Baraka za Huduma ya Upainia
1 “Najua kwamba hakuna kazi nyingine ambayo ingeweza kuniridhisha kama vile nimeridhika kutokana na kuwafundisha wengine kweli,” akasema painia mmoja. Mwingine alisema hivi: “Mwishoni mwa kila siku, usingizi wangu huwa mtamu, na moyo wangu hujaa shangwe.” Mapainia hao wanawakilisha ndugu na dada kila mahali ambao wameonja baraka za huduma ya upainia.—Mit. 10:22.
2 Kuwasaidia wengine wapate ujuzi wa Neno la Mungu unaookoa uhai huridhisha kikweli. (Mdo. 20:35; 1 The. 2:19, 20) “Inasisimua na kutia imani nguvu kuona jinsi Neno la Mungu lilivyo na nguvu za kuwachochea watu kufanya mabadiliko maishani mwao,” akaandika painia mmoja wa muda mrefu. Naam, kwa kujitolea kuwasaidia watu na kuongoza mafunzo ya Biblia, mapainia watapata baraka kama hizo.
3 Kumtegemea Yehova: Kuitegemea roho ya Mungu kila siku wanapofanya huduma yao, huwasaidia mapainia wasitawishe “matunda ya roho” ambayo huwalinda. (Gal. 5:16, 22, 23) Pia, kwa kuwa wanalitumia Neno la Mungu daima, mara nyingi mapainia hutumia Maandiko kwa ustadi kuitetea kweli na kuwaimarisha wengine. (2 Tim. 2:15) Ndugu ambaye amefanya upainia kwa miaka mingi alisema hivi: “Upainia umenisaidia kupata ujuzi mwingi wa Biblia, ujuzi ambao nimeutumia kuwasaidia watu wengi kumjua Yehova na makusudi yake.” Hilo ni jambo lenye kuridhisha kama nini!
4 Mapainia wa kawaida lazima pia wamtegemee Yehova katika njia nyingine nyingi. Imani yao hutiwa nguvu wanapoona jinsi anavyobariki jitihada zao za kujiruzuku. Ndugu mwenye umri wa miaka 72 ambaye amefanya upainia wa kawaida kwa miaka 55 alisema hivi: “Yehova hajawahi kamwe kunikatisha tamaa.” Isitoshe, kwa kurahisisha maisha yao, mapainia huepuka mahangaiko mengi ya maisha. Je, hilo linakuvutia wewe?—Mt. 6:22; Ebr. 13:5, 6.
5 Kumkaribia Mungu: Uhusiano wetu pamoja na Yehova ndilo jambo muhimu zaidi kwetu. (Zab. 63:3) Tunaposhiriki kikamili katika huduma kwa sababu tunampenda Yehova, uhusiano huo huzidi kuwa wa karibu zaidi. (Yak. 4:8) Ndugu mmoja ambaye amefanya upainia kwa zaidi ya miaka 18 alisema hivi: “Utumishi wa upainia hutuwezesha ‘kuonja na kuona kwamba Yehova yu mwema,’ siku kwa siku tukijenga uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Muumba wetu.”—Zab. 34:8.
6 Zaidi ya kuwa na hali zinazohitajika, mapainia wanapaswa kuwa na imani yenye nguvu, kumpenda Mungu na jirani kikweli, na kuwa tayari kujidhabihu. (Mt. 16:24; 17:20; 22:37-39) Hata hivyo, kama nyuso zenye shangwe za mapainia zinavyoshuhudia kila mahali, huduma ya upainia huleta baraka nyingi. (Mal. 3:10) Si mapainia tu ambao hupata baraka hizo, bali familia zao na makutaniko yao pia hufaidika sana kutokana na roho nzuri ambayo mapainia huonyesha.—Flp. 4:23.
[Maswali ya Funzo]
1, 2. Ni baraka gani ambazo hutokana na huduma ya upainia, na kwa nini?
3, 4. Upainia humfundishaje mtu kumtegemea Yehova, na hilo humsaidiaje kukua kiroho?
5. Upainia humsaidiaje mtu amkaribie Yehova?
6. Mapainia wanapaswa kuwa na nini, na ni nani wengine zaidi ya mapainia ambao hufaidika?