Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w90 11/1 kur. 10-15
  • Maoni ya Mkristo Juu ya Mamlaka za Juu Zaidi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maoni ya Mkristo Juu ya Mamlaka za Juu Zaidi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuzitambua Mamlaka za Juu Zaidi
  • “Zimewekwa na Mungu
  • “Mungu wa Huu Mfumo wa Mambo”
  • Mamlaka Zenye Akili za Kutopendelea
  • Maoni ya Mkristo Kuhusu Mamlaka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Mamlaka Zilizo Kubwa
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Ni Mamlaka ya Nani Unayopaswa Kutambua?
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Mungu na Kaisari
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
w90 11/1 kur. 10-15

Maoni ya Mkristo Juu ya Mamlaka za Juu Zaidi

“Acheni kila nafsi iwe katika kutii mamlaka za juu zaidi, kwa maana hakuna mamlaka isipokuwa kwa njia ya Mungu; mamlaka zilizoko zimesimama zikiwa zimewekwa na Mungu katika vyeo vinavyozihusu.”—WARUMI 13:1, NW.

1, 2. (a) Kwa nini Paulo alikuwa mfungwa gerezani katika Roma? (b) Ombi la rufani ya Paulo kwa Kaisari latokeza maswali gani?

MTUME Paulo aliwaandikia Waroma maneno yaliyo juu karibu 56 W.K. Miaka michache baadaye, alijipata Roma akiwa mfungwa gerezani. Kwa nini? Alikuwa ameshambuliwa na watu wenye ghasia katika Yerusalemu na kuponyoshwa na askari Waroma. Alipopelekwa Kaisaria, alikabiliana na mashtaka bandia, lakini alijitetea kihodari mbele ya Feliki, gavana Mroma. Feliki, kwa kutumainia hongo, alimzuia gerezani kwa miaka miwili. Mwishowe, Paulo alidai kwa gavana aliyefuata, Festo, kwamba kesi yake isikiwe na Kaisari.—Matendo 21:27-32; 24:1–25:12.

2 Hii ilikuwa haki yake akiwa raia Mroma. Lakini je! lilikuwa jambo lenye upatani Paulo aombe rufani kwa mamlaka hiyo ya kibeberu hali Yesu alikuwa amemrejezea Shetani kuwa ndiye hasa “mtawala wa ulimwengu” na Paulo mwenyewe akiwa amekwisha mwita Shetani “mungu wa mfumo huu wa mambo”? (Yohana 14:30; 2 Wakorintho 4:4, NW) Au mamlaka ya Kiroma ilikalia ‘cheo fulani chenye kuihusu’ kilichofanya ifae Paulo kutegemea mamlaka hiyo kwa ulinzi wa haki zake? Kwa kweli, je! yale maneno ya mitume ya mapema kidogo, “Ni lazima sisi tutii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu,” yaruhusu kuwa na utii wa Kikristo kwa watawala wa kibinadamu wakati wowote ambapo kutotii Mungu hakuhusiki?—Matendo 5:29, NW.

3. Ni maoni gani ya ukomavu ambayo Paulo afunua, na dhamiri yahusikaje?

3 Paulo atusaidia kujibu maswali haya katika barua yake kwa Waroma, ambapo afunua maoni ya ukomavu juu ya utawala wa kibinadamu. Kwenye Warumi 13:1-7, Paulo aonyesha wazi sehemu ambayo ni lazima dhamiri ya Mkristo ihusike katika kusawazisha utii kamili kwa ile Mamlaka Kuu Kupita Zote, Yehova Mungu, pamoja na utii unaozihusu “mamlaka za juu zaidi.”

Kuzitambua Mamlaka za Juu Zaidi

4. Ni rekebisho gani la maoni lililofanywa katika 1962, lijapotokeza maswali gani?

4 Kwa miaka kadhaa, mpaka 1962, Mashahidi wa Yehova walishikilia kwamba mamlaka za juu zaidi zilikuwa Yehova Mungu na Kristo Yesu. Hata hivyo, kupatana na Mithali 4:18, nuru iliongezeka, na maoni haya yakarekebishwa, jambo ambalo huenda likatokeza maswali katika akili za watu fulani. Je! sasa sisi tuko sahihi kwa kusema kwamba mamlaka hizi ni wafalme, marais, mawaziri wakuu, mameya, mahakimu (majistriti), na wengine walio na nguvu ya kilimwengu, ya kisiasa katika ulimwengu na kwamba sisi tuna deni lao la utii unaowahusu?

