Akila na Prisila—Wenzi Walio Kielelezo Chema
“NISALIMIENI Priska na Akila, watenda kazi pamoja nami katika Kristo Yesu; waliokuwa tayari hata kukatwa kichwa kwa ajili ya maisha yangu; ambao ninawashukuru, wala si mimi tu, ila na makanisa ya Mataifa yote pia.”—Warumi 16:3, 4.
Maneno hayo ya mtume Paulo kwa kutaniko la Kikristo katika Roma yaonyesha staha kubwa na upendo mchangamfu aliokuwa nao kuelekea mume na mke hao. Alihakikisha kwamba hakuwapuuza alipokuwa akiandikia kutaniko lao. Lakini “watenda kazi [hao] pamoja” na Paulo walikuwa nani, na kwa nini walikuwa wapendwa sana kwake na kwa makutaniko?—2 Timotheo 4:19.
Akila alikuwa Myahudi wa diaspora (Wayahudi waliotawanywa) na mwenyeji wa Ponto, eneo katika kaskazini mwa Asia Ndogo. Yeye na mkewe Prisila (Priska) walikuwa wamekaa Roma. Kulikuwa kumekuwa na jumuiya kubwa ya Wayahudi katika jiji hilo angalau tangu Pompei ateke Yerusalemu katika 63 K.W.K., wakati ambapo idadi kubwa ya wafungwa waliongozwa kuelekea Roma wakiwa watumwa. Kwa hakika, maandishi ya Kiroma yafunua kuwako kwa masinagogi 12 au zaidi katika hilo jiji la kale. Wayahudi kadhaa kutoka Roma walikuwapo Yerusalemu kwenye Pentekoste 33 W.K., waliposikia habari njema. Labda ilikuwa ni kupitia wao kwamba ujumbe wa Kikristo ulifikia kwa mara ya kwanza jiji kuu la Milki ya Roma.—Matendo 2:10.
Hata hivyo, Wayahudi walikuwa wamefukuzwa Roma mwaka wa 49 au mapema mwaka wa 50 W.K. kwa amri ya Maliki Klaudio. Kwa sababu hiyo, ilikuwa katika jiji la Kigiriki la Korintho ambapo mtume Paulo alikutana na Akila na Prisila. Paulo alipofika Korintho, Akila na Prisila walimtolea kwa fadhili ukaribishaji-wageni na pia kazi, kwa kuwa walikuwa na kazi ileile—kutengeneza-mahema.—Matendo 18:2, 3.
Watengeneza-Mahema
Hiyo haikuwa kazi rahisi. Kutengeneza mahema kulitia ndani kukata na kushona pamoja vipande vya nguo au ngozi vilivyo vigumu na visivyo laini. Kulingana na mwanahistoria Fernando Bea, ilikuwa “kazi iliyotaka ustadi na uangalifu” kwa upande wa watengeneza-mahema waliofanya kazi kwa kutumia “vitambaa vigumu visivyo napukivu sana, vilivyotumiwa katika kupiga kambi wakati wa kusafiri, vikiandaa kivuli kutoka kwa jua na mvua, au vya kupakia mizigo ndani ya meli.”
Hilo huzusha swali. Je, Paulo hakusema kwamba alikuwa ‘ameelimishwa penye miguu ya Gamalieli,’ hivyo akitayarishwa kufuatia kazi-maisha yenye sifa katika miaka iliyofuata? (Matendo 22:3, NW) Ingawa hilo ni kweli, Wayahudi wa karne ya kwanza waliliona kuwa jambo lenye staha kumfundisha mvulana kazi fulani hata ikiwa angepokea elimu ya ziada. Kwa hiyo yamkini kwamba Akila na pia Paulo walikuwa wamepata stadi zao za kutengeneza-mahema walipokuwa wachanga. Uzoefu huo ulithibitika kuwa wenye kutumika sana baadaye. Lakini wakiwa Wakristo, hawakuona kazi hiyo ya kimwili kuwa kusudi lao kuu. Paulo alieleza kwamba kazi aliyofanya Korintho pamoja na Akila na Prisila ilikuwa tu njia ya kutegemeza utendaji wao mkuu, ule wa kutangaza habari njema bila ‘kumlemea yeyote.’—2 Wathesalonike 3:8; 1 Wakorintho 9:18; 2 Wakorintho 11:7.
Yaonekana, Akila na Prisila walifurahia kufanya yote ambayo wangeweza ili kuendeleza utumishi wa umishonari wa Paulo. Ni nani ajuaye ni mara ngapi rafiki hao watatu walipotua wakati wa kazi yao na kutolea wateja au wapita-njia ushahidi wa vivi hivi! Na ingawa kazi yao ya kutengeneza-mahema ilikuwa ya hali ya chini na yenye kuchosha, walifurahia kuifanya, hata wakifanya kazi “mchana na usiku” ili kuendeleza masilahi ya Mungu—kama vile tu Wakristo wengi wa siku ya kisasa wanavyojitegemeza kwa kazi isiyo ya wakati wote au ya kimsimu ili watoe mwingi wa wakati wao unaobaki katika kuwasaidia watu wasikie habari njema.—1 Wathesalonike 2:9; Mathayo 24:14; 1 Timotheo 6:6.
Vielelezo vya Ukaribishaji-Wageni
Yamkini Paulo alitumia nyumba ya Akila kuwa kitovu cha utendaji wake wa umishonari wakati wa ile miezi 18 aliyokaa Korintho. (Matendo 18:3, 11) Basi, yawezekana kwamba Akila na Prisila walikuwa na furaha ya kuwa pia na Sila (Silvano) na Timotheo wakiwa wageni-waalikwa walipofika kutoka Makedonia. (Matendo 18:5) Zile barua mbili za Paulo kwa Wathesalonike, ambazo baadaye zilikuwa sehemu ya vitabu vya Biblia vinavyokubaliwa, zaweza kuwa ziliandikwa wakati huyo mtume alipokuwa akikaa na Akila na Prisila.
Ni rahisi kuwazia kwamba wakati huo nyumba ya Prisila na Akila ilikuwa kitovu kwelikweli cha utendaji wa kitheokrasi. Labda rafiki wengi wapendwa waliizuru mara nyingi—Stefanasi na familia yake, Wakristo wa kwanza katika mkoa wa Akaya, waliobatizwa na Paulo mwenyewe; Titio Yustasi, aliyemruhusu Paulo atumie nyumba yake ili kutoa hotuba mbalimbali; na Krispo, yule ofisa-msimamizi wa sinagogi, aliyekubali kweli pamoja na wote wa nyumba yake. (Matendo 18:7, 8; 1 Wakorintho 1:16) Kisha kulikuwa na Fortunato na Akaiko; Gayo, ambaye huenda ikawa mikutano ya kutaniko ilifanyiwa nyumbani kwake; Erasto, yule mtumishi wa jiji; Tertio, mwandishi ambaye Paulo alimtumia kuwaandikia Waroma barua; na Fibi, dada mwaminifu wa kutaniko la karibu la Kenkrea, ambaye labda alibeba hiyo barua kutoka Korintho hadi Roma.—Warumi 16:1, 22, 23; 1 Wakorintho 16:17.
Watumishi wa Yehova wa siku ya kisasa ambao wamekuwa na fursa ya kuonyesha ukaribishaji-wageni kwa mhudumu asafiriye wanajua jinsi liwezavyo kuwa jambo lenye kutia moyo na lenye kukumbukwa. Mambo yaliyoonwa yenye kujenga yasimuliwayo kwenye pindi hizo yaweza kuwa chanzo halisi cha burudisho la kiroho kwa wote. (Warumi 1:11, 12) Na, kama Akila na Prisila walivyofanya, wale wanaofungua nyumba zao wazi kwa ajili ya mikutano, labda Funzo la Kitabu la Kutaniko, wana shangwe na uradhi wa kuweza kuchangia kwa njia hiyo maendeleo ya ibada ya kweli.
Urafiki wao na Paulo ulikuwa wa karibu sana hivi kwamba Akila na Prisila waliondoka Korintho pamoja naye katika masika ya mwaka wa 52 W.K., wakiandamana naye hata kufikia Efeso. (Matendo 18:18-21) Walikaa katika jiji hilo na kuwekea msingi ziara ambayo ingefuata ya huyo mtume. Hapo ndipo walimu hao stadi wa habari njema walipomchukua Apolo mwenye ufasaha “kwao” na kuwa na shangwe ya kumsaidia aelewe “njia ya Bwana kwa usahihi zaidi.” (Matendo 18:24-26) Paulo alipozuru Efeso tena wakati wa safari yake ya tatu ya umishonari, wakati fulani karibu na kipupwe cha mwaka wa 52/53 W.K., shamba lililokuwa limelimwa na wenzi hao wenye nishati lilikuwa tayari kwa mavuno. Kwa miaka mitatu hivi, Paulo alihubiri na kufundisha huko juu ya “Njia ile,” huku kutaniko la Efeso likifanya mikutano nyumbani mwa Akila.—Matendo 19:1-20, 26; 20:31; 1 Wakorintho 16:8, 19.
Baadaye, waliporudi Roma, rafiki hao wawili wa Paulo waliendelea “[kufuata] mwendo wa ukaribishaji-wageni,” wakiruhusu nyumba yao itumiwe kwa ajili ya mikutano ya Kikristo.—Warumi 12:13; 16:3-5, NW.
Wao ‘Walikuwa Tayari Hata Kukatwa Kichwa’ kwa Ajili ya Paulo
Labda Paulo aliishi pia na Akila na Prisila alipokuwa Efeso. Je, alikuwa akikaa nao wakati wa ile vurugu ya wafua-fedha? Kulingana na simulizi kwenye Matendo 19:23-31, wale wasanii waliofanyiza vihekalu walipoasi dhidi ya kuhubiriwa kwa habari njema, hao ndugu walilazimika kumzuia Paulo asijihatarishe kwa kwenda mbele ya kikundi cha wafanya-ghasia. Waelezaji fulani wa Biblia wametoa nadharia ya kwamba huenda ikawa ni katika wakati huo barabara wa hatari ambapo Paulo ‘alikata tamaa ya kuishi’ na kwamba Akila na Prisila waliingilia katika njia fulani, ‘wakiwa tayari hata kukatwa kichwa’ kwa ajili yake.—2 Wakorintho 1:8; Warumi 16:3, 4.
“Kishindo kile kilipokoma,” Paulo aliondoka hilo jiji kwa hekima. (Matendo 20:1) Bila shaka Akila na Prisila walikabili pia upinzani na dhihaka. Je, hilo liliwafanya wavunjike moyo? Kinyume na hivyo, Akila na Prisila waliendelea kwa moyo mkuu katika juhudi zao za Kikristo.
Wenzi Wenye Ukaribu
Baada ya utawala wa Klaudio kuisha, Akila na Prisila walirudi Roma. (Warumi 16:3-15) Hata hivyo, mara ya mwisho wanapotajwa katika Biblia, twawakuta Efeso tena. (2 Timotheo 4:19) Tena, kama ilivyo katika marejezo yote mengine katika Maandiko, hao mume na mke wanatajwa pamoja. Walikuwa wenzi wenye ukaribu na wenye muungano kama nini! Paulo hakuweza kumfikiria ndugu huyo mpendwa, Akila, bila kukumbuka ushirikiano mwaminifu wa mke wa Akila. Na ni kielelezo chema kama nini kwa wenzi Wakristo leo, kwa kuwa usaidizi mwaminifu-mshikamanifu wa mwenzi mwenye kujitoa humsaidia mtu kufanya mengi “[katika] kazi ya Bwana” na, nyakati nyingine, hata zaidi ya yale ambayo angeweza kufanya ikiwa angekuwa mseja.—1 Wakorintho 15:58.
Akila na Prisila walitumikia katika makutaniko kadhaa tofauti-tofauti. Kama wao, Wakristo wengi wa siku ya kisasa wenye bidii wamekuwa tayari kuhamia mahali penye uhitaji mkubwa zaidi. Wao wanakuwa pia na furaha na uradhi utokanao na kuona masilahi ya Ufalme yakikua na utokanao na kuweza kukuza urafiki mbalimbali wa Kikristo wenye uchangamfu na wa thamani.
Kwa kielelezo chao chema cha upendo wa Kikristo, Akila na Prisila walipata uthamini wa Paulo na wengine. Lakini la maana hata zaidi, walipata sifa nzuri mbele za Yehova mwenyewe. Maandiko yanatuhakikishia hivi: “Maana Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu, na hata hivi sasa mngali mkiwahudumia.”—Waebrania 6:10.
Huenda tusiwe na fursa za kujitoa wenyewe katika njia zinazofanana na vile walivyofanya Akila na Prisila, hata hivyo twaweza kuiga kielelezo chao chema. Tutakuwa na uradhi wenye kina huku tukitoa nishati yetu na uhai wetu katika utumishi mtakatifu, bila kusahau kamwe “kutenda mema na kushirikiana; maana sadaka kama hizo ndizo zimpendezazo Mungu.”—Waebrania 13:15, 16.