Sanduku La Swali
◼ Je! inafaa kutokeza nakala za vichapo vya Sosaiti ili kugawia wengine?
Kwa miaka mingi, Sosaiti imetokeza vichapo vingi vinavyoshughulika na kila upande wa ujuzi wa Biblia. Watu mmoja mmoja ambao wamejifunza kweli karibuni huenda wakahisi wamekosa manufaa za habari zilizochapwa wakati uliopita na hazipatikani tena kwa Sosaiti. Wengine wamejitahidi kujipatia nakala za vichapo vya zamani, na wengine wameamua wenyewe kutokeza tena nakala za vichapo vya Sosaiti na kuvifanya vipatikane katika njia tofauti-tofauti. Hiyo imetia ndani kuvichapisha tena na pia kuvitokeza kwa kompyuta. Katika visa vingine, jambo hilo limefanywa kwa kujifaidi kifedha.
Yule “mtumwa” mwaminifu anajua mahitaji yetu ya kiroho na huandaa chakula “kwa wakati wake.” (Mt. 24:45) Wakati ambapo kumekuwa na uhitaji wa kutokeza habari iliyochapishwa zamani, Sosaiti imefanya mipango kwa ajili yayo. Kwa mfano, mabuku yaliyojalidiwa ya Mnara wa Mlinzi kuanzia 1960 hadi 1985 yamechapishwa yapatikane kwa wote. Hata hivyo, watu mmoja mmoja waamuapo wenyewe kutokeza na kugawanya vichapo kama hivyo, matatizo yaweza kutokea.
Matatizo makubwa hutokea wakati vichapo hivi hutokezwa na kugawanywa kwa sababu ya kupata faida ya kifedha. Sanduku la Swali kwenye Utumishi Wetu wa Ufalme wa Julai 1977 ulisema: “Kwa hiyo ni afadhali zaidi kutotumia ushirika wa kitheokrasi kama njia ya kuanza kuuza bidhaa au kuzitangaa kwa kusudi la kupata biashara katika Jumba la Ufalme, katika mafunzo ya kitabu ya kundi na katika makusanyiko ya watu wa Yehova. Tukiepuka hilo tutasaidiwa tuangalie faida za kiroho jinsi zinavyostahili kuangaliwa, tena mambo ya biashara tutayafikiria wakati unaoyafaa.” Kwa hiyo, ni jambo la maana tuepuke kuwa wenye akili ya kujipatia faida inapohusu kufanyia biashara Neno la Mungu au mambo yanayolihusu.