SURA YA TISA
Kuwatendea Wengine Kama Mungu Anavyotaka
1-3. (a) Huenda Wakristo wengi wakafikiria nini kuhusu jiji la kale la Tiro? (b) Eleza baadhi ya shughuli zilizokuwapo kati ya Mfalme Hiramu na Israeli. (c) Tungependa kujifunza nini kuhusu Tiro?
WEWE hufikiria nini unaposikia jiji la kale la Tiro likitajwa? Wakristo wengi hufikiria jinsi unabii ulivyotimizwa wakati Aleksanda Mkuu alipoondoa vifusi kutoka katika magofu ya jiji la Tiro lililokuwa barani na kutengeneza njia hadi kwenye jiji jipya la Tiro lililokuwa kisiwani na kuliharibu. (Ezekieli 26:4, 12; Zekaria 9:3, 4) Hata hivyo, je, jina Tiro linaweza kukufanya ufikirie jinsi unavyopaswa au usivyopaswa kuwatendea ndugu zako wa kiroho au watu wengine?
2 Tiro liliharibiwa kwa sababu gani? “Kwa sababu ya maasi matatu ya Tiro, . . . kwa sababu ya kulitia mkononi mwa Edomu kundi zima la wahamishwa, na kwa sababu hawakukumbuka agano la ndugu. Nami nitapeleka moto kwenye ukuta wa Tiro.” (Amosi 1:9, 10) Katika nyakati zilizopita, Mfalme Hiramu wa Tiro alimtendea wema Daudi na kuleta vifaa vya ujenzi wa hekalu la Sulemani. Sulemani alifanya agano na Hiramu na kumpa majiji katika Galilaya. Hiramu alimwita Sulemani “ndugu yangu.” (1 Wafalme 5:1-18; 9:10-13, 26-28; 2 Samweli 5:11) Wakati Tiro ‘halikukumbuka agano la ndugu’ na kuwauza baadhi ya watu wa Mungu utumwani, Yehova aliona matendo ya Tiro.
3 Tunajifunza nini kutokana na hatua ya Mungu ya kuwahukumu Wakanaani wa Tiro kwa sababu ya kuwatendea kikatili watu wake? Jambo kuu tunalojifunza linahusu jinsi tunavyowatendea ndugu zetu wa kiroho. Katika sura zilizotangulia za kitabu hiki, tulijifunza mashauri fulani yaliyotolewa na wale manabii 12 kuhusiana na jinsi tunavyopaswa kuwatendea wengine, kama vile kufuata haki katika mambo ya kibiashara na kuwa na mwenendo safi. Hata hivyo, vitabu hivi 12 vinasema mengi kuhusu jinsi Mungu anavyotaka tuwatendee wengine.
USISHANGILIE WENGINE WANAPOPATA MATATIZO
4. Waedomu walikuwa “ndugu” za Waisraeli jinsi gani, lakini waliwatendeaje “ndugu” zao?
4 Unaweza kujifunza jambo fulani kutokana na hatua ya Mungu ya kushutumu Edomu, nchi jirani ya Israeli: “Hupaswi kutazama tukio katika siku ya ndugu yako, katika siku ya maafa yake; wala kushangilia juu ya wana wa Yuda katika siku ya kuangamia kwao.” (Obadia 12) Huenda watu wa Tiro walikuwa “ndugu” zao kibiashara, lakini Waedomu walikuwa “ndugu” za Waisraeli kihalisi, kwa kuwa walikuwa wazao wa Esau, ndugu pacha wa Yakobo. Hata Yehova aliwaita Waedomu “ndugu” za Waisraeli. (Kumbukumbu la Torati 2:1-4) Kwa hiyo, Waedomu walionyesha chuki kikweli kwa kushangilia msiba wa Wayahudi mikononi mwa Wababiloni.—Ezekieli 25:12-14.
5. Huenda tukaonyesha roho kama ya Waedomu katika hali gani?
5 Ni wazi kwamba Mungu hakufurahia jinsi Waedomu walivyowatendea ndugu zao Wayahudi. Hata hivyo, twaweza kujiuliza hivi: ‘Mungu anaonaje matendo yangu kuelekea ndugu zangu?’ Jambo moja la kufikiria ni jinsi tunavyomwona na kumtendea ndugu tunapokosana naye. Kwa mfano, tuseme kwamba Mkristo amekuudhi au amekosana na mtu wako wa ukoo. Ikiwa una “sababu ya kulalamika,” je, utamwekea kinyongo, na kukataa kumsamehe au kutojaribu kutatua tatizo hilo? (Wakolosai 3:13; Yoshua 22:9-30; Mathayo 5:23, 24) Kufanya hivyo kunaweza kuathiri jinsi unavyomtendea ndugu yako; unaweza kumwonyesha ubaridi, kumwepuka au kuongea vibaya kumhusu. Au tuseme kwamba baadaye ndugu huyo anakosea, labda hata anahitaji kushauriwa au kurekebishwa na wazee wa kutaniko. (Wagalatia 6:1) Je, ungeonyesha roho kama ya Waedomu kwa kushangilia kwa sababu ya tatizo linalomkabili ndugu huyo? Mungu anataka utendeje?
6. Tofauti na Zekaria 7:10, andiko la Mika 7:18 linapendekeza tufanye nini?
6 Yehova alimwongoza Zekaria kusema kwamba hataki ‘tupangiane jambo lolote baya mioyoni mwetu.’ (Zekaria 7:9, 10; 8:17) Shauri hilo linafaa hasa tunapohisi kwamba ndugu ametuumiza au amemkosea mtu fulani katika familia yetu. Katika hali kama hizo, ni rahisi ‘kupangiana jambo baya mioyoni mwetu’ na kuonyesha hivyo kwa matendo. Kwa upande mwingine, Mungu anataka tuige mfano wake mzuri. Kumbuka, Mika aliandika kwamba Yehova ‘anasamehe kosa na kuuachilia ukosaji.’a (Mika 7:18) Tutafanyaje hivyo katika shughuli zetu?
7. Kwa nini tunaweza kuamua kuacha tu makosa tuliyotendewa?
7 Huenda tukaumia moyoni kwa sababu ya jinsi tulivyotendewa au jinsi mtu wetu wa ukoo alivyotendewa, lakini kwa kweli, ni jambo zito kadiri gani? Biblia hutaja hatua za kuchukua tunapokosana, au hata tunapomkosea ndugu. Hata hivyo, mara nyingi ni vizuri kutotilia maanani makosa hayo, au ‘kuuachilia ukosaji.’ Jiulize: ‘Je, hii yaweza kuwa moja kati ya zile mara 77 ambazo ninapaswa kumsamehe? Mbona nisiliache tu kosa hilo?’ (Mathayo 18:15-17, 21, 22) Hata ikiwa kosa linaonekana kuwa kubwa sasa, je, litabaki kubwa miaka 1,000 ijayo? Jifunze jambo muhimu kutokana na maelezo ya Mhubiri 5:20 kuhusu mfanyakazi anayefurahia chakula na kinywaji: “Si mara nyingi atakumbuka siku za maisha yake, kwa maana Mungu wa kweli anamshughulisha kwa shangwe ya moyo wake.” Mtu huyo anapofurahia raha yake ya sasa, husahau matatizo anayokabili katika maisha yake ya kila siku. Je, tunaweza kuiga mtazamo huo? Tukikazia fikira shangwe za undugu wetu wa Kikristo, tunaweza kusahau mambo ambayo ni ya muda tu, yale ambayo hatutakumbuka katika ulimwengu mpya. Kufanya hivyo ni tofauti kabisa na kushangilia wengine wanapokabili matatizo au kukumbuka makosa tuliyotendewa.
Mtu anapokukosea, unapaswa kuepuka kufanya nini?
WAAMBIE WENGINE UKWELI
8. Ni wakati gani inapokuwa vigumu kusema ukweli?
8 Vile vitabu 12 vya kinabii huonyesha pia jinsi Mungu anavyotaka sana tuseme ukweli tunaposhughulika na wengine. Bila shaka, tunajitahidi sana kuwaambia wengine “ile kweli ya habari njema.” (Wakolosai 1:5; 2 Wakorintho 4:2; 1 Timotheo 2:4, 7) Hata hivyo, ni vigumu zaidi kusema ukweli katika mazungumzo yetu ya kila siku pamoja na watu wa familia zetu na ndugu zetu wa kiroho kuhusu hali na mambo mbalimbali. Kwa nini?
9. Ni lini tunapoweza kushawishika kutosema ukweli kamili, lakini tunapaswa kujiuliza nini?
9 Ni nani kati yetu hajawahi kusema au kufanya jambo fulani lisilo la fadhili kisha akajulishwa kosa lake? Inaelekea kwamba tuliaibika au kuhisi hatia. Hisia kama hizo zinaweza kumfanya mtu akatae kosa lake au atoe “sababu” ambayo si ya kweli akijaribu kutetea kosa lake au kuonyesha kwamba mashtaka hayo si ya kweli. Au tunapoona aibu, huenda tukashawishiwa kutaja mambo fulani tu na kuacha yale ambayo yanaonekana kuwa mabaya. Hivyo, mambo tunayosema yanaweza kuwa kweli, hata hivyo huenda yakaeleweka kwa njia tofauti kabisa. Ingawa huenda tusiwe tunasema uwongo waziwazi, kama ilivyo kawaida katika ulimwengu leo, je, kweli tutakuwa ‘tukisema kweli kila mmoja na jirani yake,’ au na ndugu yake? (Waefeso 4:15, 25; 1 Timotheo 4:1, 2) Unafikiri Mungu anahisije Mkristo anaposema mambo kwa njia fulani ya werevu akiwa na nia ya kuwapotosha ndugu zake waamini jambo ambalo si la kweli, au si sahihi?
10. Manabii wanaelezaje hali ambayo ilikuwa imeenea katika Yuda na Israeli la kale?
10 Manabii walitambua kwamba hata wanaume na wanawake walio wakfu kwa Yehova nyakati nyingine hupuuza matakwa yake. Hosea alieleza hisia za Mungu kuelekea watu fulani walioishi siku zake: “Na waporwe, kwa maana wamenikosea! Nami mwenyewe nikachukua hatua ya kuwakomboa, bali wao wenyewe wamesema uwongo juu yangu.” Mbali na kusema uwongo ulio wazi na usioweza kukanushwa kumhusu Yehova, baadhi yao walianza “kutangaza laana na kuzoea kufanya udanganyifu,” labda ili wafiche ukweli na kuwapotosha wengine. (Hosea 4:1, 2; 7:1-3, 13; 10:4; 12:1) Hosea aliandika maneno hayo akiwa katika ufalme wa kaskazini wa Samaria. Je, hali ilikuwa tofauti huko Yuda? Mika ajibu: “Watu wake mwenyewe walio matajiri wamejaa jeuri, na wakaaji wake mwenyewe wamesema uwongo, na ulimi wao una udanganyifu kinywani mwao.” (Mika 6:12) Ni vizuri tuzingatie jinsi manabii hao walivyoshutumu “kuzoea kufanya udanganyifu” na wale ambao “ulimi wao una udanganyifu kinywani mwao.” Kwa hiyo, hata Wakristo, ambao bila shaka hawawezi kusema uwongo kimakusudi, wanapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, nyakati nyingine mimi huzoea udanganyifu au huwa na ulimi wenye udanganyifu kinywani mwangu? Mungu anataka nijiendesheje kuhusiana na mambo hayo?’
11. Manabii wanaonyeshaje mapenzi ya Mungu kuhusiana na usemi wetu?
11 Inapendeza kwamba Mungu aliwatumia manabii hao pia kueleza waziwazi mambo mema anayotaka tufanye. Andiko la Zekaria 8:16 linasema: “Haya ndiyo mambo ambayo mnapaswa kufanya: Semeni ukweli kila mtu na mwenzake. Hukumuni kwa hukumu ya kweli na ya amani malangoni mwenu.” Katika siku za Zekaria eneo la malango lilikuwa sehemu za umma na wanaume wazee walisikiliza kesi katika sehemu hizo. (Ruthu 4:1; Nehemia 8:1) Hata hivyo, Zekaria hakusema kwamba huo ndio uliokuwa wakati pekee wa kusema ukweli. Ni lazima tuwe wanyoofu hadharani, lakini pia tunahimizwa hivi: “Semeni ukweli kila mtu na mwenzake.” Hiyo inatia ndani kusema ukweli nyumbani mwetu tunapozungumza na mwenzi wetu wa ndoa au watu wetu wa ukoo. Inatia ndani pia mazungumzo yetu ya kila siku pamoja na ndugu na dada zetu wa kiroho, iwe tunazungumza nao uso kwa uso, kupitia simu, au tunawasiliana nao kwa njia nyingineyo. Wana kila sababu ya kuamini kwamba yale tunayosema ni ya kweli. Wazazi Wakristo wanapaswa kukazia akilini mwa watoto wao umuhimu wa kutosema uwongo. Kwa njia hiyo watoto wanapokua wataelewa kwamba Mungu anataka waepuke ulimi ulio na udanganyifu na kuwa wanyoofu kabisa katika yale wanayosema.—Sefania 3:13.
12. Tunaweza kujifunza jambo gani muhimu kutokana na vitabu vya manabii?
12 Kijana au mtu mzima anayeshikamana na njia ya kweli anakubaliana na himizo hili la Zekaria: “Pendeni kweli na amani.” (Zekaria 8:19) Zingatia pia maelezo ya Malaki kuhusu sifa ambazo Yehova aliona katika Mwana Wake: “Sheria ya kweli ilikuwa katika kinywa chake, wala ukosefu wa uadilifu haukupatikana midomoni mwake. Kwa amani na kwa unyoofu alitembea nami.” (Malaki 2:6) Bila shaka Yehova anataka tuonyeshe sifa hizo, sivyo? Kumbuka kwamba tuna Neno lake kamili, kutia ndani vitabu vya wale manabii 12 na mambo yote tunayoweza kujifunza kutokana nao.
EPUKA JEURI
13. Andiko la Mika 6:12 linataja tatizo gani lingine lililokuwapo?
13 Andiko la Mika 6:12 linatuambia kwamba njia moja ambayo watu wa kale wa Mungu waliwatendea wengine vibaya ni kwa ‘kusema uwongo, na ulimi wao ulikuwa na udanganyifu kinywani mwao.’ Hata hivyo, andiko hilo linataja tatizo lingine kubwa sana. Linataja kwamba ‘watu walio matajiri walikuwa wamejaa jeuri.’ Jinsi gani, nasi tunaweza kujifunza nini?
14, 15. Rekodi zinaonyesha nini kuhusu jeuri katika mataifa yaliyokuwa karibu na watu wa Mungu?
14 Fikiria jinsi mataifa fulani ambayo yalikuwa karibu na watu wa Mungu yalivyokuwa. Taifa la Ashuru, na jiji lake kuu la Ninawi, lilikuwa upande wa kaskazini-mashariki. Nahumu aliandika hivi kuhusu taifa hilo: “Ole wake jiji la umwagaji wa damu. Limejaa udanganyifu na unyang’anyi. Mawindo hayaondoki!” (Nahumu 3:1) Waashuru walijulikana kwa sababu ya kupigana kwa ukali na kuwatesa kikatili wafungwa wa vita—baadhi ya wafungwa waliteketezwa au kutolewa ngozi wakiwa hai, na wengine walipofushwa au kukatwa pua, masikio, au vidole. Kitabu kimoja (Gods, Graves, and Scholars) kinasema: “Waninawi walijulikana sana kwa sababu ya kuua, kupora, kuwakandamiza watu, na kuwatesa walio dhaifu; kupitia vita na jeuri ya kila namna.” Tuna maneno yaliyosemwa na mtu aliyeshuhudia (na labda hata kushiriki) jeuri hiyo. Baada ya kusikia ujumbe wa Yona, mfalme wa Ninawi alisema hivi kuhusu watu wake: “Nao wajifunike nguo za magunia, mwanadamu na mnyama wa kufugwa; na wamwite Mungu kwa nguvu na warudi, kila mmoja kutoka katika njia yake mbaya na kutoka katika jeuri iliyokuwa mikononi mwao.”—Yona 3:6-8.b
15 Jeuri ilienea katika mataifa mengine mbali na Ashuru. Edomu, lililokuwa kusini-mashariki mwa Yuda lingeadhibiwa pia. Kwa nini? “Nayo Edomu itakuwa nyika ya mahame yenye ukiwa, kwa sababu ya jeuri kwa wana wa Yuda, ambao walimwaga damu isiyo na hatia katika nchi yao.” (Yoeli 3:19) Je, Waedomu walitii onyo hilo na kuacha matendo yao ya jeuri? Karne mbili hivi baadaye, Obadia aliandika hivi: “Wanaume wako wenye nguvu wataingiwa na woga, Ee Temani [jiji la Edomu], . . . Kwa sababu ya jeuri uliyomtendea ndugu yako Yakobo, . . . utakatiliwa mbali mpaka wakati usio na kipimo.” (Obadia 9, 10) Lakini namna gani watu wa Mungu?
16. Amosi na Habakuki wanatufunulia tatizo gani lililokuwapo siku zao?
16 Amosi alieleza jinsi hali ilivyokuwa katika Samaria, jiji kuu la ufalme wa kaskazini: “‘Mwone machafuko mengi yaliyo katikati yake na visa vya upunjaji vilivyo ndani yake. Nao hawajajua jinsi ya kufanya yaliyo manyoofu,’ asema Yehova, ‘wale wanaoweka jeuri akiba na uporaji.’” (Amosi 3:9, 10) Huenda ukadhani kwamba hali ilikuwa tofauti huko Yuda, ambako kulikuwa na hekalu la Yehova. Lakini Habakuki, aliyeishi Yuda, alimuuliza Mungu hivi: “Nitakuomba msaada kutokana na jeuri mpaka wakati gani, nawe usiokoe? Kwa nini unanionyesha jambo lenye kudhuru, nawe unaendelea kutazama taabu tupu? Na kwa nini kuna uporaji na jeuri mbele yangu?”—Habakuki 1:2, 3; 2:12.
17. Kwa nini huenda jeuri ilisitawi miongoni mwa watu wa Mungu?
17 Je, huenda jeuri ilisitawi miongoni mwa watu wa Mungu kwa sababu walijiruhusu waathiriwe na mtazamo wa Ashuru, Edomu, au mataifa mengine kuelekea jeuri? Sulemani alikuwa amewaonya kuhusu jambo hilo: “Usimwonee wivu mtu mwenye jeuri, wala kuchagua yoyote kati ya njia zake.” (Methali 3:31; 24:1) Baadaye, Yeremia alitaja mambo waziwazi: “Yehova amesema hivi: ‘Msijifunze njia ya mataifa hata kidogo.’”—Yeremia 10:2; Kumbukumbu la Torati 18:9.
Katuni na michezo mingi ya video huwapumbaza vijana na kuwafanya wafikiri kwamba jeuri inakubalika
18, 19. (a) Kama Habakuki angekuwa hai leo, angehisije kuhusu jeuri iliyopo leo? (b) Unahisije kuhusu jeuri katika nyakati zetu?
18 Kama Habakuki angekuwa hai leo, je, hangeshtuliwa na jeuri iliyopo leo? Watu wengi huzoea jeuri tangu ujanani. Katuni zinazowafurahisha wavulana na wasichana huonyesha jeuri. Katuni moja hujaribu kuiponda, kuilipua, au kuiangamiza katuni nyingine. Punde si punde, vijana wengi hupiga hatua na kuanza kucheza michezo ya video inayohusisha kuwashinda maadui kwa kuwapiga risasi, kuwalipua, au kuwaangamiza. Baadhi yao huenda wakadai, ‘Hiyo ni michezo tu.’ Hata hivyo, michezo yenye jeuri inayochezwa kwenye kompyuta nyumbani au katika ukumbi wa michezo hiyo huwazoeza wachezaji kutenda jeuri, na huathiri mitazamo na matendo yao. Shauri hili lililoandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu ni la kweli kabisa: “Mtu wa jeuri atamshawishi mwenzake, naye hakika humfanya aende katika njia isiyo njema”!—Methali 16:29.
19 Ingawa Habakuki alilazimika kuendelea kutazama taabu tupu na ‘jeuri iliyokuwa mbele yake,’ mambo hayo yalimhuzunisha sana. Unaweza kujiuliza hivi: ‘Je, angefurahia kuketi pamoja nami na kutazama vipindi vya televisheni ambavyo mimi hutazama kwa ukawaida?’ Pia jiulize, ‘Je, angetenga wakati wa kutazama michezo yenye jeuri, ambayo hata wachezaji huvalia mavazi ya kujikinga kama yale yaliyovaliwa na wale walioshiriki mapigano ya kale ya kufa na kupona?’ Katika michezo fulani, watu wengi husisimuka wanapoona watu wakipigana kijeuri viwanjani au mashabiki wenye fujo wakitwangana. Katika baadhi ya tamaduni, wengi hutazama sinema na video zenye jeuri zinazokazia hasa kupigana vita au karate. Huenda wakadai ni sawa kwa sababu ni mambo ya kihistoria au ni utamaduni wa kale wa taifa, lakini je, sababu hizo zinafanya jeuri ikubalike?—Methali 4:17.
20. Malaki alizungumzia maoni ya Yehova kuhusu jeuri ya aina gani?
20 Malaki anataja zoea lingine la kijeuri anapoeleza maoni ya Yehova kuhusu hila ambayo Wayahudi fulani waliwatendea wake zao. “‘Amechukia talaka,’ Yehova, Mungu wa Israeli, amesema; ‘na yule ambaye amefunika vazi lake kwa jeuri.’” (Malaki 2:16) Maneno ya Kiebrania yaliyotafsiriwa “ambaye amefunika vazi lake kwa jeuri” yameeleweka kwa njia mbalimbali. Wasomi fulani husema kwamba maneno hayo yanamaanisha vazi la mtu kumwagikiwa na damu anapomshambulia mwingine kwa jeuri. Vyovyote vile, kwa wazi Malaki alikuwa akishutumu kumtendea vibaya mwenzi wa ndoa. Naam, Malaki alikuwa akizungumzia jeuri kuelekea washiriki wa familia naye alionyesha kwamba Mungu hakupendezwa na zoea hilo.
21. Wakristo wanapaswa kuepuka jeuri katika hali gani?
21 Jeuri inayofanywa faraghani ndani ya nyumba ya Mkristo, iwe ni kwa maneno au kupitia matendo haikubaliki kama vile jeuri inayofanywa hadharani isivyokubalika. Mungu anaona aina hizo zote za jeuri. (Mhubiri 5:8) Ingawa Malaki alikuwa akizungumza kuhusu mume kumtendea mke jeuri, hakuna andiko lolote la Biblia linalosema kwamba ni sawa kwake kuwatendea jeuri watoto au wazazi wake waliozeeka. Mke pia haruhusiwi kumtendea jeuri mume, watoto, au wazazi wake. Ni kweli kwamba katika familia yenye wanadamu wasiokamilika, wanaweza kukosana, kuchokozana, na nyakati nyingine kuwaka hasira. Hata hivyo, Biblia inatushauri hivi: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.”—Waefeso 4:26; 6:4; Zaburi 4:4; Wakolosai 3:19.
22. Tunajuaje kwamba tunaweza kuepuka jeuri tujapozungukwa na watu wengi wajeuri?
22 Huenda watu fulani wakajitetea wanapotenda jeuri, kwa kusema, ‘Nilizaliwa katika familia yenye jeuri kwa hiyo siwezi kuiepuka,’ au ‘Watu wa jamii yetu au utamaduni wetu ni wakali sana, wanakasirika haraka sana.’ Hata hivyo, Mika alipowashutumu ‘matajiri waliojaa jeuri,’ hakuzungumza nao kana kwamba hawangeweza kuepuka jeuri kwa sababu walilelewa katika mazingira ya jeuri. (Mika 6:12) Noa aliishi wakati ambapo dunia ‘ilikuwa imejaa jeuri,’ na wanawe walilelewa katika mazingira hayo. Je, waliiga matendo hayo ya jeuri? La hasha! ‘Noa alipata kibali machoni pa Yehova,’ na wanawe walimfuata wakaokolewa wakati wa Furiko.—Mwanzo 6:8, 11-13; Zaburi 11:5.
23, 24. (a) Ni nini kinachotusaidia kuepuka kujulikana kuwa watu wajeuri? (b) Yehova anahisije kuhusu wale wanaowatendea wengine kama anavyotaka?
23 Mashahidi wa Yehova wanajulikana duniani pote kuwa watu wanaofanya amani wala si wenye jeuri. Wanaheshimu na kutii sheria za Kaisari zinazopinga matendo ya jeuri. (Waroma 13:1-4) Wamejitahidi ‘kufua panga zao ziwe majembe na mikuki yao kuwa miundu’ nao hujitahidi sana kufuatia amani. (Isaya 2:4) Wanajitahidi kuvaa “utu mpya,” ambao unawasaidia kuepuka jeuri. (Waefeso 4:22-26) Wao huiga mfano mzuri wa wazee Wakristo, ambao hawawezi ‘kuwapiga watu’ kwa maneno au kihalisi.—1 Timotheo 3:3; Tito 1:7.
24 Tunaweza na tunapaswa kuwatendea wengine kama Mungu anavyotaka tuwatendee. Hosea anasema: “Ni nani aliye na hekima, apate kuelewa mambo haya? Mwenye busara, apate kuyajua? Kwa maana njia za Yehova zimenyooka, na waadilifu ndio watakaotembea katika hizo.”—Hosea 14:9.
a Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “kuuachilia ukosaji” kihalisi linamaanisha “kupita kosa.” Kuhusu maneno “kupita kosa,” msomi mmoja anasema kwamba “yanatokana na wazo la msafiri anayepita bila kuona kitu fulani ambacho hataki kukikazia fikira. Haimaanishi [kwamba Mungu haoni dhambi] bali kwamba hakazii uangalifu visa fulani vya dhambi akiwa na nia ya kuadhibu; yeye husamehe badala ya kuadhibu.”
b Jiji la Kala (Nimrud) lililojengwa upya na Ashurnasirpal lilikuwa umbali wa kilometa 35 hivi kusini-mashariki ya Ninawi. Jumba la Makumbusho la Uingereza lina mabamba ya kuta kutoka Kala, na maelezo yake yanasema hivi: “Ashurnasirpal alieleza kinaganaga ukatili na unyama wake katika vita. Wafungwa walinyongwa au kutundikwa mitini kwenye kuta za majiji yaliyoshindwa . . . ; vijana wanaume na wanawake walitolewa ngozi wakiwa hai.”—Archaeology of the Bible.