Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yp2 sura 32 kur. 263-272
  • Ninaweza Kujifurahisha Jinsi Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ninaweza Kujifurahisha Jinsi Gani?
  • Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Uwe Macho?
  • Vipi Kwenda Disko?
    Amkeni!—2004
  • Naweza Kuchaguaje Sinema ya Adabu?
    Amkeni!—1992
  • Utatazama Sinema Zipi?
    Amkeni!—2005
  • Kwa Nini Wazazi Wangu Hawaniachi Nijifurahishe?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
Pata Habari Zaidi
Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
yp2 sura 32 kur. 263-272

SURA YA 32

Ninaweza Kujifurahisha Jinsi Gani?

Tia alama maswali yafuatayo kweli au si kweli.

Kulingana na Biblia . . .

Ni kosa kushiriki michezo ya aina yoyote.

□ Kweli □ Si kweli

Sinema zote na vipindi vyote vya televisheni ni vibaya.

□ Kweli □ Si kweli

Dansi zote ni mbaya.

□ Kweli □ Si kweli

UMESOMA kwa bidii juma zima. Mwisho juma umefika. Kazi za nyumbani zimekwisha. Lakini ungali na nguvu—mojawapo ya baraka za kuwa kijana. (Methali 20:29) Sasa, kile ungependa kufanya ni kujifurahisha kidogo.

Huenda vijana wenzako wakahisi kwamba Biblia inashutumu kujifurahisha, na hivyo inakuzuia kufurahia maisha. Lakini, je, hilo ni kweli? Acheni tuchunguze maswali yaliyo katika ukurasa unaotangulia tuone maoni ya Biblia kuhusu kujifurahisha.

● Ni kosa kushiriki michezo ya aina yoyote.

Si kweli. Biblia inasema kwamba “mazoezi ya kimwili ni yenye faida.” (1 Timotheo 4:8) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mazoezi” ambalo Paulo alitumia katika mstari huo linamaanisha ‘kujizoeza kama mwanasarakasi.’ Leo kuna michezo mingi—kama vile kuteleza barafuni, kuendesha baiskeli, kukimbia mchakamchaka, tenisi, besiboli, soka, voliboli, na mingine mingi—inayoweza kumsaidia mtu kufanya mazoezi na pia kujifurahisha.

Hata hivyo, kuna haja yoyote ya kuchukua tahadhari? Fikiria muktadha wa mstari ulionukuliwa hapo juu. Akimwandikia kijana Timotheo, mtume Paulo alisema: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida kidogo; lakini ujitoaji-kimungu ni wenye faida kwa mambo yote, kwa kuwa una ahadi ya uzima wa sasa na ule utakaokuja.” Maneno ya Paulo yanatukumbusha kwamba jambo kuu maishani mwetu ni kumpendeza Mungu. Unaweza kuhakikisha kwamba unatanguliza ujitoaji-kimungu—hata unapochagua mchezo fulani—kwa kujiuliza maswali haya matatu:

1. Kuna hatari yoyote inayohusika katika mchezo huo? Usitegemee tu mambo ya watu au kukubaliana na maoni ya vijana wenzako ambao ni mashabiki wa mchezo huo. Tafuta ukweli wa mambo. Kwa mfano, uliza: Ni watu wangapi wanaoumia katika mchezo huo? Ni tahadhari gani inayochukuliwa wakati wa mchezo huo? Ni mazoezi na vifaa gani vinavyohitajiwa ili kucheza mchezo huo bila kujihatarisha? Ingawa kuna hatari fulani katika karibu kila mchezo, je, lengo kuu la mchezo huo ni kufanya mambo yanayohatarisha uhai?

Uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu. Kulingana na Sheria ya Mungu kwa Waisraeli, hata mtu aliyemuua mwingine bila kukusudia alipata adhabu. (Kutoka 21:29; Hesabu 35:22-25) Hivyo, watu wa Mungu walitiwa moyo kuzingatia sana usalama. (Kumbukumbu la Torati 22:8) Vivyo hivyo, Wakristo leo wanapaswa kuheshimu uhai.

2. Katika mchezo huo, je, kuna mashirika mazuri? Ikiwa wewe ni mwanariadha hodari, huenda marafiki na walimu wakataka ujiunge na timu ya shule. Huenda ukashawishika kufanya hivyo. Kijana Mkristo, Mark anasema, “Sielewi ni kwa nini wazazi wangu hawataki nijiunge na timu ya shule.” Lakini badala ya kujaribu kuwabembeleza wazazi wako wakubali maoni yako, fikiria mambo yanayofuata: Kwa kawaida mazoezi na michezo hufanywa baada ya saa za kawaida za shule. Ukitia fora, utahitajika kutumia muda mwingi zaidi katika michezo. Usipofaulu, bado utalazimika kutumia muda mwingi zaidi kufanya mazoezi. Pia, timu nyingi hupenda kusherehekea ushindi pamoja au kwenda “kuomboleza” pamoja wanaposhindwa.

Sasa jiulize: ‘Je, kutumia wakati wangu katika mchezo unaoweza kunifanya nijenge urafiki wa karibu na vijana ambao hawaongozwi na viwango kama vyangu, kutanisaidia kiroho?’ (1 Wakorintho 15:33) ‘Nitalazimika kudhabihu mambo gani ili tu nijiunge na timu hiyo?’

3. Mchezo huo utachukua kiasi gani cha wakati na pesa? Biblia inatushauri ‘tuhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.’ (Wafilipi 1:10) Ili kukusaidia kuona jinsi unavyoweza kutumia shauri hilo, jiulize: ‘Je, mchezo huo utakula wakati ambao nimepangia kazi za shule au mambo ya kiroho? Kwa ujumla mchezo huo utanigharimu pesa ngapi? Je, ninaweza kuugharimia?’ Kujibu maswali hayo kutakusaidia kutanguliza mambo yaliyo ya maana zaidi.

● Sinema zote na vipindi vyote vya televisheni ni vibaya.

Si kweli. Biblia inawaamuru Wakristo ‘washike sana yaliyo mazuri’ na ‘wajiepushe na kila namna ya uovu.’ (1 Wathesalonike 5:21, 22) Si sinema zote na vipindi vyote vya televisheni vinavyopingana na kanuni hiyo.a

Bila shaka, kwenda kutazama sinema kunaweza kuwa njia nzuri ya kutumia wakati pamoja na marafiki. Leigh, msichana kutoka Afrika Kusini anasema, “Ninapotaka kutazama sinema fulani, mimi humpigia simu mmoja wa rafiki zangu, kisha tunasambaza habari kwa marafiki wengine.” Kwa kawaida kikundi hicho hutazama sinema hiyo mapema. Baadaye, wao huchukuliwa na wazazi wao na kwenda kula hotelini.

Sinema na televisheni ni uvumbuzi wa karibuni, hata hivyo, ni njia mpya tu ya kufanya jambo lililoanza zamani za kale, yaani usimuliaji wa hadithi. Yesu alikuwa stadi wa kusimulia hadithi zilizochochea mioyo ya watu. Kwa mfano, hadithi yake kuhusu Msamaria mwema huchochea hisia za huruma na kufundisha mambo muhimu.—Luka 10:29-37.

Leo pia, watengenezaji wa sinema hufundisha mambo yanayochochea maoni ya watu. Wao hujaribu kufanya watazamaji wavutiwe na wahusika katika sinema hizo, hata iwe mhusika mkuu ni mhalifu au mkatili. Usipokuwa mwangalifu, huenda ukajikuta ukishabikia mtu mhalifu, na kutetea mwenendo wake mpotovu au wenye ukatili! Unaweza kuepuka mtego huo jinsi gani?

Unapochagua sinema au kipindi cha televisheni, jiulize: ‘Je, kipindi hiki kitanisaidia kuwa mwenye huruma nyororo?’ (Waefeso 4:32) ‘Au kitanifanya niwacheke wengine wanapoumia?’ (Methali 17:5) ‘Kitafanya iwe vigumu kwangu “[kuchukia] yaliyo mabaya”?’ (Zaburi 97:10) ‘Je, ninawaunga mkono “watenda maovu” kwa kutazama kipindi au sinema hiyo?’—Zaburi 26:4, 5.

Uchambuzi na matangazo ya sinema yanaweza kukusaidia kujua yaliyomo katika sinema hiyo. Hata hivyo, ‘usiamini tu kila neno’ kipumbavu. (Methali 14:15) Kwa nini? Uchambuzi wa sinema ni maoni tu ya mtu mwingine. Nayo matangazo huenda yasionyeshe kwamba sinema hiyo ina mandhari zenye kuchukiza. Tineja anayeitwa Connie anasema, “Nimeona kwamba mara nyingi kuwajua wahusika wakuu katika sinema kunasaidia kujua sinema hiyo itakuwaje.”

Vijana wenzako Wakristo ambao pia huongozwa na kanuni za Biblia wanaweza kujua ikiwa sinema fulani inafaa. Lakini kumbuka kwamba mara nyingi watu hueleza mambo waliyofurahia katika sinema. Kwa nini usiulize kile ambacho hawakufurahia? Uliza habari hususa. Kwa mfano, waulize ikiwa kuna sehemu zinazoonyesha jeuri, ngono, au kuwasiliana na pepo. Wazazi wako pia wanaweza kukusaidia. Vanessa anasema: “Mimi huzungumza na wazazi wangu kuhusu sinema. Wakisema inafaa, ninaenda kuitazama.”

Kuchagua sinema au programu ya televisheni ni jambo zito. Kwa nini? Kwa sababu burudani unayochagua inaonyesha kilicho moyoni mwako, inafunua mambo unayoona kuwa muhimu. (Luka 6:45) Uchaguzi wako unaonyesha aina ya watu unaopenda kushirikiana nao, usemi unaofurahia, na mapendezi yako ya kiadili. Kwa hiyo, uwe mteuzi!

● Dansi zote ni mbaya.

Si kweli. Waisraeli walipovuka Bahari Nyekundu na kulikimbia jeshi la Misri, Miriamu aliwaongoza wanawake katika kucheza dansi. (Kutoka 15:20) Pia, katika ule mfano wa Yesu wa mwana mpotevu, mwana huyo aliporudi watu walishangilia kwa “muziki na dansi.”—Luka 15:25.

Ndivyo ilivyo leo. Katika utamaduni wa nchi nyingi, vijana kwa wazee hucheza dansi familia na marafiki wanapokusanyika pamoja. Hata hivyo, kuna uhitaji wa tahadhari. Ingawa Biblia haishutumu karamu zenye kiasi, inaonya dhidi ya “karamu za kupindukia.” (Wagalatia 5:19-21) Nabii Isaya aliandika: “Ole wao wanaoamka asubuhi na mapema ili watafute tu kileo, wanaokawia mpaka giza la jioni sana hivi kwamba divai inawawasha! Na kutakuwa na kinubi na kinanda, tari na filimbi, na divai katika karamu zao; lakini hawauangalii utendaji wa Yehova, wala hawakuiona kazi ya mikono yake.”—Isaya 5:11, 12.

Karamu hizo zilitia ndani “kileo” na dansi potovu. Zilianza mapema na kuendelea mpaka jioni. Ona pia kwamba waliokuwa katika karamu hizo walijiendesha kana kwamba hakuna Mungu! Si ajabu Mungu alishutumu karamu za namna hiyo.

Ukialikwa katika karamu ambayo watu watacheza dansi, jiulize: ‘Ni nani watakaokuwako? Wana sifa gani? Imepangwa na nani? Ni nani atakayeisimamia? Wazazi wangu watakubali niende? Kutakuwa na dansi ya aina gani?’ Dansi nyingi hukusudiwa kuamsha tamaa za ngono. Je, kucheza au kutazama tu dansi za aina hiyo kutakusaidia ‘kuukimbia uasherati’?—1 Wakorintho 6:18.

Namna gani ukialikwa kwenda disko? Fikiria maneno ya kijana anayeitwa Shawn ambaye kabla ya kuwa Mkristo alipenda kwenda disko. Anakumbuka: “Kwa kawaida muziki unaochezwa ni mbaya, dansi zinazochezwa ni chafu, na watu wengi huenda huko wakiwa na kusudi fulani.” Kusudi lenyewe ni kutoka huko na mtu wa kufanya ngono naye, anasema Shawn. Baada ya kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, Shawn alibadili nia yake. Ana maoni gani sasa? “Klabu hizo haziwafai Wakristo.”

Kwa Nini Uwe Macho?

Unafikiri ni wakati gani askari anaweza kushambuliwa kwa urahisi zaidi—akiwa vitani au anapopumzika na marafiki? Bila shaka ni wakati anapopumzika. Vivyo hivyo unapokuwa shuleni au kazini uko chonjo kiroho. Unaweza kuona hatari zinazoweza kutokea. Lakini, wakati wa starehe pamoja na marafiki wako, ni rahisi zaidi kulegeza viwango vyako na kuvunja msimamo wako wa kiadili.

Huenda vijana wenzako wakakudhihaki kwa sababu ya msimamo wako thabiti wa kiadili hata wakati wa burudani. Unaweza hata kushinikizwa na vijana ambao wamelelewa na wazazi Wakristo. Lakini dhamiri za vijana hao zimekuwa sugu. (1 Timotheo 4:2) Huenda wakadai kuwa huna usawaziko au una maringo. Hata hivyo, badala ya kushindwa na msongo wa marika, jitahidi ‘kuwa na dhamiri njema.’—1 Petro 3:16.

Jambo la maana si jinsi marafiki wako wanavyokuona bali ni jinsi Yehova anavyokuona! Na ikiwa rafiki zako wanakudhihaki kwa sababu ya kufuata dhamiri yako, tafuta marafiki wapya. (Methali 13:20) Kumbuka kwamba wewe tu ndiwe unayeweza kujiamulia jinsi utakavyojiendesha kiadili—hata unapokuwa katika starehe.—Methali 4:23.

PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 37

KATIKA SURA INAYOFUATA

Siku hizi ponografia imeenea sana na inaweza kupatikana kwa urahisi. Unaweza kuepuka mtego huo jinsi gani?

[Maelezo ya Chini]

a Unaweza kupata habari zaidi katika Buku la 1, sura ya 36.

MAANDIKO MUHIMU

“Ewe kijana, shangilia katika ujana wako, . . . nawe utembee katika njia za moyo wako na katika mambo ambayo macho yako yameona. Lakini ujue kwamba kwa ajili ya mambo yote hayo, Mungu wa kweli atakuleta hukumuni.”—Mhubiri 11:9.

PENDEKEZO

Waulize wazazi wako ikiwa wanaweza kupanga pindi kadhaa kila mwezi ambapo familia nzima inaweza kufanya mambo fulani yenye kufurahisha badala ya kutazama televisheni tu.

JE, WAJUA . . .?

Muziki na dansi zilikuwa sehemu muhimu katika ibada ya kweli ya Waisraeli.—Zaburi 150:4.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Nikiombwa kujiunga na timu ya mchezo fulani baada ya saa za shule, nitasema ․․․․․

Ikiwa sinema ninayotazama pamoja na marafiki wangu haifai, nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini Wakristo wanapaswa kujiepusha na michezo hatari?

● Unaweza kuamua jinsi gani ikiwa sinema fulani inafaa?

● Ni dansi ya aina gani inayofaa?

[Blabu katika ukurasa wa 269]

‘‘Ninapenda kucheza dansi, lakini nimeona faida ya kusikiliza mashauri ya wazazi wangu. Sitangulizi dansi maishani mwangu.’’—Tina

[Picha katika ukurasa wa 268]

Kama vile ambavyo askari anaweza kushambuliwa kwa urahisi asipokuwa macho, wewe pia unaweza kulegeza msimamo wako wa maadili unapostarehe

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki