Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • od sura 10 kur. 105-115
  • Njia za Kupanua Huduma Yako

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Njia za Kupanua Huduma Yako
  • Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUWA MHUBIRI WA KUTANIKO
  • KUTUMIKIA KATIKA MAENEO YENYE UHITAJI MKUBWA
  • KUHUBIRI KATIKA LUGHA NYINGINE
  • UTUMISHI WA PAINIA
  • WAMISHONARI
  • KAZI YA MZUNGUKO
  • SHULE ZA KITHEOKRASI
  • UTUMISHI WA BETHELI
  • KUTUMIKIA KATIKA KAZI YA UJENZI
  • UNA MALENGO GANI YA KIROHO?
  • Wakumbuke Watumishi wa Wakati Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Je! Waweza Kufanya Zaidi Umheshimu Yehova?
    Huduma Yetu ya Ufalme—1993
  • Waangalizi Wanaochunga Kundi
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Vijana—Mtatumiaje Maisha Yenu?
    Vijana—Mtatumiaje Maisha Yenu?
Pata Habari Zaidi
Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
od sura 10 kur. 105-115

SURA YA 10

Njia za Kupanua Huduma Yako

YESU alipowaagiza wanafunzi wake wahubiri Ufalme, aliwaambia hivi: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache.” Kulikuwa na kazi nyingi, basi akaongeza hivi: “Mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mt. 9:37, 38) Yesu aliwapa wanafunzi wake maagizo ya kutimiza huduma yao. Alionyesha umuhimu wa kazi hiyo aliposema: “Hamtamaliza kamwe kuzunguka majiji ya Israeli kabla ya Mwana wa binadamu kufika.”—Mt. 10:23.

2 Leo pia, kuna kazi nyingi ya kufanya katika huduma ya shambani. Lazima habari njema ya Ufalme ihubiriwe kabla ya mwisho kuja, na muda unayoyoma! (Marko 13:10) Kwa kuwa shamba ni ulimwengu, tunakabili hali kama ya Yesu na wanafunzi wake, ingawa kwa kiwango kikubwa zaidi. Idadi yetu ni ndogo ikilinganishwa na mabilioni ya wanadamu ulimwenguni, lakini tuna hakika kwamba Yehova atatusaidia. Habari njema ya Ufalme itahubiriwa ulimwenguni pote, na wakati uliowekwa na Yehova utakapofika, mwisho utakuja. Je, tutatanguliza Ufalme wa Mungu maishani ili tutimize huduma yetu kikamili? Tunaweza kujiwekea malengo gani ya kitheokrasi?

3 Akieleza matakwa ya Yehova kwa watumishi wake waliojiweka wakfu, Yesu alisema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Tunapaswa kumtumikia Mungu kwa nafsi yote. Hilo linamaanisha kuwa tunaonyesha kwamba tumejiweka wakfu na tumejitoa kikamili kwa kufanya yote tunayoweza katika utumishi wa Yehova. (2 Tim. 2:15) Kila mmoja wetu anaweza kupanua utumishi wake katika njia mbalimbali ikitegemea hali na uwezo wake. Hebu fikiria baadhi ya njia hizo, na uamue malengo ya kitheokrasi unayoweza kujiwekea unapotimiza huduma yako.

KUWA MHUBIRI WA KUTANIKO

4 Wote wanaokubali kweli wana pendeleo la kutangaza habari njema. Hiyo ndiyo kazi kuu ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Kwa kawaida, mwanafunzi wa Yesu Kristo huanza kuzungumza na wengine kuhusu habari njema mara tu anaposikia ujumbe huo. Hivyo ndivyo Andrea, Filipo, Kornelio, na wengine walivyofanya. (Yoh. 1:40, 41, 43-45; Mdo. 10:1, 2, 24; 16:14, 15, 25-34) Je, inamaanisha kwamba mtu anaweza kuzungumza na wengine kuhusu habari njema kabla hajabatizwa? Ndiyo! Mara tu mtu anapostahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa kutanikoni, anaweza kuanza kuhubiri nyumba kwa nyumba. Anaweza pia kushiriki katika sehemu mbalimbali za huduma ikitegemea hali na uwezo wake.

5 Mhubiri anapobatizwa, bila shaka yuko tayari kufanya yote anayoweza ili awasaidie wengine wajifunze habari njema. Wanaume na wanawake wana pendeleo la kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Ni pendeleo kushiriki hata kwa sehemu ndogo katika kuendeleza kazi ya Ufalme wa Mungu. Bila shaka, tukipanua huduma yetu na kufikia mapendeleo zaidi ya utumishi tutakuwa na furaha sana.

KUTUMIKIA KATIKA MAENEO YENYE UHITAJI MKUBWA

6 Huenda eneo la kutaniko lenu huhubiriwa kwa ukawaida na ushahidi mzuri unatolewa. Ikiwa ndivyo, huenda ukahisi kwamba unaweza kupanua huduma yako kwa kuhamia eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri. (Mdo. 16:9) Ikiwa unatumikia ukiwa mzee au mtumishi wa huduma, huenda kuna kutaniko lingine ambalo litathamini msaada wako. Mwangalizi wenu wa mzunguko anaweza kukupendekezea jinsi ya kusaidia kutaniko lingine katika mzunguko wenu. Ikiwa ungependa kutumikia katika eneo lingine nchini kwenu, ofisi ya tawi inaweza kukupatia habari zaidi.

7 Je, ungependa kutumikia katika nchi nyingine? Ikiwa ndivyo, unapaswa kufikiria jambo hilo kwa makini. Kwa nini usizungumzie jambo hilo na wazee wa kutaniko lenu? Bila shaka, hilo litakuwa badiliko kubwa kwako na kwa wale watakaoenda nawe. (Luka 14:28) Hata hivyo, ikiwa hukusudii kukaa kwa muda mrefu, huenda ikafaa ufikirie kutumikia katika eneo lililo nchini kwenu.

8 Katika nchi fulani, ndugu wanaosimamia kazi ni wapya katika kweli. Kwa unyenyekevu, ndugu wenyeji wako tayari kuwaachia wazee wenye uzoefu wanaohamia katika makutaniko yao waongoze mambo. Ikiwa wewe ni mzee na unafikiria kuhamia katika nchi kama hizo, kumbuka kwamba lengo lako si kuchukua mapendeleo ya ndugu wenyeji. Badala yake, tumikia pamoja nao. Watie moyo wafanye maendeleo na wakubali majukumu kutanikoni. (1 Tim. 3:1) Uwe na subira ikiwa mambo fulani hayafanywi kama yanavyofanywa katika nchi yenu. Tumia uzoefu wako ukiwa mzee kuwasaidia akina ndugu. Kisha, ikiwa wakati fulani utalazimika kurudi katika nchi yenu, wazee wenyeji watakuwa na uwezo wa kusimamia kutaniko.

9 Kabla ofisi ya tawi haijakupa majina ya makutaniko yanayoweza kufaidika na msaada wako, Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko lenu itahitaji kutuma barua ya kukupendekeza. Barua hiyo inahitajiwa hata kama wewe ni mzee, mtumishi wa huduma, painia, au mhubiri. Halmashauri ya utumishi itatuma barua ya kukupendekeza pamoja na ombi lako moja kwa moja kwenye ofisi ya tawi ya nchi unayotaka kutumikia.

KUHUBIRI KATIKA LUGHA NYINGINE

10 Ili upanue huduma yako, huenda ukafikiria kujifunza lugha nyingine, kutia ndani lugha ya alama. Kama una lengo la kujifunza kuhubiri katika lugha nyingine, unaweza kuzungumza na wazee na mwangalizi wa mzunguko. Wanaweza kukupa madokezo na kukutia moyo. Kupitia mwelekezo wa ofisi ya tawi, mizunguko fulani imepanga madarasa ya lugha ili kuwazoeza wahubiri wenye uwezo na mapainia kuhubiri katika lugha nyingine.

UTUMISHI WA PAINIA

11 Wahubiri wote wanapaswa kujua matakwa ya msingi ya utumishi wa painia msaidizi, wa kawaida, na wa pekee na pia utumishi mwingine wa wakati wote. Painia anapaswa kuwa Mkristo aliyebatizwa mwenye mfano mzuri ambaye hali zake zinamruhusu kutumia saa hususa kuhubiri habari njema. Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko huidhinisha maombi ya utumishi wa upainia msaidizi na wa kawaida, nayo ofisi ya tawi huweka rasmi mapainia wa pekee.

12 Mhubiri anaweza kuwa painia msaidizi kwa angalau mwezi mmoja, miezi kadhaa mfululizo, au kwa kuendelea, ikitegemea hali zake. Wahubiri wengi wa Ufalme hufanya upainia msaidizi katika pindi za pekee, kama vile majira ya Ukumbusho au mwezi wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko. Wengine huamua kuwa mapainia wakati wa likizo. Wahubiri waliobatizwa wanaosoma wanaweza kujiandikisha kuwa mapainia wasaidizi shule zinapofungwa. Wahubiri wanaweza kuchagua kuwa mapainia wasaidizi kwa punguzo la takwa la saa kila mwezi wa Machi na Aprili na mwezi wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko. Hata hali zako ziweje, ikiwa una maadili mazuri, ikiwa unaweza kupanga kutimiza takwa lililowekwa la saa, na unaamini kwamba unaweza kutumikia kwa mwezi mmoja au zaidi ukiwa painia msaidizi, wazee watafurahia kufikiria ombi lako la kushiriki katika pendeleo hilo la utumishi.

13 Ili ustahili kuwa painia wa kawaida, unapaswa kuwa na uwezo wa kutimiza takwa la saa kwa mwaka. Ukiwa painia wa kawaida, unapaswa kushirikiana kwa ukaribu na kutaniko lenu. Mapainia wenye bidii ni baraka kutanikoni, huwachochea wahubiri washiriki katika huduma ya shambani na hata kuwatia moyo wawe mapainia. Hata hivyo, kabla ya kujaza ombi la kuwa painia wa kawaida, lazima uwe umebatizwa angalau miezi sita iliyopita na uwe mhubiri mwenye mfano mzuri.

14 Kwa kawaida mapainia wa pekee huchaguliwa kati ya mapainia wa kawaida ambao wamekuwa na matokeo mazuri katika huduma. Lazima wawe na hali zitakazowaruhusu kutumikia popote ambapo ofisi ya tawi itawatuma. Mara nyingi wao hutumwa kwenye maeneo ya mbali ili watafute watu wanaopendezwa na kuanzisha makutaniko mapya. Nyakati nyingine, mapainia wa pekee hutumwa kwenye makutaniko yanayohitaji kusaidiwa kuhubiri eneo lao kubwa. Baadhi ya mapainia wa pekee ambao pia ni wazee hutumwa ili kusaidia makutaniko madogo, hata yasiyo na uhitaji hususa wa kuhubiri. Mapainia wa pekee hupokea pesa kidogo ili kugharimia mahitaji yao. Baadhi ya mapainia wa pekee huwekwa rasmi kwa muda.

WAMISHONARI

15 Halmashauri ya Utumishi ya Baraza Linaloongoza huwaweka rasmi wamishonari, kisha Halmashauri ya Tawi ya nchi wanayotumikia huwapa mgawo wa kuhubiri katika maeneo yenye watu wengi. Wao hutimiza mengi katika kuimarisha kazi ya kuhubiri na kuyatia nguvu makutaniko. Kwa kawaida, wamishonari huzoezwa kwenye Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Wao hupewa makao na pesa kidogo ili kugharimia mahitaji yao.

KAZI YA MZUNGUKO

16 Wale wanaowekwa rasmi na Baraza Linaloongoza kuwa waangalizi wa mzunguko hupata mazoezi na uzoefu kwanza kwa kutumikia wakiwa waangalizi badala wa mzunguko. Wanaume hao wanaipenda huduma na ndugu zao pia. Ni mapainia wenye bidii, wanajifunza Biblia kwa bidii, na ni wasemaji na walimu wazuri. Wanaonyesha kwa kiwango kikubwa tunda la roho, ni wenye usawaziko na busara. Ikiwa ndugu ameoa, mkewe anapaswa kuwa painia mwenye mwenendo mzuri anayewatendea wengine vizuri. Ni mhubiri mwenye matokeo mazuri. Pia, anatambua wajibu wake wa kujitiisha akiwa mke Mkristo, hazungumzi kwa niaba ya mumewe au kutawala mazungumzo. Waangalizi wa mzunguko na wake zao huwa na ratiba yenye mambo mengi, kwa hiyo wale wanaojitahidi kufikia utumishi huo wanapaswa kuwa na afya nzuri. Mapainia hawatumi maombi ya kufanya kazi ya mzunguko. Badala yake, wanamwambia mwangalizi wao wa mzunguko tamaa yao, naye huwapa madokezo ya kufikia pendeleo hilo.

SHULE ZA KITHEOKRASI

17 Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme: Waeneza-injili zaidi wa Ufalme wanahitajiwa ili kuhubiri maeneo yasiyohubiriwa kwa ukawaida na kuimarisha makutaniko kiroho. Kwa hiyo, ndugu na dada waseja na wenzi wa ndoa wanaweza kujaza maombi ya kupata mazoezi ya pekee katika Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Baada ya kuhudhuria shule hiyo, wahitimu hutumwa wakiwa mapainia wa kawaida kwenye maeneo yenye uhitaji mkubwa katika nchi yao. Hata hivyo, wale ambao hali zao zinawaruhusu wanaweza kupewa migawo mingine nchini mwao au katika nchi nyingine. Huenda wachache wakatumwa wakiwa mapainia wa pekee wa muda au wa kudumu. Mapainia ambao wangependa kuhudhuria shule hii wanaweza kujua matakwa kwenye mkutano unaofanywa wakati wa kusanyiko la eneo.

18 Shule ya Gileadi: Ndugu na dada waseja na wenzi wa ndoa wanaochaguliwa kuhudhuria shule hii wanazungumza Kiingereza na wanatumikia wakiwa watumishi wa pekee wa wakati wote. Wana uwezo wa kuimarisha kazi ya kuhubiri au kutumikia kwenye ofisi ya tawi. Tayari wameonyesha kwamba wanafurahia kuwatumikia ndugu zao na wanaweza kuwasaidia wengine kwa fadhili kujifunza na kufuata mwongozo wa Kimaandiko na wa kitheokrasi. Halmashauri ya Tawi huwaomba wanafunzi watume maombi. Wahitimu wa shule hii hupewa mgawo wa kuhubiri au kutumikia kwenye ofisi ya tawi katika nchi yao au nchi nyingine.

UTUMISHI WA BETHELI

19 Kutumikia Betheli ni pendeleo la pekee. Jina Betheli linamaanisha “Nyumba ya Mungu,” na vituo hivyo vya utendaji wa kitheokrasi vinastahili kabisa kuitwa hivyo. Ndugu na dada wanaotumikia Betheli hufanya kazi muhimu inayohusisha kutayarisha, kutafsiri, na kusambaza machapisho ya Biblia. Utumishi wao unathaminiwa sana na Baraza Linaloongoza, ambalo husimamia na kuelekeza makutaniko duniani kote. Wanabetheli wengi ambao ni watafsiri, huishi na kufanya kazi katika maeneo ya ofisi yao ya tawi ambayo lugha wanayotafsiri huzungumzwa. Hilo huwasaidia kusikia lugha hiyo ikizungumzwa katika shughuli za kila siku. Pia, wanaweza kujionea ikiwa watu wanaelewa lugha iliyotumiwa katika machapisho yaliyotafsiriwa.

20 Kazi nyingi inayofanywa Betheli inahitaji nguvu nyingi. Kwa hiyo, hasa ndugu vijana waliojiweka wakfu na kubatizwa, wenye nguvu na afya nzuri ndio wanaoitwa Betheli. Ikiwa kuna uhitaji katika ofisi ya tawi inayosimamia nchi yenu na ungependa kutumikia Betheli, unaweza kupata habari zaidi kuhusu matakwa unayopaswa kutimiza kutoka kwa wazee wa kutaniko lako.

KUTUMIKIA KATIKA KAZI YA UJENZI

21 Ujenzi wa majengo ya kitheokrasi ni utumishi mtakatifu, kama ule uliofanywa wakati wa ujenzi wa hekalu la Sulemani. (1 Fal. 8:13-18) Ndugu na dada wengi huonyesha bidii ya pekee kwa kutumia wakati na mali zao ili kushiriki katika kazi hiyo.

22 Je, unaweza kusaidia? Ikiwa wewe ni mhubiri aliyebatizwa na ungependa kushiriki katika kazi hiyo, ndugu wanaosimamia ujenzi katika eneo lenu watathamini msaada wako, na ikiwa huna ujuzi watakuzoeza. Ikiwa ungependa kusaidia, kwa nini usiwajulishe wazee? Baadhi ya wahubiri wanaostahili wamejitolea kushiriki katika ujenzi wa majengo ya kitheokrasi katika nchi nyingine.

23 Kuna fursa nyingi za kushiriki katika utumishi wa ujenzi. Wahubiri waliobatizwa ambao ni mfano mzuri na wana ujuzi fulani, wanaweza kujitolea katika maeneo yaliyo karibu na kwao wakitumikia wakiwa wajitoleaji wa Idara ya Usanifu-Majengo na Ujenzi. Wengine wanaweza kwenda kujitolea maeneo ya mbali na kwao kwa kipindi fulani cha wakati, na hutumwa na ofisi ya tawi kwa majuma mawili hadi miezi mitatu wakitumikia wakiwa wajitoleaji wa ujenzi. Wale wanaotumwa na ofisi ya tawi kutumikia kwa muda mrefu wanaitwa watumishi wa ujenzi. Mtumishi wa ujenzi anayepewa mgawo katika nchi nyingine anaitwa mtumishi wa ujenzi kutoka nchi nyingine. Kikundi cha Ujenzi kinafanyizwa na watumishi na wajitoleaji wa ujenzi na huongoza katika kila mradi wa ujenzi kikisaidiwa na wajitoleaji wa Idara ya Usanifu-Majengo na Ujenzi wa eneo hilo pamoja na wajitoleaji kutoka kutaniko ambalo ujenzi unafanywa. Vikundi vya Ujenzi huhama kutoka mradi mmoja hadi mwingine ulio chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi.

UNA MALENGO GANI YA KIROHO?

24 Ikiwa umejiweka wakfu kwa Yehova, bila shaka unatamani kumtumikia milele. Hata hivyo, kwa sasa una malengo gani ya kiroho? Kuwa na malengo ya kiroho kutakusaidia utumie nguvu na mali zako kwa hekima. (1 Kor. 9:26) Kujiwekea malengo kama hayo hukusaidia kukua kiroho na kutakusaidia kuzingatia mambo muhimu zaidi unapojitahidi kufikia mapendeleo mengine ya utumishi.—Flp. 1:10; 1 Tim. 4:15, 16.

25 Mtume Paulo alituwekea mfano mzuri wa kuiga tunapomtumikia Mungu. (1 Kor. 11:1) Paulo alijitahidi sana kumtumikia Yehova. Alitambua kwamba Yehova alikuwa amempa nafasi nyingi za kumtumikia. Paulo aliwaandikia hivi ndugu huko Korintho: “Nimefunguliwa mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji.” Je, sivyo ilivyo kwetu pia? Naam, tuna nafasi nyingi za kumtumikia Yehova tunaposhirikiana na kutaniko, hasa katika kuhubiri habari njema ya Ufalme. Lakini kama Paulo, tunatambua kwamba kupita katika ‘mlango huo mkubwa’ kunahusisha kukabiliana na “wapinzani wengi.” (1 Kor. 16:9) Paulo alikuwa tayari kujitia nidhamu. Ona alivyosema: “Naupigapiga mwili wangu na kuuongoza kama mtumwa.” (1 Kor. 9:24-27) Je, unamwiga Paulo?

Kuwa na malengo ya kiroho kutakusaidia utumie nguvu na mali zako kwa hekima

26 Kila mmoja wetu anaweza kujiwekea malengo ya kitheokrasi kulingana na hali zake. Wengi wanashiriki katika utumishi wa wakati wote kwa sababu walijiwekea malengo ya kitheokrasi mapema maishani. Walipokuwa bado watoto, wazazi wao waliwatia moyo wajiwekee malengo. Hivyo, wamefurahia baraka nyingi katika utumishi wa Yehova na hawajuti kamwe. (Met. 10:22) Malengo mengine mazuri tunayoweza kujiwekea ni kama vile kushiriki katika utumishi wa shambani kila juma, kuanzisha na kuongoza funzo la Biblia, au kutenga wakati zaidi wa kutayarisha mikutano. Jambo muhimu ni kubaki washikamanifu na kutimiza huduma yetu kikamili. Tukifanya hivyo, tutamletea Yehova sifa na kufikia lengo letu kuu zaidi la kumtumikia milele.—Luka 13:24; 1 Tim. 4:7b, 8.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki