Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jr sura 5 kur. 54-66
  • Utachagua Marafiki wa Aina Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Utachagua Marafiki wa Aina Gani?
  • Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UNA MARAFIKI WA AINA GANI?
  • JE, MARAFIKI WAKO NI WATU WASIO NA IMANI?
  • YEREMIA ALICHAGUA MARAFIKI WA AINA GANI?
  • CHAGUA MARAFIKI WAKO KWA HEKIMA
  • “Siwezi Kunyamaza Kimya”
    Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
  • “Nitaishibisha Nafsi Iliyochoka”
    Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
  • “Nimeyatia Maneno Yangu Katika Kinywa Chako”
    Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
  • Yehova Amtuma Yeremia Akahubiri
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
Pata Habari Zaidi
Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
jr sura 5 kur. 54-66

SURA YA TANO

Utachagua Marafiki wa Aina Gani?

1, 2. (a) Kuhusu watu wanaochangamana nao, Wakristo wanakabili hali gani? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na marafiki ambao Yeremia alichagua?

UNGEFANYA nini ikiwa wafanyakazi, majirani, au wanafunzi wenzako wangekualika usherehekee Krismasi pamoja nao? Namna gani ikiwa mkubwa wako kazini angekuambia udanganye au kufanya jambo fulani lisilo halali? Au tuseme kwamba wenye mamlaka wanakuagiza ufanye mambo fulani yanayovunja msimamo wako wa kutokuwamo? Huenda dhamiri yako ikakuonya usifanye lolote kati ya mambo hayo, hata kama kukataa kwako huenda kukafanya udhihakiwe au kutendewa isivyofaa.

2 Kama tutakavyoona, mara nyingi Yeremia alijikuta katika hali kama hizo. Tunaweza kupata faida kwa kuchunguza maisha ya watu ambao Yeremia alishirikiana nao wakati wa huduma yake. Baadhi yao walijaribu kumvunja moyo asitimize mgawo wake. Ijapokuwa Yeremia alilazimika kuchangamana nao, hakuwaona kuwa marafiki wake. Kwa upande mwingine, unaweza kufaidika kwa kuwafikiria wale waliokuwa marafiki wa Yeremia, waliomuunga mkono na kumtia moyo aendelee kuwa mwaminifu. Kwa kweli, kuna mengi tunayoweza kujifunza kutokana na marafiki ambao Yeremia alichagua.

UNA MARAFIKI WA AINA GANI?

3. Sedekia alitaka nini kutoka kwa Yeremia, naye Yeremia alifanya nini?

3 Mara kadha wa kadha, Mfalme Sedekia alitafuta ushauri wa Yeremia kabla ya Yerusalemu kuharibiwa. Kwa nini? Mfalme huyo alitazamia kupata majibu yenye kutia moyo kuhusu wakati ujao wa utawala wake. Alitaka Yeremia atangaze kwamba Mungu ataingilia kati na kukomboa Yuda kutoka kwa maadui wake. Kupitia wajumbe, Sedekia alimsihi Yeremia: “Tafadhali muulize Yehova kwa ajili yetu, kwa sababu Nebukadreza mfalme wa Babiloni anapiga vita juu yetu. Labda Yehova atatutendea kulingana na kazi zake zote za ajabu, hivi kwamba [Nebukadreza] aondoke kwetu.” (Yer. 21:2) Mfalme huyo hakutaka kufuata mwongozo wa Mungu wa kujitia mikononi mwa Babiloni. Msomi mmoja alimfananisha Sedekia na “mgonjwa anayerudi kwa daktari tena na tena ili kuhakikishiwa kwamba atapona, lakini hataki kutumia dawa alizoandikiwa.” Namna gani Yeremia? Angeweza kumfurahisha Sedekia kwa kumwambia alichotaka kusikia. Kwa nini basi Yeremia hakubadili ujumbe wake na kujirahisishia mambo? Alikataa kufanya hivyo kwa sababu Yehova alikuwa amemwambia atangaze kwamba jiji la Yerusalemu litaanguka.—Soma Yeremia 32:1-5.

Picha katika ukurasa wa 54, 55

Unaposoma kuhusu Yeremia na Ebed-meleki, je, unaamini kwamba walikuwa watu halisi? Hivi majuzi, masimulizi ya Yeremia sura ya 38 yanayowataja yaliungwa mkono na machimbuzi mawili yaliyofanywa katika Jiji la Daudi la kale.

Mtaalamu wa vitu vya kale, Eilat Mazar anaripoti kwamba alichimbua kipande cha udongo chenye alama za muhuri. (chini kushoto) Kilipatikana mwaka wa 2005, uchimbuzi wa tabaka la wakati ambapo Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. Kipande hicho kina jina la kale la Kiebrania “Yehuchal ben Shelemyahu,” yaani, “Yukali mwana wa Shelemia” katika Kiswahili.

Baadaye, katika tabaka lingine kama hilo, mita chache tu karibu na lile la kwanza, kipande kingine kilichimbuliwa. (chini kulia) Kipande hicho kina jina “Gedalyahu ben Pashhur,” au “Gedalia mwana wa Pashuri.”

Sasa soma andiko la Yeremia 38:1 lenye majina ya wakuu wawili waliomsihi Mfalme Sedekia aagize Yeremia auawe, njama iliyozuiwa na Ebed-meleki. Ndiyo, wale wanaotajwa katika Yeremia sura ya 38 ni watu halisi.

4. Ni maamuzi gani tunayokabili kuhusu kuanzisha urafiki, kama vile tunapokuwa kazini?

4 Kwa njia fulani, hali yako ni kama ya Yeremia. Huwezi kuepuka kuchangamana na majirani, wafanyakazi, au wanafunzi tunaoweza kuwaita wenzako au waandamani wako. Lakini je, utaanzisha urafiki nao hata ingawa wameonyesha waziwazi kwamba hawataki kusikia au kufuata mwongozo wa Mungu? Yeremia hangeweza kukatiza kabisa ushirikiano wake na Sedekia; hata wakati ambapo Sedekia alikataa kufuata shauri la Mungu, bado ndiye aliyekuwa mfalme. Hata hivyo, haikumaanisha kwamba lazima Yeremia afuate maoni yaliyopotoka ya mfalme au kumpendeza. Ni kweli kwamba kama Yeremia angefanya jinsi mfalme alivyotaka, Sedekia angeweza kumpa zawadi nyingi na kumfaa kwa njia nyinginezo. Badala yake, Yeremia alikataa kushinikizwa kuwa rafiki ya Sedekia. Kwa nini? Kwa sababu Yeremia hakuwa tayari kulegeza msimamo ambao Yehova alikuwa amemwambia achukue. Mfano wa Yeremia unapaswa kutuchochea kuchunguza ikiwa rafiki zetu wanatutia moyo kuwa washikamanifu kwa Mungu. Huwezi kuepuka kabisa kuchangamana na watu wasiomtumikia Mungu—kazini, shuleni, au katika ujirani. (1 Kor. 5:9, 10) Hata hivyo, ukisitawisha urafiki pamoja nao, utahatarisha urafiki wako pamoja na Mungu.

Picha katika ukurasa wa 57

JE, MARAFIKI WAKO NI WATU WASIO NA IMANI?

5, 6. Watu fulani walifanya nini ili kujaribu kumnyamazisha Yeremia?

5 Mbali na Sedekia, wengine pia walijaribu kumshawishi Yeremia kwa njia isiyofaa. Kuhani anayeitwa Pashuri ‘alimpiga’ Yeremia, huenda kwa kuagiza apigwe mapigo 39. (Yer. 20:2; Kum. 25:3) Wakuu fulani wa Yudea walifanya vivyo hivyo kisha wakamfunga Yeremia katika “nyumba ya pingu.” Yeremia alitupwa katika shimo. Akiwa humo, alikuwa katika hali mbaya sana hivi kwamba baada ya siku nyingi alihofu kwamba atafia humo. (Soma Yeremia 37:3, 15, 16.) Kisha baada ya Yeremia kuachiliwa kwa muda, wakuu wengine walianza kumchochea Sedekia amuue. Machoni pao, alikuwa anayadhoofisha majeshi ya Yuda. Kwa sababu hiyo, nabii huyo alitupwa ndani ya tangi lenye matope afie humo. (Yer. 38:1-4) Yeremia aliokolewa asifie humo. Hata hivyo, matukio hayo yanaonyesha jinsi wale ambao walitazamiwa kuwa na imani walivyokosa kuamini mambo ambayo nabii wa Mungu alikuwa akitangaza; nao wakamgeukia.

6 Mbali na watu wenye mamlaka, Yeremia alikuwa na maadui wengine. Pindi moja, wanaume fulani kutoka nyumbani kwa Yeremia, mji wa Anathothi—tunaoweza kuwaita majirani wake—walitisha kumuua ikiwa hataacha kutoa unabii. (Yer. 11:21) Hawakupendezwa na ujumbe wake na kwa sababu hiyo walimtisha. Hata hivyo, badala ya kuwa rafiki ya majirani hao, Yeremia alikuwa alimchagua Yehova kuwa rafiki yake. Wengine walioishi siku zake hawakumtisha kwa maneno tu. Yeremia alipojitwika nira ili kuwasihi Wayahudi wajitwike nira ya mfalme wa Babiloni ili wapate kuendelea kuishi, Hanania alimvua Yeremia nira hiyo na kuivunja. Kulingana na nabii huyo mwongo, Yehova alikuwa amesema: “Nitaivunja nira ya mfalme wa Babiloni.” Hanania alikufa mwaka huohuo. Hivyo basi, si vigumu kujua aliyekuwa nabii wa kweli ni nani kati ya manabii hao wawili. (Yer. 28:1-11, 17) Baada ya Yerusalemu kuharibiwa kama Yeremia alivyokuwa ametabiri, Yohanani na wakuu wengine wa majeshi walikataa kutii amri ya Mungu iliyowataka wabaki Yuda. Walimwambia Yeremia: “Ni uwongo ambao wewe unasema. Yehova Mungu wetu hakukutuma, kusema, ‘Msiingie Misri kukaa humo.’” Walimkaidi Yehova hata zaidi kwa kumchukua kwa nguvu Yeremia na Baruku na kwenda nao Misri.—Yer. 42:1–43:7.

Picha katika ukurasa wa 58

Yeremia alilazimika kushughulika na watu wa aina gani? Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yeremia?

7. Ni hali gani unazokabili zinazofanya iwe vigumu kwako kudumisha uaminifu kwa Yehova?

7 Kwa miaka mingi, Yeremia aliishi katikati ya watu wasio na imani na wapinzani. Fikiria maisha yake. Haikuwa vigumu kufanya urafiki na watu wasiomheshimu Mungu wala Neno Lake. Hao ndio waliokuwa majirani wake. Namna gani wewe? Huenda wewe pia hushughulika na watu kama hao. Iwe wanakupinga wewe na Mungu wako au wanaonekana kuwa watu wazuri kiasi, je, utawachagua kuwa marafiki wako? Je, ingefaa kushirikiana na watu ambao wanapuuza unabii wa Mungu? Kama Yeremia angekuwako leo, je, angekuwa rafiki ya watu ambao maisha yao hayapatani na ukweli wa Neno la Mungu au ambao wanawatumaini wanadamu? (2 Nya. 19:2) Mungu alimweleza Yeremia waziwazi matokeo ya kuwategemea wanadamu badala ya kumtegemea Mungu. (Soma Yeremia 17:5, 6.) Unapotafakari maneno hayo, unahisi namna gani?

Picha katika ukurasa wa 63

8. Ni hali gani zinazowakabili Wakristo katika eneo lenu?

8 Wakristo fulani huonelea kwamba ili kuendeleza biashara au kazi zao wanahitaji kuwaalika wateja wasio Wakristo mara kwa mara. Je, kushirikiana na watu kama hao kwaweza kumfanya Mkristo aanze kuwa na usemi mchafu au kutumbukia katika ulevi? Inaeleweka ni kwa nini Wakristo wengi wanaojikuta katika hali kama hizo wameamua kuepuka mashirika mabaya hata ikiwa kufanya hivyo kutawanyima faida za kimwili. Kwa upande mwingine, huenda mwajiri au wafanyakazi wenzako wasisite kuwatendea wateja isivyo haki. Hata hivyo, Wakristo wa kweli hawafuati upepo. Wakati mwingine si rahisi kufanya maamuzi kuhusu mambo kama hayo. Tunaweza kumwiga Yeremia, ambaye alijiendesha kwa njia iliyomfanya abaki na dhamiri nzuri na uhusiano mzuri pamoja na Mungu.

9. Tamaa ya kutaka kuwa na marafiki inaweza kutokeza hatari gani?

9 Wayudea kadhaa walimdhihaki Yeremia kwa sababu ya msimamo na imani yake. (Yer. 18:18) Hata hivyo, aliazimia kuwa tofauti na watu wa siku zake waliofuata “mwendo unaopendwa na wengi.” (Yer. 8:5, 6) Nyakati nyingine Yeremia ‘aliketi yeye peke yake.’ Aliona afadhali kuwa peke yake kuliko kufanya urafiki na watu ambao wangeweza kumshawishi kufanya mambo yasiyofaa. (Soma Yeremia 9:4, 5; 15:17.) Namna gani wewe? Leo, kama ilivyokuwa katika siku za Yeremia, watu wengi wanaishi maisha yasiyompendeza Mungu. Kwa miaka mingi, watumishi wa Yehova wamekuwa waangalifu sana wanapochagua marafiki. Haimaanishi kwamba Yeremia hakuwa na marafiki. Watu fulani walimtetea na kumuunga mkono. Ni nani hao? Kuwajua kutakusaidia sana.

YEREMIA ALICHAGUA MARAFIKI WA AINA GANI?

10, 11. (a) Yeremia aliongozwa na kanuni gani kuchagua marafiki? (b) Ni nani waliokuwa marafiki wa Yeremia, nasi tunaweza kuuliza nini kuwahusu?

10 Yeremia angefanya urafiki na nani? Akifuata mwongozo wa Yehova hakuacha kuwashutumu waovu, wadanganyifu, wasiotenda haki, wajeuri, wasiojali, na wenye maadili mapotovu—walioacha ibada safi na kuanza kuabudu sanamu, ukahaba wa kiroho. Aliwahimiza Wayudea wenzake: “Geukeni, tafadhali, kila mmoja kutoka katika njia yake mbaya, na mfanye njia zenu na matendo yenu kuwa mema.” (Yer. 18:11) Hata baada ya Yerusalemu kuharibiwa, Yeremia alitangaza “matendo ya fadhili zenye upendo za Yehova” “rehema” na “uaminifu” wake. (Omb. 3:22-24) Yeremia alichagua marafiki miongoni mwa watumishi waaminifu wa Yehova.—Soma Yeremia 17:7.

11 Tunajua baadhi ya marafiki wa Yeremia. Tunajua kwamba Yeremia alishirikiana na Ebed-meleki, Baruku, Seraya, na wana wa Shafani. Swali ni: ‘Walikuwa watu wa aina gani? Walikuwa na urafiki wa aina gani? Kwa nini tunaweza kusema kwamba walikuwa marafiki wazuri? Nao walimsaidia jinsi gani Yeremia kudumisha utimilifu wake?’ Huku tukifikiria hali zetu leo, acheni tuchanganue maswali hayo.

12. (a) Kuna ulinganifu gani kati ya maisha ya Yeremia na ya Baruku, wanaoonekana katika ukurasa wa 58? (b) Seraya ni nani, nasi tunajua nini juu yake?

12 Yaonekana kwamba Baruku, mwana wa Neria ndiye aliyekuwa rafiki mkubwa wa Yeremia. Yeremia alimwamini Baruku naye alimkabidhi jukumu la kuandika jumbe za Yehova kupitia kinywa chake na kuzisoma mbele za watu wote na mbele za wakuu wa Yuda. (Yer. 36:4-8, 14, 15) Sawa na Yeremia, Baruku pia alikuwa na imani kwamba mambo ambayo Mungu alitabiri yangetimia. Wanaume hao wawili walikumbwa na hali ngumu sana wakati wa ile miaka 18 ya mwisho ya taifa la Yuda. Kwa muda mrefu walifanya kazi bega kwa bega katika mgawo wao waliopewa na Mungu. Wote wawili walilazimika kujificha kwa sababu ya maadui. Na kila mmoja wao alitiwa moyo na Yehova. Yaonekana Baruku alitokana na familia mashuhuri ya waandishi katika taifa la Yuda. Maandiko yanamwita Baruku “mwandishi,” na Seraya ndugu yake alikuwa na wadhifa katika serikali. Kama Baruku, baadaye Seraya alimsaidia Yeremia kuwasilisha ujumbe wa kinabii wa Yehova. (Yer. 36:32; 51:59-64) Wana hao wawili wa Neria walijitolea kutumikia pamoja na Yeremia katika kipindi kigumu, jambo lililomwimarisha na kumtia moyo sana. Wewe pia unaweza kuimarishwa na kutiwa moyo kwa kufanya kazi bega kwa bega pamoja na watumishi waaminifu wa Yehova.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na marafiki ambao Yeremia alichagua?

13. Kama inavyoonyeshwa kwenye ukurasa wa 63, Ebed-meleki alithibitisha jinsi gani kuwa rafiki mzuri wa Yeremia?

13 Mwingine aliyekuwa rafiki wa karibu wa Yeremia ni Ebed-meleki. Wakuu wenye hasira walipomtupa Yeremia ndani ya tangi ili afe, Ebed-meleki Mwethiopia, mtu wa taifa lingine, ndiye aliyejasiria kumwokoa. Alikuwa towashi, afisa katika nyumba ya mfalme. Alimwendea Sedekia akiwa ameketi katika Lango la Benyamini. Kwa ujasiri, Ebed-meleki alimwomba Sedekia ruhusa amtoe Yeremia ndani ya tangi lenye matope. Aliandamana na wanaume 30 kufanya kazi hiyo. Huenda alitazamia mapambano makali kati yao na maadui wa Yeremia. (Yer. 38:7-13) Hatujui Ebed-meleki alishirikiana na Yeremia kwa kiasi gani. Kwa kuwa wote wawili walikuwa rafiki za Yehova, tunaweza kukata kauli kwamba walikuwa marafiki pia. Ebed-meleki alijua kwamba Yeremia ni nabii wa Yehova. Alisema kwamba matendo ya wakuu ni “mabaya” naye alikuwa tayari kupoteza hata cheo chake ili kufanya yaliyo sawa. Bila shaka Ebed-meleki alikuwa mtu mzuri. Ndiyo sababu Yehova alimhakikishia: “Nitakukomboa wewe katika siku ile [ya msiba wa Yerusalemu] . . . kwa sababu umenitegemea mimi.” (Soma Yeremia 39:15-18.) Sifa nzuri kama nini! Wewe pia ungependa kuwa na rafiki kama huyo, sivyo?

14. Tunajua nini kuhusu familia ya Shafani na uhusiano wao na Yeremia?

14 Wana watatu na mjukuu wa Shafani walikuwa pia marafiki wa Yeremia. Walitokana na familia za wanaume wenye vyeo. Awali, Shafani alikuwa mwandishi wa Mfalme Yosia. Mwanzoni adui za Yeremia walipotaka kumuua, “mkono wa Ahikamu mwana wa Shafani ndio uliokuwa pamoja na Yeremia, asitiwe mkononi mwa watu.” (Yer. 26:24) Ahikamu alikuwa na ndugu anayeitwa Gemaria. Baruku aliposoma hukumu za Yehova mbele za watu wote, Mikaya, mwana wa Gemaria alimsikia naye akampasha habari baba yake na wakuu wengine. Wakihofia jinsi Yehoyakimu atakavyotenda, walimshauri Yeremia na Baruku wajifiche. Na mfalme alipokataa ujumbe wa Mungu, Gemaria alikuwa kati ya watu waliomsihi mfalme asikiteketeze kitabu hicho cha kukunjwa. (Yer. 36:9-25) Yeremia alimkabidhi Elasa, mwana mwingine wa Shafani, barua yenye unabii awapelekee Wayahudi waliokuwa uhamishoni Babiloni. (Yer. 29:1-3) Katika familia hiyo moja, wana watatu na mjukuu mmoja wa Shafani, watu wanne walimuunga mkono nabii wa Mungu. Haikosi Yeremia aliwathamini sana wanaume hao! Msingi wa urafiki wao haukuwa kwamba wana mapendezi yaleyale katika vyakula, vinywaji, au burudani. Urafiki wao ulitegemea mambo muhimu zaidi.

CHAGUA MARAFIKI WAKO KWA HEKIMA

15. Yeremia alituwekea mfano gani mzuri katika kuchagua marafiki?

15 Tunaweza kujifunza mengi kutokana na jinsi Yeremia alivyoshughulika na watu wa siku zake, wabaya na wazuri. Mfalme, wakuu wengi, manabii wa uwongo, na majemadari walimshinikiza abadili ujumbe wake. Hata hivyo, Yeremia hakulegeza msimamo wake. Msimamo wake uliwachukiza, hata hivyo, Yeremia hakuwa akitafuta urafiki wao. Yehova ndiye aliyekuwa rafiki yake mkubwa. Yeremia aliazimia kuwa mwaminifu kwa Mungu hata ikiwa angechukiwa. (Soma Maombolezo 3:52-59.) Na kama ambavyo tumeona, Yeremia hakuwa peke yake katika azimio lake la kumtumikia Yehova.

16, 17. (a) Mtumishi wa Yehova anaweza kupata msaada gani kutoka kwa rafiki mzuri? (b) Katika nchi yoyote unamoishi, unaweza kupata wapi marafiki wazuri?

16 Ebed-meleki alikuwa rafiki mzuri kwa sababu ya imani yake na kumtegemea Yehova. Alitenda kwa ujasiri ili kumwokoa Yeremia. Baruku naye alitumia muda mwingi pamoja na Yeremia akimsaidia kuwasilisha ujumbe wa Yehova. Marafiki wa kweli katika kutaniko la Kikristo leo waweza kuwa wenye thamani kama wanaume hao walivyokuwa. Cameron, painia wa kawaida mwenye umri wa miaka 20, anathamini msaada aliopata kutoka kwa Kara, ambaye pia ni painia. Cameron anasema, “Kara alinitia moyo kumtanguliza Yehova maishani, kupitia maneno na matendo yake.” Ingawa kila mmoja wa dada hao anaishi mbali, Kara alikuwa akimpigia simu au kumwandikia barua Cameron kwa ukawaida ili kumjulia hali na kumtia moyo. Cameron akumbuka: “Alijua kila kitu kuhusu familia yetu. Alijua jinsi nilivyovunjika moyo dada yangu alipoasi na kuacha kweli. Alikuwa rafiki wa kweli, nami sijui ningefanya nini pasipo msaada wake na maneno yake yenye kutia moyo. Amenitegemeza sana.”

Picha katika ukurasa wa 64

17 Unaweza kupata marafiki wazuri katika kutaniko la Kikristo, wawe ni wa rika lako au hapana. Ndugu na dada zako wana imani, maadili, na matumaini kama yako, wanampenda Yehova kama wewe na huenda hata wamekumbwa na hali kama zako maishani. Unaweza kufanya kazi pamoja nao bega kwa bega katika huduma ya Kikristo. Wanaweza kukutia moyo wakati wa shida, nawe pia, unaweza kuwatia moyo. Watashangilia pamoja nawe unapofurahia utumishi wako kwa Yehova. Isitoshe, urafiki wa aina hiyo unaweza kudumu milele.—Met. 17:17; 18:24; 27:9.

18. Tunaweza kujifunza nini kutokana na marafiki ambao Yeremia alichagua?

18 Bila shaka tunaweza kujifunza mengi kutokana na marafiki ambao Yeremia alichagua. Kumbuka ukweli huu: Huwezi kufanya urafiki na watu ambao imani yao inapingana na mafundisho ya Biblia na bado usimame imara. Kutenda kupatana na ukweli huo ni muhimu leo kama ilivyokuwa siku za Yeremia. Ili kutimiza mgawo wake kwa uaminifu na kupata baraka za Yehova, Yeremia alikuwa tayari kuwa tofauti na watu wengi wa siku zake. Je, ndivyo ilivyo kwako pia? Yeremia alichagua marafiki wenye imani kama yake na waliomsaidia kutimiza mgawo wake. Kila Mkristo mwaminifu leo anaweza kujifunza kutoka kwa Yeremia jinsi ya kuchagua marafiki kwa hekima!—Met. 13:20; 22:17.

Unaweza kufuata mfano wa Yeremia jinsi gani unapochagua marafiki?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki