Je! Waweza Kufanya Zaidi Umheshimu Yehova?
1 Hilo ni swali muhimu kwetu sote kulifikiria. Tukiwa waigaji waaminifu wa Bwana wetu Yesu Kristo, twamheshimu Mungu wetu leo kwa kutoa tangazo la hadharani kwa jina lake. Hili ni daraka ambalo lazima tulibebe ikiwa tutapata kibali cha Mungu. (Mk. 13:10; Lk. 4:18; Mdo. 4:20; Ebr. 13:15) Ni pendeleo lisilofafanulika kama nini—ndiyo, heshima—kupeleka habari njema hizi kwa “kondoo” wenye kutawanyika wanaobaki ambao bado huenda wakawa sehemu ya zizi la ulimwenguni pote la Yehova!—Yn. 10:16.
2 Je! wewe na watoto wako mwaweza kufanya zaidi kumheshimu Yehova kwa kuongeza utendaji wenu katika huduma? Kwa idadi zinazoongezeka ulimwenguni pote, ndugu na dada zako wanaingia katika utumishi wa painia. Wakati wa mwezi wa Aprili 1992, jumla ya 5,651 katika Afrika Mashariki walikuwa kwenye utumishi wa painia wa pekee, wa kawaida au msaidizi. Je! wewe mwenyewe umefikiria kwa uzito juu ya kufanya upainia? Je! unawatia moyo watoto wako wafuatie kazi-maisha ya huduma ya wakati wote?
3 Kwa nini usichanganue hisia zako binafsi kuelekea utumishi wa painia? Mara tu jambo hilo linapotajwa, je! wewe huamua tu mara moja kwamba hali zako hazikuruhusu utumikie ukiwa mhudumu painia? Ni kweli kwamba upainia hauwezekani kwa kila mtu. Madaraka ya Kimaandiko na vizuizi vingine huzuia wengi kutumikia wakati wote. (1 Tim. 5:8) Lakini je! umefikiria jambo hilo katika sala hivi karibuni? Je! mmezungumzia jambo hilo mkiwa familia kuona kama angalau mshiriki mmoja aweza kupainia? Toleo la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1983, lilitoa wazo hili la maana kwenye ukurasa 15: “Kusema kweli, inampasa kila mhudumu Mkristo afikirie kwa kusali kama anaweza au hawezi kupainia. Mume na mke wa Afrika Kusini ambao wamepainia muda wa miaka kumi na mitano walisema: ‘Kwa sababu gani tunapainia? Tungeweza kweli kupata sababu nzuri ya kujitetea mbele za Yehova kama hatungepainia?’ Ingefaa wengi ambao si mapainia wajiulize ulizo hili linalohusiana na hilo jingine: ‘Je! mimi naweza kweli kupata sababu nzuri ya kujitetea mbele za Yehova juu ya kinachofanya nisiwe painia?’”
4 Makala nyingine ya Mnara wa Mlinzi juu ya jambo hilo ilitoa elezo hili: “Kila mmoja wetu apaswa kujichunguza kwa unyoofu. Je! wewe unasema, ‘Roho inapenda, bali mwili ni dhaifu’? Lakini je! kweli roho inapenda? Na tuepuke kutumia udhaifu wa mwili kama sababu ya kutopenda kwa roho.”—w79-SW 1/1 uku. 6.
5 Wazazi Wanaotaka Watoto Wao Wafanikiwe: Mithali 15:20 hutuhakikishia: “Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye.” Wazazi wenye kumcha Mungu bila shaka hufurahi wana na binti zao wafuatapo maisha ya utumishi wa wakfu kwa Yehova. Hata hivyo, watoto wako hawatachagua njia ya hekima wao wenyewe tu. Ushawishi wa ulimwengu huu ni wenye nguvu sana. Wazazi, watoto wenu wanaiga kanuni zenu kwa kadiri kubwa. Ikiwa sikuzote wewe huongea ifaavyo kuhusu manufaa za utumishi wa wakati wote, ikiwa wewe huwatia moyo watoto wako watafute ushirika wa mapainia wenye kujitolea, ikiwa umesadikishwa kikweli kwamba huduma ya wakati wote ndiyo kazi-maisha yenye kuheshimika ambayo watoto wako waweza kufanya, mwelekeo huo unaofaa bila shaka utakuwa na athari kubwa sana kwa watoto wako. Wasaidie wajue thamani ya kufanya jina zuri na Yehova badala ya kufanya na wanadamu.
6 Vijana, Mithali 22:1 hukazia uchaguzi mnaopaswa kufanya: “Heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi; Na neema kuliko fedha na dhahabu.” Utajifanyia jina la aina gani? Fikiria wanaume na wanawake tunaosoma juu yao katika Biblia ambao walijifanyia jina na Mungu kupitia utumishi wa wakfu. Kulikuwa na Luka, yule tabibu mpendwa, na Henoko, aliyetembea na Mungu wa kweli. Samweli alipokea elimu nzuri zaidi ilivyowezekana, akianza utumishi wake kwenye hekalu la Yehova akiwa na umri mchanga mno. Unafikiri watumishi waaminifu hawa walisikitika kwa uchaguzi waliofanya? Kwa nini wasikitike? Wote hao waliishi maisha yenye furaha, yenye matokeo, na yenye kusisimua. Na walipata kibali cha Yehova cha milele! —Zab. 110:3; 148:12, 13; Mit. 20:29a; 1 Tim. 4:8b.
7 Watoto wanapofanikiwa maishani, wazazi wao huona fahari. Kujitoa kwao katika kufundisha, kutoa nidhamu, na kuelimisha huu “urithi wa BWANA [Yehova, NW]” kunalipwa mara nyingi zaidi. (Zab. 127:3) Ni nini kingemfanya mzazi aone fahari zaidi kuliko kuwa na mwana au binti anayefanya yote ili amheshimu Yehova? Vijana wengi nyakati za ki-siku-hizi wanafuata hatua za Luka, Henoko, na Samweli, kama vile barua moja inavyotoa kielezi: “Mimi nina miaka 16. Nilianza upainia wa kawaida . . . miezi tisa baada ya kubatizwa, na nimekuwa nikipokea baraka kutoka kwa Yehova tangu wakati huo. . . . Upainia pia hukusaidia shuleni. Mwanzoni, nilidhihakiwa na wanadarasa wenzi kwa sababu ya kuwa Shahidi. Sasa, kwa kuwa ninafanya funzo la binafsi mara nyingi zaidi, ninaweza ‘kumjibu anilaumuye.’”
8 Elimu ya Kumtayarisha Mmoja Katika Huduma: Kufikia hapa twaweza kufikiria swali la elimu ya kilimwengu. Hapa ndipo usawaziko wa maoni unahitajiwa hasa. Mnara wa Mlinzi wa Novemba 1, 1992, ulikuwa na makala “Elimu Yenye Kusudi.” Chini ya kichwa kidogo “Elimu ya Kutosha,” jambo hili lilitokezwa: “Wakristo wanapaswa waweze kujitegemeza wenyewe, hata ikiwa wao ni wahudumu mapainia wa wakati wote. (2 Wathesalonike 3:10-12) . . . Mkristo mchanga anahitaji elimu ya kiasi gani ili astahi kanuni hizo za Biblia na kutimiza wajibu wake mbalimbali wa Kikristo? . . . Ni nini [mishahara] chaweza kuitwa ‘kiasi kinachofaa,’ kwa wale wanaotamani kuwa wahudumu mapainia wa habari njema? Kwa ujumla wao huhitaji kazi ya muda-muda ili waepuke kuwa ‘mzigo’ kwa ndugu zao au familia yao.—1 Wathesalonike 2:9, HNWW.”
9 Ikiwa elimu ya ziada inaonwa kuwa ya lazima na anayetazamia kuwa painia ili kumsaidia afuatie utumishi wa wakati wote, Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1992 lapendekeza: “Shahidi mchanga angefanya vema, ikiwezekana, kuipokea akiwa bado anaishi nyumbani, hivyo aweze kudumisha tabia za Kikristo za kawaida za kujifunza, kuhudhuria mikutano, na utendaji wa kuhubiri.”
10 Kutoka Afrika kuna yalioonwa ya kijana mwenye miaka 22 ambaye alilazimika kwenda kwenye shule ya kiufundi, ingawa moyo wake ulikuwa kwenye utumishi wa painia. Akiwa kwenye shule ya kiufundi, alichukua upainia msaidizi. Marika wake walimdhihaki, wakisema kwa hakika ataanguka mitihani yake. Jibu lake kwao sikuzote lilikuwa: “Utafuteni kwanza Ufalme na haki yake.” Akijizoeza nidhamu, angeamka asubuhi na mapema na kufanya matayarisho ya saa mbili kwa ajili ya masomo ya darasa na kushiriki katika utumishi alasiri wakati masomo yalipokuwa yamemalizika. Shule yote ilishikwa na bumbuazi wakati kijana huyo alipopata nafasi ya tatu katika mtihani wa pekee wa kuchagua wanafunzi watatu waliofanya vizuri zaidi kwa ajili ya kutuzwa udhamini. Mwanafunzi aliyechukua nafasi ya pili alikuwa mwenye kupendezwa ambaye ndugu yetu alikuwa anajifunza naye Biblia shuleni. Mwanafunzi aliyechukua nafasi ya kwanza alikuwa Shahidi mwingine kijana mwenye bidii katika shule.
11 Wazee Hufanya Sehemu Yao: Wazee wa kundi, ambao huonea fahari kazi wanayofanya mapainia, hutoa kitia-moyo kikubwa kwa wahudumu hawa wenye bidii. Wazee wanapendezwa kufanya hivyo kwa sababu wanajua kwamba mapainia wenye bidii, na wenye matokeo ni baraka kwa kundi lolote lile. Baada ya kushiriki kwa mwaka au zaidi katika utumishi wa painia wa kawaida, hao wanaweza kupata mazoezi ya ziada katika Shule ya Utumishi wa Painia. Mazoezi hayo yamethibitika kuwa yenye thamani sana katika kufanya matokeo ya mapainia yawe bora zaidi. Ijapokuwa mapainia wako katika mstari wa mbele katika kazi hiyo, wao pia wanahitaji kitia-moyo chenye upendo, na wazee wanapaswa kuwa chonjo kutimiza uhitaji huo.—1 Pet. 5:1-3.
12 Wazee wanaweza kutoaje kichocheo kwa kazi ya painia? Mwanzo mzuri utakuwa kutafuta kwa kurudiarudia wale ambao huenda wakawa wanaweza kufikia pendeleo hili. Wazee wanaweza kuwafikia watu mmoja mmoja wanaoonekana kuwa katika hali nzuri ya kupainia, kutia ndani wengi wanaofanya upainia msaidizi kwa kawaida, watu waliostaafu, wake wa nyumbani, na wanafunzi. Ijapokuwa yeyote hapaswi kufanywa ahisi kuwa chini ya wajibu wa kujiandikisha, wale walio na tamaa lakini wamesita-sita huenda, kwa kitia-moyo kidogo, wakatambua kuwa wanaweza kufanya upainia.
13 Wazee wanapowapa kitia-moyo wale ambao wanataka kufanya maombi, wanapaswa kukumbuka kwamba si lazima mwenye kujaza atumike miezi kadha akiwa painia msaidizi kabla ya kujiandikisha kuwa painia wa kawaida. (km-SW 9/86 nyongeza maf. 24-26) Bila shaka, wazee wanapaswa kuwa na uhakika kwamba mwenye kufanya maombi anaweza kutimiza takwa la saa.
14 Baada ya maombi kupitiwa na Halmashauri ya Utumishi ya Kundi na kuangaliwa kwa uangalifu na mwandishi kuhakikisha kwamba maswali yote yamejibiwa, yanapaswa kupelekwa haraka kwa Sosaiti.
15 Mwandishi apaswa kuwajulisha wazee matatizo yoyote ambayo huenda mapainia wakawa wanapata. Hili ni jambo la maana hasa katika makundi yanye mapainia wengi. Pamoja na pitio la utendaji wa painia mwishoni mwa mwaka wa utumishi kama inavyoombwa kwenye Ripoti ya Mchanganuo wa Kundi (S-10-SW), mwandishi anapaswa kualika mwangalizi wa utumishi wakutane mapema katika Machi ili kuona ni nani huenda akawa anashindwa kutimiza takwa la saa na anahitaji uangalifu wa binafsi. (Ona Matangazo ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Februari 1993.) Msaada ukitolewa bila kuchelewa, painia huenda akamaliza mwaka wa utumishi kwa mafanikio.
16 Idadi kubwa ya mapainia ni wachanga kwa umri na ni wapya kwa kadiri fulani kwa kweli. Roho yao ya kupenda kwa hakika hutufanya tuone shangwe! Lakini wapya hao bado wanahitaji mazoezi ili wakuze stadi katika kazi ya nyumba kwa nyumba, kufanya ziara za kurudia zenye matokeo, kufundisha kwenye mafunzo ya Biblia. Mazoezi yasipopokewa, mpya anaweza kuvunjika moyo baada ya mwaka mmoja hivi na hatimaye aache utumishi wa painia kwa sababu ya kutopata matokeo mazuri katika huduma. Wazee waangalifu wanaweza kugundua tatizo dogo au kupungua kwa utendaji. Ikiwa uangalifu wa haraka unatolewa na painia asaidiwe tatizo lake, huenda akafurahia miaka mingi ya utumishi wenye matokeo.
17 Je! Unaweza Kuvua Katika Maji ya Mbali? Baadhi ya wanafunzi wa Yesu walikuwa wavuvi. Wakati mwingine baada ya kuvua usiku kucha, nyavu zao zilikuwa tupu. (Yn. 21:3) Katika maeneo mengine ambapo ‘uvuvi wa watu’ umeendelea kwa miaka mingi, mapainia wengine huenda wakaamua kuwa kuna “samaki” wachache wanaobaki kwenye “maji” ya kundi lao. (Mt. 4:19) Kwa kutofautisha, je! hatusisimuki kwa kusoma ripoti zinazokuja kutoka maeneo mengine ambako wahubiri na mapainia wanaongoza mafunzo mengi ya Biblia? Shangwe inayopatwa na mapainia na wamishonari katika maeneo hayo ni wazi kabisa. (w92-SW 9/1 uku. 20 fu. 15) Hivyo, ikiwa baadhi ya mapainia wenye bidii wangeweza kuhamia kwenye eneo ambalo lina uhitaji mkubwa, wanapaswa kufikiria hilo kupitia ofisi ya tawi au mwangalizi wao wa mzunguko kabla ya kuhama.
18 Hapo mwanzoni, wengine huenda walianza upainia kwa sababu walijua lilikuwa jambo linalofaa kufanya lakini hawakujua kama wangeweza kufanikiwa. Labda walifanya maombi hayo kwa kutilia shaka na kutokuwa na hakika. Walipoanza, matokeo yao katika shamba huenda yalikuwa ya kadiri ndogo. Hata hivyo, baada ya wakati, ustadi wao ukaongezeka, na kukawa na uthibitisho wa baraka za Yehova katika kazi yao. Kwa sababu hiyo, shangwe yao na uhakika ukaongezeka. Kwa wengine, upainia umekuwa jiwe la kukanyagia kuelekea utumishi wa Betheli, mazoezi ya Gileadi na kazi ya umishonari, Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, na kazi ya kusafiri.
19 Huenda isiwezekane kwako kuhamia nchi nyingine au kunufaika na mazoezi ya Gileadi, lakini bado kuna fursa za kuvua kwenye maji katika nchi yako mwenyewe ikiwa eneo lako la wakati huu hasa halina matokeo au ikiwa unaweza kuhamia jingine. Kuhama huko huenda kukataka marekebisho upande wa mtindo-maisha wako, lakini zawadi za kiroho zitakuwa nyingi kwelikweli.—Mt. 6:19-21.
20 Au ikiwa hali zako zaruhusu, unaweza kusaidia kundi la karibu la mzunguko wako. Ukistahili, mwangalizi wako wa mzunguko atafurahia kukupa mapendekezo juu ya makundi ya mzunguko huo ambayo yatanufaishwa na painia mwingine.
21 Mapainia na wahubiri wengine wameweza kutumikia mahitaji katika maeneo yao wakibaki nyumbani kwao. Huenda wakawa wanajua lugha nyingine. Je! unaona katika eneo lako kwamba sehemu kubwa ya idadi inaongea lugha nyingine? Je! kuna watu wanaohitaji kupata ujumbe wa Ufalme kutoka kwa mtu mwenye kutumia lugha ya ishara? Wale wanaojua lugha nyingine wanaweza kuwa msaada mkubwa katika kufikia watu wa aina yote wakiwa na ujumbe wa Ufalme. Ingawa hilo laweza kuwa jambo gumu kwelikweli, laweza kuwa lenye kuthawabisha pia.—1 Tim. 2:4; Tit. 2:11.
22 Ikiwa kwa sasa unafanya yote uwezayo kumheshimu Yehova, onea shangwe mapendeleo yako ya sasa ya utumishi. Ikiwa unahisi unaweza kufanya zaidi, mpelekee Yehova jambo hilo kwa sala. Changanua kihalisi ni mabadiliko gani hali zako zingekuruhusu kufanya. Ongea juu ya mipango yako na mzee mwenye roho ya upainia au mwangalizi wa mzunguko. Wakati umefanya uamuzi wa sala na wenye kutumika, fuata bila kusita, ukiwa na uhakika wa ahadi ya Yehova ya kuheshimu wale wanaomheshimu yeye.—Ebr. 13:5, 6; 1 Sam. 2:30.