Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • rk seh. ya 5 kur. 12-14
  • Kuthamini Sifa za Mungu Zisizo na Kifani

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuthamini Sifa za Mungu Zisizo na Kifani
  • Imani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nguvu Zake Hazina Mipaka
  • Mungu Mwenye Haki
  • Mungu Mwenye Hekima
  • “Mungu Ni Upendo”
  • Mkaribie Mungu
  • “Tazama, Huyu Ndiye Mungu Wetu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Mungu Ana Sifa Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu Wote)—2019
  • Je, Kweli Unaweza ‘Kumkaribia Mungu’?
    Mkaribie Yehova
  • Mtu Aweza Kuwaje Katika Mfano wa Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
Pata Habari Zaidi
Imani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
rk seh. ya 5 kur. 12-14

Sehemu ya 5

Kuthamini Sifa za Mungu Zisizo na Kifani

MAANDIKO Matakatifu hufunua sifa nyingi nzuri za Mungu na kutusaidia kumjua. Kwa mfano, Maandiko hutuambia kuhusu sifa nne kuu za Mungu—nguvu, haki, hekima, na upendo. Acheni tuchunguze kila moja ya sifa hizo.

Nguvu Zake Hazina Mipaka

Mwanamume akitazama anga lenye nyota nyingi

Mungu ana nguvu nyingi

Yehova alimwambia Abrahamu: “Mimi ni Mungu Mweza-Yote.” (Mwanzo 17:1) Nguvu zake hazina kifani, hazina mipaka, wala haziwezi kwisha. Mungu aliumba ulimwengu wote mzima kwa nguvu zake.

Mungu hatumii nguvu zake vibaya kamwe. Sikuzote anazitumia kwa njia inayofaa na kwa kusudi. Anatumia nguvu zake kwa njia inayopatana kabisa na sifa yake ya haki, hekima, na upendo.

Yehova hutumia nguvu zake kuwasaidia watumishi wake waaminifu. “Macho yake yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.” (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Je, huvutiwi na Mungu huyo mwenye nguvu nyingi lakini mwenye kujali?

Mungu Mwenye Haki

“Yehova ni mpenda-haki.” (Zaburi 37:28) Sikuzote yeye hufanya yaliyo sawa na haki kulingana na viwango vyake vikamilifu.

Watu kutoka mataifa mbalimbali wenye umri tofauti-tofauti

Mungu hana ubaguzi

Mungu huchukia ukosefu wa haki. ‘Hamtendei yeyote kwa upendeleo wala hakubali rushwa.’ (Kumbukumbu la Torati 10:17) Huwapinga wanaowakandamiza wengine, naye hutenda kwa niaba ya wanaoonewa, kutia ndani ‘mjane yeyote au mvulana asiye na baba.’ (Kutoka 22:22) Mungu huwatendea wanadamu wote bila ubaguzi. “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Matendo 10:34, 35.

Haki ya Yehova imesawazishwa kikamili. Yeye hawaendekezi watu wala si mkali kupita kiasi. Huwaadhibu wakosaji wasiotubu lakini huwaonyesha rehema wanaotubu. “Yehova ni mwenye rehema na mwenye neema, si mwepesi wa hasira na ni mwingi wa fadhili zenye upendo. Yeye hataendelea kutafuta makosa wakati wote, wala hataendelea kuweka kinyongo mpaka wakati usio na kipimo. Hakututendea kulingana na dhambi zetu; wala kuleta juu yetu kile tunachostahili kulingana na makosa yetu.” (Zaburi 103:8-10) Pia, Mungu hukumbuka na kuwapa thawabu watumishi wake washikamanifu. Je, hupaswi kumtegemea Mungu huyu mwenye haki?

Mungu Mwenye Hekima

Mwanamume ameshika maandiko Matakatifu

Maandiko Matakatifu yana hekima ya Mungu

Yehova ndiye chanzo cha hekima yote. “Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi!” (Waroma 11:33) Hekima yake haina kifani na haina mwisho.

Hekima ya Mungu inaonekana waziwazi katika uumbaji. Mtunga-zaburi alisema: “Jinsi kazi zako zilivyo nyingi, Ee Yehova! Zote umezifanya kwa hekima.”—Zaburi 104:24.

Hekima ya Mungu inafunuliwa pia katika Maandiko Matakatifu. Mfalme Daudi aliandika: “Kikumbusho cha Yehova ni chenye kutegemeka, humfanya asiye na uzoefu awe na hekima.” (Zaburi 19:7) Hebu wazia—unaweza kujifunza kutokana na hekima ya Mungu isiyo na mipaka! Je, utafanya hivyo?

“Mungu Ni Upendo”

Sifa kuu ya Yehova ni upendo. Maandiko yanasema: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Upendo huchochea na kuongoza kila anachofanya.

Mungu hutuonyesha upendo kwa njia nyingi. Yeye hutupa vitu vizuri. “Alitenda mema, akiwapa ninyi mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo yenu kikamili kwa chakula na uchangamfu.” (Matendo 14:17) Bila shaka, “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu hutoka juu, kwa maana hushuka kutoka kwa Baba wa mianga ya mbinguni.” (Yakobo 1:17) Kupitia zawadi yenye thamani sana ya Maandiko, Mungu hutufunulia kweli kumhusu na kuhusu sheria na kanuni zake zenye upendo. Yesu alisali hivi: “Neno lako ni kweli.”—Yohana 17:17.

Milima

Hekima ya Mungu inayoonekana katika uumbaji hutuchochea kumheshimu

Pia, Mungu hutusaidia tunapopata matatizo. “Mtupie Yehova mzigo wako, Naye mwenyewe atakutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.” (Zaburi 55:22) Mungu hutusamehe dhambi zetu. “Wewe, Ee Yehova, ni mwema na uko tayari kusamehe; na fadhili zenye upendo ni nyingi kwa wale wote wanaokuitia.” (Zaburi 86:5) Hata ametuahidi uzima wa milele. “Atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Utaonyesha jinsi gani kwamba unathamini upendo wa Mungu? Je, utampenda pia?

Mkaribie Mungu

Mwanamke akisali

Kusali na kutafakari kuhusu sifa za Mungu kutakusaidia kumkaribia zaidi

Mungu anataka umjue vizuri. Neno lake linahimiza: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Mungu alimwita nabii mwaminifu Abrahamu (Ibrahimu) “rafiki yangu.” (Isaya 41:8) Yehova anataka wewe pia uwe rafiki yake.

Kadiri unavyozidi kujifunza kumhusu Mungu, ndivyo utakavyohisi kuwa karibu naye na kuwa mwenye furaha zaidi. “Mwenye furaha ni mtu” ambaye “mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova, naye huisoma sheria yake kwa sauti ya chini mchana na usiku.” (Zaburi 1:1, 2) Hivyo basi, endelea kujifunza Maandiko Matakatifu. Tafakari sifa na kazi za Mungu. Onyesha kwamba unampenda Mungu kwa kutumia mambo unayojifunza. “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yohana 5:3) Basi, sali kama alivyosali mtunga-zaburi: “Nijulishe njia zako, Ee Yehova; nifundishe mapito yako mwenyewe. Nitembeze katika kweli yako.” (Zaburi 25:4, 5) Utapata kujua kwamba Mungu “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.”—Matendo 17:27.

Una Maoni Gani?

  • Ni sifa gani kati ya sifa za Mungu inayokuvutia hasa? Kwa nini?

  • Unaweza kumkaribia Mungu jinsi gani?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki