SURA YA 17
Marafiki Shuleni—Kuna Uhitaji Wowote wa Kuwa Mwangalifu?
“Wakati fulani ningewaona vijana wenzangu na kusema, ‘Hawa ni marafiki wa kufa kuzikana. Ningependa kuwa mmoja wao.’”—Joe.
“Haikuwa vigumu kupata marafiki shuleni. Kwa hiyo mara kwa mara nilijikuta katika matatizo.”—Maria.
KILA mtu anahitaji marafiki—watu anaoweza kuwa nao wakati wa dhiki na faraja. Yesu alikuwa na marafiki na alifurahia kuwa pamoja nao. (Yohana 15:15) Yesu alipokuwa kwenye mti wa mateso, Yohana, “mwanafunzi ambaye alimpenda,” na aliyekuwa rafiki yake wa karibu alikuwapo. (Yohana 19:25-27; 21:20) Unahitaji marafiki kama hao, watu wanaoweza kushikamana nawe nyakati zote, hata iweje!
Huenda utasema kwamba tayari umeshapata marafiki kama hao shuleni—mwanafunzi mmoja au wawili mnaoelewana vizuri. Mna mapendezi yaleyale nanyi hupenda kupiga gumzo. Machoni pako, huenda wasionekane kuwa “mashirika mabaya.” (1 Wakorintho 15:33) “Unakutana na vijana hao karibu kila siku,” Anne anasema. “Kwa hiyo unapokuwa pamoja nao, unajisikia huru kabisa. Si kama unapokuwa na ndugu na dada zako wa kiroho, unapohitaji kuwa mwangalifu kuhusu kila jambo unalofanya. Shuleni unaweza kujiachilia.” Pia, unaweza kuwa na maoni kama ya Lois, ambaye alisema, “Nilitaka marafiki wangu shuleni waone kwamba Mashahidi wa Yehova si watu tofauti kama vile wengine wanavyofikiri, nilitaka kuwaonyesha kwamba sisi ni watu wa kawaida.” Je, hizo ni sababu zinazotosha za kuwa na urafiki wa karibu na wanafunzi wenzako?
Kwa Nini Uwe Mwangalifu?
Fikiria yaliyompata Maria, aliyetajwa mwanzoni. Utu wake ulifanya iwe rahisi kwake kupata marafiki lakini ikawa vigumu kujiwekea mipaka. Anasema: “Nilipenda kuwa na marafiki wanaonipenda, wavulana na wasichana. Muda si muda nilijikuta nikizama zaidi na zaidi katika tope la ulimwengu huu.” Lois alikuwa katika hali kama hiyo. Anasema: “Nilianza kuwaiga vijana wengine na kujiendesha kama wao.”
Hilo halishangazi kwa kuwa ili kuendeleza urafiki wa karibu na mtu mwingine, lazima mpendezwe na mambo yaleyale na kuongozwa na kanuni zilezile. Ukianzisha urafiki wa karibu na watu ambao hawaongozwi na mafundisho na kanuni za Biblia zinazokuongoza, bila shaka wataathiri mwenendo wako. (Methali 13:20) Ndiyo sababu mtume Paulo aliandika: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.”—2 Wakorintho 6:14.
Mambo Unayoweza Kufanya
Je, shauri la Paulo linamaanisha kwamba unapaswa kuwaepuka wanafunzi wenzako na kujitenga nao? Hapana! Ili Wakristo watimize kazi yao ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ wanahitaji kuchangamana na watu wa jamii, dini, na desturi mbalimbali.—Mathayo 28:19.
Mtume Paulo alituwekea mfano mzuri sana. Alijua kuzungumza na “watu wa namna zote,” ingawa hakuwa na imani kama yao. (1 Wakorintho 9:22, 23) Unaweza kumwiga Paulo. Wachangamkie vijana wenzako. Jifunze kuwasiliana nao. Lakini kataa katakata kushawishiwa kuiga usemi na mwenendo wa wanafunzi wenzako. Badala yake, usisite kuwaeleza kwa heshima kwa nini unafuata kanuni za Biblia.—2 Timotheo 2:25.
Ni kweli kwamba utaonekana kuwa tofauti, na hilo si jambo rahisi. (Yohana 15:19) Hata hivyo, fikiria mfano huu: Ikiwa ungekuwa katika mashua ya kuokolea uhai huku ukiwa umezungukwa na watu wanaotapatapa ndani ya maji, unaweza kuwasaidia jinsi gani, je, ni kwa kuruka kutoka katika mashua hiyo na kujitosa ndani ya maji ili ujiunge nao? Huwezi kufanya hivyo hata kidogo!
Vivyo hivyo, unapokuwa shuleni unazungukwa na watu ambao hawana ulinzi unaotokana na kuwa rafiki ya Yehova. (Zaburi 121:2-8) Ikiwa ungeacha kufuata kanuni za Yehova ili uwe na uhusiano wa karibu na wanafunzi wenzako, ungekuwa ukihatarisha furaha yako na hali yako ya kiroho. (Waefeso 4:14, 15; Yakobo 4:4) Ingekuwa afadhali kama nini ikiwa ungejaribu kuwasaidia wanafunzi wenzako wajiunge nawe katika mashua ya mfano, kwa kuwaonyesha jinsi wanavyoweza kumtumikia Yehova! Huo ndio urafiki wa kweli.
MAANDIKO MUHIMU
“Ninafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili niishiriki hiyo pamoja na wengine.”—1 Wakorintho 9:23.
PENDEKEZO
Ikiwa wanafunzi wenzako wangependa kujua kuhusu dini yako, waruhusu waeleze maoni yao pia. Wasikilize vizuri. Unapozungumza, fanya hivyo “kwa tabia-pole na heshima kubwa.”—1 Petro 3:15.
JE, WAJUA . . .?
Wengi ambao wanamtumikia Mungu leo walisaidiwa kujifunza Biblia na mwanafunzi mwenzao ambaye hakuogopa kuzungumza nao kuhusu imani yake.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Nikiona kwamba uhusiano wangu pamoja na mwanafunzi mwenzangu umekuwa wa karibu kupita kiasi, nita ․․․․․
Mwanafunzi mwenzangu akidhihaki imani yangu, nitashughulikia hali hiyo kwa ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Unafikiri ni kwa nini huenda ikaonekana kuwa rahisi kupata marafiki shuleni kuliko katika kutaniko la Kikristo?
● Kutumia wakati mwingi pamoja na mwanafunzi mwenzako baada ya saa za shule kunaweza kuwa na matokeo gani mabaya?
● Utapata faida gani kwa kuwaeleza wanafunzi wenzako kwamba wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova?
[Blabu katika ukurasa wa 143]
“Nilikuwa nikitenda kama wanafunzi wenzangu shuleni, kwa hiyo ilikuwa rahisi kupata marafiki huko. Lakini nilijifunza kutokana na makosa yangu. Sasa nina marafiki katika kutaniko—marafiki ninaoweza kuwaamini.’’—Daniel
[Picha katika ukurasa wa 146]
Ni njia gani bora ya kumsaidia mtu anayezama? Kwa kujitosa ndani ya maji, au kwa kutafuta njia ya kumwokoa?