Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yp2 sura 34 kur. 282-288
  • Kwa Nini Niishi Kulingana na Viwango vya Biblia?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Niishi Kulingana na Viwango vya Biblia?
  • Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ukweli wa Mambo
  • Viwango vya Biblia—Pingu au Mkanda wa Usalama?
  • Kwa nini niishi kupatana na viwango vya Biblia?
    Amkeni!—2007
  • Je, Ngono Itafanya Urafiki Wetu Uwe Mzuri Zaidi?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
  • Viwango vya Yehova Vinatusaidia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Mtumikie Yehova Kulingana na Viwango Vyake vya Juu
    Izingatie Siku ya Yehova Maishani
Pata Habari Zaidi
Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
yp2 sura 34 kur. 282-288

SURA YA 34

Kwa Nini Niishi Kulingana na Viwango vya Biblia?

Unakula chakula cha mchana shuleni pamoja na wasichana wawili wakati mvulana aliyehamia shule yenu karibuni anapoingia.

“Wajua nini, Brett anakupenda kwelikweli,” msichana wa kwanza akuambia. “Mimi huona jinsi anavyokutazama. Macho yake hayabanduki!”

“Tena ngoja nikwambie,” msichana wa pili anong’oneza huku akiinama kukuelekea. “Hana rafiki msichana!”

Tayari unajua. Juzi tu, Brett alikuwa amekualika kwao kwa sherehe. Ijapokuwa hukwenda, umekuwa ukiwazia jinsi ambavyo mambo yangekuwa kama ungeenda.

Msichana wa kwanza anakatiza mawazo yako.

“Laiti nisingekuwa na rafiki mvulana,” anasema. “Ningemkubali mara moja.”

Kisha anakutazama kwa mshangao. Unajua tu atakuuliza nini.

“Na wewe, mbona huna rafiki mvulana?” anakuuliza.

Hupendi hata kidogo swali hilo! Ukweli ni kwamba ungependa kuwa na rafiki mvulana. Lakini umeambiwa unapaswa kungoja hadi utakapokuwa tayari kuolewa. Kama si  . . .

“Ni dini yenu, sivyo?” yule msichana wa pili anasema.

‘Amejuaje nilichokuwa nikifikiria?’ unawaza moyoni.

“Wewe nawe, ni Biblia, Biblia, Biblia kila siku,” asema kwa dhihaka. “Kwa nini usifurahie maisha kidogo tu wakati mwingine?”

UMEWAHI kudhihakiwa kwa sababu ya kujitahidi kuishi kulingana na viwango vya Biblia? Ikiwa ndivyo, huenda umekuwa ukijiuliza ikiwa kuna kitu fulani unachokosa. Msichana anayeitwa Deborah alihisi hivyo. Anakumbuka, “Niliona viwango vya Biblia vinaninyima mambo mengi. Nilitamani uhuru ambao wanafunzi wenzangu walikuwa nao.”

Ukweli wa Mambo

Si lazima sikuzote upotee njia ndiyo ujue njia. Kujifunza kutokana na makosa ya wengine ni jambo zuri na linapatana na Maandiko. Ndivyo alivyofanya mtunga-zaburi Asafu. Wakati fulani, aliona viwango vya Mungu vinamnyima mambo mengi. Lakini alipochunguza maisha ya wale walioacha njia za Mungu alijionea ukweli wa mambo. Baadaye Asafu alikata kauli kwamba walikuwa “kwenye udongo unaoteleza.”—Zaburi 73:18.

Ukitafakari hayo, fikiria maelezo yanayofuata ya vijana ambao wakati fulani waliacha viwango vya Biblia na kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa.

● Ni mambo gani yaliyochochea fikira na matendo yako?

Deborah: “Nilipokuwa shuleni kila mtu alikuwa na rafiki, nao walionekana kuwa na furaha. Tulipoenda matembezi nao na kuona wakipigana busu na kukumbatiana, niliwaonea wivu na kuhisi upweke. Mara nyingi nilikuwa nikimwazia kwa saa nyingi mvulana fulani niliyempenda. Kufanya hivyo kulizidisha tamaa yangu ya kutaka kuwa naye.”

Mike: “Nilisoma vitabu na kutazama vipindi vilivyohusu ngono. Kuzungumzia ngono pamoja na rafiki zangu kulizidisha tamaa yangu ya kutaka kujaribu. Halafu, nilipokuwa peke yangu na msichana, nilifikiri kwamba ningeweza kumshikashika kimahaba pasipo kufanya ngono naye, na kwamba ningeweza kuacha wakati wowote.”

Andrew: “Nilikuwa na mazoea ya kutazama ponografia (picha za ngono) katika Intaneti. Nilianza kunywa pombe kupita kiasi. Nami nilikwenda katika sherehe pamoja na vijana ambao hawakuheshimu hata kidogo viwango vya Biblia kuhusu maadili.”

Tracy: “Nilijua akilini kwamba ni vibaya kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa, lakini sikuchukia jambo hilo. Sikupanga kuanza kufanya ngono kabla ya ndoa, lakini hisia zangu zilinilemea. Kwa muda fulani, dhamiri yangu haikunisumbua hata kidogo.”

● Je, maisha hayo yalikuletea furaha?

Deborah: “Mwanzoni, nilijiona huru kwelikweli nami nilifurahi kwamba niko sawa na vijana wenzangu. Lakini hisia hizo hazikudumu. Nilianza kujiona mchafu, mwenye hatia, na mtu asiyefaa kitu. Nilijuta sana kwamba nilipoteza ubikira wangu.”

Andrew: “Ilikuwa rahisi zaidi na zaidi kutosheleza tamaa zisizofaa. Lakini wakati huohuo, nililemewa na hisia za hatia na kujichukia.”

Tracy: “Ukosefu wa adili uliniharibia ujana wangu. Nilidhani mimi na mvulana aliyekuwa rafiki yangu tungekuwa na furaha isiyo na kifani. Haikuwa hivyo. Tulisababishiana maumivu, huzuni, na mfadhaiko. Usiku mmoja baada ya mwingine nilikesha kitandani nikilia, na kutamani kwamba laiti ningefuata maagizo ya Yehova.”

Mike: “Nilianza kuhisi kana kwamba nimekufa. Nilijaribu kupuuza matokeo ya matendo yangu kwa wengine, lakini nikashindwa. Niliumia sana kuona kwamba huku nikitafuta kujifurahisha mwenyewe, nilikuwa nikiwaumiza wengine.”

● Ungewapa ushauri gani vijana wanaoona kwamba viwango vya Biblia vinawanyima mambo mengi?

Tracy: “Ishi kulingana na viwango vya Yehova, na ushirikiane na watu wanaofanya vivyo hivyo. Utakuwa na furaha nyingi zaidi ukifanya hivyo.”

Deborah: “Usijifikirie mwenyewe tu, au mambo unayotaka. Matendo yako yatawaathiri wengine. Ukipuuza shauri la Mungu, utajiletea msiba.”

Andrew: “Kwa sababu ya kukosa ukomavu, unafikiri kwamba maisha ya vijana wenzako yanafurahisha. Mitazamo yao inaweza kukuambukiza. Kwa hiyo chagua rafiki zako kwa hekima. Mtegemee Yehova, nawe utajiepusha na majonzi mengi.”

Mike: “Baadhi ya vitu vyenye thamani sana ambavyo Yehova amekupa ni kujiheshimu na dhamiri safi. Kutupa zawadi hizo kwa sababu tu huwezi kujizuia ni kujidharau. Zungumza na wazazi wako na watu wengine wakomavu kuhusu matatizo yako. Ukifanya kosa, usisite kulifunua na kurekebisha hali hiyo. Ukifuata maagizo ya Yehova, utapata amani ya kweli.”

Viwango vya Biblia—Pingu au Mkanda wa Usalama?

Yehova ni “Mungu mwenye furaha,” na anataka wewe pia uwe na furaha. (1 Timotheo 1:11; Mhubiri 11:9) Viwango vilivyo katika Biblia vinaweza kukunufaisha. Ni kweli kwamba huenda ukaviona kama pingu zinazokunyima uhuru. Lakini kwa kweli, kanuni za maadili zilizo katika Biblia ni kama mkanda wa usalama unaomlinda abiria asipatwe na madhara.

Bila shaka unaweza kuitumaini Biblia. Ukiamua kuishi kulingana na viwango vyake, utamfurahisha Yehova na wakati uleule utajiletea baraka.—Isaya 48:17.

KATIKA SURA INAYOFUATA

Unaweza kuwa rafiki ya Mungu. Soma uone jinsi hilo linavyowezekana.

MAANDIKO MUHIMU

“Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.”—Isaya 48:17.

PENDEKEZO

Fikiria jinsi unavyoweza kumsadikisha mdogo wako aone hekima ya kufuata viwango vya Biblia. Kuzungumza kuhusu imani yako ni njia nzuri sana ya kukusaidia kujenga imani hiyo moyoni mwako.

JE, WAJUA . . .?

Kwa muda mfupi tu unaweza kuharibu uhusiano wako na Yehova, lakini huenda ikakuchukua miaka mingi kuurekebisha.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Kitakachonisaidia kuona faida ya kufuata viwango vya Biblia ni ․․․․․

Nikianza kuwaonea wivu wale wanaoishi kulingana na viwango vya ulimwengu, nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kuhusu matokeo mabaya ya kutotii sheria za Mungu, kwa nini si lazima upotee njia ndio ujue njia?

● Umejifunza nini kutokana na maelezo ya Deborah, Mike, Andrew, na Tracy?

● Kwa nini huenda watu fulani wakaona viwango vya Biblia kama pingu zinazowanyima uhuru, lakini kwa nini maoni hayo yana kasoro?

[Blabu katika ukurasa wa 285]

‘‘Huwezi kulinganisha wasiwasi wa kuogopa kuadhibiwa na maumivu yanayotokana na kuficha kosa.’’—Donna

[Picha katika ukurasa wa 288]

Viwango vya Biblia havikunyimi furaha; vinakulinda

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki