nini mpango wa “wazee waliochaguliwa” ulipoacha kutumiwa?
21 Kuacha kutumia mpango wa ‘wazee waliochaguliwa’ lilikuwa badiliko kubwa katika namna tengenezo la Mungu linavyotenda katika karne hii ya 20. Lilikuwa jaribu kali sana kwa wale waliokuwamo katika tengenezo. Watu wengine waliliruhusu liwe sababu kubwa ya kubishania. Wakikataa kusonga mbele na tengenezo, waliliacha. Lakini idadi kubwa ilifuata badiliko hilo ikasonga mbele katika kupata nuru zaidi pamoja na mapendeleo makubwa zaidi ya utumishi. Wale walioacha tengenezo si kwamba tu waliacha kusonga mbele bali pia walipoteza nuru waliyokuwa wamepata walipokuwa ndani yake.
22. (a) Watumishi katika tengenezo wanachaguliwaje sasa? (b) Badiliko hili limelifaidi tengenezo?
22 Sasa Yehova kupitia kwa jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” anawaweka waangalizi na watumishi wa huduma katika tengenezo lake la kidunia. Likitenda katika njia ya kitheokrasi, linafurahia kuwa na umoja na lina matokeo zaidi katika utumishi wa Yehova kuliko ilivyokuwa katika siku za wazee wenye kuchaguliwa. Mungu hamwongozi ye yote awachague watumishi katika kundi kama alivyofanya kwa Samweli alipomchagua Sauli awe mfalme wa Israeli. Kwa kuwapa Wakristo wenye madaraka wanaoshirikiana kama jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” roho yake takatifu, inaweza kusemwa kwamba kuwekwa kwa watumishi na jamii hii kunatoka kwake. Hivyo, kama ilivyokuwa katika tengenezo la karne ya kwanza, baraza yenye kuongoza ya tengenezo la kidunia la Mungu, ambayo huwakilisha jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” ndiyo inayowaweka watumishi wote. Hilo lilikuwa badiliko lenye maana sana katika tengenezo la Mungu lenye kusonga mbele. Watu waliosonga mbele pamoja na tengenezo wakati mpango huu wa kitheokrasi ulipoanzishwa katika mwaka 1938, wameona tangu wakati huo namna umekuwa wenye faida. Umekuwa sababu kubwa iliyofanya tengenezo lipanuke sana. Lakini badiliko hilo halikuwa jambo rahisi kwa wengi.
23. (a) Sababu gani ni vigumu kukubali mabadiliko, na sababu gani ni ya lazima? (b) Sababu gani ni jambo lisilo la hekima kupinga mabadiliko?
23 Kuacha kutumia wazee waliochaguliwa ni mfano wa namna ya mabadiliko yanavyoweza kuwaudhi watu kwanza. Katika muda wote wa historia ya tengenezo la kidunia la Mungu lenye kusonga mbele, wengine wamekuwa na maelekeo ya kupinga mabadiliko, wakipendelea kushikilia njia na maoni ya kale. Walakini mabadiliko ni ya lazima kwa sababu Mungu huwapa watu wake ufahamu wa Neno lake na makusudi yake kidogo kidogo katika wakati wake. Ili mtu azidi kukua katika maarifa ya kweli anahitajiwa awe mtu mwenye kusonga mbele, si mwenye kusimama mahali pale pale. Ijapokuwa huenda mtu asione uhitaji wa badiliko fulani mwanzoni, kadiri muda upitapo ataona namna linavyofaidi tengenezo. Kwa hiyo, mahali pa kupinga badiliko fulani katika ufahamu wa Maandiko, mipango ya tengenezo au muundo wake, inafaa zaidi kufuata badiliko hilo, tukikumbuka kwamba badiliko liwalo lote linalofanywa na tengenezo la Mungu, ni kwa faida ya wale waliomo ndani yake. Kupinga kusonga mbele huku ni kupinga roho ya Yehova inayotenda kazi katika tengenezo, ikilifanya lisonge mbele. Paulo alisema juu ya watu waliopinga roho takatifu katika siku zake, kama vile wazee wengine waliochaguliwa walivyofanya. “Kama vile Yane na Yambre walivyopingana na Musa, vivyo hivyo na hawa wanapingana na ile kweli.”—2 Tim. 3:8.
24. Wote waliomo ndani ya tengenezo la Mungu wanahitaji uongozi gani, na kwa sababu gani?
24 Wote waliomo katika tengenezo la Yehova wanahitaji aongoze hatua zao katika njia iongozayo kwenye utimizo wa makusudi yake. “Ee [Yehova] najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yer. 10:23) Tunahitaji Neno la Mungu na tengenezo lake. Kwa kukaa karibu na tengenezo lake kadiri linavyozidi kusonga mbele katika maarifa na kwa kuendelea pamoja nalo, bado tutakuwa tukiishi linaposonga mbele katika wakati mpya na kupanuka na kuijaza dunia yote na watu wanaompenda na kumtii Mtawala mkuu wa ulimwengu wote.