Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 7/1 kur. 18-23
  • Maoni ya Mkristo Kuhusu Mamlaka

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maoni ya Mkristo Kuhusu Mamlaka
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Hakuna Mamlaka Ila kwa Njia ya Mungu”
  • Wakristo wa Mapema na Mamlaka za Roma
  • Staha Ifaayo kwa Mamlaka
  • Mamlaka Katika Nyumba za Kikristo
  • Mamlaka Katika Kutaniko
  • Maoni ya Mkristo Juu ya Mamlaka za Juu Zaidi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Ni Mamlaka ya Nani Unayopaswa Kutambua?
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Heshima kwa Mamlaka—Kwa Nini Ni Muhimu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Kwa Nini Tuheshimu Mamlaka?
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 7/1 kur. 18-23

Maoni ya Mkristo Kuhusu Mamlaka

“Hakuna mamlaka ila kwa njia ya Mungu.”—WARUMI 13:1, NW.

1. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba Yehova ndiye mwenye Mamlaka ya Juu Zaidi?

MAMLAKA yafungamana na uumbaji. Aliye Mkuu Zaidi ambaye alianzisha uumbaji wote, ulio hai na usio hai, ni Yehova Mungu. Bila shaka yeye ndiye Mamlaka ya Juu Zaidi. Wakristo wa kweli wana hisia kama zile za viumbe vya kimbingu vinavyotangaza: “Umestahili wewe, Bwana wetu na Mungu wetu, kuupokea utukufu na heshima na uweza; kwa kuwa wewe ndiwe uliyeviumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako, navyo vikaumbwa.”—Ufunuo 4:11.

2. Watawala wa mapema wa kibinadamu walikirije kwa maana fulani kwamba hawakuwa na haki ya kiasili ya kutawala wanadamu wenzao, na Yesu alimwambia Pontio Pilato nini?

2 Lile jambo tu la kwamba wengi wa watawala wa kibinadamu wa nyakati za mapema walijaribu kuhalalisha mamlaka yao kwa kudai kuwa mungu au kuwa wawakilishi wa mungu fulani lilikuwa ni utambuzi wa ukimya kwamba hakuna binadamu alikuwa na haki ya kiasili ya kutawala wanadamu wengine.a (Yeremia 10:23) Chanzo pekee halali cha mamlaka ni Yehova Mungu. Kristo alimwambia Pontio Pilato, gavana Mroma wa Yudea hivi: “Wewe hungekuwa na mamlaka yo yote juu yangu, kama usingepewa kutoka juu.”—Yohana 19:11.

“Hakuna Mamlaka Ila kwa Njia ya Mungu”

3. Mtume Paulo alisema nini kuhusu “mamlaka zilizo kubwa,” na taarifa za Yesu na Paulo zilitokeza maswali gani?

3 Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo waliokuwa wakitawalwa na Milki ya Roma hivi: “Kila nafsi na iwe katika ujitiisho kwa mamlaka zilizo kubwa, kwa maana hakuna mamlaka ila kwa njia ya Mungu; mamlaka zilizopo zimesimama zikiwa zimewekwa na Mungu katika mahali pa vyeo vyazo vyenye kuhusu.” (Warumi 13:1) Yesu alimaanisha nini aliposema kwamba Pilato alikuwa amepewa mamlaka “kutoka juu”? Na ni kwa njia gani Paulo aliona kwamba Mungu aliziweka mamlaka za kisiasa za siku yake mahali pazo? Je! walimaanisha kwamba Yehova mwenyewe anaweka kila mmoja wa mtawala wa kisiasa wa ulimwengu huu?

4. Yesu na Paulo walimwitaje Shetani, na Yesu hakukana dai gani la Shetani?

4 Jambo hilo lingekuwaje kweli ikiwa Yesu alimwita Shetani “mkuu wa ulimwengu huu,” na mtume Paulo akambandika jina “mungu wa dunia hii”? (Yohana 12:31; 16:11; 2 Wakorintho 4:4) Isitoshe, Shetani alipokuwa akimjaribu Yesu, alimtolea “mamlaka” juu ya “falme zote za dunia inayokaliwa,” akidai kwamba mamlaka hiyo imo mikononi mwake. Yesu alikataa toleo lake, lakini hakupinga kwamba hiyo haikuwa mamlaka ya Shetani aipeane.—Luka 4:5-8.

5. (a) Tueleweje maneno ya Yesu na Paulo kuhusu mamlaka ya kibinadamu? (b) Ni kwa maana gani mamlaka zilizo kubwa “zimesimama zikiwa zimewekwa na Mungu katika mahali pa vyeo vyazo”?

5 Yehova alimpa Shetani utawala wa ulimwengu huu kwa kumruhusu aendelee kuishi baada ya yeye kuasi na baada ya kuwajaribu Adamu na Hawa na kuwafanya waasi dhidi ya enzi kuu Yake. (Mwanzo 3:1-6; linganisha Kutoka 9:15, 16.) Kwa hiyo ni lazima maneno ya Yesu na Paulo yamaanishe kwamba baada ya wanadamu wawili wa kwanza katika Edeni kukataa theokrasi, au utawala wa Mungu, Yehova aliruhusu wanadamu waliojitenga wajifanyizie mifumo ya mamlaka ambayo ingewawezesha kuishi katika jamii yenye utaratibu. Nyakati nyingine, Yehova amesababisha watawala fulani au serikali fulani zianguke ili atimize kusudi lake. (Danieli 2:19-21) Ameruhusu wengine waendelee kuwa mamlakani. Juu ya watawala ambao Yehova ameruhusu waendelee kuwapo, yaweza kusemwa kwamba “zimesimama zikiwa zimewekwa na Mungu katika mahali pa vyeo vyazo.”

Wakristo wa Mapema na Mamlaka za Roma

6. Wakristo wa mapema waliwaonaje wenye mamlaka wa Roma, na kwa nini?

6 Wakristo wa mapema hawakujiunga na madhehebu ya Wayahudi waliofanya hila na kupigana na Waroma waliokalia Israeli. Maadamu mamlaka za Waroma, zikiwa na katiba ya kisheria, ziliendeleza utulivu barani na baharini; na kujenga mifereji ya maji, barabara, na madaraja mengi yenye kusaidia sana; na kwa ujumla kushughulikia hali njema ya wote, Wakristo waliziona kuwa ‘mhudumu wa Mungu [au, “mtumishi,” kielezi-chini] kwao kwa faida yao.’ (Warumi 13:3, 4, NW) Sheria na amani zilitokeza hali zilizoruhusu Wakristo kuhubiri habari njema kwa mapana na marefu, kama ilivyoamriwa na Yesu. (Mathayo 28:19, 20) Kwa dhamiri njema, wangelipa kodi zilizotozwa na Waroma, hata kama baadhi ya fedha hizo zilitumiwa kwa makusudi ambayo Mungu hapendelei.—Warumi 13:5-7, NW.

7, 8. (a) Usomaji wa uangalifu wa Warumi 13:1-7 wafunua nini, na muktadha waonyesha nini? (b) Ni katika hali zipi wenye mamlaka za Roma hawakutenda wakiwa “mhudumu wa Mungu,” na katika hali hiyo, Wakristo wa mapema walichukua msimamo gani?

7 Usomaji wa uangalifu wa mistari saba ya kwanza ya Warumi sura ya 13 wafunua kwamba “mamlaka zilizo kubwa” za kisiasa zilikuwa “mhudumu wa Mungu” za kusifu wale watendao mema na kuadhibu wale watendao mabaya. Muktadha (mistari inayozunguka) waonyesha kwamba Mungu, bali si mamlaka zilizo kubwa, ndiye aamuaye yaliyo mema na mabaya. Kwa hiyo, kama maliki wa Roma au mamlaka nyingine ya kisiasa ilitaka mambo ambayo Mungu amekataza yafanywe au, kwa upande mwingine, akataze mambo ambayo Mungu alitaka yafanywe, basi alikoma kuwa mhudumu wa Mungu. Yesu alisema hivi: “Mlipeni Kaisari yaliyo ya Kaisari, na Mungu yaliyo ya Mungu.” (Mathayo 22:21) Kama Taifa la Roma lingetaka kwa lazima yaliyo ya Mungu, kama vile ibada au uhai wa mtu, Wakristo wa kweli walifuata shauri la mitume: “Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29.

8 Kukataa kwa Wakristo wa mapema kuabudu maliki na sanamu, kutokosa kwao mikutano ya Kikristo, na kutoacha kwao kuhubiri habari njema kulifanya wanyanyaswe. Inaaminiwa kwa ujumla kwamba mtume Paulo aliuawa kwa amri za Maliki Nero. Maliki wengine, hasa Domitiani, Markas Aurelio, Septimio Severo, Desio, na Diokletiani, vilevile walinyanyasa Wakristo wa mapema. Maliki hao na mamlaka zilizokuwa chini yao waliponyanyasa Wakristo, kwa hakika hawakuwa wakitenda wakiwa “mhudumu wa Mungu.”

9. (a) Ni jambo gani labaki kuwa kweli juu ya mamlaka zilizo kubwa za kisiasa, na hayawani-mwitu wa kisiasa apokea uwezo na mamlaka kutoka kwa nani? (b) Kwa kupatana na akili, ni jambo gani laweza kusemwa juu ya unyenyekeo wa Kikristo kwa mamlaka zilizo kubwa?

9 Hayo yote yaonyesha kwamba ingawa kwa njia fulani mamlaka zilizo kubwa za kisiasa zatumika kwa njia fulani zikiwa “mpango wa Mungu” ili kudumisha amani miongoni mwa binadamu, bado hizo ni sehemu ya ulimwengu wa mfumo huu wa mambo ambao Shetani ni mungu wao. (1 Yohana 5:19) Hizo ni sehemu ya tengenezo la ulimwenguni pote la kisiasa linalofananishwa na “hayawani-mwitu” wa Ufunuo 13:1, 2, NW. Huyo hayawani-mwitu apokea uwezo wake na mamlaka yake kutoka kwa yule “joka,” Shetani Ibilisi. (Ufunuo 12:9) Kwa hiyo, ni jambo la akili kwamba unyenyekeo wa Wakristo kwa mamlaka kama hizo ni wa kadiri, si kamili.—Linganisha Danieli 3:16-18.

Staha Ifaayo kwa Mamlaka

10, 11. (a) Paulo alionyeshaje kwamba twapaswa kustahi watu wenye mamlaka, wawe wanastahili staha hiyo au la? (b) Ni kwa njia gani na kwa nini sala zaweza kutolewa “kwa ajili ya wafalme na wote wenye mamlaka”?

10 Lakini, hilo halimaanishi kwamba Wakristo wasitawishe mtazamo wa kishupavu na wa ukaidi kuelekea mamlaka zilizo kubwa za kisiasa. Ni kweli kwamba huenda wengi wa watu hao hasa wasistahili staha kwa jinsi wanavyoishi maisha zao za faraghani na hata za hadharani. Lakini, mitume, kwa kielelezo chao na shauri lao, walionyesha kwamba watu walio na mamlaka wapaswa kustahiwa. Wakati Paulo aliletwa mbele ya Mfalme Herode Agrippa 2 ambaye alikuwa mgoni wa maharimu, alisema naye kwa heshima iliyofaa.—Matendo 26:2, 3, 25.

11 Paulo hata alisema kwamba ilikuwa sawa kutaja mamlaka za kilimwengu katika sala zetu, hasa wakati wana wajibu wa kufanya maamuzi yanayohusu maisha zetu na utendaji wa Kikristo. Yeye aliandika hivi: “Basi, kabla ya mambo yote, nataka dua, na sala, na maombezi, na shukrani, zifanyike kwa ajili ya watu wote; kwa ajili ya wafalme na wote wenye mamlaka, tuishi maisha ya utulivu na amani, katika utauwa wote na ustahivu. Hili ni zuri, nalo lakubalika mbele za Mungu Mwokozi wetu; ambaye hutaka watu wote waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli.” (1 Timotheo 2:1-4) Mitazamo yetu yenye staha kwa mamlaka kama hizo yaweza kufanya waturuhusu kuendeleza kwa uhuru zaidi kazi yetu ya kujaribu kuokoa “watu wote.”

12, 13. (a) Petro alitoa shauri gani lenye usawaziko kuhusu mamlaka? (b) Twaweza kuzibaje “vinywa vya ujinga vya watu wapumbavu” wanaotokeza chuki dhidi ya Mashahidi wa Yehova?

12 Mtume Petro aliandika hivi: “Tiini kila kiamriwacho na watu, kwa ajili ya Bwana; ikiwa ni mfalme, kama mwenye cheo kikubwa; ikiwa ni wakubwa, kama wanaotumwa naye ili kuwalipiza kisasi watenda mabaya na kuwasifu watenda mema. Kwa sababu ndiyo mapenzi ya Mungu, kwamba kwa kutenda mema mzibe vinywa vya ujinga vya watu wapumbavu; kama walio huru, ila wasioutumia uhuru huo kwa kusitiri ubaya, bali kama watumwa wa Mungu. Waheshimuni watu wote. Wapendeni ndugu. Mcheni Mungu. Mpeni heshima mfalme.” (1 Petro 2:13-17) Ni shauri lenye usawaziko kama nini! Tuna deni la kunyenyekea Mungu kabisa tukiwa watumwa wake, na tunanyenyekea kwa kadiri na kwa staha mamlaka za kisiasa zinazotumiwa kuwalipiza kisasi watenda mabaya.

13 Imeonekana kwamba mamlaka nyingi za kilimwengu zinaona Mashahidi wa Yehova kwa njia ya kimakosa sana. Hiyo hutukia kwa sababu wamearifiwa habari zisizo za kweli na maadui waovu wa watu wa Mungu. Ama huenda ikawa kwamba wanatujua tu kutokana na mambo wanayosikia kwa vyombo vya habari, ambazo nyakati nyingine hazitupendelei. Wakati mwingine twaweza kutuliza chuki hiyo kwa mtazamo wetu wenye staha na, popote pale iwezekanapo, kuandalia wenye mamlaka ufafanuzi halisi wa kazi na itikadi za Mashahidi wa Yehova. Kwa maofisa wenye shughuli nyingi, ile broshua Mashahidi wa Yehova Katika Karne ya 20 yaandaa maelezo yanayofaa. Kwa habari kamili, wao waweza kupewa kitabu Jehovah’s Witnesses—Proclaimers of God’s Kingdom, kitabu kifaacho kinachostahili kuwekwa katika maktaba za sehemu za kwenu na za umma.

Mamlaka Katika Nyumba za Kikristo

14, 15. (a) Kuna msingi gani wa mamlaka iliyoko katika nyumba ya Kikristo? (b) Wanawake Wakristo wapaswa kuwa na mtazamo gani kwa waume zao, na kwa nini?

14 Kama Wakristo wanahitajiwa na Mungu waonyeshe staha ifaayo kwa mamlaka za kilimwengu, bila shaka wao wapaswa vilevile kustahi mfumo wa mamlaka iliyowekwa na Mungu katika nyumba za Kikristo. Mtume Paulo aliorodhesha kwa maneno rahisi kanuni ya ukichwa inayotumiwa miongoni mwa watu wa Yehova. Yeye aliandika hivi: “Nataka mjue ya kuwa kichwa cha kila mwanamume ni Kristo, na kichwa cha mwanamke ni mwanamume, na kichwa cha Kristo ni Mungu.” (1 Wakorintho 11:3) Hiyo ni kanuni ya theokrasi, au utawala wa Mungu. Hiyo yahusisha nini?

15 Staha kwa theokrasi huanza nyumbani. Mke Mkristo ambaye hastahi ifaavyo mamlaka ya mume wake—mume awe ni mwamini mwenzake au asiwe—hafuati theokrasi. Paulo aliwashauri hivi Wakristo: ‘Nyenyekeeni katika kicho cha Kristo. Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu. Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili. Lakini kama vile Kanisa limtiivyo Kristo, vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo.’ (Waefeso 5:21-24) Kama vile ni lazima wanaume Wakristo wanyenyekee ukichwa wa Kristo, wanawake Wakristo wapaswa waone hekima ya kunyenyekea mamlaka za waume zao zitokazo kwa Mungu. Jambo hilo litawaletea uradhi wa kindani na, muhimu zaidi, baraka za Yehova.

16, 17. (a) Watoto waliolelewa katika nyumba za Kikristo waweza kujitofautishaje na vijana wengi leo, nao wana kichocheo gani? (b) Yesu alikuwaje kielelezo chema kwa vijana leo, nao wanatiwa moyo wafanye nini?

16 Watoto wenye kufuata theokrasi hufurahi kustahi wazazi wao ifaavyo. Kuhusu kizazi cha vijana katika siku za mwisho, ilitabiriwa kwamba wangekuwa “wasiotii wazazi wao.” (2 Timotheo 3:1, 2) Lakini kwa watoto wa Kikristo Neno la Mungu lililovuviwa lasema hivi: “Ninyi watoto, watiini wazazi wenu katika mambo yote; maana jambo hili lapendeza katika Bwana.” (Wakolosai 3:20) Kustahi mamlaka ya mzazi humfurahisha Yehova na huleta baraka zake.

17 Jambo hilo laonyeshwa na kisa cha Yesu. Simulizi la Luka laeleza hivi: “Akashuka pamoja nao [wazazi wake] mpaka Nazareti, naye alikuwa akiwatii; . . . Naye Yesu akazidi kuendelea katika hekima na kimo, akimpendeza Mungu na wanadamu.” (Luka 2:51, 52) Yesu alikuwa na miaka 12 wakati huo, na namna ya neno la kitenzi la Kigiriki lililotumiwa hapo lakazia kwamba ‘aliendelea kuwatii’ wazazi wake. Kwa hiyo hakuacha unyenyekeo wake alipokuja kuwa tineja. Vijana wakitaka kufanya maendeleo kiroho na kwa kumpendeza Yehova na watu wanaomhofu Mungu, basi utaonyesha staha kwa mamlaka ya nyumbani na ya nje pia.

Mamlaka Katika Kutaniko

18. Ni nani Kichwa cha kutaniko la Kikristo, naye amewapa nani mamlaka?

18 Akizungumzia uhitaji wa utaratibu katika kutaniko la Kikristo, Paulo aliandika hivi: “Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani. . . . Mambo yote na yatendeke kwa uzuri na kwa utaratibu [au, “kwa kupatana na utaratibu,” kielezi-chini, NW].” (1 Wakorintho 14:33, 40) Ili mambo yote yatendeke kwa njia ya utaratibu, Kristo, aliye Kichwa cha kutaniko la Kikristo, amewapa mamlaka wanaume wenye imani. Twasoma hivi: “Alitoa wengine kuwa mitume; na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti; na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke . . . Lakini tuishike kweli katika upendo na kukua hata tumfikie yeye katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo.”—Waefeso 4:11, 12, 15.

19. (a) Kristo ameweka nani kuwa juu ya mali yake yote duniani, naye amewapa nani mamlaka ya kipekee? (b) Ni kupeana gani kwa mamlaka kunakofanyika katika kutaniko la Kikristo, na jambo hilo lamaanisha tufanye nini kwa upande wetu?

19 Katika wakati huu wa mwisho, Kristo ameweka rasmi jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” juu ya “vitu vyake vyote,” au masilahi ya Ufalme duniani. (Mathayo 24:45-47) Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, mtumwa huyu anawakilishwa na baraza linaloongoza la wanaume Wakristo waliotiwa mafuta ambao Kristo amewapa mamlaka ya kufanya maamuzi na kuweka rasmi waangalizi wengine. (Matendo 6:2, 3; 15:2) Baraza Linaloongoza nalo lawapa mamlaka Halmashauri za Tawi, waangalizi wa wilaya na wa mzunguko, na wazee katika kila moja ya makutaniko zaidi ya 73,000 ya Mashahidi wa Yehova duniani kote. Wanaume hao wote Wakristo ambao wamejitoa wanastahili utegemezo wetu na staha yetu.—1 Timotheo 5:17.

20. Ni kielelezo gani kinachoonyesha kwamba Yehova hafurahii wale wanaokosa kustahi Wakristo wenzao wenye mamlaka?

20 Kwa habari ya staha tunayostahili kuwapa wale walio na mamlaka katika kutaniko la Kikristo, twaweza kufanya ulinganisho wenye kupendeza na unyenyekeo tunaostahili kuwapa mamlaka za kilimwengu. Mtu akivunja sheria ya kibinadamu anayoikubali Mungu, adhabu inayotozwa na “wale wanaotawala” kwa hakika, ni wonyesho usio wa moja kwa moja wa ghadhabu ya Mungu “juu ya yeye anayezoea kufanya lililo baya.” (Warumi 13:3, 4) Ikiwa Yehova anakasirika mtu anapovunja sheria za wanadamu na kukosa staha ifaayo kwa mamlaka za kilimwengu, basi ni lazima awe anakasirika kama nini ikiwa Mkristo aliyejitoa wakfu avunja kanuni za Biblia na akosa kustahi Wakristo wenzake walio na mamlaka!

21. Tutafurahi kufuata shauri gani la Kimaandiko, na ni nini kitakachofikiriwa katika makala ifuatayo?

21 Badala ya kupatwa na hasira ya Mungu kwa kuwa na mtazamo wa kuasi au kujitegemea, tutafuata shauri la Paulo kwa Wakristo katika Filipi: “Basi, wapendwa wangu, kama vile mlivyotii sikuzote, si wakati mimi nilipokuwapo tu, bali sasa zaidi sana mimi nisipokuwapo, utimizeni wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka. Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema. Yatendeni mambo yote pasipo manung’uniko wala mashindano, mpate kuwa wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekana kuwa kama mianga katika ulimwengu.” (Wafilipi 2:12-15) Watu wa Yehova hunyenyekea mamlaka kwa utayari jambo lililo tofauti na kizazi cha sasa kilicho kibaya na chenye kupotoka ambacho kimejiletea tatizo la mamlaka. Hivyo, wao huvuna thawabu bora, kama tutakavyoona katika makala ifuatayo.

[Maelezo ya Chini]

a Ona makala inayotangulia.

Kwa Kupitia

◻ Ni nani aliye na Mamlaka ya Juu Zaidi, na kwa nini mamlaka yake ni halali?

◻ Ni kwa maana gani mamlaka zilizo kubwa “zimesimama zikiwa zimewekwa na Mungu katika mahali pa vyeo vyazo”?

◻ Mamlaka zilizo kubwa zakoma kuwa “mhudumu wa Mungu” wakati gani?

◻ Kuna mfumo gani wa mamlaka ulioko katika familia ya Kikristo?

◻ Ni kupeana gani kwa mamlaka kunakofanyika katika kutaniko la Kikristo?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yesu alisema hivi: “Mlipeni Kaisari yaliyo ya Kaisari”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki