Msifu Yehova Pamoja na Watu Wake
“Nitamwimbia [Yehova] maadamu ninaishi; nitamshangilia Mungu wangu nikiwa hai.”—Zab. 104:33.
1, 2. (a) Nini “wimbo mpya,” nao wengine wameuitikiaje? (b) Taja maulizo fulani ya kipekee yanayostahili kuangaliwa.
YEHOVA anasifiwa katika wimbo unaosikika duniani mwote leo. Hapana, hauimbwi na Walawi. Wala hatuwezi kusikia jamii ya waimbaji ya kimalaika juu mbinguni wakimsifu Mungu. Lakini twaweza kuusikia “wimbo mpya,” uimbwao kwa sauti moja na wanaotazamiwa kuwa warithi wa serikali ya Yehova ya kimbinguni. (Ufu. 14:1-4; 20:6; 22:5; Zab. 96:1, 10) Ndio wimbo wenye kuamsha wa ufalme wa Mungu uliosimamishwa ambao umefanya kazi mbinguni tangu mwaka wa 1914 C.E. Yesu Kristo aliyetukuzwa akiwa ndiye Mfalme. Maelfu yameusikia wimbo huo wenye kutia nguvu kwa shukrani nyingi.
2 Je! wewe umeuitikia “wimbo mpya” huo kwa shukrani? Je! unamsifu Yehova pamoja na watu wake? Je! umeshirikiana na tengenezo analolitumia Mungu kutangaza duniani pote “habari njema hizi za ufalme”? (Mt. 24:14, NW) Ikiwa ndivyo, je! unalishukuru tengenezo la kidunia la Yehova kweli kweli? Ziko sababu nyingi za kuliheshimu sana. Ziangalie chache kwa ufupi.
KWA SABABU GANI KULISHUKURU TENGENEZO LA MUNGU
3. Wafuasi waliotiwa mafuta wa Yesu na wenzi wao wanalo pendeleo la kuwakilisha nini na nani?
3 Kwanza, wafuasi waliotiwa mafuta wa Yesu, ambao ni sehemu ya tengenezo la kidunia la Yehova, ni “mabalozi badala ya Kristo.” Wenzi wao wenye matumaini ya kidunia vile vile wanatumikia faida za Ufalme. (2 Kor. 5:20, NW) Kumbuka, wao si mabalozi na wajumbe wa serikali ya kibinadamu tu na ya watawala wenye dhambi. Wao wanamwakilisha Yehova, mfalme wake wa kiroho aliyetukuzwa Yesu Kristo na ufalme mkuu wa Mungu. Lo! pendeleo kubwa kama nini! Bila shaka, ili kumtumikia na kumsifu Mwenye Enzi Yote wa Ulimwengu, lazima mtu ashirikiane na tengenezo la mashahidi wa Yehova wa Kikristo.
4. Kwa sababu gani wale waliomo katika tengenezo la kidunia la Yehova wanaweza kufahamu mambo ya kiroho?
4 Vile vile, angalia uhakika wa kwamba tengenezo la Yehova peke yake, katika dunia yote, linaongozwa na roho takatifu ya Mungu au nguvu ya utendaji. (Zek. 4:6) Ni tengenezo hili peke yake linalofanya kazi kwa ajili ya kusudi la Yehova na kwa sifa yake. Kwalo peke yake Neno Takatifu la Mungu, Biblia, si kitabu kilichotiwa muhuri. Watu wengi wa ulimwengu ni wenye akili sana, wenye uwezo wa kufahamu mambo magumu. Wao wanaweza kuyasoma Maandiko Matakatifu, lakini hawawezi kufahamu maana yake kubwa. Hali watu wa Mungu wanaweza kuyafahamu mambo hayo ya kiroho. Kwa sababu gani? Si kwa sababu ya akili ya pekee kwa upande wao, lakini kama vile mtume Paulo alivyotangaza: “Mungu ametufunulia sisi kwa [roho]. Maana [roho] huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu.” (1 Kor. 2:10) Yesu Kristo alimsifu Baba yake wa kimbinguni kwa ‘kuwaficha mambo hayo wenye hekima na akili lakini akawafunulia watoto wachanga.’ (Mt. 11:25) Lo! Wakristo wa kweli wanashukuru sana namna gani kushirikiana na tengenezo la pekee duniani linaloyafahamu “mafumbo ya Mungu”!
5. Uongozi wa roho ya Mungu uliwawezesha watumishi wa Yehova zamani sana kufahamu nini juu ya mwaka wa 1914 C.E.?
5 Uongozi wa roho ya Mungu unawawezesha watumishi wa Yehova kuwa na nuru ya kimungu katika ulimwengu wa giza la kiroho. (2 Kor. 4:4) Kwa mfano, zamani sana walifahamu kwamba mwaka wa 1914 C.E. ungeonyesha mwisho wa Majira ya Mataifa au “nyakati zilizowekwa za mataifa,” nyakati ambapo mataifa yasiyo ya Kiyahudi yaliruhusiwa utawala wa dunia usiokatizwa. (Luka 21:24, NW) Kipindi hiki cha miaka 2,520 kilianza wakati wa uharibifu wa Yerusalemu na hekalu lake ulioletwa na Wababeli mwishoni mwa karne ya saba B.C.E. Kwa mfano, Zion’s Watch Tower la Machi 1880 lilikuwa limekwisha tangaza: “‘Majira ya Mataifa’ yanafika mwaka wa 1914, nao ufalme wa kimbinguni hautakuwa na enzi yote mpaka wakati huo.” Ni Mungu peke yake kwa roho takatifu yake ambaye angaliweza kufunua hili kwa wale wanafunzi wa Biblia wa kwanza mapema sana.
6. Kwa habari ya uzima, ni tumaini gani linalotuwekea mbele yetu tengenezo la Kikristo?
6 Sababu nyingine ya kulishukuru tengenezo la mashahidi wa Yehova wa Kikristo ni kwamba linatusaidia kuifahamu mipango ya Mungu ya kuwabarikia watiifu, kisha kupatanisha maisha zetu na mapenzi ya kimungu. (Mt. 24:45-47) Hii inatuletea furaha sasa ijapokuwa huzuni ya ulimwengu, kwa maana inaridhisha kweli kweli kujua kwamba mtu anampendeza Mungu. Kwa vitabu vyake na kupitia kwa njia nyingine, tengenezo la kweli la Kikristo linaweka waziwazi mbele yetu tumaini la Biblia la uzima usio na kikomo, wenye furaha chini ya utawala wa ufalme wa Mungu. (Ufu. 21:3-5) Ni baraka kama nini! Lo! imetupasa tulishukuru tengenezo la kidunia la Mungu na nafasi zetu za kumsifu Yehova pamoja na watu wake sana kadiri gani!
7. Ni kusudi gani linalotumikiwa na “vipawa katika wanadamu”?
7 Zaidi ya hayo, tengenezo hili peke yake linapewa “vipawa katika wanadamu,” kama vile wenye kutangaza injili, wachungaji na waalimu, wanaotumikia kusudi la Mungu kwa kufuatana na usitawi wa kiroho na hali njema ya watu wake. (Efe. 4:7-16, NW) Waangalizi waliowekwa au wazee na watumishi wa huduma wanatimiza matakwa ya Maandiko kwa vyeo vyao vyenye, madaraka katika tengenezo la Yehova. Kati ya mambo mengine, wao wanakaribisha watu wenye mioyo minyofu katika kundi la Kikristo na kusaidia kuwaelimisha katika njia za Yehova. (1 Tim. 3:1-10, 12, 13; Tito 1:5-9) Chini ya maongozi ya roho takatifu ya Mungu, wewe waweza kushiriki katika kazi hii kubwa ya kuwatafuta, kuwakaribisha na kuwaelimisha wale watakaokuwa wasifaji wenzetu wa Yehova. Ni pendeleo lenye baraka namna gani!
8. Ni watu wa namna gani wanaofanyiza tengenezo la kidunia la Yehova?
8 Fikiri juu ya watu wenyewe—wale wanaomsifu Yehova kama sehemu ya tengenezo lake la kidunia. Wao ndio “vitu vinavyotamanika vya mataifa yote.” (Hag. 2:7, NW) Wakristo wa kweli wanao ndugu wengi wa kiroho, dada, mama na watoto (Marko 10:29, 30) Kuwa na ushirika na wasifaji kama hao wenye adili nzuri, wanaomcha Yehova na wanaoishi kulingana na Maandiko Matakatifu ni jambo la kushukuru.
WENYE SHUKRANI KWA KUWA SEHEMU YA TENGENEZO LA MUNGU
9. Ni kwa njia gani kijana mmoja mwenye umri wa miaka kumi na mitano alivyotoa shukrani kwa ushirika na watu wa Mungu?
9 Si ajabu watu wengi sana ni wenye shukrani nyingi kuwa wanashirikiana na tengenezo la kidunia la Yehova na kuwa wakimsifu Mungu pamoja na watu wake. Kijana mwenye umri wa miaka kumi na mitano alisema:
Nilitaka kuwaandikieni tu kuwaelezeni namna nilivyo mwenye furaha kuweza kuwa mmoja wa mashahidi wa Yehova. Mimi nawashukuru sana wazazi wangu kwa kunifundisha juu ya kweli. . . . Nikiuona upotovu katika ulimwengu, naona fahari na nashukuru kwa ajili ya kuweza kusema kwamba mimi si sehemu yake, na ya kwamba mimi ni mmoja wa mashahidi wa Yehova.
10. Tengenezo la Yehova na roho yake vilimaanisha nini kwa jamaa moja iliyofiwa?
10 Nyuma ya kifo cha ajali cha mwana wao, jamaa moja ya Kikristo ilieleza upendo ambao waamini wenzao waliwaonyesha, na vile vile wakaandika:
Acheni niwahakikishieni—kwa mioyo yetu—kwamba Yehova ameufanya upendo wake, upendo wa ndugu zetu na wa tengenezo lake hakika sana kwetu. Kupitia kwa msiba tumeona roho ya Yehova ikitenda kazi mbele ya macho yetu penyewe. Twashukuru sana kwa unyenyekevu kuwa kati ya hawa ambao Yehova anawaita ‘wanaotamanika kutoka kwa mataifa.’ . . .
Twatumaini tumewafanya mjue kwa kadiri ndogo namna tulivyo wenye shukrani kuwa na ndugu kama ninyi, kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova, kuona utendaji wa roho ya Mungu na kupata faraja yake. Furaha hiyo haiwezi kuandikwa katika karatasi.
11. Betheli ilionwaje na mwanamume mmoja aliyetumikia humo kwa miaka mingi?
11 Mwanamume aliyetumikia kwa uaminifu kwa miaka mingi katika makao makuu ya mashahidi wa Yehova (yanayoitwa Betheli) katika Brooklyn, New York, alisema:
Katika miaka tangu kifo [cha mke wangu], nimepata kuishukuru Betheli hata zaidi. . . Betheli yaweza kuangaliwa kama njia panda, njia panda za watu wa Yehova. Sikuzote tunakutana na watu kutoka kila mahali, wakielekea kila mahali. Mara mbili kwa mwaka kuna. . . . wanafunzi wanaokuja hapa kuhudhuria Shule ya Gilead [ya wamisionari]. Kunao wamisionari wanaotembelea na wajumbe wenye kusafiri wa Sosaiti. Vile vile, bila shaka, wapo washiriki wa jamaa [ya Betheli] yenyewe wa kukutana nao. . . . Nyuma ya miaka 45 hapa sikuzote nakutana na watu ninaowajua au wanaoshiriki ujuzi pamoja. Jamaa yangu ya marafiki inaenea kuizunguka dunia.
12. Je! inafaa kwa Wakristo kutoa shukrani kwa ajili ya waamini wenzao?
12 Lo! ni vema namna gani kuwa na ‘jamaa ya marafiki’ duniani pote! Basi, wale ambao ni sehemu ya tengenezo la Mungu kwa haki wanatoa shukrani yao kwa Yehova kwa ajili ya waamini wenzao. Mtume Paulo alifanya hivyo. Aliandika juu ya mshiriki wake wa Kikristo Timotheo: “Namshukuru Mungu, nimwabuduye kwa dhamiri safi tangu zamani za wazee wangu, kama vile nikukumbukavyo wewe daima, katika kuomba kwangu usiku na mchana. Nami natamani sana kukuona, nikiyakumbuka machozi yako, ili nijae furaha.” (2 Tim. 1:3, 4) Juu ya waabudu wenzake katika Rumi, Paulo alisema: “Namshukuru Mungu wangu katika Yesu Kristo kwa ajili yenu nyote, kwa kuwa imani yenu inahubiriwa katika dunia nzima.” (Rum. 1:8) Kwa kweli, kwa ajili ya washiriki hao wema, na kwa ajili ya sababu nyinginezo nyingi, wale walio sehemu ya tengenezo la kidunia la Mungu wanashukuru sana pendeleo lao la kumsifu Yehova pamoja na watu wake.
KUONYESHA SHUKRANI YAKO KWA TENGENEZO LA MUNGU
13. Kwa sababu gani yakupasa kusoma na kujifunza Biblia na vitabu vya Kikristo kwa kawaida?
13 Lakini je! wawezaje kuonyesha kwamba unalishukuru tengenezo la Yehova kweli kweli? Kati ya mambo mengine, waweza kujifunza kwa kawaida Biblia na vitabu vya Kikristo vinavyotolewa na Mungu kupitia kwa tengenezo lake. Usiviachilie mbali. Shauri lililotolewa kwa ajili ya wafalme wa Israeli linastahili fikira kwa habari hii. Kupitia kwa Musa, Mungu alisema: “Tena na iwe, zamani aketipo juu ya kiti cha ufalme wake, ajiandikie nakala ya torati hii katika chuo, kufuata hicho kilicho mbele ya makuhani Walawi; na awe nayo, asome humo siku zote atakazoishi; ili apate kujifunza kumcha [Yehova], Mungu wake, ayashike maneno yote ya torati hii na amri hizi, kwa kuyafanya; moyo wake usije ukainuliwa juu ya ndugu zake, wala asikengeuke katika maagizo, kwa mkono wa kuume wala wa kushoto; ili apate kuzifanya siku zake kuwa nyingi katika ufalme wake, yeye na wanawe, katikati ya Israeli.” (Kum. 17:18-20) Neno la Yehova na vitabu vya kweli vya Kikristo vinasisitizia sheria zenye haki za Mungu na kanuni. Kwa hiyo uzisome na kujifunza hizo kwa kawaida. Utunze uongozi wa kiroho zinavyoutoa. Uwe kama mtunga Zaburi aliyesema: “Ee [Yehova], umehimidiwa, unifundishe amri zako. . . . Nitajifurahisha sana kwa amri zako, sitalisahau neno lako.”—Zab. 119:12-16.
14, 15. Ikiwa twalishukuru tengenezo la Yehova la kidunia, tutaionaje mikutano ya Kikristo na makusanyiko, nasi twafaidikaje kutokana nayo?
14 Njia nyingine ya kuonyesha kwamba unalishukuru tengenezo la Yehova na pendeleo lako la kumsifu Mungu pamoja na watu wake ni kwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa kawaida. Ilimpendeza sana Daudi kuwa kati ya waabudu wa Yehova katika patakatifu pa Mungu. Yeye alitangaza: “Neno moja nimelitaka kwa [Yehova], nalo ndilo nitakalolitafuta, nikae nyumbani mwa [Yehova] siku zote za maisha yangu. Niutazame uzuri wa [Yehova], na kutafakari hekaluni mwake [kwa shukrani].” (Zab. 27:4) Ikiwa twalishukuru tengenezo la kidunia la Yehova kweli kweli, tutataka kuwa katika mikutano ya Kikristo na makusanyiko.—Zab. 84:1-4.
15 Kwa kutoiachilia mbali nyumba ya Mungu ya nyakati za kale (Neh. 10:39), lakini kwa kuitegemeza kwa shukrani na kuhudhuria sikukuu humo, Waisraeli walisaidiwa kutumia maagizo ya Mungu katika maisha. Iliwalazimu kukutana na majaribu ya imani na vishawishi. Kama ilivyokuwa kwa watu wengine, bila shaka walizungukwa na vishawishi vya kusema uongo, kuiba, kufanya uzinzi au kujitia katika makosa mengine. Lakini kama lingalitokea jaribu, wangaliweza kufikiria sana waliyokuwa wamesomewa penye makusanyiko yao. (Kum. 31:10-13) Wangeweza kuzikumbuka sheria za Yehova na ahadi. Kwa hiyo ingewezekana kushinda majaribu na kushika ukamilifu kwa Mungu. Tunafaidika namna ile ile kwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo na makusanyiko leo. Vile vile, kwa kuwapo kwetu tunachocheana “katika upendo na kazi nzuri.”—Ebr. 10:24, 25.
16. Uaminifu kwa tengenezo la Yehova una umuhimu gani?
16 Ikiwa twalishukuru tengenezo la kidunia la Yehova kweli kweli, tutabaki waaminifu kwalo, tukijua kwamba tengenezo ni lake. Kama tungeliacha, ni wapi pengine ambapo tungeweza kwenda? Hakuna tengenezo jinginelo linalofanya mapenzi ya kimungu wala linalowaelimisha watu kwa ajili ya uzima wa milele. Wakati wengi walipomwacha Yesu Kristo, yeye aliwauliza mitume wake: “Je! ninyi nanyi mwataka kuondoka?” Petro alijibu: “Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele. Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu.” (Yohana 6:66-69) Wakristo waaminifu wa kwanza walivumilia mateso makali na hali walibaki waaminifu kwa Mungu na kwa tengenezo lake, kundi la Kikristo. Kwa mfano, Wakristo walioteswa katika Rumi walitafuta kimbilio katika mapango ya kuzikia watu ya mji huo. Vyumba vya jamaa vya kuzikia watu huko vilitoa nafasi kwa mikutano midogo ya vikundi. Wakristo wa kwanza waliijua haja yao ya kiroho na haja ya kukusanyika kwa ajili ya kutiwa moyo na maagizo, hata kama hili lilihitaji kwenda chinichini ya ardhi yenyewe. Ikiwa sisi tunayo shukrani ya Kikristo, sisi, vile vile, tutabaki na tengenezo la Yehova, kundi lake la Kikristo, yajapokuwa magumu na mateso leo.
17. Kwa sababu gani yakupasa kujitia katika huduma ya Kikristo kwa kuona haraka?
17 Wewe vile vile waweza kuonyesha shukrani kwa tengenezo la kidunia la Mungu kwa kujiunga kwa moyo wote katika huduma ya Kikristo, kulichukua Neno la Mungu kwa watu wengine. Kwa njia hiyo unaendeleza kazi ya kuelimisha linayoiendesha tengenezo. Kuna uhitaji wa kushiriki katika kazi hiyo kwa kuona haraka, vile vile, kwa maana mwisho wa hii taratibu mbovu ya mambo unakaribia. Wakati ni mfupi. Mavuno ni mengi nao wafanya kazi ni wachache. (Mt. 9:37, 38) Ni pendeleo kama nini kuwa mmoja wa wafanya kazi wa mavuno ya kisasa na kufanya kazi ya kuokoa uhai ya kuhubiri! Kwa vyo vyote, endelea kuwa mwenye shughuli nyingi katika huduma ya Kikristo, ‘ukizidi sana kutenda kazi ya Bwana sikuzote, ukijua kuwa taabu yako siyo bure katika Bwana.’—1 Kor. 15:58.
18. Ili kuendelea vema katika huduma, sala na roho takatifu ya Mungu ni vya muhimu namna gani?
18 Walio waaminifu, wenye shukrani wanataka kumtolea Mungu “dhabihu ya sifa” njema. (Ebr. 13:15) Lakini je! hii yaweza kufanywaje? Utafute msaada wa Yehova katika sala. Uongozi wa roho takatifu yake unahitajiwa ili kusaidia watu wenye mfano wa kondoo na kufanya yote awezayo mtu katika huduma. Kwa hiyo uiombe roho takatifu ya Mungu ikukalie. Yehova anaitoa hiyo kwa watumishi wake walio wakf wanaofanya ombi hili kwa rehema. Yesu Kristo alisema: “Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa [roho takatifu] hao wamwombao?”—Luka 11:13.
19, 20. (a) Roho ya Mungu ilikuwa na ukamatano gani na malaika watakatifu na huduma ya Kikristo wakati uliopita? (b) Je! roho takatifu ya Mungu na uongozi wa kimalaika vingali vinaupasa utendaji mbalimbali wa kuhubiri wa Kikristo?
19 Malaika watakatifu vile vile wanafanya sehemu yao. Kwa kukubali uongozi wa kimalaika na maongozi ya roho takatifu ya Yehova, Filipo mtangazaji wa injili alimkuta towashi wa Ethiopia naye “akamhubiri habari njema za Yesu.” Matokeo yalifuata mara hiyo. Kwa haraka Mwethiopia akabatizwa. Nyuma ya hapo ‘roho ya Yehova ikamnyakua Filipo’ na karibuni alikuwa anatunza mgawo mwingine wa huduma. (Matendo 8:26-40) Roho takatifu ya Mungu na uongozi wa kimalaika vile vile vilifanya sehemu yavyo katika kazi ya kuhubiri iliyofanywa na mtume Petro nyumbani kwa Kornelio Mtaifa.—Matendo sura ya 10.
20 Roho takatifu ile ile na uongozi wa kimalaika vingali vinaupasa utendaji mbalimbali wa wahudumu wa Kikristo. Mtume mzee Yohana alimwona ‘malaika akiruka katikati ya mbingu’ mwenye “Injili ya milele” ya kutangazia wakaaji wa dunia. (Ufu. 14:6, 7) Hapana, leo huwezi kumwona malaika huyo akiruka angani, wala kumsikia akisema waziwazi. Lakini waweza kuusikia ujumbe wake, kwa maana unatolewa duniani na waabudu wa Yehova. Kwa hakika, wanasema juu ya Yehova: “Tazama, huyu ndiye Mungu wetu, ndiye tuliyemngoja atusaidie; huyu ndiye [Yehova] tuliyemngoja, na tushangilie na kuufurahia wokovu wake.” (Isa. 25:9) Ni sana kadiri gani inavyompasa mtu kushukuru kwa kuongozwa na roho takatifu ya Mungu na kuwa na uongozi wa kimalaika anapolichukua jina na kuyatangaza makusudi na sifa za Aliye Juu Zaidi Sana kama mmoja wa mashahidi wa Yehova wa Kikristo!—Isa. 43:10.
21. Mtu awezaje kufanya ziara za kurudia zenye matokeo na kuongoza mafunzo mazuri ya nyumbani ya Biblia?
21 Pendeleo hilo lenye kuogofya linataka jitihada zilizo bora za Mkristo katika huduma. Ikiwa wewe u mhudumu wa Kikristo, wawezaje kuwa mwenye matokeo katika utumishi wa shambani? Kwanza, weka kumbukumbu nzuri ya utendaji wa huduma. Halafu itawezekana kufanya ziara za kurudia za haraka. Zaidi ya hayo,zifanye hizi zenye matokeo kwa kufikiri mapema juu ya magumu ya mtu, mapendezi au mahitaji. Weka maandiko ya Biblia yatakayomsaidia mtu huyo. Inapowezekana, nyuma ya hapo uanze na kuongoza mafunzo ya nyumbani ya Biblia mazuri na mtu huyo. Katika hili msaada wa roho takatifu ya Yehova ni wa lazima nao utakuwa wazi. Kati ya mambo mengine, itakumbusha habari iliyosomwa wakati uliopita. (Marko 13:11) Jitahidi kurahisisha habari katika akili yako mwenyewe. Ndipo utakapoweza kutoa maoni yanayofahamika na ya kweli na kusaidia wengine kufahamu. Uwe kama Ezra na Walawi walioshirikiana naye waliosomea Waisraeli waliokusanyika katika Yerusalemu sheria ya Mungu. Waalimu hao walijua waliyokuwa wakiyazungumza, kwa maana twaambiwa: “Nao wakasoma katika kitabu, katika torati ya Mungu, kwa sauti ya kusikilika; wakaeleza maana yake, hata wakayafahamu yaliyosomwa.” Je! jitihada zao zilitokeza matokeo mazuri? Ndiyo, kwa maana watu walifahamu, wakafurahi sana, nao wakaadhimisha sikukuu ya vibanda.—Neh. 8:8, 12-18.
WAELEKEZE WENGINE KWENYE TENGENEZO LA YEHOVA
22. Ni kwa njia gani huenda mtu akasitawisha shukrani kwa Neno la Mungu na tengenezo katika mioyo ya watu wanaopendezwa?
22 Unapoongoza mafunzo ya Biblia yenye kufundisha na watu wanaopendezwa, jaribu kusitawisha mioyoni mwao shukrani kwa Neno la Mungu na tengenezo lake, kundi la Kikristo. Kwa mfano, ugumu unapotokea na njia ya kuumaliza ya Maandiko yapatikana katika kitabu cha Kikristo, huenda mwanafunzi wa Biblia akaulizwa: ‘Kama tengenezo la Yehova lisingalitupa sisi ufahamu wa Biblia katika mashauri kama haya, tusingejua mwendo wa kuchukua ili kumpendeza Mungu, sivyo?’ Maulizo kama hayo yenye kuchochea mawazo yaweza kutumiwa kwa matokeo yenye nguvu. Yatamfanya mwanafunzi afikiri na aujue ubora na umuhimu wa Biblia na tengenezo la Yehova.
23. Unawezaje kwa shauku kuelekeza wengine kwenye tengenezo la Mungu?
23 Ikiwa wewe unalishukuru tengenezo la Yehova kweli kweli, utawaelekeza wengine kwenye hilo kwa shauku. Yohana Mbatizaji alipowaambia wawili wa wanafunzi wake kwamba Yesu alikuwa ndiye “Mwana-kondoo wa Mungu,” wao waliitikiaje? Kwa ulegevu, kwa ubaridi? Wakati Andrea alipomweleza Petro juu ya uvumbuzi wao, je! wadhani kwamba yeye alisema polepole, kwa kunong’ona tu, “Tumemwona Masihi”? Hata. Lazima kuwe kulikuwamo msisimko kadiri fulani katika sauti yake. Ebu fikiri! Walikuwa wamempata Masihi, Yeye Aliyetiwa Mafuta wa Mungu! (Yohana 1:35-41) Basi, ikiwa wewe wazoea Ukristo wa kweli, umelipata tengenezo linaloelimisha watu kwa ajili ya uzima wa milele, tengenezo lililo la pekee duniani linalomtumikia Yehova Mungu chini ya Mfalme wake wa Kimasihi. Hilo ni jambo la kushukuru kweli kweli. Kwa hiyo, kwa shauku uwaelekeze wengine kwenye tengenezo la Mungu. Waambie juu ya kundi la Kikristo la kweli na historia yake ya kisasa. Waonyeshe namna wale wanaoshirikiana na tengenezo la kidunia la Yehova wanavyotembea katika nuru ya kiroho, walivyo na tegemezo la Mungu na uongozi wa roho takatifu yake na wanavyofurahia baraka zake nyingi. Eleza kwamba mashahidi wa Yehova wa Kikristo wametengenezwa ili wamsifu Mungu na kwamba watu wanaostahili wanalo pendeleo la kumsifu Yehova pamoja na watu wake. Usitawishe katika wanafunzi wako wa Biblia shukrani kwa Yehova na tengenezo lake linaloelimisha watu kwa ajili ya uzima wa milele.
24. Nini atakachofanya mtu mwenye shukrani ya kweli kwa Yehova na tengenezo lake Yeye?
24 Shetani Ibilisi ana tengenezo la mashetani na wanadamu. Sasa linaelekea kwenye. kushindwa kabisa na uharibifu wa milele utakaoletwa na Mungu na majeshi yake ya kufishia yakiongozwa na Yesu Kristo. Lakini tengenezo la Yehova limo katika mwendo likiwa na matumaini ya ajabu mbele yake. Kwa mwendo ulioharakishwa linasonga mbele nalo litazidi kusonga mbele, katika huzuni iliyopo na “dhiki kubwa” ambayo ingali mbele, hata kuingia katika taratibu mpya ya ahadi ya Mungu. (Mt. 24:21; 2 Pet. 3:13) Je! wewe, kwa fadhili zisizostahili za Mungu, u mwenye nia ya kusonga pamoja nalo kwa uaminifu? Je! umesitawisha shukrani ya kadiri hiyo kwa Yehova na tengenezo analolitumia kuelimisha watu kwa ajili ya uzima wa milele? Ikiwa ndivyo, basi songa mbele, nyimbo za sifa kwa Yehova zikiwa midomoni pako. Umsifu Mungu, kama walivyofanya waimbaji Walawi wa kale na kama majeshi ya kimalaika ya mbinguni. Uendelee kumsifu Yehova pamoja na watu wake. Uwe hodari kama Daudi, aliyesema kwa mkazo: “Nitamwimbia [Yehova] maadamu ninaishi; nitamshangilia Mungu wangu nikiwa hai; kutafakari kwangu na kuwe kutamu kwake; mimi nitamfurahia [Yehova].”—Zab. 104:33, 34.
—Kutoka The Watchtower, July 1, 1973.