Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 10/15 kur. 18-23
  • Baraka za Huduma ya Painia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Baraka za Huduma ya Painia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Hisia Zenye Kina Kirefu za Utoshelezo na Shangwe
  • Uthibitisho wa Utunzaji wa Yehova
  • “Njia Bora Kabisa ya Kumkaribia Yehova”
  • Je, Moyo Wako Watamani Sana Kufanya Mengi Zaidi?
  • Wote Wanaweza Kuonyesha Roho ya Upainia
  • Baraka za Huduma ya Upainia
    Huduma Yetu ya Ufalme—2003
  • Mapainia Hutoa na Kupokea Baraka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Yehova Ategemeza Jeshi Lake la Watumishi wa Wakati Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Upainia Huimarisha Uhusiano Wetu na Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 10/15 kur. 18-23

Baraka za Huduma ya Painia

“Baraka ya BWANA hutajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo.”—MITHALI 10:22.

1, 2. (a) Painia mmoja alielezaje hisia zake kuhusu huduma ya wakati wote? (b) Kwa nini mapainia wako katika hali ya kuona kikamili zaidi shangwe za kufanya wanafunzi?

“JE, KWAWEZA kuwa na shangwe kubwa kuliko kuona mtu fulani unayejifunza naye akiwa msifaji wa Yehova mwenye bidii? Inasisimua na kutia nguvu imani kuona jinsi Neno la Mungu lilivyo na nguvu katika kuchochea watu wafanye mabadiliko katika maisha yao ili kumpendeza Yehova.” Ndivyo alivyoandika painia kutoka Kanada ambaye amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka zaidi ya 32. Kuhusu huduma yake ya painia, yeye asema: “Siwezi kuwazia nikifanya jambo jingine lolote. Hakika siwezi kuwazia chochote ambacho kingeleta shangwe kama hiyo.”

2 Je, wakubali kwamba kuna shangwe kubwa katika kushiriki kusaidia mtu fulani katika njia ya uhai? Bila shaka, si mapainia peke yao wanaoona shangwe hiyo. Watumishi wa Yehova wote wako chini ya agizo la “[ku]fanya wanafunzi kutoka kwa watu,” nao hujitahidi kufanya hivyo. (Mathayo 28:19) Hata hivyo, kwa kuwa mapainia wanaweza kushiriki muda wa saa nyingi katika huduma ya shambani, mara nyingi wako katika hali ya kuona shangwe nyingi za kufanya wanafunzi kwa ukamili zaidi. Lakini kupainia kuna thawabu nyingine pia. Ongea na mapainia, nao watakuambia kwamba kupainia ni njia nzuri ajabu ya kuona ‘baraka za Yehova ambazo humtajirisha mtu.’—Mithali 10:22.

3. Ni jambo gani liwezalo kutuchochea tuendeleapo kumtumikia Yehova?

3 Hivi majuzi, mapainia kutoka sehemu mbalimbali za ulimwengu waliombwa wafafanue baraka ambazo wameona katika huduma ya wakati wote. Acheni tufikirie yale waliyosema. Hata hivyo, usivunjike moyo, utumishi wako ukipungukiwa kwa sababu ya afya mbaya, uzee, au hali nyingine. Kumbuka, jambo la maana ni kumtumikia Yehova kwa nafsi yote, katika kiwango chochote kile. Ingawa hivyo, huenda kusikia maelezo ya mapainia fulani kukaongeza kupendezwa kwako katika kuchukua utendaji huu wenye kuthawabisha ikiwezekana.

Hisia Zenye Kina Kirefu za Utoshelezo na Shangwe

4, 5. (a) Kwa nini kushiriki habari njema na wengine ni ono lenye kuthawabisha? (b) Mapainia wanahisije kuhusu kushiriki katika huduma ya wakati wote?

4 “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea,” akasema Yesu. (Matendo 20:35) Ndiyo, kutoa kusiko kwa ubinafsi kuna thawabu zake. (Mithali 11:25) Hasa hilo ni kweli kuhusu kushiriki habari njema na wengine. Kwa kweli, tungeweza kutoa zawadi gani kubwa zaidi kwa binadamu mwenzetu kuliko kumsaidia apate ujuzi kuhusu Mungu, uongozao kwenye uhai udumuo milele?—Yohana 17:3.

5 Haishangazi kwamba, wale wanaoshiriki katika huduma ya wakati wote mara nyingi huelezea shangwe na hisi yenye kina ya utimizo wanayopata kutokana na huduma yao. “Najua kwamba hakuna kazi nyingine ambayo ingeweza kuniletea utoshelezo unaotokana na kushiriki kweli na wengine,” asema painia mwenye umri wa miaka 64 kutoka Uingereza. Mjane kutoka Zaire alieleza kile ambacho kupainia kumemaanisha kwake: “Utumishi wa painia ulikuwa faraja kwangu baada ya kumpoteza mume wangu mpendwa. Kadiri ninapoenda katika utumishi kusaidia wengine, ndivyo huzuni yangu inapopungua. Naweka imani yangu katika ahadi za Yehova na kufikiri zaidi jinsi ninavyoweza kusaidia wale ninaojifunza nao wafanye mabadiliko katika maisha zao. Mwishoni mwa kila siku, usingizi wangu ni mtamu na moyo wangu umejawa shangwe.”

6. Ni shangwe gani za pekee ambazo baadhi ya mapainia wameziona?

6 Baadhi ya watu ambao wamekuwa wakipainia kwa miongo mingi wamekuwa na shangwe ya pekee ya kutumikia maeneo ya mbali sana, wakianzisha makutaniko, ambayo hatimaye yalikua hadi kufikia kuwa mizunguko. Kwa mfano, katika Abashiri, Hokkaido (kisiwa cha kusini sana mwa Japani), kuna dada ambaye amekuwa akipainia kwa miaka 33. Anakumbuka kwamba kwenye kusanyiko lake la kwanza la mzunguko—Hokkaido yote—kulikuwa na hudhurio la watu 70 tu. Na sasa? Kuna mizunguko 12 kwenye kisiwa hicho, kukiwa na jumla ya wahubiri 12,000. Wazia jinsi ambavyo moyo wake hufurika kwa shangwe anapohudhuria makusanyiko na mikusanyiko pamoja na songamano la wapiga-mbiu wa Ufalme wenzake kwenye kisiwa hicho!

7, 8. Ni shangwe gani ambayo mapainia walio wengi wa muda mrefu wameona?

7 Mapainia wengine wa muda mrefu wamekuwa na shangwe ya kuona wanafunzi wa Biblia wakibatizwa kisha wakifikia mapendeleo makubwa zaidi ya utumishi. Katika Japani dada ambaye ametumikia kwa migawo tisa tofauti ya painia tangu 1957 akumbuka akimwangushia mwanamke mmoja mchanga gazeti la Amkeni! aliyekuwa akifanya kazi benki. Mwanamke huyo alibatizwa kati ya muda wa miezi tisa. Baadaye aliolewa, na yeye na mume wake wakawa mapainia wa pekee. Ilikuwa shangwe kama nini kwa dada huyo painia, wakati, akiwa katika mgawo wake wa tatu, kutaniko lake lilipotembelewa na mwangalizi wake mpya wa mzunguko pamoja na mke wake—mwanafunzi wake wa zamani wa Biblia!

8 Si ajabu kwamba wale ambao wamefanya huduma ya painia kuwa kazi-maisha yao wanaoiona kuwa “pendeleo lenye thamani sana la kuthaminiwa,” kama alivyoeleza painia mmoja wa muda wa miaka 22!

Uthibitisho wa Utunzaji wa Yehova

9. Yehova akiwa Mwandalizi Mkuu, ameahidi watumishi wake nini, na hilo lamaanisha nini kwetu?

9 Yehova, Mwandalizi Mkuu, anaahidi kutegemeza watumishi wake, akiwatunza kiroho na kimwili. Mfalme Daudi wa kale aliweza kusema vizuri hivi: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa wala mzao wake akiomba chakula.” (Zaburi 37:25) Bila shaka, huu uhakikisho kamili wa kimungu hautupi sababu ya kujitetea kuwa na wajibu wa kuandalia kimwili familia zetu, wala hautupi kibali cha kutumia vibaya ukarimu wa ndugu zetu Wakristo. (1 Wathesalonike 4:11, 12; 1 Timotheo 5:8) Hata hivyo, tunapojidhabihu kwa hiari katika maisha yetu ili kumtumikia Yehova kikamili zaidi, hatatuacha kamwe.—Mathayo 6:33.

10, 11. Kutokana na mambo yaliyoonwa, mapainia wengi wanajua jambo gani kuhusu uwezo wa Yehova wa kuandaa?

10 Mapainia ulimwenguni pote wanajua kutokana na mambo waliyojionea kwamba Yehova huandalia wale wanaojiweka katika mikono yake ya utunzaji. Fikiria kisa cha wenzi wa ndoa mapainia ambao walihamia mji mdogo ambapo kulikuwa na uhitaji wa wahubiri wa Ufalme. Baada ya miezi michache, kazi ya kimwili ikawa haipatikani, na fedha zao walizokuwa wameweka zilimalizika kabisa. Kisha walipokea hati ya malipo ya bima ya gari ya dola 81. “Hatukuwa na njia ya kuilipia,” aeleza ndugu huyo. “Tulisali sana usiku huo.” Siku iliyofuata, walipokea kadi kutoka kwa familia ambayo wao wenyewe walikuwa wanapambana kifedha. Familia hiyo ilikuwa imepokea fedha za kodi zinazorudishwa, kadi hiyo ilieleza, na kwa kuwa zilikuwa nyingi kuliko walivyotazamia, walitaka kushiriki baadhi yake na wenzi wa ndoa mapainia. Pamoja nayo, iliandamanishwa hundi ya dola 81! “Sitasahau kamwe siku hiyo—nywele katika shingo langu zilisimama wima!” asema ndugu painia. “Tulithamini sana ukarimu wa familia hii.” Pia Yehova huthamini fadhili ya aina hiyo, ambayo yafanana na roho ya ukarimu anayotia moyo watumishi wake kuwa nayo.—Mithali 19:17; Waebrania 13:16.

11 Mapainia wengi wanaweza kusimulia mambo yaliyoonwa yaliyo sawa na hayo. Waulize, nao watakuambia kwamba “hawakuachwa kabisa.” Akitazama nyuma baada ya miaka 55 ya huduma ya wakati wote, painia mwenye umri wa miaka 72 asema, “Yehova hakunisikitisha kamwe.”—Waebrania 13:5, 6.

“Njia Bora Kabisa ya Kumkaribia Yehova”

12. Kwa nini kazi ya kutangaza habari njema ni pendeleo lenye kutokeza?

12 Kwamba Yehova hata hutuomba tutangaze habari njema ya Ufalme wake hutupatia pendeleo. Yeye hutuona—ingawa sisi ni binadamu wasio wakamilifu—kuwa “wafanyakazi wenzi” katika utendaji huu wa kuokoa uhai. (1 Wakorintho 3:9; 1 Timotheo 4:16) Tunapohubiri wengine juu ya Ufalme wa Mungu, tutangazapo mwisho wa uovu, tuelezapo watu upendo wake wa ajabu katika kuandaa fidia, tufunguapo Neno lake lililo hai na kufundisha yaliyomo ndani yake yenye thamani kwa watu wenye mioyo ya kufuatia haki, bila shaka twavutwa karibu zaidi na Muumba, Yehova.—Zaburi 145:11; Yohana 3:16; Waebrania 4:12.

13. Wengine wanasema nini kuhusu tokeo la huduma yao ya painia na uhusiano wao na Yehova?

13 Mapainia wanaweza kutumia wakati mwingi kila mwezi katika kujifunza kuhusu Yehova na kufundisha kumhusu. Wanahisi kwamba hilo huathirije uhusiano wao na Mungu? “Kupainia ni njia bora kabisa ya kumkaribia Yehova,” ajibu mzee katika Ufaransa ambaye amekuwa akipainia kwa miaka zaidi ya kumi. Painia mwingine katika nchi hiyo, ambaye ametumia miaka 18 katika huduma ya wakati wote, asema: “Utumishi wa painia huturuhusu ‘kuonja tuone ya kwamba Yehova ni mwema,’ siku baada ya siku tukijenga uhusiano wenye nguvu hata zaidi pamoja na Muumba wetu.” (Zaburi 34:8) Dada mmoja Uingereza ambaye amekuwa akipainia kwa miaka 30 anahisi vivyo hivyo. “Kupata mwongozo wa roho ya Yehova katika huduma hunileta karibu naye,” yeye asema. “Kwa kweli nimehisi kwamba roho ya Yehova katika pindi nyingi imeniongoza kwenye nyumba mahususi kwa wakati ufaao.”—Linganisha Matendo 16:6-10.

14. Mapainia wananufaikaje kwa kutumia Biblia na vichapo vya Biblia siku baada ya siku kufundisha wengine?

14 Mapainia wengi huona kwamba kutumia Biblia na vichapo vya Biblia siku baada ya siku ili kueleza na kufundisha kweli za Maandiko huwasaidia wakue katika ujuzi wa Neno la Mungu. Ndugu mwenye umri wa miaka 85 katika Hispania ambaye amepainia kwa miaka 31 aeleza: “Kupainia kumenisaidia kujipatia ujuzi wa Biblia wenye kina, ujuzi ambao lazima nitumie ili kusaidia watu wapate kumjua Yehova na makusudi yake.” Dada kutoka Uingereza ambaye amekuwa akipainia kwa miaka 23 asema: “Huduma ya wakati wote imenisaidia kusitawisha hamu ya moyoni ya chakula cha kiroho.” Kuelezea wengine “sababu ya tumaini lililo katika [wewe]” kwaweza kuimarisha usadikisho wako mwenyewe kuhusu itikadi unazozipenda sana. (1 Petro 3:15) Painia kutoka Australia asema hivi: “Kupainia huboresha imani yangu ninapojieleza kwa wengine.”

15. Wengi wamekuwa tayari kufanya nini ili kuingia katika huduma ya painia na kudumu katika hiyo, na kwa nini?

15 Kwa wazi, hawa wahudumu mapainia wamesadikishwa kwamba wamechagua aina ya utumishi utakaowaletea baraka zisizohesabika kutoka kwa Yehova. Si ajabu kwamba wengi wamekuwa tayari kufanya marekebisho katika maisha zao, hata kuacha kazi-maisha za kilimwengu na utajiri wa kimwili, kuingia katika huduma ya painia na kudumu katika hiyo!—Mithali 28:20.

Je, Moyo Wako Watamani Sana Kufanya Mengi Zaidi?

16, 17. (a) Ikiwa unajiuliza kama unaweza kupainia, unaweza kufanya nini? (b) Wengine huhisije wanaposhindwa kupainia?

16 Baada ya kufikiria yale ambayo mapainia husema juu ya baraka za huduma ya painia, labda unajiuliza kama kupainia ni jambo linalokufaa. Ikiwa ndivyo, kwa nini usiongee na painia ambaye amefanikiwa katika huduma ya wakati wote? Huenda ukaona kuwa jambo lenye msaada pia kuongea na mmoja wa wazee katika kutaniko, mtu ambaye anakujua—hali ya afya yako, udhaifu wako mbalimbali, na madaraka yako ya familia. (Mithali 15:22) Maelezo halisi ya wengine yanaweza kukusaidia ukadirie kwa uangalifu kama waweza kupainia. (Linganisha Luka 14:28.) Ikiwa unaweza kupainia, utakuwa na baraka nyingi kwelikweli.—Malaki 3:10.

17 Ingawa hivyo, vipi wahubiri wengi waaminifu wa Ufalme ambao hawawezi kupainia, ijapokuwa huenda wakatamani kufanya mengi zaidi katika huduma? Kwa mfano, fikiria, hisia za dada mmoja Mkristo anayejitahidi sana kulea watoto wake wanne akiwa peke yake. “Nahuzunika,” yeye asema, “kwa sababu nilikuwa painia wa kawaida, lakini sasa, kwa sababu ya hali zangu, siwezi kwenda katika utumishi wa shambani kama nitakavyo.” Dada huyo anawapenda sana watoto wake naye anataka kuwaandalia. Wakati uleule, anatamani sana kufanya mengi katika kazi ya kuhubiri. “Napenda huduma,” aeleza. Wakristo wengine ambao upendo wao kwa Mungu unawachochea watake kumtumikia Yehova ‘kwa moyo wao wote’ wana hisia hizohizo.—Zaburi 86:12.

18. (a) Yehova anatarajia nini kutoka kwetu? (b) Kwa nini hatupaswi kuvunjika moyo hali zikikomesha yale tuwezayo kufanya?

18 Kumbuka kwamba lile ambalo Yehova atarajia kutoka kwetu ni utumishi wa nafsi yote. Kile ambacho jambo hilo hutaka kinaweza kutofautiana sana ikitegemea nafsi moja hadi nyingine. Wengine wanaweza kurekebisha mambo yao ili watumikie wakiwa mapainia wa kawaida. Wengine wengi wanajiandikisha wawe mapainia-wasaidizi ama pindi kwa pindi ama kwa kuendelea, wakitumia muda wa saa 60 kila mwezi katika huduma. Hata hivyo, walio wengi zaidi kati ya watu wa Yehova, hujitoa wenyewe katika kazi ya kuhubiri na kufundisha kwa nafsi yote wakiwa wahubiri wa kutaniko. Kwa hiyo ikiwa kwa kweli unakomeshwa na afya mbaya, uzee, madaraka ya familia, au hali nyingine, usivunjike moyo. Maadamu unatoa yote uwezayo, utumishi wako ni wenye thamani machoni pa Mungu, kama ulivyo ule wa walio katika huduma ya wakati wote!

Wote Wanaweza Kuonyesha Roho ya Upainia

19. Roho ya upainia ni nini?

19 Hata ingawa huenda ukashindwa kujiandikisha uwe painia, unaweza kuonyesha roho ya upainia. Roho ya upainia ni nini? Huduma ya Ufalme Yetu ya Julai 1988 ilisema: “Huenda ikafasiliwa kuwa na mwelekeo chanya kuelekea amri ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, kujitia kabisa katika kuonyesha upendo na hangaikio kwa watu, kuwa mwenye kujidhabihu, kupata shangwe katika kufuata Bwana-Mkubwa kwa ukaribu, na kupendezwa si na vitu vya kimwili, bali vya kiroho.” Unaweza kuonyeshaje roho ya upainia?

20. Wazazi wanaweza kuonyeshaje roho ya upainia?

20 Ikiwa wewe ni mzazi uliye na watoto wachanga, unaweza kuwapendekezea kwa moyo wote kazi-maisha wawe mapainia. Mtazamo wako chanya kuelekea huduma unaweza kukazia kwao uhitaji wa kufanya utumishi wa Yehova uwe jambo la maana zaidi maishani mwao. Unaweza kualika mapainia na waangalizi wasafirio pamoja na wake zao nyumbani kwako ili watoto wako wanufaike kutokana na vielelezo vya wale ambao wamepata shangwe katika huduma ya wakati wote. (Linganisha Waebrania 13:7.) Hata katika nyumba zilizogawanyika kidini, wazazi wenye kuamini, kwa maneno na kwa kielelezo, wanaweza kusaidia watoto wao kufanya utumishi wa wakati wote uwe mradi maishani.—2 Timotheo 1:5; 3:15.

21. (a) Sisi sote twaweza kuwategemezaje wale wanaopainia? (b) Wazee wanaweza kufanya nini ili wawatie moyo mapainia?

21 Katika kutaniko, sisi sote twaweza kuunga mkono kwa moyo wote wale wanaoweza kupainia. Kwa mfano, je, waweza kujitahidi kuhubiri na painia katika huduma, hasa nyakati ambazo huenda ikawa painia anahubiri peke yake? Utaona kwamba kutakuwa na “badilishano la kitia-moyo.” (Waroma 1:11, 12) Ikiwa wewe ni mzee, unaweza kufanya hata zaidi utie moyo mapainia. Baraza la wazee likutanapo, wanapaswa kufikiria kwa ukawaida mahitaji ya mapainia. Painia anapovunjika moyo au anapopatwa na magumu fulani, usipendekeze kwa uharaka kwamba aache upainia. Ijapokuwa kutoa pendekezo hilo huenda kukawa lazima katika visa fulani, usisahau kwamba upainia ni pendeleo la thamani ambalo mtumishi wa wakati wote huenda akawa analithamini sana. Kitia-moyo kidogo na ushauri wenye kutumika au msaada huenda ukawa ndio unaohitajika tu. Ofisi ya tawi ya Sosaiti Hispania yaandika hivi: “Wazee wanapotia moyo kupainia, wanapounga mkono mapainia katika huduma, na kuwachunga kwa ukawaida, mapainia wana shangwe nyingi, wanahisi kuwa wenye mafaa, na wanataka kuendelea vijapokuwa vizuizi ambavyo huenda vikatokea.”

22. Katika kipindi hiki chenye hatari cha historia ya binadamu, twapaswa kuazimia kufanya nini?

22 Tunaishi katika kipindi chenye hatari cha historia ya binadamu. Yehova ametupatia kazi ya kuokoa uhai tutimize. (Waroma 10:13, 14) Iwe tunaweza kushiriki katika kazi hii wakati wote tukiwa mapainia au hatuwezi, acheni tuonyeshe roho ya upainia. Acheni tuwe na hisi ya uharaka na roho ya kujidhabihu. Acheni tuazimie kumpa Yehova yale anayotuomba—utumishi wa nafsi yote. Na acheni tukumbuke kwamba tunapotoa yote tuwezayo, iwe yanafanana na sarafu ndogo za mjane au mafuta ghali ya Maria, utumishi wetu ni wa nafsi yote, na Yehova huthamini utumishi wetu wa nafsi yote!

Je, Wakumbuka?

◻ Kwa nini huduma ya wakati wote huleta hisia za utoshelezo na shangwe?

◻ Kutokana na mambo yaliyoonwa, mapainia wengi wanajua nini juu ya uwezo wa Yehova wa kutunza watumishi wake?

◻ Mapainia wanahisi kwamba huduma yao ina matokeo gani kuhusu uhusiano wao na Yehova?

◻ Unaweza kuonyeshaje roho ya upainia?

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mapainia hupata shangwe kubwa kutokana na kufanya wanafunzi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Watoto wako wanaweza kunufaika na ushirika pamoja na wapiga-mbiu wa Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wazee wanaweza kutia moyo mapainia katika huduma ya shambani

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki