“Jaribuni Kuwa Kama Yeye”
“Katika neno, kama watoto wapendwa wa Mungu, jaribuni kuwa kama yeye.”—Efe. 5:1, New English Bible.
1. (a) Maelekeo ya kawaida ya kuiga wengine yanawezaje kuongoza mtu? (b) Biblia inatutia moyo tuige nani hasa?
WAKATI fulani kila mtu hujaribu kuiga mwingine. Watoto hujaribu kuiga wazazi wao au mara nyingi sana kuiga watoto wanaocheza nao. Wakijaribu kuiga sifa njema, wanafaidika. Wakiiga mabaya, wanapatwa na madhara. Linalopendeza ni kwamba sisi tunakaribishwa ‘tumwige Mungu, kama watoto wanaopendwa.’ (Efe. 5:1) Je! tunaweza kweli kumwiga Mungu? Acheni tuone kama kuna uwezekano wa wote.
2. Kulingana na Mwanzo 1:26, 27, mwanadamu wa kwanza alifanywaje, na hiyo ingemaanisha nini kwa wazao wake wote?
2 Basi, hapo mwanzo, wakati Mungu alipomwumba mwanadamu karibu miaka 6,000 iliyopita, Biblia inatuambia hivi: “Mungu akasema, Na tufanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu; . . . Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba.” (Mwa. 1:28) Sasa bila shaka kuna mamilioni ya mamilioni ya watu, wote wakiwa ni wazao wa Adamu na Hawa, ambao wangetazamiwa kuwa wamekwisha pata mfano na sura ya Mungu, Baba yao. Mungu ndiye aliyekuwa Baba yao. Hiyo inaweza kuhakikishwa kwa kusoma aliyoandika Luka katika sura ya 3, mstari wa 38 wa masimulizi yake ya Injili, ambayo yamtaja “Adamu, wa Mungu.” Kwa hiyo Adamu alikuwa mwana wa Mungu, nasi sote tumetoka kwa Adamu. Alipoumbwa alikuwa na sifa za Mungu, sifa zake njema za hekima, haki ya hukumu, upendo na uwezo. Adamu alikuwa mwanadamu mkamilifu.—Kum. 32:4.
3. Kwa sababu gani leo wanadamu hawaonyeshi sifa za Mungu kwa ukamilifu?
3 Lakini mambo yamebadilika tangu wakati huo. Kwa sababu gani Kwa sababu Adamu alikosa kumtii Mungu, na ingawa wanadamu wengine wanaonyesha? kwa kadiri fulani sifa njema zilizotiwa ndani hapo kwanza katika mwanadamu mkamilifu, dhambi ndiyo hutawala. Mtume Paulo alieleza jambo hilo vizuri sana katika Warumi 5:12: “Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” Kwa hiyo “mauti ilitawala” kama mfalme tangu Adamu mpaka wakati huu. Aibu! (Rum. 5:14) Je! hakuna tumaini? Sivyo! Neno la Mungu, Biblia Takatifu, linatupa tumaini, likisema hivi: “Kwa kuwa kama katika Adamu wote wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote watahuishwa.” (1 Kor. 15:22) Hiyo ilipangwaje?
YESU KRISTO, “MFANO WA MUNGU ASIYEONEKANA”
4. Ni kwa mpango gani imewezekana kwa wazao wa Adamu kupata uzima wa milele?
4 Kumbuka hili: Baada ya kuanguka kwa Adamu Yehova Mungu bado alipendezwa sana na wanadamu, naye alikusudia viumbe vya kibinadamu viijaze dunia hii. Lakini, ilikuwa lazima haki ya hukumu ya Mungu itoshelezwe, na kwa hiyo yeye alitoa mkombozi kwa ajili ya wazao wa Adamu. Maandiko yatupasha habari hizi: “Mungu aliupenda ulimwengu [wa wanadamu], hata akamtoa Mwanawe pekee [kama ukombozi], ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Ni upendo wa namna gani huo! Mwana wa Mungu alitokea akiwa kiumbe kikamilifu cha kibinadamu kwa kuzaliwa na bikira Mariamu. Kwa hakika alikuwa ndiye ‘Adamu wa pili’ au mwanadamu wa pili aliye mkamilifu duniani. (1 Kor. 15:45) Aliumwaga uhai wake akainunua jamaa yote ya kibinadamu. Yesu Kristo alijihakikisha kuwa ndiye mkombozi wa wanadamu, kama inavyosemwa: “Mwana wa Adamu . . . [alikuja] kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.” (Mt. 20:28) Wakristo wanajua kwamba kuna Mungu “mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi [unaolingana] kwa ajili ya wote.”—1 Tim. 2:5, 6.
5. (a) Kulikuwa na ulinganifu gani kati ya mwanadamu wa kwanza, Adamu, na Yesu Kristo? (b) Ikiwa tutakuwa kama Mungu, tutafuata mfano wa nani?
5 Tunaweza kusema kwamba huyu ‘Adamu wa pili’ pia, Yesu Kristo, alikuwa kama Baba yake wa mbinguni. (Ebr. 1:3) “Naye ni mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.” (Kol. 1:15) Wakristo wanaombwa watembee kwa njia inayomfaa Yehova hata kumpendeza kabisa. (Kol. 1:10) Kwa hiyo wale wanaotaka kuwa kama Yehova Mungu watamtegemea Kristo Yesu kama mfano wao ili watembee katika nyayo zake.
6. (a) Ni sifa gani ya Yesu iliyomwezesha kujipatanisha kabisa na mapenzi ya Baba yake? (b) Tunapojifunza mambo ambayo Yesu alisema na kufanya, tunafahamiana vizuri zaidi na nani mwingine, na kwa sababu gani?
6 Ingawa Yesu alifanywa kwa mfano wa Baba yake wa mbinguni, yeye hakujaribu kamwe kuwa sawa na Mungu, kwa maana twasoma hivi: “Kristo Yesu . . . ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya [mti wa mateso].” (FIp. 2:5-8) Kwa hiyo twaona kwamba Yesu Kristo mwenyewe, akiwa na namna ya mwanadamu mkamilifu, alitii kila jambo ambalo Yehova Mungu alimwagiza kufanya. Wale wanaotaka ‘kumfuata Mungu’ lazima watembee kama Yesu alivyotembea, kwa maana Yesu alisema hivi: “Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia silo langu, ila ni lake Baba aliyenipeleka.” (Yohana 14:24) Yesu alifanana sana na Baba yake Yehova Mungu, alitenda sana kupatana na njia na maisha Yake ya haki, hata aliposema mwenye kumsikia hakusikia Yesu akinena jambo la kuwaza kwake mwenyewe. Kwa sababu gani? Kwa sababu Biblia yasema hivi: “Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda; kwa maana yote ayatendayo yeye, ndiyo ayatendayo Mwana vile vile. Kwa kuwa Baba ampenda Mwana, naye humwonyesha yote ayatendayo mwenyewe; hata na kazi kubwa zaidi kuliko hizo atamwonyesha.”—Yohana 5:19, 20.
7. Twayaona wapi maandishi ya mfano mwema ambao Yesu alituwekea?
7 Katika Biblia, leo tunayo maandishi ya mfano huo mzuri sana wa Yesu Kristo, Mwana mzaliwa pekee wa Mungu. Yeye alijihakikisha kuwa kama Baba yake wa mbinguni kwa miaka 33 na nusu alipokuwa hapa duniani kama kiumbe cha kibinadamu. Bila shaka aliweka mfano bora kuonyesha alifanywa kwa mfano wa Mungu. Ingawa alikuwa mwanadamu kwa kweli alikuwa Mwana wa Mungu, ‘Adamu wa pili,’ ambaye huchukua dhambi ya ulimwengu.—Yohana 1:29.
8. Ni utimizo wa tumaini gani unaotegemea kujitahidi kwetu kuwa kama Mungu?
8 Leo Wakristo wanaonywa kwa upole wajitahidi sana sana kuwa kama Yehova Mungu, na hakuna sababu ya kumfanya Mkristo aache kujaribu kuwa hivyo. Ikiwa Mkristo leo anayo matumaini ya kuishi duniani milele baada ya utawala wa miaka elfu wa Kimasihi wa Kristo Yesu, itampasa aonyeshe mfano na sura ya Mungu kufikia wakati huo. Kwa sababu gani? Ni kwa sababu wakati Kristo Yesu atakapomrudishia Baba kila kitu, kila mtu atakayekuwa hai duniani wakati huo atakuwa mwana wa Mungu kupitia kwa Kristo—kama alivyosema Yehova, “kwa mfano wetu, kwa sura yetu.” Kusudi la Yehova kwa wanadamu wawili wa kwanza litakuwa limetimizwa la ‘kuzaa, mkaongezeke, mkaijaze nchi.’—Mwa. 1:26-28; Rum. 8:20, 21.
WANADAMU WENYE DHAMBI WANAWEZA KUWA KAMA MUNGU?
9. (a) Je! haiwezekani kwetu ‘kujaribu kuwa kama Mungu’ kwa sababu tumezaliwa katika dhambi? (b) Ni kwa kuonyesha sifa gani hasa tunaweza kutoa ushuhuda wa kwamba tunajaribu?
9 Ni kweli, katika taratibu ya mambo iliyopo mwanadamu kwa kawaida huwa na maelekeo ya kufanya mabaya. Hiyo ni kwa sababu amezaliwa katika dhambi na kulelewa katika udhalimu. Hata hivyo, Neno la Mungu husema hivi katika Waefeso sura ya tano, kuanza na mstari wa kwanza, kulingana na The New English Bible: “Katika neno, kama watoto wapendwa wa Mungu, jaribuni kuwa kama yeye, na kuishi katika upendo kama Kristo alivyowapenda ninyi, akajitoa mwenyewe kwa ajili yenu kama toleo na dhabihu ambaye manukato yake yanampendeza Mungu.” Twajua kwamba Yehova Mungu alimtuma Mwanawe ulimwenguni, nayo dhabihu yake juu ya mti wa mateso ililipa bei au ukombozi. Lakini Yesu alifanya jambo jingine. Alitupa mfano mkamilifu wa kufuata! Alikuwa mwanadamu mwenye ukamilifu, kwa hiyo imetupasa tuwe kama yeye katika upendo wetu. Bila shaka Kristo alitupenda ama sivyo asingalikufa kamwe juu ya mti wa mateso—kifo kibaya sana—ili atoe dhabihu ya ukombozi. Njia hii ya maisha, mfano huu ambao Yesu aliweka, ulimfurahisha na kumpendeza Yehova. Hata kabla Yesu hajailipa bei ya ukombozi kwa damu yake, Yohana Mbatizaji alisema hivi juu ya Yesu Kristo: “Tazama, Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu.”—Yohana 1:29.
10. (a) Ni mfano gani wa Biblia unaoonyesha kwamba hata mwanadamu asiye mkamilifu anaweza kuwa ‘bila lawama na kuwa mnyofu’ mbele za Mungu? (b) Shetani alitoa dai gani juu ya Ayubu?
10 Tukitembea katika njia ya maisha ambayo Kristo Yesu alitembea, bila shaka pia tutakuwa tunajaribu kuwa kama Yehova Mungu, Baba yake na Baba yetu aliye mbinguni. Ni vyepesi sana kwa mtu kusema, “Lakini mimi si mkamilifu, wala siwezi kufanya vile Yesu alivyofanya.” Lakini, Kumbuka tafadhali, kwamba alikuwako mwanadamu mmoja asiye mkamilifu duniani aliyetembea katika ukamilifu akampendeza Mungu mpaka mwisho wa maisha yake. Huo ulikuwa muda mrefu kabla Yesu hajaishi duniani. Jina la mwanadamu huyo alikuwa Ayubu. Kitabu cha Biblia cha Ayubu chatuambia kwamba mwanadamu huyu aliishi katika nchi ya Uzi, na kwamba alikuwa “mwanadamu mwenye maisha yasiyo na lawama na manyofu.” (Ayubu 1:1, NE) Ayubu alimwamini Mungu kweli kweli naye aliyapa mabaya kisogo. Alikuwa na wana saba na binti watatu tena alikuwa mwenye ufanisi mwingi. Alikuwa na makundi mengi ya kondoo na ng’ombe na ngamia naye akawa mtu mashuhuri katika nchi za Mashariki. Wakati Ayubu alipokuwa akifurahia ufanisi wote huo na baraka kutoka kwa Yehova Mungu, masimulizi ya Biblia yatuambia hivi: “Ilikuwa, siku moja ambayo hao wana wa Mungu walikwenda kujihudhurisha mbele za [Yehova], Shetani naye akaenda kati yao. [Yehova] akamwuliza Shetani, Umetoka wapi wewe? Ndipo Shetani akamjibu [Yehova], na kusema, Natoka katika kuzunguka-zunguka duniani, na katika kutembea huku na huku humo. Kisha [Yehova] akamwuliza Shetani, Je! umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na uelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu. Ndipo Shetani akamjibu [Yehova], na kusema, Je! huyo Ayubu yuamcha [Yehova] bure? Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi. Lakini nyosha mkono wako sasa, uyaguse hayo yote aliyo nayo, naye atakukufuru mbele za uso wako. [Yehova] akamwambia Shetani, Tazama, yote aliyo nayo yamo katika uwezo wako; lakini usinyoshe mkono wako juu yake yeye mwenyewe. Basi Shetani akatoka mbele za uso wa [Yehova].”—Ayubu 1:6-12.
11, 12. (a) Ayubu alikuwa mwaminifu kwa Mungu alipopatwa na mambo gani? (b) Alithawabishwaje kwa kujaribu kuwa kama Mungu?
11 Kuanzia wakati huo, Shetani alifanya kila jambo aliloweza avunje ukamilifu na unyofu wa mtumishi wa Yehova Ayubu, lakini Ayubu hakushindwa hata na ukatili wa Shetani. Yeye hakuuacha mwendo wake wa uaminifu hata watoto wake walipouawa, alipopoteza utajiri wake wote, hata alipotembelewa na wenye hekima wa jina tu kwa kusudi la kumwambia alivyokuwa amekosa. Rafiki hao wa jina tu walijibiwa hivi na Ayubu: “Nimesikia maneno mengi mfano wa hayo; ninyi nyote, ni wafariji wenye kutaabisha.” (Ayubu 16:2) Kwa kweli, mambo yalimhuzunisha Ayubu sana hata akampazia Mungu sauti akisema, “Kaburi i tayari kunipokea.” (Ayubu 17:1) Lakini Ayubu hakufa. Aliendelea kuwa mwaminifu na mnyofu mbele za Mungu, hata kati ya wapinzani wake wote. Mwishowe, kulingana na masimulizi ya Biblia, “BWANA akaubarikia huo mwisho wa Ayubu zaidi ya mwanzo wake; naye alikuwa na kondoo kumi na nne elfu, na ngamia elfu sita, na jozi za ng’ombe elfu, na punda wake elfu. Tena alikuwa na wana waume saba, na binti watatu. Akamwita huyo wa kwanza jina lake Yemima; na wa pili akamwita jina lake Kesia; na wa tatu akamwita jina lake Keren-hapuhu. Katika nchi hiyo yote hawakuwapo wanawake waliokuwa wazuri kama hao wana wa Ayubu; na baba yao akawapa urithi kati ya ndugu zao wana waume. Kisha baada ya mambo hayo Ayubu akaishi miaka mia na arobaini, naye akawaona wanawe, na wana wa wanawe, hata vizazi vinne.”—Ayubu 42:12-17.
12 Tunaposoma maisha yote ya Ayubu na kuona jinsi alivyoyavumilia magumu yake yote, bila shaka tunaweza kusema kama Mungu kwamba alikuwa mwanadamu asiye na lawama tena mnyofu aliyemcha Mungu na kuyapa mabaya kisogo. Ayubu alijaribu kuwa kama Mungu. Alithawabishwa kwa ukamilifu wake, naye atapokea thawabu zaidi katika wakati unaofaa. Yakobo aliandika hivi juu yake: “Mmesikia habari ya subira yake Ayubu, mmeuona mwisho wa Bwana ya kwamba Bwana ni mwingi wa rehema, mwenye huruma.”—Yak. 5.11.
13. Huenda bado mtu akasema nini juu ya mifano hii?
13 Huenda mtu akasema hivi: “Ilikuwa vyepesi kwa Kristo Yesu, mwanadamu mkamilifu, kuendeleza ukamilifu na kutembea kwa unyofu mbele za Mungu wake. Na ni kweli kwamba Ayubu, mwanadamu asiyekamilika, alifanya vivyo hivyo. Lakini sisi twawezaje kufanya hivyo leo?” Hata siku za mtume Paulo, hilo lingeweza kufanywaje? Paulo alilionya kwa upole kundi la Efeso akisema hivi: “Kama watoto wapendwa wa Mungu, jaribuni kuwa kama yeye, na kuishi katika upendo kama Kristo alivyowapenda ninyi.” (Efe. 5:1, 2, NE) Je! Paulo alikuwa akiwaomba Wakristo hao wafanye jambo lisilowezekana? Sivyo kabisa!
KUWA “WATOTO WA KUTII,” SI WAASI
14. Ili mtu amwige Mungu, lazima achukie mambo gani?
14 Mtunga zaburi alilieleza jambo hilo vizuri sana. Alisema hivi: “Enyi mmpendao [Yehova], uchukieni uovu.” (Zab. 97:10) Ikiwa imetupasa kuchukia uovu, basi imetupasa tujue uovu ni nini na kutenda mema. Paulo atusaidia kwa kutushauri juu ya uovu. Alipokuwa akiandikia Waefeso aliendelea kusema hivi: “Uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wala kutamani, [pupa, NW] kama iwastahilivyo watakatifu; wala aibu wala maneno ya upuzi wala ubishi; hayo hayapendezi; bali afadhali kushukuru. Maana neno hili mnalijua hakika, ya kwamba hakuna mwasherati wala mchafu wala mwenye tamaa, ndiye mwabudu sanamu, aliye na urithi katika ufalme wa Kristo na Mungu.” (Efe. 5:3-5) Basi, twaona kutokana na hayo kwamba lazima Mkristo awe mwadilifu. Lazima usemi wake uwe sahihi anaposema na watu wengine. Hawezi kuwa mwenye pupa. Yeye atakuwa mwaminifu kwa watu walio karibu yake. Kwa ufupi, atachukia mabaya ikiwa kweli ampenda Yehova Mungu. Na kwa hiyo ikiwa mtu ataka kuwa kama Mungu kwa hakika hatayafanya mambo yaliyotajwa na Paulo.
15. (a) Paulo anasema hukumu ya Mungu itawajia akina nani? (b) Wanajionyeshaje kuwa waasi?
15 Ni nini huwapata wale wanaofanya mambo anayotaja Paulo—uasherati, maneno ya upuzi na pupa? Yeye asema hivi: “Mtu asiwadanganye kwa maneno yasiyo na maana; kwa kuwa kwa sababu ya hayo hasira ya Mungu huwajia wana wa uasi. Basi msishirikiane nao.” (Efe. 5:6, 7) Mungu asema mambo wazi sana. Hukumu ya kuogofya itawajia wenye kumwasi. Adamu alikuwa mwasi. Hakumsikiliza Mungu ingawa alipewa sifa za hekima, haki ya hukumu, upendo na uwezo, naye alipewa hali nzuri za maisha. Hata hivyo, alitaka kujiamulia mwenyewe yaliyo mema na yaliyo mabaya. Walakini, Yehova ndiye mwenye haki za kufanya maamuzi hayo. Yeye ndiye Muumba wa ulimwengu wote na Muumba wa vitu vyote vilivyo hai, naye ataka viumbe vyote vilivyo hai na vyenye akili viwe kama yeye; yeye atukaribisha sisi tuwe hivyo ingawa hatu wakamilifu. Mungu apendezwa na wanadamu. Je! sisi twapendezwa na Yehova Mungu? Ikiwa hatupendezwi naye na twakataa kufuata njia yake tukitaka kufuata njia yetu wenyewe na kujifanyia uamuzi katika mambo yote, kinyume cha shauri la Mungu, basi tunaweza kutazamia ‘hasira itakayowajia wana wa uasi.’ Paulo aonya kundi la Kikristo kwa ukali kwamba Wakristo hawapaswi kushirikiana na ‘wana hao wa uasi’—wale wanaotenda kinyume cha njia ya Mungu.
16. Ni nia gani inayohusu uasherati lazima iepukwe na wale wanaotaka kibali ya Mungu?
16 Twajua uasherati ni nini, lakini leo wanadini husema kijasiri kwamba hakuna ubaya wa kufanya ngono kabla ya kuoana, hakuna ubaya wa mwanamume au mwanamke kulala mwenzake. Lakini je! Biblia haisemi kwamba malazi ya ndoa yasichafuliwe na kwamba wanaume wenye kulala na wanaume wenzao ni machukizo mbele za Mungu na kwamba watapokea hukumu Yake?’ Inasema hivyo. (Ebr. 13:4; Rum. 1:27, 32) Kwa hiyo ikiwa mtu ajidai kuwa Mkristo na ajaribu kuwa kama Mungu kwa kuwa na mwendo wa maisha ambayo Yesu Kristo alituwekea kama mfano, inampasa ahakikishe anajitahidi sana sana kuishi kama Mkristo, ili apate kibali na baraka nyingi za Mungu.—1 Kor. 6:18; 1 The. 4:3, 8.
17. Wakati Petro alipokuwa akieleza mabadiliko ambayo lazima Wakristo wafanye katika maisha zao, aliwasihi wawe watu wa aina gani?
17 Wakati mtu anapokuwa Mkristo lazima afanye mabadiliko makubwa katika maisha yake. Mtume Petro aliandika barua kwa Wakristo wa kwanza akalieleza jambo hilo hivi: “Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza, za ujinga wenu; bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.” (1 Pet. 1:14-16) Linalopendeza ni kwamba, hapa Petro ataja kundi la Mungu kama “watoto wa kutii.” Ikiwa watalitii Neno la Mungu lazima waache kufuata tamaa zao wenyewe na kutotembea katika njia waliyokuwa zamani. Lakini watajaribu kuwa kama Mungu na kutembea katika nyayo za Kristo Yesu.
KUFAIDIKA KUTOKANA NA UPENDO WA MUNGU
18. Katika kuonyesha upendo, lazima tufanye nini kujihakikisha ‘wana wa Baba yetu aliye mbinguni’?
18 Wakati Yesu alipokuwa hapa duniani alisema hivi kwa wenye kumsikiliza: “Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako; lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi; ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki. Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi, mwapata thawabu gani?” (Mt. 5:43-46) Ikiwa ‘mtapata kuwa wana wa Baba yenu’ kama Kristo Yesu, hamtapenda jirani zenu tu bali pia mtaonyesha adui zenu upendo. Je! wewe hufanya hivyo?
19. Kama inavyosemwa katika Waefeso 3:18, 19, lazima watu wote wa Mungu waelewe nini?
19 Katika Neno la Bwana, katika 1 Yohana 4:11, twayaona maneno haya: “Wapenzi, ikiwa Mungu alitupenda sisi hivi, imetupasa na sisi kupendana.” Wakati mtu anapokuwa Mkristo lazima asitawishe mizizi yenye kina kirefu. Lazima ajaribu kufikia ukamili ambao Mungu hutaka. Paulo ataja jambo hilo kwa njia hii anapowaandikia Waefeso: “Mkiwa na mizizi yenye kina kirefu na misingi imara, na mwe na nguvu za kuelewa, pamoja na watu wote wa Mungu, ni nini upana na urefu na kimo na kina cha upendo wa Kristo, na kuujua, ingawa unapita kiasi cha kuweza kujulikana. Kwa hiyo na mfikie ukamili wa kuwa, ukamili wa Mungu mwenyewe.” (Efe. 3:18, 19, NE) Neno la Mungu linatia moyo Wakristo wajitahidi sana kuelewa upendo ulioonyeshwa kupitia kwa Kristo kisha wajaribu kuwa kama Mungu kwa kumwiga Kristo. Lazima Wakristo wajitahidi kufanya hivyo.
20. Maneno aliyoandika Paulo juu ya upendo katika Warumi 8:31-39 yanatutiaje moyo?
20 Tunatiwa moyo sana katika jambo hilo, kama lilivyoandikwa na mtume Paulo. Aliandika hivi: “Basi, tuseme nini juu ya hayo? Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu? Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia na mambo yote pamoja naye? Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea. Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! ni dhiki, au shida; au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga? Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa. Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda. Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kingenecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”—Rum. 8:31-39.
21. (a) Kwa sababu gani Paulo aliambia wengine wamwige (b) Katika habari hii, sote tuna daraka gani?
21 Paulo alikuwa na hakika kabisa kwamba Yehova alimpenda, na kwa hiyo alikuwa akijitahidi kwa moyo kumwiga Mungu. Hivyo, alipokuwa akiwaandikia Wafilipi, Paulo alisema hivi: “Mambo mliyojifunza kwangu na kuyapokea, na kuyasikia na kuyaona kwangu, yatendeni hayo; na Mungu wa amani atakuwa pamoja nanyi.” (Flp. 4:9) Mtume Paulo alifahamu kabisa kwamba sote hufanya makosa, lakini alijua kwamba alikuwa akijitahidi na kuwekea ndugu mfano unaofaa. Ndiyo sababu alisema hivi: “Mnifuate mimi, mkawatazame wao waendao kwa kuufuata mfano tuliowapa ninyi.” (FIp. 3:17) Wazee, vilevile wengine ambao wamekuwa katika kweli kwa muda mrefu au hata kwa muda mfupi, wana daraka kubwa la kuweka mfano unaofaa, kama Paulo. Wasipofanya hivyo, hiyo inaweza kukwaza ndugu wengine ndani ya tengenezo la Mungu. Tunaonywa hivi kwa upole na Paulo: “Msiwakoseshe Wayahudi wala Wayunani wala kanisa la Mungu; vile vile kama mimi niwapendezavyo watu wote katika mambo yote, nisitake faida yangu mwenyewe, ila faida yao walio wengi, wapate kuokolewa.”—1 Kor. 10:32, 33.
22. Ni nini kinachoweza kutusaidia tujitahidi kuwa kama Mungu?
22 Paulo alikuwa na roho ile ile ambayo Yehova Mungu huonyesha wanadamu. Alijifunza hilo kwa Yehova. Aliujua uhitaji wa kupenda jirani na kuwapa nafasi kamili ya kupata uzima wa milele. Ndiyo sababu, katika mstari ule ule unaofuata, yeye asema hivi: “Mnifuate mimi kama mimi ninavyomfuata Kristo.” (1 Kor. 11:1) Paulo aliendelea kumwiga Mwana wa Mungu. Alijua kwamba Yesu alikuwa mkamilifu na kwamba aliweka mfano mzuri sana kwa kujaribu kuwa sawa kabisa na Baba yake, na kwa hiyo Paulo alijisikia vivyo hivyo. Paulo alijua yaliyokuwa yameandikwa katika Neno la Mungu na kwa hiyo atuonya sote kwa upole ‘tuwakumbuke wale wanaotuongoza, waliotuambia neno la Mungu, kwa kuuchunguza sana mwisho wa mwenendo wao, tuiige imani yao.’ (Ebr. 13:7) Hatutaki kuzifuata njia za ulimwengu wa kale. Ingawa tumo katika ulimwengu, sisi si sehemu yake. Mfano bora tunaoweza kufuata ni ule unaotolewa na Yehova Mungu mwenyewe. Pia, wakati Yesu alipokuwa duniani, alisema kwamba “aliyeniona mimi amemwona Baba.” (Yohana 14:9) Kwa hiyo ikiwa tunataka kumwiga Yehova Mungu, au kuwa kama yeye, bila shaka tunataka kuwa kama Kristo Yesu, mwanadamu mwenye ukamilifu.
[Picha katika ukurasa wa 295]
Adamu alikuwa mwana wa Mungu, alifanywa “kwa mfano wa Mungu” nasi sote tumetoka kwa Adamu
[Picha katika ukurasa wa 296]
Tunapomwiga Yesu Kristo tunakuwa kama Mungu, kwa sababu Yesu alikuwa kama Baba yake wa mbinguni. Yohana Mbatizaji alisema kwamba Yesu ndiye “Mwana wa Mungu”