SURA YA 1
Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
ULIMWENGUNI pote, kuna mashirika mengi ya kidini, kisiasa, kibiashara, na kijamii yenye mpangilio, malengo, maoni, na falsafa mbalimbali. Lakini kuna tengenezo moja lililo tofauti kabisa na mashirika mengine yote. Neno la Mungu linaonyesha waziwazi kwamba tengenezo hilo ni Mashahidi wa Yehova.
2 Inafurahisha kwamba umeanza kushirikiana na tengenezo la Yehova. Baada ya kujihakikishia mwenyewe mapenzi ya Mungu, sasa unayafanya. (Zab. 143:10; Rom. 12:2) Wewe ni mhudumu mwenye bidii anayeshirikiana na ushirika wenye upendo wa akina ndugu ulimwenguni pote. (2 Kor. 6:4; 1 Pet. 2:17; 5:9) Kama vile Neno la Mungu linavyoahidi, kufanya hivyo kunakuletea baraka na furaha nyingi. (Met. 10:22; Marko 10:30) Kwa kufanya mapenzi ya Yehova kwa uaminifu, unatayarishwa kufurahia uzima wa milele wakati ujao.—1 Tim. 6:18, 19; 1 Yoh. 2:17.
3 Muumba wetu Mkuu ana tengenezo la pekee la ulimwenguni pote linaloongozwa kitheokrasi. Hilo linamaanisha kwamba Yehova ndiye anayelitawala akiwa Kichwa cha wote. Tunamtumaini kabisa. Yeye ndiye Mwamuzi wetu, Mpaji-sheria wetu, na Mfalme wetu. (Isa. 33:22) Kwa kuwa yeye ni Mungu mwenye utaratibu, amefanya mipango inayotuwezesha ‘kufanya kazi pamoja naye’ ili kutimiza kusudi lake.—2 Kor. 6:1, 2.
4 Mwisho wa mfumo huu wa mambo unapozidi kukaribia, tunasonga mbele tukiongozwa na Mfalme aliyeteuliwa, Kristo Yesu. (Isa. 55:4; Ufu. 6:2; 11:15) Yesu alitabiri kwamba wafuasi wake wangefanya kazi kubwa zaidi kuliko zile alizofanya wakati wa huduma yake hapa duniani. (Yoh. 14:12) Hilo lingewezekana kwa sababu baada ya muda kupita na idadi yao kuongezeka, wafuasi wa Yesu wangefika maeneo ya mbali zaidi. Wangetangaza habari njema ya Ufalme hadi sehemu za mbali za dunia.—Mt. 24:14; 28:19, 20; Mdo. 1:8.
5 Tayari unabii huo umetimia. Hata hivyo, kama Yesu alivyosema waziwazi, kazi ya kutangaza habari njema itakoma wakati uliowekwa wa Yehova utakapofika. Kulingana na Neno la Mungu la kinabii, ni wazi kwamba ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha imekaribia.—Yoeli 2:31; Sef. 1:14-18; 2:2, 3; 1 Pet. 4:7.
Tunahitaji kuongeza jitihada katika kazi ambayo Mungu alitupatia. Ili tufanikiwe kufanya hivyo, tunapaswa kujua vizuri jinsi tengenezo la Mungu linavyofanya kazi na kushirikiana nalo kikamili
6 Tunapotambua mapenzi ya Yehova katika siku hizi za mwisho, tunahitaji kuongeza jitihada katika kazi aliyotupatia. Ili tufanikiwe kufanya hivyo, tunapaswa kujua vizuri jinsi tengenezo la Mungu linavyofanya kazi na kushirikiana nalo kikamili. Utendaji wa tengenezo hilo unategemea kanuni za Kimaandiko, kutia ndani amri, sheria, maagizo, miongozo, na mafundisho yaliyo katika Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho.—Zab. 19: 7-9.
7 Watu wa Yehova wanapofuata mwongozo huo wa Biblia, wanashirikiana na kufanya kazi kwa amani na umoja. (Zab. 133:1; Isa. 60:17; Rom. 14:19) Ni nini kinachowaunganisha ndugu na dada zetu ulimwenguni pote? Ni upendo. Tunachochewa na upendo na tumejivika upendo. (Yoh. 13:34, 35; Kol. 3:14) Kwa kufuata njia hiyo inayompendeza Mungu, tunaenda sambamba na sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova.
SEHEMU YA KIMBINGU YA TENGENEZO LA YEHOVA
8 Nabii Isaya, Ezekieli, na Danieli waliona maono ya sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova. (Isa., sura ya 6; Eze., sura ya 1; Dan. 7:9, 10) Mtume Yohana pia alipata maono ya mpangilio wa kimbingu na kutueleza juu yake katika kitabu cha Ufunuo. Alimwona Yehova kwenye kiti chenye utukufu cha ufalme pamoja na malaika, waliokuwa wakitangaza hivi: “Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu ni Yehova Mungu, Mweza-Yote, aliyekuwako na aliyeko na anayekuja.” (Ufu. 4:8) Yohana pia alimwona “mwanakondoo . . . akiwa amesimama katikati ya kile kiti cha ufalme,” yaani, Yesu Kristo, Mwanakondoo wa Mungu.—Ufu. 5:6, 13, 14; Yoh. 1:29.
9 Maono hayo ya Yehova akiwa ameketi kwenye kiti cha ufalme yanaonyesha kwamba yeye ndiye Kichwa cha tengenezo hilo. Kitabu cha 1 Mambo ya Nyakati 29:11, 12 kinasema hivi kuhusu cheo chake kikuu: “Ee Yehova, ukuu ni wako na nguvu na uzuri na fahari na utukufu, kwa maana kila kitu mbinguni na duniani ni chako. Ufalme ni wako, Ee Yehova. Wewe Ndiye unayejikweza mwenyewe ukiwa mkuu juu ya vyote. Utajiri na utukufu hutoka kwako, nawe hutawala kila kitu, na mkononi mwako mna nguvu na uwezo, na mkono wako unaweza kumfanya mtu awe mkuu na unaweza kuwapa wote nguvu.”
10 Akiwa mfanyakazi mwenzi wa Yehova, Yesu Kristo ana cheo cha juu mbinguni, naye amepewa mamlaka kubwa. Kwa kweli, Mungu ‘alivitiisha vitu vyote chini ya miguu yake, na kumfanya kuwa kichwa juu ya vitu vyote kuhusiana na kutaniko.’ (Efe. 1:22) Mtume Paulo alisema hivi kumhusu Yesu: “Mungu alimpandisha kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu kuliko kila jina lingine, ili katika jina la Yesu kila goti lipigwe—la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya ardhi—na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.” (Flp. 2:9-11) Kwa hiyo, tunaweza kuutumaini kabisa uongozi mwadilifu wa Yesu Kristo.
11 Katika maono, nabii Danieli alimwona Mzee wa Siku kwenye kiti Chake cha ufalme mbinguni na malaika “elfu kwa maelfu [walioendelea] kumhudumia, na elfu kumi mara elfu kumi [waliosimama] mbele zake.” (Dan. 7:10) Biblia inawaita malaika hao “roho kwa ajili ya utumishi mtakatifu, waliotumwa kuhudumu kwa ajili ya wale watakaorithi wokovu.” (Ebr. 1:14) Malaika hao wote wamepangwa katika ‘viti vya ufalme, utawala, serikali, na mamlaka.’—Kol. 1:16.
12 Tukitenga wakati ili kutafakari kuhusu sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova, tunaweza kuelewa jinsi Isaya alivyohisi ‘alipomwona Yehova, akiwa ameketi juu ya kiti cha ufalme kilicho juu na kilichoinuliwa’ na ‘maserafi wakiwa wamesimama juu yake.’ Isaya alisema: “Ole wangu! Kwa maana ni kama nimekufa, kwa maana mimi ni mtu asiye na midomo safi, nami ninaishi kati ya watu wasio na midomo safi; kwa maana macho yangu yamemwona Mfalme, Yehova wa majeshi mwenyewe!” Kwa kweli, Isaya aliogopa na kunyenyekea alipotambua ukubwa wa tengenezo la Yehova. Alichochewa sana na jambo hilo hivi kwamba mwito ulipotolewa kutoka mbinguni kuhusu kazi ya pekee ya kutangaza hukumu za Yehova, Isaya aliitikia hivi: “Mimi hapa! Nitume mimi.”—Isa. 6:1-5, 8.
13 Vivyo hivyo, watu wa Yehova huchochewa wanapolitambua na kulithamini tengenezo lake. Tengenezo linaposonga mbele, sisi hujitahidi kwenda nalo sambamba. Tunajitahidi kuonyesha kwamba tunalitumaini tengenezo la Yehova leo.
TENGENEZO LA YEHOVA LINASONGA MBELE
14 Katika sura ya kwanza ya unabii wa Ezekieli, Yehova anaonekana akiendesha gari kubwa sana la kimbingu. Gari hilo lenye fahari linawakilisha sehemu isiyoonekana ya tengenezo la Yehova. Analiendesha gari hilo katika maana ya kwamba analielekeza ifaavyo na kulitumia kutimiza kusudi lake.—Zab. 103:20.
15 Kila gurudumu la gari hilo lina gurudumu lingine ndani yake lenye ukubwa uleule. Ndiyo sababu inasemekana kwamba magurudumu hayo yaliweza “kwenda upande wowote kati ya zile pande nne.” (Eze. 1:17) Magurudumu hayo yanaweza kubadili mwelekeo mara moja. Hata hivyo, haimaanishi kwamba gari hilo linajielekeza lenyewe tu. Yehova haliachi tengenezo lake liende popote linapotaka. Andiko la Ezekieli 1:20 linasema hivi: ‘Lilienda popote ambapo roho ililielekeza kwenda.’ Kwa hiyo, Yehova ndiye hufanya tengenezo lake liende mahali popote ambapo roho yake inalielekeza. Basi, tunapaswa kujiuliza, ‘Je, ninaenda sambamba na tengenezo hilo?’
16 Kwenda sambamba na tengenezo la Yehova kunahusisha mengi zaidi ya kuhudhuria mikutano na kushiriki katika huduma ya shambani. Kwanza kabisa, kwenda sambamba na tengenezo kunahusisha kufanya maendeleo na kukua kiroho. ‘Tunahakikisha mambo muhimu zaidi’ na kwenda sambamba na programu ya ulishaji wa kiroho. (Flp. 1:10; 4:8, 9; Yoh. 17:3) Pia, lazima tukumbuke kwamba kila shirika au tengenezo linahitaji kuwa na utaratibu na ushirikiano mzuri. Kwa hiyo tunapaswa kutambua umuhimu wa kutumia kikamili vipaji, mali, na ujuzi wa kiroho ambao Yehova ametupatia ili tutimize kazi yake. Tunapoenda sambamba na gari la kimbingu la Yehova, maisha yetu yanapatana na ujumbe tunaotangaza.
17 Kwa msaada wa tengenezo la Yehova, sote tunaendelea kufanya mapenzi ya Mungu. Kumbuka kwamba Mwendeshaji wa gari hilo la kimbingu ni Yehova. Kwa hiyo, kwenda sambamba na gari hilo kunaonyesha kwamba tunamheshimu na kumtumaini Yehova, Mwamba wetu. (Zab. 18:31) Biblia inaahidi hivi: “Yehova atawapa nguvu watu wake. Yehova atawabariki watu wake kwa amani.” (Zab. 29:11) Tukiwa sehemu ya tengenezo la Yehova leo, tunapata nguvu kutoka kwake na kuwa na amani anayowapa watu walio katika tengenezo lake. Naam, hatuna shaka hata kidogo kwamba tutaendelea kupata baraka nyingi tunapofanya mapenzi ya Yehova sasa na milele.