Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • lv sura 4 kur. 36-49
  • Kwa Nini Tuheshimu Mamlaka?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Tuheshimu Mamlaka?
  • “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KWA NINI NI VIGUMU?
  • KWA NINI TUHESHIMU MAMLAKA?
  • KUONYESHA HESHIMA KATIKA FAMILIA
  • KUONYESHA HESHIMA KATIKA KUTANIKO
  • KUHESHIMU MAMLAKA ZA ULIMWENGU
  • Kwa Nini Unapaswa Kuheshimu Mamlaka?
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Waheshimuni Waliopewa Mamlaka Juu Yenu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Maoni ya Mkristo Kuhusu Mamlaka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Kubali Mamlaka ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
Pata Habari Zaidi
“Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
lv sura 4 kur. 36-49
Baba akifundisha familia yake

SURA YA 4

Kwa Nini Tuheshimu Mamlaka?

“Waheshimuni watu wa namna zote.”—1 PETRO 2:17.

1, 2. (a) Kwa nini ni vigumu kwetu kuheshimu mamlaka? (b) Tutachunguza maswali gani?

JE, UMEPATA kuona jinsi mtoto mdogo anavyotenda anapoambiwa afanye jambo fulani ambalo hataki kulifanya? Sura yake inaweza kuonyesha wazi kabisa kwamba hataki. Anasikia sauti ya mzazi wake, naye anajua kwamba anapaswa kuheshimu mamlaka ya mzazi wake. Lakini katika kisa hiki, hataki kutii. Hali hiyo inafanana sana na hali ambayo kila mmoja wetu anakabili.

2 Si rahisi kuheshimu mamlaka sikuzote. Je, nyakati nyingine wewe huona ni vigumu kuwaheshimu wale walio na mamlaka fulani juu yako? Ikiwa ndivyo, si wewe tu unayepambana na jambo hilo. Leo, watu wengi sana hawaheshimu mamlaka. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba tunahitaji kuwaheshimu wale walio na mamlaka juu yetu. (Methali 24:21) Kwa hakika, lazima tufanye hivyo ikiwa tunataka kukaa katika upendo wa Mungu. Hivyo basi, maswali fulani yanahitaji kujibiwa. Kwa nini inaweza kuwa vigumu sana kwetu kuheshimu mamlaka? Kwa nini Yehova anataka tuheshimu mamlaka, na ni nini kitakachotusaidia kutii? Mwishowe, ni kwa njia gani tunaweza kuonyesha kwamba tunaheshimu mamlaka?

KWA NINI NI VIGUMU?

3, 4. Dhambi na hali ya kutokamilika zilianza jinsi gani, na kwa nini mwelekeo wetu wa kutenda dhambi hufanya iwe vigumu kwetu kuheshimu mamlaka?

3 Acheni tuzungumzie kwa ufupi sababu mbili zinazoonyesha kwa nini inaweza kuwa vigumu sana kwetu kuheshimu wale walio na mamlaka. Kwanza, sisi si wakamilifu; pili, hata wale walio na mamlaka juu yetu si wakamilifu. Dhambi na hali ya kutokamilika ya wanadamu zilianza zamani sana katika bustani ya Edeni wakati ambapo Adamu na Hawa waliasi mamlaka ya Mungu. Kwa hiyo dhambi ya kwanza ilikuwa uasi. Mpaka leo hii tunazaliwa tukiwa na mwelekeo wa kuasi.—Mwanzo 2:15-17; 3:1-7; Zaburi 51:5; Waroma 5:12.

4 Kwa sababu ya mwelekeo wetu wa kutenda dhambi, wengi wetu husitawisha kiburi na majivuno kwa urahisi. Kwa upande mwingine, sifa ya unyenyekevu haipatikani kwa urahisi nasi tunahitaji jitihada nyingi ili kusitawisha na kudumisha sifa hiyo. Hata baada ya kumtumikia Mungu kwa uaminifu kwa miaka mingi, tunaweza kuonyesha ukaidi na kiburi. Kwa mfano, mfikirie Kora. Ijapokuwa alishikamana kwa uaminifu na watu wa Yehova wakati wa dhiki nyingi, alitamani kupata mamlaka zaidi na kwa ushupavu akawachochea watu wamwasi Musa, ambaye alikuwa mwanamume mpole zaidi kuliko watu wote wakati huo. (Hesabu 12:3; 16:1-3) Pia, mfikirie Mfalme Uzia, ambaye alichochewa na kiburi kuingia katika hekalu la Yehova na kufanya kazi takatifu iliyopaswa kufanywa na makuhani tu. (2 Mambo ya Nyakati 26:16-21) Watu hao walipata adhabu kali kwa sababu ya uasi wao. Hata hivyo, sisi sote tunaweza kujifunza mambo muhimu kutokana na mifano yao mibaya. Tunahitaji kupambana na kiburi ambacho hufanya iwe vigumu kwetu kuheshimu mamlaka.

5. Ni kwa njia gani wanadamu wasio wakamilifu wametumia mamlaka yao vibaya?

5 Kwa upande mwingine, wanadamu wasio wakamilifu ambao wana mamlaka wamechangia sana kutoheshimiwa kwa mamlaka. Wengi wao wamekuwa wakatili, wenye kukandamiza, na wametawala kwa mabavu. Katika sehemu kubwa ya historia ya wanadamu, mamlaka imetumiwa vibaya. (Mhubiri 8:9) Kwa mfano, Sauli alikuwa mtu mzuri na mnyenyekevu Yehova alipomchagua awe mfalme. Lakini, alishindwa na kiburi na wivu; kisha akamtesa Daudi ambaye alikuwa mwaminifu. (1 Samweli 9:20, 21; 10:20-22; 18:7-11) Baadaye, Daudi akawa mmoja wa wafalme bora wa Israeli, lakini akatumia mamlaka yake vibaya alipomchukua mke wa Uria Mhiti na kuagiza mtu huyo asiye na hatia awekwe kwenye mstari wa mbele vitani ili auawe. (2 Samweli 11:1-17) Ndiyo, hali ya kutokamilika inafanya iwe vigumu kwa watu kutumia mamlaka vizuri. Na ikiwa wale walio na mamlaka hawamheshimu Yehova, wanatumia mamlaka yao vibaya hata zaidi. Baada ya kueleza jinsi mapapa fulani wa Katoliki walivyoanzisha mateso yaliyoenea sana, kiongozi mmoja wa Uingereza aliandika: “Mamlaka inaharibu watu, na mamlaka kamili inawaharibu kabisa.” Tukiwa na hilo akilini, acheni tufikirie swali hili: Kwa nini tunapaswa kuheshimu mamlaka?

KWA NINI TUHESHIMU MAMLAKA?

6, 7. (a) Kumpenda Yehova kunatuchochea kufanya nini, na kwa nini? (b) Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tuna sifa ya kujitiisha?

6 Sababu kuu za kuheshimu mamlaka zinatokana na upendo—kumpenda Yehova, kuwapenda wanadamu wenzetu, na hata kujipenda wenyewe. Kwa sababu tunampenda Yehova kuliko mtu mwingine yeyote, tunataka kuufurahisha moyo wake. (Methali 27:11; Marko 12:29, 30) Tunajua kwamba enzi kuu yake, haki yake ya kutawala ulimwengu, ilitiliwa shaka duniani tangu uasi ulipotokea Edeni. Pia, tunajua kwamba wanadamu wengi wamemuunga mkono Shetani na kuukataa utawala wa Yehova. Sisi, tunafurahi kuwa upande wa Yehova. Tunaposoma maneno yenye kusisimua ya Ufunuo 4:11, mioyo yetu inasisimuka kwelikweli. Hatuna shaka lolote kwamba Yehova ndiye mwenye haki ya kuwa Mtawala wa ulimwengu! Tunaiunga mkono enzi kuu ya Yehova na kuukubali utawala wake kila siku maishani mwetu.

7 Heshima hiyo inatuchochea kufanya mengi zaidi ya kutii tu. Bila shaka, tunamtii Yehova kwa hiari kwa sababu tunampenda. Hata hivyo, kuna nyakati ambapo itakuwa vigumu sana kwetu kutii. Nyakati hizo, kama yule mvulana aliyetajwa mwanzoni, tunahitaji kujifunza kujitiisha. Tunakumbuka kwamba Yesu alijitiisha kwa mapenzi ya Baba yake hata ilipoonekana kuwa vigumu sana. Alimwambia hivi Baba yake: “Acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.”—Luka 22:42.

8. (a) Kujitiisha chini ya mamlaka ya Yehova leo kunahusisha nini, na ni nini kinachoonyesha maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo? (b) Ni nini kinachoweza kutusaidia kusikiliza shauri na kukubali nidhamu? (Ona sanduku “Sikiliza Shauri na Kukubali Nidhamu.”)

8 Bila shaka, Yehova hazungumzi na mtu mmoja-mmoja leo; anatumia Neno lake na wanadamu wanaomwakilisha duniani. Hivyo, mara nyingi tunajitiisha kwa mamlaka ya Yehova kwa kuwaheshimu wanadamu ambao ameweka au ambao ameruhusu waendelee kuwa na mamlaka juu yetu. Tukiasi mwongozo wao—kwa mfano kwa kukataa wanapotushauri na kuturekebisha kwa kutumia Maandiko—tunamchukiza Mungu. Waisraeli waliponung’unika na kumwasi Musa, Yehova aliona kwamba walikuwa wakimnung’unikia na kumwasi yeye mwenyewe.—Hesabu 14:26, 27.

9. Kuwapenda wanadamu wenzetu kunatuchochea jinsi gani kuheshimu mamlaka? Toa mfano.

9 Pia, tunaheshimu mamlaka kwa sababu tunawapenda wanadamu wenzetu. Jinsi gani? Wazia kwamba wewe ni askari katika jeshi. Ili jeshi hilo lifanikiwe na hata kuokoka, kila askari anahitaji kuwa na moyo wa ushirikiano, kutii, na kuheshimu maofisa mbalimbali wenye mamlaka. Ikiwa ungeasi mamlaka hiyo, hilo linaweza kuhatarisha askari wengine wote. Ni kweli kwamba majeshi ya wanadamu yanasababisha uharibifu mwingi ulimwenguni leo. Hata hivyo, Yehova ana majeshi ambayo kazi yake ni kuwasaidia watu. Katika mamia ya maandiko, Mungu anatajwa kuwa “Yehova wa majeshi.” (1 Samweli 1:3) Yeye ndiye Amiri-Jeshi wa viumbe wengi wa roho wenye nguvu. Nyakati nyingine, Yehova anawalinganisha watumishi wake walio duniani na jeshi. (Zaburi 68:11; Ezekieli 37:1-10) Tukiasi mwongozo wa wanadamu ambao Yehova amewapa mamlaka juu yetu, je, hatuhatarishi askari wenzetu katika vita vya kiroho? Mkristo anapoasi mwongozo wa wazee waliowekwa rasmi, wengine katika kutaniko wanaweza kuumia. (1 Wakorintho 12:14, 25, 26) Mtoto anapoasi, familia yote inaweza kuumia. Kwa hiyo, tunaonyesha tunawapenda wanadamu wenzetu tunapokuza roho ya heshima na ushirikiano.

10, 11. Ni jambo gani lingine linalotuchochea kutii mamlaka?

10 Pia, tunaheshimu mamlaka kwa sababu sisi wenyewe tunafaidika. Yehova anapotuagiza tuheshimu mamlaka, mara nyingi anataja faida tutakazopata tunapofanya hivyo. Kwa mfano, anawaambia watoto wawatii wazazi wao ili waishi kwa muda mrefu na kwa furaha. (Kumbukumbu la Torati 5:16; Waefeso 6:2, 3) Anatuagiza tuwaheshimu wazee wa kutaniko kwa sababu kutofanya hivyo kutatuletea madhara ya kiroho. (Waebrania 13:7, 17) Naye anatuambia tutii mamlaka za ulimwengu kwa faida yetu wenyewe.—Waroma 13:4.

11 Je, hukubali kwamba kujua kwa nini Yehova anataka tutii kunatusaidia kuheshimu mamlaka? Basi, acheni sasa tuchunguze jinsi tunavyoweza kuheshimu mamlaka katika sehemu tatu muhimu za maisha yetu.

KUONYESHA HESHIMA KATIKA FAMILIA

12. Yehova amempa mume au baba jukumu gani katika familia, na mwanamume anaweza kulitimiza jukumu hilo jinsi gani?

12 Yehova mwenyewe ndiye aliyeanzisha mpango wa familia. Kwa kuwa yeye ni Mungu wa utaratibu, ameweka utaratibu katika familia ili mambo yawe shwari. (1 Wakorintho 14:33) Amempa mume au baba mamlaka ya kuwa kichwa cha familia. Mume anaonyesha kwamba anaheshimu Kichwa chake, Kristo Yesu, kwa kuiga jinsi Yesu anavyotumia ukichwa wake kusimamia kutaniko. (Waefeso 5:23) Hivyo, mume hapaswi kupuuza jukumu lake bali anapaswa kulitekeleza kwa ujasiri; wala hapaswi kuwa mkatili au mkali, badala yake awe mwenye upendo, mwenye usawaziko, na mwenye fadhili. Sikuzote, anakumbuka kwamba mamlaka yake ni ya kadiri—haipiti kamwe mamlaka ya Yehova.

Baba Mkristo anaiga jinsi Kristo anavyotumia ukichwa

13. Ni katika njia gani mke au mama anaweza kutimiza jukumu lake katika familia kwa njia inayompendeza Yehova?

13 Mke au mama anapaswa kuwa msaidizi au kikamilisho cha mume. Yeye pia amepewa mamlaka katika familia kwa kuwa Biblia hutaja “sheria ya mama yako.” (Methali 1:8) Bila shaka, mamlaka yake iko chini ya mamlaka ya mume wake. Mke Mkristo huonyesha kwamba anaheshimu mamlaka ya mume wake kwa kumsaidia atimize jukumu lake akiwa kichwa cha familia. Hamdharau, hatumii hila ili kumshawishi, wala hajaribu kunyakua mamlaka yake. Badala yake, anamuunga mkono na kushirikiana naye. Mume anapofanya maamuzi ambayo hayampendezi, anaweza kueleza maoni yake kwa heshima, lakini bado ataendelea kujitiisha kwake. Ikiwa mume wake si mwamini, huenda hali ikawa ngumu, hata hivyo, kujitiisha kwake kunaweza kumchochea mume wake amtafute Yehova.—1 Petro 3:1.

Baba mwenye upendo akimrekebisha mwanae aliyeleta matope ndani ya nyumaba

14. Ni kwa njia gani watoto wanaweza kuwafanya wazazi wao na Yehova wawe na shangwe?

14 Watoto hufurahisha moyo wa Yehova wanapotii baba na mama yao. Pia wanawaletea wazazi wao sifa na shangwe. (Methali 10:1) Katika familia za mzazi mmoja, watoto hufuata kanuni hiyohiyo ya utii wakikumbuka kwamba mzazi huyo anahitaji hata zaidi utegemezo na ushirikiano wao. Familia ambazo washiriki wote wanatimiza majukumu waliyopewa na Mungu huwa na amani na shangwe nyingi. Hilo linamletea sifa Mwanzilishi wa familia zote, Yehova Mungu.—Waefeso 3:14, 15.

KUONYESHA HESHIMA KATIKA KUTANIKO

15. (a) Katika kutaniko, ni kwa njia gani tunaweza kuonyesha kwamba tunaheshimu mamlaka ya Yehova? (b) Ni kanuni gani zinazoweza kutusaidia kuwatii wale wanaoongoza? (Ona sanduku “Watiini Wale Wanaoongoza.”)

15 Yehova amemweka Mwana wake kuwa Mtawala wa kutaniko la Kikristo. (Wakolosai 1:13) Naye Yesu amempa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” mgawo wa kushughulikia mahitaji ya kiroho ya watu wa Mungu walio duniani. (Mathayo 24:45-47) Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova linawakilisha jamii ya mtumwa huyo. Kama ilivyokuwa katika makutaniko ya Kikristo ya karne ya kwanza, leo wazee wanapokea maagizo na mashauri kutoka kwa Baraza Linaloongoza, moja kwa moja au kupitia wawakilishi wake, kama vile waangalizi wanaosafiri. Tunapoheshimu mamlaka ya wazee Wakristo tukiwa mtu mmoja-mmoja, tunamtii Yehova.—Waebrania 13:17.

16. Ni katika njia gani wazee wanawekwa na roho takatifu?

16 Wazee na watumishi wa huduma si wakamilifu. Kama sisi, wanaweza kukosea pia. Hata hivyo, wazee ni “zawadi katika wanadamu,” ambao wameandaliwa ili kulisaidia kutaniko liendelee kuwa imara kiroho. (Waefeso 4:8) Wazee wanawekwa na roho takatifu. (Matendo 20:28) Jinsi gani? Kwa sababu lazima kwanza watimize matakwa yaliyoandikwa katika Neno la Mungu lililoongozwa na roho. (1 Timotheo 3:1-7, 12; Tito 1:5-9) Pia, wazee wanaochunguza sifa za kustahili za ndugu husali kwa bidii ili roho takatifu ya Yehova iwaongoze.

17. Kwa nini wanawake Wakristo nyakati nyingine wanajifunika kichwa wanaposhughulikia mambo fulani ya kutaniko?

17 Katika kutaniko, huenda nyakati nyingine kusiwe na wazee au watumishi wa huduma wa kushughulikia migawo ambayo kwa kawaida ni kazi yao, kama vile kuongoza mkutano wa utumishi wa shambani. Katika nyakati kama hizo, ndugu wengine ambao wamebatizwa wanaweza kutimiza migawo hiyo. Ikiwa hakuna ndugu wowote, basi dada Wakristo wanaostahili wanaweza kushughulikia migawo hiyo. Hata hivyo, mwanamke anaposhughulikia mgawo ambao kwa kawaida hushughulikiwa na mwanamume aliyebatizwa, anapaswa kujifunika kichwa.a (1 Wakorintho 11:3-10) Takwa hilo haliwavunjii heshima wanawake. Badala yake linawapa nafasi ya kuonyesha kwamba wanaheshimu mpango wa Yehova wa ukichwa katika familia na katika kutaniko.

KUHESHIMU MAMLAKA ZA ULIMWENGU

18, 19. (a) Fafanua kanuni zilizo katika Waroma 13:1-7. (b) Ni kwa njia gani tunaonyesha kwamba tunaheshimu mamlaka za ulimwengu?

18 Wakristo wa kweli wanajitahidi sana kufuata kanuni zilizo katika Waroma 13:1-7. Unaposoma mistari hiyo, unaweza kuona kwamba “mamlaka zilizo kubwa” zinazotajwa ni serikali za ulimwengu. Maadamu Yehova anaruhusu serikali hizo za ulimwengu ziendelee kuwapo, zinatimiza mambo muhimu, zikidumisha utaratibu kwa kadiri fulani na kutoa huduma zinazohitajiwa. Tunaonyesha kwamba tunaheshimu mamlaka hizo kwa kutii sheria. Tunahakikisha kwamba tunalipa kodi zozote tunazodaiwa, kujaza kwa usahihi fomu au karatasi zozote zinazohitajiwa na serikali, na kutii sheria zozote zinazotuhusu sisi, familia yetu, biashara yetu, au mali yetu. Hata hivyo, hatuwezi kutii mamlaka za ulimwengu zinapotuagiza tusimtii Mungu. Badala yake tunasema kama mitume wa kale walivyosema: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:28, 29; Ona sanduku “Ni Mamlaka ya Nani Ninayopaswa Kutii?”.

NI MAMLAKA YA NANI NINAYOPASWA KUTII?

Kanuni: “Yehova ni Mwamuzi wetu, Yehova ni Mpaji-sheria wetu, Yehova ni Mfalme wetu.”—Isaya 33:22.

Jiulize

  • Nitafanya nini nikiagizwa nivunje viwango vya Yehova?—Mathayo 22:37-39; 26:52; Yohana 18:36.

  • Nitafanya nini nikiagizwa niache kushika amri za Yehova?—Matendo 5:27-29; Waebrania 10:24, 25.

  • Ni nini kinachoweza kunisaidia kuwatii kutoka moyoni wale walio na mamlaka juu yangu?—Waroma 13:1-4; 1 Wakorintho 11:3; Waefeso 6:1-3.

19 Pia, tunaheshimu mamlaka za ulimwengu kupitia mwenendo wetu. Nyakati nyingine, huenda tukashughulika moja kwa moja na maofisa wa serikali. Mtume Paulo alishughulika na watawala kama Mfalme Herode Agripa na Gavana Festo. Watu hao walikuwa na udhaifu mkubwa, lakini Paulo alizungumza nao kwa heshima. (Matendo 26:2, 25) Tunaiga mfano wa Paulo, iwe ofisa tunayezungumza naye ni mtawala mwenye mamlaka kubwa au ni polisi. Shuleni, vijana Wakristo wanajitahidi kuwaheshimu walimu, maofisa, na wafanyakazi wa shule. Bila shaka, hatuwaheshimu tu wale wanaokubali imani yetu; tunaonyesha heshima pia tunaposhughulika na watu ambao wanawapinga Mashahidi wa Yehova. Kwa kweli, watu ambao si waamini wanapaswa kutambua kwamba tuna heshima.—Waroma 12:17, 18; 1 Petro 3:15.

20, 21. Ni faida gani tunazopata kwa kuheshimu mamlaka?

20 Tusiwe wachoyo katika kuwaonyesha wengine heshima. Mtume Petro aliandika hivi: “Waheshimuni watu wa namna zote.” (1 Petro 2:17) Watu wanapotambua kwamba tunawaheshimu kikweli, wanaweza kuchochewa sana. Kumbuka kwamba sifa hiyo inazidi kuwa haba. Hivyo, kuwa wenye heshima ni njia moja ya kutii amri hii ya Yesu: “Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili wapate kuona matendo yenu mazuri na kumpa utukufu Baba yenu aliye mbinguni.”—Mathayo 5:16.

21 Katika ulimwengu huu wenye giza, watu wenye moyo mzuri wanavutwa kwenye nuru ya kiroho. Kwa hiyo, tunapoonyesha heshima katika familia, katika kutaniko, na kwa mamlaka za ulimwengu, tunaweza kuwavutia wengine na kuwachochea waanze kutembea pamoja nasi katika nuru. Hilo ni jambo zuri kama nini! Hata lisipotukia, tuna hakika ya jambo moja. Kuwaheshimu wanadamu kunampendeza Yehova Mungu na kunatusaidia kukaa katika upendo wake. Hakuna thawabu kubwa kuliko hiyo!

a Nyongeza “Kufunika Kichwa—Wakati Gani na kwa Nini?” inazungumzia jinsi kanuni hiyo inavyoweza kutumiwa katika visa mbalimbali.

“SIKILIZA SHAURI NA KUKUBALI NIDHAMU”

Roho ya Shetani—mtazamo wake wa uasi na ushindani—imejaa ulimwenguni leo. Ndiyo sababu Biblia inamwita Shetani “mtawala wa mamlaka ya hewa, roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii.” (Waefeso 2:2) Watu wengi leo hawataki kuwa chini ya mamlaka yoyote. Inasikitisha kwamba roho hiyo ya kujitegemea hata imeathiri wengine katika kutaniko la Kikristo. Kwa mfano, mzee anaweza kutoa shauri kwa fadhili kuhusu hatari za burudani yenye upotovu wa kingono au jeuri, lakini huenda wengine wakapinga au hata kuchukizwa na shauri hilo. Kila mmoja wetu anahitaji kutenda kupatana na maneno yaliyo katika Methali 19:20: “Sikiliza shauri na kukubali nidhamu, ili upate kuwa na hekima katika wakati wako ujao.”

Ni nini kinachoweza kutusaidia kufanya hivyo? Fikiria sababu tatu za kawaida zin azowafanya watu wakatae shauri au nidhamu, kisha uone maoni ya Kimaandiko kuhusu sababu hizo.

  • “Sidhani shauri hilo linafaa.” Huenda tukahisi kwamba shauri fulani halifai hali zetu au labda anayetoa shauri hilo haelewi kabisa hali zetu. Huenda hata tukalipuuza shauri lenyewe. (Waebrania 12:5) Kwa kuwa sisi sote hatujakamilika, je, inawezekana kwamba sisi ndio tunaohitaji kubadili maoni yetu? (Methali 19:3) Je, kweli shauri hilo lilitolewa bure tu au kulikuwa na sababu fulani? Ikiwa kulikuwa na sababu, basi tunapaswa kuikazia fikira. Neno la Mungu linatushauri hivi: “Shika nidhamu; usiiache. Ilinde, kwa maana hiyo ndiyo uzima wako.”—Methali 4:13.

  • “Sipendi jinsi shauri hilo lilivyotolewa.” Ni kweli kwamba Neno la Mungu linaonyesha jinsi ambavyo shauri linapaswa kutolewa. (Wagalatia 6:1) Hata hivyo, Biblia inasema pia: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Hivyo, mtu mkamilifu tu ndiye anayeweza kutupa shauri linalofaa kabisa hali zetu na linalotolewa kwa njia inayofaa. (Yakobo 3:2) Yehova anatumia wanadamu wasio wakamilifu kutushauri, kwa hiyo si jambo la hekima kukazia fikira jinsi ambavyo shauri linatolewa. Badala yake, kazia fikira shauri lenyewe na usali ili upate msaada wa kulitumia.

  • “Hastahili hata kidogo kunishauri!” Tukifikiri kwamba udhaifu wa yule anayetushauri unafanya shauri lake lisifae, tunahitaji kukumbuka mambo yaliyotajwa juu. Vivyo hivyo, ikiwa tunafikiri kwamba hatuhitaji kushauriwa kwa sababu ya umri, uzoefu, au majukumu yetu katika kutaniko, tunahitaji kurekebisha maoni yetu. Katika Israeli la kale, mfalme alikuwa na majukumu makubwa, lakini alihitaji kukubali shauri kutoka kwa manabii, makuhani, na wengine waliokuwa raia zake. (2 Samweli 12:1-13; 2 Mambo ya Nyakati 26:16-20) Leo, tengenezo la Yehova linawaweka wanaume wasio wakamilifu ili watoe mashauri, na Wakristo wakomavu hukubali na kutumia mashauri hayo bila kulazimishwa. Ikiwa tuna majukumu makubwa au uzoefu mwingi kuliko wengine, tunapaswa kutambua kwamba tunahitaji hata zaidi kuweka mfano mzuri kwa kuwa wenye usawaziko na wanyenyekevu kwa kukubali na kutumia shauri.—1 Timotheo 3:2, 3; Tito 3:2.

Kwa kweli, hakuna yeyote kati yetu asiyehitaji shauri. Kwa hiyo, na tuazimie kukubali shauri kwa hiari, kulitumia, na kumshukuru Yehova kutoka moyoni kwa zawadi hiyo inayookoa uhai. Kwa hakika, mashauri ni wonyesho wa kwamba Yehova anatupenda, nasi tunataka kubaki katika upendo wa Mungu.—Waebrania 12:6-11.

“WATIINI WALE WANAOONGOZA”

Katika Israeli la kale, kulikuwa na uhitaji mkubwa wa usimamizi. Akiwa peke yake, Musa hangeweza kusimamia mamilioni ya watu waliokuwa wakisafiri pamoja katika nyika hatari. Alifanya nini? “Musa akachagua wanaume wenye uwezo kutoka Israeli lote na kuwapa vyeo vya kuwa vichwa juu ya watu, kuwa wakuu wa maelfu, wakuu wa mamia, wakuu wa 50 na wakuu wa makumi.”—Kutoka 18:25.

Leo pia, kuna uhitaji wa usimamizi katika kutaniko la Kikristo. Ndiyo sababu kikundi cha utumishi wa shambani kina mwangalizi, kutaniko lina wazee, makutaniko kadhaa yana mwangalizi wa mzunguko, na nchi ina Halmashauri ya Nchi au Halmashauri ya Tawi. Kwa sababu ya utaratibu huo, kila mwanamume ambaye ni mchungaji anaweza kuwatunza kwa uangalifu kondoo wa Yehova aliopewa awatunze. Wachungaji hao wana wajibu mbele za Yehova na Kristo.—Matendo 20:28.

Ili utaratibu huo ufaulu, kila mmoja wetu anapaswa kuwa mtiifu na mwenye kujitiisha. Hatupaswi kamwe kuwa kama Diotrefe ambaye hakuwaheshimu hata kidogo wale waliokuwa wakiongoza katika siku zake. (3 Yohana 9, 10) Badala yake tunapaswa kutii maneno ya mtume Paulo, aliyeandika: “Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee, kwa maana wanaendelea kuzilinda nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu; ili wafanye hivyo kwa shangwe na si kwa kuugua, kwa maana kufanya hivyo kungewadhuru ninyi.” (Waebrania 13:17) Watu fulani hutii wanapokubaliana na maelekezo yanayotolewa na wale wanaoongoza lakini hukataa kujitiisha wanapokosa kukubaliana na maelekezo hayo au wakati ambapo hawaelewi ni kwa nini yametolewa. Hata hivyo, kumbuka kwamba kujitiisha kunahusisha kutii hata wakati ambapo hatutaki kufanya hivyo. Hivyo basi, kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Je, mimi hutii na kujitiisha kwa wale wanaoongoza?’

Bila shaka, Neno la Mungu halina orodha ya mipango yote au utaratibu mbalimbali unaohitajiwa ili kuendesha kutaniko. Hata hivyo, Biblia inasema: “Mambo yote na yatendeke kwa adabu na kwa mpango.” (1 Wakorintho 14:40) Baraza Linaloongoza linatii mwongozo huo kwa kuweka utaratibu wa kufuatwa na miongozo inayosaidia kuendesha kutaniko kwa utaratibu na amani. Wanaume Wakristo walio na majukumu mazito wanatimiza sehemu yao kwa kuwa vielelezo katika kutii wanapofuata miongozo iliyowekwa. Pia wanaonyesha kwamba wana “usawaziko” na wako “tayari kutii” wale wanaoongoza. (Yakobo 3:17) Hivyo, katika kila kikundi, kutaniko, mzunguko, na nchi, kuna waamini wenye umoja na wenye utaratibu wanaomwakilisha Mungu mwenye furaha.—1 Wakorintho 14:33; 1 Timotheo 1:11.

Kwa upande mwingine, maneno ya Paulo kwenye Waebrania 13:17 yanaonyesha pia madhara ya roho ya kutotii. Inaweza kufanya ndugu wenye madaraka wafanye kazi yao “kwa kuugua.” Mgawo ambao unapaswa kuonwa kuwa pendeleo la utumishi mtakatifu unaweza kuwa mzigo wakati ambapo ndugu analazimika kushughulika na roho ya uasi na ya kutoshirikiana katika kundi. Hilo linawadhuru “ninyi,” kutaniko zima. Bila shaka, kuna madhara mengine yanayotokea mtu anapokataa kujitiisha kwa utaratibu wa kitheokrasi. Hali yake ya kiroho inaharibika ikiwa ana kiburi mno asiweze kujitiisha, na hilo huweka pengo kati yake na Baba yake wa mbinguni. (Zaburi 138:6) Hivyo basi, sisi sote na tuazimie kuendelea kutii na kujitiisha.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki