Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 4/1 kur. 25-28
  • Mtu Aweza Kuwaje Katika Mfano wa Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mtu Aweza Kuwaje Katika Mfano wa Mungu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sifa za Yehova
  • Jitihada za Kumwiga Mungu
  • Twaweza Kuwaje Zaidi Kama Mungu Leo?
  • Kuhubiri Habari Njema
  • Mtukuze Yehova—Mungu wa Pekee wa Kweli
    Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
  • “Jaribuni Kuwa Kama Yeye”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Kuthamini Sifa za Mungu Zisizo na Kifani
    Imani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
  • “Hivi Ndivyo Mungu Alivyotupenda”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 4/1 kur. 25-28

Mtu Aweza Kuwaje Katika Mfano wa Mungu?

“MUNGU akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba.” Ndivyo yasemavyo masimulizi yaliyopuliziwa, lakini hayo yamaanisha nini? Mwanamume na mwanamke wa kwanza waliumbwaje katika mfano wa Mungu?—Mwanzo 1:27.

Je! walikuwa kama Mungu kimwili? La, hilo haliwezekani. Mtu ni wa kibinadamu, wa kimwili, amekusudiwa kuishi duniani. Mungu ni roho, aishiye katika utukufu wa kimbingu usiowazika ambao hakuna binadamu yeyote awezaye kuukaribia. (Kutoka 33:18-20; 1 Wakorintho 15:50) Basi, mtu aliumbwaje katika mfano wa Mungu? Ni kwa jambo la kwamba mwanadamu alipewa uwezo wa kuzoea sifa za Mungu zenye kutokeza—upendo, haki, hekima, na nguvu—pamoja na sifa nyinginezo.

Sifa za Yehova

Sifa za Yehova Mungu zinaonyeshwa katika uumbaji wake wote, lakini zilionyeshwa kwa njia ya kutokeza katika shughuli zake pamoja na wale mume na mke wa kwanza wa kibinadamu, Adamu na Hawa. (Warumi 1:20) Upendo wake ulionwa kwa habari ya kwamba aliiumba dunia ikiwa yenye kufaa kabisa kwa mwanadamu kuishi. Yehova alimuumbia mwanamume mke mkamilifu awe mshiriki wake na mama wa watoto wake. Aliwaweka hao wawili katika bustani nzuri akawapa kwa wingi vitu vyote walivyohitaji ili kuendelea kuishi na kuwa na furaha. La ajabu kushinda yote, Mungu aliwapa fursa ya kuishi milele.—Mwanzo 2:7-9, 15-24.

Hekima ya Mungu ilionwa katika kutahini kwake wale mume na mke wa kwanza wa kibinadamu. Ikiwa wangeendelea kuwa washiriki wa familia ya Yehova ya ulimwengu wote mzima na ikiwa wangeishi milele wakiwa wazazi wa jamii ya kibinadamu, wangehitaji kuwa vielelezo katika uaminifu na ibada ya kweli. Kwa hiyo, Yehova aliwapa fursa ya kuonyesha hali ya mioyo yao chini ya mtihani uliofaa—hawakupaswa kula kutokana na mti wa ujuzi wa mema na mabaya. Yehova alionyesha hekima kama nini kuwaruhusu wanadamu wathibitishe utii na upendo wao kwake kabla ya kuwapa yale mapendeleo mazuri ajabu aliyotaka kuwapa.

Haki ya Mungu ilionwa katika kusisitiza kwake kwamba viumbe vyake vifuate viwango vya juu na katika yeye mwenyewe kuvifuata bila kuridhiana. Ilionwa katika yeye kuwatolea Adamu na Hawa kila fursa ya kufanya mema. Na waliposhindwa kufanya hivyo, ilionwa katika hukumu yake juu yao ya kupatwa na ile adhabu iliyotamkwa kwa sababu ya uasi.

Nguvu za Yehova zilionwa katika kutekeleza kwake hukumu yake. Shetani, yule mwasi mkuu, alikuwa amedokeza kwamba Yehova alikuwa mwongo, na Shetani alimtolea Hawa mambo makuu ikiwa hangemtii Mungu. (Mwanzo 3:1-7) Lakini Shetani hakuweza kutimiza ahadi yake. Yeye hakuweza kumzuia Yehova asiwaondoshe Adamu na Hawa kutoka katika bustani ya Edeni, naye alishindwa kuzuia utimizo wa maneno ya Mungu kwa Adamu: “U mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” (Mwanzo 3:19) Hata hivyo, Yehova hakutekeleza hukumu ya kifo mara iyo hiyo, na katika jambo hilo alionyesha upendo wake hata zaidi. Aliwaruhusu Adamu na Hawa wakati wa kuzaa watoto ambao kupitia hao kusudi lake la awali kwa ajili ya wanadamu lingetimizwa hatimaye.—Mwanzo 1:28.

Hatimaye, haki, upendo, nguvu, na hekima za Yehova Mungu zilidhihirishwa katika ahadi yake ya kutokeza mbegu ambayo ingeharibu kazi za Shetani na kupindua matokeo yenye kuhuzunisha ya ule uasi wa kwanza dhidi ya enzi kuu ya kimungu. (Mwanzo 3:15) Tuna Muumba wa ajabu kama nini!

Jitihada za Kumwiga Mungu

Ingawa wao si wakamilifu tena, bado wanadamu waweza kuonyesha sifa za Mungu. Kwa hiyo, Paulo aliwatia moyo Wakristo wa siku zake hivi: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.” (Waefeso 5:1, NW) Lakini, muda wote wa historia watu walio wengi wameonyesha kudharau sana sifa za Mungu. Kufikia wakati wa Noa, watu walikuja kuwa wafisadi sana hivi kwamba Yehova aliazimia kuharibu wanadamu wote isipokuwa Noa na familia yake. Noa alikuwa mwanamume “wa haki [mwadilifu, NW], mkamilifu katika vizazi vyake,” naye alionyesha upendo wake kwa Mungu kwa kutii amri za Mungu.a “Ndivyo alivyofanya Nuhu [Noa, NW], sawasawa na vyote alivyomwamuru Mungu, hivyo ndivyo alivyofanya.” (Mwanzo 6:9, 22) Noa alionyesha upendo kwa mwanadamu mwenzake na ushikamano wake kwa haki kwa kuwa “mhubiri wa uadilifu.” (2 Petro 2:5, NW) Alionyesha hekima akatumia nguvu zake za kimwili kwa njia ifaayo kwa kufuata mwelekezo wa Mungu na kujenga safina kubwa sana, kuweka akiba ya chakula, kukusanya wanyama, na kuingia safina kwa amri ya Yehova. Alionyesha pia kupenda kwake uadilifu kwa kutowaruhusu majirani wake waovu wamfisidi.

Biblia hueleza juu ya wengine wengi walioonyesha sifa za kimungu vivyo hivyo. Wa kwanza kabisa alikuwa Yesu Kristo, ambaye alikuwa katika mfano wa Mungu kikamilifu na hivyo angeweza kusema hivi: “Aliyeniona mimi amemwona Baba.” (Yohana 14:9) Miongoni mwa sifa ambazo Yesu alionyesha, upendo wake uliokuwa wenye kutokeza. Kumpenda Babake na wanadamu kulimsukuma aache makao yake ya kimbingu na kuishi akiwa mwanadamu duniani. Kulimsukuma amtukuze Babake kwa mwenendo mwadilifu na kuhubiria wanadamu habari njema za wokovu. (Mathayo 4:23; Yohana 13:31) Kisha, upendo ulimsukuma Yesu atoe uhai wake mkamilifu kwa ajili ya wokovu wa wanadamu na, jambo la maana zaidi ni kwa ajili ya kutakaswa kwa jina la Mungu. (Yohana 13:1) Katika kujitahidi kumwiga Mungu, je, kuna kielelezo bora zaidi cha kufuatwa kuliko cha Yesu Kristo?—1 Petro 2:21.

Twaweza Kuwaje Zaidi Kama Mungu Leo?

Leo, sisi twaweza kuonyeshaje sifa za Mungu na hivyo kutenda katika mfano wa Mungu? Kwanza fikiria sifa ya upendo. Yesu alisema: “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote.” Twaonyeshaje kumpenda Mungu? Mtume Yohana ajibu: “Huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake; wala amri zake si nzito.”—Mathayo 22:37; 1 Yohana 5:3.

Bila shaka, ili kutii amri za Yehova, ni lazima tuzijue. Hilo latia ndani kusoma, kujifunza, na kutafakari juu ya Neno la Mungu, Biblia, na juu ya fasihi ya Biblia. Kama vile mtunga-zaburi, twapaswa kuweza kusema: “Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.” (Zaburi 119:97) Tupatapo uelewevu mwingi zaidi na zaidi wa Neno la Mungu, twakaziwa kikiki njia ya Mungu ya kufikiri. Twapata kupenda uadilifu na kuchukia uasi-sheria. (Zaburi 45:7) Hapo ndipo Adamu alikosea. Alijua sheria ya Yehova, lakini hakuipenda vya kutosha kushikamana nayo. Tusomapo Neno la Mungu, twapaswa kujiuliza daima, ‘Hili lanihusuje? Naweza kufanyaje ili mwenendo wangu upatane zaidi na sifa za Mungu?’

Yesu alisema pia: “Mpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mathayo 22:39) Kila mtu mmoja-mmoja mwenye afya hujipenda mwenyewe na hujitakia mema. Hilo si kosa. Lakini je, sisi huonyesha upendo unaolingana na huo kwa jirani yetu? Je! sisi hufuata amri hii ya Kibiblia: “Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao, ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda”?—Mithali 3:27; Wagalatia 6:10.

Namna gani sifa ya hekima? Kujaribu kwetu kudhihirisha sifa hiyo hutuongoza kwenye funzo la Biblia kwa sababu hiyo ndiyo chanzo cha hekima ya kimungu. Zaburi 119:98-100 husomwa hivi: “Maagizo yako hunitia hekima kuliko adui zangu, kwa maana ninayo sikuzote. Ninazo akili kuliko wakufunzi wangu wote, maana shuhuda zako ndizo nizifikirizo. Ninao ufahamu kuliko wazee, kwa kuwa nimeyashika mausia yako.” Kwenye Mithali 3:18, hekima inaelezwa kuwa “mti wa uzima.” Tukipata hekima na kuizoea, tutapokea kibali cha Mungu na thawabu ya uhai wa milele.—Mhubiri 7:12.

Namna gani haki? Katika ulimwengu huu mbovu, haki ni sifa muhimu kwa wale watakao kumpendeza Mungu. Yesu alipenda uadilifu (haki) na kuchukia uasi-sheria. (Waebrania 1:9) Wakristo hufanya vivyo hivyo leo. Haki huwasukuma kuthamini sifa zifaazo. Wao huepuka njia za ulimwengu huu zisizo za uadilifu na hufanya kazi ya kufanya mapenzi ya Mungu iwe jambo la maana zaidi maishani mwao.—1 Yohana 2:15-17.

Kwa habari ya nguvu, sisi sote tuna kiasi fulani. Kwa asili, sisi tuna nguvu za kimwili na za kiakili, na tukuapo tukiwa Wakristo, tunasitawisha nguvu za kiroho. Yehova huongeza nguvu zetu kwa roho takatifu yake kwa kadiri ambayo, ingawa twaonekana kuwa dhaifu, twaweza kutimiza penzi la Yehova. Paulo alisema hivi: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” (Wafilipi 4:13) Nguvu izo hizo zinapatikana kwetu tukimwomba Yehova roho yake.

Kuhubiri Habari Njema

Kuonyesha kwetu zile sifa kuu nne za Mungu kwaonwa vema katika kutii kwetu amri hii: “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW] na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari.” (Mathayo 28:19, 20) Kazi ya kielimu kama hiyo huwaletea uhai wale waitikiao. Ni wonyesho mzuri kama nini wa upendo kwa wale ambao kwa ujumla, huanza wakiwa watu tusiowajua kabisa!

Zaidi ya hayo, kufundisha kwa jinsi hiyo ni mwendo wa hekima. Kwatokeza matunda yanayodumu. Ni kazi gani nyingineyo iwezayo kusemwa hivi juu yayo: “Kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia”? (1 Timotheo 4:16) Hakuna wowote watakaoshindwa katika kazi ya kufanya wanafunzi. Wale wasikiao na pia wale wafundishao hupata baraka za milele.

Kwa habari ya haki, Wakristo wanafundisha wanafunzi wao wa Biblia kanuni zenye haki na uadilifu. Tunawasaidia wamtumikie Yehova, “Mungu wa haki.” (Malaki 2:17, NW) Wale leo wanaoweka wakfu maisha zao kumtumikia Yehova na kuendelea katika uaminifu wanajulishwa rasmi kuwa waadilifu, wenye haki, na hilo linaongoza kwenye kuokoka kwao Har–Magedoni.—Warumi 3:24; Yakobo 2:24-26.

Kule kuhubiri na kufundisha habari njema ulimwenguni pote ni wonyesho wa nguvu kama nini! (Mathayo 24:14) Kuhubiri daima katika maeneo ambako watu walio wengi hawataki kusikiliza kwahitaji uvumilivu. Lakini Yehova, kupitia roho yake, hutoa nguvu zinazohitajiwa ili kuvumilia hadi mwisho.—Isaya 40:30, 31; Mathayo 24:13; Luka 11:13.

Ni kweli, tukiwa wazao wa Adamu wasio wakamilifu, hatuwezi kuzoea sifa hizo nzuri kikamilifu. Lakini, kumbuka kwamba mtu aliumbwa katika mfano wa Mungu, na tukijitahidi kuwa zaidi na zaidi kama Mungu, basi tunatimiza kwa sehemu sababu ya kuwako kwetu. (Mhubiri 12:13) Tukijikakamua kufanya bora tuwezavyo na kuomba msamaha tunapopungukiwa, basi twaweza kuwa na tumaini la kuokoka kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu, ambamo twaweza kufikia ukamilifu hatimaye. Ndipo, tutakuwa katika dunia-paradiso yenye kukaliwa na watu wakamilifu, wote wakionyesha sifa za Yehova Mungu kikamili. Ni shangwe iliyoje! Hatimaye, wanadamu watakuwa katika mfano wa Mungu kikamili.

[Maelezo ya Chini]

a “Uadilifu” na “haki” zinahusiana kwa ukaribu sana. Katika Maandiko ya Kigiriki, zinawakilishwa kwa lile neno moja, diʹkai·os.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Yesu alituonyesha jinsi ya kusitawisha sifa za kimungu za Yehova

[Picha katika ukurasa wa 26]

Hatimaye, wanadamu watakuwa katika mfano wa Mungu kikamili

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki