Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • bt sura 19 kur. 148-155
  • “Endelea Kusema na Usinyamaze”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Endelea Kusema na Usinyamaze”
  • “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Kazi Yao Ilikuwa ya Kutengeneza Mahema” (Mdo. 18:1-4)
  • “Wakorintho Wengi . . . Wakaanza Kuamini” (Mdo. 18:5-8)
  • “Nina Watu Wengi Katika Jiji Hili” (Mdo. 18:9-17)
  • “Yehova Akipenda” (Mdo. 18:18-22)
  • Akila na Prisila—Wenzi Walio Kielelezo Chema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Neno la Yehova Laenea kwa Nguvu Nyingi!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Kitabu Cha Biblia Namba 46—1 Wakorintho
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • “Mimi Sina Hatia ya Damu ya Mtu Yeyote”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
“Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
bt sura 19 kur. 148-155

SURA YA 19

“Endelea Kusema na Usinyamaze”

Paulo ajitegemeza kimwili na kutanguliza huduma

Matendo 18:1-22

1-3. Mtume Paulo ameenda Korintho kufanya nini, na anakabili changamoto gani?

NI MWISHONI mwa mwaka wa 50 W.K. Mtume Paulo yuko Korintho, jiji tajiri lenye wakaaji wengi Wagiriki, Waroma, na Wayahudi.a Paulo hakwenda kununua wala kuuza bidhaa au kutafuta kazi ya kimwili. Ameenda hapo ili kufanya kazi muhimu zaidi—kutoa ushahidi kuhusu Ufalme wa Mungu. Hata hivyo, Paulo anahitaji mahali pa kuishi, na hataki kuwa mzigo kwa wengine. Hataki mtu yeyote afikiri kwamba anajiruzuku kutokana na neno la Mungu. Atafanya nini?

2 Paulo ana ujuzi wa kutengeneza mahema. Kazi ya kutengeneza mahema si rahisi, hata hivyo, yuko tayari kufanya kazi kwa mikono yake ili ajitegemeze. Je, atapata kazi katika jiji hili lenye shughuli nyingi? Je, atapata mahali pazuri pa kuishi? Ingawa ana mahitaji mengi, Paulo hasahau kamwe kazi yake kuu, kazi ya kuhubiri.

3 Paulo alikaa Korintho kwa muda fulani, naye alipata matokeo mazuri katika huduma yake. Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na utendaji mbalimbali wa Paulo alipokuwa Korintho ambayo yanaweza kutusaidia kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu katika eneo letu?

KORINTHO—JIJI LENYE BAHARI MBILI

Jiji la kale la Korintho lilikuwa kwenye kipande cha eneo kinachounganisha nchi ya Ugiriki na rasi ya kusini inayoitwa Peloponesia. Sehemu nyembamba zaidi ya eneo hilo ilikuwa na upana usiozidi kilomita sita, na kwa sababu hiyo Korintho lilikuwa na bandari mbili. Bandari ya Lekayo, ilikuwa kwenye Ghuba ya Korintho, na ilitumiwa na meli zilizokuwa zikielekea magharibi hadi Hispania, Italia, na Sisili. Na bandari ya Kenkrea, iliyokuwa katika Ghuba ya Saroni, ilitumiwa na meli zinazoenda na zinazotoka eneo la Aegea, Asia Ndogo, Siria, na Misri.

Kwa kuwa kulikuwa na upepo mkali kwenye eneo la kusini la Ugiriki, ilikuwa hatari kusafiri kwa meli. Ndio sababu manahodha walipendelea kutia nanga katika mojawapo ya bandari hizo mbili za Korintho, kisha kusafirisha shehena yao juu ya nchi kavu, na kuipakia tena katika bandari ya pili. Ikiwa meli ilikuwa nyepesi ingeweza kuvushwa kupitia barabara ya pekee kutoka bandari moja hadi bandari nyingine. Kwa sababu ya mahali lilipokuwa, jiji hilo lilitawala biashara za meli pande zote mbili za bahari, mashariki na magharibi, na pia za nchi kavu, kaskazini na kusini. Mbali na utajiri, jiji la Korintho lilikuwa na ufisadi mwingi ambao hupatikana katika bandari nyingi.

Katika siku za Paulo, Korintho lilikuwa jiji kuu la mkoa wa Roma ya Akaya na kituo muhimu cha kuendesha shughuli za serikali. Kulikuwa na dini nyingi sana katika jiji hilo. Kwa mfano kulikuwa na hekalu la kumwabudu Maliki wa Roma, maeneo mengi ya ibada kwa ajili ya kuabudu miungu ya Wagiriki na Wamisri, na pia sinagogi la Wayahudi.​—Mdo. 18:4.

Mashindano ya mbio yaliyofanywa Isthmia kila baada ya miaka miwili yalikuwa ya pili kwa umaarufu, Michezo ya Olimpiki ikiwa katika nafasi ya kwanza. Huenda mtume Paulo alikuwa Korintho mashindano ya mwaka wa 51 W.K. yalipokuwa yakiendelea. Kamusi moja ya Biblia inasema, “haishangazi kwamba Paulo alitumia mfano wa mashindano ya mbio kwa mara ya kwanza katika barua yake kwa Wakorintho.”​—1 Kor. 9:24-27.

“Kazi Yao Ilikuwa ya Kutengeneza Mahema” (Mdo. 18:1-4)

4, 5. (a) Paulo aliishi wapi alipokuwa Korintho, naye alifanya kazi gani ya kimwili? (b) Huenda Paulo alijifunzaje kazi ya kutengeneza mahema?

4 Baada ya kufika Korintho, Paulo alikutana na wenzi wa ndoa wakarimu—Akila mwenye asili ya Kiyahudi, na mke wake, Prisila, au Priska. Akila na Prisila walihamia Korintho kwa sababu Maliki Klaudio aliagiza “Wayahudi wote waondoke Roma.” (Mdo. 18:1, 2) Akila na Prisila walimkaribisha Paulo nyumbani kwao na pia katika kazi yao ya kimwili. Tunasoma: “Kwa sababu [Paulo alifanya] kazi ileile, akakaa nyumbani kwao na kufanya kazi pamoja nao, kwa maana kazi yao ilikuwa ya kutengeneza mahema.” (Mdo. 18:3) Kipindi chote cha huduma yake jijini Korintho, Paulo alikaa nyumbani kwa wenzi hao wenye fadhili na wakarimu. Inawezekana Paulo aliandika baadhi ya barua ambazo baadaye zilikuwa sehemu ya Biblia alipokuwa akiishi nyumbani kwa Akila na Prisila.b

5 Paulo, mtu aliyeelimishwa “miguuni pa Gamalieli,” angewezaje kuwa na ujuzi wa kutengeneza mahema? (Mdo. 22:3) Inaonekana kwamba Wayahudi wa karne ya kwanza hawakuona aibu kuwafundisha watoto wao kazi fulani ya mikono, ingawa watoto hao walipata elimu ya ziada pia. Kwa kuwa alikuwa mwenyeji wa Tarso ya Kilikia, eneo lililojulikana sana kwa sababu ya kitambaa kinachoitwa cilicium kilichotumiwa kutengeneza mahema, inaelekea Paulo alijifunza kazi hiyo alipokuwa kijana. Kazi hiyo ya kutengeneza mahema ilifanywaje? Huenda ilitia ndani kufuma kitambaa cha hema au kukata na kushona kitambaa hicho kigumu ili kutengeneza mahema. Bila shaka, kazi hiyo ilikuwa ngumu sana.

6, 7. (a) Paulo aliionaje kazi ya kutengeneza mahema, na ni nini kinachoonyesha kwamba Akila na Prisila walikuwa na maoni hayohayo? (b) Wakristo leo wanafuataje mfano wa Paulo, Akila, na Prisila?

6 Paulo hakuiona kazi ya kutengeneza mahema kuwa kazi muhimu sana maishani mwake. Alifanya kazi hiyo ili kujitegemeza na lengo lake lilikuwa kuhubiri habari njema “bila gharama.” (2 Kor. 11:7) Akila na Prisila waliionaje kazi yao ya kimwili? Kwa kuwa walikuwa Wakristo, bila shaka walikuwa na maoni kama ya Paulo. Isitoshe, Paulo alipoondoka Korintho mwaka wa 52 W.K., Akila na Prisila waliacha biashara yao na kusafiri pamoja na Paulo hadi Efeso, ambapo nyumba yao ilitumiwa kwa ajili ya mikutano ya kutaniko. (1 Kor. 16:19) Baadaye, walirudi Roma, halafu wakaenda tena Efeso. Wenzi hao wenye bidii walitanguliza Ufalme na walijitoa kwa hiari ili kuwatumikia wengine. Kwa sababu hiyo “makutaniko yote ya mataifa” yaliwashukuru.​—Rom. 16:3-5; 2 Tim. 4:19.

7 Leo, Wakristo hufuata mfano wa Paulo, Akila, na Prisila. Wahubiri wenye bidii leo hufanya yote wawezayo ili ‘wasimpe yeyote kati yetu mzigo wenye gharama.’ (1 The. 2:9) Mapainia wengi wanatuwekea mfano mzuri kwa kufanya kazi kwa siku kadhaa katika juma au miezi fulani katika mwaka ili waweze kulipia gharama zao za maisha. Hata hivyo, wanatanguliza kazi ya upainia. Kama Akila na Prisila, watumishi wengi wa Yehova huonyesha ukarimu kwa kuwakaribisha nyumbani kwao waangalizi wa mzunguko. ‘Wakaribishaji wageni’ wanajua kwamba kuwa wakarimu hutia moyo na kujenga.​—Rom. 12:13.

BARUA ZENYE KUTIA MOYO ZILIZOONGOZWA NA ROHO YA MUNGU

Katika kipindi cha miezi 18 ambacho mtume Paulo alikaa Korintho, mwaka wa 50-52 hivi W.K., aliandika barua mbili zilizokuja kuwa sehemu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo—Barua ya Kwanza na ya Pili kwa Wathesalonike. Huenda pia aliandika barua yake kwa Wagalatia wakati huohuo au muda mfupi baadaye.

Barua ya Kwanza kwa Wathesalonike ndiyo maandishi ya kwanza ambayo Paulo aliongozwa na roho kuyaandika. Paulo alitembelea Thesalonike mwaka wa 50 hivi W.K., alipokuwa katika safari yake ya pili ya kuhubiri. Muda mfupi baadaye, kutaniko jipya lililokuwa limeanzishwa lilikumbwa na upinzani uliowalazimu Paulo na Sila kuondoka jijini humo. (Mdo. 17:1-10, 13) Akihangaikia hali ya kutaniko hilo jipya, Paulo alijaribu mara mbili kurudi huko lakini “Shetani aliifunga njia [yake].” Hivyo Paulo akamtuma Timotheo awafariji na kuwaimarisha akina ndugu. Mwishoni mwa mwaka wa 50 hivi W.K., Timotheo aliungana na Paulo jijini Korintho na kumweleza habari njema kuhusu kutaniko la Thesalonike. Kisha, Paulo akawaandikia barua ya kwanza.​—1 The. 2:17–3:7.

Huenda Barua ya Pili kwa Wathesalonike iliandikwa muda mfupi baada ya ile ya kwanza, mnamo mwaka wa 51 hivi W.K. Katika barua zote mbili, Timotheo na Silvano (anayeitwa Sila katika kitabu cha Matendo) walituma salamu zao pamoja na Paulo, na hakuna uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba watu hao watatu walikuwa pamoja tena baada ya wakati huo ambao Paulo alikuwa akikaa Korintho. (Mdo. 18:5, 18; 1 The. 1:1; 2 The. 1:1) Kwa nini Paulo aliwaandikia Wathesalonike barua ya pili? Inaonekana alipata habari zaidi kuhusu kutaniko, labda kupitia mtu aliyemtuma apeleke barua ya kwanza. Habari alizopata zilimchochea Paulo kuwapongeza akina ndugu kwa upendo na uvumilivu wao na pia kurekebisha maoni ya baadhi ya Wathesalonike ya kwamba kuwapo kwa Bwana kumefika.​—2 The. 1:3-12; 2:1, 2.

Kutokana na barua ya Paulo kwa Wagalatia inaonekana alikuwa amewatembelea angalau mara mbili kabla ya kuwaandikia. Mwaka wa 47-48 W.K., Paulo na Barnaba walitembelea Antiokia ya Pisidia, Ikoniamu, Listra, na Derbe, majiji yaliyokuwa katika jimbo la Roma lililoitwa Galatia. Mwaka wa 49 W.K., Paulo alirudi katika eneo hilo akiwa na Sila. (Mdo. 13:1–14:23; 16:1-6) Paulo aliandika barua hii kwa sababu ndugu wa uwongo, waliotokea mara tu baada ya ziara ya Paulo, walikuwa wakifundisha kwamba Wakristo wanapaswa kutahiriwa na kushika Sheria ya Musa. Bila shaka, Paulo aliwaandikia Wagalatia mara tu aliposikia kuhusu mafundisho hayo ya uongo. Huenda aliandika barua hiyo akiwa Korintho, lakini inawezekana pia aliiandika akiwa Efeso, muda mfupi alipofika huko akiwa safarini kurudi Antiokia ya Siria au akitoka Antiokia kwenyewe.​—Mdo. 18:18-23.

“Wakorintho Wengi . . . Wakaanza Kuamini” (Mdo. 18:5-8)

8, 9. Paulo alifanya nini alipopingwa na Wayahudi aliowahubiria, naye alienda kuhubiri wapi?

8 Paulo aliiona kazi ya kimwili kuwa njia ya kumtegemeza katika huduma yake. Hilo lilionekana wazi Sila na Timotheo walipowasili kutoka Makedonia wakiwa na zawadi nyingi. (2 Kor. 11:9) Mara moja, Paulo “akaanza kushughulika sana na lile neno [“alianza kutumia wakati wake wote kwa ajili ya kuhubiri,” Biblia Habari Njema].” (Mdo. 18:5) Hata hivyo, Wayahudi aliowahubiria walimpinga. Alijiondolea lawama kwa sababu walikataa ujumbe unaookoa uhai kumhusu Kristo. Paulo alikung’uta mavazi yake na kuwaambia Wayahudi hao waliompinga: “Damu yenu na iwe juu ya vichwa vyenu wenyewe. Mimi ni safi. Kuanzia sasa nitaenda kwa watu wa mataifa.”​—Mdo. 18:6; Eze. 3:18, 19.

9 Paulo angehubiri wapi? Mtu anayeitwa Titio Yusto, huenda alikuwa Myahudi mgeuzwa imani na ambaye nyumba yake ilikuwa karibu na sinagogi, alimkaribisha Paulo. Hivyo, Paulo akaacha kuhubiri kwenye Sinagogi na kuendelea kuhubiri akiwa kwenye nyumba ya Yusto. (Mdo. 18:7) Paulo aliendelea kuishi katika nyumba ya Akila na Prisila alipokuwa Korintho, lakini aliitumia nyumba ya Yusto kwa ajili ya huduma yake.

10. Ni nini kinachoonyesha kwamba Paulo hakuazimia kuwahubiria tu watu wa mataifa?

10 Paulo aliposema angeenda kwa watu wa mataifa, je alimaanisha hangewahubiria kabisa Wayahudi na Wayahudi wageuzwa imani, kutia ndani wale waliokubali ujumbe wake? Hapana. Kwa mfano, “Krispo, ofisa msimamizi wa sinagogi akamwamini Bwana, yeye pamoja na watu wote wa nyumba yake.” Inaonekana kwamba wengi kati ya wale waliokuwa wakienda katika sinagogi walijiunga na Krispo, kwa sababu Biblia inasema: “Wakorintho wengi waliosikia wakaanza kuamini na kubatizwa.” (Mdo. 18:8) Basi, kutaniko jipya la Kikristo lililoanzishwa jijini Korintho likaanza kukutanika katika nyumba ya Titio Yusto. Ikiwa masimulizi ya kitabu cha Matendo yanafuata mtindo wa Luka—yaani, yanafuatana kulingana na wakati yalipotukia—basi hilo linamaanisha kwamba Wayahudi hao au Wayahudi wageuzwa imani walikuwa Wakristo baada ya Paulo kukung’uta mavazi yake. Ikiwa ndivyo, basi ni wazi kwamba Paulo alikuwa tayari kubadilika kulingana na hali.

11. Mashahidi wa Yehova leo wanafuata mfano wa Paulo jinsi gani wanapowahubiria watu walio katika dini zinazodai kuwa za Kikristo?

11 Leo watu katika nchi nyingi wanadai kwamba wao ni washiriki wa kanisa fulani linalomfuata Kristo. Na makanisa hayo yana uvutano mkubwa katika maisha yao. Wamishonari wa dini hizo wamepata wafuasi wengi. Watu wanaodai kuwa Wakristo mara nyingi huwa watumwa wa desturi, kama walivyokuwa Wayahudi wa karne ya kwanza jijini Korintho. Hata hivyo, kama Paulo, sisi hujitahidi kuwasaidia watu hao waelewe mambo wanayosoma katika Biblia zao. Hata wanapotupinga, au viongozi wao wa kidini wanapotunyanyasa, hatukati tamaa. Huenda kuna wapole kadhaa miongoni mwa watu wenye “bidii kwa ajili ya Mungu, lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” Tunahitaji kuwatafuta wapole hao.​—Rom. 10:2.

“Nina Watu Wengi Katika Jiji Hili” (Mdo. 18:9-17)

12. Paulo alihakikishiwa nini katika maono?

12 Ikiwa Paulo alikuwa na mashaka yoyote kuhusu kuendelea na huduma yake jijini Korintho, mashaka hayo yaliisha Bwana Yesu alipomtokea katika maono ya usiku na kumwambia: “Usiogope, bali endelea kusema na usinyamaze, kwa sababu niko pamoja nawe na hakuna mtu atakayekushambulia ili kukudhuru; kwa maana nina watu wengi katika jiji hili.” (Mdo. 18:9, 10) Hayo yalikuwa maono yenye kutia moyo sana! Bwana mwenyewe alimhakikishia Paulo kwamba angelindwa ili asipatwe na madhara na kuna wengi wanaostahili katika jiji hilo. Paulo alitendaje baada ya kuona maono hayo? Tunasoma hivi: “Akakaa huko kwa mwaka mmoja na miezi sita, akifundisha neno la Mungu kati yao.”​—Mdo. 18:11.

13. Huenda Paulo alikumbuka tukio gani alipokaribia kiti cha hukumu, lakini kwa nini hali yake ingekuwa tofauti?

13 Baada ya kukaa Korintho mwaka mmoja hivi, Paulo alipata uthibitisho zaidi kwamba Bwana angemsaidia. “Wayahudi wakaungana, wakamshambulia Paulo na kumpeleka kwenye kiti cha hukumu,” kinachoitwa beʹma. (Mdo. 18:12) Baadhi ya watu husema kwamba kiti hicho cha hukumu kilikuwa juu ya jukwaa lililokuwa karibu na eneo la katikati ya soko la Korintho. Kiti hicho kilitengenezwa kwa marumaru za rangi ya bluu na nyeupe zilizochongwa vizuri. Eneo la mbele la beʹma lilikuwa kubwa na umati mkubwa wa watu ungeweza kukusanyika hapo. Uvumbuzi wa vitu vya kale unaonyesha kwamba huenda kiti hicho cha hukumu kilikuwa karibu sana na sinagogi, na ikiwa ndivyo, basi hakikuwa mbali na nyumba ya Yusto. Paulo alipokaribia beʹma, huenda alikumbuka jinsi Stefano, ambaye huitwa mfia-imani wa kwanza, alivyopigwa mawe. Paulo, ambaye wakati huo aliitwa Sauli, aliunga mkono “kuuawa kwa Stefano.” (Mdo. 8:1) Je, sasa jambo hilohilo lingempata Paulo? Hapana, kwa kuwa Yesu alimwahidi hivi: “Hakuna mtu atakayekushambulia ili kukudhuru.”​—Mdo. 18:10.

Galio akitupilia mbali kesi ya Paulo mbele ya watu wenye hasira wanaomshtaki. Askari Waroma wakijaribu kutuliza umati wa wanaume wenye hasira.

“Ndipo akawafukuza kutoka mbele ya kiti cha hukumu.”—Matendo 18:16

14, 15. (a) Wayahudi walimshtaki Paulo kwa kosa gani, na kwa nini Galio aliitupilia mbali kesi hiyo? (b) Ni nini kilichompata Sosthene, na huenda baadaye alifanya nini?

14 Ni nini kilichotokea Paulo alipofika kwenye kiti cha hukumu? Hakimu aliyekuwa ameketi juu ya kiti hicho alikuwa liwali Akaya, anayeitwa Galio—kaka ya mwanafalsafa Mroma Seneka. Wayahudi wakamshtaki Paulo: “Mtu huyu anawashawishi watu wamwabudu Mungu kwa njia iliyo kinyume cha sheria.” (Mdo. 18:13) Walidai kwamba Paulo anageuza imani ya watu kinyume cha sheria. Hata hivyo, Galio akaona kwamba Paulo hajafanya “kosa” lolote na hana hatia ya “uhalifu mkubwa.” (Mdo. 18:14) Galio hakuwa na nia yoyote ya kujiingiza katika mizozo ya Wayahudi. Hata kabla ya Paulo kusema neno lolote ili kujitetea, Galio akaitupilia mbali kesi hiyo! Washtaki hao wakakasirika sana. Walimalizia hasira yao kwa Sosthene, ofisa msimamizi wa sinagogi, ambaye huenda alichukua nafasi ya Krispo. Walimkamata Sosthene “na kuanza kumpiga mbele ya kiti cha hukumu.”​—Mdo. 18:17.

15 Kwa nini Galio hakuuzuia umati usimpige Sosthene? Huenda Galio alifikiri kwamba Sosthene ndiye aliyeuchochea umati huo dhidi ya Paulo na kwa hiyo anapata haki yake. Iwe ndivyo ilivyokuwa au la, kulikuwa na matokeo mazuri. Katika barua yake ya kwanza kwa kutaniko la Korintho, iliyoandikwa miaka kadhaa baadaye, Paulo alimtaja mtu fulani anayeitwa Sosthene akimwita ndugu. (1 Kor. 1:1, 2) Je, huyo ni Sosthene yuleyule aliyepigwa jijini Korintho? Ikiwa ndiye, kisa hicho kilimsaidia Sosthene kuukubali Ukristo.

16. Maneno ya Bwana, “endelea kusema na usinyamaze, kwa sababu niko pamoja nawe,” yanatutiaje moyo katika huduma yetu?

16 Kumbuka kwamba baada ya Wayahudi kumpinga Paulo, Bwana Yesu alimwimarisha na kumwambia, “Usiogope, bali endelea kusema na usinyamaze, kwa sababu niko pamoja nawe.” (Mdo. 18:9, 10) Tusisahau kamwe maneno hayo, hasa watu wanapokataa ujumbe wetu. Usisahau kamwe kwamba Yehova anasoma mioyo na huwavuta watu wanyofu kwake. (1 Sam. 16:7; Yoh. 6:44) Jambo hilo linatutia moyo tuendelee kuwa na bidii katika huduma! Kila mwaka, mamia ya maelfu ya watu hubatizwa, hilo linamaanisha kila siku mamia ya watu hubatizwa. Wale wanaotii amri ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ Yesu anawahakikishia hivi: “Mimi nipo pamoja nanyi sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”​—Mt. 28:19, 20.

“Yehova Akipenda” (Mdo. 18:18-22)

17, 18. Huenda Paulo alitafakari nini alipokuwa njiani kuelekea Efeso?

17 Hatujui ikiwa maoni ya Galio kuelekea watu waliomshtaki Paulo yaliliwezesha kutaniko hilo changa la Kikristo jijini Korintho kukaa kwa amani kwa muda. Hata hivyo, Paulo alikaa “siku kadhaa” kabla ya kuwaaga ndugu zake wa Korintho. Mwaka wa 52 W.K., alipanga kusafiri hadi Siria kutoka bandari ya Kenkrea, kilomita 11 hivi upande wa mashariki wa Korintho. Hata hivyo, kabla ya kuondoka Kenkrea, Paulo “alikuwa amekata nywele zake . . . , kwa sababu alikuwa ameweka nadhiri.”c (Mdo. 18:18) Baadaye, aliwachukua Akila na Prisila na kusafiri katika bahari ya Aegea hadi Efeso katika Asia Ndogo.

18 Paulo aliposafiri kutoka Kenkrea, inawezekana alikuwa akitafakari maisha yake jijini Korintho. Alikuwa na kumbukumbu kadhaa nzuri na sababu nyingi za kuridhika. Huduma yake ya miezi 18 jijini humo ilikuwa na matokeo mazuri. Kutaniko la kwanza jijini Korintho lilianzishwa, na lilikutana katika nyumba ya Yusto. Yusto, Krispo na familia yake, na wengine wengi walikuwa waamini. Paulo aliwapenda sana waamini hao wapya, kwa sababu aliwasaidia kuwa Wakristo. Baadaye aliwaandikia barua na kuwaita barua za pendekezo zilizoandikwa moyoni mwake. Sisi pia huwa na uhusiano wa karibu na watu tunaowasaidia kukubali ibada ya kweli. Ni jambo lenye kuridhisha sana kuona ‘barua hizo za pendekezo!’​—2 Kor. 3:1-3.

19, 20. Paulo alifanya nini alipofika Efeso, na tunaweza kujifunza nini kutoka kwake kuhusu kufuatia malengo ya kiroho?

19 Alipofika Efeso, Paulo alianza kazi yake mara moja. “Akaingia ndani ya sinagogi na kujadiliana na Wayahudi.” (Mdo. 18:19) Pindi hiyo, Paulo alikaa Efeso kwa muda mfupi tu. Ingawa aliombwa akae muda mrefu, “hakukubali.” Alipokuwa akiwaaga, aliwaambia Waefeso: “Nitarudi kwenu tena, Yehova akipenda.” (Mdo. 18:20, 21) Paulo alijua kwamba bado kulikuwa na kazi kubwa ya kuhubiri jijini Efeso. Alipanga kurudi, hata hivyo aliamua kuacha mambo mikononi mwa Yehova. Je, huo si mfano mzuri tunaoweza kuiga? Tunapofuatia malengo ya kiroho, lazima tuchukue hatua zinazohitajika. Hata hivyo, lazima sikuzote tutegemee mwongozo wa Yehova na kujitahidi kutenda kupatana na mapenzi yake.​—Yak. 4:15.

20 Akiwaacha Akila na Prisila, Paulo alisafiri baharini hadi Kaisaria. Huenda ‘alipanda’ kwenda Yerusalemu na kulisalimu kutaniko lililokuwa huko. (Mdo. 18:22) Kisha Paulo akarudi nyumbani kwake—Antiokia ya Siria. Alikuwa ameimaliza kwa mafanikio safari yake ya pili ya umishonari. Ni nini kinachomsubiri katika safari yake ya mwisho ya umishonari?

NADHIRI YA PAULO

Andiko la Matendo 18:18 linasema kwamba alipokuwa Kenkrea, Paulo “alikuwa amekata nywele zake . . . , kwa sababu alikuwa ameweka nadhiri.” Hiyo ilikuwa nadhiri ya aina gani?

Kwa kawaida, nadhiri ni ahadi nzito ambayo mtu huweka kwa Mungu kwa hiari, akiahidi kufanya jambo fulani, kutoa toleo, au kuingia katika utumishi fulani. Watu fulani husema kwamba Paulo alikata nywele zake ili kutimiza nadhiri ya Wanadhiri. Hata hivyo, kulingana na Maandiko, baada ya Mnadhiri kumaliza kipindi cha utumishi fulani wa pekee kwa Yehova, alipaswa kunyoa kichwa chake “kwenye mlango wa hema la mkutano.” Inaonekana takwa hilo lingeweza kutekelezwa Yerusalemu wala si Kenkrea.​—Hes. 6:5, 18.

Masimulizi ya kitabu cha Matendo hayataji Paulo aliweka nadhiri yake wakati gani. Huenda hata aliiweka kabla ya kuwa Mkristo. Pia, masimulizi hayo hayataji iwapo Paulo alimwomba Yehova jambo lolote hususa. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kwamba huenda Paulo alikata nywele zake ili “kumshukuru Mungu kwa ulinzi wake, uliomwezesha kutimiza huduma yake huko Korintho.”

a Ona Sanduku lenye kichwa “Korintho—Jiji Lenye Bahari Mbili.”

b Ona Sanduku lenye kichwa “Barua Zenye Kutia Moyo Zilizoongozwa na Roho ya Mungu.”

c Ona sanduku lenye kichwa “Nadhiri ya Paulo.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki