Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • kr sura 16 kur. 170-181
  • Kukusanyika Pamoja kwa Ajili ya Ibada

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kukusanyika Pamoja kwa Ajili ya Ibada
  • Ufalme wa Mungu Unatawala!
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Tukusanyike Pamoja?
  • Mikutano ya Kila Juma Ambayo Huchochea “Upendo na Matendo Mazuri”
  • Mkutano Muhimu Zaidi Katika Mwaka
  • Mtazamo Wetu Unafunua Nini?
  • Mikutano ‘Inayotuchochea Katika Upendo na Matendo Mazuri’
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Mikutano Kwa Ajili ya Ibada, Funzo, na Kitia-moyo
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Unaalikwa kwa Uchangamfu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Mikutano ya Mashahidi wa Yehova Inaweza Kukunufaishaje?
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
Pata Habari Zaidi
Ufalme wa Mungu Unatawala!
kr sura 16 kur. 170-181

SURA YA 16

Kukusanyika Pamoja kwa Ajili ya Ibada

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Kuchunguza historia na umuhimu wa mikutano yetu

1. Wanafunzi walipokusanyika pamoja walipata msaada gani, na kwa nini walihitaji msaada huo?

MUDA mfupi baada ya Yesu kufufuliwa, wanafunzi wake walikusanyika pamoja ili kutiana moyo. Hata hivyo, walifunga milango kwa sababu ya kuogopa maadui wao. Woga wao ulitoweka Yesu alipotokea katikati yao na kuwaambia: “Pokeeni roho takatifu”! (Soma Yohana 20:19-22.) Baadaye, mitume walikusanyika tena pamoja, na Yehova akawamiminia roho takatifu. Walipata nguvu za kufanya kazi ya kuhubiri iliyokuwa mbele yao!—Mdo. 2:1-7.

2. (a) Yehova anatupatia nguvu jinsi gani, na kwa nini tunahitaji nguvu hizo? (b) Kwa nini mpango wa Ibada ya Familia ni muhimu sana? (Ona maelezo ya chini na sanduku “Ibada ya Familia,” ukurasa wa 175.)

2 Tunakabiliana na hali ileile ambayo ndugu zetu wa karne ya kwanza walikabili. (1 Pet. 5:9) Nyakati nyingine, huenda baadhi yetu tukaogopa wanadamu. Na tunahitaji nguvu ambazo Yehova hutoa ili tuvumilie katika kazi ya kuhubiri. (Efe. 6:10) Yehova hutoa kiasi kikubwa cha nguvu hizo kupitia mikutano yetu. Leo tuna fursa ya kuhudhuria mikutano mitano kwa juma—Mkutano wa Watu Wote, Funzo la Mnara wa Mlinzi, Funzo la Biblia la Kutaniko, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na Mkutano wa Utumishi.a Pia, tunafurahia matukio manne kila mwaka—kusanyiko la kanda, makusanyiko mawili ya mzunguko, na Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Kwa nini ni muhimu tuhudhurie mikutano hiyo yote? Mikutano ya siku za kisasa ilianzaje? Na mtazamo wetu kuhusu mikutano unafunua nini kutuhusu?

Kwa Nini Tukusanyike Pamoja?

3, 4. Yehova anataka watu wake wafanye nini? Toa mifano.

3 Tangu zamani Yehova amewataka watu wake wakusanyike pamoja ili kumwabudu. Kwa mfano, katika mwaka wa 1513 K.W.K. Yehova alilipa taifa la Israeli Sheria yake, na Sheria hiyo ilitia ndani Sabato ya kila juma ili kwamba kila familia iweze kumwabudu na kufundishwa Sheria hiyo. (Kum. 5:12; 6:4-9) Waisraeli walipofuata amri hiyo, familia ziliimarishwa na taifa lote kwa ujumla lilibaki likiwa safi na imara kiroho. Taifa hilo lilipokataa kufuata Sheria, na kupuuza matakwa kama vile kukusanyika kwa ukawaida ili kumwabudu Yehova, walipoteza kibali cha Mungu.—Law. 10:11; 26:31-35; 2 Nya. 36:20, 21.

4 Fikiria pia mfano ambao Yesu aliweka. Alikuwa na desturi ya kwenda katika sinagogi kila juma siku ya Sabato. (Luka 4:16) Baada ya Yesu kufa na kufufuliwa, wanafunzi wake waliendelea na desturi ya kukusanyika pamoja kwa ukawaida licha ya kwamba hawakuwa tena chini ya sheria ya Sabato. (Mdo. 1:6, 12-14; 2:1-4; Rom. 14:5; Kol. 2:13, 14) Kwenye mikutano hiyo, Wakristo wa karne ya kwanza walifundishwa na kutiwa moyo, na pia walimtolea Mungu dhabihu za sifa kupitia sala, maelezo yao, na nyimbo.—Kol. 3:16; Ebr. 13:15.

Baada ya kufufuliwa, Yesu walitokea wanafunzi wake katika chumba walichokuwa wamekusanyika

Wanafunzi wa Yesu walikusanyika pamoja ili kuimarishana na kutiana moyo

5. Kwa nini tunahudhuria mikutano ya kila juma na makusanyiko ya kila mwaka? (Ona pia sanduku “Makusanyiko ya Kila Mwaka Ambayo Huwaunganisha Watu wa Mungu,” ukurasa wa 176.)

5 Sisi pia, tunapohudhuria mikutano yetu ya kila juma, makusanyiko ya kila mwaka, tunaonyesha kwamba tunaunga mkono Ufalme wa Mungu, tunatiwa nguvu na roho takatifu, na kuwatia moyo wengine kwa maelezo yanayoonyesha imani yetu. Jambo muhimu zaidi ni kwamba tuna fursa ya kumwabudu Yehova kupitia sala zetu, maelezo, na nyimbo. Utaratibu wa mikutano yetu huenda ukawa tofauti na ule ambao Waisraeli na Wakristo wa karne ya kwanza walifuata, lakini mikutano yetu ina umuhimu uleule. Mikutano yetu ya siku za kisasa ilianzaje?

Mikutano ya Kila Juma Ambayo Huchochea “Upendo na Matendo Mazuri”

6, 7. (a) Mikutano yetu ina kusudi gani? (b) Mikutano ilitofautianaje kati ya kikundi kimoja na kingine?

6 Ndugu Charles Taze Russell alipoanza kuitafuta kweli katika Neno la Mungu, aliona umuhimu wa kukusanyika pamoja na wale waliokuwa na lengo kama lake. Mwaka wa 1879, Russell aliandika hivi: “Mimi, pamoja na wale nilioshirikiana nao huko Pittsburgh, tulipanga na kuendeleza darasa la biblia kwa ajili ya kuchunguza Maandiko, tukikusanyika kila Jumapili.” Wasomaji wa Zion’s Watch Tower walitiwa moyo wakusanyike pamoja, na kufikia mwaka wa 1881, mikutano ilikuwa ikifanywa huko Pittsburgh, Pennsylvania, kila Jumapili na Jumatano. Toleo la Novemba 1895 la Mnara wa Mlinzi lilisema kwamba kusudi la mikutano hiyo ilikuwa kusitawisha “ushirika wa Kikristo, upendo na ushirikiano” na wale waliohudhuria walipata fursa ya kutiana moyo.—Soma Waebrania 10:24, 25.

7 Kwa miaka mingi, utaratibu na mara ambazo mikutano hiyo ilifanywa zilitofautiana kati ya kikundi kimoja cha Wanafunzi wa Biblia na kingine. Kwa mfano, barua iliyoandikwa na kikundi kimoja nchini Marekani ambayo ilichapishwa mwaka wa 1911 ilisema hivi: “Tunafanya angalau mikutano mitano kila juma.” Walifanya mikutano hiyo siku za Jumatatu, Jumatano, Ijumaa, na mara mbili siku ya Jumapili. Barua nyingine kutoka kikundi kimoja barani Afrika iliyochapishwa mwaka wa 1914 ilisema hivi: “Tunafanya mikutano mara mbili kwa mwezi, tunaanza Ijumaa na kumaliza Jumapili.” Hata hivyo, baadaye, utaratibu tunaofuata leo katika mikutano yetu ulianzishwa. Chunguza kwa ufupi historia ya kila mkutano.

8. Baadhi ya hotuba za mapema zilizungumzia habari gani?

8 Mkutano wa Watu Wote. Katika mwaka wa 1880, mwaka mmoja baada ya Ndugu Russell kuanza kuchapisha gazeti Zion’s Watch Tower, alifuata mfano uliowekwa na Yesu na akaanza safari ya kuhubiri. (Luka 4:43) Kwa kufanya hivyo, Ndugu Russell aliweka kielelezo cha mkutano ambao leo unaitwa Mkutano wa Watu Wote. Likitangaza safari hiyo, gazeti Mnara wa Mlinzi lilisema kwamba Russell “angependa kuhutubia mikutano ya hadhara kuhusu ‘Mambo yanayohusiana na ufalme wa Mungu.’” Katika mwaka wa 1911, baada ya madarasa au makutaniko, kuanzishwa katika nchi nyingi, kila darasa lilitiwa moyo kumchagua msemaji anayestahili kwenda katika maeneo ya karibu na kutoa mfululizo wa hotuba sita zilizozungumzia habari kama vile hukumu na fidia. Mwishoni mwa kila hotuba, jina la msemaji na kichwa cha hotuba ya juma lililofuata kilitangazwa.

9. Mkutano wa Watu Wote umebadilikaje kadiri miaka ilivyopita, na unawezaje kuunga mkono mkutano huo?

9 Katika mwaka wa 1945, gazeti Mnara wa Mlinzi lilitangaza kuanzishwa kwa kampeni ya ulimwenguni pote ya Mkutano wa Watu Wote uliotia ndani mifululizo ya hotuba nane za Biblia zilizozungumzia “matatizo yaliyopaswa kushughulikiwa haraka wakati huo.” Kwa miaka mingi, wasemaji walitumia habari walizopewa na mtumwa mwaminifu na pia walijitayarishia mihtasari yao wenyewe. Hata hivyo, mwaka wa 1981, wasemaji wote walielekezwa watoe hotuba zinazotegemea mihtasari ambayo makutaniko yalitumiwa.b Kabla ya mwaka wa 1990, baadhi ya mihtasari ya hotuba za watu wote ilihusisha mazungumzo pamoja na wasikilizaji au maonyesho; lakini katika mwaka huo maagizo yalibadilishwa, na kuanzia wakati huo na kuendelea, mihtasari hiyo ilitolewa kwa njia ya hotuba tu. Badiliko lingine lilifanywa Januari 2008, muda wa hotuba za watu wote ulipopunguzwa kutoka dakika 45 hadi dakika 30. Hata ingawa hotuba za watu wote zimefanyiwa mabadiliko, hotuba zilizotayarishwa vizuri zinaendelea kujenga imani katika Neno la Mungu na kutufundisha mambo mbalimbali yanayohusu Ufalme wa Mungu. (1 Tim. 4:13, 16) Je, unawaalika kwa shauku wale wote unaowafanyia ziara za kurudia na watu wengine ambao si Mashahidi kuja kusikiliza hotuba hizo muhimu zinazotegemea Biblia?

10-12. (a) Funzo la Mnara wa Mlinzi limefanyiwa mabadiliko gani? (b) Ingefaa ujiulize maswali gani?

10 Funzo la Mnara wa Mlinzi. Katika mwaka wa 1922, ndugu waliojulikana kama mapilgrimu—wahudumu waliotumwa na shirika la Watch Tower Society ili kutoa hotuba makutanikoni na kuongoza katika kazi ya kuhubiri—walipendekeza kwamba kuwe na mkutano wa kawaida wa kujifunza gazeti Mnara wa Mlinzi. Pendekezo hilo lilikubaliwa, na mwanzoni mafunzo ya Mnara wa Mlinzi yalifanywa katikati ya juma au Jumapili.

Mkutano wa Wanafunzi wa Biblia nchini Ghana katika mwaka wa 1931

Funzo la Mnara wa Mlinzi, nchini Ghana, 1931

11 Gazeti Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 1932, lilitoa mwongozo zaidi jinsi ambavyo mkutano huo ulipaswa kufanywa. Ikitumia funzo lililofanywa Betheli kama kielelezo, makala hiyo ilieleza kwamba ndugu alipaswa kuongoza mkutano huo. Ndugu watatu wangekaa mbele na kusoma mafungu kwa zamu. Wakati huo makala hazikuwa na maswali, hivyo kiongozi wa funzo aliambiwa awaombe wasikilizaji waulize maswali kuhusu habari iliyokuwa ikizungumziwa. Kisha angewaalika wasikilizaji kujibu maswali hayo. Ikiwa ufafanuzi zaidi ulihitajika, aliyekuwa anaongoza aliambiwa atoe maelezo “mafupi na yaliyo wazi.”

12 Mwanzoni, kila kutaniko liliruhusiwa kuchagua toleo la gazeti ambalo wengi walitaka kujifunza. Hata hivyo, gazeti Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1933 lilipendekeza kwamba makutaniko yote yatumie toleo la karibuni. Katika mwaka wa 1937, mwongozo ulitolewa kwamba funzo hilo linapaswa kufanywa siku ya Jumapili. Marekebisho zaidi yaliyotokeza utaratibu wa mkutano tunaofuata leo, yalichapishwa katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 1942. Kwanza, gazeti hilo lilitangaza kwamba sehemu ya chini ya kila ukurasa katika makala ya funzo itakuwa na maswali, na maswali hayo ndiyo yanayopaswa kutumiwa. Kisha, likasema kwamba mkutano huo ulipaswa kufanywa kwa saa moja. Na pia liliwatia moyo wale waliokuwa wakitoa majibu kujieleza “kwa maneno yao wenyewe” badala ya kusoma sehemu fulani ya fungu. Funzo la Mnara wa Mlinzi linaendelea kuwa njia kuu ambayo mtumwa mwaminifu anatumia kutoa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. (Mt. 24:45) Inafaa kila mmoja wetu ajiulize: ‘Je, ninatayarisha funzo la Mnara wa Mlinzi kila juma? Na je, ninajitahidi kutoa maelezo inapowezekana?’

13, 14. Eleza historia ya Funzo la Biblia la Kutaniko, na jambo unalofurahia kuhusu mkutano huo.

13 Funzo la Biblia la Kutaniko. Mwanzoni mwa miaka ya 1890, baada ya mabuku kadhaa ya Millennial Dawn kutolewa, Ndugu H. N. Rahn, Mwanafunzi wa Biblia aliyeishi katika jiji la Baltimore, Maryland, Marekani, alipendekeza kuwe na “Vikundi vya Mapambazuko” kwa ajili ya kujifunza Biblia. Mwanzoni, mikutano hiyo ambayo mara nyingi ilifanywa katika nyumba za watu, ilikuwa ya majaribio. Hata hivyo, kufikia Septemba 1895, kulikuwa na Vikundi vya Mapambazuko katika majiji mengi ya Marekani. Hivyo, gazeti Mnara wa Mlinzi la mwezi huo lilipendekeza kwamba wanafunzi wote wa ile kweli wafanye mikutano hiyo. Lilielekeza kwamba yule aliyekuwa akiongoza alipaswa kuwa msomaji mzuri. Alipaswa kusoma sentensi na kisha asubiri waliohudhuria watoe maelezo. Baada ya kusoma kila sentensi katika fungu na kuzizungumzia, alipaswa kusoma maandiko yalionyeshwa. Mwishoni mwa sura, kila mtu aliyehudhuria alieleza kwa ufupi mambo yaliyozungumziwa.

14 Jina la mkutano huo lilibadilishwa mara kadhaa. Lilibadilishwa na kuitwa Vikundi vya Kiberoya kwa Ajili ya Funzo la Biblia, likirejelea Waberoya wa karne ya kwanza ambao walichunguza Maandiko kwa uangalifu. (Mdo. 17:11) Baada ya muda, jina hilo lilibadilishwa na kuwa Funzo la Kitabu la Kutaniko. Sasa mkutano huo unaitwa Funzo la Biblia la Kutaniko, na kutaniko zima hukutanika pamoja katika Jumba la Ufalme badala ya kukutana kwenye vikundi katika nyumba za watu. Kwa miaka mingi, vitabu, broshua, na hata makala za gazeti Mnara wa Mlinzi zimetumiwa kwa ajili ya funzo hilo. Tangu mwanzoni, wote waliohudhuria walitiwa moyo kushiriki katika mkutano huo. Mkutano huo umechangia sana kuongeza ujuzi wetu wa Biblia. Je, unajitayarisha kwa ukawaida na kushiriki katika mkutano huo kadiri uwezavyo?

Wazazu na binti zao wadogo wakifurahia ibada ya familia pamoja

Je, ibada ya familia ni sehemu ya ratiba yako ya kila juma?

IBADA YA FAMILIA

KADIRI siku za mwisho zinavyosonga, tengenezo la Yehova limekazia fikira zaidi uhitaji wa kila familia kuwa na ratiba ya kujifunza Biblia. (2 Tim. 3:1) Kwa mfano, kijitabu Home and Happiness kilichochapishwa mwaka wa 1932 kilisema hivi waziwazi: “Kila familia na ianze haraka iwezekanavyo kuwa na funzo la Biblia nyumbani.” Na gazeti Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 1956, lilihimiza familia zote za Kikristo “zijifunze Biblia kwa ukawaida katika nyumba zao kwa manufaa ya familia nzima.” Kisha likauliza: “Je, familia yako imetenga jioni fulani ili kujifunza pamoja gazeti Mnara wa Mlinzi kabla ya mkutano?”

Katika mwaka wa 2009, tengenezo lilikazia umuhimu wa funzo la familia kwa kurekebisha ratiba ya mikutano ya katikati ya juma; kuanzia wakati huo na kuendelea, Funzo la Biblia la Kutaniko lilipaswa kufanywa pamoja na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi. Huduma Yetu ya Ufalme ya Januari 2011 ilisema hivi: “Sababu moja ya badiliko hilo ilikuwa kuzisaidia familia kupata nafasi ya kuimarisha uhusiano wao pamoja na Yehova kwa kupanga jioni hususa kila juma kwa ajili ya ibada ya familia.” Kisha ikaendelea kusema hivi: ‘Tumieni wakati huo kuwa na mazungumzo ya Biblia yasiyo ya haraka na funzo linalokusudiwa kushughulikia mahitaji ya familia.’c

Kwa nini mpango wa Ibada ya Familia ni muhimu sana—jambo ambalo hatupaswi kukosa? Kwa sababu inaimarisha hali ya kiroho ya familia na ya kutaniko pia. Kwa mfano: Kutaniko linaweza kufananishwa na nyumba iliyojengwa kwa matofali. (Soma Waebrania 3:4-6.)d Uimara wa ukuta wa nyumba hiyo unategemea vitu viwili—ubora wa msingi wa nyumba hiyo na ugumu wa tofali moja-moja. Ikiwa msingi ni dhaifu, nyumba itabomoka. Lakini hata nyumba yenye msingi imara itabomoka kwa urahisi ikiwa matofali yanavunjika-vunjika. Kutaniko la Kikristo limejengwa kwenye msingi imara, yaani mafundisho ya Kristo. (Soma 1 Wakorintho 3:10-15.)e Watu mmoja-mmoja na familia katika kutaniko ni kama matofali. Vipindi vya Ibada ya Familia vinatoa fursa ya pekee kwa kila mtu na familia kujenga na kudumisha imani isiyoweza kushika moto. Watu mmoja-mmoja wenye imani imara, na familia zenye imani thabiti hufanyiza makutaniko imara. Je, ibada ya familia ni sehemu ya ratiba yako ya kila juma?

c Baadhi ya mapendekezo ya habari ambazo zinaweza kutumiwa wakati wa ibada ya familia yanapatikana katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Januari 2011.

d Maneno ya Paulo yanaelekezwa kwa wale ambao wana “mwito wa mbinguni.” (Ebr. 3:1) Hata hivyo, kanuni iliyo kwenye shauri hilo inawahusu Wakristo wote.

e Kwa maelezo zaidi kuhusu Andiko hilo, ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 1999, ukurasa wa 12-14, fungu la 15-20. Kwa nini usisome habari hiyo na utafakari jinsi unavyoweza kuitumia katika Ibada yenu ya Familia?

15. Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ina kusudi gani?

15 Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Carey Barber, ambaye wakati huo alikuwa akitumikia katika makao makuu huko Brooklyn, New York, alisema hivi: “Jumatatu usiku, Februari 16, 1942, ndugu wote katika familia ya Betheli ya Brooklyn walialikwa wajiandikishe katika shule ambayo baadaye ilikuja kuitwa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.” Ndugu Barber, ambaye miaka mingi baadaye alikuja kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, aliifafanua shule hiyo kuwa “mojawapo ya njia muhimu sana ambazo Yehova ametumia kuwafundisha watu wake katika siku za kisasa.” Shule hiyo ilifanikiwa sana kuwasaidia akina ndugu kuboresha ustadi wao wa kufundisha na kuhubiri, hivi kwamba kuanzia mwaka wa 1943, kijitabu Course in Theocratic Ministry kilitolewa hatua kwa hatua katika makutaniko ulimwenguni pote. Gazeti Mnara wa Mlinzi la Juni 1, 1943, lilisema kwamba Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ilikusudiwa kuwasaidia watu wa Mungu “kujizoeza wenyewe ili wawe mashahidi wazuri katika kuutangaza Ufalme.”—2 Tim. 2:15.

16, 17. Je, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inafundisha ustadi wa kufundisha tu? Eleza.

16 Mwanzoni, wengi waliona ilikuwa vigumu kutoa hotuba mbele ya watu wengi. Clayton Woodworth, Jr., ambaye baba yake alifungwa isivyo haki pamoja na Ndugu Rutherford na wengine mwaka wa 1918, alikumbuka jinsi alivyohisi alipojiunga na shule hiyo mwaka wa 1943. Ndugu Woodworth alisema hivi: “Ilikuwa vigumu kwangu kutoa hotuba, ulimi wangu ulionekana kana kwamba umekuwa mrefu, mdomo wangu ulikauka, na sauti yangu ikabadilika.” Hata hivyo, uwezo wa Clayton ulipoendelea kuboreshwa, alipata mapendeleo mengi ya kutoa hotuba mbele za watu. Shule hiyo ilimfundisha mambo mengi zaidi ya ustadi wa kufundisha. Ilimfundisha umuhimu wa unyenyekevu na kumtegemea Yehova. Alisema hivi: “Nilikuja kutambua kwamba haitoshi tu kuwa msemaji. Bali ikiwa msemaji atajitayarisha vizuri na kumtegemea Yehova, wasikilizaji watafurahia kumsikiliza na watajifunza jambo fulani.”

17 Katika mwaka wa 1959, akina dada walialikwa kujiandikisha katika shule hiyo. Dada Edna Bauer anakumbuka akisikia tangazo hilo likitolewa kwenye kusanyiko alilohudhuria. Alisema hivi: “Nakumbuka jinsi akina dada walivyosisimka. Sasa walikuwa na fursa nyingi.” Iwe wewe ni mwanaume au mwanamke, je, umetumia fursa hii kujiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ili ufundishwe na Yehova?—Soma Isaya 54:13.

18, 19. (a) Mkutano wa Utumishi unafuata kielelezo gani? (b) Kwa nini sisi huimba kwenye mikutano yetu? (Ona sanduku “Kuimba Kuhusu Kweli.”)

18 Mkutano wa Utumishi. Hata kabla ya mwaka wa 1919, mikutano ilikuwa ikifanywa ili kupanga utumishi wa shambani. Wakati huo, si wote katika kutaniko waliohudhuria mikutano hiyo—ni wale tu waliohusika moja kwa moja kugawa machapisho. Karibu muda wote wa mwaka wa 1923, Mkutano wa Utumishi ulifanywa mara moja kwa mwezi, na wote katika darasa, au kutaniko walipaswa kuhudhuria. Kufikia mwaka wa 1928, makutaniko yalihimizwa kufanya Mkutano wa Utumishi kila juma, na katika mwaka wa 1935, gazeti Mnara wa Mlinzi liliyatia moyo makutaniko yote yatumie habari zilizochapishwa katika kijitabu Director (baadaye kiliitwa Informant na sasa, Huduma Yetu ya Ufalme) katika Mkutano wa Utumishi. Punde si punde, mkutano huo ukaanza kufanywa kwa ukawaida katika kila kutaniko.

19 Mkutano wa Utumishi unaendelea kufuata kielelezo kilichowekwa na Kristo, kwa kutupatia mwongozo unaofaa tunaposhiriki katika kazi ya kuhubiri. (Mt. 10:5-13) Ikiwa unastahili kupata nakala ya Huduma Yetu ya Ufalme, je, unaisoma na kutumia mapendekezo yanayotolewa unaposhiriki katika huduma?

Mkutano Muhimu Zaidi Katika Mwaka

Kutaniko la Wakristo wa mapema waiadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Yesu

Tangu karne ya kwanza W.K., Wakristo wamekusanyika pamoja kila mwaka ili kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo (Ona fungu la 20)

20-22. (a) Kwa nini sisi hukumbuka kifo cha Yesu? (b) Unapata faida gani kwa kuhudhuria Ukumbusho wa kila mwaka?

20 Wafuasi wa Yesu waliambiwa wakumbuke kifo chake hadi atakapowasili. Kama ilivyokuwa kwa sherehe ya Pasaka, Ukumbusho wa kifo cha Kristo ni tukio linalofanywa mara moja kwa mwaka. (1 Kor. 11:23-26) Kila mwaka mamilioni ya watu huhudhuria mkutano huo. Unawakumbusha watiwa-mafuta kuhusu pendeleo lao la kuwa warithi wa Ufalme. (Rom. 8:17) Na unawachochea kondoo wengine kumheshimu sana Mfalme wa Ufalme wa Mungu na kuwa washikamanifu kwake.—Yoh. 10:16.

21 Ndugu Russell na wenzake walitambua umuhimu wa kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana na walijua kwamba ulipaswa kufanywa mara moja kwa mwaka. Gazeti Mnara wa Mlinzi la Aprili 1880 lilisema hivi: “Kwa miaka kadhaa imekuwa desturi ya wengi wetu hapa Pittsburgh . . . kukumbuka Pasaka [Ukumbusho] na kula mifano ya mwili na damu ya Bwana wetu.” Punde si punde, makusanyiko yalianza kufanywa baada ya Ukumbusho. Rekodi ya kwanza kuchukuliwa kwa ajili ya tukio kama hilo ilikuwa mwaka wa 1889, ambapo watu 225 walihudhuria na 22 wakabatizwa.

22 Leo, hatufanyi tena Ukumbusho kuwa sehemu ya programu ya kusanyiko, badala yake tunawaalika watu wote katika jamii tunayoishi waungane nasi katika Jumba la Ufalme au kumbi tulizokodi. Katika mwaka wa 2013, watu zaidi za milioni 19 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Ni pendeleo kama nini kuhudhuria Ukumbusho na pia kuwaalika wengine kuungana nasi katika usiku huo mtakatifu! Je, unawaalika kwa shauku watu wengi kadiri unavyoweza kwenye Ukumbusho wa kila mwaka?

Mtazamo Wetu Unafunua Nini?

23. Una maoni gani kuhusu mikutano yetu?

23 Watumishi washikamanifu wa Yehova hawaoni maagizo ya kukusanyika pamoja kuwa mzigo. (Ebr. 10:24, 25; 1 Yoh. 5:3) Kwa mfano, Mfalme Daudi alipenda kwenda kwenye nyumba ya Yehova ili kuabudu. (Zab. 27:4) Alifurahia hasa kufanya hivyo akiwa na watu wengine waliompenda Mungu. (Zab. 35:18) Fikiria pia mfano wa Yesu. Hata alipokuwa mtoto, alitamani sana kuwa katika nyumba ya ibada ya Baba yake.—Luka 2:41-49.

Tamaa yetu ya kukusanyika pamoja inafunua kwamba Ufalme wa Mungu ni halisi kwetu

24. Tunapata fursa gani tunapohudhuria mikutano?

24 Tunapohudhuria mikutano, tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova na tunatamani kuwajenga waamini wenzetu. Pia tunaonyesha hamu yetu ya kujifunza jinsi ya kuishi tukiwa raia wa Ufalme wa Mungu, kwa sababu tunapata mazoezi hayo kwenye mikutano na makusanyiko. Kwa kuongezea, mikutano yetu inatupatia ustadi na nguvu tunazohitaji ili tuendelee kuvumilia katika kazi muhimu inayofanywa na Ufalme wa Mungu leo, yaani, kuwafanya watu kuwa wanafunzi wa Mfalme Yesu Kristo na kuwazoeza. (Soma Mathayo 28:19, 20.) Bila shaka, tamaa yetu ya kukusanyika pamoja inafunua kwamba Ufalme wa Mungu ni halisi kwetu. Acheni sikuzote tuthamini mikutano yetu!

a Mbali na mikutano yetu ya kila juma, kila familia au mtu mmoja-mmoja wanatiwa moyo kutenga wakati wa kuwa na funzo la kibinafsi au ibada ya familia.

b Kufikia mwaka wa 2013, mihtasari zaidi ya 180 ya hotuba za watu wote ilikuwa imetolewa.

Ufalme Ni Halisi Kwako Kadiri Gani?

  • Kwa nini sisi hukusanyika pamoja?

  • Unahisije kuhusu mikutano mbalimbali?

  • Mtazamo wako unafunua nini kuhusu mikutano? Eleza.

Wahudhuriaji wa kusanyiko wakiwa wameshikilia Biblia zao za Tafsiri ya Ulimwengu mpya ya Maandiko ya Kikristo Kigiriki

MAKUSANYIKO YA KILA MWAKA AMBAYO HUWAUNGANISHA WATU WA MUNGU

YEHOVA aliwaamuru wanaume wote Waisraeli wakusanyike pamoja mara tatu kwa mwaka huko Yerusalemu. (Kut. 23:14-17; Law. 23:34-36) Yosefu, baba mlezi wa Yesu, aliipeleka familia yake yote Yerusalemu kwa ajili ya makusanyiko hayo. Huenda wanaume wengine Waisraeli walifanya vivyo hivyo. Watu wa Mungu leo pia wanakusanyika mara tatu kila mwaka kwa ajili ya makusanyiko. Baadhi ya makusanyiko hayo yalikuwa na matukio muhimu ambayo yalichangia ukuzi wa sehemu ya kidunia ya tengenezo la Mungu wakati wa siku za mwisho. Ona baadhi ya makusanyiko hayo na mambo yanayofanya yakumbukwe sana.

  • 1919: Cedar Point, Ohio, Marekani

    Lilikuwa kusanyiko la kwanza kubwa baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu.

    Kazi ya kuhubiri ilianzishwa tena.

    Tangazo kuhusu kutolewa kwa gazeti The Golden Age (sasa Amkeni!) lilitolewa.

  • 1922: Cedar Point, Ohio

    Kazi ya kuhubiri ilikaziwa katika hotuba yenye kichwa “Ufalme.” Hotuba hiyo ilikuwa na mwito wenye kuchochea “Mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na Ufalme wake”!

  • 1931: Columbus, Ohio

    Tulikubali kuitwa kwa jina Mashahidi wa Yehova.

  • 1935: Washington, D.C.

    Kwa mara ya kwanza, tulielewa kwamba “mkutano mkubwa,” unaotajwa kwenye Ufunuo 7:9 katika tafsiri ya Union Version, utaishi milele duniani.

  • 1942: Kusanyiko la Kitheokrasi la Ulimwengu Mpya, lilifanywa katika majiji 85 ulimwenguni pote

    Hotuba yenye kichwa “Amani—Je, Inaweza Kudumu?” ilisaidia kuelewa unabii unaotajwa katika Ufunuo sura ya 17, kwa kuonyesha kwamba baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, kungekuwa na fursa ya kukusanya raia wengi zaidi wa Ufalme wa Mungu.

  • 1950: Kusanyiko la Ongezeko la Kitheokrasi

    Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilitolewa.

  • 1958: Kusanyiko la Kimataifa la Mapenzi ya Mungu

    Hilo lilikuwa kusanyiko kubwa kufanywa katika jiji moja; wajumbe zaidi ya 250,000 kutoka nchi 123 walikusanyika katika jiji la New York.

  • 1961: Kusanyiko la Waabudu Wenye Umoja

    Tafsiri nzima ya Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa katika buku moja.

  • 1992: Kusanyiko la “Wachukuaji Nuru”

    Lilikuwa Kusanyiko la kwanza la kimataifa la Mashahidi wa Yehova kufanywa katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti, jijini St. Petersburg, Urusi.

  • 1993: Kusanyiko la “Ufundishaji wa Kimungu,” Kyiv, Ukrainia

    Watu wengi sana walibatizwa katika kusanyiko hilo—wahudumu wapya 7,402 walibatizwa.

  • 2011: Kusanyiko la “Ufalme wa Mungu na Uje!”

    Uelewaji wetu kuhusu sanamu ya kiunabii inayotajwa katika Danieli sura ya 2 ulirekebishwa. Sasa tunaelewa kwamba nyayo za chuma na udongo zinawakilisha Serikali ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani, ambayo itakuwa ikitawala Ufalme wa Mungu utakapoivunja-vunja sanamu hiyo ya mfano.

  • 2014: Kusanyiko la “Endeleeni Kuutafuta Kwanza Ufalme wa Mungu!”

    Kutimia kwa miaka 100 tangu Ufalme wa Kristo uanze kutawala mbinguni.

Yesu na wanafunzi wake wakiimba nyimbo za sifa pamoja

“Kuimba Kuhusu Kweli”

WATU wa Yehova wanapenda kuonyesha ujitoaji wao kwake kwa kumwimbia na kuimba kumhusu. Kwa mfano, Yehova alipowakomboa Waisraeli kutoka kwa Wamisri kwenye Bahari Nyekundu, walimheshimu na kumshukuru kwa wimbo wenye hisia. (Kut. 15:1-21) Baadaye, nyimbo zikawa sehemu muhimu ya ibada ya Yehova hekaluni. (1 Nya. 23:4, 5; 25:7) Katika karne ya kwanza, Yesu na wanafunzi wake walionyesha hisia zao kumwelekea Yehova katika nyimbo za sifa.—Mt. 26:30; Efe. 5:19.

Vivyo hivyo, tangu Ndugu Russell na wenzake walipoanza kuitafuta kweli, tumetumia vitabu kadhaa vya nyimbo katika ibada yetu kwa Yehova. Likizungumzia umuhimu wa nyimbo, gazeti Mnara wa Mlinzi la Februari 15, 1896 lilisema: “Kuimba kuhusu kweli ni njia nzuri ya kuifanya itie mizizi katika akili na mioyo ya watu wa Mungu.”

Jalada la kitabu Nyimbo za Bibi Harusi, 1879

1879

Jalada la kitabu Poems and Hymns of Millennial Dawn, 1890

1890

Ukurasa wenye alama za mziki wa wimbo The Shining Light, kutoka kwa kitabu Zion’s Glad Songs of the Morning, 1896

1896

Jalada za kitabu Zion’s Glad Songs, 1900

1900

Jalada la kitabu Hymns of the Millennial Dawn, 1905

1905

Jalada la kitabu Kingdom Hymns, 1925

1925

Jalada la kitabu Songs of Praise to Jehovah, 1928

1928

Jalada la kitabu Utumishi wa Ufalme, 1944

1944

Jalada la kitabu Nyimbo za Kumsifu Yehova, 1950

1950

Jalada la kitabu “Kuimba na Kufuatanisha mziki katika Mioyo Yetu,” 1966

1966

Jalada la kitabu Mwimbie Yehova Sifa, 1984

1984

Jalada la kitabu Mwimbie Yehova

SASA

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki