Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w01 6/1 kur. 4-6
  • Unaweza Kutumaini Viwango vya Nani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Unaweza Kutumaini Viwango vya Nani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Somo Tuwezalo Kujifunza Kutokana na Sheria
  • Kwa Nini Viwango Vinashuka Leo?
  • Kuishi Kupatana na Viwango vya Mungu
  • Viwango vya Yehova Vinatusaidia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Mtumikie Yehova Kulingana na Viwango Vyake vya Juu
    Izingatie Siku ya Yehova Maishani
  • Mema na Mabaya: Uamuzi Unaopaswa Kufanya
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2024
  • Watu wa Yehova Wanapenda Uadilifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
w01 6/1 kur. 4-6

Unaweza Kutumaini Viwango vya Nani?

Mtu mmoja ambaye alikuwa ametembea Afrika kwa mara yawanza alivutiwa na mwanamume aliyekuwa amesimama wima kando ya barabara. Aliona kwamba baada ya kila dakika chache, mtu huyo alisonga kidogo kuelekea upande mmoja akiwa angali amesimama wima. Baadaye mgeni huyo alitambua ni kwa nini mtu huyo alikuwa anafanya hivyo. Alikuwa hasa anajaribu kubaki kwenye kivuli cha nguzo ya waya ya simu. Kivuli hicho kilikuwa kinasonga polepole kadiri jua la alasiri lilivyosonga.

KAMA kivuli cha nguzo hiyo, shughuli na viwango vya wanadamu hubadilika-badilika daima. Kinyume cha hilo, Yehova Mungu, “Baba wa mianga ya kimbingu,” habadiliki. “Kwake yeye hakuna badiliko-badiliko la kugeuka kwa kivuli,” akaandika mwanafunzi Yakobo. (Yakobo 1:17) Nabii Mwebrania Malaki aliandika taarifa ya Mungu mwenyewe: “Mimi BWANA, sigeuki.” (Malaki 3:6, Zaire Swahili Bible) Mungu aliliambia hivi taifa la Israeli wakati wa Isaya: “Mimi ni yuleyule hata katika uzee wenu; hata katika uzee wenu mimi nitawabeba.  . . Nitafanya hivyo.” (Isaya 46:4, Biblia Habari Njema) Kwa hiyo, kupita kwa wakati hakubadili tumaini tulilo nalo katika ahadi za Mweza Yote.

Somo Tuwezalo Kujifunza Kutokana na Sheria

Ahadi za Yehova na pia viwango vyake kuhusu mema na mabaya vinategemeka na havibadiliki-badiliki. Je, ungemtumaini mfanyabiashara anayetumia mizani mbili, moja ikiwa si sahihi? La, hasha. Vivyo hivyo, “mizani ya hadaa ni chukizo kwa BWANA; bali vipimo vilivyo sawasawa humpendeza.” (Mithali 11:1; 20:10) Katika Sheria aliyowapa Waisraeli, Yehova alitia ndani amri hii: “Msifanye yasiyo haki katika hukumu, wala katika kupima, wala katika mizani, wala katika cheo. Mizani ya haki, vipimo vya haki, efa ya haki, hini ya haki, ndivyo mtakavyokuwa navyo. Mimi ndimi BWANA, Mungu wenu, niliyewatoa katika nchi ya Misri.”—Mambo ya Walawi 19:35, 36.

Waisraeli walipata kibali cha Mungu na vilevile faida nyingi za kimwili walipotii amri hiyo. Vivyo hivyo, kufuata viwango vya Yehova visivyobadilika-badilika, sio tu katika kutumia mizani bali pia katika maisha, huletea mwabudu wa Yehova anayemtumaini baraka nyingi. Mungu anatangaza hivi: “Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.”—Isaya 48:17.

Kwa Nini Viwango Vinashuka Leo?

Biblia inaonyesha sababu inayofanya viwango vishuke leo. Ufunuo, kitabu cha mwisho cha Biblia, kinaeleza juu ya vita iliyopiganwa mbinguni, ambayo matokeo yake yameathiri wanadamu wote hadi leo. Mtume Yohana aliandika: “Vita ikatokea ghafula mbinguni: Mikaeli na malaika zake wakapigana na joka kubwa, hilo joka na malaika zalo walipigana lakini halikuweza, wala mahali hapakupatikana mbinguni kwa ajili yao tena. Kwa hiyo likavurumishwa chini hilo joka kubwa mno, nyoka wa awali, yeye aitwaye Ibilisi na Shetani, anayeiongoza vibaya dunia nzima inayokaliwa; akavurumishwa chini kwenye dunia, na malaika zake wakavurumishwa chini pamoja naye.”—Ufunuo 12:7-9.

Matokeo ya papo hapo ya vita hiyo yalikuwa nini? Yohana aliendelea kusema: “Kwa ajili ya hili teremeni, nyinyi mbingu nanyi mkaao ndani yazo! Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameteremka kwenu, akiwa na hasira kubwa, akijua ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufunuo 12:12.

‘Dunia ilipatwa na ole’ wakati Vita ya Kwanza ya Ulimwengu ilipoanza mwaka wa 1914 na kukomesha viwango vya wakati huo ambavyo vilikuwa tofauti sana na vya leo. “Vita Kuu ya 1914-1918 ni kama mpaka unaotenganisha wakati huo na wetu,” asema mwanahistoria Barbara Tuchman. ‘Vita hiyo Kuu ilisababisha vifo vya watu wengi ambao wangetimiza mambo yenye manufaa katika miaka iliyofuata. Iliharibu imani, ikabadili mawazo, na kusababisha madhara ya kudumu ya kukatisha tamaa, hivyo ikafanya kufikiri na mitazamo ya watu iwe tofauti na ilivyokuwa kabla ya vita hiyo.’ Mwanahistoria mwingine, Eric Hobsbawm, ana maoni kama hayo: ‘Tangu mwaka wa 1914, inasikitisha kwamba viwango ambavyo wakati huo vilionekana kuwa vya kawaida katika nchi zilizositawi vimeshuka sana kufikia hali ambayo mababu wetu wa karne ya 19 wangeviita viwango visivyo vya ustaarabu.’

Katika kitabu chake Humanity—A Moral History of the Twentieth Century, mwandishi Jonathan Glover asema: “Jambo moja linalotambulisha wakati wetu ni kuzorota kwa sheria ya maadili.” Japo anatilia shaka sheria za maadili kwa sababu ya kuzorota kwa dini katika nchi za Magharibi, yeye anatoa tahadhari hii: “Wale miongoni mwetu ambao hawana imani na sheria ya maadili ya kidini, bado wanapaswa kutiwa wasiwasi kwa kuzorota kwake.”

Leo, kuvunjwa kwa matumaini na matokeo yake mabaya—iwe ni katika biashara, siasa, au dini au hata katika mahusiano ya kibinafsi na ya familia—ni mojawapo ya mbinu mbovu za Shetani za kuwaletea wakaaji wa dunia ole. Shetani ameazimia kupigana vita hadi mwisho na kujaribu kuona kwamba wale wanaojitahidi kuishi kupatana na viwango vya Mungu wanaharibiwa pamoja naye.—Ufunuo 12:17.

Je, kuna njia ya kusuluhisha kuvunjwa kwa matumaini ambako kumeenea sana? Mtume Petro anajibu: “Lakini ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo tunangojea kulingana na ahadi [ya Mungu], na katika hizo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Tunaweza kutumaini ahadi hiyo kwa sababu Mungu ana uwezo wa kutimiza kusudi lake na pia anatoa uhakikisho wa kutimizwa kwa kusudi hilo. Kuhusu neno lolote ‘litokalo katika kinywa chake’ Yehova asema: “Halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.” Ni ahadi yenye kutumainika kama nini!—Isaya 55:11; Ufunuo 21:4, 5.

Kuishi Kupatana na Viwango vya Mungu

Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuishi kupatana na viwango vya Biblia ingawa wamo katika ulimwengu wenye viwango vinavyobadilika-badilika na vinavyozidi kushuka. Kwa sababu hiyo wao wanakuwa tofauti na watu walio wengi. Mara nyingi jambo hilo linafanya watu wengine wavutiwe na Mashahidi na wengine kuwadharau.

Kwenye mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova huko London, msemaji mmoja aliulizwa na mwandishi wa habari wa televisheni kama kweli Mashahidi wa Yehova ni Wakristo. Alijibu hivi: “Ndiyo, sisi ni Wakristo kwa sababu tunamwiga Yesu. Kuna ubinafsi mwingi ulimwenguni, nasi humwona Yesu Kristo kuwa njia, kweli, na uhai. Tunaamini kwamba yeye ni Mwana wa Mungu na si sehemu ya Utatu, kwa hiyo uelewevu wetu wa Biblia ni tofauti na wa dini maarufu.”

Mahojiano hayo yalipotangazwa na kituo cha televisheni cha BBC, mtangazaji huyo wa habari alimalizia kwa kusema: “Nimejifunza mengi kuhusu sababu inayofanya Mashahidi wa Yehova watutembelee. Ilikuwa mara ya kwanza kuona watu 25,000 waliovalia vizuri na wenye adabu jinsi hiyo, wote wakiwa mahali pale pale, wakati ule ule.” Ni uthibitisho mzuri kama nini kutoka kwa mtu asiye Shahidi kuhusu hekima ya kufuata viwango vya Mungu visivyobadilika!

Ingawa watu wengine huenda wakachukia wazo la kuishi kupatana na viwango ambavyo vimewekwa na wengine, tunakutia moyo uchunguze Biblia yako ujue viwango vya Mungu. Lakini usiridhike na uchunguzi wa kijuujuu tu. Fuata ushauri huu wa mtume Paulo: “Komeni kufanyizwa kulingana na mtindo wa mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe umbo kwa kufanya upya akili yenu, ili mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Tembelea Jumba la Ufalme mahali unapoishi ili uwajue Mashahidi wa eneo hilo. Utaona kwamba wao ni watu wa kawaida tu ambao hutumaini ahadi za Biblia na ambao huonyesha tumaini lao katika Mungu kwa kujitahidi kuishi kulingana na viwango vyake.

Hapana shaka utapata baraka kwa kuishi kupatana na viwango vya Mungu vyenye kutumainika na visivyobadilika-badilika. Tii mwito huu kutoka kwa Mungu mwenyewe: “Laiti ungalisikiliza amri zangu! ndipo amani yako ingalikuwa kama mto wa maji, na haki yako kama mawimbi ya bahari.”—Isaya 48:18.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Leo, matumaini yanavunjwa katika biashara, siasa, dini, na katika mahusiano ya familia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki