Msingi wa Maisha Yenye Kusudi
“Tazameni, ni pendo la namna gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu.”—1 Yohana 3:1.
1-3. Ni Mambo gani yanayozuia watu kufurahia maisha?
KILA mtu wa kawaida angependa kutimiza jambo fulani na maisha yake. Lakini wengi wanalalamika kwamba taratibu ambayo katika hiyo tunaishi haitii watu moyo wawe na kusudi la kweli.
2 Watu hawa mmoja mmoja wanaonyesha uhakika wa kwamba huenda mtu akawa na mradi fulani mwanzoni, atumie miaka mingi akipata elimu juu ya jambo analotaka kufanya halafu baadaye aone kwamba hawezi kupata kazi ya kuajiriwa. Watu wengi wenye masomo ya juu wanalazimika kukubali kazi ya hivi hivi tu ili wajipatie riziki.
3 Kwa upande mwingine, wale ambao wamepata fedha nyingi wanajua kwamba vita au msiba mwingine unaweza kwa upesi kumaliza yote ambayo wamejipatia. Nacho kifo cha mtu anayependwa kinaweza kuwaletea maisha ya upweke.
4. (a) Ni kwa sababu gani wengine wanasema, ‘Mungu amefariki’? (b) Yehova anaonaje juu ya wanadamu? (Ayubu 14:14, 15; Omb. 3:34-36; Yon. 4:10, 11)
4 Wakiyaona mambo kwa njia hii, wengine wanasema, ‘Mungu amefariki,’ Yaani, Mungu hapendezwi na mambo ya wanadamu. Lakini, Mungu anapendezwa sana na ulimwengu apate kushughulika (kushirikiana) nao kwa vile aliuumba. Kwa kweli, Mungu amewatayarishia wanadamu wakati ujao mzuri tena anakusudi juu ya kila mtu anayeishi, au ambaye ameishi. Zaidi ya hayo, kusudi hili latia maoni yetu, hata kutimiza kwetu kusudi la maisha kunamaanisha pia furaha na uradhi wetu mwingi zaidi. Ndivyo tunavyotaka, sivyo?
HALI YETU YA KUTOWEZA KITU
5. Musa alielezaje hali ya wanadamu?
5 Lakini yapaswa ikubaliwe kwamba wanadamu hawawezi kugeuza mambo. Musa, mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu alisimulia hali yetu ya kutoweza kitu hivi: “Siku za miaka yetu ni miaka sabini, na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; na kiburi chake ni taabu na ubatili.” —Zab. 90:10.
6. Ni kwa sababu gani wanadamu hawawezi kujiweka huru na utumwa wa mauti?
6 Kutoweza kwa wanadamu kujitoa katika utumwa wa mauti kunaelezwa katika zaburi ya arobaini na tisa (49), mstari wa sita mpaka tisa hivi: “Hao wanaozitumainia mali zao, na kujisifia wingi wa utajiri wao; hakuna mtu awezaye kumkomboa ndugu yake, wala kumpa Mungu fidia kwa ajili yake, (maana fidia ya nafsi zao ina gharama, wala hana budi kuiacha hata milele;) ili aishi sikuzote asilione kaburi.” Mwandikaji wa zaburi alijua kwamba bei ya ukombozi ilikuwa juu sana, usiweze kupatikana na wanadamu. Kulingana na uwezo wa wanadamu, ukombozi ulikuwa usiowezekana “hata milele,” bila tumaini.
7. Adamu aliuzaje watoto wake, na alipokea nini kutokana na “mnada” huu?
7 Hali hii yenye kusikitisha na ya kutoweza kitu imetufikia sote kwa sababu babu yetu Adamu aliuza watoto wake waliokuwa bado kuzaliwa katika utumwa wa dhambi na mauti, bila idhini (ruhusa) yetu. Ile bei aliyopokea kwa “mnada” huo ilikuwa kufanya alilotaka kufanya kwa choyo, yaani, kujitegemea, kwa kumwasi Mungu. Kila mtu yuko kama Paulo alivyosema alikuwa, yaani, “mtu wa mwilini, nimeuzwa chini ya dhambi.”—Rum. 7:14.
8. Watu wenye moyo mnyofu wanaweza kulilia Mungu namna gani kwa sababu ya utumwa wao?
8 Hivyo, ilimpasa Mungu afanye mipango ili wanadamu wapate kukombolewa. Watu walio na moyo mnyofu wanalia hivi: “Ee Mungu wa wokovu wetu, utusaidie, kwa ajili ya utukufu wa jina lako. Utuokoe, utughofiri dhambi zetu, kwa ajili ya jina lako.”—Zab. 79:9.
MUNGU HAWEZI KUACHILIA DHAMBI
9. Kuhusu (kupatana na) Mungu, watu walikuja katika hali gani?
9 Je! Yehova Mungu anasikia sala hii? Na kama anasikia, je! anaweza kuijibu? Je! kutoweza kitu kwa mwanadamu ni tatizo (taabu) analoweza Mungu kuondoa? Maana hili ni tatizo (taabu) kweli kweli. Lilitokea yapata miaka elfu sita iliyopita. Yule mtu wa kwanza, Adamu, alikuwa ameungana na adui ya Mungu, Shetani, katika kuingiza uovu katika dunia hii. Alijifanya kuwa adui ya Mungu, nao watoto wake wakatenda matendo yasiyo ya haki kwa sababu ya kurithi dhambi na kutokamilika kutoka kwake. Kama mtume Paulo anavyotuambia, Adamu aliingiza jamii ya wanadamu katika hali ya kuwa adui za Mungu.—Rum. 5:10.
10, 11. (a) Ni kwa sababu gani Yehova hangeweza kuachilia dhambi ambayo ilikuwa imeingia katika ulimwengu wote? (b) Ni jambo gani linaloonyesha kwamba kutoona uhalifu kwa uzito kunatokeza matatizo (magumu) makubwa?
10 Hata hivyo, Yehova alipenda viumbe wake, akijua kwamba hawangeweza kujisaidia wenyewe. Lakini, je! angeachilia uovu ambao Shetani pamoja na Adamu walikuwa wameingiza katika ulimwengu wote, kwa kuwapenda wanadamu? Je! Mungu angeweza kumwambia mtu ye yote anayetenda dhambi hivi, ‘Nakupenda, nami nataka nikuonyeshe rehema, basi nitaachilia dhambi yako’? Kupatana na uadilifu wake na haki yake, hangeweza kuachilia dhambi bila kutoa adhabu. Ikiwa angefanya hivi, angekuwa akiharibu msingi wa serikali yake, maana Biblia yasema hivi: “Haki na hukumu ndio msingi wa kiti chako.”—Zab. 89:14.
11 Tuna mfano katika mataifa fulani ya dunia leo, unaoonyesha matokeo ya kutokushikamana na yaliyo haki, ya kuachilia uvunjaji wa sheria. Wamekuwa na uzembe na kukosa bidii mara nyingi ya kuchukulia watenda mabaya hatua. Wahalifu wameachiliwa. Kwa sababu hiyo watu hawana imani na serikali, na mwishowe kila jambo linaharibika. Walakini, yule Mtawala wa Ulimwengu Wote hataruhusu hayo yaharibu sheria ambazo ametunga.
KUMALIZWA KWA MATATIZO (MAGUMU) KUPITIA KWA “UZAO”
12. Mungu alifunuaje njia yake ya kuwaokoa wanadamu Adamu alipokwisha kufanya dhambi?
12 Kulingana na maoni ya wanadamu, hakukuwako na njia ya kuondolea tatizo (gumu) hilo. Lakini Yehova anaondoa kwa njia ya ajabu matatizo (magumu) yanayoonekana kuwa hayawezi kutatuliwa (kuondolewa), akiwa bado anaendeleza adhama (utukufu) ya enzi yake kuu ya ulimwengu wote na kuonyesha rehema wakati uo huo. Tukiisha kuyaona yaliyotokea, twasema, ‘Haingaliweza kufanywa kwa njia nyingine yo yote na kuwa kamili sana, haki na njema kabisa.’ Basi, kama Biblia inavyoonyesha, wakati ule ule Adamu alipohukumiwa kwa sababu ya dhambi yake, Mungu alifunua kwamba angeiokoa jamii ya wanadamu alipotangaza hivi: “Huo [uzao] utakuponda [Shetani] kichwa.” (Mwa. 3:15) Baadaye, Mungu angeonyesha wanadamu utimizo wa kusudi lake.
13. ‘Uzao wa mwanamke’ ulionekana kuwa nani. Na kwa sababu gani ni yeye aliyechaguliwa na Mungu?
13 Ni nani zaidi angechaguliwa na Mungu awe “uzao” huo ambao baadaye ungemponda Shetani kichwa? Mwana wa Yehova mzaliwa pekee! Alichaguliwa kuwa wa kwanza ili amalize suala (sababu ya) linalohusu (linalopatana) kufaa na haki ya utawala au enzi kuu ya Yehova, iliyokuwa imetiliwa mashaka. Kwa sababu gani Yehova alimchagua mkuu huyu aliyekuwa mpendwa wake sana? Shetani alipofanya upinzani wake, alionea mashaka ushikamanifu wa watu wote katika ulimwengu wote, kutia na Mwana huyu wa Mungu. Zaidi ya hayo, suala la ushikamanifu lingemtegemea yeye zaidi ya mwingine ye yote kati ya viumbe vya Mungu, kwa sababu yeye ndiye aliyekuwa Mwana wa Yehova aliye mkuu kuliko na wa pili Kwake katika ulimwengu wote.
14. Mwana wa Mungu alionaje juu ya wanadamu?
14 Tena, katika Mithali, sura ya nane, Mwana huyu, akifananishwa na hekima, anasema juu ya kazi ya Mungu ya uumbaji hivi: “Furaha yangu ilikuwa pamoja na wanadamu.” (Mst. 31) Alipenda sana wanadamu. Alikubali mgawo huu kwa furaha amtetee Baba yake, kwa kuonyesha ushikamanifu Kwake kwanza na, tena, kwa upendo aliokuwa nao kwa wanadamu.
15. Ni kwa sababu gani Mungu ameruhusu dhambi iendelee?
15 Kwa sababu ya suala la ulimwengu wote, Yehova Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote hangeweza kuifuta dhambi wakati huo; ilimpasa aiache kwa muda ili amalize lile suala la enzi yake kuu na la ushikamanifu wa jamaa yake kuu ya viumbe vyenye akili. Ilimpasa vilevile awe na wakati wa kuweka msingi wa kuondolewa kwa dhambi kisha awaruhusu wanadamu nafasi ya kujifunza juu ya mipango yake na kuifuata. Kwa hiyo, Mungu ameruhusu kutenda mabaya kuweko kwa kusudi jema na kwa muda ulio mfupi kwa kadiri. Kwa kweli, njia ambayo Mungu amechagua, ndiyo njia peke yake anayoweza kusaidia sana nayo wanadamu.
MSINGI HALALI WA KUTENDEA WANADAMU
16. Ni kwa sababu gani Mungu alihitaji msingi halali wa kutendea wanadamu?
16 Basi, ili ashughulike (ashirikiane) na wale waliozaliwa katika dhambi, ijapokuwa si kwa kosa lao wenyewe, Mungu alipaswa awe na msingi halali wa kuwatendea wanadamu. Bila hivyo, ingaliwapasa wanadamu wote wafe milele, kwa vile sheria ya Mungu ilivyotaka watenda dhambi waondolewe katika ulimwengu wote. Dhabihu ya mwanadamu mwingine, aliye mkamilifu, akiwa kama bei “yenye thamani” (bei) ambayo wanadamu hawangeweza kufikia, ndiyo ingeweza peke yake kukomboa kile ambacho Adamu alikuwa amepoteza, ikiondoa ile hukumu ambayo wanadamu walihukumiwa nayo na baraza ya haki ya Mungu. Yesu alisema juu ya hili hivi: “Kama vile Mwana wa watu asivyokuja kutumikiwa, lakini kutumikia, na kutoa uzima wake uwe ukombozi kwa watu wengi.”—Mt. 20:28, Zaire Swahili Bible.
17, 18. Mungu angekuwa akionyesha nini kwa kuweka msingi huu wa halali?
17 Kwa kuweka msingi huu wa halali, Yehova angeonyesha kufaa kwa utawala wake wa ulimwengu wote. Vilevile angeweza kuwarehemu wanadamu. Mtume Paulo anaeleza hili kwa njia hii:
18 “Kwa sababu wote wamefanya dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu; wanahesabiwa haki bure kwa neema yake, kwa njia ya ukombozi ulio katika Kristo Yesu; ambaye Mungu amekwisha kumweka awe upatanisho [yaani, kifuniko cha dhambi] kwa njia ya imani katika damu yake, ili aonyeshe haki yake, . . . wakati huu, ili awe mwenye haki na mwenye kumhesabia haki yeye amwaminiye Yesu.”—Rum. 3:23-26.
19. Mwanadamu wanapataje msimamo mzuri na Yehova Mungu?
19 Kwa kweli, Mungu anashughulika (anashirikiana) na wanadamu kupitia kwa Mwanawe, Yesu Kristo, anayemwakilisha Yehova katika jambo hili. Ile dhabihu ya uhai wake ilitoa malipo ya hukumu, ikiinunua jamii ya wanadamu. Ndipo, wale wanaoutii mpango wa Mungu wanaweza kuwa na hali ya halali inayokubaliwa na Yeye. Mtume Paulo alisema juu ya hatua hii yenye rehema ya Yehova na Mwanawe hivi: “Kwa maana kuna Mungu mmoja, na mpatanishi mmoja kati ya Mungu na wanadamu, mwanadamu Kristo Yesu, ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi unaolingana kwa ajili ya wote.”—1 Tim. 2:5, 6, NW.
20. Mwana wa Mungu alipaswa atimize nini alipokuwa duniani?
20 Katika hekima yake, Mungu alikusudia njia moja tu ambayo kwa hiyo angeweza kusaidia wanadamu wawe na hali ya haki na kutumainia uzima wa milele kama washiriki wa jamaa yake safi, yenye haki na ukamilifu ya ulimwengu wote. Mungu alionyesha ukarimu wake mkuu zaidi ulipofika wakati wake unaofaa. Alimtuma Mwanawe duniani kutoka mbinguni, awe mwanadamu. Akiwa hapa duniani Mwana huyu angeweza kuonyesha kwanza kwamba wanadamu wakamilifu wanaompenda Mungu wanaweza kushikamana na Mungu na utawala wake katika jaribu lo lote au kila hali. Uhai wake ungekuwa bei ya kukombolea wanadamu, maana kati yao hakupatikana mtu wa kutoa bei hii. Bila shaka, jambo hili lingemtaka afe.—Tito 2:11-14.
21. Kulingana na 1 Yohana 2:1. 2, maisha ya uaminifu ya Yesu yalimstahilisha awe nini?
21 Kwa mwendo huu wa uaminifu Yesu alistahili kuwa Msaidizi wa wote wanaotamani kumtumikia Mungu. Mtume Yohana aliandika hivi: “Mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki, naye ndiye kipatanisho [kifaniko] kwa dhambi zetu.”—1 Yohana 2:1, 2.
22. Ni kwa sababu gani watumishi waaminifu wa Mungu hawapotezi msimamo wao uliokubalika wanapopungukiwa katika njia fulani?
22 Tangu wakati wa Habili mwana wa Adamu, Ibilisi amejaribu kulaumu watumishi wa Mungu. Sana sana Shetani anaitwa “mshitaki wa ndugu zetu, yeye awashitakiye mbele za Mungu wetu, mchana na usiku” (Ufu. 12:10) Hivyo, katika kushindania ukamilifu, Yesu Kristo ametokea mbele za Mungu kama msaidizi kwa wakati unaofaa. Yeye ana ruhusa ya kukikaribia kiti cha enzi cha Mungu kwa ajili yetu. Wakati watumishi waaminifu wa Mungu wamekosea, wamefanya dhambi, wakatubu na kuungama kwa moyo mnyofu, Yesu ametoa uzuri wa dhabihu yake ili wasiuawe—maana dhabihu yake ya upatanisho inaweza kufunika makosa na dhambi zao.
23. Ni maoni gani tunayopaswa kuendeleza juu ya hali yetu yenye dhambi?
23 Mtume Paulo anasimulia vita vyake na vya Wakristo wengine wote, na namna bila kukusudia na kutaka, wanavyofanya makosa ijapokuwa wanajitahidi sana. Alisema hivi: “Lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo. Basi kama lile nisilolipenda ndilo nilitendalo, si mimi nafsi yangu nilitendaye, bali ni ile dhambi ikaayo ndani yangu.” (Rum. 7:19, 20) Ubora wa dhabihu ya Kristo yenye kufunika dhambi zao wanazozitubia na kuziungama, ndio msingi wa kuwatangaza kuwa wenye haki. —1 Yohana 1:9.
24. Katika cheo chake kama msaidizi. Yesu anawezaje kuonyesha kwamba mashtaka ya Shetani ni ya uongo?
24 Vilevile, katika cheo chake cha msaidizi, Yesu ameonyesha mbele za Mungu kwamba mashtaka ya Ibilisi juu ya Wakristo ni uchongezi mtupu. Anaonyesha matendo yenye imani ya Wakristo na namna wanavyomwomba Mungu katika toba la kweli wanapofanya dhambi. Maana kama inavyoelezwa katika Waebrania 6:10, anajua kwamba: “Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu, na hata hivi sasa mngali mkiwahudumia.” Vilevile Yesu ameonyesha mbele ya baraza ya mbinguni kwamba watumishi wa Mungu duniani wamefahamu kutoweza kwao na ukosefu wao wa haki wakaomba rehema kupitia kwa dhabihu ya Kristo—njia aliyoweka Mungu.
25. Ni kwa sababu gani wale walio na umoja na Kristo hawana hukumu ya adhabu juu yao?
25 Naye Yehova Mungu amekubali maombezi ambayo Yesu anawatolea. Ibilisi ameshindwa katika kila shambulio ambalo amefanya. Kwa njia hiyo Yesu ametimiza ukuhani wake mkuu kwa ushikamanifu, akiwalinda na hukumu yote, kama Biblia inavyosema: “Sasa, basi, hakuna hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo Yesu. Kwa sababu sheria ya [roho ya] uzima ule ulio katika Kristo Yesu imeniacha huru, mbali na sheria ya dhambi ya mauti.”—Rum. 8:1, 2.
26, 27. Ni kwa njia gani watu mmoja mmoja wanaweza kuzaliwa kama watoto wa Kristo, wakiwa na msimamo safi mbele za Mungu?
26 Nabii Isaya anatusaidia zaidi tufahamu jinsi Kristo anavyowapa uzima halisi wale wanaomwamini. Isaya aliandika kwa kutoa unabii wa mateso ya Kristo akisema juu ya Yehova hivi: “Utakapofanya nafsi yake kuwa dhabihu kwa dhambi, ataona uzao wake.” (Isa. 53:10) Kristo hapati uzao kwa njia ya kawaida. Alipokuwa duniani, alikuwa na uwezo wa kujizalia watoto. Lakini hakuwa na watoto hao. Badala yake, aliutoa uwezo huo katika dhabihu yake. Kama alivyosema: “Mwana wa Adamu alivyokuja . . . kutoa nafsi yake ukombozi badala ya wengi.”—Mt. 20:28, NW.
27 Kwa hiyo Yesu akawa “Adamu wa mwisho.” Adamu alizaa watoto wasiokamilika, wenye tabia mbaya. Yesu Kristo alizaa watoto wanaofikia haki. Watu mmoja mmoja wanaweza kutoka katika jamaa ya Adamu wazaliwe upya kupitia kwa haki ya Yesu Kristo na, kwa kuuvaa utu mpya, wanaweza kuwa ‘katika mfano wake.’ Wanaweza kusafishwa wawe wana wa “Baba wa milele,” yule “Adamu wa mwisho.” Yehova‘amefanya nafsi yake kuwa dhabihu kwa dhambi,’ na kukubali dhabihu hii ili dhambi za wote walio na imani zifunikwe.—1 Kor. 15:45; Isa. 9:6.
28. Yesu anazalia nani jamaa ya wanadamu wakamilifu?
28 Kwa kweli, kwa sababu ya mambo ambayo Yehova Mungu na Yesu Kristo wamefanyia wanadamu, maisha yetu yanaweza kuwa na kusudi. Wote wanaojifaidi na dhabihu ya Yesu yenye kufunika dhambi wakati wa utawala wake akiwa Mfalme-kuhani wanaweza kuwa watoto wakamilifu wa kibinadamu wa Mwana wa Mungu. Hii vilevile inaongoza kwenye kuhesabiwa kuwa wana wa Aliye Juu Zaidi milele na kuishi katika hali zenye haki. Namna gani hivyo? Kwa sababu Yesu hazai jamaa iwe yake mwenyewe. Baada ya kuwaleta kwenye ukamilifu wa kibinadamu, anawatoa wanadamu hawa walionunuliwa na kutengenezwa kwa Yehova Mungu, “Baba, . . . ambaye kwa jina lake ubaba wote wa mbinguni na wa duniani unaitwa,” ili Mungu ajaribu ushikamanifu na kustahili kwao kuwa watoto wake milele.—Efe. 3:14,15; 1 Kor. 15:26, 28.