Sehemu ya 8
Kataa Dini Isiyo ya Kweli; Fuata Dini ya Kweli
1. Watu wapaswa kufanya uchaguzi gani leo kuhusu ibada?
YESU alisema: “Yeye asiyekuwa upande wangu yuko dhidi yangu.” (Mathayo 12:30) Tunakuwa ama upande wa Yehova ama upande wa Shetani. Watu wengi hufikiri kwamba wanamtumikia Mungu kwa njia inayokubalika, lakini Biblia inasema kwamba Shetani ‘anaiongoza vibaya dunia nzima inayokaliwa.’ (Ufunuo 12:9) Mamilioni ya watu wanaamini kwamba wanamwabudu Mungu, lakini ukweli ni kwamba wanamtumikia Shetani Ibilisi! Leo ni lazima watu wachague kama watamtumikia Yehova, “Mungu wa kweli,” au Shetani, “baba ya uwongo.”—Zaburi 31:5; Yohana 8:44.
Toka Katika Dini Isiyo ya Kweli
2. Shetani hutumia njia gani kujaribu kuwazuia watu wasimwabudu Yehova?
2 Ni jambo la hekima kuchagua kumtumikia Yehova kwa sababu kufanya hivyo hufanya mtu akubaliwe naye. Lakini Shetani hampendi mtu yeyote anayemtumikia Mungu; yeye huwanyanyasa wale wanaomtumikia Mungu. Njia moja anayotumia ni dhihaka au upinzani kutoka kwa wengine, hata kutoka kwa marafiki na watu wa familia. Yesu alionya hivi: “Kwa kweli, maadui wa mtu watakuwa watu wa nyumbani mwake mwenyewe.”—Mathayo 10:36.
3. Watu wa familia yenu au marafiki wakikupinga usimwabudu Mungu, utafanya nini?
3 Utafanya nini iwapo utapatwa na mambo hayo? Watu wengi husita kuacha dini yao hata ingawa wanajua si ya kweli. Wanaona kwamba kufanya hivyo ni kukosa uaminifu kwa familia zao. Je, kweli hayo ni maoni mazuri? Kama ungegundua kwamba wengine katika familia yenu wanatumia dawa za kulevya, je, hungewaonya kwamba dawa hizo zitawadhuru? Je, hungekataa kujiunga nao kutumia dawa hizo?
4. Yoshua aliwaambia nini Waisraeli kuhusu ibada katika siku zake?
4 Yoshua aliwatia moyo Waisraeli waache matendo na mapokeo ya kidini ya mababu zao ambayo hayakufaa. Alisema: “Sasa mcheni BWANA, mkamtumikie kwa unyofu wa moyo na kwa kweli; na kuiweka mbali miungu ambayo baba zenu waliitumikia ng’ambo ya Mto, na huko Misri; mkamtumikie yeye BWANA.” (Yoshua 24:14) Yehova alimbariki Yoshua kwa sababu alikuwa mwaminifu-mshikamanifu kwake. Yehova atatubariki pia ikiwa tutakuwa waaminifu kwake.—2 Samweli 22:26.
Haribu Vitu Vinavyotumiwa Katika Ibada Isiyo ya Kweli
5. Kwa nini tunapaswa kuharibu vitu vya uchawi?
5 Kutoka katika dini isiyo ya kweli pia kunatia ndani kuharibu vitu vyovyote vya uchawi ambavyo huenda tukawa navyo, kama vile hirizi, pete za uchawi, bangili za uchawi, na kadhalika. Jambo hilo ni muhimu kwa sababu linaonyesha kwamba tunamtumaini Yehova kabisa.
6. Wakristo wa mapema walifanya nini na vitabu vyao vya uchawi?
6 Ona jinsi Wakristo fulani wa mapema walivyofanya walipoamua kufuata dini ya kweli. Biblia inasema: “Idadi kubwa ya wale waliozoea kufanya ufundi wa kimzungu wakaleta pamoja vitabu vyao wakavichoma kabisa mbele ya kila mtu.”—Matendo 19:19.
7. Tunaweza kufanya nini roho waovu wakitusumbua?
7 Huenda watu fulani wanaoanza kumtumikia Yehova na ambao walihusika na ulozi au uchawi wakasumbuliwa na roho waovu. Roho hao wakikusumbua, sali kwa Yehova ukitaja jina lake kwa sauti kubwa. Atakusaidia.—Mithali 18:10; Yakobo 4:7.
8. Wakristo huzionaje sanamu, mifano, na picha zinazotumiwa katika ibada isiyo ya kweli?
8 Wale wanaotaka kumtumikia Yehova hawapaswi kuweka au kutumia sanamu, mfano, au picha yoyote inayohusiana na ibada isiyo ya kweli. Wakristo wa kweli ‘wanatembea kwa imani, si kwa kuona.’ (2 Wakorintho 5:7) Wanaheshimu sheria ya Mungu inayokataza kutumia mfano wowote katika ibada.—Kutoka 20:4, 5.
Shirikiana na Watu wa Yehova
9. Biblia inatoa ushauri gani kuhusu kupata hekima?
9 Biblia inasema: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima.” (Mithali 13:20) Tukitaka kuwa na hekima, tunahitaji kutembea, au kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Hao ndio watu wanaotembea katika barabara inayoongoza kwenye uhai.—Mathayo 7:14.
10. Mashahidi wa Yehova wanaweza kukusaidiaje umtumikie Mungu?
10 Mashahidi wa Yehova hujali watu kikweli. Kazi yao ni kusaidia watu wenye mioyo minyofu waelewe kweli za Biblia zinazoongoza kwenye uhai wa milele. Wanaweza kukusaidia ujifunze Biblia bila malipo. Watajibu maswali yako na kukuonyesha jinsi ya kutumia ujuzi wa Biblia maishani mwako.—Yohana 17:3.
11. Mikutano ya Kikristo itakusaidiaje?
11 Kwenye mikutano yao, ambayo kwa ukawaida hufanywa kwenye Majumba ya Ufalme, utajifunza mengi kuhusu njia za Yehova. Tamaa yako ya kufuata dini ya kweli itachochewa. Utazoezwa pia jinsi ya kuwasaidia wengine wajifunze kweli za Biblia.—Waebrania 10:24, 25.
12. Sala inaweza kukusaidiaje umtumikie Mungu?
12 Unapoendelea kujifunza mengi juu ya mapenzi na kusudi la Mungu, inaelekea utathamini zaidi njia zake zenye upendo. Unapaswa pia kuzidisha tamaa yako ya kufanya mambo yanayompendeza na kuepuka yale yasiyompendeza. Kumbuka kwamba unaweza kusali kwa Yehova na kumwomba akusaidie kufanya mambo yanayofaa na kuepuka yale yasiyofaa.—1 Wakorintho 6:9, 10; Wafilipi 4:6.
13. Unaweza kufurahishaje moyo wa Yehova?
13 Unapoendelea kukua kiroho, inaelekea utaona uhitaji wa kujiweka wakfu, na kubatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Utaufurahisha moyo wa Yehova kwa kujiunga na watu wake. (Mithali 27:11) Utakuwa kati ya watu wenye furaha ambao Mungu anasema hivi kuwahusu: “Mimi nitakaa miongoni mwao na kutembea miongoni mwao, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.”—2 Wakorintho 6:16.
Mafundisho ya Kidini—Ya Kweli na Yasiyo ya Kweli
● Utatu: Dini nyingi hufundisha kwamba Mungu ni Utatu. Zinasema kwamba “Baba ni Mungu, Mwana [Yesu] ni Mungu, na Roho Takatifu ni Mungu, na hata hivyo, hawa si Miungu watatu bali ni Mungu mmoja.”
Biblia hata haitaji neno “Utatu,” wala haifundishi kwamba Yehova ni watu watatu katika mmoja. Yehova peke yake ndiye Mungu. Andiko la 1 Wakorintho 8:6 lasema: “Kwa kweli kwetu kuna Mungu mmoja Baba.” Yehova ndiye Mkuu Kuliko Wote. Yesu si Mungu, bali yeye ni “Mwana wa Mungu.” (1 Yohana 4:15) Vivyo hivyo, roho takatifu si Mungu wala hata si mtu. Hiyo ni nguvu ya Mungu ya utendaji.—Matendo 1:8; Waefeso 5:18.
● Nafsi: Dini nyingi hufundisha kwamba nafsi ni kitu fulani ndani ya mtu ambacho hakiwezi kufa. Biblia hufundisha kwamba nafsi ni mtu na hapana shaka mtu anaweza kufa.—Mwanzo 2:7; Ezekieli 18:4, ZSB.
● Moto wa Mateso: Dini zisizo za kweli hufundisha kwamba nafsi za waovu huteswa milele katika moto. Biblia husema kwamba wafu “hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Biblia pia hufundisha kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Yehova, Mungu mwenye upendo, hawezi kutesa watu kwa moto.
[Swali ya Funzo]
Sanduku: Biblia hufundisha nini kuhusu Utatu, nafsi, na moto wa mateso?
Niliacha Kushirikiana na Roho Waovu
Usiku mmoja nilipokuwa nimelala usingizi pamoja na mume wangu, nilisikia sauti ikiniita kwa jina mara tatu. Kisha nikaona dari likipasuka, na kitu kama mpira unaowaka moto, kikaniangukia tumboni. Mume wangu hata hakuona mambo hayo. Kwa miezi kadhaa, nilihisi joto kali.
Miezi sita baadaye, ile sauti iliniita tena. Mara, nyumba nzima ikaonekana kana kwamba imo ndani ya maji mengi. Nyoka mkubwa alitoka katika yale maji na kujiviringisha kwenye mkono wangu. Nilijaribu bila mafanikio kumwondoa nyoka huyo kwa kutikisa mkono. Niliogopa sana. Kisha yale maji na yule nyoka akatoweka, nami nikaangushwa chini kwa kishindo. Nilipoteza fahamu kwa muda wa saa kadhaa. Kisha ile sauti ikaniambia nirudi kwenye hekalu moja kijijini la watu waliokuwa wakiponya kwa kuwasiliana na roho. Nilipomwuliza roho huyo anaitwaje, alinipa jina lililomaanisha “utakuwa tajiri lakini hutapata mtoto.” Aliahidi kunitajirisha kwa kunipa nguvu za kuponya.
Wagonjwa kutoka mbali na karibu walikuja kwangu. Kabla hawajafika nyumbani kwangu, ningewaona katika kioo changu cha pekee. Kisha mtu alipofika, ningepiga mkono wake kwa mkono wangu nami ningefunuliwa mara moja tatizo au ugonjwa wake pamoja na tiba yake. Roho huyo pia aliniambia kiasi cha pesa ambacho watu wangepaswa kulipa.
Nilipata pesa na zawadi nyingi sana kutoka kwa watu nilioponya. Nikawa “tajiri,” lakini pia nikajua maana ya maneno “hutapata mtoto.” Kila wakati nilipozaa mtoto, yule aliyemtangulia alikufa. Jambo hili lilinihuzunisha sana. Katika miaka 12 niliyotumikia roho huyo, sita kati ya watoto wangu walikufa.
Nilianza kusali kwa bidii ili Mungu anisaidie. Siku moja Mashahidi wa Yehova walinitembelea na ingawa kwa kawaida nilikuwa nikiwafukuza, siku hiyo niliamua kuwasikiliza. Tulipokuwa tunazungumza, niligundua kwamba nilikuwa nikimtumikia roho mwovu! Niliamua kuacha kuwasiliana na roho.
Nilipomwambia roho huyo uamuzi wangu, alinionya nisifanye uamuzi huo. Hata hivyo, nilimwambia, “Uhusiano wangu na wewe umekwisha.”
Nilichoma vitu vyote nilivyotumia katika uaguzi. Nikajifunza Biblia na wale Mashahidi, nikawa mtumishi wa Yehova na kubatizwa mwaka wa 1973. Sasa nina watoto watano wenye afya. Mume wangu pia alibatizwa na kuwa Shahidi.”—Imesimuliwa na Josephine Ikezu.
Sanduku: Mwanamke mmoja aliachaje kushirikiana na roho waovu?
[Picha katika ukurasa wa 26]
Unaweza kufuataje dini ya kweli?