5. Muktadha wa Warumi 13:1 watusaidiaje tutambue mamlaka za juu zaidi, na ni jinsi gani tafsiri mbalimbali za Biblia zaunga mkono utambulisho huu?

5 Irenayo, mwandikaji wa karne ya pili W.K., alisema kwamba kulingana na watu fulani katika siku yake, kwenye Warumi 13:1 Paulo alikuwa akisema “kuhusu watawala wa kimalaika [au] juu ya watawala wasioonekana.” Ingawa hivyo, Irenayo mwenyewe aliziona mamlaka za juu zaidi kuwa “mamlaka hakika za kibinadamu.” Muktadha wa maneno ya Paulo waonyesha kwamba Irenayo alikuwa sahihi. Katika mistari inayomalizia ya Warumi sura ya 12, Paulo aeleza jinsi Wakristo wapaswavyo kujiendesha mbele ya “watu wote,” wakitendea hata ‘maadui’ kwa upendo na ufikirio. (Warumi 12:17-21) Kwa wazi, maneno “watu wote” yana utumizi kwa wanadamu nje ya kundi la Kikristo. Hivyo basi “mamlaka za juu zaidi,” ambazo Paulo aendelea kuzizungumza, ni lazima pia ziwe nje ya kundi la Kikristo. Kupatana na hilo, angalia jinsi tafsiri mbalimbali hufasiri sehemu ya kwanza ya Warumi 13:1: “Kila mtu ni lazima atii mamlaka za kiserikali” (Today’s English Version); “kila mtu ni lazima ajinyenyekeze kwa mamlaka zenye kugavana” (New International Version); “kila mtu ni sharti atii mamlaka zenye kusimamia raia.”—New Testament in Modern English ya Phillip.

6. Maneno ya Paulo juu ya kulipa kodi na ushuru yaonyeshaje kwamba ni lazima mamlaka za juu zaidi ziwe ni mamlaka za kilimwengu?

6 Paulo aendelea kusema kwamba mamlaka hizi huitisha kodi na ushuru. (Warumi 13:6, 7) Kundi la Kikristo haliitishi kodi wala ushuru; wala Yehova wala Yesu wala wowote wa wale “watawala wasioonekana” wengine. (2 Wakorintho 9:7) Kodi hulipwa kwa wenye mamlaka walimwengu tu. Kwa kuafikiana na hilo, maneno ya Kigiriki kwa “kodi” na “ushuru” yaliyotumiwa na Paulo kwenye Warumi 13:7 hurejezea hasa pesa zilipwazo kwa Serikali.a

7, 8. (a) Maandiko mbalimbali yapatanaje na maoni ya kwamba Wakristo wapaswa kujitiisha kwa mamlaka za kisiasa za ulimwengu huu? (b) Ni wakati gani tu Mkristo hangefuata maagizo ya “mamlaka”?

7 Zaidi ya hilo, himizo la Paulo kutii mamlaka za juu zaidi lapatana na amri ya Yesu kulipa “Kaisari yaliyo ya Kaisari, na Mungu yaliyo ya Mungu,” ambapo “Kaisari” awakilisha mamlaka ya kilimwengu. (Mathayo 22:21) Pia jambo hilo laafikiana na maneno ya baa-daye ya Paulo kwa Tito: “Uwakumbushe watu kunyenyekea kwa wenye uwezo na mamlaka, na kutii, na kuwa tayari kwa kila kazi njema.” (Tito 3:1) Kwa sababu hiyo, Wakristo waagizwapo na serikali washiriki katika kazi za kijumuiya, kwa kufaa wao hukubali maadamu kazi hizo si kuridhiana kufanya utumishi fulani usio wa kimaandiko au kuvunja kanuni za Kimaandiko kwa njia nyingineyo, kama ile ipatikanayo kwenye Isaya 2:4.

8 Petro aliyakinisha pia kwamba twapaswa kutii mamlaka za kilimwengu za ulimwengu huu aliposema: “Tiini kila kiamriwacho na watu, kwa ajili ya Bwana; ikiwa ni mfalme, kama mwenye cheo kikubwa; ikiwa ni wakubwa, kama wanaotumwa naye ili k[u]walipiza kisasi watenda mabaya na kuwasifu watenda mema.” (1 Petro 2:13, 14) Kupatana na hilo, Wakristo wangetii pia onyo la upole la Paulo kwa Timotheo: “Basi, naomba dua, sala, maombi na sala za shukrani zitolewe kwa Mungu kwa ajili ya watu wote, kwa ajili ya wafalme na wote wenye mamlaka, ili tupate kuishi maisha ya utulivu na amani pamoja na uchaji wa Mungu na mwenendo mwema.”b—1 Timotheo 2:1, 2, HNWW.

9. Kwa nini haipunguzi utukufu wa Yehova kurejezea mamlaka za kibinadamu kuwa “za juu zaidi”?

9 Kwa kuziita mamlaka za kilimwengu kuwa “za juu zaidi,” je! kwa njia fulani twaipunguza heshima impasayo Yehova? Sivyo, kwa sababu Yehova ni zaidi ya kuwa mkuu tu. Yeye ndiye “Bwana Mwenye Enzi Kuu,” “Aliye Mkuu Kupita Wote.” (Zaburi 73:28; Danieli 7:18, 22, 25, 27; Ufunuo 4:11; 6:10, NW) Utii ufaao kwa mamlaka za kibinadamu haupunguzi kwa vyovyote ibada yetu kwa ile Mamlaka Kuu Kupita Zote, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. Basi, ni kwa kadiri gani mamlaka hizi zilivyo za juu zaidi? Ni kuhusiana na wanadamu wengine tu na katika kizio cha utendaji wazo zenyewe. Hizo zina daraka la kusimamia na kulinda jumuiya za kibinadamu, na kwa ajili ya hilo huweka virekebi vya kuongoza mwenendo wa mambo ya umma.

“Zimewekwa na Mungu

Katika Vyeo Vinavyozihusu”

10. (a) Taarifa ya Paulo juu ya ‘kuweka’ mamlaka za juu zaidi yathibitisha nini juu ya mamlaka ya Yehova mwenyewe? (b) Yehova ameruhusu nini kwa habari ya ‘kuweka’ watawala fulani, na watumishi Wake hutahiniwaje kwa njia hiyo?

10 Ukuu wa Yehova Mungu juu ya hata mamlaka za kilimwengu waonwa katika jambo la kwamba mamlaka hizi “zimesimama zikiwa zimewekwa na Mungu katika vyeo vinavyozihusu.” Hata hivyo, taarifa hii yatokeza swali. Miaka fulani baada ya Paulo kuandika maneno haya, maliki Mroma Nero alifyatusha kampeni ya mnyanyaso mbaya sana dhidi ya Wakristo. Je! Mungu alimweka Nero kibinafsi katika cheo chake? Pishia hilo mbali! Si kwamba kila mtawala mmoja mmoja huchaguliwa na Mungu na kuwekwa cheoni ‘kwa neema ya Mungu.’ Bali, nyakati fulani Shetani hutumia mbinu zake kuingiza wanadamu wakatili cheoni wakiwa watawala, na Yehova huruhusu hilo, pamoja na mitihani ambayo watawala hao huleta juu ya watumishi wake washikao uaminifu wa kimaadili.—Linganisha Ayubu 2:2-10.

11, 12. Ni visa gani vilivyo katika rekodi ambamo Yehova alitumia mbinu zake kibinafsi ili kuingiza au kuondoa mamlaka za kilimwengu mahali pazo?

11 Hata hivyo, Yehova ameingilia kibinafsi kisa cha watawala au serikali fulani ili kutumikia kusudi lake lililotukuka. Kwa kielelezo, wakati wa Abrahamu Wakanaani waliruhusiwa wabaki katika bara la Kanaani. Ingawa hivyo, baadaye Yehova aliwang’oa na kuipa mbegu ya Abrahamu bara hilo. Wakati wa mkao wa muda wa Waisraeli jangwani, Yehova hakuwaacha waingilie mipaka ya Edomu, Moabu, na Mlima Seiri. Lakini aliwaagiza waharibu falme za Sihoni na Ogu.—Mwanzo 15:18-21; 24:37; Kutoka 34:11; Kumbukumbu 2:4, 5, 9, 19, 24; 3:1, 2.

12 Baada ya Israeli kutua katika Kanaani, Yehova aliendelea kupendezwa moja kwa moja na mamlaka zilizoathiri watu wake. Nyakati fulani, Israeli walipotenda dhambi, Yehova aliwaruhusu waje chini ya mamlaka ya kipagani. Walipotubu, aliondoa mamlaka hiyo barani. (Waamuzi 2:11-23) Hatimaye, aliruhusu Yuda, pamoja na mataifa mengine mengi, waje chini ya udhibiti wa Babuloni. (Isaya 14:28–19:17; 23:1-12; 39:5-7) Baada ya Israeli kuingia uhamishoni katika Babuloni, Yehova alitabiri inuko na anguko la serikali kubwa za ulimwengu ambazo zingeathiri watu wake kuanzia wakati wa Babuloni hadi siku yetu wenyewe.—Danieli, sura 2, 7, 8, na 11.

13. (a) Kulingana na wimbo wa Musa, kwa nini Yehova aliamrisha mpaka wa vikundi vya watu? (b) Kwa nini baadaye Mungu alirudisha Israeli kwenye bara lalo?

13 Musa aliimba hivi juu ya Yehova: “Yeye Aliye Juu alipowapa mataifa urithi wao, alipowabagua wanadamu, aliweka mipaka ya watu kwa kadiri ya hesabu ya wana wa Israeli. Maana, sehemu ya BWANA [Yehova, NW] ni watu wake, Yakobo ni kura ya urithi wake.” (Kumbukumbu 32:8, 9; linganisha Matendo 17:26.) Ndiyo, ili kutekeleza makusudi yake, hapo Mungu aliamrisha ni mamlaka zipi zingebaki na ni zipi zingeharibiwa. Kwa njia hii, aliugawia uzao wa Abrahamu bara la kurithi na baadaye akawarudisha kwenye bara hilo, hivi kwamba hatimaye ile Mbegu iliyoahidiwa ingeweza kutokea huko, sawasawa na ilivyosemwa kwa unabii.—Danieli 9:25, 26; Mika 5:2.

14. Sana-sana, ni katika maana gani Yehova huweka mamlaka za kibinadamu katika vyeo vinavyozihusu?

14 Hata hivyo, katika visa vilivyo vingi Yehova huweka watawala katika vyeo vinavyowahusu katika maana ya kwamba yeye huruhusu wanadamu watwae vyeo vya mamlaka yenye kuhusu wao kwa wao lakini sikuzote vikiwa chini kuliko yeye mwenyewe. Hivyo, Yesu aliposimama mbele ya Pontio Pilato, alimwambia hivi mtawala huyo: “Wewe hungekuwa na mamlaka yo yote juu yangu, kama usingepewa kutoka juu.” (Yohana 19:11) Hiyo haikumaanisha kwamba Pilato aliwekwa cheoni na Mungu kibinafsi, bali ilimaanisha kwamba mamlaka yake ya kuamua uhai au kifo juu ya Yesu ilikuwa kwa ruhusa ya Mungu tu.

“Mungu wa Huu Mfumo wa Mambo”

15. Shetani hutumia mamlaka kwa njia gani katika ulimwengu huu?

15 Ingawa hivyo, namna gani ile taarifa ya Biblia kwamba Shetani ndiye mungu, au mtawala, wa ulimwengu huu? (Yohana 12:31; 2 Wakorintho 4:4, NW) Kwa kweli, namna gani juu ya jisifu la Shetani kwa Yesu wakati alipomwonyesha Yesu falme zote za ulimwengu na kusema: “Mamlaka haya yote . . . nimepewa . . . na kwake ye yote ninayetaka nitamupa.” (Luka 4:6, ZSB) Yesu hakupinganisha jisifu la Shetani. Na maneno ya Shetani yapatana na yale ambayo Paulo aliwaandikia Waefeso baadaye: “Sisi tuna kushindana mweleka, si dhidi ya damu na mnofu, bali dhidi ya serikali, dhidi ya mamlaka, dhidi ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, dhidi ya kani za roho zenye uovu katika mahali pa kimbingu.” (Waefeso 6:12, NW) Zaidi ya hilo, kitabu cha Ufunuo huonyesha Shetani kuwa drakoni mkubwa ambaye humpa hayawani wa mfano aliye mfumo wa kisiasa wa ulimwengu “nguvu zake na kiti cha ufalme chake na mamlaka kubwa.”—Ufunuo 13:2, NW.

16. (a) Yaweza kuonwaje kwamba mamlaka ya Shetani ina mipaka? (b) Kwa nini Yehova huruhusu Shetani awe na mamlaka miongoni mwa ainabinadamu?

16 Ingawa hivyo, angalia kwamba taarifa ya Shetani kwa Yesu, ‘mamlaka haya yote nimepewa,’ yaonyesha kwamba yeye pia hutumia mamlaka kwa kuruhusiwa tu. Kwa nini Mungu hutoa ruhusa hii? Kazi-maisha ya Shetani akiwa mtawala wa ulimwengu ilianza katika Edeni alipomshtaki Mungu peupe juu ya kusema uwongo na kutumia enzi kuu Yake bila haki. (Mwanzo 3:1-6) Adamu na Hawa walimfuata Shetani na kukosa kumtii Yehova Mungu. Kufikia hapo Yehova angaliweza, kwa haki kamilifu, kufisha Shetani na wafuasi wake wapya wawili. (Mwanzo 2:16, 17) Lakini maneno ya Shetani kwa kweli yalikuwa wito wa ushindani wa kibinafsi kwa Yehova. Hivyo basi Mungu katika hekima yake alimruhusu Shetani aendelee kuishi kwa muda, na Adamu na Hawa waliruhusiwa wazidishe watoto kabla hawajafa. Kwa njia hii, Mungu aliandaa wakati na fursa ili ubandia wa shtaka la Shetani uonyeshwe.—Mwanzo 3:15-19.

17, 18. (a) Kwa nini twaweza kusema kwamba Shetani ndiye mungu wa ulimwengu huu? (b) Ni kwa njia gani “hakuna mamlaka” katika ulimwengu huu “isipokuwa kwa njia ya Mungu”?

17 Matukio ya tangu Edeni yameonyesha kwamba mashtaka ya Shetani yalikuwa uwongo wa kupindukia. Wazao wa Adamu hawajapata furaha ama chini ya utawala wa Shetani ama chini ya utawala wa binadamu. (Mhubiri 8:9) Kwa upande mwingine, mishughuliko ya Mungu pamoja na watu wake mwenyewe imeonyesha utawala wa kimungu ni mkubwa zaidi. (Isaya 33:22) Lakini kwa kuwa walio wengi wa wazao wa Adamu hawakubali enzi kuu ya Yehova, wao hutumikia Shetani akiwa mungu kwa kujua au bila kujua.—Zaburi 14:1; 1 Yohana 5:19.

18 Karibuni, yale masuala yaliyotokezwa katika Edeni yatatatuliwa. Ufalme wa Mungu utachukua usimamizi kamili wa mambo ya ainabinadamu, na Shetani atafungwa katika abiso. (Isaya 11:1-5; Ufunuo 20:1-6, NW) Ingawa hivyo, kwa sasa mpango au muundo wa aina fulani umehitajika kabisa miongoni mwa ainabinadamu ili iwezekane kuwa na maisha yenye utaratibu. Yehova “si Mungu wa machafuko, bali wa amani.” (1 Wakorintho 14:33) Kwa sababu hiyo, ameruhusu miundo ya mamlaka itokee katika jumuiya mbalimbali zilizositawi nje ya Edeni, naye ameruhusu wanadamu watumie mamlaka katika mpango huu. Kwa njia hii, “hakuna mamlaka isipokuwa kwa njia ya Mungu.”

Mamlaka Zenye Akili za Kutopendelea

19. Je! kila mtawala wa kibinadamu yuko chini ya udhibiti wa Shetani wa moja kwa moja?

19 Tangu Edeni, Shetani amekuwa na uhuru mpana miongoni mwa ainabinadamu, naye ametumia uhuru huu kutumia mbinu zake kuelekeza matukio duniani, kupatana na lile jisifu lake kwa Yesu. (Ayubu 1:7; Mathayo 4:1-10) Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba kila mtawala katika ulimwengu huu hujiweka moja kwa moja kwenye udhibiti wa Shetani. Baadhi yao—kama Nero katika karne ya kwanza na Adolf Hitler katika karne yetu—wamedhihirisha roho ya kishetani kweli kweli. Lakini wengine hawakufanya hivyo. Sergio Paulo, yule liwali wa Saiprasi, alikuwa “mtu mwelewa sana” aliyetafuta “ili asikie neno la Mungu.” (Matendo 13:7, HNWW) Galio, yule liwali wa Akaya, alikataa kushurutishwa na washtaki Wayahudi wa Paulo. (Matendo 18:12-17) Watawala wengine wengi wametumia mamlaka yao kwa njia yenye kuheshimika kwa kufuata dhamiri.—Linganisha Warumi 2:15.

20, 21. Ni matukio gani katika karne ya 20 yaonyesha kwamba si sikuzote ambapo watawala wa kibinadamu hufanya mapenzi ya Shetani?

20 Kitabu cha Ufunuo kilitabiri kwamba wakati wa “siku ya Bwana,” kuanzia 1914, Yehova hata angetumia mbinu zake kuelekeza mamlaka za kibinadamu zizuie makusudi ya Shetani. Ufunuo hueleza juu ya furiko la mnyanyaso, lenye kufyatushwa na Shetani dhidi ya Wakristo wapakwa mafuta, ambalo lingemezwa kabisa na “dunia.” (Ufunuo 1:10; 12:16, ZSB) Visehemu vilivyo ndani ya “dunia,” jamii ya kibinadamu iliyopo duniani sasa, vingelinda watu wa Yehova na mnyanyaso wa Shetani.

21 Je! hilo limetukia kikweli? Ndiyo. Kwa kielelezo, katika miaka ya 1930 na ya 1940, Mashahidi wa Yehova katika United States walikuwa chini ya msongo mkubwa, wakishambuliwa-shambuliwa na wenye ghasia na kukamatwa-kamatwa isivyo haki. Walipokea kitulizo wakati Mahakama Kuu ya United States ilipokata maamuzi yenye kutambua uhalali wa kazi yao. Mahali pengine pia, wenye mamlaka wamekuja kuwasaidia watu wa Mungu. Yapata miaka 40 iliyopita katika Ailandi, wenye ghasia Waroma Wakatoliki walishambulia Mashahidi wawili katika jiji la Cork. Polisi wa huko alikuja kuwasaidia Mashahidi, na mahakama ikawatia nidhamu washambuliaji hao. Mwaka uliopita tu katika Fiji, mkutano wa machifu wakuu ulisikia pendekezo la kupiga marufuku utendaji wa Mashahidi wa Yehova. Chifu mmoja aliseme kijasiri kutetea Mashahidi, na pendekezo hilo likashindwa kwa urahisi.

22. Ni maswali gani yatakayofuata kuzungumzwa?

22 Si sikuzote ambapo wenye mamlaka wa kilimwengu hutumikia malengo ya Shetani, hapana. Wakristo waweza kutii mamlaka za juu zaidi bila kutii Shetani mwenyewe. Kwa kweli, wao watatii mamlaka hizi maadamu Mungu aruhusu mamlaka hizo ziwepo. Ingawa hivyo, utii huo wamaanisha nini? Na Wakristo waweza kutarajia marudisho gani kutoka kwa mamlaka za juu zaidi? Maswali haya yatazungumzwa katika makala za mafunzo kuanzia ukurasa 18 na 23 za gazeti hili.

[Maelezo ya Chini]

a Ona, kwa kielelezo, utumizi wa neno “kodi” (phoʹros) kwenye Luka 20:22. Ona pia utumizi wa neno la Kigiriki te’los, lililotafsiriwa hapa “ushuru,” kwenye Mathayo 17:25, ambapo limetafsiriwa “wajibu mbalimbali.

b Nomino ya Kigiriki iliyotafsiriwa “wenye mamlaka” (“wenye cheo cha juu,” NW) hy·pe·ro·kheʹ, yahusiana na kitenzi hy·pe·re’kho. Neno hili “za juu zaidi” katika “mamlaka za juu zaidi” limetolewa katika kitenzi kile kile cha Kigiriki, jambo ambalo laongezea uthibitisho wa kwamba mamlaka za juu zaidi ni mamlaka za kilimwengu. Fasiri ya Warumi 13:1 katika Union Version ya Kiswahili, “Kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu,” si sahihi. Wanadamu walio ‘katika cheo cha juu zaidi’ si wakuu kabisa, ingawa huenda wakawa wenye cheo cha juu zaidi kwa wanadamu wengine.

Wewe Ungejibuje?

◻ Ni nani walio mamlaka za juu zaidi?

◻ Twaweza kusemaje kwamba “hakuna mamlaka isipokuwa kwa njia ya Mungu”?

◻ Kwa nini Yehova huruhusu ulimwengu uwe chini ya mamlaka ya Shetani?

◻ Ni kwa njia gani Mungu huweka mamlaka za kibinadamu “katika vyeo vinavyozihusu”?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Baada ya kuteketezwa kwa Roma, Nero alionyesha roho ya kishetani kweli kweli

[Picha katika ukurasa wa 15]

Sergio Paulo, yule liwali wa Saiprasi, alitafuta kulisikia neno la Mungu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki