Viwango vya Yehova Vinatusaidia
“Akujalie kwa kadiri ya haja ya moyo wako, na kuyatimiza mashauri yako yote.”—ZABURI 20:4.
1. Ni viwango vya namna gani vilivyoko kwa wingi? (Kumbukumbu la Torati 25:15)
MWAKA wa 1266 Mfalme Henri wa Tatu wa Uingereza aliagiza kwamba peni moja la pesa liwe sawa na uzito wa chembe 32 za ngano. Kwa njia hiyo aliweka kiwango. Vivyo hivyo, vitu vingi sana vinavyotuzunguka vinahusu viwango. Tunapofungua redio au televisheni yetu tunaifungua katika mahali fulani pasipogeuka-geuka saa zote ili tupate matangazo. Viwango vingine vinaonyesha ustadi wa mtu; uwezo wa kusoma wa mwanafunzi unaweza kupimwa kwa kutumia mtihani uliowekewa kiwango fulani.
2. Ni viwango vya namna gani nyingine visivyokuwako kwa wingi, na kwa sababu gani?
2 Lakini, viwango vya maadili na mwenendo ndivyo vya maana zaidi. Bila hivyo, viwango vya ile namna ya kwanza ni kazi-bure. Kwa mfano, baraza la kuchunguza elimu ya juu lilikuta kwamba kati ya wanafunzi 25,000 karibu asilimia 50 (%) walisema wenzao walipita mtihani kwa kutumia udanganyifu, si kwa kujifunza. Namna gani juu ya viwango vya watu katika afisi za serikali? Je! vijana wa leo wanaweza kujifunza viwango vya maadili kwa viongozi walio wengi? Barbara Tuchman mwenye kuchunguza mambo ya kihistoria alieleza hivi: “Uongozi wa kiadili umeachiliwa bila kutunzwa katika maana ya kwamba kwa ujumla watu hawataki kutaja viwango vinavyopasa kufuatwa.”
3. Kwa sababu gani tumtazamie Yehova awe ana viwango vya adili?
3 Hata hivyo, namna gani juu ya Yehova Mungu? Yeye ana viwango, sawa na vile baba wa kibinadamu anavyoweza kuwa ameweka viwango na matakwa ya kufuatwa na jamaa katika mwenendo wao nyumbani na katika kushughulika na wengine. Yehova, yule Mwamuzi wa ulimwengu mzima, Mpaji-Sheria na Mfalme, anatia katika sheria za Biblia kanuni zilizotajwa waziwazi za kuonyesha viwango vya adili ambavyo ameweka na mambo anayotazamia wanadamu watimize, yaani, miongozo ya kutuonyesha tunavyopaswa kutembea.—Zaburi 25:4, 5; 86:10, 11; Isaya 33:22.
4. Kwa sababu gani inatupasa tutake kujua sababu ya kukubali viwango vya Mungu?
4 Ni nani kati yetu angekataa akisema kwamba viwango vya Yehova havina ubora? Huenda tusikatae. Lakini huenda tukavisukumia mbali wakati vinapopingana na tamaa fulani ya kibinafsi tuliyo nayo. Huenda tukapunguza uzito wa viwango vyake au tukawa na maoni ya kwamba hali yetu ni tofauti na kwa hiyo haiko kati ya hali zinazopasa kufuata viwango hivyo. Au huenda tukawa na maoni ya kwamba hali hiyo inahitaji sheria zilizowekwa zigeuzwe kidogo zilingane nayo. Hivyo, acheni turudie kujikumbusha sababu fulani zinazotupa wajibu wa kukubali viwango vya adili vya Mungu na namna tunavyoweza kufaidika navyo.
Viwango vya Mungu Vinapolinganishwa na vya Mwanadamu
5, 6. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mambo aliyoyatimiza Yehova wakati wa siku sita za kwanza za kuumba?
5 Zilipokwisha siku sita za kuumba, Mungu aliitangaza kazi yake kuwa ‘njema sana.’ (Mwanzo 1:31) Kila kitu kilikuwa kimeumbwa kwa kufuata utaratibu mzuri na hakuna kilichokuwa na kasoro. Mimea na wanyama waliumbwa wakiwa katika hali zenye kuwafaa kabisa kabisa, vikawa ni viumbe vyenye kuzaa kufuatana na namna yavyo, wala havikuwa na uhitaji wa kugeuka viwe namna nyingine mpya. (Mwanzo 1:25) Jiulize mwenyewe, Ni mtu gani au ni kitu gani ambacho Yehova alilazimika kushauriana nacho ili apate mielekezo katika kazi hiyo ya kuumba? Ni wazi kwamba ndani yake mwenyewe alikuwa na maarifa na hekima ya kufanya uumbaji wote. Zaidi ya kujua kuufanya, yeye aliufanya kikamilifu pia, kwa njia iliyoweka viwango vya kufuatwa na vitu vinavyoonekana. (Isaya 40:12-14) Kwa sababu ya viwango vya Mungu tunaweza kupanga katika jamii-jamii na kutambua namna nyingi sana sana za mimea, samaki, ndege na wanyama wa nchi kavu.
6 Wakati mmoja Yehova alitokeza maulizo fulani yanayoweza kutusaidia tulinganishe maarifa yake, uwezo wa kufanya mambo mbalimbali na viwango vyake pamoja na viwango vya mwanadamu. Mungu alimwuliza Ayubu hivi: “Ulikuwa wapi nilipoiweka misingi ya nchi? Haya! sema, kama ukiwa na ufahamu.” Kile ambacho wanasayansi wanaweza kufanya ni kutoa tu makadirio yasiyo na uhakika kamili ya muda ambao umepita tangu ulimwengu mzima ulipoanza kuwako. Ni wazi wanadamu hawakuwako Mungu alipoiumba dunia. Basi hawajui aliiumba wakati gani na namna gani. “Je!” Mungu akauliza, “umeiamuru asubuhi tangu siku zako zilipoanza? Umeyajulisha mapambazuko mahali pake?” Wataalamu wa fizikia wanachunguza mzunguko wa dunia, wanajaribu kuigiza mchanganyiko wa joto ambao jua letu linatumia kutokeza nishati inayoendeleza uhai wa vitu, tena wanafanya kazi ngumu wakitumia maelezo yaliyo magumu kufahamika ili wajulishe watu namna nuru ilivyo, ijapokuwa nuru ni kitu cha kawaida tu. Mambo ambayo wametimiza yanaonekana kuwa namna gani yanapolinganishwa na ya Mungu? Yehova aliendelea kuuliza: ‘Umezijua amri zilizoamuriwa mbingu? Waweza kuiinua sauti yako mpaka mawinguni, ili wingi wa maji ukufunikize? Waweza kuutuma umeme, nao ukaenda?’ Mwishowe Ayubu alikubali hivi: “Tazama, mimi si kitu kabisa, nikujibu nini?” “[Nimepata kujua] ya kuwa waweza kufanya mambo yote, na ya kuwa makusudi yako hayawezi kuzuilika.” Je! wewe binafsi una maoni ayo hayo?—Ayubu 38:4, 12, 33-35; 40:4; 42:2.
7, 8. Wewe kiumbe cha kibinadamu unatoaje ushuhuda wa kuonyesha mambo yaliyotimizwa na Mungu?
7 Kiumbe cha Mungu cha kidunia kilichomalizia uumbaji wake kwa uzuri sana ni mtu. Kamera ya kisasa ya kupigia picha ni kiigizo cha hali ya chini cha kiwango kilicho juu zaidi, yaani, ni kiigizo cha jicho lako. Mfumo wa viungo vyenye kuyeyusha chakula ndani ya mwili wako unapita kitu cho chote ambacho mafundi wanaoshughulika na kemikali na wachunguzi wa vitu vilivyo hai wamepata kutengeneza. Ingawa tunaona namna ya miili yenye maumbo mbalimbali yaliyo mazuri sana, miili yetu inatoa ushuhuda wa viwango vinavyohitajiwa kabisa. Kama daktari-mpasuaji angehitaji kukupasua apendiksi, je! ingekupasa kuwa na wasiwasi kwamba atapata ndani ya tumbo lako vinundu vya kooni (tonsils) au ubongo? Hapana, usawaziko wa viwango vilivyowekwa (katika uumbaji wa Mungu) unawezesha daktari-mpasuaji ajifunze umbo la mwili wa mtu ili aweze kufanya upasuaji ukihitajiwa.
8 Katika fuvu la kichwa chako, si katika tumbo lako, wewe una kompyuta inayoshinda kwa mbali sana kompyuta ya umeme iliyo ya hali ya juu kupita zote katika ujuzi wa kufahamu mambo na katika uwezo wa kutunza kumbukumbu la mambo. Ubongo wako unakuruhusu wewe ushangae na kustaajabia uumbaji wa Mungu, kutia ndani mabilioni ya majua yaliyo katika yale mamilioni ya galaksi (makundi ya nyota) zilizo katika mbingu. Mungu aliimarisha sheria za kuongoza mwendo sahihi kabisa wa maumbo hayo ya kimbingu ili sisi tuweze kuyatumia kama viwango vya kuhesabia wakati wetu, mchana na usiku, majira na miaka.—Mwanzo 1:14; Zaburi 8:3, 4.
9. Kwa kulinganisha mambo yaliyotimizwa na Mungu na kanuni alizo nazo pamoja na zile za mwanadamu, tunaweza kukata shauri gani?
9 Linganisha mambo ambayo Mungu ametimiza na yale ambayo mwanadamu amefanya. Ijapokuwa serikali zimesimamisha viwango vya namna zote vya kuongozea watu, wanadamu wamechafua maji na hewa, wakamaliza kabisa namna nyingi sana za wanyama wa pori, wakagawanya watu kisiasa, kidini na kikabila, na kuiacha jamaa ya kibinadamu ikiwa na wasiwasi juu ya kama vita, uchafuzi au kukosa chakula kunaweza kufagilia mbali uhai wa kibinadamu umalizike duniani. Basi ni wazi kwamba Mungu hakuwa akitia chumvi aliposema hivi juu ya mwanadamu: “Kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.” (Isaya 55:9) Basi, je! si jambo linalofaa kwamba badala ya kutegemea maoni ya kibinadamu juu ya viwango vinavyopasa kutimizwa, inatupasa tutake kujua mielekezo au viwango vya Yehova?—Mithali 16:25; Isaya 30:21.
10. Uumbaji wenye kuonekana unaonyesha nini juu ya kumtegemea Mungu kwa viwango vya adili?
10 Uumbaji unaoonekana unahakikisha kwamba “kazi [yote ya Mungu] ni kamilifu.” Hata hivyo Kumbukumbu la Torati 32:4 linaendelea kutaja sifa za Yehova za adili. Kwa sababu ya mambo ambayo ametimiza na kwa sababu ya viwango vyake vilivyo katika makao yanayoonekana—kuanzia kwenye nyota mpaka kwenye vijisehemu vidogo sana vya atomi, kuanzia kwenye vitu vidogo sana vilivyo hai vinavyoweza kuonwa kwa darubini tu mpaka kwenye miili yetu ya kibinadamu—je! haitupasi tumtegemee yeye tukiwa na uhakika wa kuamini viwango vyake vya adili? Jambo la hakika ni kwamba yeye ameweka viwango bora kabisa vya adili tunavyoweza kufuata tuongoze uhusiano wetu pamoja naye na pamoja na wanadamu wenzetu.—Mika 6:6-8.
11. Ni katika pande gani viwango vya Mungu vinaweza kukufaidi wewe?
11 Yehova hatoi mashauri yanayohusu pande chache tu za maisha yetu, kama vile imani za mafundisho au desturi zilizowekwa rasmi za kidini. Viwango vyake vya adili vinahusu pande zote za maisha, kutia ndani mambo ya kijamaa, namna ya kushughulika na wengine katika biashara, pia maoni na mwenendo unaopasa kufuatwa kuelekeana na wanawake au wanaume, nia inayopasa kufuatwa kuelekea Wakristo wenzetu na ushiriki katika ibada. (Isaya 48:17; Yakobo 1:25) Kwenye Isaya 55:11 Yehova alisema kwamba ‘neno litokalo kwake litafanikiwa.’ Tunaweza kuwa na uhakika uo huo kwamba wakati tunapojitahidi sana kufuata viwango vyake tutapata mafanikio zaidi, tutimize mambo mengi zaidi na kupata furaha nyingi zaidi.
Msaada Kutoka kwa Miongozo Salama na Hakika ya Mungu
12, 13. Tukio fulani la hivi majuzi juu ya afya linahusuje viwango vya Mungu vya adili inayohusu ngono?
12 Tunaweza kupokea msaada kutoka kwenye viwango vya Mungu kwa njia nyingi za moja kwa moja, za kimwili. Kwa mfano, gazeti The New York Times Magazine (Februari 6, 1983) lilitoa habari juu ya ugonjwa mpya ambao ‘wapelelezi wa mambo ya dawa wanauita ugonjwa wa kipuku wenye kuua watu zaidi ya mengine yote.’ Ugonjwa huo ni AIDS (maana: Mchanganyiko wa viini vibaya vinavyoondoa nguvu za mwili za kujikinga na magonjwa). Ugonjwa huo unaacha mwili wa mtu ukiwa katika hali rahisi ya kuingiliwa na namna zisizoonekana mara nyingi za kansa (sarkoma ya Kaposi), ugonjwa wa pumu na magonjwa mengine ya ajabu-ajabu. AIDS ni hatari kiasi gani? Kadiri ya vifo vilivyotukia muda wa miaka miwili inasemwa ni zaidi ya asilimia 65 (%).
13 Wanasayansi wanaamini kwamba ugonjwa wa AIDS unaenezwa kupitia umajimaji unaotokezwa na mwili (hasa shahawa) na damu. Kufika sasa wanaume wengi wenye kulalana na wanaume wenzao wameupata kutokana na ufisadi wao wa ovyo-ovyo, ingawa umeenea pia kwa wanaume na wanawake wenye kufanya ngono pamoja. Mwanamume mmoja mwenye kulalana na wanaume wenzake alikiri hivi: “Iko sawa na kuwa katika wakati wa vita. Hatujui wakati kombora litakapoanguka. Rafiki zangu 18 walikufa mwaka jana na nusu yao waliuawa na AIDS. Wengine 12 ni wagonjwa sana sasa.” Makala hiyo ilisema: “Wagonjwa wengi wa AIDS wanapoendelea kuwa na afya mbaya zaidi, wanaanza kufikiria maisha yao, nyakati nyingine wakijisikia kuwa wanaadhibiwa kwa sababu ya njia zao za maisha ya kutokujali kitu, ya kuishi kwa kusudi la kupata raha tu.” Bila shaka, viwango vya adili vya Mungu, kama vile vinavyotajwa kwenye 1 Wakorintho 6:9, 10, vinatusaidia. Hakika vinatulinda!
14. Ni kwa njia gani nyingine tatizo la ugonjwa wa AIDS linakazia ubora wa viwango vya Mungu? (Kumbukumbu la Torati 12:23-25)
14 Kuna habari zaidi. Ugonjwa wa AIDS umepatikana katika watu wengi wa watu wa visiwa vya Karibea. Dakt. Sheldon Landesman alieleza hivi: ‘Sisi tunajua kwamba mara nyingi wagonjwa wetu huwa wamehusika katika mambo ya uchawi na kupashana habari na ulimwengu wa roho.’ Inaonekana kwamba wanaambukizana ugonjwa wa AIDS wakati wa sherehe hizo za desturi zao. Ugonjwa huo unasemwa pia unapatikana kwa kutiwa damu mishipani na kutokana na vyakula vilivyotengenezwa kwa kutumia damu. “AIDS umekuwa ndicho kisababishi kilicho cha pili kwa kuua watu wenye damu isiyoweza kugandamana ijizuie kutoka kwa wingi mno. Kisababishi cha kwanza ni kutokwa na damu kusikozuilika. Hivi juzi tu, wagonjwa kadha wenye kupasuliwa ambao wametiwa damu mishipani wamepata ugonjwa wa AIDS, jambo hilo likafanya watazamaji wengine wawe na woga wa kwamba taifa linaweza kupungukiwa na akiba ya damu.” Kipindi kinachopita ili viini vya ugonjwa huo vianze maambukizo ni kati ya miezi sita na miaka miwili. Kwa hiyo kufika wakati ambao watu wengine wanakuja kujua kwamba wana AIDS “huenda wakawa wamekwisha kuambukiza mamia ya watu wengine zaidi bila kujua—kupitia ngono, kupitia upaji wa damu kwa waliopungukiwa, au kupitia njia fulani ambayo bado haijawaziwa.” Viwango vya Mungu vinavyokataza uasherati, vyenye kusema kwamba tuepuke kupashana habari na ulimwengu wa roho na ‘kujiepusha na damu’ vinatusaidia tusipatwe na ugonjwa huo na magonjwa mengineyo.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Mithali 5:18-23; Matendo 15:29; 21:25.
15. Kiwango cha Yehova juu ya unywaji wa vileo kinakuwaje chenye msaada?
15 Ili kuona ushuhuda mwingine wa kwamba viwango vya Yehova vinasaidia, kumbuka kwamba yeye anakataza ulevi. Hata anakataza “kutumia mvinyo sana.” (1 Timotheo 3:3, 8; Warumi 13:13) Wengi wanaopuza kiwango cha Mungu wanapatwa na magonjwa yaliyosababishwa au yaliyoongezwa nguvu na kunywa kupita kiasi. Wakristo wengine wamepuza shauri la Paulo la kutumia “mvinyo kidogo” tu, wakaingilia mazoea ya kunywa sana sana ili kinywaji wanachotumia ‘kiwasaidie kupata starehe.’ (1 Timotheo 5:23) Pole kwa pole huenda mtu akasitawisha mazoea ya kutumia vileo (ambayo yanaleta matatizo ya kimwili, kimoyoni na kiadili). Kwa sababu hiyo magumu mengi yanatokea, kutia ndani ukosefu wa heshima, kuwa na migogoro katika jamaa (hata mtengano wa jamaa), kuharibu mapato na kufutwa kazi. Je! viwango vya Mungu vinavyohusu matumizi ya vileo si ulinzi katika upande huo?
16. Viwango vya Mungu vimewapa Mashahidi wa Yehova msaada gani wa kiuchumi?
16 Hata katika mambo ya uwekevu wa pesa viwango vya Mungu vimekuwa vyenye mafaa. Yeye anahimiza Wakristo wawe wanyofu na wafanye kazi kwa bidii. (Waefeso 4:28; Wakolosai 3:23; linganisha Luka 16:10-12.) Habari zinazotoka kote kote duniani zinaonyesha kwamba wengi wa Mashahidi wa Yehova wameendelea na kazi zao huku watu wengine wakifutwa kwa muda, au hata Mashahidi hao wamepandishwa vyeo kwa sababu ya kuwa wanyofu na wenye bidii. Je! wewe unajua mifano ya tukio hilo? Bila shaka, ikiwa mtu ameandikwa kazi hawi na magumu mengi nyakati za matatizo. Mtu akiepuka tabia na mazoea ya kutumia vitu fulani visivyokubaliwa na Maandiko anapata faida za kifedha pia. Habari zaidi juu ya jambo hilo zinapatikana katika sura inayosema “Matatizo ya Kifedha—Kuna Msaada Gani?” ya kitabu Furaha—Namna ya Kuipata.a Bila shaka wewe unaweza kufikiria mifano mingine inayoonyesha viwango vya Mungu vinasaidia watu katika uwekevu wa pesa.
17. Mungu anatoa mwelekezo gani juu ya kutenga watu na ushirika, na kwa sababu gani ni mwelekezo wa hekima?
17 Viwango vya Yehova kuhusiana na kundi la Kikristo pia ni vyenye hekima na msaada. Kwa mfano, Mungu anaelekeza kwamba Mkristo anayefanya mazoea ya dhambi bila kutaka kutubu anapaswa kuondoshwa katika kundi. Wale wengine wanapaswa kuacha ‘kuchangamana na mtu aitwaye ndugu, akiwa ni mzinzi au mwenye kutamani au mwenye kuabudu sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi; mtu wa namna hii wasikubali hata kula naye.’ Ingawa huenda jambo hilo likaonekana kuwa la kukosa upendo kulingana na viwango vya watu fulani, Mungu ndiye mwenye maarifa zaidi. Kuchukua hatua hiyo kunalinda usafi wa kundi, kwa maana “chachu kidogo hulichachusha donge zima.” (1 Wakorintho 5:11, 6) Maelezo ya Dakt. A. L. McGinnis, mwandikaji wa kitabu The Friendship Factor, yanaonyesha hekima ya katazo la Mungu la kwamba tusile pamoja na waliotengwa na ushirika:
“Moja ya njia zilizo bora zaidi za kuongezea urafiki ni kula pamoja. Kuna kautakatifu katika namna fulani katika kumega mkate pamoja na mtu mwingine. Kwa mfano, hujaona kwamba ukila chakula pamoja na adui, inakuwa vigumu sana kwa ninyi wawili kuendelea kuwa maadui?”
18. Kiwango cha Mungu kinaweza kufaidije kuhusu waasi-imani?
18 Kushikilia sana kiwango cha Mungu kunasaidia pia kuzuia uenezaji wa mafundisho na maoni ya uongo. Katika karne ya kwanza, Himenayo na Fileto waligeuka wakawa waasi-imani na kujaribu kupindua imani ya wengine. Kiwango cha Mungu kilisema: ‘Jiepushe na semi hizo zisizo na faida yo yote zinazochafua kilicho kitakatifu.’ (2 Timotheo 2:16-19, NW) Wakristo wenye kushika kiwango hicho wasingalipendezwa na kuwasikiliza waasi-imani hao, wala wasingalipendezwa na kujipatia maandishi yo yote yenye sumu ambayo watu hao wangaliweza kugawa “kwa ajili ya mapato ya aibu.” Mbona wauchangie uovu wao pesa kwa kununua vitabu vyao? (Tito 1:11) Sisi Wakristo washikamanifu na tushike viwango vya Mungu, tulishe akili zetu mambo yaliyo ya kweli na ya uadilifu, tuufuate kwa ushikamanifu na kuthamini kipitio kilichotumiwa kutufunza kweli ya Biblia hapo kwanza.—Linganisha 1 Timotheo 4:16.
19. Ni katika upande gani mwingine viwango vya Yehova vinaweza kutoa msaada?
19 Viwango vya Mungu vinasaidia Mashahidi wa Yehova kwa njia nyingi sana. Katika ndoa vinawatia watu moyo wawe na upendo, heshima na umoja katika wakati huu ambao talaka nyingi sana zinatokea kwa sababu watu hawajali maadili na walioolewa wanapaza sauti za kujitakia uhuru wao wenyewe. Viwango vya Yehova vinasaidia watoto Wakristo wakubali mwelekezo wa wazazi, si kuwa na haraka ya kuasi kama wengi wa wanashule wenzao. Badala ya kuonyesha wanaona uchungu juu ya mamlaka ya wazazi na kuondoka nyumbani wakiwa na umri mdogo na kwenda zao, vijana wanaothamini viwango vya Mungu wanafurahia kufaidika kutokana na mashauri yanayotegemea Biblia na msaada ambao wazazi Wakristo wanaweza kuwapa.—Wakolosai 3:18-21.
Kubali Viwango vya Yehova kwa Utii
20-22. Wewe unahitajiwa ukumbuke nini juu ya viwango vya Mungu?
20 Tungeweza kuzungumza njia nyingine zilizo nyingi sana ambazo kwa kuzifuata viwango vya Mungu vinaweza kutusaidia. Huenda wewe ukawa unakumbuka mambo fulani ya wazi juu ya namna zimekusaidia wewe binafsi. Ni vizuri sana! Kama ni hivyo, ingefaa unapozungumza na Wakristo wale wengine uwaeleze mambo hayo kwa maana ni mazuri na yanatia moyo.
21 Hata hivyo, ni lazima sisi sote tukumbuke ni jambo jepesi sana kuondolewa katika viwango vya Mungu. Lakini kumbuka kwamba Yehova aliwaambia hivi Waisraeli kwenye Mlima Sinai: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu.” Nao wakaitikia kwa shauku hivi: “hayo yote aliyoyasema [Yehova] tutayatenda.” Lakini mwendo katika miaka iliyofuata ulikuwa tofauti kabisa na maneno yao!—Kutoka 19:5, 8; Hesabu 14:1-4, 10.
22 Basi acheni tuvikubali viwango vya Yehova na kuvishika! Hiyo ni kwa sababu mwendo ulio wa hekima na furaha kweli kweli ni kufuata sana viwango visivyolinganika ambavyo Yehova ameweka kutusaidia tuongoze maisha yetu.—Zaburi 19:7-11.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichochapishwa na Sosaiti.
Wewe Unakumbuka?
□ Uumbaji wenye kuonekana unatoa ushuhuda gani kuonyesha Yehova ni chanzo cha viwango?
□ Kwa sababu gani inatupasa tumtegemee Yehova kwa viwango vya adili?
□ Ni mifano gani ambayo wewe ungeweza kutoa uonyeshe namna viwango vya Yehova vinaweza kukusaidia wewe?
□ Wewe una maoni gani juu ya kufuata viwango vya Mungu?
[Sanduku katika ukurasa wa 12]
AIDS—Ugonjwa wa Kipuku wa Miaka ya 1980
“Karibu robo tatu za watu waliokuwa wa kwanza kupata ugonjwa huo wamekwisha kufa. Wachunguzi fulani wanaamini kwamba hakuna mtu anayeweza kuendelea kuwa hai akipatwa nao.” Ugonjwa wenyewe ni AIDS, au mchanganyiko wa viini vibaya vinavyoondoa nguvu za mwili za kujikinga na magonjwa.—Science 83, Machi.
Daktari mmoja alisema: “Uko kama mashine. Ukiisha kuanza, unajua kwamba hautakoma. Unaweza kuona mfumo wa mwili wa kujikinga na magonjwa ukiendelea kuharibika. Utakapokuwa ukimaliza kutibu ambukizo la ugonjwa mmoja, utaona ambukizo la mwingine likitokea. Mgonjwa anakuwa na ugonjwa wa pumu, halafu ugonjwa wa malengelenge, halafu ubongo unaanza kumea vitu visivyofaa, halafu viini fulani vinashambulia uti wa mgongo.” Mmoja wa wagonjwa aliokuwa akitibu alikuwa amekuwa akitumia wakati fulani akiwa bondia na wakati fulani akiwa mcheza tenisi. Pia alikuwa akiinua vyuma vizito. Mwanamume huyo “alikuwa na rafiki msichana ambaye alishikamana naye, na mwanamume mwenyewe alikuwa amelala mwanamume mwenzake mara moja tu miezi sita kabla hajapatwa na ugonjwa huu.” Ikawaje kwake? “Mwanamume huyu alikufa majuma sita baada ya ugonjwa huo kuonekana. Alikufa kwa sababu ya chango kuwa na matundu, akiwa na umri wa miaka 30.”
Ni hatua gani inayochukuliwa kujua ugonjwa wa AIDS unapatikana kwa akina nani, unaanza wakati gani na mahali gani? Vituo vya Uzuiaji wa Magonjwa (CDC) viko Atlanta, Georgia. Tarehe ya Februari 13, 1983, gazeti fulani kuu la Atlanta lilitoa habari hizi: “Hakujapata kuwa na wakati mwingine kama sasa ambao CDC imewapa kazi wafanya kazi wengi namna hii—sasa wanafika karibu 100—kushughulika kwa muda mrefu hivyo na tatizo la afya ya watu. Kazi inayofanywa na kikundi hicho ni moja kati ya shughuli kubwa sana ambazo zimepewa misaada mingi zaidi katika upelelezi wa magonjwa katika historia . . . Ingawa hawana uhakika juu ya kinacholeta ugonjwa huo, wanasayansi wanajaribu kukuza kiini wanachowazia katika wanyama au mirija ya uchunguzi wa kisayansi.” Lakini kwa kuwa ugonjwa wa AIDS unaweza kuchukua kuanzia miezi sita kufikia miaka miwili ndipo uweze kutokea waziwazi kabisa, majaribio ya uchunguzi unaofanywa sasa huenda yasifunue lo lote kabla ya mwaka wa 1985. Kwa sasa, wachunguzi wa CDC wa viini vya magonjwa na wataalamu wao wanaochunguza viini vidogo vilivyo hai ‘wanajisikia kwamba wakati wa sasa hawajakaribia zaidi kugundua kile [kinachosababisha AIDS] kuliko wakati walipoanza utafiti wao zaidi ya mwaka mmoja uliopita.”
Mwezi wa Januari CDC ilifanya mkutano wa kuuzungumza ugonjwa wa AIDS. Kama ilivyosemwa katika jarida linaloitwa Journal of the American Medical Association, Dakt. D. Armstrong wa kituo cha ugonjwa wa kansa kinachoitwa “Memorial Sloan-Kettering Cancer Center” aliuamba mkutano hivi: “Mimi sina shaka kamwe kamwe kwamba ugonjwa wa AIDS unapitishwa kutoka mtu mmoja kwenda kwa mwingine kupitia ngono na vitu vilivyotayarishwa kutokana na damu.” Science 83 kilitoa maoni ya ujumla tu: “Wanasayansi wanafikiri unapitishwa kwa kufanya ‘uhusiano wa karibu sana?—kwa mfano kwa kutumia sindano zilizotumiwa na mtu mwingine kuingiza mishipani dawa za kulevya au kwa kufanya ngono. Jambo hilo linaonyesha kuna kitu fulani kilicho katika damu inayozunguka mwilini. Na basi maafisa wengi wa afya wana wasiwasi juu ya mamilioni ya watu wanaochanga damu na wale wanaoipokea.”
Kwa sasa hakuna njia za kutumiwa ili watu walio na ugonjwa wa AIDS wajulikane, kwa hiyo banki za damu haziwezi kujua ni wachangaji gani wa damu walio na ugonjwa huo. Wazo limetolewa ikasemwa kwamba damu inayochangwa na watu wanaoelekea sana kuwa na ugonjwa huo isikubaliwe, hasa ile ya wanaume wenye kulalana na wanaume wenzao. Lakini wanaume hao wamepiga makelele wakisema kuna ubaguzi na kwamba haki zao zimeingiliwa isivyofaa. (Lakini ni nani anayejali haki za watu wanaopewa damu ya namna hiyo?) Tena, mjumbe wa Kikosi cha Taifa Kinachoshughulika na Ulalanaji wa Wanaume kwa Wanaume aliuambia mkutano huo wa CDC hivi: “Wanaume wengi wanaolalana na wenzao hawakubali kwamba ndivyo walivyo na hawataki kujibu maulizo wanayoulizwa.” Mateto ya namna iyo hiyo yalisikiwa Afrika Kusini wakati wazo lilipotolewa kwamba mambo yasifunuliwe wazi baada ya kifo cha marubani wawili wa kiume wa Shirika la Ndege la Afrika ya Kusini.
Ushuhuda wa karibuni zaidi unaonyesha kwamba wanawake ambao wamefanya ngono na wanaume wenye ugonjwa wa AIDS wanaweza kuupata. Kikundi kingine kipya cha wenye kupatwa na ugonjwa huo ni watoto. Baada ya kuzaliwa, vitoto fulani vilipatwa na ugonjwa huo kwa sababu ya kutiwa damu, kusudi la kuvitia damu likiwa ni kufanya chembe za damu yavyo ya aina ya “Rh” zipatane vizuri, badala ya kukaa zikiwa zimechanganyika na chembe nyingine tofauti zenye kuzivuruga. Huenda ikawa vitoto vingine vilipata kasoro hiyo katika tumbo la uzazi au kutokana na uhusiano wa karibu sana pamoja na mzazi au mtu mwingine mwenye ugonjwa wa AIDS.
Kwa kuwa hesabu ya visa vinavyotajwa imekuwa ikiongezeka mara mbili kila miezi sita, kwa uhakika tutakuwa tukisikia habari nyingi zaidi juu ya huu ugonjwa wa kipuku wenye kuchukiza sana wa miaka ya 1980.—Wagalatia 6:7, 8.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Uumbaji, kuanzia ule mdogo sana mpaka ule mkubwa kabisa kabisa, unashuhudia kwamba Yehova ana uwezo wa kuweka viwango