AKILA
(Akila) [kutokana na Kil., linalomaanisha “Tai”].
Myahudi wa asili na mzaliwa wa Ponto iliyo kaskazini mwa Asia Ndogo. Prisila, mke wake na mwandamani wake mshikamanifu anatajwa mara zote pamoja naye. Baada ya kufukuzwa kutoka Roma kwa amri ya Maliki Klaudio dhidi ya Wayahudi kipindi fulani mwaka wa 49 au mapema mwaka wa 50 W.K, walianza kuishi Korintho. (Mdo 18:1, 2) Paulo alipofika Korintho katika majira ya kupukutika ya mwaka wa 50 W.K., kwa fadhili Akila na Prisila walimkaribisha nyumbani mwao. Urafiki wa karibu sana ulisitawi kati yao kadiri walivyofanya kazi pamoja katika biashara yao ya kutengeneza mahema na kadiri Akila na Prisila walivyomsaidia Paulo katika kuliimarisha kutaniko hilo jipya.—Mdo 18:3.
Paulo aliposafiri kwenda Siria mwishoni mwa safari yake ya pili ya umishonari katika masika ya mwaka wa 52 W.K. hivi, Akila na Prisila walisafiri pamoja naye hadi Efeso. (Mdo 18:18, 19) Walibaki Efeso mpaka Paulo alipowaandikia Wakorintho akiwa huko mwaka wa 55 W.K. hivi. Nyumba yao ilitumiwa kama mahali pa kukutania katika eneo hilo kwa ajili ya kutaniko, na walikuwa na pendeleo la kumsaidia Apolo aliyekuwa na ufasaha kuelewa kwa usahihi zaidi njia ya Mungu. (1Ko 16:19; Mdo 18:26) Kufikia mwaka wa 56 W.K. hivi, Paulo alipowaandikia Waroma, utawala wa Klaudio ulikuwa umeisha na Akila na Prisila walikuwa wamerudi Roma, kwa kuwa Paulo alituma salamu zake kwao, akiwaita ‘wafanyakazi wenzake.’ (Ro 16:3) Huko pia, kutaniko lilikutanika katika nyumba yao. (Ro 16:5) Pindi fulani, Akila na Prisila ‘walihatarisha shingo zao’ kwa ajili ya Paulo, na hivyo kustahili shukrani kutoka kwa makutaniko yote. (Ro 16:4) Baadaye walihamia tena Efeso, kwa kuwa Paulo akiwa Roma kabla tu ya kuuawa (karibu na 65 W.K. hivi), alimwomba Timotheo awape salamu zake huko Efeso.—1Ti 1:3; 2Ti 4:19.