Sura ya 16
Mikutano Kwa Ajili ya Ibada, Funzo, na Kitia-moyo
MIKUTANO ya kutaniko ni sehemu ya maana ya utendaji wa Mashahidi wa Yehova. Hata hali zinapoifanya iwe vigumu sana, wao hujitahidi kuhudhuria mikutano yao kwa ukawaida, kupatana na himizo hili la Biblia: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, si kuachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali kutiana moyo, na zaidi sana hivyo kwa kadiri mwonavyo siku ikikaribia.” (Ebr. 10:24, 25, NW) Iwezekanapo, kila kutaniko hufanya mikutano mara tatu kwa juma, kwa jumla ya saa 4 na dakika 45. Hata hivyo, hali ya mikutano, pamoja na mara ifanywapo, imetofautiana kulingana na kilichokuwa kimehitajiwa wakati ule.
Katika karne ya kwanza, madhihirisho ya karama za kimuujiza za roho yalikuwa sehemu yenye kutokeza ya mikutano ya Kikristo. Kwa nini? Kwa sababu kwa njia ya karama hizo, Mungu alitoa ushahidi kwenye uhakika wa kwamba yeye hakuwa akitumia tena mfumo wa kidini wa Kiyahudi bali kwamba sasa roho yake ilikuwa juu ya kutaniko la Kikristo lililofanyizwa karibuni. (Mdo. 2:1-21; Ebr. 2:2-4) Kwenye mikutano ya Wakristo wa mapema, sala zilitolewa, nyimbo za kumsifu Mungu ziliimbwa, na mkazo ulitiwa juu ya kutoa unabii (yaani, kuwasilisha mafunuo ya mapenzi na kusudi la kimungu) na kutoa mafunzo ambayo yangejenga walioyasikia. Wakristo hao waliishi wakati ambao kulikuwa matukio yenye kustaajabisha kuhusiana na kusudi la Mungu. Walihitaji kuelewa hayo na kujua jinsi ya kufanya kazi kupatana nayo. Hata hivyo, njia ambayo baadhi yao walishughulikia mambo kwenye mikutano yao haikuwa yenye usawaziko, na kama vile Biblia ionyeshavyo, shauri lilihitajiwa ili mambo yafanywe kwa njia yenye kunufaisha zaidi.—1 Kor. 14:1-40.
Je, sehemu zilizoitambulisha mikutano ya Wakristo hao wa mapema zilionekana pia wakati Wanafunzi wa Biblia walipokutana pamoja katika miaka ya 1870 na baada ya hapo?
Kutimiza Mahitaji ya Kiroho ya Wanafunzi wa Biblia wa Mapema
Charles Taze Russell na kikundi kidogo cha washirika katika Allegheny, Pennsylvania, walifanyiza darasa kwa ajili ya funzo la Biblia katika 1870. Likiwa tokeo la mikutano yao, walikua hatua kwa hatua katika kumpenda Mungu na Neno lake na kwa kuendelea wakaja kujua yale ambayo Biblia yenyewe hufundisha. Hakukuwa na kusema kimuujiza katika ndimi kwenye mikutano hiyo. Kwa nini? Karama hizo za kimuujiza zilikuwa zimetimiza lengo lazo katika karne ya kwanza, na kama vile Biblia ilivyotabiri, zilikuwa zimekoma. “Hatua iliyofuata ya maendeleo,” Ndugu Russell akaeleza, “ilikuwa udhihirisho wa matunda ya Roho, kama vile Mta. Paulo aonyeshavyo wazi sana.” (1 Kor. 13:4-10) Zaidi ya hilo, kama vile katika karne ya kwanza pia, kulikuwa na kazi muhimu ya kufanya ya kueneza evanjeli, na kwa ajili ya hiyo walihitaji kitia-moyo. (Ebr. 10:24, 25) Kabla ya muda mrefu, wakawa wakifanya mikutano miwili ya ukawaida kila juma.
Ndugu Russell aling’amua kwamba lilikuwa jambo la maana kwa watumishi wa Yehova kuwa watu walioungamanika, si kitu wawe wametawanyika wapi duniani pote. Hivyo, katika 1879, muda mfupi baada ya Watch Tower kuanza kutangazwa, wasomaji walo walialikwa waombe Ndugu Russell au mmoja wa washirika wake awazuru. Takwa lililotaarifiwa wazi lilikuwa “Hakuna kutozwa wala fedha kuchukuliwa.” Baada ya maombi kadhaa kupokewa, Ndugu Russell akaanza safari ya mwezi mzima iliyompeleka mbali sana kufika Lynn, Massachusetts, akifanya mikutano kwa saa nne kufika sita kila siku katika kila kituo. Habari iliyotolewa ilikuwa “Mambo Yahusuyo Ufalme wa Mungu.”
Mapema katika 1881, Ndugu Russell aliwahimiza wasomaji wa Watch Tower ambao walikuwa hawafanyi mikutano kwa ukawaida katika eneo lao: “Anzisha mmoja katika makao yako mwenyewe pamoja na familia yako mwenyewe, au hata wachache ambao huenda wakapendezwa. Someni, jifunzeni, toeni sifa na kuabudu pamoja, na wakutanapo wawili au watatu katika jina Lake, Bwana atakuwa kati yenu—mwalimu wenu. Hiyo ndiyo iliyokuwa hali ya baadhi ya mikutano ya kanisa katika siku za Mitume. (Ona Filemoni, 2).”
Programu ya mikutano ilisitawi hatua kwa hatua. Madokezo yalitolewa, lakini kila kikundi cha mahali kiliachwa kiamue lililofaa zaidi hali zao. Msemaji angetoa hotuba pindi kwa pindi, lakini mkazo zaidi ulitolewa kwa mikutano ambamo kila mtu angeweza kujisikia huru kushiriki. Baadhi ya madarasa ya Wanafunzi wa Biblia mwanzoni hayakutumia sana vichapo vya Sosaiti kwenye mikutano yao, lakini wahudumu wasafirio, wale mapilgrimu, waliwasaidia waone thamani ya kufanya hivyo.
Baada ya baadhi ya yale mabuku ya Millenial Dawn kutangazwa, hayo yakaanza kutumiwa kuwa msingi wa funzo. Katika 1895 vikundi vya funzo vikaja kujulikana kuwa Vikundi vya Mapambazuko kwa Ajili ya Funzo la Biblia.a Wengine katika Norway baadaye walivirejezea kuwa “mikutano ya kusoma na kuzungumza,” wakiongeza: “Vifungu kutoka vitabu vya Ndugu Russell vilisomwa kwa sauti, na watu walipokuwa na maelezo au maswali, waliinua mikono yao.” Ndugu Russell alipendekeza kwamba kwenye mafunzo hayo washiriki watumie tafsiri tofauti-tofauti za Maandiko, marejezo ya pambizoni katika Biblia, na konkodansi za Biblia. Mara nyingi mafunzo yalifanywa pamoja na vikundi vyenye ukubwa wa kiasi, katika makao ya watu binafsi, katika jioni iliyokifaa kikundi. Mikutano hiyo ilikuwa tangulizi za Funzo la Kitabu la Kutaniko la siku hizi.
Ndugu Russell aling’amua kwamba mengi yalihitajiwa zaidi ya kujifunza mambo ya kimafundisho tu. Lazima kuwe pia na wonyesho wa ujitoaji ili mioyo ya watu isukumwe na uthamini wa upendo wa Mungu na tamaa ya kumheshimu na kumtumikia. Madarasa yalihimizwa yapange mkutano wa pekee kwa kusudi hilo mara moja kila juma. Ilirejezewa nyakati nyingine kuwa “Mikutano ya Nyumbani” kwa sababu ilifanywa katika makao ya watu binafsi. Programu ilitia ndani sala, nyimbo za sifa, na shuhuda zilizosimuliwa na wale waliohudhuria.b Shuhuda hizo zilikuwa nyakati nyingine mambo yaliyoonwa yenye kutia moyo; majaribu, magumu, na matatizo yaliyokabiliwa wakati wa siku za karibuni yalitiwa ndani pia. Katika sehemu fulanifulani mikutano hiyo ilipungukiwa sana katika lengo layo kwa sababu ya kukazia kupita kiasi mambo ya kibinafsi. Madokezo yenye fadhili ya kufanyia maendeleo yalionyeshwa katika The Watch Tower.
Akikumbuka mikutano hiyo, Edith Brenisen, mke wa mmojawapo mapilgrimu wa mapema katika Marekani, alisema hivi: “Ilikuwa jioni ya kutafakari juu ya utunzaji wenye upendo wa Yehova na ya ushirika wa karibu pamoja na ndugu na dada zetu. Tulipokuwa tukisikiliza baadhi ya mambo waliyoona tulizidi kuwajua vema zaidi. Kutazama uaminifu wao, kuona jinsi walivyoshinda magumu yao, mara nyingi kulitusaidia kutatua baadhi ya matatizo yetu wenyewe.” Hata hivyo, baada ya wakati ikawa wazi kwamba mikutano iliyokusudiwa kutayarisha kila mmoja kushiriki katika kazi ya kueneza evanjeli ilikuwa yenye kunufaisha zaidi.
Njia ambayo mikutano ya Jumapili iliendeshwa katika sehemu fulani ilihangaisha akina ndugu. Madarasa fulani yalijaribu kuzungumza Biblia mstari kwa mstari. Lakini nyakati nyingine tofauti za maoni kuhusu maana hazikuwa zenye kujenga hata kidogo. Ili kuleta maendeleo katika hali hiyo, watu fulani katika kutaniko la Los Angeles, California, walitayarisha mihtasari yenye kichwa cha habari kwa ajili ya funzo la Biblia. Mihtasari hiyo ilikuwa na maswali na marejezo ya kuchunguzwa na darasa zima kabla ya kuja kwenye mkutano. Katika 1902 Sosaiti ilitoa Biblia iliyokuwa na “Misaada ya Funzo la Biblia la Kiberoya,” kutia na fahirisi ya vichwa vya habari.c Ili kusahilisha mambo zaidi, kuanzia na Watch Tower la Machi 1, 1905, mihtasari kwa ajili ya mazungumzo ya kutaniko ilitangazwa, ikiwa na maswali pamoja na marejezo kwenye Biblia na vichapo vya Sosaiti kwa ajili ya utafiti. Mihtasari hiyo iliendelea mpaka 1914, kufikia wakati ambapo maswali ya funzo katika mabuku ya Studies in the Scriptures yalitangazwa ili kutumiwa yakiwa msingi kwa ajili ya Mafunzo ya Kiberoya.
Habari ileile ilipatikana kwa madarasa yote, lakini hesabu ya mikutano ya kila juma ilitofautiana kuanzia mmoja kufika minne au zaidi, kulingana na mipango ya mahali. Katika Colombo, Ceylon (sasa ni Sri Lanka), kuanzia 1914, mikutano ilikuwa kwa kweli ikifanywa siku saba kila juma.
Wanafunzi wa Biblia walitiwa moyo wajifunze kufanya utafiti, ili “kuthibitisha mambo yote,” na kueleza mawazo kwa maneno yao wenyewe. (1 The. 5:21, KJ) Ndugu Russell alitia moyo ushiriki kamili na wa hiari wa mazungumzo ya habari ya funzo. Pia alitahadharisha hivi: “Msisahau kamwe kwamba Biblia ndiyo Kiwango chetu na kwamba hata misaada yetu iwe yenye kubarikiwa na Mungu kadiri gani hiyo ni ‘misaada’ na haiwi badala ya Biblia.”
Mwadhimisho wa Kifo cha Bwana
Kuanzia kama 1876, mipango ilifanywa kila mwaka na Wanafunzi wa Biblia kwa ajili ya mwadhimisho wa kifo cha Bwana.d Mwanzoni, kikundi katika Pittsburgh, Pennsylvania, na sehemu za karibu kilikutana katika makao ya mmoja wa akina ndugu. Kufikia 1883, hudhurio lilikuwa limekua kufikia mia moja hivi katika Pittsburgh, na jumba lililokodiwa lilitumiwa. Ili kuwe na nafasi kwa ajili ya idadi kubwa ya wasikilizaji iliyotazamiwa huko katika 1905, ndugu waliamua kujipatia Carnegie Hall lenye nafasi kubwa ili walitumie.
Wanafunzi wa Biblia walitambua huo kuwa mwadhimisho wa kila mwaka, si jambo lililopasa kufanywa kila juma. Tarehe waliyoshika mwadhimisho ililingana na Nisani 14 katika kalenda ya Kiyahudi, wakati wa kifo cha Yesu. Katika muda wa miaka iliyopita, kumekuwako na kusafishwa katika njia ambayo tarehe hiyo ilihesabiwa.e Lakini jambo kuu la kuhangaikiwa ni umaana wa tukio lenyewe.
Ijapokuwa Wanafunzi wa Biblia walikutana kwa ajili ya mwadhimisho huo katika vikundi vyenye ukubwa unaotofautiana katika sehemu nyingi, wowote ambao wangeweza kujiunga na akina ndugu katika Pittsburgh walikaribishwa. Tokea 1886 kufika 1893, wasomaji wa Watch Tower hasa walialikwa waje Pittsburgh ikiwezekana, nao walifanya hivyo, kutoka sehemu mbalimbali za Marekani na Kanada. Hilo halikuwawezesha tu kuadhimisha Ukumbusho pamoja bali pia liliwasaidia kuimarisha vifungo vya umoja wa kiroho. Hata hivyo, kadiri idadi ya madarasa ilivyokua, katika Marekani na sehemu nyingine za ulimwengu pia, halikuwa jambo liwezalo kutumika kujaribu kukutana katika mahali pamoja, nao wakang’amua kwamba mambo mengi mazuri yangeweza kutimizwa kwa kukutana na waamini wenzao katika eneo la nyumbani kwa mtu.
Kama vile Watch Tower lilivyoonyesha, kulikuwa na wengi waliodai kuiamini fidia, na hakuna wowote wa hawa walioukosa mwadhimisho huo wa kila mwaka. Lakini pindi hiyo ilikuwa na umaana wa pekee kwa wale waliokuwa kikweli wa “kundi dogo” la Kristo. Hao ndio ambao wangeshiriki katika Ufalme wa kimbingu. Katika usiku wa kabla ya kifo cha Yesu, wakati alipoanzisha Ukumbusho, watu mmoja-mmoja waliokuwa wakitolewa tumaini hilo ndio ambao Kristo aliambia: “Fulizeni kufanya hili katika ukumbuko wangu.”—Luka 12:32; 22:19, 20, 28-30, NW.
Hasa kuanzia miaka ya 1930, waliotazamiwa kuwa washiriki wa “halaiki kubwa,” au “umati mkubwa” wa kondoo wengine, walianza kujidhihirisha. (Ufu. 7:9, 10, KJ; Yn. 10:16, NW) Wakati huo hao walikuwa wakirejezewa kuwa Wayonadabu. Kwa mara ya kwanza, katika toleo lalo la Februari 15, 1938, Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) liliwaalika hususa wawepo kwenye Ukumbusho, likisema: “Baada ya saa 12 jioni katika Aprili 15 kila kampuni ya watiwa-mafuta na ikusanyike kuadhimisha Ukumbusho, waandamani wao Wayonadabu wakiwapo pia.” Walihudhuria, si wakiwa washiriki, bali wakiwa watazamaji. Kuwapo kwao kulianza kuongeza idadi ya wale waliokuwapo wakati wa Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Katika 1938 jumla ya hudhurio ilikuwa 73,420, hali idadi ya walioshiriki mifano ya mkate na divai ilikuwa 39,225. Katika miaka iliyofuata, wale waliokuwapo wakiwa watazamaji walianza kutia ndani pia idadi kubwa za wapya wenye kupendezwa na wengine ambao hawakuwa wamekuwa Mashahidi wa Yehova watendaji. Hivyo, katika 1992, wakati kilele cha idadi ya wale waliokuwa wakishiriki katika huduma ya shambani ilipokuwa 4,472,787, hudhurio kwenye Ukumbusho lilikuwa 11,431,171, na idadi ya washiriki wa mifano ilikuwa 8,683 tu. Katika nchi fulani hudhurio limekuwa kubwa sana kama mara tano au sita zaidi ya idadi ya Mashahidi watendaji.
Kwa sababu ya kustahi sana umaana wa kifo cha Kristo, Mashahidi wa Yehova huadhimisha Ukumbusho hata wanapokabiliwa na hali ngumu sana. Wakati wa miaka ya 1970, kafyu (sheria ya kutotoka nje) za usiku za wakati wa vita katika Rhodesia (sasa yaitwa Zimbabwe) zilipofanya iwe vigumu kutoka nje jioni, akina ndugu katika maeneo fulani walikuwa wakikusanyika wote katika makao ya mmoja wa Mashahidi wa Yehova wakati wa mchana na kisha kuadhimisha Ukumbusho jioni. Bila shaka, hawangeweza kurudi nyumbani baada ya mkutano, hivyo walikuwa wakikaa humo usiku huo. Saa za jioni zilizobaki zilitumiwa kuimba nyimbo za Ufalme na kusimulia yaliyoonwa, jambo lililokuwa chanzo cha kiburudisho cha ziada.
Katika kambi za mateso wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, Ukumbusho uliadhimishwa, hata ingawa kufanya hivyo kungalitokeza adhabu kali kama walinzi wangaligundua. Alipofungwa peke yake katika gereza la China ya Kikomunisti kutoka 1958 hadi 1963 kwa sababu ya imani yake ya Kikristo, Harold King aliadhimisha Ukumbusho vizuri kadiri alivyoweza chini ya hali hizo. Baadaye alisema hivi: “Kutoka dirisha la gereza langu nilitazama mwezi ukipevuka karibu na mwanzo wa masika. Nilihesabu tarehe ya mwadhimisho kwa uangalifu kadiri nilivyoweza.” Alifanyiza mifano iliyohitajiwa, akafanya vivi hivi divai kidogo kutokana na zabibu nyeusi na kutumia wali, usio na chachu, kama mkate. Alisema pia hivi: “Niliimba na nikasali na nikatoa hotuba kwa ukawaida kwa ajili ya pindi hiyo, kama vile ingefanywa katika kutaniko lolote la watu wa Yehova. Hivyo nilihisi kwamba kila mwaka niliungamana na ndugu zangu ulimwenguni pote katika pindi hiyo ya maana zaidi sana.”
Mahali pa Wachanga
Wakati wa miaka ya mapema, vichapo na mikutano ya Wanafunzi wa Biblia haikutayarishwa hasa ili kutosheleza mahitaji ya wachanga. Wangeweza kuhudhuria mikutano, na baadhi yao walifanya hivyo na wakasikiliza kwa hamu. Lakini hakukuwa na jitihada ya pekee ya kuwahusisha katika yale yaliyotukia. Kwa nini?
Uelewevu wa akina ndugu wakati ule ulikuwa kwamba ni muda mfupi sana uliobaki mpaka washiriki wote wa bibi-arusi wa Kristo waunganishwe naye katika utukufu wa kimbingu. Watch Tower, katika 1883 lilieleza hivi: “Sisi tulio katika mazoezi kwa ajili ya mwito wa juu hatuwezi kukengeushwa kutoka ile kazi ya pekee ya enzi hii—kazi ya kumtayarisha ‘Bibi-arusi, mke wa Mwana-Kondoo.’ Bibi-arusi apaswa kujiweka tayari; na katika muda huuhuu, wakati ambapo mapambo ya mwisho yanapowekwa katika matayarisho ya arusi, utumishi wa kila mshiriki unatakwa katika kazi hii iliyopo, iliyo ya maana zaidi ya zote.”
Wazazi walihimizwa sana wachukue daraka lao wenyewe walilopewa na Mungu la kuhangaikia ufunzaji wa kiroho wa watoto wao. Haikupendekezwa kuwa na shule za Jumapili zilizo tofauti kwa ajili ya vijana. Ilikuwa wazi kwamba utumizi wa shule za Jumapili wa Jumuiya ya Wakristo ulikuwa umeleta madhara makubwa. Wazazi waliopeleka watoto wao kwenye shule hizo walikuwa na maoni ya kwamba mpango huo uliwaondolea daraka la kuwapa watoto wao mafunzo ya kidini. Watoto, kwa upande wao, kwa sababu hawakutegemea wazazi wao kuwa chanzo cha msingi cha mafunzo juu ya Mungu, hawakusukumwa wawaheshimu wazazi wao na kuwatii kama iwapasavyo.
Hata hivyo, kutoka 1892 kufika 1927, Watch Tower lilitenga nafasi kwa ajili ya maelezo juu ya andiko lililotolewa katika “Masomo ya Shule ya Jumapili ya Kimataifa,” yaliyopendwa na wengi wakati huo katika makanisa ya Protestanti. Maandiko hayo yaliteuliwa kwa miaka mingi na F. N. Peloubet, kasisi wa Congregational Church, na wasaidizi wake. Watch Tower lilizungumzia maandiko hayo kutokana na maoni ya uelewevu wa hali ya juu wa Maandiko wa Wanafunzi wa Biblia, usiofungwa na imani za Jumuiya ya Wakristo. Ilitumainiwa kwamba kwa njia hiyo Watch Tower lingeingizwa ndani ya baadhi ya makanisa, kwamba kwa njia hiyo kweli ingetolewa, na kwamba baadhi ya washiriki wa kanisa wangeikubali. Bila shaka, tofauti ilikuwa wazi, na hilo liliwakasirisha makasisi wa Protestanti.
Mwaka 1918 ukaja, na mabaki, au wabakio wa watiwa-mafuta, walikuwa wangali duniani. Idadi ya watoto kwenye mikutano yao ilikuwa pia imeongezeka sana. Mara nyingi watoto waliruhusiwa kucheza tu huku wazazi wao wakijifunza. Hata hivyo, vijana pia, walihitaji kujifunza ‘kutafuta sana haki, kutafuta sana unyenyekevu,’ ikiwa ‘wangefichwa katika siku ya hasira ya BWANA.’ (Sef. 2:3, KJ) Kwa hiyo, katika 1918 Sosaiti ilitia makutaniko moyo yapange darasa la vijana kwa ajili ya watoto kuanzia umri wa miaka 8 hadi 15. Katika sehemu fulani hata kulikuwa na madarasa ya msingi kwa ajili ya wale walio wachanga mno kuweza kuhudhuria darasa la vijana. Wakati uleule, daraka la wazazi kuelekea watoto lilikaziwa tena.
Hilo liliongoza kwenye matukio zaidi. The Golden Age, katika 1920, lilikuwa na sehemu yenye kichwa “Funzo la Biblia kwa Vijana,” ikiwa na maswali yakiambatana na mitajo ya Maandiko ambamo majibu yangepatikana. Mwaka huohuo, The Golden Age ABC kilitangazwa; kilikuwa kijitabu chenye vielezi kwa matumizi ya wazazi katika kufundisha watoto wao kweli za msingi za Biblia na sifa za Kikristo. Kitabu chenye kichwa The Way to Paradise (Njia ya Kwenda Paradiso), kilichoandikwa na W. E. Van Amburgh, kilifuata katika 1924. Kiliwafaa “wanafunzi wa Biblia wenye ujuzi wa kadiri.” Kwa wakati fulani kilitumiwa kwenye mikutano ya walio wachanga zaidi. Kwa kuongezea, katika Amerika, “Mashahidi Wachanga” walikuwa na mipango yao wenyewe kwa ajili ya utumishi wa shambani. Katika Uswisi kikundi cha vijana kilifanyiza shirika lililoitwa “Vijana wa Yehova,” kwa ajili ya wale wa umri wa miaka kati ya 13 na 25. Walikuwa na ofisi ya mwandishi wao wenyewe katika Berne, na gazeti la pekee, Jehovah’s Youth, lilihaririwa na kuchapwa kwa matbaa za Sosaiti huko. Vijana hao walikuwa na mikutano yao wenyewe na hata walifanya drama za Biblia, kama walivyofanya katika jengo la Volkshaus katika Zurich kwa ajili ya wasikilizaji 1,500.
Hata hivyo, lililokuwa likitukia ni kwamba tengenezo lilikuwa likisitawi ndani ya tengenezo la watumishi wa Yehova. Jambo hilo halingechangia umoja, nalo lilikomeshwa katika 1936. Katika Aprili 1938, wakati wa ziara yake katika Australia, J. F. Rutherford, msimamizi wa Sosaiti, alipata kwamba darasa la watoto lilikuwa likiongozwa kando na mkusanyiko wa watu wazima. Alipanga mara moja watoto wote waletwe katika mkusanyiko mkuu, jambo ambalo liliwanufaisha sana.
Mwaka huohuo, Mnara wa Mlinzi lilipitia jambo hilo lote la madarasa tofauti kwa ajili ya vijana kutanikoni. Funzo hilo lilikazia tena uhakika wa kwamba wazazi wana daraka la kufunza watoto wao. (Efe. 6:4; linganisha Kumbukumbu la Torati 4:9, 10; Yeremia 35:6-10.) Lilionyesha pia kwamba Biblia haitoi kiolezo cha kutenga wachanga kwa njia ya madarasa ya watoto. Badala ya hivyo, walipaswa kuwapo pamoja na wazazi wao kusikia Neno la Mungu. (Kum. 31:12, 13; Yos. 8:34, 35) Maelezo zaidi ya habari ya funzo yalipohitajiwa, hayo yangeweza kutolewa na wazazi nyumbani. Zaidi ya hilo, makala hizo zilieleza kwamba mipango kwa ajili ya madarasa hayo tofauti kwa kweli ilikuwa ikiondoa fikira kwenye kazi ya kuhubiri habari njema nyumba hadi nyumba. Jinsi gani hivyo? Kwa sababu walimu hawakuwa wakienda nje kwenye utumishi wa shambani ili watayarishe kwa ajili ya madarasa hayo na kuyaongoza. Hivyo, madarasa yote tofauti kwa ajili ya vijana yakakomeshwa.
Hadi leo hii, ingali ni desturi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova kwa familia yote kuhudhuria mikutano ya kutaniko pamoja. Watoto husaidiwa na wazazi wao kutayarisha ili waweze kushiriki katika njia zifaazo. Kwa kuongezea, wazazi wameandaliwa mfululizo mzuri wa vichapo wautumie katika kuwapa wachanga mafunzo nyumbani. Miongoni mwavyo kumekuwa vitabu Children (Watoto, Kiingereza), katika 1941; Kumsikiliza Mwalimu Mkuu, katika 1971; Kupata Faida Zote za Ujana Wako, katika 1976; Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, katika 1978; na Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, katika 1989.
Kuwatayarisha Wote kwa Vifaa Wawe Waeneza-Evanjeli Wenye Bidii
Tangu matoleo ya kwanza ya Watch Tower yatangazwe, wasomaji wayo wamekumbushwa kwa ukawaida juu ya pendeleo na daraka la Wakristo wote wa kweli la kupiga mbiu ya habari njema juu ya kusudi la Mungu. Mikutano ya kutaniko imesaidia kutayarisha mioyo na akili zao kwa ajili ya utendaji huo kwa kujenga upendo wao kwa Yehova na ujuzi wao wa kusudi lake. Hasa kufuatia mkusanyiko katika Cedar Point, Ohio, katika 1922, mkazo ulioongezeka sana uliwekwa juu ya jambo lililokuwa likitimizwa katika utumishi wa shambani na jinsi ya kuushiriki kwa mafanikio.
Kichapo Bulletinf (Taarifa Rasmi), kijarida kilichokuwa na habari iliyohusiana moja kwa moja na utumishi wa shambani, kilikuwa na ushuhuda mfupi, ulioitwa wakati ule mazungumzo, ambayo yalipasa kukaririwa na kutumiwa wakati wa kutoa ushahidi kwa watu. Wakati wa sehemu kubwa ya 1923, kwenye tarehe ya kwanza ya kila mwezi, kama kichocheo cha jitihada ya umoja ya kutangaza Ufalme, nusu ya vipindi vya Sala ya usiku wa Jumatano, Mkutano wa Sifa na Ushuhuda, ilitengwa itumiwe kutoa shuhuda kuhusu utumishi wa shambani.
Angalau kufikia 1926, mikutano ya kila mwezi ambamo utumishi wa shambani ulizungumzwa iliitwa Mikutano ya Wafanyakazi. Kwa kawaida wale walioshiriki hasa katika utumishi ndio waliohudhuria. Kwenye mikutano hiyo, njia zilizokuwa zikitumiwa kutoa ushahidi kwa wengine zilizungumzwa, na mipango ya utendaji wa wakati ujao ilifanywa. Kufikia 1928, Sosaiti ilikuwa ikihimiza makutaniko yafanye mikutano hiyo kila juma. Katika muda wa miaka mingine minne, badala ya Mikutano ya Ushuhuda (au, Julisho) Makutaniko yalikuwa yanaanza kufanya ule uliokuja kujulikana kuwa Mkutano wa Utumishi, na Sosaiti ilitia kila mtu moyo ahudhurie. Kwa zaidi ya miaka 60, makutaniko yamefanya mkutano huu wa kila juma. Kwa njia ya hotuba, mazungumzo yahusishayo ushirika wa wasikilizaji, maonyesho, na mahoji, msaada hususa umeandaliwa kuhusiana na pande zote za huduma ya Kikristo.
Kwa hakika namna hii ya mkutano haikuanzishwa katika karne ya 20. Yesu mwenyewe alitoa maagizo kamili kwa wanafunzi wake kabla ya kuwatuma nje kuhubiri. (Mt. 10:5–11:1; Luka 10:1-16) Baadaye, walijengana mmoja na mwenzake kwa kukutana kusimulia mambo waliyoona walipokuwa wakishiriki katika huduma.—Mdo. 4:21-31; 15:3.
Kwa habari ya mazoezi katika kutoa hotuba za watu wote, katika miaka ya mapema, hilo halikufanywa kwenye mikutano ya kutaniko ya kawaida. Hata hivyo, angalau kufikia 1916, ilidokezwa kwamba wale waliohisi kwamba walikuwa na uwezekano fulani wa kuwa wasemaji wa hadhara wangeweza kuwa na darasa lao wenyewe, kukiwa labda na mzee mmoja akiwa mratibu ili kuwasikiliza na kutoa shauri kwa ajili ya kufanyia maendeleo habari inayozungumzwa na utoaji wa hotuba zao. Mikutano hiyo iliyohudhuriwa na wanaume pekee kutanikoni, baadaye ilikuja kujulikana kuwa Shule za Manabii. Alipokuwa akipitia matukio ya siku hizo, Grant Suiter alikumbuka hivi: “Uchambuzi wenye kujenga niliopata katika shule haukuwa kitu ukilinganishwa na ule niliopokea mimi binafsi kutoka kwa baba baada ya yeye kuhudhuria kimojawapo vipindi hivyo ili kunisikia nikijaribu kutoa hotuba.” Ili kusaidia wale waliokuwa wakijaribu kufanya maendeleo, ndugu walitunga na wakachapa wao wenyewe kitabu cha mafundisho cha maagizo juu ya kusema, pamoja na mihtasari ya hotuba tofauti-tofauti. Hata hivyo, baada ya wakati, hizo Shule za Manabii zilikomeshwa. Ili kujazia uhitaji wa pekee uliokuwako wakati ule, uangalifu kamili ulikuwa ukikazwa juu ya kumtayarisha kila mshiriki wa kutaniko ili kushiriki kikamili katika kazi ya kueneza evanjeli nyumba hadi nyumba.
Je, yawezekana kumtayarisha kila mshiriki wa tengenezo hili la kimataifa lenye kukua aweze kutoa ushahidi mfupi na kutoa fasihi ya Biblia na pia kusema kwa matokeo na kuwa mwalimu wa Neno la Mungu? Hilo ndilo lililokuwa lengo la shule ya pekee iliyoanzishwa katika kila kutaniko la Mashahidi wa Yehova, kuanzia 1943. Tayari ilikuwa imekuwa ikiongozwa katika makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova tangu Februari 1942. Kila juma, maagizo yalitolewa, nao wanafunzi walitoa hotuba na kushauriwa juu yazo. Mwanzoni, ni wanaume pekee waliokuwa wakitoa hotuba katika shule hiyo, ingawa kutaniko lote lilitiwa moyo lihudhurie, litayarishe masomo, na kushiriki katika mapitio. Katika 1959 dada walipata pia pendeleo la kujiandikisha, kwa ajili ya mazoezi katika mazungumzo juu ya habari za Biblia katika kikao cha mmoja akizungumza na mwingine.
Kuhusu matokeo ya shule hiyo, tawi la Watch Tower Society la Afrika Kusini liliripoti hivi: “Mpango huo mzuri sana ulifaulu katika muda mfupi kusaidia ndugu wengi waliokuwa wamewaza kwamba hawangeweza kuwa wasemaji mbele ya watu wengi wawe wenye matokeo sana jukwaani na wenye mafanikio zaidi shambani. Katika sehemu zote za Afrika Kusini ndugu walikaribisha upaji huo mpya wa Yehova na wakautumia kwa idili. Hilo lilifanywa vijapokuwa vizuizi vikubwa vya lugha na ukosefu wa elimu wa baadhi yao.”
Shule ya Huduma ya Kitheokrasi huendelea kuwa mkutano wa maana katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Karibu wote wawezao kufanya hivyo huandikishwa. Vijana kwa wazee, Mashahidi wapya na wale wenye ujuzi mwingi hushiriki. Ni programu ya kutoa elimu yenye kuendelea.
Umma Waalikwa Uone na Kusikia
Mashahidi wa Yehova si sosaiti ya siri katika maana yoyote. Imani zao zenye msingi wa Biblia huelezwa kikamili katika vichapo vinavyopatikana kwa yeyote. Kwa kuongezea, wao hutia jitihada ya pekee kualika umma uhudhurie mikutano yao wajionee na kusikia wao wenyewe lile litukialo.
Yesu Kristo aliwapa wanafunzi wake mafunzo ya faragha, lakini pia alisema hadharani—kando ya bahari, mlimani, katika masinagogi, katika eneo la hekalu katika Yerusalemu—mahali ambapo umati ungeweza kusikia. (Mt. 5:1, 2; 13:1-9; Yn. 18:20) Katika kuiga hilo, mapema sana kama miaka ya 1870, Wanafunzi wa Biblia walianza kupanga mikutano ambamo marafiki na majirani na wengine ambao huenda wakapendezwa wangeweza kusikia hotuba juu ya kusudi la Mungu kwa wanadamu.
Jitihada ya pekee ilifanywa ili hotuba hizo zitolewe mahali ambapo pangeufaa umma. Hiyo ilijulikana kuwa kazi ya darasa la nyongeza. Katika 1911, makutaniko yaliyokuwa na wasemaji wa kutosha wenye vipawa yalitiwa moyo yapange baadhi yao waende kwenye miji na vijiji vilivyo karibu wapange na kutoa hotuba katika majumba ya umma. Mahali ilipowezekana, walipanga mfululizo wa hotuba sita. Baada ya ile ya mwisho, msemaji aliuliza ni wangapi katika wasikilizaji waliohisi kupendezwa vya kutosha katika funzo la Biblia kuweza kukutana kwa ukawaida. Hotuba kama hizo zaidi ya 3,000 zilitolewa mwaka wa kwanza.
Kuanzia 1914, ile “Photo-Drama of Creation” pia ilipelekwa kwa umma. Ndugu hawakutoza malipo ya kuingia. Tangu hapo, wametumia sinema nyinginezo na maonyesho ya slaidi. Kuanzia miaka ya 1920, redio ilianza kutumiwa sana na Watch Tower Society kuwezesha watu wasikie hotuba za Biblia nyumbani mwao wenyewe. Halafu, katika miaka ya 1930, hotuba zilizotolewa na J. F. Rutherford zilirekodiwa na kupigwa kwenye maelfu ya mikusanyiko ya watu wote.
Kufikia 1945, kulikuwa idadi kubwa ya wasemaji wa watu wote waliozoezwa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Katika Januari wa mwaka huo, kampeni iliyoratibiwa vizuri ya mikutano ya watu wote ilianzishwa. Sosaiti iliandaa mihtasari kwa ajili ya mfululizo wa hotuba nane zenye kuufaa wakati. Vikaratasi vya ukaribishaji, na nyakati nyingine mabango, zilitumiwa kutangazia hotuba hizo. Zaidi ya kutumia mahali pa kawaida pa mikutano ya kutaniko, ndugu walitia jitihada za pekee kupangia mikutano hiyo ya watu wote katika maeneo ambayo hayakuwa na kutaniko. Wote kutanikoni wangeweza kushiriki—kwa kutangaza mikutano hiyo, kwa kuhudhuria, pamoja na kukaribisha wapya na kujibu maswali yao. Wakati wa mwaka wa kwanza wa utendaji huu wa pekee, mikutano ya watu wote 18,646 ilifanywa katika Marekani, kukiwa na jumla ya hudhurio la 917,352. Mwaka uliofuata idadi ya mikutano ya watu wote ilipanda kufikia 28,703 katika shamba la Amerika. Na katika Kanada, ambako mikutano kama hiyo 2,552 ilikuwa imepangwa katika 1945, kulikuwa 4,645 mwaka uliofuata.
Katika mengi zaidi ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova, Mikutano ya Watu Wote sasa ni sehemu ya ratiba ya kawaida ya mikutano ya kila juma. Mikutano hiyo inafanywa kwa namna ya hotuba ambapo kila mtu hutiwa moyo aangalie Maandiko makuu yanaposomwa na kuzungumzwa. Mikutano hiyo ni chanzo tajiri cha mafunzo ya kiroho kwa kutaniko na wapya pia.
Watu wahudhuriao mikutano ya Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza mara nyingi hupata mshangao wenye kupendeza. Mwanasiasa mashuhuri katika Zimbabwe alienda kwenye Jumba la Ufalme apate kujua yaliyokuwa yakitukia humo. Alikuwa mtu mjeuri, naye alienda bila kunyoa ndevu na bila kuchana nywele kimakusudi. Alitarajia kwamba Mashahidi wangemfukuza. Badala ya hivyo, walionyesha kupendezwa naye kikweli na wakamtia moyo awe na funzo la Biblia nyumbani. Sasa yeye ni Shahidi Mkristo mnyenyekevu na mwenye amani.
Kihalisi kuna mamilioni ya watu ambao, wakiisha kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova, wamehisi wakisukumwa kusema: “Mungu kwa kweli yumo miongoni mwenu.”—1 Kor. 14:25, NW.
Mahali Pafaapo pa Kukutania
Katika siku za mitume wa Yesu Kristo, mara nyingi Wakristo walifanya mikutano yao katika nyumba za watu binafsi. Katika sehemu fulani waliweza kusema katika masinagogi ya Kiyahudi. Katika Efeso mtume Paulo alitoa hotuba kwa miaka miwili katika jumba la shule. (Mdo. 19:8-10; 1 Kor. 16:19; Flm. 1, 2) Vivyo hivyo, katika sehemu ya pili ya karne ya 19, Wanafunzi wa Biblia walikutana katika nyumba za watu binafsi, nyakati nyingine walisema katika chapeli (vikanisa) za makanisa, na wakatumia majumba mengine ambayo yangeweza kukodiwa. Katika visa vichache, baadaye walinunua majengo ambayo hapo kwanza yalikuwa yametumiwa na vikundi vingine vya kidini na kuyatumia kwa ukawaida. Ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya Brooklyn Tabernacle na London Tabernacle.
Lakini hawakuhitaji wala hawakutaka majengo yaliyopambwa kupita kiasi kwa ajili ya mikutano yao. Makutaniko machache yalinunua na kurekebisha majengo yenye kufaa; mengine yalijenga majumba mapya. Baada ya 1935 jina Jumba la Ufalme likaja kutumiwa hatua kwa hatua kuita mahali hapo pa mikutano ya kutaniko. Kwa kawaida hayo ni yenye sura yenye kuvutia lakini si ya kujionyesha. Huenda muundo ukatofautiana mahali na mahali, lakini kusudi la jengo ni kuwa lenye kutumika.
Programu Yenye Umoja ya Mafunzo
Wakati wa sehemu ya pili ya karne ya 19 na sehemu ya kwanza ya karne ya 20, ukuzi wa kiroho na utendaji ulitofautiana sana kutaniko moja na lingine. Walishiriki pamoja imani fulani za msingi zilizowatenga na Jumuiya ya Wakristo. Hata hivyo, ingawa baadhi ya akina ndugu walikuwa wakithamini sana njia ambayo Yehova alikuwa akilisha watu wake, wengine walikengeushwa vyepesi na maoni ya kibinafsi yaliyoshikiliwa sana na watu mmoja-mmoja tofauti juu ya mambo.
Kabla ya kifo chake Yesu alisali kwamba wafuasi wake wangekuwa ‘wote na umoja’—wenye umoja pamoja na Mungu na Kristo na mmoja na mwenzake. (Yn. 17:20, 21) Huo haukupaswa kuwa umoja wa kulazimishwa. Ungetokana na programu yenye umoja ya elimu ipatayo itikio katika mioyo yenye kuitikia. Kama ilivyokuwa imetabiriwa muda mrefu uliopita: “Na watoto wako wote watafundishwa na BWANA; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.” (Isa. 54:13) Ili kupata shangwe ya amani hiyo kwa kipimo kamili, wote walihitaji fursa ya kunufaika na funzo lenye kuendelea ambalo Yehova alikuwa akiandaa kupitia chombo chake kionekanacho cha mawasiliano.
Kwa miaka mingi Wanafunzi wa Biblia walitumia yale mabuku mbalimbali ya Studies in the Scriptures, pamoja na Biblia, vikiwa msingi wa mazungumzo. Yaliyokuwamo yalikuwa, kwelikweli, ‘chakula [cha kiroho] kwa wakati ufaao.’ (Mt. 24:45, NW) Hata hivyo, uchunguzi zaidi wa Maandiko chini ya mwelekezo wa roho ya Mungu ulifanya iwe wazi kwamba kulikuwa mengi zaidi ya kujifunza na kwamba watumishi wa Yehova walikuwa wangali wanahitaji usafishaji mwingi wa kiroho. (Mal. 3:1-3; Isa. 6:1-8) Zaidi ya hilo, baada ya Ufalme kusimamishwa katika 1914, unabii mwingi ulikuwa ukitimizwa kwa mfululizo wenye kufuatana kasi, nao ulielekeza kwenye kazi ya haraka ambayo Wakristo wote wa kweli walipaswa kushiriki. Habari hii ya Kimaandiko yenye kuufaa wakati ilikuwa ikiandaliwa kwa ukawaida kupitia safu za The Watch Tower.
Waking’amua kwamba si kila mtu makutanikoni aliyekuwa akinufaishwa na makala hizo, baadhi ya wawakilishi wasafirio wa Sosaiti walipendekeza kwa ofisi ya makao makuu kwamba kwenye mikutano ya kawaida ya kila juma makutaniko yote yajifunze The Watch Tower. Pendekezo hilo lilipitishwa kwenye makutaniko, na “Maswali ya Kiberoya” ya kutumiwa katika funzo la makala kuu za Watch Tower yakawa sehemu ya kawaida ya gazeti hilo kuanzia na toleo la Mei 15, 1922. Makutaniko mengi zaidi yalikuwa na funzo kama hilo mara moja au zaidi kila juma, lakini kadiri ambayo walijifunza kikweli yaliyokuwamo gazetini ilitofautiana. Katika sehemu fulani, kwa sababu kiongozi alikuwa na mengi ya kusema, funzo hilo liliendelea kwa saa mbili au zaidi.
Hata hivyo, katika miaka ya 1930, mpango wa kitheokrasi ulichukua mahali pa taratibu za kidemokrasi. Jambo hilo lilikuwa na uvutano mwingi juu ya jinsi funzo la Mnara wa Mlinzig lilivyoonwa. Uangalifu mwingi zaidi ulielekezwa katika kuelewa yaliyokuwamo katika habari ya funzo iliyoandaliwa na Sosaiti. Wale waliokuwa wametumia mikutano kuwa fursa za kutetea maoni yao ya kibinafsi na ambao walikinza daraka la kushiriki katika huduma ya shambani waliondoka hatua kwa hatua. Kwa msaada wenye saburi ndugu walijifunza kumaliza funzo kwa saa moja. Likiwa tokeo, kukawa na ushirika zaidi; mikutano ikawa yenye uchangamfu zaidi. Roho ya umoja wa kweli ikaja pia kuenea makutanikoni, ikitegemea programu yenye kuungamanisha ya ulishaji wa kiroho ambamo Neno la Mungu lilikuwa ndilo kiwango cha kupimia kweli.
Katika 1938, Mnara wa Mlinzi lilikuwa likitangazwa katika lugha kama 20. Kila kitu kilitokea kwanza katika Kiingereza. Kwa kawaida halikupatikana katika lugha nyinginezo kwa miezi kadhaa, au labda hata mwaka, kwa sababu ya wakati uliohitajiwa wa kulitafsiri na kulichapa. Hata hivyo, kwa sababu ya badiliko katika njia za kuchapa, wakati wa miaka ya 1980, utangazaji sawia wa Mnara wa Mlinzi uliwezekana katika lugha nyingi. Kufikia 1992, makutaniko yaelewayo yoyote ya lugha 66 yaliweza kujifunza habari ileile kwa wakati uleule mmoja. Hivyo idadi iliyo kubwa zaidi ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote hushiriki chakula cha kiroho kilekile juma kwa juma. Katika Amerika Kaskazini na Kusini yote, katika sehemu kubwa zaidi ya Ulaya, nchi kadhaa katika Mashariki, katika sehemu nyingi za Afrika, na visiwa vingi duniani pote, watu wa Yehova hufurahia mpango sawia wa ulishaji wa kiroho. Pamoja, ‘wanaunganishwa katika akili ileile na katika mstari ule ule wa fikira.’—1 Kor. 1:10, NW.
Tarakimu za mikutano yao ya kutaniko huonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova huchukua mikutano yao kwa uzito. Katika Italia, ambako kulikuwa na Mashahidi watendaji kama 172,000 katika 1989, hudhurio la kila juma kwenye mikutano inayofanywa katika Jumba la Ufalme lilikuwa 220,458. Kwa kutofautisha, chombo cha habari cha Katoliki kilisema kwamba Waitalia asilimia 80 husema kwamba ni Wakatoliki lakini kwamba ni asilimia ipatayo 30 tu huhudhuria ibada za kanisa kwa kadiri fulani ya ukawaida. Ikionwa kwa kukadiria, hali ni hiyohiyo katika Brazili. Katika Denmark, kufikia 1989, Kanisa la Taifa lilidai asilimia 89.7 ya idadi ya watu kuwa washiriki walo, lakini ni asilimia 2 tu waliokuwa wakihudhuria kanisa kila juma! Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova katika Denmark, tarakimu za hudhurio wakati huo zilijumlika kuwa asilimia 94.7. Katika Ujerumani, uchunguzi uliofanywa na Taasisi ya Utafiti wa Maoni ya Allensbach katika 1989 ulionyesha kwamba asilimia 5 ya Walutheri na asilimia 25 ya Wakatoliki katika Jamhuri ya Muungano ilihudhuria kanisa kwa ukawaida. Hata hivyo, kwenye Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova, hudhurio la kila juma lilizidi idadi ya Mashahidi.
Wale wahudhuriao huwa mara nyingi wametia jitihada kubwa ili wawepo. Katika miaka ya 1980, mwanamke mmoja katika Kenya mwenye umri wa miaka 70, alikuwa akitembea kwa ukawaida kilometa 10 na kuvuka mto ili kufika kwenye mikutano kila juma. Ili ahudhurie mikutano katika lugha yake mwenyewe, Shahidi Mkorea katika Marekani alisafiri kwa ukawaida saa tatu kwenda tu, akipanda basi, garimoshi, na mashua, pamoja na kutembea. Katika Suriname, familia moja yenye pato dogo ilitumia mshahara wa siku nzima kulipia nauli ya basi kila juma ili kufika kwenye mikutano. Katika Argentina, familia moja ilisafiri kwa ukawaida kilometa 50 na kutumia robo moja ya pato la familia ili kuhudhuria mikutano kwa ajili ya funzo la Biblia. Iwapo ugonjwa unawazuia kabisa baadhi yao kuhudhuria mikutano ya kutaniko, mara nyingi mipango hufanywa ya kuwaunganisha kwa simu au wasikie programu iliyorekodiwa katika utepe.
Mashahidi wa Yehova huchukua kwa uzito shauri la Biblia la kutoacha kukusanyika pamoja kwa ajili ya kujengwa kiroho. (Ebr. 10:24, 25) Wao hawahudhurii mikutano ya makutaniko ya kwao tu. Kuhudhuria mikusanyiko pia ni jambo kuu la programu yao ya mambo ya kila mwaka.
[Maelezo ya Chini]
a Baadaye mikutano hiyo iliitwa Vikundi vya Kiberoya kwa Ajili ya Funzo la Biblia, katika kuiga Waberoya wa karne ya kwanza waliosifiwa kwa ‘kuyachunguza Maandiko kwa uangalifu.’—Mdo. 17:11, NW.
b Kwa sababu ya yale yaliyoandikwa, mikutano hiyo iliitwa pia Mikutano ya Sala, Sifa na Ushuhuda. Kwa sababu ya umaana wa sala, baada ya wakati ilipendekezwa kwamba mara moja kila miezi mitatu mkutano uwe ibada ya sala tu, kutia na nyimbo lakini bila yaliyoonwa.
c Katika 1907 misaada ya funzo la Kiberoya ilisahihishwa, ikaongezwa sana, na kufanywa kuwa ya karibuni zaidi. Kurasa zaidi zipatazo 300 za habari yenye kusaidia ziliongezwa katika chapa ya 1908.
d Mkutano huo, nyakati nyingine, ulirejezewa kuwa Sikukuu ya Kupitwa ya ufananisho, yaani, mwadhimisho wa kifo cha Yesu Kristo, aliyefananishwa na mwana-kondoo wa Sikukuu ya Kupitwa na hivyo akaitwa “Kristo kafara wetu wa sikukuu ya kupitwa,” kwenye 1 Wakorintho 5:7. (NW) Kupatana na 1 Wakorintho 11:20, uliitwa pia Mlo wa Jioni wa Bwana. Nyakati nyingine uliitwa “Mlo wa Jioni wa Kila Mwaka,” ili kuvuta fikira kwenye uhakika wa kwamba ulikuwa mwadhimisho wa kila mwaka.
e Linganisha matoleo ya Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) ya Machi 1891, kurasa 33-34; Machi 15, 1907, ukurasa 88; Februari 1, 1935, ukurasa 46; na Februari 1, 1948, kurasa 41-43.
f Hata kabla ya 1900 kijitabu kiitwacho Suggestive Hints to Colporteurs kilipelekwa kwa wale waliojiandikisha kwa ajili ya utumishi huo wa pekee. Kuanzia 1919 kichapo Bulletin kilitangazwa kuandaa kichocheo kwa ajili ya utumishi wa shambani, kwanza katika kugawanya The Golden Age na baadaye kwa habari ya namna zote mbalimbali za utendaji wa kueneza evanjeli.
g Jina Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence lilibadilishwa, katika Januari 1, 1909, kuwa The Watch Tower and Herald of Christ’s Presence. Tokea Oktoba 15, 1931, jina likawa The Watchtower and Herald of Christ’s Presence.
[Blabu katika ukurasa wa 237]
Mikutano iliyotaka ushiriki wa kibinafsi
[Blabu katika ukurasa wa 238]
Si falsafa ya kiakili tu bali maneno ambayo yangeweza kuusukuma moyo
[Blabu katika ukurasa wa 246]
Wote katika familia hutiwa moyo wahudhurie mikutano pamoja
[Blabu katika ukurasa wa 252]
Kuungamanisha programu ya ulishaji wa kiroho
[Blabu katika ukurasa wa 253]
Mashahidi huchukua mikutano yao kwa uzito
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 239]
Makutaniko ya Mapema
Kufikia 1916, kulikuwako vikundi vipatavyo 1,200 vya Wanafunzi wa Biblia ulimwenguni pote
Durban, Afrika Kusini, 1915 (juu kabisa kulia); Guiana ya Uingereza (Guyana), 1915 (katikati kulia); Trondheim, Norway, 1915 (chini kulia); Hamilton, Ontario, Kanada, 1912 (chini kabisa); Ceylon (Sri Lanka), 1915 (chini kushoto); India, 1915 (juu kushoto)
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 240, 241]
Kumsifu Yehova kwa Wimbo
Kama vile Waisraeli wa kale na Yesu mwenyewe walivyotumia nyimbo katika ibada, ndivyo wafanyavyo Mashahidi wa Yehova katika nyakati za kisasa. (Neh. 12:46; Mk. 14:26) Huku kukiwa kunatoa sifa kwa Yehova na uthamini kwa ajili ya kazi zake, kuimba kama huko kumesaidia kukaza kweli za Biblia katika akili na moyo pia.
Mkusanyo mwingi wa nyimbo umetumiwa na Mashahidi wa Yehova kwa miaka iliyopita. Maneno ya kisasa zaidi yametumiwa kupatana na uelewevu wenye kuendelea wa Neno la Mungu.
1879: “Songs of the Bride” (Nyimbo za Bibi-Arusi)
(Nyimbo 144 zikieleza tamaa na matumaini ya bibi-arusi wa Kristo)
1890: “Poems and Hymns of Millennial Dawn” (Mashairi na Nyimbo za Mapambazuko ya Mileani)
(Mashairi 151 na Nyimbo 333, zilizotangazwa bila muziki. Nyingi zazo zilikuwa mitungo ya waandikaji mashuhuri)
1896: “Watch Tower” la Februari 1 lilitumiwa kabisa kwa ajili ya “Zion’s Glad Songs of the Morning” (Nyimbo za Nderemo za Asubuhi za Zayoni)
(Maneno ya nyimbo 11, yenye muziki; mashairi yaliyoandikwa na Wanafunzi wa Biblia)
1900: “Zion’s Glad Songs” (Nyimbo za Nderemo za Zayoni)
(Nyimbo 82, nyingi zazo zikiwa zimeandikwa na Mwanafunzi wa Biblia; kuongezea ule mkusanyo wa mapema)
1905: “Hymns of the Millennial Dawn” (Nyimbo za Mapambazuko ya Mileani)
(Nyimbo 333 zilizotangazwa katika 1890, lakini zikiwa na muziki)
1925: “Kingdom Hymns” (Nyimbo za Ufalme)
(Nyimbo 80, pamoja na muziki, hasa kwa watoto)
1928: “Songs of Praise to Jehovah” (Nyimbo za Sifa kwa Yehova)
(Nyimbo 337, mchanganyiko wa nyimbo mpya zilizoandikwa na Wanafunzi wa Biblia na nyimbo za zamani zaidi. Katika maneno hayo, jitihada ya pekee ilifanywa ili kuondoa mawazo ya dini bandia na ibada ya kiumbe)
1944: “Kingdom Service Song Book” (Kitabu cha Nyimbo za Utumishi wa Ufalme)
(Nyimbo 62. Zilizopatanishwa na mahitaji ya utumishi wa Ufalme wa nyakati zile. Sifa hazikutolewa kwa watungaji)
1950: “Songs to Jehovah’s Praise” (Nyimbo kwa Sifa ya Yehova)
(Nyimbo 91. Kitabu hicho cha nyimbo kilikuwa na vichwa vya kisasa zaidi nacho kiliacha kutumia lugha ya kikale. Kilitafsiriwa katika lugha 18)
1966: “Kuimba na Kufuatana Wenyewe kwa Muziki Katika Mioyo Yenu”
(Nyimbo 119 zenye kutia ndani kila upande wa maisha na ibada ya Kikristo. Muziki uliojulikana kuwa ulitokana na vyanzo vya kilimwengu au vya dini bandia ulifutwa. Mirekodi ya okestra ya kitabu chote ilifanywa na ikatumiwa sana kuwa ufuatanisho katika mikutano ya kutaniko. Nyimbo fulani zenye sauti ziliteuliwa zikarekodiwa pia. Kuanzia na 1980, mirekodi ya okestra ya “Melodia za Ufalme” ilitokezwa ili watu mmoja-mmoja waweze kufurahia nyumbani muziki uwezao kujenga)
1984: “Mwimbieni Yehova Sifa”
(Nyimbo za Ufalme 225, zenye maneno na melodia zikiwa zote zimetungwa na watumishi wa Yehova walio wakfu kutoka sehemu zote za dunia. Mirekodi ya sahani za santuri na kaseti ilitokezwa ili kufuatana na uimbaji)
Kwenye Mikutano ya Nyumbani ya mapema, Wanafunzi wa Biblia walitia ndani nyimbo za sifa. Upesi kuimba kukawa pia sehemu ya mikusanyiko yao. Baadhi yao waliimba mmojawapo nyimbo hizo kabla ya kiamshakinywa, wakati wa ibada yao ya asubuhi, kama ilivyofanywa kwa miaka mingi kwenye Bible House. Ingawa kuimba katika makutaniko ya mahali kuliachwa kwa sehemu kubwa kama katika mwaka 1938, kulianza tena katika 1944 na huendelea kuwa sehemu ya maana ya mikutano ya kutaniko na programu za mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova.
[Picha]
Karl Klein akiongoza okestra ya mkusanyiko katika 1947
[Grafu katika ukurasa wa 242]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Ukumbusho wa Kifo cha Kristo
Mashahidi Watendaji
Hudhurio
11,000,000
10,000,000
9,000,000
8,000,000
7,000,000
6,000,000
5,000,000
4,000,000
3,000,000
2,000,000
1,000,000
1935 1945 1955 1965 1975 1985 1992
[Picha katika ukurasa wa 243]
Ajapofungwa peke yake katika gereza la China, Harold King aliendelea kuadhimisha Ukumbusho
[Picha katika ukurasa wa 244]
Darasa la Biblia kwa vijana katika Ujerumani, katika miaka ya mapema ya 1930
[Picha katika ukurasa wa 244]
Katika Uswisi, katika miaka ya katikati ya 1930, vijana Mashahidi walitangaza gazeti hili (chini) na wakafanya drama za Biblia (kama ionyeshwavyo chini katikati) kwa idadi kubwa za watazamaji
[Picha katika ukurasa wa 247]
“Bulletin” (Taarifa Rasmi) (1919-1935), “Director” (Mwelekezi) (1935-1936), “Informant” (Mpasha-Habari) (1936-1956), na sasa “Huduma ya Ufalme Yetu” katika lugha 100—vijarida vyote hivyo vimeandaa maagizo ya ukawaida kwa ajili ya huduma ya shambani yenye umoja ya Mashahidi wa Yehova
[Picha katika ukurasa wa 248]
Maonyesho kwenye Mikutano ya Utumishi husaidia Mashahidi kuifanya huduma yao ya shambani ya kibinafsi iwe bora (Sweden)
[Picha katika ukurasa wa 249]
Shahidi mchanga katika Kenya apata ujuzi kwa kumtolea baba yake hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
[Picha katika ukurasa wa 250]
Kufikia 1992, habari ya funzo la Biblia kwa ajili ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa ikitangazwa sawia katika lugha 66, na zaidi huendelea kuongezwa