Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 7/98 kur. 3-6
  • Utumishi wa Painia—Je, Wakufaa Wewe?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Utumishi wa Painia—Je, Wakufaa Wewe?
  • Huduma Yetu ya Ufalme—1998
  • Habari Zinazolingana
  • Kutembea kwa Nafsi Yote katika Njia ya Uzima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Mapainia Hutoa na Kupokea Baraka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Baraka za Huduma ya Painia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Yehova Ategemeza Jeshi Lake la Watumishi wa Wakati Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
Pata Habari Zaidi
Huduma Yetu ya Ufalme—1998
km 7/98 kur. 3-6

Utumishi wa Painia—Je, Wakufaa Wewe?

1 “Siwezi kuwazia nikifanya jambo jingine lolote. Hakika siwezi kuwazia chochote ambacho kingeleta shangwe iyo hiyo.” Ni nani aliyesema hivyo? Mmoja wa mamia ya maelfu ya Mashahidi wa Yehova ambao wameufanya utumishi wa wakati wote kuwa kazi yao ya maisha yenye shangwe. Kwa njia ya sala, je, umefikiria kama waweza kufanya utumishi wa painia? Tukiwa tumejiweka wakfu kwa Yehova bila masharti, bila shaka twahitaji kuchunguza kama twaweza kushiriki kikamili zaidi katika kueneza habari njema ya Ufalme. Ukiwa na mradi huo akilini, tafadhali fikiria maswali kadhaa ambayo wengi huuliza kuhusu utumishi wa painia.

SWALI LA 1: “Watu fulani husema upainia si wa kila mtu. Najuaje kama wanifaa?”

2 Jibu lategemea hali zako na wajibu wako wa Kimaandiko. Kuna wengi ambao afya yao au hali yao ya sasa maishani haiwaruhusu kuhubiri muda wa saa 90 kila mwezi katika huduma. Mfano mmoja ni dada wengi waaminifu ambao ni wake na ni akina mama Wakristo. Wao hushiriki katika huduma mara nyingi wawezavyo kadiri hali zao ziruhusuvyo. Fursa ipatikanapo, wao hufanya upainia-msaidizi kwa mwezi mmoja au zaidi kila mwaka, wakipata shangwe ambazo hutokana na kupanua ushiriki wao katika utumishi. (Gal. 6:9) Ijapokuwa huenda hali zao zisiwaruhusu kutumikia wakiwa mapainia wa wakati wote wakati huu, hao huchochea roho ya upainia nao ni baraka kwa kutaniko wakiwa wahubiri wenye bidii wa habari njema.

3 Kwa upande ule mwingine, ndugu na dada wengi wasio na wajibu kwa kulinganisha wamerekebisha mambo yao ya kutangulizwa ili wapate nafasi kwa ajili ya utumishi wa painia. Vipi wewe? Wewe ni kijana ambaye umemaliza shule? Wewe ni mke ambaye mume wako aweza kuandalia familia yako ifaavyo? Je, mmeoana na hamna watoto wanaowategemea? Je, umestaafu kazi yako ya kimwili? Kupainia au kutopainia ni uamuzi ambao kila mtu lazima aufanye mwenyewe. Swali ni hili, Waweza kuupa upainia nafasi maishani mwako?

4 Shetani hutumia mfumo wake wa mambo wa kilimwengu kujaza maisha zetu na vikengeusha-fikira na vilevile kutulemeza katika maisha ya ubinafsi. Tukiazimia kutokuwa sehemu ya ulimwengu, Yehova atatusaidia tutangulize masilahi za Ufalme na tufikie mapendeleo yote ya utumishi wa kitheokrasi yanayopatikana kwetu. Ikiwa waweza kurekebisha hali zako ili utumikie ukiwa painia, kwa nini usifanye hivyo?

SWALI LA 2: “Nawezaje kuwa na uhakika kwamba nitaweza kujiruzuku kifedha nikiwa katika utumishi wa wakati wote?”

5 Ni kweli kwamba katika nchi nyingi saa za kazi ya kimwili ya kupata kile kinachoonwa kuwa mahitaji ya lazima ya maisha kila juma zimeongezeka katika muda wa miaka iliyopita. Hata hivyo, wengi wamepainia kwa miongo kadhaa, na Yehova huendelea kuwategemeza. Ili kufanikiwa ukiwa painia, imani na roho ya kujidhabihu vyahitajiwa. (Mt. 17:20) Katika Zaburi 34:10 tuna uhakikisho kwamba ‘wamtafutao Yehova hawatakosa kitu chochote chema.’ Yeyote anayeingia utumishi wa painia apaswa kufanya hivyo akiwa na uhakika kabisa kwamba Yehova atamwandalia. Yeye anafanya hivyo kwa mapainia waaminifu kila mahali! (Zab. 37:25) Bila shaka, kupatana na kanuni zilizo katika 2 Wathesalonike 3:8, 10, na 1 Timotheo 5:8, mapainia hawatazamii wengine wawategemeze kifedha.

6 Mtu yeyote anayefikiria utumishi wa painia apaswa kufanya kama vile Yesu alivyosema: ‘Keti kwanza na kupiga hesabu ya gharama.’ (Luka 14:28) Kufanya hivyo huonyesha hekima ifaayo. Zungumza na wale ambao wamepainia kwa mafanikio kwa miaka kadhaa. Waulize jinsi ambavyo Yehova amewategemeza. Mwangalizi wa mzunguko wako ni painia mwenye uzoefu ambaye atafurahi kukupa madokezo ya jinsi ya kufanikiwa katika huduma ya wakati wote.

7 Huenda mtu asipate kuona kikamili ukweli wa ahadi ya Yesu iliyo kwenye Mathayo 6:33 mpaka ajiweke mwenyewe mikononi mwa Yehova. Painia mwaminifu alisimulia hivi: “Wakati mimi na mwenzangu tulipofika kwenye mgawo wetu mpya tukiwa mapainia, tulikuwa na mboga chache tu, pakiti ya majarini, na bila fedha. Tulimaliza chakula cha jioni, tukasema, ‘Sasa hatuna cha kesho.’ Tulisali kuhusu jambo hilo, na tukalala. Mapema asubuhi kesho yake Shahidi wa mahali hapo alikuja naye akajijulisha, akisema, ‘Nilisali kwamba Yehova atuletee mapainia. Sasa naweza kuandamana nanyi karibu siku yote, lakini kwa kuwa naishi mashambani, itanibidi nile chakula cha mchana nanyi, kwa hiyo nimeleta chakula hiki kwa ajili yetu sote.’ Kilikuwa kiasi kikubwa mno cha nyama ya ng’ombe na mboga.” Si ajabu Yesu alituhakikishia kwamba ‘tukome kuhangaikia nafsi zetu’! Kisha akaongezea: “Ni nani kati yenu kwa kuhangaika aweza kuongeza dhiraa moja kwenye muda wake wa uhai?”—Mt. 6:25, 27.

8 Ulimwengu unaotuzunguka unakuwa wenye kupenda zaidi vitu vya kimwili. Msongo unaoongezeka unakaziwa juu yetu tujipatanishe nao. Hata hivyo, kuthamini kwa unyenyekevu huduma ya wakati wote hutufanya turidhike na vitu vichache vya kimwili. (1 Tim. 6:8) Mapainia wanaoweka maisha zao zikiwa sahili na zenye utaratibu wana wakati mwingi wa utumishi nao hupata shangwe kubwa na nguvu za kiroho kutokana na kuwafundisha wengine kweli. Ijapokuwa hawajaribu kuishi maisha ya kujinyima raha, kushughulika kwao na hali yao ya kiuchumi kwa njia yenye usawaziko kumewawezesha kufurahia baraka za upainia.

9 Ikiwa wahisi sana kwamba tunaishi katika siku za mwisho na kwamba wakati wa ulimwengu huu mwovu unakwisha, utachochewa kiroho ujidhabihu inavyohitajiwa ili uhubiri habari njema katika kila fursa. Kwa kuangalia tena hali yako ya kiuchumi na kuacha jambo hilo mikononi mwa Yehova, huenda ukatambua kwamba waweza kumtumikia kwa wakati wote. Hata kama utalazimika kukosa vitu fulani vya kimwili unavyovitaka ili upainie, utafurahia baraka nyingi za Yehova.—Zab. 145:16.

SWALI LA 3: “Nikiwa tineja, kwa nini nifikirie utumishi wa painia kuwa chaguo langu la kazi ya maisha?”

10 Unapokuwa ukimaliza miaka yako michache ya shule, ni jambo la asili kufikiria wakati ujao. Wataka uwe salama, wenye furaha, na wenye kutosheleza. Washauri wa shule wa kutoa miongozo huenda wakajaribu kukuchochea ufuatie kazi yenye kuleta faida ambayo yahitaji miaka mingi ya elimu ya chuo. Dhamiri yako ya Kikristo iliyozoezwa vizuri yakuambia kwamba wapaswa kujitayarisha kumtumikia Yehova kikamili iwezekanavyo. (Mhu. 12:1) Pia huenda ukafikiria kuoa au kuolewa hatimaye na kuwa na familia. Utafanyaje?

11 Maamuzi ufanyayo wakati huu maishani mwako yanaweza kuunda wakati wako ujao wote. Ikiwa tayari wewe ni Shahidi wa Yehova, aliyejiweka wakfu, umejitoa mwenyewe kwa nafsi yote kwa Yehova. (Ebr. 10:7) Fursa ya kwanza uliyo nayo, jaribu upainia-msaidizi kwa mwezi mmoja au miwili. Huo utakupatia mwonjo wa shangwe na madaraka yatokanayo na upainia wa kawaida, na maoni yako kuhusu yale upaswayo kufanya na maisha yako bila shaka yatakuwa wazi. Kisha, badala ya kujaza nafasi na kazi ya kimwili ya wakati wote baada ya kumaliza shule, kwa nini usianze kufanya upainia wa kawaida? Wengine ambao walingoja hadi baadaye maishani kufurahia utumishi wa painia wanasikitika kwamba hawakuanza mara moja.

12 Ukiwa kijana, tumia kwa manufaa fursa zako za kufuatia useja na ufurahie manufaa ambazo huo hutokeza katika utendaji wa kuhubiri wakati wote. Ikiwa una tamaa ya kuoa siku moja, hakuna msingi wa ndoa ambao ungewekwa bora kuliko kutumikia kwanza katika kazi ya upainia wa kawaida. Unapokua katika ukomavu na kiroho, huenda ukachagua kupainia kuwe kazi yako ya maisha pamoja na mwenzi wa ndoa mwenye mradi kama wako. Wenzi fulani ambao wamepainia pamoja wameenda katika kazi ya mzunguko au shamba la umishonari. Hayo ndiyo maisha yenye kuridhisha kwelikweli!

13 Bila kujali waendelea kupainia kwa muda gani, utakuwa umepanua elimu yako na kupokea mazoezi ambayo hakuna kazi nyingine duniani iwezayo kuandaa. Upainia hufundisha nidhamu, utaratibu wa kibinafsi, jinsi ya kushughulika na watu, kumtegemea Yehova, na jinsi ya kusitawisha subira na fadhili—sifa zitakazokutayarisha uchukue madaraka makubwa zaidi.

14 Maisha hayajapata kamwe kukosa uhakika kwa binadamu kama sasa. Si vitu vingi vilivyo vya kudumu, mbali na vile ambavyo Yehova ameahidi. Kwa kuwa wakati wako ujao uko wazi mbele yako, hakuna wakati mwingine bora kuliko sasa wa kufikiria kwa uzito utakachofanya na maisha yako miaka inayokuja? Fikiria kwa uangalifu pendeleo la upainia. Hutasikitikia kamwe kuchagua utumishi wa painia kuwa kazi yako ya maisha.

SWALI LA 4: “Je, kutimiza takwa la saa si msongo wa daima? Vipi nikishindwa kutimiza saa zangu?”

15 Unapojaza ombi la painia wa kawaida, lazima ujibu swali hili: “Je! umepanga mambo yako ya kibinafsi hivi kwamba unaweza kutazamia kwa kiasi kutimiza takwa la mwaka la saa 1,000?” Ili ulifikie, wahitaji muda wa saa tatu hivi kwa siku katika utumishi. Bila shaka, hilo lahitaji ratiba nzuri na kujitia nidhamu. Mapainia wengi husitawisha kawaida inayofaa, ifanyayo kazi kwa muda wa miezi michache.

16 Hata hivyo, Mhubiri 9:11 husema hivi kikweli, ‘Wakati na mambo yasiyotazamiwa hutupata sote.’ Ugonjwa mbaya au hali nyingine zisizotazamiwa zaweza kumfanya painia ashindwe kutimiza takwa la saa. Ikiwa tatizo si la muda mrefu nalo latukia mwanzoni wa mwaka wa utumishi, labda ratiba iliyoongezwa ndiyo inayohitajiwa tu ili kukomboa wakati uliopotezwa. Lakini vipi ikiwa tatizo kubwa latokea wakati miezi michache tu imebaki katika mwaka wa utumishi na painia hawezi kufikia takwa?

17 Ikiwa wewe ni mgonjwa kwa muda mfupi kwa miezi michache au kwa sababu ya dharura usiyoweza kuidhibiti huwezi kutimiza saa zinazotakwa, waweza kumfikia mshiriki wa Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko, umweleze tatizo hilo. Wazee hawa wakifikiria kwamba ingefaa wakuruhusu uendelee katika utumishi wa painia bila kujali kulipia wakati uliopotezwa, wanaweza kufanya uamuzi huo. Mwandishi atatia alama kwenye kadi ya Rekodi ya Kutaniko ya Mhubiri kuonyesha kwamba hauhitajiwi kulipia wakati uliopotezwa. Hiyo si ruhusa ya kutokuwako utumishini, bali ni ufikirio wa pekee kwa sababu ya hali zako.—Ona nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Septemba 1986, fungu la 18.

18 Mapainia wazoefu hufanya muda wa saa nyingi mwanzoni mwa mwaka wa utumishi ili kuwa na akiba ya saa. Wao hutanguliza utumishi wao wa painia, kwa hiyo nyakati nyingine wao huhitaji kupunguza baadhi ya utendaji usio muhimu. Painia akishindwa kwa sababu ya ratiba mbaya au kukosa kujitia nidhamu katika kuishikilia, apaswa kuhisi kwamba ni daraka lake kukomboa wakati uliopotezwa na asitazamie ufikirio wa pekee.

19 Kuna nyakati ambazo painia anapatwa na badiliko lisiloepukika katika hali zake. Huenda akaona kwamba hawezi kutimiza takwa la saa kwa muda mrefu kwa sababu ya tatizo lenye kuendelea la afya, daraka kubwa la familia, na kadhalika. Kuhusu kisa hiki, mwendo wa hekima utakuwa kurudia kuwa mhubiri na kushiriki iwezekanapo katika utumishi wa painia-msaidizi. Hakuna uandalizi wa kawaida wa kumruhusu mtu akae katika orodha ya painia ikiwa hali zake hazimruhusu tena kutimiza takwa la saa.

20 Twatumaini kwamba uandalizi wa kufikiria kipekee wale wanaostahili kutatia moyo wengi zaidi kujiandikisha katika utumishi wa painia bila kuwa na wasiwasi isivyo lazima. Pia wapaswa kutia moyo wale ambao tayari wako katika utumishi wa wakati wote waendelee kupainia. Twataka mapainia wafanikiwe katika utumishi wao wa wakati wote.

SWALI LA 5: “Nataka kutimiza kitu fulani na nifurahie kukifanya. Je, utumishi wa painia utaniridhisha?”

21 Furaha ya kweli yategemea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na usadikisho wa kwamba tunamtumikia kwa uaminifu. Yesu alivumilia mti wa mateso “kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake.” (Ebr. 12:2) Furaha yake ilitokana na kufanya mapenzi ya Mungu. (Zab. 40:8) Katika mfumo wa mambo wa sasa, twaweza kuwa na furaha ya kweli ikiwa shughuli zetu nyingi za maisha zahusiana na ibada yetu kwa Yehova. Kufuatia mambo ya kiroho hutupa hisi ya kuwa na kusudi kwa sababu moyoni mwetu twajua kwamba twafanya yaliyo sawa. Furaha hutokana na kutoa, twajua hakuna njia bora kuliko kujitoa wenyewe kufundisha wengine jinsi ya kupata uhai udumuo milele katika ulimwengu mpya wa Mungu.—Mdo. 20:35.

22 Painia aliyenukuliwa katika fungu la kwanza alieleza hivi: “Je, kwaweza kuwa na shangwe kubwa kuliko kuona mtu fulani unayejifunza naye akiwa msifaji wa Yehova mwenye bidii? Inasisimua na kutia nguvu imani kuona jinsi Neno la Mungu lilivyo na nguvu katika kuchochea watu wafanye mabadiliko katika maisha yao ili kumpendeza Yehova.” (Ona Mnara wa Mlinzi, Oktoba 15, 1997, ukurasa wa 18-23.) Kwa hiyo, ni nini ambacho hukuletea furaha? Ikiwa, badala ya kufurahia mambo yenye kuleta raha ya muda mfupi ya ulimwengu, unathamini mambo yafaayo ya kudumu, kupainia kutakupatia hisi ya ajabu ya utimizo ambayo itakufanya uwe mwenye furaha kikweli.

SWALI LA 6: “Ikiwa si takwa la kupata uhai wa milele, je, si ni juu yangu nipainie au nisipainie?”

23 Ni kweli, uamuzi wa kupainia lazima uwe wako. Ni Yehova tu awezaye kuhukumu hali zako za kibinafsi za maisha. (Rom. 14:4) Yeye hutazamia kwa haki umtumikie kwa moyo wako wote, nafsi yako yote, akili zako zote, na nguvu zako zote. (Mr. 12:30; Gal. 6:4, 5) Yeye humpenda mpaji mchangamfu, yule amtumikiaye kwa shangwe, si kwa kinyongo au kwa kushurutishwa. (2 Kor. 9:7; Kol. 3:23) Sababu yako ya kutumikia wakati wote lazima iwe wampenda Yehova na watu katika eneo. (Mt. 9:36-38; Mr. 12:30, 31) Ikiwa hivyo ndivyo unavyohisi, basi wastahili kufikiria utumishi wa painia kwa uzito.

24 Twatumaini kwamba yale yaliyoelezwa hapa yatakusaidia upime matazamio yako ya upainia. Je, waweza kurekebisha hali zako ufanye upainia wa kawaida? Chini kuna kalenda iliyochapwa yenye kichwa “Ratiba Yangu ya Kila Juma ya Utumishi wa Painia.” Angalia kama waweza kujaza ratiba inayokufaa binafsi ambayo itakuruhusu kuwa na wastani wa muda wa saa 23 kila juma katika huduma. Kisha, uwe na imani kamili na umtumaini Yehova. Kwa msaada wake waweza kufanikiwa! Yeye ameahidi hivi: ‘Nitawamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha.’—Mal. 3:10.

25 Kwa hiyo twauliza, “Utumishi wa painia—je, wakufaa wewe?” Ukiweza kusema “Ndiyo,” weka tarehe ya kuanza kufanya upainia wa kawaida upesi na uhakikishiwe kwamba Yehova atakubariki kwa maisha yenye shangwe!

[Chati katika ukurasa wa 6]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Ratiba Yangu ya Kila Juma ya Utumishi wa Painia

JUMATATU Asubuhi utumishi wa shambani

JUMANNE Asubuhi utumishi wa shambani

JUMATANO Asubuhi utumishi wa shambani

ALHAMISI Asubuhi utumishi wa shambani

IJUMAA Asubuhi utumishi wa shambani

JUMAMOSI Asubuhi utumishi wa shambani

JUMAPILI Asubuhi utumishi wa shambani

JUMATATU Alasiri utumishi wa shambani

JUMANNE Alasiri utumishi wa shambani

JUMATANO Alasiri utumishi wa shambani

ALHAMISI Alasiri utumishi wa shambani

IJUMAA Alasiri utumishi wa shambani

JUMAMOSI Alasiri utumishi wa shambani

JUMAPILI Alasiri utumishi wa shambani

JUMATATU Jioni utumishi wa shambani

JUMANNE Jioni utumishi wa shambani

JUMATANO Jioni utumishi wa shambani

ALHAMISI Jioni utumishi wa shambani

IJUMAA Jioni utumishi wa shambani

JUMAMOSI Jioni utumishi wa shambani

JUMAPILI Jioni utumishi wa shambani

Tumia penseli kuandika ratiba yako kila siku katika juma.

Ratibu jumla ya muda wa saa 23 kila juma katika utumishi wa shambani.

Jumla ya saa za kila juma zilizoratibiwa ____________________

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki