Yehova Ategemeza Jeshi Lake la Watumishi wa Wakati Wote
“Fadhili za upendo zako mwenyewe, Ee Yehova, zikawa zinanitegemeza.”—Zaburi 94:18, NW.
1. Ni nini kilichomvuta Mfalme Daudi karibu na Yehova?
MCHANA kutwa nitakubariki wewe, nami nitalisifu jina lako mpaka wakati usiojulikana, hata milele.” (Zaburi 145:2, NW) Je! unaweza kuwaza namna Mfalme Daudi, aliyeandika maneno hayo, alivyojiona kuwa karibu na Mungu? Unaweza kuhisi jinsi alivyothamini mambo, akawa amejitolea sana utumishi. Zaidi ya hayo, yeye alikuwa akitaja woga na heshima aliyokuwa nayo kwa Muumba wake, yule aliyekuwa amemfanyia mengi mno.
2. Daudi alionyeshaje kuthamini kwake wema wa Mungu?
2 Kama Zaburi 145:2 (NW) inavyoonyesha, nyakati nyingine kuthamini kwa Daudi wema wa Mungu kulifurika kukawa maneno na nyimbo za sifa. Lakini vilevile maneno na nyimbo hizo zilionyeshwa na mwendo wake wa maisha. Yeye alikuwa ametaka kumjengea Mungu hekalu, walakini aliponyimwa pendeleo hilo, Daudi alitoa hesabu kubwa sana za fedha na vitu vya kujengea kwa matayarisho yalo. Yeye hakuridhika mpaka alipowaondoa adui zote wa Mungu kutoka Nchi ya Ahadi. Kwa kipindi fulani yeye alivumilia magumu na shida, hata kuteswa, mahali pa kumkasirisha Mungu kwa kulipa kisasi juu ya mtiwa mafuta wa Mungu, Mfalme Sauli. Daudi angaliweza kuukumbuka wakati alipopigana na Goliathi na alipoua simba na dubu. Ndiyo, Mungu alimtegemeza Daudi.
3. Wewe unahisije juu ya wema wa Mungu, na huenda hilo likaonyeshwaje?
3 Je! umepata kuhisi (kuona) kama Daudi, kufurishwa na kuthamini wema wa Mungu kwako? Pengine hata ulishuka moyo kwa sababu ulitaka kuonyesha kuthamini kwako kwa kadiri kubwa zaidi ya ulivyokuwa ukifanya. Katika nyakati kama hizo inafariji kukumbuka kwamba Yehova anapendezwa na utumishi wa nafsi yote na si kitu kama utumishi huo umepungua kwa sababu una madaraka mengine ya Kimaandiko. (Linganisha Wakolosai 3:23.) Hata hivyo, Wakristo wengi wamechanganua maisha zao kwa njia ya sala waone mahali ambapo wanaweza kutafuta nafasi ya kufanya mengi katika kuonyesha upendo na kujitolea utumishi wa Mungu. Maelfu mengi wameweza kupanga waweze kuingia katika kazi ya kuhubiri na kufundisha Biblia kwa wakati wote, utumishi wa painia.
VIJANA MKARIBIENI YEHOVA
4. (a) Vijana wengi wameona nini, na wakachochewa kufanya nini? (b) Kitabu Tengenezo kinatoa pendekezo gani juu ya hilo?
4 Wengi ambao wamevutwa kwa Yehova katika miaka ya karibuni wamekuwa ni vijana. Wameona unafiki wa dini ya uongo na kushindwa kwayo kuzuia wimbi la uovu linalofurikisha dunia yote. Wameona kushindwa kabisa kwa wanadamu kujitawala kwa mafanikio na wamefadhaishwa sana na kuharibiwa kwa dunia yetu yenye thamani na wanabiashara wenye pupa. Baada ya kujifunza juu ya utatuzi wa Biblia wenye kutosheleza wa matatizo hayo, wametii shauri la mwandikaji mwenye hekima, aliyesema hivi: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako.” (Mhubiri 12:1) Mara nyingi matokeo yamekuwa kutumikia wakiwa wahudumu mapainia. Kwa sababu gani? Kitabu Tengenezo kwa Kuhubiri Ufalme na Kufanya Wanafunzi kinatoa hivi maelezo juu ya hilo: “Kila mtu ambaye ni kijana yampasa afikirie sehemu hii ya utumishi [kupainia] kwa uzito. Anapomaliza miaka yake ya elimu ya kilimwengu inayotakiwa, atayafanyia maisha yake kazi gani? Je! kweli yeye anampenda Yehova na kuwahurumia watu wale ambao bila kutaka wamo katika utumwa wa taratibu ya kale ya mambo? Ikiwa yeye ni msifaji wa Yehova aliyejiweka wakf na kubatizwa, hakutakuwako shaka. Moyo wake utamwongoza amtumikie Yehova kwa nafsi yote.”—Ukurasa 135.
5. vijana wawili walionaje hali yao?
5 Tineja mmoja katika Japan alichochewa sana na kweli ya Kimaandiko aliyokuwa amejifunza hata akawa painia msaidizi mara 19 baada ya ubatizo wake katika mwaka 1978. Kisha katika Desemba 1980, akiwa mwenye umri wa miaka 18, miezi mitatu kabla hajafuzu (hajamaliza) shule, akawa painia wa kawaida. Wakati mamaye, ambaye vilevile alikuwa painia, alipomwuliza juu ya mipango yake ya wakati ujao, jibu lake la mara moja lilikuwa kwamba sasa hivi hakuna jambo la maana zaidi ya kutimiza kazi ya kuhubiri na kuiokoka ile “dhiki kubwa.” (Mathayo 24:21) Kuthamini kwa namna hiyo kulionyeshwa na painia mmoja katika Netherlands, aliyeanza miaka tisa iliyopita akiwa mwenye umri wa miaka 19. Alipoulizwa sababu ya kuchukua utumishi wa wakati wote, yeye alijibu hivi: “Dhamiri yangu ilinisumbua kwa sababu nilikuwa nimefungwa kabisa na kazi yangu na nilimtolea Yehova masalio tu ya wakati wangu.”
JINSI YEHOVA ANAVYOWATEGEMEZA
6. Kwa sababu gani unaweza kuwa na hakika juu ya uwezo wa Mungu wenye kutegemeza?
6 Kumkaribia Mungu hivi kwa uaminifu kunatokeza jibu kutoka kwake. Mwanafunzi Yakobo anatuambia hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Ebu fikiria hilo! Mweza Yote Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote wa juu na chini kwa kweli atamkaribia mtu anayejitahidi kumfikia kwa unyofu katika vitendo vya kujitoa sana Mungu anafanyaje hivyo? Kwa sehemu anafanya hivyo kwa kumtegemeza mtu huyo kwa njia ya kiroho na hata kwa njia ya kimwili inapokuwa lazima. (Zaburi 34:10; 146:7) Dada mmoja painia mwenye umri wa miaka 71 kutoka Filipino ambaye amekuwa painia mwaminifu sana kwa miaka 31, anaandika hivi: “Tukiwa na fedha chache tunaweza kujipatia mahitaji yetu na kuendelea na kazi yangu ya painia. Sijapata kamwe kuhisi nimedhoofika kiroho.”
7. (a) Furaha na nguvu za kiroho zinahusianaje? (b) Hayo yametimiaje kwa dada wawili?
7 Njia nyingine ambayo Yehova anategemeza jeshi lake la watumishi wa wakati wote ni kwa kuwapa FURAHA, tunda la roho yake. (Wagalatia 5:22, 23) Mtume Paulo anaiandika ikiwa ya pili baada ya upendo tu anapoyataja matunda ya roho, na hiyo inafaa. Furaha inamtia mtu nguvu, ambayo pasipo hiyo hakuna “askari” ye yote anayeweza kuvumilia. Nehemia 8:10 inasema: “Furaha ya [Yehova] ni nguvu zenu [au, “itawatia nguvu,” Today’s English Version].” Ukweli wa hilo unashuhudiwa na maelezo ya dada Mkristo katika Los Angeles, California:
“Nilitaka tu kuwajulisha jinsi nilivyo mwenye furaha. Nilipokea ombi la upainia kutoka kwa mwangalizi wa mzunguko . . . na nikafanya mipango ya kuanza katika Januari 1, 1981. Januari ilipofika nilikuwa ninatetemeka sana, lakini nilimwomba Yehova abariki jitihada zangu na tafadhali aniwezeshe nimpate mtu mwenye kutaka kikweli kujifunza na mwenye kutaka ile kweli. Nilijazwa hata kufurika. Pamoja na kuwapata watu wengi wenye kupendezwa, ripoti yangu ya Januari 1981 ilikuwa ya saa 102 katika kazi ya kuhubiri, magazeti 135, vitabu 23, ziara za kurudia 47, vijitabu 2, maandikisho 3 na mafunzo ya Biblia 9. Madirisha ya mbinguni yalifunguka na baraka kutoka kwa Yehova zimenijaza sana hata moyo wangu unadunda kiasi cha kunitoka.”
Furaha hiyo yenye kutia nguvu inaelezwa pia na dada mwenye umri wa miaka 14 kutoka Brazil aliyetumia likizo lake la shule kufanya upainia msaidizi pamoja na mamaye. Yeye anaeleza hivi:
“Kila mara ninapokwenda kwenye utumishi wa shambani, ninahisi kutiwa moyo, na ninapoendelea kuhubiri ninaona kwamba ni rahisi zaidi kwangu kuwafikia watu. Huo ni utumishi unaonipa furaha nyingi, kujua kwamba ninampendeza Yehova na kwamba ndiyo njia bora ya kuutumia ujana wangu Kwa faida.”
8. Upainia unaweza kuwa na matokeo gani juu ya kuhubiri kwako kwa waziwazi?
8 Je! uliona aliyosema dada huyo kijana kwamba inazidi kuwa rahisi ‘anapoendelea kuhubiri’? Je! umepata kujionea hivyo? Mapainia wengi wamethibitisha uhakika huo, na kusema kwamba kweli kweli walianza kufurahia utumishi wa shambani sana sana walipoweza kuufanya siku baada ya siku. Kwa sababu gani? Wakristo wengi wanaoweza kuushiriki pindi kwa pindi tu wanaona kwamba wana kipingamizi kidogo kila mara wanapoanza kuhubiri mlango kwa mlango. Mara tu wakiisha kufanya ziara za kwanza chache wanaona unapendeza. kweli kweli. Hata hivyo, mapainia wanashiriki katika kuhubiri na kufundisha waziwazi kila siku, nao wamesitawisha ufundi mwingi wa kufanya hivyo, kwa hiyo ni rahisi zaidi na unafurahisha zaidi.
9. Mwangalizi mmoja anayesafiri alitoa pendekezo gani kuhusu kupainia?
9 Mwangalizi asafiriye mmoja katika Amerika alitambua kwamba wengine bila shaka wanaweza kuwa mapainia wazuri kama tu wangeonja furaha na nguvu inayotolewa na upainia na wangekuwa na uhakika kwamba wangeweza kuendelea kuwa mapainia. Yeye anaeleza aliyopendekeza:
“Inaonekana kama kwamba wengi wenye roho ya upainia wanaepuka, wakiogopa kwamba hawangeweza kuendelea katika sehemu hiyo ya utumishi. Nimependekeza kwamba waweke mradi wa kuwa mapainia kwa mwaka mmoja; kisha wanaweza kuona jinsi afya yao, orodha, na kadhalika, itakavyokuwa. Ikiwa, mwishoni mwa mwaka wanahisi hawawezi kuendelea, bado watakuwa wamekuwa na mwaka mwema wa kupainia ambao hawatasahau kamwe. Hata hivyo, wengi wanaweza kuendelea, mara wakiisha kuonja furaha zake.”
Mpango wa upainia msaidizi, ambao katika huo Mkristo anaweza kutumikia kwa wakati usiopungua mwezi mmoja au kwa miezi mingi kulingana na anavyochagua, mara nyingi umekuwa hatua yenye kuelekeza kwenye upainia wa kawaida.
10. Kwa kufaa mapainia wanaonaje juu ya msaada wa kimwili?
10 Mapainia wako mbele katika vita ya kiroho na wanafanya kazi bora sana. Hata hivyo, wao hawafikiri kwamba wanapaswa kutendewa kipekee kwa sababu ya hilo. Wanatambua kwamba wao ni ‘askari wenzi’ pamoja na mamilioni wanaomtumikia Mungu kwa uaminifu walakini wasiokuwa katika hali ya kutumikia kama mapainia. Kwa sababu ya hali zao, upainia unawasaidia kutoa utumishi wa nafsi yote, ambalo ni takwa kwa wale wote wenye kibali ya Mungu. Hawatazamii wengine wawalishe, wawavishe au wawategemeze kwa njia nyingineyo ya kimwili. Wao wanahisi sana kama Paulo, aliyesema hivi: “Kwa kazi na taabu usiku na mchana tulikuwa tukifanya kazi ili tusimwekelee ye yote wenu mzigo wa gharama nyingi.”—2 Wathesalonike 3:8, NW.
11. Kwa sababu gani Wakristo wengi wanafurahia kuwasaidia wale waliomo katika huduma ya wakati wote?
11 Ingawa Paulo hakutaka kuwa mzigo kwa ye yote, baadhi ya Wakristo wa kwanza walionyesha walithamini huduma yake kwa kumsaidia kwa njia ya kimwili. Kwa njia hiyo walimsaidia aendelee kufanya yale ambayo wao wasingeweza kufanya wakati huo. (Wafilipi 4:14-19; 2 Wakorintho 11:8) Vivyo hivyo, kuna Wakristo wengi leo ambao kweli kweli wanajitahidi sana kufikia mradi wa kupainia, lakini ambao hali zao zinafanya jambo hilo lisiwezekane kwa wakati huo. Mara nyingi wao wanashiriki kwa kujitolea kuwasaidia kimwili wale ambao kwa sasa wanaweza kupainia, na ukarimu huo, ingawa si wa kutazamiwa, unathaminiwa sana na mapainia.
12. Mapainia wangali wanahitaji kutumaini nini, kama inavyoonyeshwa na dada mmoja?
12 Wajapoonyeshwa ukarimu na washiriki wengi Wakristo, bado mapainia wanahitaji kuutumaini uwezo wa Mungu wa kuwasaidia. Painia mmoja aliandika yafuatayo hivi karibuni:
“Nimekuwa na furaha ya kuwa painia wa kawaida kwa miaka mitatu kamili. Imekuwa miaka bora ya maisha yangu. Ninamshukuru sana Yehova kwa kuniruhusu nitumikie katika cheo hicho. Hiyo imekuwa sehemu yenye kutia nguvu imani zaidi maishani mwangu katika ile kweli kwa kuwa mara nyingi nimeona Yehova akinitolea msaada. Utumishi wa wakati wote umenisaidia kuthamini sana maneno ya Yesu katika Mathayo 6:25-33. Lazima nikubali kwamba pindi kwa pindi nimekuwa na hangaiko, walakini mara nyingi ni kwa muda mfupi tu, kwa kuwa ninakumbuka tu jinsi Yehova ametimiza ahadi yake katika wakati uliopita. Kwa sababu gani nimtilie shaka sasa? Kila siku ninajaribu kuichanganua hali yangu na kukata maneno kwamba nina chakula, mavazi na makao ya kufunika kichwa changu, kama vile Yesu alisema ningepata. Unapofanya kazi ya kimwili siku mbili peke yake kila juma, unajua kwamba ni Yehova anayekuangalia. Maono hayo yanatoa usalama kama nini!”
KUPAINIA NI WONYESHO WA IMANI
13. Tunaona katika Biblia mambo gani ya kujifunza juu ya wonyesho wa imani?
13 Biblia imejawa na maonyesho ya imani. Kujenga safina kulikuwa wonyesho ulio wazi sana wa imani ya Noa na jamaa yake. Wala hatuwezi kusahau imani aliyoonyesha Ibrahimu, Sara, Yusufu, Musa na Rahabu. Lakini, kama alivyosema Paulo, “wakati usingenitosha kuleta habari za Gideoni na Baraka na Samsoni na Yeftha na Daudi na Samweli na za manabii.” (Waebrania 11:32) Kazi zao za imani hazikuwa jambo la kawaida, jambo ambalo huenda wengine wakaeleza kuwa ni ‘kutenda zaidi ya wajibu unavyokutaka.’ Hata hivyo, hawakuchochewa tu na wajibu. Upendo wao kwa Mungu na imani yao kwake, kutia uhakika wa kwamba Mungu alikuwa anakusudia kuwapa mahali “bora,” uliwachochea ‘waikiri’ imani yao. Yehova alivionaje vitendo vyao vya imani? Neno lake linajibu hivi: “Mungu haoni haya kuitwa Mungu wao; maana amewatengenezea mji.”—Waebrania 11:13-16.
14. Kupainia kunawezaje kuwa kazi ya imani kwako leo?
14 Ni kazi gani zisizo za kawaida zinazoweza kufanywa leo? Kwa wengi jibu linatia utumishi wa wakati wote, huduma ya painia. Inafahamika kwamba si wote walio washiriki wa “ushirika mzima wa ndugu” katika ulimwengu wanaoweza kupainia hata kufanya upainia msaidizi kwa ukawaida. (1 Petro 2:17, NW) Walakini hata kwa wale ambao hali zinawaruhusu, imani inatakiwa. Ndugu mmoja katika Ulaya aliandika hivi: “Wengi walinishauri nisiwe painia, kwa sababu ni wa watu wenye nguvu. Mimi sina nguvu za kimwili, na, kwa kweli, nina mgongo wenye nundu. Hata hivyo, nilianza na kwa msaada wa Yehova nimekuwa painia kwa miaka 30 sasa.” Yeye anaongeza kwamba ‘amepata uradhi mwingi kwa kuwa na orodha yenye mambo mengi inayomsaidia kumkaribia Yehova.’ Hakika Yehova amemtegemeza ndugu huyo katika utumishi wa painia.
15. Ndugu mmoja katika Japan aliionyeshaje imani yake?
15 Wala si watu wa umri fulani tu wanaopaswa kuonyesha imani katika huduma ya painia. Ndugu mmoja katika Japan alijifunza kweli ya Kikristo baada ya kuacha kazi ya ualimu wa shule, karibuni akabatizwa akiwa mwenye umri wa miaka 60, na mara moja akaingia katika kazi ya painia msaidizi. Alipokuwa mhudumu painia wa kawaida akiwa mwenye umri wa miaka 61, alifikiria juu ya mji wa mlimani alikokuwa amekulia ambako hakukuwako Shahidi wa Yehova ye yote. Yeye pamoja na mkewe, ambaye ni painia pia, waliuza nyumba yao mjini na wakahamia kwenye mji huo. Wakiwa na fedha walizopata kwa kuuza nyumba yao, jamaa hiyo ilijenga Jumba la Ufalme huko, nao wamekuwa na baraka ya kuona kundi likitengenezwa.
16, 17. Kwa sababu gani sasa ni wakati unaofaa ufikirie kwa uzito kuwa painia?
16 Wakati wa hii taratibu mbovu ya mambo iliyopo unakwisha haraka. Kama Waisraeli walivyoongeza safari yao ya kuzunguka mji mbovu wa Yeriko kabla tu ya uharibifu wake, ndivyo sasa, kabla tu Yehova hajaiharibu taratibu iliyopo, anavyowaalika watu watoe sauti kuu. (Yoshua 6:20) Je! unaweza kushiriki kikamilifu zaidi katika kutoa ile sauti kuu ya ushindi kwa kuwa painia? Ikiwa unaweza kupanga hali zako jambo hilo liwezekane, je! una imani ya kufanya hivyo? Uwe na hakika kwamba Yehova atatimiza fungu lake, akutegemeze na kuongeza furaha yako. Yeye atabariki jitihada zako. Huenda ukawa kama dada yule ambaye amepainia kwa miaka 10 katika Netherlands, aliyesema hivi: “Dhamiri yangu ilianza kuzungumza nami kwa sababu kwa kweli nilikuwa na wakati. Nilianza kupainia ili ninyamazishe dhamiri yangu yenye kusumbua na ili nijionyeshe kwamba afya yangu mbaya haingeniruhusu niendelee kuwa painia. Ningali napainia.”
17 Ndiyo, Yehova anatimiza mambo makuu katika hizi “siku za mwisho” za taratibu mbovu ya mambo iliyopo. Sasa ndio wakati wa kumkaribia na kulibariki jina lake mchana kutwa, kama alivyofanya Daudi. Uwe na imani katika ahadi ya Mungu ya kukutegemeza. Daudi aliandika hivi: “Niliposema: ‘Mguu wangu utatikisika kwa hakika,’ fadhili za upendo wako mwenyewe, Ee Yehova, zikawa zinanitegemeza.”—Zaburi 94:18, NW.
—Kutoka The Watchtower, March 1,1982.
JE! UNAWEZA KUELEZA . . .
◻ Kwa sababu gani inafaa vijana Wakristo wafikirie kupainia?
◻ Jinsi Yehova anavyowategemeza watumishi wake wa wakati wote?
◻ Kwa sababu gani kupainia ni wonyesho wa pekee wa imani?
[Picha katika ukurasa wa 20]
Mapainia wanaiona kazi ya kuhubiri waziwazi ikiwa inafurahisha na mara nyingi ikiwa na matokeo sana
[Picha katika ukurasa wa 21]
Wengi wasioweza kupainia sasa hivi wanaweza kushiriki vitu vya kimwili pamoja na wale waliomo katika utumishi wa wakati wote