Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 9/15 kur. 417-423
  • Kutembea kwa Nafsi Yote katika Njia ya Uzima

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutembea kwa Nafsi Yote katika Njia ya Uzima
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “MPATE KUZIDI SANA”
  • KUTAFUTA NAFASI YA UTUMISHI WA UPAINIA
  • JE! UPAINIA UNAKUFAA WEWE?
  • Utumishi wa Painia—Je, Wakufaa Wewe?
    Huduma Yetu ya Ufalme—1998
  • Baraka za Huduma ya Painia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Mapainia Hutoa na Kupokea Baraka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Je! Waweza Kufanya Zaidi Umheshimu Yehova?
    Huduma Yetu ya Ufalme—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 9/15 kur. 417-423

Kutembea kwa Nafsi Yote katika Njia ya Uzima

“‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa nguvu zako zote na kwa akili zako zote,’ na, ‘jirani yako kama wewe mwenyewe.’ . . . ‘Endelea kufanya hivi nawe utapata uzima.’”​—Luka 10:27, 28, NW.

1. Ni njia gani mbili za maisha zinazotofautiana zinazoonekana duniani leo?

KUPITIA kwa Mwanawe Yesu Kristo, Mpaji Mkuu wa Uzima, Yehova, sasa anatolea wanadamu “uzima ulio kweli kweli.” Ni uzima wenye maana, wenye kuleta amani na kutosheleza. Lakini watu wengi leo wanachagua namna tofauti ya uzima. Mioyo yao na nafsi zao zinaongozwa na choyo, nao wanatumia nguvu nyingi mno na akili wakifuatia anasa za muda tu za jamii ‘ya mamboleo’ yenye kuruhusu watu wafanye mambo watakavyo wenyewe. Bila ya kuwa na tumaini la wakati ujao, wanafuata wazo hili: “Na tule, na tunywe, maana kesho tutakufa.” (1 Kor. 15:32) Tofauti na hao, wako wengine wanaotazamia kuishi kesho, na milele. Hao ndio wanaopenda Mungu na jirani kweli kweli. Wao wana bidii ya ‘kutenda mema, kuwa matajiri kwa kutenda mema, kuwa tayari kutoa mali zao, washirikiane na wengine kwa moyo; huku wakijiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao.’ Na kwa sababu gani? “Ili wapate uzima ulio kweli kweli.”​—1 Tim. 6:18, 19; Zab. 36:7, 9; Yohana 17:3.

2. (a) Mungu anataka nini kwa wale watakao uzima? (b) Kwa sababu gani tunaweza kusifu wengi wasio na nafasi nyingi za utumishi wa shambani?

2 Anachotaka Mungu kwa wale watakao uzima ni utumishi wa nafsi yote. Hii maana yake ni kujitoa sisi wenyewe kama watumwa wa Mungu, na wa Kristo. (Efe. 6:6; Kol. 3:23, 24) Utumishi kwa Mungu unatia ndani na kazi ya maana ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Mashahidi wengi wanajitia katika kazi hii huku wakiangalia jamaa au madaraka mengine ya kimwili yanayopatana na Maandiko. (1 Tim. 5:8) Nyakati nyingine, inakuwa lazima hawa washinde magumu makubwa, kama vile kazi nzito sana za kila siku, mateso au afya mbaya, ili watoe saa chache tu kwa utumishi wa shambani. Lakini hata utumishi huu uliotolewa kwa kusudi hili la pekee una thamani kuu machoni pa Mungu. Ni kama zile “senti mbili” za mjane alizozizungumza Yesu kwa kuzikubali katika Marko 12:41-44. Wale ambao hawawezi kufanya utumishi mwingi sana wa shambani kwa sababu ya hali kama hizo wasivunjike moyo wakati wo wote kwamba hawawezi kuwa mapainia, wakitoa saa zisizopungua 1,200 kila mwaka katika kulihubiri na kulifundisha Neno la Mungu kwa watu wote. Jambo la maana ni kumtumikia Mungu kwa nafsi yote, katika cheo cho chote kile.​—Marko 12:30.

3. Huenda ikawezekana kuingia katika mlango unaoongoza kwenye utendaji mkubwa zaidi kwa njia gani?

3 Walakini, “mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji” uko wazi sana kwa watumishi wengi wa Mungu waliojiweka wakf, vijana na wazee. (1 Kor. 16:9, NW) Ni mlango unaoongoza kwenye utumishi wa upainia. Kwa kuwa na maoni yanayofaa juu ya magumu yanayoleta vizuizi, na kwa kuonyesha imani, wengi wanaweza kuondolea mbali vizuizi vilivyo kama mlima ili watumikie kama mapainia.​—Mt. 17:20.

4. Tukikumbuka maneno ya Paulo, Yohana na Yesu, tunaweza sasa kujiuliza maulizo gani?

4 Na tujiulize maulizo fulani: Je! kweli tunaiona haraka na kupungua kwa wakati? Je! ‘tunazidi kuhakiki ni nini impendezayo Bwana’? Je! kazi yetu ya sasa inapatana kabisa na wakf wetu kwa Yehova? Je! tunafahamu kwamba kuhangaikia mali za kimwili isivyofaa hakutatusaidia kitu? “Dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.”​—Efe. 5:10; 1 Yohana 2:17; Luka 21:34-36.

“MPATE KUZIDI SANA”

5. Imetupasa tuwe tunafanya nini kabla ya kubatizwa, na baadaye? Toa mfano wa maono ya mahali penu au ya mahali pengine.

5 Wengi wamefanya mabadiliko makubwa katika maisha zao ili wastahili kubatizwa. Wamejisafisha wakaacha njia za kilimwengu. Wametubia njia yao ya zamani ya maisha, wakageuka, wakafanya wakf wa kipekee kwa Mungu na hivyo wanatafuta kuwa na dhamiri njema kwa sababu ya kuamini damu ya dhabihu ya Yesu. Hawatimizi tena “mapenzi ya Mataifa.” (1 Pet. 4:3, 7) Lakini je! maendeleo yanakoma mtu anapojiweka wakf hivyo na kubatizwa? Hayapaswi kukoma. Katika 1 Wathesalonike 4:1, Paulo aliomba Wakristo waliokuwa wamejiweka wakf karibuni wafanye hivi: “Iliyobaki ndugu, tunakusihini na kuwaonya kwamba mwenende katika Bwana Yesu; kama mlivyopokea kwetu jinsi iwapasavyo kuenenda na kumpendeza Mungu, kama nanyi mnavyoenenda, vivyo hivyo mpate kuzidi sana.i” Hii maana yake ni kufikiri na kutenda kwa njia yenye hakika ili kupanua ushirika wa mtu katika kazi ya Mungu, ikiwezekana. Mwangalizi Mkristo anaandika hivi:

Miaka mitano iliyopita, nilimpinga mke wangu alipojifunza na mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza. Lo! ninashukuru namna gani kwamba yeye hakuacha! Wakati huo nilikuwa mcheza golf sana (mchezo wa kutumia fimbo za kupigia mipira midogo migumu na kuiingiza katika mfululizo wa vishimo tisa au kumi na vinane), mvua samaki, mcheza kamari katika MahJongg. Nilikuwa nikivuta sigara 40 kwa siku. Lakini kweli ikatia mizizi katika moyo wangu pia. Nikaacha mambo haya yote kama yasiyofaa kitu na yasiyostahili. Waliokuwa rafiki zangu kwanza wakanifanyia mzaha, lakini baadaye wakaacha kunipinga na hata wakanitia moyo niendelee na mwendo wangu. Mama na dada yangu wakanipinga vikali. Lakini nikaanza kufanya kazi ya kibarua ambayo mshahara wake ulikuwa sehemu moja tu kwa tano ya mshahara niliokuwa nikipata hapo kwanza, ili niingie utumishi wa upainia. Nikaweza kuangalia mke wangu painia na mtoto wangu mdogo kwa kuongezea akiba yangu kwa kiasi hicho. Nikapata kujifunza namna Yehova anavyosaidia kwa njia mbalimbali za ajabu. Sasa ninaongoza mafunzo saba ya nyumbani ya Biblia, na, kati ya haya, watu wawili wamekwisha anza kutumikia kama wahubiri wenye bidii. Sasa mama anasifu jamaa yetu kwa sababu ya kutembea katika njia ya kweli, nami nasali kwamba yeye, pia, awe mmoja wa mashahidi wa Yehova karibuni.

Shahidi huyu hakuacha kusonga mbele alipojiweka wakf. Lo! imetokea furaha ya namna gani!

6. Ni kwa njia gani tunavyoweza kuona kazi ya kila siku kama Paulo, katika taratibu iliyopo? Onyesha jambo hili linavyofaa kwa kutumia maono ya mahali pako au ya mahali pengine.

6 Sote tunaojiweka wakf kwa Yehova tumepaswa tufikirie haya: Je! tunafanya mapenzi yake kweli kila siku ya maisha zetu? Au tungali tunaishi hasa kwa ajili yetu wenyewe, bila kufikiria kwa uzito kufanya mapenzi ya Mungu? Ingawa huenda utumishi wa upainia ukahitaji mtu aache kazi na kujinyima faida za kimwili, unaleta baraka za kiroho zisizo na kifani. Mtume Paulo aliona faida za kilimwengu kuwa “mavi,” na kwa hiyo ‘akayachuchumilia yaliyo mbele.’ (Flp. 3:7, 8, 13) Wote wanaojiweka wakf kwa Yehova leo wamepaswa wafikirie kwa uzito kama Paulo, kama wanaweza kupanua utendaji wao.

Afisa wa serikali alikuwa amefanya kazi miaka 34, miaka kumi akiwa msimamizi. Mke wake na binti zake wawili wakajifunza kweli wakawa mapainia. Yeye akajifunza pia, halafu akaanza kuvutwa moja kwa moja. Alipokuwa katika safari ya biashara New York, akafika siku moja Yankee Stadium, ambako Kusanyiko la Mataifa Yote la Mashahidi wa Yehova la mwaka wa 1969 lilikuwa linafanyiwa. Alipouona umoja, upendo na amani kati ya makundi katika kusanyiko hilo akasadiki kwamba tumaini la taratibu mpya si ndoto. Baadaye mwaka uo huo, akahudhuria kusanyiko hilo lote katika Hawaii, pamoja na mke wake. Ukarimu alioonyeshwa na Mashahidi huko katika mazingira ya kupendeza ukamwonyesha namna paradiso inavyoweza kuwa. Akafanya marekebisho ili astahili kubatizwa. Lakini je! kweli yeye alipaswa kufanya kazi ya kimwili? Kwa kweli sivyo. “Ushindi wa Kimungu” Kusanyiko la Mataifa Yote katika Julai 1973 likamsadikisha kwamba kazi yake imepaswa kuwa upainia. Siku mbili baada ya kusanyiko, akaacha cheo chake, na mwezi mmoja baadaye akajiunga na jamaa yake katika utendaji wa upainia wa kawaida. Amepata baraka ya Yehova kweli kweli​—vile vile akawa na ngozi yenye afya ya rangi ya maji ya kunde kwa sababu ya kupigwa na miale ya jua.

7. (a) Kulingana na aliyosema Paulo, imetupasa tukimbie mambo gani, na ni mambo gani imetupasa tufuatie? (b) Toa mfano wa namna Yehova anavyobariki mtu anapoacha kufuatia mali za kimwili.

7 Ni hatari kuingia sana katika njia ya maisha ya kutafuta mali za kimwili, kuweka mioyo yetu juu ya mali za kimwili na anasa, na kuacha shughuli hizo zitawale maisha zetu. Biblia inashauri, si kuondolea mbali tu “mambo yenye kudhuru” ya kimwili yanayotokana na “kupenda fedha,” bali pia ‘kuyakimbia mambo haya.’ Hii maana yake ni kutenda kwa haraka, sawa na ilivyo katika ‘kukimbia’ tamaa mbaya, ‘kukimbia’ uasherati na ‘kukimbia’ ibada ya sanamu. Kufanya haraka tufuate njia iliyo tofauti na hiyo kutatusaidia tukimbie utafutaji wa mali za kimwili tukichukua hatua zinazofaa, ili ‘tufuate haki, na imani, na upendo, na amani.’ Wengi wamefanya hivi kwa kuingia utumishi wa upainia, ambao unawatayarisha vizuri sana ‘kupiga vita vizuri vya imani’ na ‘kushikilia sana’ uzima wa milele. (1 Tim. 6:10-12, 17-19, NW; 2 Tim. 2:22; 1 Kor. 6:18; 10:14) Dada kijana anaandika hivi:

“Kizuizi kimoja nilichopaswa kushinda niingie utumishi wa upainia kilikuwa mazingira yangu​—utajiri na utafutaji wa mali za kimwili, pamoja na vishawishi vingi vya kilimwengu. Kilikuwa kama Mathayo 13:22 inavyosema juu ya mbegu iliyopandwa kati ya miiba mingi, lakini mimi nikazidi kufikiria ingekuwa vema namna gani kuonyesha imani yenye nguvu kama ya Musa. (Ebr. 11:24-27)” Kwa hiyo dada huyu akaepuka maisha ya kijamii yaliyohusiana na hoteli ya jamaa yao yenye mambo ya anasa inayojulikana katika mataifa yote. Alipopangiwa kuwa na arusi ya heshima nyingi, hii nayo akaikataa. Akasitawisha roho ya kufanya upainia pamoja na mama yake na dada yake mdogo. Akawa painia wa kawaida katika eneo asilogawiwa mtu lililo karibu na mpaka wa mgawo wa painia wa pekee. Ameshiriki na mapainia wengine katika furaha ya kukuza eneo hili, hata leo wanalo kundi jipya lenye wahubiri 39 wa kundi, pamoja na mapainia saba, nao walikuwa na hudhurio la watu 116 katika Ukumbusho mwaka wa 1974. Dada huyu anasema hivi: “Kikundi kilichomo katika eneo langu kinaendelea kuongezeka. Sasa watu 20 wanahudhuria mkutano wetu wa Jumanne jioni, na dada watatu wapya walibatizwa katika kusanyiko letu la mzunguko. Nashukuru sana kwa baraka na ongezeko ambalo Yehova anatoa. Afya yangu, niliyokuwa na wasiwasi nayo, imekuwa nzuri sana, nami natumikia kwa furaha kila siku.”

Shahidi huyu kijana hakika alichagua “uzima ulio kweli kweli.”

8. (a) Ni kazi gani ya kila siku yenye kuthawabisha inayongoja vijana leo? (b) Wazee wengi pia wamejirudishiaje furaha ya ujana?

8 Kumpenda Yehova kumepaswa kutuongoze tutumie nguvu zetu na mali zetu na uwezo wetu katika utumishi wake. Ni nafasi nzuri namna gani zilizoko mbele yetu wakati tungali vijana! “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, kabla hazijaja siku zilizo mbaya, wala haijakaribia miaka utakaposema, Mimi sina furaha katika hiyo.” (Mhu. 12:1) Kwa kutumia nguvu za ujana na uwezo ili kusaidia wengine wajifunze mapenzi ya Mungu, vijana watapata kazi yenye kutosheleza na yenye kuthawabisha kuliko zote duniani leo. Wazee, wengi, pia, wanatoa msaada unaostahili sana kusifiwa, ingawa nguvu zao zinazidi kupungua.

Dada aliye painia wa kawaida mwenye umri wa miaka 82 anapingwa na jamaa yake. Lakini yeye anaamka saa tisa usiku afanye kazi zake za nyumba iliyo katika shamba, ili aweze kuwa na wakati wa utumishi wa shambani baadaye mchana. Kila mwezi anatoa saa 120 kwa wastani za utendaji wa shambani, akigawa magazeti 140 na kuongoza mafunzo kadha ya nyumbani ya Biblia.

9. (a) Wazazi wanawezaje kusaidia sana watoto wao? (b) Mfano wa wazazi wenyewe unawezaje kusaidia jamaa zao na wengine katika kundi?

9 Je! wewe ni mzazi mwenye watoto wadogo? Wazazi wanaweza kusaidia watoto wao sana kwa kubadili kufikiri kwao kulingane na kanuni za Biblia, wakipendekeza kwa moyo wote watoto wachague upainia uwe kazi yao ya kila siku. Hivyo watoto wanapata mradi wa kweli katika maisha, pamoja na imani yenye nguvu. (Ebr. 11:6) Ikiwa wazazi wenyewe wanaweza kutafuta nafasi ya kufanya upainia, basi jamaa yote inafaidika kutokana na kujitoa kwa kila siku kufanya mambo ya kitheokrasi, na wote wanaweza kusaidiwa kwa njia hiyo kukua pamoja kiroho wakiwa katika kifungo cha upendo wa kweli wa Kikristo. (Kol. 3:14-21) Mfano huu unaweza kuwa na matokeo yanayofaa, pia, juu ya maoni ya jamaa nyingine katika kundi.​—Flp. 3:17; 1 The. 2-7.

Mmoja wa mashahidi wa Yehova aliacha kazi yake ya usimamizi katika kiwanda cha motokaa, ili yeye na mke wake waweze kutumikia pamoja kama mapainia na kulea watoto wao wadogo wakiwa na mradi uo huo. Baada ya miaka mitatu pesa zao zikaisha, lakini wao wakatafuta njia ya kubaki katika utumishi wa upainia kupatana na Mathayo 6:33. Yehova akajibu sala zao, na mume huyo, ambaye sasa ni mwangalizi wa Kikristo, akaweza kupata kazi inayofaa ya kibarua pamoja na ndugu wengine. Anasema kwamba wakati wa miaka yake ya utendaji wa upainia amejifunza kutokuwa na maoni ya kibinadamu juu ya mambo. Anaona Waebrania 1:1, 2 ndicho kiongozi cha utumishi wa upainia wenye matokeo mazuri. Mwana mmoja sasa anatumikia katika Betheli Japan, naye binti ni painia wa kawaida. Katika Julai 1970, wakati ndugu huyu alipoingia utumishi wa upainia, kundi la mahali pake lilikuwa na jumla ya wahubiri 60 tu lakini katika Machi 1974 wakaripoti mapainia 63, na mwezi uo huo wapya 51 wa kundi hili wakabatizwa katika kusanyiko la mzunguko. Kwa jumla, sasa wana wahubiri 225. Jamaa hii moja imeleta zaidi ya wapya 30, kutia na jamaa nzima sita nyingine, kwenye ushiriki wa kundi la Kikristo.

Wakati roho ya kufanya upainia kwa jamaa yote inapoenea katika kundi, inaleta baraka ya ajabu kweli kweli kutoka kwa Yehova.​—Mit. 28:20.

10, 11. (a) Waamini katika jamaa zilizogawanyika wanabarikiwaje mara nyingi? (b) Ukitumia mfano wa mahali pako au mifano ya mahali pengine, onyesha namna upainia unavyoleta baraka na ulinzi.

10 Katika jamaa zilizogawanyika pia, akili za watoto zinaweza kutengenezwa na mzazi mwenye kuamini. Watoto wanajaribu mara nyingi sana kufuata mfano wa maisha wa mzazi huyo! Bila shaka, mara nyingi hii ni kwa sababu mtoto anaona na kuthamini mwenyewe “haki ile itokayo kwa Mungu, kwa imani.” (Flp. 3:9) Kwa neno na kwa mfano, wazazi waliojitoa wanaweza kutia watoto wao moyo wanapojitayarisha kufanya utumishi wa Yehova kazi yao ya maisha, kama vile Eunike alivyomtia moyo mwana wake Timotheo.​—2 Tim. 1:5; 3:15; Mit. 4:1-9.

Shahidi kijana alitiwa moyo na mama yake ambaye ni painia ashiriki katika utumishi wa upainia wa muda mara kwa mara wakati wa miaka yake mitatu akiwa katika shule ya masomo ya juu. Kijana huyo akamwomba baba yake asiyeamini mara nyingi ampe ruhusa ya kuingia utumishi wa upainia wa kawaida akiisha kuhitimu, lakini baba yake akataka aendelee mpaka chuo kikuu. Mwalimu wake akamlaumu kwa sababu ya kuhubiri kwake kwa bidii wakati wa likizo ambapo angaliweza kuwa anajitayarishia mtihani wa kuingia katika chuo kikuu. Lakini bila ya kutazamiwa, karatasi ya mtihani ilikuwa na maulizo mengi juu ya Biblia. Kwa hiyo akaweza kupita akiwa mbele ya wengi wa wanafunzi wale wengine. Kwa kupanga asiwe na orodha yenye mipango mingi ya masomo ya chuo kikuu, sasa akaweza kujiandikisha awe painia wa kawaida. Kati ya mafunzo mengi ya nyumbani ya Biblia ambayo ameongoza, manne yalifanywa jioni kwa waume wenye kupendezwa wa akina dada katika kundi. Wawili kati ya waume hawa walibatizwa katika “Ushindi wa Kimungu” Kusanyiko la Mataifa Yote.

11 Kutumikia kila mwezi na kila mwaka katika utumishi wa upainia ni maisha yenye kazi nyingi sana. Lakini kufanya kazi nyingi hivi ya Ufalme kunaweza kuwa ulinzi mzuri sana leo.​—Efe. 5:15-17.

KUTAFUTA NAFASI YA UTUMISHI WA UPAINIA

12. Jamaa zinaweza kushirikiana kwa njia gani ili mshiriki mmoja au washiriki zaidi waweze kutumikia kama mapainia?

12 Mtume Paulo aliweka mfano bora katika kujitafutia riziki (chakula n.k.) yeye mwenyewe pamoja na wenzake ili wote waweze kuendeleza kabisa faida za kiroho. Angeweza kusema hivi: “Sikutamani fedha wala dhahabu, wala mavazi ya mtu. Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami.” (Matendo 20:33, 34) Kanuni iyo hiyo inaweza kutumiwa kwa jamaa za Kikristo. Mradi wa jamaa unaweza kufanywa uwe kwamba mshiriki mmoja au washiriki zaidi wa jamaa, au hata jamaa yote, itaingia utumishi wa upainia. Hata hivyo, inafaa kila mmoja aliye katika utumishi wa upainia atumie mikono yake mwenyewe asaidie kujiruzuku (kujitafutia chakula, mavazi n.k.) mwenyewe. Washiriki wote wa jamaa, wawe hasa katika utumishi wa upainia au wasiwe, wamepaswa wapendezwe na kuendeleza utendaji wa upainia na kuwa wenye nia ya kujinyima mambo fulani kwa kusudi hilo.​—2 Kor. 8:13-15.

13. Ni nini kinacholipia mambo ambayo mtu amejinyima ili awe painia? Toa mfano.

13 Huenda ikawa lazima mume aache kazi yenye mshahara mkubwa ili aingie utumishi wa upainia, au huenda ikawa lazima jamaa iache mambo fulani ya anasa za kimwili. Lakini baraka na furaha ya utumishi huu wa wakati wote zinalipa zaidi.​—Marko 10:29, 30; Rum. 14:17.

Daktari mmoja kijana, ambaye sasa m mwangalizi katika kundi la Kikristo, anaandika hivi: “Ilinipasa kufanya kazi asubuhi na mapema mpaka usiku sana, kutia na siku ya Jumapili na nyakati za sikukuu, katika Hospitali ya Chuo Kikuu. Walakini, nikapata kazi ya udaktari ya kibarua katika mji mwingine, ambayo iliniwezesha nianze upainia. Mke wangu alikuwa amelelewa katika jamaa yenye utajiri, lakini kwa furaha akaacha njia yake ya maisha ya juu ili awe painia. Akaendelea kutumia mavazi aliyokuwa nayo kabla hajaingia utumishi wa upainia, naye alitoshelezwa na vyakula visivyo vya bei ya juu. Akafahamu sana kwamba mavazi bora na upishi unaomaliza wakati mwingi si wa lazima katika kumtumikia Yehova. Afya yake iliyokuwa mbaya ikawa na maendeleo, naye ameweza kufurahia utumishi wake wa upainia, akaongoza watu wanne wajiweke wakf, wawe wenzi wake wa kweli. Mimi mwenyewe nimeweza kusaidia mtu mwenye nyumba ya unyoaji wa nywele ajiweke wakf, na watu watano wa nyumba hiyo sasa wamekuwa wahubiri wenye bidii, wakifanya zamu za kwenda katika utumishi wa shambani. Wanamsifu Yehova katika mpango wa jamaa. Kwa kuthamini baraka hizi za ajabu kutoka kwa Yehova, tunaomba kwa moyo wote atuendeleze katika utumishi wa upainia.”

14. (a) Wakati magumu ya hali ya uchumi yanapotokea, yanaweza kumalizwaje? (b) Toa mfano wa ukweli wa yanayosemwa na Wafilipi 4:13.

14 Ni mapainia wangapi wanaoshindana na magumu ya hali ya uchumi yanayotokea? Jambo la maana ni imani, kutafuta Ufalme kwanza. (Mt. 6:33) Palipo na imani, pana njia. Huenda ikawa lazima painia ajinyime vitu fulani, lakini kufanya hivyo kunampendeza Mungu.​—Luka 9:23-25; 18:29, 30.

Mmoja aliyekuwa mwangalizi wa mzunguko, ambaye anaendelea kufanya upainia na mke huku wakiangalia kitoto chao pia, anasema hivi: “Tulipopata mtoto wetu huo ulikuwa ugumu uliotuhitaji tumtegemee Yehova huku tukikaza nia kwa moyo wote tuangalia daraka hili. Kupatana na Luka 14:28, 29, tukahesabu gharama (bei) za maisha zingekuwa kadiri gani kwetu watatu. Nikapata kazi ya kugawa magazeti asubuhi na mapema, kwa maana haikutumia nguvu nyingi mno. Mtoto wetu akazaliwa siku mbili tu kabla ya ‘Ushindi wa Kimungu’ Kusanyiko la Mataifa Yote nasi tukapanga kwa uangalifu kufunga safari hiyo ya maili 1,300 kwenda na kurudi, ingawa ilikuwa imeshauriwa mke wangu apumzike juma tatu. Hivyo tukaweza kuhudhuria, nacho kitoto kikarudi nyumbani kikiwa kinene na salama. Tunapohubiri mlango kwa mlango, kila mmoja wetu anakuwa na zamu ya saa moja na nusu ya kuwa na kitoto hiki. Kwa sababu kitoto kinakuwa pamoja nasi katika utumishi mchana kutwa, kinalala fofofo usiku, nasi hatuwi na magumu kama watu wengine ambao inakuwa lazima waamke usiku kuangalia kitoto kinacholia. Sote tunalala vya kutosha. Kwa kuona mfano watu, akina mama wengine wa nyumbani katika kundi wamepanga sasa kuingia utumishi wa upainia. Wote wawili, tunaongoza mafunzo ya nyumbani ya Biblia kumi na matano sasa, na Septemba tuliweza kusaidia mama wawili wa nyumbani na mume mmoja waanze kwenda katika utumishi wa shambani. Wengine watano kati ya mafunzo yetu wanaohudhuria mikutano wanatazamiwa kuanza utendaji wa shambani karibuni. Tumepata kufahamu mioyoni mwetu kwamba Mkristo anayeshindana na ugumu anaweza kutimiza mengi kwa nguvu za Yehova.​—Flp. 4:13.

15. (a) Yesu anatoa uhakikisho gani katika Mahubiri juu ya Mlima? (b) Ni matayarisho gani yamepaswa yafanywe kwa ajili ya utumishi wa upainia?

15 Imani yenye nguvu na akili ni ya lazima katika kufanya marekebisho ya kuingia na kukaa katika utumishi wa upainia. Yehova anaweza kuruzuku kwa njia ya ajabu. Je! maneno ya Yesu katika Mathayo 6:24-34 hayahakikishi ndivyo ilivyo? Wote wanaotaka kupanua utumishi wao kwa Mungu wamepaswa wafikirie fungu hili la maneno kwa uangalifu na andiko jingine linalohusiana na hilo katika Luka 12:22-31. Hii haina maana ya kujitupa katika kazi ya upainia bila ya kujitayarisha vya kutosha. Haina maana ya kuweka akiba ya pesa za kutosha tu zikufikishe kwenye tarehe fulani ya 1975. Bali, maana yake ni kupanga mambo yako ili ukae katika utumishi wa wakati wote, mwaka baada ya mwaka, wakati uo huo ukiangalia jamaa na madaraka mengine inavyofaa. Kwanza, ‘hesabu gharama,’ kisha uchukue hatua zinazofaa kufikia mradi wa utumishi wa upainia.​—Luka 14:28; 17:5, 6.

16. (a) Mapainia wanawezaje kuendeleza bidii na furaha? (b) Toa mfano wa namna kubadilika ili tuchukuane na magumu kunavyoweza kuleta baraka ya Mchungaji Mkuu?

16 Ili kuwa na upainia wenye matokeo mazuri, ni jambo la maana kuendeleza hali ya kiroho. Kuhudhuria kwa kawaida mikutanoni na kushiriki katika hiyo kwa bidii, kusoma Biblia kila siku na kuzungumza andiko la siku katika Mnara wa Mlinzi, kuwa na orodha ya funzo la pekee lenye bidii​—⁠mambo haya yanaweza kusaidia painia aendeleze bidii na furaha yake, na kumtayarisha kushinda magumu yasiyo ya kawaida yasiyotazamiwa. (Zab. 1:1-3) Baada ya miaka kumi ya utumishi wenye mazao mengi sana akiwa painia, dada mmoja anaandika hivi:

Kwa kuwa kazi ya mume wangu ya televisheni inamtaka ahamie sehemu nyingine ya nchi kila miaka miwili, nimetumikia katika makundi tisa, matano kati ya hayo tangu nilipoanza utumishi wa upainia wa kawaida. Ninaacha upesi mafunzo yasiyofanya maendeleo, na kujaribu kutia nguvu wale ambao wanamtambua Yehova kweli kweli. Kila mahali, Mungu wetu wa ajabu ameonyesha uwezo wake, kwa maana nimesaidia wastani ya watu watano wapate kweli. Mkutano wa kwanza niliohudhuria katika mji mmoja ulikuwa katika chumba kimoja kidogo cha majamvi wakiwako watu wengine watano. Nilipotoka huko miaka miwili baadaye, watu 62 walikuwa wakihudhuria mkutano huu. Katika mji uliofuata nikaweza kusaidia watu wanane wawe wasifaji wa Yehova, nami nikaona hudhurio likiongezeka kutoka watu 25 kufikia karibu 100. Katika mji uliofuata, tulianza tukiwa na mapainia wa kawaida wawili tu, lakini mimi nikaona wengine kumi wakiwa mapainia. Nilipokwisha kuhudhuria vipindi vyote vya “Uhuru wa Wana wa Mungu” Kusanyiko la Wilaya mwaka wa 1966, nikazaa mtoto wangu wa tatu asubuhi iliyofuata. Lakini nikaweza kutoa ripoti ya saa 1,294 za utumishi mwaka huo. Badala ya kuzuiwa na kitoto hiki, nikarekebisha maisha yangu nikiwa pamoja na kitoto kufuata mwendo unaofaa, nami nikaweza kuendelea kufanya upainia. Watu ambao nimejifunza nao, wamerekebisha maisha zao pia baada ya kubatizwa ili waingie utumishi wa upainia wa muda halafu wa kawaida. Wao, kama mimi, wamejifunza kutoacha wakati wo wote kusoma Biblia kila siku, kujifunza na kusali, hata wanaendelea kuwa na furaha na nguvu nyingi. Katika hali zote, Yehova, Mchungaji wetu Mkuu, yuko karibu sana.​—Isa. 40:11, 31.

17. Wazee wanawezaje kusaidia mapainia na wengine wawe wenye bidii katika utumishi wa Mungu?

17 Wazee katika kundi wana pendeleo kubwa sana katika kutia moyo utumishi wa upainia ufanywe. Mara nyingi wanaweza kutoa mashauri na msaada unaofaa, ili mapainia waweze kuendelea katika utendaji huo. Pia, wanaweza kupendekeza utumishi wa upainia kwa wengine.​—Linganisha Waebrania 6:11, 12.

JE! UPAINIA UNAKUFAA WEWE?

18, 19. (a) Ni maulizo gani yanayoweza kufaa sasa? (b) Je! Iko sababu ya mtu kuvunjika moyo asipoweza kuwa painia?

18 Ni wewe peke yako unayeweza kujibu ulizo hilo. Wewe umeuonaje utumishi wa upainia kufikia hapo? Kama jambo linalopaswa kufanywa na wengine? Je! umesita-sita kwa sababu unapendelea kazi ya kimwili badala ya kuhubiri habari njema kila siku? Au kweli hali zako ndizo zimetaka ufanye unalofanya? Kutumikia kidogo tu kumeelekea kutosha? Moyo wako unakuongoza ufanye nini sasa? Baada ya kufikiria mambo haya yote, unaweza kusema NDIYO kwa ulizo, Je! utumishi wa upainia unakufaa wewe? Ikiwa ndivyo, baraka yako itakuwa kubwa kweli kweli.​—Mal. 3:10.

19 Lakini namna gani hesabu kubwa ya wasomaji wetu ambao hawako katika hali ya kuingia utumishi wa upainia wa kawaida? Je! wavunjike moyo wakati wanapoona wengine wakianza utendaji huu? Hata kidogo! Kila mmoja wa watu wa Yehova anaweza na amepaswa awe mwenye kutumikia kwa nafsi yote katika utumishi wa Yehova. Nyakati nyingine huenda wakaweza kurekebisha mambo yao watumie juma mbili, au mwezi au zaidi, katika utumishi wa upainia wa muda, nayo hii italeta baraka kubwa. Wengine wanaweza kujitoa wahubiri na kufundisha kwa nafsi yote wakiwa wahubiri wa kundi.

20. (a) Ingawa nafasi za utumishi zinaweza kuwa chache, sikuzote tuna uhakikisho gani? (b) Toa mfano wa namna Yehova anavyobariki mtu akitia jitihada ya nafsi yote.

20 ‘Yehova anawajua walio wake,’ na wote hawa anawabariki, hata utumishi wao wa shambani uwe mdogo namna gani. (2 Tim. 2:19; Mit. 10:22) Hata anaweza kubariki wale wasioweza kushiriki na wahubiri wengine katika utumishi wa shambani uliopangwa, kwa sababu ya ugonjwa, uzee, mateso na sababu nyingine. Yehova anaijua mioyo yao.​—Linganisha 1 Samweli 16:7.

Kijana wa kike wa shule ya masomo ya juu alijifunza kweli akaanza utumishi wa nyumba kwa nyumba. Lakini baba yake akampinga vikali sana na kumkataza asishiriki utendaji wo wote pamoja na mashahidi wa Yehova. Angeweza kufanya nini? Akawapa wanadarasa wenzake ushuhuda shuleni, akaanza mafunzo mengi ya Biblia katika daraka alilokuwa na madarasa mengine. Matokeo yenye furaha yalikuwa nini? Watatu kati ya wale aliokuwa akijifunza nao ni wenye bidii sana sasa katika kweli​—dada mmoja akiwa painia wa pekee, ndugu mmoja akiwa painia wa kawaida na mtumishi wa huduma, na ndugu mwingine akiwa painia wa kawaida na mwangalizi. Sasa, miaka mingi baadaye, dada huyu mwaminifu ameweza kutoka katika upinzani, naye mwenyewe anashiriki katika utumishi wa upainia wa muda.

Yehova anabariki utumishi wa nafsi yote.

21, 22. (a) Kutumikia “kwa nafsi yote” kunatofautianaje kati ya watu? (b) Kwa sababu gani imetupasa tusali hivi, “Tuongezee imani”?

21 Wakati Paulo alipotia waamini moyo kwamba, “Kama watumwa wa Kristo, fanyeni ya Mungu kwa nafsi yote,” hakuwa akiomba Wakristo wafanye jambo lisilowezekana. Nafsi yako ndiyo WEWE. Unaweza kujitoa ufanye mapenzi ya Mungu kulingana na ulivyo, kulingana na uwezo wako mbalimbali na nafasi zako. Watu wanatofautiana, na hii inakubaliwa katika mifano mingine ya Yesu, ambamo wengine wanapewa vitu zaidi, na wengine wanaonyeshwa wakileta mazao machache zaidi, ingawa wanakubaliwa.​—Efe. 6:6; Mt. 13:23; 25:19-23; Luka 19:15-19.

22 Mambo na yawe kwako kulingana na nafasi na imani yako. Kwa kutembea kwa nafsi yote sasa katika njia inayoongoza kwenye uzima wa milele, utosheke na kufurahi unaposhiriki katika kazi hii ambayo haitarudiwa tena kwa kadiri inayowezekana​—⁠yote kwa sifa ya Yehova. Unapofikiria unavyoweza kufanya hili, na uwe na hali ile ile ya kusali waliyokuwa nayo mitume wa Bwana wetu, wakati walipomwambia hivi: “Tuongezee imani.”​—Luka 17:5, 6.

​—Kutoka The Watchtower, Mar. 15, 1975.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki