Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • kp kur. 12-15
  • “Saa Ya Hukumu” Imefika

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Saa Ya Hukumu” Imefika
  • Endeleeni Kukesha!
  • Habari Zinazolingana
  • Mwisho Wenye Kutazamisha wa Dini ya Uwongo Waonekana Kimbele
    Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
  • “Yule Kahaba Mkuu” Akaribia Kuuawa Kwake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Jiji Kubwa Lateketezwa
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
  • “Kimbieni Kutoka Kati ya Babeli”
    Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
Pata Habari Zaidi
Endeleeni Kukesha!
kp kur. 12-15

“Saa Ya Hukumu” Imefika

UFUNUO, kitabu cha mwisho cha Biblia kinatuarifu kwamba malaika anayeruka katikati ya mbingu ana “habari njema ya milele ili aitangaze kuwa habari za furaha.” Anasema hivi kwa sauti kubwa: “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imefika.” (Ufunuo 14:6, 7) ‘Saa hiyo ya hukumu’ inatia ndani kutangazwa na kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu. “Saa” ni kipindi kifupi cha wakati. Kutekelezwa kwa hukumu ndio upeo wa “siku za mwisho” tunamoishi leo.—2 Timotheo 3:1.

“Saa ya hukumu” ni habari njema kwa wale wanaopenda uadilifu. Ni wakati ambapo Mungu atawaletea kitulizo watumishi wake ambao wameteseka mikononi mwa ulimwengu huu wenye jeuri na usio na upendo.

Sasa, kabla “saa ya hukumu” kufikia upeo kwenye uharibifu wa ulimwengu huu mwovu, tunahimizwa hivi: “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu.” Je, unafanya hivyo? Kufanya hivyo kunahusisha mengi zaidi ya kusema tu “ninamwamini Mungu.” (Mathayo 7:21-23; Yakobo 2:19, 20) Woga unaofaa wa Mungu unapaswa kutufanya tumheshimu. Unapaswa kutufanya tuepuke mabaya. (Methali 8:13) Unapaswa kutusaidia tupende mema na kuchukia mabaya. (Amosi 5:14, 15) Ikiwa tunamheshimu Mungu, tutamsikiliza kwa makini. Hatutaruhusu shughuli nyingine zitufanye tupuuze kusoma Neno lake, Biblia, kwa ukawaida. Tutamtegemea kwa moyo wetu wote nyakati zote. (Zaburi 62:8; Methali 3:5, 6) Wale wanaomheshimu kikweli humtambua kuwa Muumba wa mbingu na dunia, Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote, nao hujitiisha kwake kwa upendo akiwa Mtawala wao. Tukitambua kwamba tunahitaji kuzingatia zaidi mambo haya, tunapaswa kufanya hivyo bila kukawia.

Kipindi cha kutekeleza hukumu iliyotajwa na malaika huitwa pia “siku ya Yehova.” “Siku” kama hiyo ilikuja juu ya Yerusalemu la kale mwaka wa 607 K.W.K. kwa sababu wakazi wake hawakutii maonyo ambayo Yehova alitoa kupitia manabii wake. Walihatarisha uhai wao hata zaidi kwa kufikiria kwamba siku ya Yehova ilikuwa mbali. Yehova alikuwa amewaonya hivi: “Iko karibu, nayo inaharakisha sana.” (Sefania 1:14) ‘Siku nyingine ya Yehova’ ilikuja juu ya Babiloni la kale mwaka wa 539 K.W.K. (Isaya 13:1, 6) Wababiloni walitegemea ngome zao na miungu yao na hivyo wakapuuza maonyo yaliyotolewa na manabii wa Yehova. Lakini katika usiku mmoja, jiji kuu la Babiloni lilitekwa na Wamedi na Waajemi.

Tunakabili nini leo? Tunakabili ‘siku nyingine ya Yehova’ iliyo kubwa zaidi. (2 Petro 3:11-14) Hukumu ya Mungu imetangazwa juu ya “Babiloni Mkubwa.” Kulingana na Ufunuo 14:8, malaika anatangaza hivi: “Babiloni Mkubwa ameanguka.” Tayari ameanguka. Hawezi tena kuwazuia waabudu wa Yehova. Ufisadi wake na kujihusisha kwake katika vita kumefunuliwa wazi. Sasa uharibifu wake wa mwisho umekaribia. Kwa sababu hiyo, Biblia inawahimiza watu wote hivi: “Tokeni kwake [Babiloni Mkubwa] . . . ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake, na ikiwa hamtaki kupokea sehemu ya mapigo yake. Kwa maana dhambi zake zimekusanyika pamoja mpaka mbinguni, naye Mungu amekumbuka matendo yake yasiyo ya haki.”—Ufunuo 18:4, 5.

Babiloni Mkubwa Ni Nini? Ni mfumo wa ulimwenguni pote wa dini zenye mazoea kama ya Babiloni la kale. (Ufunuo, sura ya 17, 18) Hebu ona baadhi ya mazoea hayo:

• Makuhani wa Babiloni la kale walijihusisha sana na siasa za taifa hilo. Ndivyo ilivyo na dini nyingi leo.

• Mara nyingi, makuhani wa Babiloni waliwatia watu moyo kwenda vitani. Mara nyingi dini za leo huwa mstari wa mbele katika kuwabariki wanajeshi wakati mataifa yanapoenda vitani.

• Mafundisho na mazoea ya Babiloni la kale yaliongoza taifa hilo katika ukosefu mbaya sana wa maadili. Viongozi wa dini leo wanapopuuza viwango vya maadili vya Biblia, ukosefu wa maadili huenea sana kati ya viongozi wa dini na pia waumini. Yafaa kuzingatia kwamba Ufunuo humtaja Babiloni Mkubwa kuwa kahaba kwa sababu anafanya uasherati na ulimwengu na mifumo yake ya kisiasa.

• Biblia pia inasema kwamba Babiloni Mkubwa anaishi “katika anasa isiyo na aibu.” Katika Babiloni la kale, wasimamizi wa hekalu walimiliki mashamba makubwa na makuhani wakawa wanabiashara mashuhuri. Leo, mbali na kumiliki makanisa mengi, Babiloni Mkubwa ana mali na biashara chungu nzima. Mafundisho yake na sikukuu zake humletea yeye pamoja na wengine katika ulimwengu wa biashara utajiri mkubwa.

• Matumizi ya sanamu, mizungu, na ulozi yalikuwa ya kawaida katika Babiloni la kale, na ndivyo ilivyo katika sehemu nyingi leo. Kifo kilionwa kuwa njia ya kuingia katika maisha mengine. Jiji la Babiloni lilijaa mahekalu na majengo yaliyotumiwa kuabudu miungu yake, lakini Wababiloni waliwapinga waabudu wa Yehova. Babiloni Mkubwa hufuata mafundisho na mazoea hayohayo.

Katika nyakati za kale, Yehova aliyatumia mataifa yenye nguvu kisiasa na kijeshi kuwaadhibu wale walioendelea kumpuuza yeye na mapenzi yake. Basi Samaria liliharibiwa na Waashuru mwaka wa 740 K.W.K. Yerusalemu liliharibiwa kabisa na Wababiloni mwaka wa 607 K.W.K. na pia na Waroma mwaka wa 70 W.K. Nalo Babiloni lilitekwa na Wamedi na Waajemi mwaka wa 539 K.W.K. Biblia inatabiri kwamba katika nyakati zetu serikali za kisiasa, kama mnyama-mwitu, zitamshambulia “yule kahaba” na kumwacha uchi na hivyo kumfunua alivyo kikweli. Zitamwangamiza kabisa.—Ufunuo 17:16.

Je, kweli serikali za ulimwengu zitafanya hivyo? Biblia inasema kwamba ‘Mungu atalitia hilo ndani ya mioyo yao.’ (Ufunuo 17:17) Shambulizi hilo litafanywa ghafula, litashangaza na kushtua na litatukia bila kutarajiwa.

Unapaswa kuchukua hatua gani? Jiulize: ‘Je, bado mimi ni mfuasi wa dini ambayo imechafuliwa na mafundisho na mazoea yanayoifanya kuwa sehemu ya Babiloni Mkubwa?’ Hata kama wewe si mfuasi wa dini kama hiyo, huenda ukajiuliza: ‘Je, nimeruhusu roho yake iniathiri?’ Roho gani? Roho ya kukubali maadili mapotovu, kupenda mali na raha badala ya kumpenda Mungu, au kupuuza kimakusudi Neno la Yehova (hata katika mambo yanayoonekana kuwa madogo). Fikiria kwa uzito jibu lako.

Ili tupate kibali cha Yehova ni muhimu tuonyeshe kwa matendo na kutoka moyoni kwamba kwa kweli sisi si sehemu ya Babiloni Mkubwa. Huu si wakati wa kukawia-kawia. Ikituonya kwamba mwisho utakuja ghafula, Biblia inasema: ‘Babiloni lile jiji kubwa litatupwa chini kwa mtupo wa kasi sana, naye hatapatikana tena.’—Ufunuo 18:21.

Lakini kuna matukio mengine. Katika “saa ya hukumu,” Yehova atahukumu pia mfumo wa kisiasa wa ulimwengu, watawala wake, na wote wanaopuuza utawala wake kupitia Ufalme wake wa kimbingu ulio mikononi mwa Yesu Kristo. (Ufunuo 13:1, 2; 19:19-21) Maono ya kinabii yaliyoandikwa katika Danieli 2:20-45 yanaonyesha serikali za kisiasa tangu wakati wa Babiloni la kale hadi leo zikiwa kama sanamu kubwa iliyotengenezwa kwa dhahabu, fedha, shaba, chuma, na udongo. Unabii huo ulitabiri hivi kuhusu nyakati zetu: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe.” Na kuhusu yale yatakayotimizwa na Ufalme huo wakati wa “saa ya hukumu” ya Yehova, Biblia inatangaza hivi: “Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote [za kibinadamu], nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Danieli 2:44.

Biblia inawaonya waabudu wa kweli wasipende “vitu vilivyo katika ulimwengu,” yaani, mtindo wa maisha unaoendelezwa na ulimwengu huu ambao umejitenga na Mungu wa kweli. (1 Yohana 2:15-17) Je, maamuzi na matendo yako yanaonyesha kwamba unaunga mkono kabisa Ufalme wa Mungu? Je, kweli wewe huutanguliza maishani mwako?—Mathayo 6:33; Yohana 17:16, 17.

[Sanduku katika ukurasa wa 14]

Mwisho Utakuja Lini?

“Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyofikiria.”—Mathayo 24:44.

“Endeleeni kukesha kwa sababu hamwijui ile siku wala saa.”—Mathayo 25:13.

‘Haitachelewa.’—Habakuki 2:3.

[Sanduku katika ukurasa wa 14]

Je, Maisha Yako Yatabadilika Ukijua Mwisho Utakuja Lini?

Ukijua kwa uhakika kwamba siku ya kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu itakawia kwa miaka kadhaa, je, utabadili jinsi unavyoishi? Je, umepunguza bidii yako katika utumishi wa Yehova kwa sababu mwisho wa mfumo huu wa kale unaonekana umekawia?—Waebrania 10:36-38.

Kutojua mwisho utakuja lini hutupa nafasi ya kuonyesha kwamba tunamtumikia Mungu kwa nia nzuri. Wale wanaomjua Yehova wanatambua kwamba hatapendezwa na bidii inayoonyeshwa dakika ya mwisho kwa kuwa yeye huona kilicho moyoni.—Yeremia 17:10; Waebrania 4:13.

Wale ambao wanampenda Yehova kikweli hutanguliza mapenzi yake sikuzote. Wakristo wa kweli hufanya kazi ya kimwili kama watu wengine. Hata hivyo, kusudi lao si kutajirika, bali ni kupata mahitaji ya lazima na kuwa na kitu cha kuwagawia wengine. (Waefeso 4:28; 1 Timotheo 6:7-12) Wao pia hufurahia tafrija zenye kujenga na starehe, lakini kusudi lao si kufanya kama kila mtu anavyofanya bali ni kuburudika. (Marko 6:31; Waroma 12:2) Kama Yesu Kristo, wao hufurahia kufanya mapenzi ya Mungu.—Zaburi 37:4; 40:8.

Wakristo wa kweli wanataka kuishi na kumtumikia Yehova milele. Tumaini hilo halipotezi maana hata kama wanalazimika kungoja baraka kwa muda mrefu kuliko wengine walivyotarajia.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]

Suala la Enzi Kuu

Ili tuelewe ni kwa nini Mungu ameruhusu wanadamu wateseke sana, lazima tuelewe suala la enzi kuu. Enzi kuu ni nini? Ni mamlaka iliyo kuu zaidi.

Yehova ndiye Muumba, kwa hiyo ana haki ya kuitawala dunia na wote wanaoishi humo. Hata hivyo, Biblia inaeleza kwamba mwanzoni mwa historia ya wanadamu, enzi kuu ya Yehova ilipingwa. Shetani Ibilisi alidai kwamba Yehova alikuwa amewawekea wazazi wetu wa kwanza vizuizi vingi, na alikuwa amewadanganya kuhusu matokeo ya kujitegemea na kupuuza sheria ya Mungu. Alidai kwamba ingekuwa afadhali kama wangejitawala pasipo msaada wa Mungu.—Mwanzo, sura ya 2 na 3.

Ikiwa Mungu angewaharibu waasi hao mara moja, angethibitisha kwamba ana nguvu, lakini hangekuwa ametatua masuala yaliyozushwa. Badala ya kuwaharibu waasi hao papo hapo, Yehova amewaacha malaika na wanadamu waone matokeo ya uasi. Ingawa jambo hilo limesababisha mateso mengi, limetokeza nafasi ya sisi kuzaliwa.

Isitoshe, Yehova alijidhabihu sana na kwa upendo akafanya mipango ili wanadamu wanaomtii na kuwa na imani katika dhabihu ya fidia ya Mwanaye wawekwe huru kutokana na dhambi na matokeo yake, kisha waishi katika Paradiso. Ikiwa lazima, jambo hilo litatimizwa kupitia ufufuo wa wafu.

Kwa kuruhusu wakati upite ili suala hilo litatuliwe, Mungu amewapa watumishi wake nafasi ya kuonyesha kwamba wanaweza kuitikia upendo wake na kuthibitisha utimilifu wao kwa Yehova chini ya hali zozote zile. Kutatuliwa kwa suala la enzi kuu ya Mungu, pamoja na suala la utimilifu wa wanadamu ni muhimu ili watu waheshimu ifaavyo sheria katika ulimwengu wote. Hakuwezi kuwa na amani ya kweli watu wasipoheshimu sheria.a

[Maelezo ya Chini]

a Masuala hayo na mambo yote yanayohusiana nayo yameelezwa kwa urefu katika kitabu Mkaribie Yehova, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha]

Mfumo wa serikali za kisiasa ulimwenguni pote utaharibiwa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki